Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb10 kur. 43-64
  • Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote
  • 2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb10 kur. 43-64

Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote

AFRIKA

IDADI YA NCHI 57

IDADI YA WATU 878,000,158

IDADI YA WAHUBIRI 1,171,674

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 2,382,709

Benin

Claude na mke wake, Marie-Claire, wamekuwa wamishonari wenye bidii kwa zaidi ya miaka 27. Mnamo Februari (Mwezi wa 2), Marie-Claire aliteleza, akavunjika mguu. Majuma mawili baadaye, Claude akiwa anafanya kazi kwenye makao ya wamishonari alianguka, akavunjika mguu pia. Wote wawili walikuwa na plasta, Marie-Claire kwenye mguu wake wa kulia na Claude kwenye mguu wake wa kushoto. Claude alitania hivi: “Sisi hupenda kufanya kila kitu pamoja!”

Plasta ambayo Claude alikuwa nayo haikumzuia kutembea, lakini Marie-Claire alilazimika kukaa nyumbani kwa majuma kadhaa. Ingawa alipanga kuongoza mafunzo yake 4 kati ya 12 akiwa nyumbani, alikosa sehemu nyingine za huduma. Kwa hiyo, aliamua kuketi mbele ya makao ya wamishonari kando ya meza iliyojaa vitabu na magazeti ili kuzungumza na wapita-njia. Mwezi wa Machi alihubiri saa 83. Je, Yehova alibariki jitihada zake? Mwezi huo watu walichukua vitabu 14, broshua 452, magazeti 290, na trakti zaidi ya 500.

Ethiopia

Arega, anayeishi kijijini, aliamua kupamba nyumba yake kwa kubandika magazeti ukutani. Nchini humo watu hupenda kurembesha nyumba zao kwa kutumia magazeti, lakini yeye alitaka picha zenye rangi. Akiwa sokoni alimwona mtu akiwapa watu broshua Furahia Milele Maisha Duniani! Arega alichukua moja. Badala ya kuisoma, alitenganisha kurasa zake na kuzibandika ukutani. Miaka miwili baadaye, alivutiwa na maneno yaliyokuwa kwenye broshua hiyo ukutani: “Yesu alikuwa Mwana wa Mungu.” Hilo lilikuwa tofauti na fumbo la Utatu alilokuwa amefundishwa. Akiwa na hamu ya kujua, Arega alitembea muda wa saa tisa kwenda mji uliokuwa karibu ili kuwatafuta watu hao wanaosema kwamba Mungu ana Mwana. Siku ya kwanza hakufanikiwa, naye akarudi nyumbani akiwa amevunjika moyo. Siku nyingine, akajaribu tena. Siku hiyo watu wakamwelekeza kwenye nyumba ya ndugu ambaye alikuwa amempa broshua hiyo. Azimio la Arega lilijaribiwa hata zaidi, kwa sababu alilazimika kusubiri hadi ndugu huyo arudi nyumbani. Mazungumzo yao yakaongoza kwenye funzo la Biblia. Miezi iliyofuata, Arega alisafiri mara nyingi kwenda mjini ili kupata ujuzi zaidi kuhusu Mungu. Alipoanza kuwahubiria wengine kijijini mambo aliyokuwa akijifunza, alipingwa vikali, na watu wengi wakaanza kumwepuka. Hata hivyo, hakukata tamaa, na wengine kati yao wakaanza kupendezwa. Idadi ya watu wanaopendezwa ilipofikia 13, mapainia wa pekee wawili walitumwa katika eneo hilo. Muda si muda, walikuwa wakijifunza Biblia na watu zaidi ya 40, na hudhurio katika mikutano lilikuwa watu 40 hivi. Leo, kuna wahubiri wanane katika kijiji hicho. Na sasa, kwa ndugu yetu mpya Arega, zile picha zilizo ukutani katika nyumba yake si mapambo tu.

