SOMO LA 40
Kusema Mambo Yaliyo Sahihi
KWA nini Mkristo anaweza kusema jambo ambalo si la kweli? Labda anaweza tu kutaja jambo ambalo alisikia, bila kuthibitisha ukweli wake. Au huenda akatia chumvi kwa sababu bila kukusudia alielewa vibaya jambo fulani. Tukiwa waangalifu sana kusema mambo ya hakika hata yakiwa madogo-madogo, wasikilizaji wanaweza kuamini mambo muhimu ya ujumbe wetu.
Katika Huduma ya Shambani. Watu wengi huogopa kuanza huduma ya shambani kwa sababu wanahisi bado hawajui mambo mengi. Lakini, watu hao huanza kutoa ushahidi wenye matokeo hata wakiwa wanafahamu tu mambo ya msingi ya kweli. Wanafauluje? Siri ni matayarisho.
Fahamu vizuri habari unayotaka kuzungumza na watu kabla ya kwenda utumishi wa shambani. Jaribu kuwazia kimbele maswali ambayo watu wanaweza kuuliza. Tafuta majibu ya Biblia yanayoridhisha. Hiyo itakusaidia kutoa majibu sahihi ukiwa umetulia. Je, unaenda kuongoza funzo la Biblia? Pitia somo hilo kwa makini. Hakikisha unaelewa Maandiko yanayotegemeza majibu ya maswali ambayo yamechapishwa.
Ufanye nini mwenyenyumba au mfanyakazi mwenzako akikuuliza swali ambalo huwezi kujibu wakati huo? Kama huna hakika na jibu, epuka kukisia-kisia. “Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu.” (Mit. 15:28) Unaweza kutumia kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko au “Vichwa vya Biblia vya Mazungumzo.” Ikiwa huna vichapo hivyo, mwambie utafanya utafiti kisha urudi. Ikiwa kweli anayeuliza swali anataka kujua jibu, atangojea jibu sahihi. Hata anaweza kuvutiwa na unyenyekevu wako.
Unaweza kupata ustadi wa kutumia vizuri Neno la Mungu ukienda katika huduma ya shambani na wahubiri wenye uzoefu. Angalia maandiko wanayotumia na jinsi wanavyoyatumia. Kubali kwa unyenyekevu madokezo yao au sahihisho lolote wanalotoa. Mwanafunzi mwenye bidii aitwaye Apolo alifaidika na msaada aliopokea. Luka alisema Apolo ni “mfasaha,” “mwenye ujuzi mwingi,” ‘mwenye kuwaka roho,’ na mwenye “kusema na kuyafundisha kwa usahihi mambo juu ya Yesu.” Lakini kuna mambo ambayo hakufahamu. Prisila na Akila walipoona hivyo, “walishirikiana naye na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.”—Mdo. 18:24-28.
‘Kushika kwa Imara Neno la Uaminifu.’ Hotuba tunazotoa mikutanoni zionyeshe kwamba tunaheshimu sana kutaniko likiwa “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Tim. 3:15) Ili kutegemeza kweli, ni muhimu tufahamu maana ya Maandiko tunayopanga kutumia katika hotuba. Fikiria muktadha wake na kusudi lake.
Watu wanaweza kurudia kutaja jambo ulilosema kwenye mkutano wa kutaniko. Tunajua kwamba “sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yak. 3:2) Lakini utafaidika ukikuza mazoea ya kusema mambo sahihi. Ndugu wengi ambao wako katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi watakuwa wazee siku moja. Wale ambao wamepewa madaraka hayo ‘hudaiwa mengi zaidi.’ (Luka 12:48) Mzee akitoa shauri lisilofaa kwa sababu hakufikiri kwanza, na shauri hilo linawaletea akina ndugu matatizo mazito, anaweza kumkasirisha Mungu. (Mt. 12:36, 37) Basi, ndugu anayestahili kuwa mzee ni lazima ajulikane kuwa mtu “mwenye kushika kwa imara lile neno la uaminifu kwa habari ya usanifu wa kufundisha.”—Tito 1:9.
Uwe mwangalifu ili maneno yako yapatane na “kiolezo cha maneno yenye afya” ya kweli zote za Maandiko. (2 Tim. 1:13) Lakini jambo hilo lisikushtue. Labda bado hujamaliza kusoma Biblia nzima. Endelea kujitahidi. Lakini, kwa wakati huu jaribu kuona jinsi madokezo yanayofuata yanavyoweza kukusaidia kuchunguza habari ambayo unataka kutumia kufundisha.
Kwanza jiulize: ‘Je, habari hii inapatana na mambo ambayo tayari nimejifunza katika Biblia? Je, itafanya wasikilizaji wavutiwe na Yehova, ama inakuza hekima ya ulimwengu huu, ikiwatia watu moyo waifuate?’ Yesu alisema: “Neno lako ni kweli.” (Yn. 17:17; Kum. 13:1-5; 1 Kor. 1:19-21) Kisha, tumia vizuri vichapo vya kujifunza vinavyoandaliwa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Vichapo hivyo vitakusaidia kuelewa maandiko vizuri na kuyatumia kwa usawaziko na kwa kiasi. Hotuba zako zikitegemea “kiolezo cha maneno yenye afya” na utegemee njia ambayo Yehova anatumia kueleza na kutumia maandiko, utasema mambo yaliyo sahihi.
Kuchunguza Usahihi wa Habari Unayozungumzia. Matukio ya wakati huu, mambo yaliyonukuliwa, na mambo yaliyoonwa yanaweza kukusaidia kutoa mifano na kuonyesha jinsi ya kutumia mambo fulani. Unawezaje kuhakikisha kwamba mambo hayo ni kweli? Njia moja ni kutumia habari zinazotokana na vyanzo vinavyotegemeka. Hakikisha habari hiyo ni ya karibuni zaidi. Habari zinazohusu tarakimu hubadilika-badilika, magunduzi ya kisayansi hupitwa na mengine, na kadiri binadamu anavyozidi kuelewa historia na lugha za awali, mambo yaliyotegemea maarifa ya zamani huhitaji kusahihishwa. Tahadhari sana unapotumia habari za magazeti, televisheni, redio, na zile zinazosambazwa kwa kompyuta au kwenye Internet. Mithali 14:15 inashauri hivi: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” Jiulize: ‘Je, chanzo cha habari hii kinajulikana kusema kweli? Je, kuna njia nyingine ya kuthibitisha habari hiyo?’ Ukishuku ukweli wa habari fulani, basi usiitumie.
Mbali na kutumia habari zinazotokana na vyanzo vya habari vinavyotegemeka, fikiria kwa makini jinsi ambavyo unapanga kutumia habari hiyo. Hakikisha kwamba manukuu unayotumia na habari zinazohusu idadi zinapatana na muktadha wa chanzo cha habari hiyo. Unapotaka kukazia mambo, jihadhari usitilie chumvi maneno kama “watu wachache” kuwa “watu wengi,” na “watu wengi” kuwa “kila mtu,” na “nyakati nyingine” kuwa “nyakati zote.” Kutilia chumvi habari zinazohusu idadi, kadiri, au uzito wa mambo fulani hutokeza shaka juu ya ukweli wa habari unayozungumzia.
Ikiwa wewe husema maneno sahihi nyakati zote, itajulikana kwamba unaiheshimu kweli. Hiyo hutukuza Mashahidi wa Yehova kwa ujumla. Na la muhimu hata zaidi ni kwamba inamletea heshima “BWANA Mungu wa kweli.”—Zab. 31:5.