Ghana

Kukiwa na ongezeko kubwa la simu za mkononi sehemu nyingi za Afrika, inasemekana kwamba tunaishi katika “enzi ya mawasiliano.” Ili kuwahamasisha wateja wa simu, kampuni nyingi za simu huwapa wateja muda wa kupiga simu bila malipo wakati fulani wa usiku. Dada mmoja anayeitwa Grace, aliamua kutumia vizuri huduma hiyo. Haikuwa rahisi kwake kujifunza na Monica, kwa sababu sikuzote Monica alikuwa na shughuli nyingi. Grace alifanya yote awezayo ili aendelee kujifunza na Monica, hata akapanga kumtembelea saa 11 alfajiri. Hata hivyo, ratiba ya Monica ilibadilika, ikawa vigumu kujifunza wakati huo. Grace aliamua kutumia huduma ya kupiga simu usiku bila malipo. Monica alikubali, nao wakapanga kujifunza saa 10 usiku kupitia simu. Walivunjika moyo walipogundua kwamba wakati huo watu wengi sana wanautumia mtandao na si rahisi kupiga simu. Kwa hiyo, wakapanga kuamka mapema hata zaidi ili wajifunze saa 9 usiku, ingawa haikuwa rahisi kufanya hivyo kwa kuwa wote wawili ni wafanyakazi. Grace anasema: “Nilimwomba Yehova anipe nguvu na uwezo wa kuendelea ili upendezi wa mwanafunzi wangu usipoe. Nilitega kengele ya simu yangu ili niamke na kuazimia kuwa macho wakati huo. Ijapokuwa nilikuwa na uchovu mwingi, nilijipa moyo.” Jitihada zake zilimletea shangwe kubwa alipomwona Monica akibatizwa katika Kusanyiko la Wilaya la “Kuongozwa na Roho ya Mungu” la mwaka wa 2008! Hivi karibuni, Grace ametumia huduma hiyohiyo ya kupiga simu usiku bila malipo kujifunza na mwanamke fulani ambaye sasa ameanza kuhudhuria mikutano.

Msumbiji

Mnamo Agosti 2008, koti lilianguka kutoka kwenye gari lililokuwa likipita karibu na nyumba ya dada mmoja mjane na maskini. Dada huyo alipoliokota, alipata katika mifuko ya koti hilo karatasi fulani, vifuko vitatu vidogo vyenye vito vya bei ghali, na dola zipatazo 1,000. Alitafuta mtu ambaye angeweza kupiga nambari za simu zilizokuwa katika karatasi hizo ili kumwarifu aliyelipoteza koti hilo. Jioni hiyo, gari lenye wanaume wanne lilifika katika kijiji hicho. Mbele ya wenye mamlaka kijijini, dada yetu alimkabidhi mwenye koti, koti lake likiwa na kila kitu. Mwenye koti alianza kutokwa na machozi na kusema ikiwa lingeokotwa na mtu mwingine yeyote ambaye si Shahidi wa Yehova, hangepata chochote. Dada yetu mwaminifu, alitoa ushahidi katika kijiji hicho, ushahidi ambao ulimletea sifa nyingi Mungu wake, Yehova.

AMERIKA

IDADI YA NCHI 55

IDADI YA WATU 910,761,124

IDADI YA WAHUBIRI 3,575,123

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 3,778,321

Barbados

Wazazi wengi hupenda kuwafundisha watoto wao kukariri maandiko ya Biblia. Familia moja huko Grenada ilifurahi sana kusikia jinsi mtoto wao mwenye umri wa miaka sita alivyoitumia Biblia kuthibitisha ukweli wa kwamba Yehova ndiye mkuu zaidi. Baba ya mtoto huyo anaandika: “Alasiri moja, mke wangu Laura alipoenda kumchukua mtoto wetu Stefan, kutoka shuleni, mwalimu alimwita kando na kumwambia: ‘Nataka kukueleza kwamba mtoto wenu ananivutia sana. Ingawa imani yangu ni tofauti, navutiwa sana na jinsi anavyofafanua imani yake.’

“Walipofika nyumbani, mke wangu akamuuliza Stefan kilichotokea shuleni na kumfanya mwalimu ampongeze sana. Stefan akasema kwamba wakati wa kipindi cha kwanza, mwalimu alisema kwamba ‘Yesu ni Mungu.’

“Stefan aliinua mkono, na mwalimu wake alipompa nafasi ya kuongea, akasema: ‘Haiwezekani mwalimu, Yesu si Mungu. Biblia inasema kwamba Yesu ni Mwana wa Yehova, kwa hiyo Yesu hawezi kuwa ndiye Yehova.’

“Mwalimu akajibu: ‘Mimi naamini kwamba Yesu ndiye Yehova.’

“Kisha Stefan akasema: ‘Lakini Biblia inasema kwamba Yehova peke yake ndiye Aliye Juu Zaidi, wala si Yesu. Ni Yehova tu Aliye Juu Zaidi.’ Alikuwa akinukuu Zaburi 83:18, andiko ambalo tulikuwa tumemsaidia kukariri na kuelewa. Ingawa mwalimu huyo huonekana mkali, hata hivyo, hakuweza kumshinda mtoto wa miaka sita aliyekuwa na ujuzi sahihi wa Maandiko.”

Ekuado

Ndugu kadhaa walipanda basi kurudi nyumbani baada ya kuhubiri katika kijiji cha watu wanaozungumza lugha ya Quichua. Kwa kuwa basi lilikuwa na vifaa vya kuchezea video, ndugu hao waliruhusiwa kuonyesha video ya Noa na Daudi katika lugha ya Quichua. Abiria walishangaa sana kuona na kusikia ujumbe katika lugha yao wenyewe! Abiria hao hawakutaka kupitwa na lolote hivi kwamba kila mara basi liliposimama, walimwambia abiria aliyeingia aketi haraka ili asiwazuie. Video hiyo ilipoisha, wengi waliomba nakala ya video hiyo. Abiria fulani walikuwa na maswali ya Biblia na waliomba vitabu; wengine walitoa majina na anwani zao ili mtu awatembelee, na wote walipokea mwaliko wa Ukumbusho ambao ungefanywa katika lugha ya Quinchua. Bila shaka, hilo lilichangia sana hudhurio kubwa wakati wa Ukumbusho katika eneo hilo.

Mexico

Akihubiri nyumba kwa nyumba, ndugu mmoja painia anayeitwa Gabino alifika kwenye nyumba fulani na kupiga hodi. Hakuna aliyefungua mlango. Akajaribu tena mara ya pili na ya tatu. Baada ya kusubiri kidogo, alijaribu tena mara ya nne. Mlango ukafunguliwa na mtu mwenye huzuni nyingi, aliyekuwa akilia. Alimkaribisha Gabino lakini hakuweza kuzungumza kwa sababu alikuwa amechanganyikiwa. Gabino akaanza kumfariji kwa habari njema, naye akatulia. “Unaona kiti kile pale?” mtu huyo akamwambia. “Ulipopiga hodi mara ya tatu nilikuwa nimepanda juu ya kiti hicho. Unaona kamba ile inayoning’inia pale? Ulipopiga hodi mara ya nne, nilikuwa nimejifunga shingoni, lakini nikaifungua ili nije kukufungulia. Asante kwa kuendelea kupiga hodi kwa sababu la sivyo ningekuwa nimejinyonga.” Alisema kwamba amechoshwa na mke wake. Gabino akapanga kujifunza naye Biblia. Kwa kawaida, Gabino hupiga hodi mara moja au mbili tu. Lakini siku hiyo kwa sababu ya kuendelea kupiga hodi, huenda akiongozwa na malaika, alipata matokeo mazuri.

Chile

Wakati wa kampeni ya kuwakaribisha watu kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo, mtoto mdogo alimuuliza Shahidi mmoja, “Una miaka mingapi?” Dada huyo alishangazwa na swali la mtoto huyo, akamuuliza, “Na wewe una miaka mingapi?” Msichana huyo mdogo akajibu kwamba ana miaka sita na mama yake amempa barua amkabidhi mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mama yake alikuwa amemtuma atafute Shahidi ambaye si mtoto wala si mzee. Basi, dada huyo akamwambia kwamba ana umri wa miaka 25. Binti huyo akamkabidhi barua aliyokuwa nayo. Barua hiyo ilisema: “Mnapofika nyumbani kwangu, huwa sina ujasiri wa kuwafungulia. Nina tatizo la kushuka moyo sana nami nimemwomba Mungu anisaidie. Nimejaribu pia kusikiliza ujumbe wenu na kusoma Biblia, lakini imekuwa vigumu sana kwangu. Ningependa kujifunza Biblia na mtu ambaye anaweza kunisaidia kukabiliana na maisha baada ya ndoa yangu kuvunjika. Ikiwa unaweza kunisaidia, tafadhali uje nyumbani kwangu leo alasiri, kwa sababu asubuhi ya leo niko kitandani. Asante.”

Alasiri hiyo, dada huyo alimtembelea na kumkaribisha kwenye Ukumbusho na hotuba ya pekee. Mikutano hiyo ilimfariji sana. Tangu wakati huo amekuwa akifaidika kwa kuhudhuria mikutano na anafanya maendeleo mazuri katika funzo lake la Biblia kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Vipi binti yake mwenye umri wa miaka sita? Yeye na dada yake mwenye umri wa miaka 12, wanafurahia pia kujifunza Biblia.

Puerto Riko

Dada mmoja anaandika hivi: “Nilikuwa nikigawa magazeti barabarani nilipomwona mwanamke mmoja akiongeza pumzi kwenye magurudumu ya gari lake. Nikamkaribia, lakini hata kabla sijaanza kuzungumza, akaniomba gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! akisema kwamba anapenda sana kuyasoma. Nilipomweleza kuhusu kujifunza Biblia, alisema hawezi kwa sababu anaishi jengo moja na mama yake ambaye hatupendi hata kidogo. Nilipomuuliza anaishi wapi, aliniambia jina la barabara tu. Siku tofauti, nilienda mahali hapo na kumtafuta lakini sikufanikiwa. Halafu siku moja, nilirudi tena na kuwauliza majirani ikiwa wanamjua mama fulani anayeitwa Nancy, mwenye watoto wawili wadogo. Nilifurahi sana waliponielekeza kwake. Hata hivyo, sikumpata, na kwa hiyo nikamwachia magazeti na ujumbe mdogo. Hatimaye tulipokutana, alianza kulia akisema anataka sana kufika kwenye Jumba la Ufalme. Alikuja na kufurahia sana upendo mchangamfu wa akina ndugu na dada. Aliniambia kwamba hakuwasiliana nami mwanzoni kwa kuwa mama yake alikuwa akiyararua magazeti pamoja na ujumbe wangu kabla hajarudi nyumbani. Tulianza kujifunzia Biblia nyumbani kwa dada yake, na punde si punde, Nancy akawa anahudhuria mikutano kwa ukawaida. Sasa hakosi mkutano wowote. Amejiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, nasi hufurahi kusikia maelezo yake pamoja na ya watoto wake wawili wadogo katika mikutano.”

ASIA NA MASHARIKI YA KATI

IDADI YA NCHI 47

IDADI YA WATU 4,073,556,172

IDADI YA WAHUBIRI 635,896

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 579,554

Korea Kusini

Mwanamume mmoja anayeishi karibu na Jumba la Ufalme alipata kikaratasi chenye ujumbe kilichochomekwa kwenye gari lake, alilokuwa ameegesha mbele ya nyumba yake. Kikaratasi hicho kilisema: “Samahani, nimekwaruza gari lako nilipokuwa nikiegesha gari langu. Tafadhali wasiliana nami kwa simu, nitalirekebisha.” Kwa kuwa alijua mwenendo wa Mashahidi wanaokutanika katika jumba lililo karibu na kwake, mwanamume huyo alikata kauli, ‘Haikosi aliyekwaruza gari langu ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.’

Aliyekuwa ameacha ujumbe huo ni dada anayeitwa Su-yeon, na mwanamume huyo alipompigia simu, dada alimwomba msamaha na kumweleza tena kwamba atalirekebisha. Wazia mshangao wa dada yetu mwanamume huyo alipomwuliza, “Samahani, wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Mwanamume huyo alimweleza dada yetu kwamba hana haja ya kuhangaika kwa sababu atalirekebisha gari hilo mwenyewe! Kisha akasema kwamba angependa kukutana naye kwa sababu kuna mambo ambayo angependa kujua kuhusu Mashahidi. Su-yeon, akiwa pamoja na baba yake na ndugu mwingine kutoka katika kutaniko lao, wakaenda kukutana naye. “Nimepata nafasi ya kuwachunguza Mashahidi,” mwanamume huyo akasema “kwa sababu ninaishi karibu na Jumba la Ufalme. Nyinyi ni watu wazuri. Sielewi kwa nini watu wanawachukia.” Baba ya Su-yeon alijibu maswali ya mwanamume huyo akitumia Biblia na kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Sasa anajifunza Biblia na baba ya Su-yeon naye anafanya maendeleo.

Nchi ambamo kazi yetu imezuiwa au kupigwa marufuku

Kanali mmoja wa jeshi alichochewa sana na jinsi kweli ilivyombadilisha mke wake, ambaye ni Shahidi wa Yehova. Kwa sababu hiyo, akakubali kujifunza Biblia. Kamanda wake, ambaye ni jenerali, aliposikia hilo akamwita azungumze naye. Jenerali huyo alimwambia ikiwa hataacha kukutana na Mashahidi wa Yehova, atahamishiwa eneo la mbali. Kwa ujasiri kanali huyo alimjibu kwamba mke wake amekuwa akijifunza Biblia kwa muda mrefu na hajaona hatari yoyote. Kwa hiyo hataacha kujifunza Biblia. Baada ya muda fulani kanali huyo akaamua kuondoka jeshini. Sasa amebatizwa naye anatumikia akiwa painia wa kawaida na mtumishi wa huduma. Mke wa yule jenerali alianza kujifunza Biblia pia. Jenerali hakuweza kumzuia na sasa yeye pia ni painia wa kawaida.

Katika nchi nyingine, dada mmoja alianza kujifunza Biblia na mwanamke ambaye mume wake alimpinga vikali. Kwa sababu hawangeweza kujifunzia nyumbani kwa mwanamke huyo, walipanga kujifunza kwenye bustani fulani ndogo. Walipokuwa wakijifunza mwanamume mmoja mzee aliyependa kufanya matembezi katika bustani hiyo alipita mahali hapo mara kadhaa, akiwatazama na kusikiliza mazungumzo yao. Siku moja aliwasogelea na kuanza kuwauliza maswali ya Biblia. Siku ya kujifunza iliyofuata, alifanya vivyo hivyo. Mwanamke aliyekuwa akijifunza Biblia alianza kukasirika, akamwambia, “Mimi nina saa moja tu ya kujifunza Biblia, halafu wewe unakuja na kunimalizia wakati kwa maswali yako yasiyo na mwisho.” Basi, dada huyo akapanga na ndugu fulani ajifunze Biblia na mwanamume huyo. Muda si muda, akafanya maendeleo ya kiroho na kuanza kuhudhuria mikutano. Kila Jumapili, wanawake wawili majirani wake, walikuwa wakimwona akiondoka nyumbani akiwa amevaa vizuri, akiwa na mkoba mkononi. Walitaka kujua huwa anaenda wapi nao wakapata fununu kwamba ameanza kushirikiana na “dini mpya.” Katika upelelezi wao, wanawake hao wawili walimfuata mpaka kwenye Jumba la Ufalme. Dada kadhaa walizungumza nao na kuwauliza ikiwa wangependa kujifunza Biblia. Mmoja wao alikubali. Watu hao watatu—yule mwanamke aliyekuwa akijifunza Biblia bustanini, mwanamume aliyepatikana bustanini, na mmoja wa wanawake waliomfuata—wamefanya maendeleo makubwa ya kiroho nao sasa wamebatizwa.

Kambodia

Painia mmoja huko Kambodia anayeitwa Louy, husafiri kwa baiskeli kwenda kijiji kimoja ambako huongoza mafunzo ya Biblia. Siku tatu kabla ya Ukumbusho, alipokuwa katika kijiji hicho, akizungumza na mmoja kati ya wanafunzi wake kuhusu Ukumbusho, watoto walianza kukusanyika na kumuuliza maswali. Idadi ya watoto hao ilizidi kuongezeka. Louy akawapa mialiko 57. Siku iliyofuata Louy alipanda baiskeli yake na kwenda mpaka kijijini kuongoza funzo lingine la Biblia. Mwanafunzi huyo alimwambia kwamba ndugu zake na marafiki pia wangependa kuhudhuria. Louy akampa mialiko 20 awape. Louy alianza kujiuliza atawasaidia jinsi gani watu wote hao kufika kwenye Ukumbusho. Baada ya kusali, alizungumza na baba ya mmoja kati ya mafunzo yake, ambaye ni mzee wa kijiji. Baba huyo akamhakikishia Louy kwamba ikiwa atapata tuk-tuk au bajaji, kila mmoja anaweza kwenda. Wanaweza kusimama au kupakatana. Louy alifurahi sana watu 18 walipohudhuria kutoka kijiji hicho.

India

Ndugu mmoja, dereva wa riksho, alimhubiria abiria mmoja ambaye kumbe alikuwa mwandishi wa habari. Mwandishi huyo alishangazwa sana na ujasiri wa ndugu huyo kwa sababu katika eneo hilo Mashahidi walikuwa wameshambuliwa na wapinzani kwa sababu ya kuhubiri habari njema. Mwandishi huyo wa habari aliamua kuchapisha mazungumzo yao katika gazeti la kitaifa. Aliandika: “Niliamua kumchokoza kidogo kwa kumuuliza, ‘Hujapata habari leo? Watu wenu wamepigwa na makanisa yenu yameshambuliwa katika sehemu mbalimbali?’ Akajibu, ‘Ndiyo nimesoma habari hizo kwenye magazeti.’ ‘Mtafanya nini wakiendelea kuwahangaisha?’ Alitikisa kichwa, na kusema: ‘Haidhuru. Hatutaacha imani yetu.’”

Akizungumza kuhusu trakti aliyopewa na Mashahidi, mwandishi huyo aliandika: “Nilipofika nyumbani niliitoa karatasi hiyo mfukoni. Ina mandhari nzuri ya bustani zenye nyasi nzuri, ziwa, miti yenye maua mazuri, watu wakivuna nafaka na matunda, na milima yenye theluji. Karatasi hiyo ina kichwa, ‘Uzima katika ulimwengu mpya wenye amani.’ Ujumbe wake ulikuwa wa kidini. Kwa kawaida hakuna mtu ambaye angekataa kupokea ujumbe, uwe kuhusu duka la nguo au maisha kwa ujumla. Lakini ukianza kuzungumzia ulimwengu mpya watu wataanza kukuchukia.”

Filipino

Sehemu fulani ya mkoa wa Zamboanga kuna mlima ambao ni mrefu sana hivi kwamba kilele chake kinaweza kuonekana umbali wa kilomita 200. Akina ndugu wanaoishi karibu na mlima huo kwa kawaida hutaniana wakiwa kwenye utumishi wa shambani wakisema, “Tutafanya nini ikiwa mtu anayependezwa atakuwa akiishi kwenye kilele cha mlima ule?” Siku moja walipokuwa wakihubiri chini ya mlima huo, mtu mmoja aliwafikia na kusema kwamba anatafuta Mashahidi wa Yehova. Alisema kwamba anahitaji wamsaidie kujifunza Biblia. Akina ndugu wakamuuliza anaishi wapi. Alipowaonyesha kwenye kilele cha mlima akina ndugu hawakuwa na la kusema. Mtu huyo akawaeleza kwamba nyumba yake haiko kwenye kilele cha mlima, lakini nyuma ya mlima na kwamba njia pekee ya kufika huko ni kupitia kilele cha mlima. Ndugu hao hawakuwa na la kufanya ila kwenda. Funzo la Biblia lilianzishwa, na kwa sasa mtu huyo anahudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, hata ingawa ni mbali sana na nyumbani kwake. Mtu huyo sasa yuko miongoni mwa watu wanaomiminika kwenye “mlima wa nyumba ya Yehova.”—Isa. 2:2.

ULAYA

IDADI YA NCHI 47

IDADI YA WATU 736,988,468

IDADI YA WAHUBIRI 1,563,910

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 819,067

Finland

Ndugu wawili walikuwa wakienda nyumba kwa nyumba ili kuanzisha mafunzo ya Biblia wakiwa na trakti Je, Ungependa Kujua Ukweli? Mwanamume mmoja alifungua mlango, akakatiza utangulizi wao na kuwakaribisha ndani. “Nina maswali mengi sana,” mwanamume huyo akasema. “Mbona mmekuja saa hizi?”

Akina ndugu hao wakajibu, “Leo tunahubiri eneo hili.”

Mwanamume huyo akasema: “Nimekuwa nikiomba Mungu kwamba Mashahidi wa Yehova wanitembelee. Kwa kawaida mimi hufanya mazoezi ya kukimbia saa hizi lakini leo sikuenda. Nanyi mmeingia!” Mwanamume huyo alifikiri kwamba sala zake zimejibiwa. Mahali anapofanyia kazi, mara nyingi watu huzungumza vibaya kuhusu Mashahidi wa Yehova. Akitaka kujua ikiwa shutuma hizo zina msingi, alienda kwenye maktaba kutafuta habari. Akapata kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga Mbiu wa Ufalme wa Mungu, alikisoma na kupata kujua kwamba shutuma kuhusu Mashahidi ni za uwongo. Hivyo, akiwa na hamu kubwa alitaka sana kukutana na Mashahidi wa Yehova. Funzo la Biblia lilianzishwa na mara moja akaanza kuhudhuria mikutano. Alimhubiria mke wake ambaye alikuwa ametengana naye pamoja na binti yao, nao pia wakaanza kujifunza.

Uingereza

Kirsty, painia wa kawaida, alijifunza Kilingala na Kifaransa ili awahubirie watu kutoka Kongo katika eneo lake. Siku moja alimwona mwanamke kutoka Kongo aliyekuwa aking’ang’ana kuingia ndani ya basi kwa sababu alikuwa na mizigo mingi. Kirsty alimuuliza katika Kilingala ikiwa anaweza kumsaidia kuingiza mizigo hiyo ndani ya basi. Mwanamke huyo akauliza hivi: “Mbona wewe, mzungu, unazungumza Kilingala?” Kirsty akamjibu kwamba anashirikiana na kutaniko la Kilingala na kwamba Mashahidi wenzake wamemfundisha lugha hiyo ili aweze kuzungumza na watu kuhusu Biblia. Kirsty alitaka kumwalika mwanamke huyo kujifunza Biblia, hivyo akapanda basi hilo hadi mahali ambapo mwanamke huyo alishukia. Kisha, Kirsty akambebea mizigo yake hadi kwenye ghorofa ya tatu aliyokuwa akikaa. Mume wa mwanamke huyo na watoto wao wanne wakamkaribisha Kirsty, naye akawaonyesha jinsi ya kujifunza Biblia wakitumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Mwanamke huyo na watoto wake wawili wakubwa, sasa wanajifunza Biblia. Wote watatu wanafanya jitihada ili kumfurahisha Yehova.

Georgia

Mapainia wawili vijana waliamua kuhamia eneo la milimani ambako kuna Mashahidi wachache. Walianza kuhubiri kijiji kimoja baada ya kingine, na matokeo yalikuwa mazuri. Waligawanya mamia ya vichapo na kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia. Ndugu hao walipoanza kuhubiri katika eneo hilo, walikuwa na vitu vichache sana vya kujikimu na hawakujua watalala wapi. Lakini sikuzote walipata walichohitaji. Watu katika vijiji hivyo vya milimani walikuwa wakiwakaribisha walale kwenye nyumba zao na waliwaandalia chakula. Nyakati fulani, hata watu ambao hawakupenda kusikiliza ujumbe wetu, waliwapa mahali pa kulala na chakula. Baada ya muda fulani, ndugu hao waliwekwa rasmi kuwa mapainia wa pekee katika eneo hilo. Kwa sababu wengi walitaka kujifunza Biblia, walijiwekea kiwango cha mafunzo ya Biblia ambayo wangeweza kuongoza. Hata hivyo, bado watu huwasimamisha barabarani na kuwaomba wajifunze nao Biblia, na licha ya kujiwekea kiwango, kila mmoja wao, kwa wastani, anaongoza mafunzo ya Biblia 20 kila mwezi.

Hungaria

Kila mara dada mmoja huletewa maziwa yakiwa kwenye chupa ndani ya mkoba ambao huning’inizwa kwenye ua wa nyumba yake. Siku moja, alipokuwa akirudisha chupa tupu, aliweka trakti Je, Ungependa Kujua Ukweli? kwenye ule mkoba. Kwa kushangaza, maziwa yalipoletwa tena, mwanamke ambaye husambaza maziwa hayo aliambatanisha karatasi iliyokuwa na maswali kuhusu trakti ile na ombi la kujifunza Biblia. Mara moja dada yetu alimtembelea mwanamke huyo kwenye shamba lake alikokuwa akiishi na kuanzisha funzo la Biblia kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Kabla ya hapo, mwanamke huyo alikuwa akitafuta majibu ya maswali hayo katika makanisa mbalimbali, lakini njaa yake ya kiroho haikuwa imetoshelezwa. Na katika harakati zake, badala ya kupata majibu, maswali yalikuwa yakiongezeka. Mmoja kati ya binti zake alipoanza kupendezwa pia, dada yetu alimpa kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Mama ya binti huyo alisema kwamba msichana huyo alikuwa akishtuka usiku kwa sababu ya kuota ndoto mbaya. Hata hivyo, baada ya kusoma baadhi ya sura katika kitabu hicho, binti yake hana woga naye hulala fofofo siku hizi. Mama huyo anaendelea kujifunza Biblia, naye anahudhuria mikutano ya Jumapili kwa ukawaida akiwa pamoja na binti zake wawili.

Italia

Cristina na Manel, ambao ni watumishi wa wakati wote, walikuwa wakigawa trakti Je, Ungependa Kujua Ukweli? katika eneo la vijijini la Italia ya kati. Kwenye shamba moja walisikia sauti nyuma ya nyumba. Mwanamke mwenye nyumba alipowaona Mashahidi hao, alipaza sauti: “Njooni haraka mnisaidie!” Mashahidi hao walipokuwa wakienda haraka kumsaidia, walimkuta akijaribu kumzuia nguruwe mkubwa mwenye hasira asiponyoke kutoka zizini. Mlango wa zizi hilo ulikuwa umevunjika na mwanamke huyo alikuwa akihofia kwamba nguruwe huyo atakimbia na kuingia kwenye msitu uliokuwa karibu. Alikuwa peke yake akihangaika kuufunga mlango. Akampaazia Cristina sauti, “Endelea kuushikilia mlango niende kutafuta kitu cha kuufunga.” Cristina akamwambia mara moja kwamba yeye huogopa sana nguruwe. Mwanamke huyo akampa Manel boga na kisu na kumwambia: “Usijali. Uwe ukimtupia nguruwe vipande vya boga ili kumkengeusha nikienda kutafuta bolti nyingine.”

Mwanamke huyo akaondoka. Dakika kadhaa zikapita. Wakati wote huo, Cristina alikuwa akimhimiza Manel afanye haraka kumtupia nguruwe chakula, lakini haikuwa rahisi kwa Manel kukata ganda gumu la boga. Mwishowe, mwanamke yule akarudi na kuurekebisha mlango. Akivuta pumzi kwa nguvu baada ya shughuli hiyo, mwanamke huyo akasema: “Mmetumwa na Mwenyezi Mungu!”

“Ni kweli kabisa!” wakajibu huku wakimtolea trakti na kumwonyesha.

Mara moja mwanamke huyo akasema: “Haya ni mambo muhimu, hatuwezi kuyazungumzia tukiwa tumesimama. Tunapaswa kuketi na kuzungumza tukiwa tumetulia.” Basi akatafuta viti, nao wakaketi nje kwenye jua, mwanamke huyo alikuwa na maswali mengi naye alisikiliza kwa makini akiwa na uthamini mwingi. Kisha, wakapanga kuanza kujifunza Biblia. Cristina na Manel wanasema kwamba walipata jambo hilo lililoonwa kwa sababu ya nguruwe aliyekuwa akitaka kukimbia.

OCEANIA

IDADI YA NCHI 30

IDADI YA WATU 38,338,482

IDADI YA WAHUBIRI 99,816

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 59,619

Australia

Shahidi mmoja anayeitwa Fred, ambaye anaishi katika mji mtulivu ulio kando ya bahari, alimwachia mwanamume mmoja DVD zetu tatu. Baadaye, Fred alipata barua kutoka kwa mwanamume huyo, ambayo kwa sehemu ilisema hivi: “Kusikiliza na kutazama DVD hizi kulinipa utulivu wa ajabu. Nilipata amani, shangwe, na hata kutabasamu kama watu waliokuwa katika DVD hizo. Sijawa na hisia hizo kwa miaka mingi. Sasa naamini kwamba maisha yatakuwa mazuri wakati ujao. Zamani nilikuwa mkaidi kwa Mashahidi waliokuwa wakija nyumbani kwangu, nami nasikitika sana. Watu wenu waliponitembelea hawakuwa na ubaya wowote ila tu walitaka kunihubiria habari njema. Huenda siku moja utaniona nimeketi nyuma yako kwenye Jumba la Ufalme.”

New Zealand

Dada wawili walienda kwenye ofisi za shirika la serikali la mfuko wa hazina ya familia nao wakafanya mipango ya kuja kumwona mkurugenzi wa shirika hilo. Ili kujiandaa kwa ajili ya ziara hiyo, walitayarisha “kifurushi cha familia,” kilichokuwa na habari za pekee ambazo zingemvutia mkurugenzi huyo katika kazi yake ya kushughulika na familia. Walitia ndani vitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia na Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi pamoja na toleo la Amkeni! la Agosti 2007, lililokuwa na makala “Hatua Saba za Kuwa Mzazi Bora” na pia Amkeni! la Oktoba (Mwezi wa 10) 2007 lililokuwa na makala “Walinde Watoto Wako!”

Walipoenda kumwona mkurugenzi wa shirika hilo, dada zetu walimweleza kuhusu kazi yetu ya kujitolea na kumwambia kwamba tunapendezwa sana kusaidia familia, hasa kwa njia ya kiroho. Walimwonyesha vitabu na magazeti yaliyokuwa katika kifurushi walichotayarisha. Mkurugenzi huyo alisikiliza, akapokea vitabu na magazeti hayo, na kusema kwamba angependa wale wafanyakazi wengine 35 wafaidike pia na ujumbe huo. Aliongeza kwamba makala za Amkeni! zitanufaisha familia zote 503 zilizo katika rekodi zake. Dada hao walikusanya nakala 557 za gazeti hilo la Amkeni! Majuma wawili baadaye, walipokea simu kwamba magazeti yote hayo yalikuwa yametumwa kwa familia hizo.

Fiji

[Picha katika ukurasa wa 63]

Kijana anayeitwa Viliame, alikuwa mchezaji stadi wa mpira wa raga naye alitamani sana kuchezea timu ya taifa. Ndugu yake, anayeitwa Leone, alitaka pia kuwa mchezaji wa raga, lakini baada ya kukubali kujifunza Biblia na painia mmoja wa pekee, akaona kwamba hawezi kutumikia mabwana wawili. Alianza kuhudhuria mikutano naye akaacha kucheza raga. Mama yake ambaye ni Shahidi, alimnunulia nguo za mikutano, lakini walipozozana, Viliame alichukua nguo hizo za Leone na kuzirarua. Leone alivunjika moyo sana, lakini hakulipiza kisasi. Baadaye, Leone alienda kuuza matikiti sokoni, naye akatumia kiasi fulani cha pesa alizopata kununua nguo za mkutano, Biblia na kalamu. Alimnunulia Viliame pia. Akikumbuka jinsi alivyomtendea ndugu yake, Viliame aliguswa moyo sana na matendo ya fadhili ya ndugu yake. Alivaa nguo zake mpya na kumshangaza ndugu yake kwa kuhudhuria mkutano. Pia, Viliame alikubali kujifunza Biblia, nao ndugu hao wawili wakafanya maendeleo ya kiroho. Walipokuwa wakijiandaa kwa ajili ya ubatizo, Viliame alipewa nafasi nzuri ya kucheza raga Ulaya, nafasi ambayo vijana wengi huitamani, kwa sababu ina donge nono na umaarufu mkubwa. Hata hivyo, miradi yake ilikuwa imebadilika naye akaamua kujiweka wakfu kwa Yehova. Viliame na Leone walitumikia wakiwa mapainia wasaidizi kwa miezi sita baada tu ya kubatizwa. Alipoona mwenendo mzuri wa watoto wake, Waisea, baba yao aliamua pia kujifunza Biblia. Waisea alifanya mabadiliko makubwa akabatizwa pamoja na binti zake wawili kwenye kusanyiko la siku ya pekee.

[Picha katika ukurasa wa 45]

Dada alijidhabihu na kutumia tekinolojia ya kisasa ili kuongoza funzo la Biblia

[Picha katika ukurasa wa 46]

Uaminifu wake ulikuwa ushahidi

[Picha katika ukurasa wa 48]

Ibada ya familia ilimtayarisha Stefan kuhubiri shuleni

[Picha katika ukurasa wa 49]

Kuendelea kwake kupiga hodi kuliokoa uhai

[Picha katika ukurasa wa 50]

Alimpata Shahidi ambaye si mtoto wala mzee

[Picha katika ukurasa wa 55]

Alikodisha tuk-tuk (bajaji) moja

[Picha katika ukurasa wa 58]

Alipata funzo la Biblia kwa sababu ya kujifunza lugha ya kigeni

[Picha katika ukurasa wa 60]

Kuna njia nyingi za kuhubiri isivyo rasmi

[Picha katika ukurasa wa 63]

Kutayarisha “kifurushi cha familia”

[Picha katika ukurasa wa 64]

Walikataa kazi ya kucheza raga yenye donge nono nao wakaamua kumtumikia Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki