Dhihirisha Itibari Katika Yehova kwa Kuzoea Mambo Uliyojifunza
“Itibari katika Yehova na utende mema; kaa katika dunia, na ushughulike kwa uaminifu.”—ZABURI 37:3, NW.
1, 2. (a) Ni nini linalopasa kutamaniwa liwe tokeo la funzo la kibinafsi? (b) Yakobo anatoa kielezi gani, na je! mtazamo unaosimuliwa naye ni wa kijuujuu tu?
FUNZO la mtu binafsi juu ya Neno la Mungu halifanywi ili kujifurahisha binafsi tu. Funzo linapasa kuwa njia ya kusitawisha itibari katika Yehova. (Mithali 3:1-5) Maneno ya mtunga zaburi yaliyopo juu yanaonyesha kwamba, nayo itibari ya kuhofu Mungu inajidhihirisha katika mtu kwa ‘kutenda kwake mema.’
2 Yakobo alihimiza hivi: “Mwe watendaji wa lile neno, si wasikiaji tu, mkiwa mnajidanganya wenyewe kwa kusababu-sababu fikira bandia, Kwa maana ikiwa mmoja ye yote ni msikiaji wa lile neno, na si mtendaji, huyu ni kama mtu ambaye anatazama uso wake wa kiasili katika kioo. Kwa maana yeye hujitazama mwenyewe, na yeye huenda zake na mara hiyo husahau yeye ni mtu wa namna gani.” (Yakobo 1:22-24, NW) Hivyo mtazamo huo haukuwa mtupo mmoja tu wa jicho. Neno la Kigiriki la “tazama,” kwa msingi ‘linamaanisha kitendo cha akili katika kushika mambo fulani ya uhakika kuhusu jambo fulani.”—An Expository Dictionary of New Testament Words, iliyotungwa na W. E. Vine; linganisha Matendo 7:31, Kingdom Interlinear.
3. Ni jinsi gani mtu anayetazama katika kioo huenda akasahau haraka “yeye ni mtu wa namna gani”?
3 Basi, wazia mtu akijichunguza sana sana katika kioo, labda akikuta kwamba ile sura ya mrudisho ni kama haivutii sana. Huenda yeye akaona kwamba kidevu kimeongezeka maradufu kutokana na kula na kunywa kupita kiasi, amefura-fura chini ya macho yake kwa kukosa usingizi, na ana makunyanzi juu ya macho yake kutokana na wasiwasi wa mambo yenye kusumbua-sumbua. Anapojikabili yeye mwenyewe uso kwa uso, anaazimia kufanya mabadiliko aliyokawiza sana katika tabia na mtindo wa maisha. Halafu ‘anaenda zake.’ Ile sura yenye kumsumbua ikiwa imetoka kabisa machoni pake, yeye ‘anasahau mara hiyo,’ si hasa vile sura yake ilivyo, bali “yeye ni mtu wa namna gani.” Azimio lake la kufanya mabadiliko linayeyuka kama mvuke.
4. Ni jinsi gani kielezi cha Yakobo kinavyotumika kwa funzo letu la Maandiko?
4 Vivyo hivyo, huenda wewe ukawa u mwanafunzi hodari wa Biblia. Hata hivyo, wewe unaitikia jinsi gani mambo ambayo unaona katika kioo cha Neno la Mungu? Wakati sura ya dosari na mawaa ya kiroho inaporudishwa na ule mwangaza, je! hiyo inakusababishia wewe hangaiko la muda tu, au wewe unafanya azimio thabiti kusahihisha kasoro zile? Yakobo aliongezea hivi: “Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri [mwenye furaha, NW] katika kutenda kwake.” (Yakobo 1:25) Mtunga zaburi alisali hivi: “Ee BWANA [Yehova, AW], unifundishe njia ya amri zako, nami nitaishika hata mwisho.”—Zaburi 119:33.
Jambo Ambalo Mazoea Yetu Yanaeleza Juu Yetu
5. (a) Mazoea yetu yanaeleza nini juu yetu? (b) Ni msiba gani unaongojea wale walio “wazoeaji wa jambo lenye kujaa maumizo”?
5 Kwa kweli, mambo ambayo sisi tunatenda au kuzoea yanathibitisha sisi tukoje kwa ndani. Na muda si muda mtu hufanya “ule unafsi wa siri” udhihirike kwa kuzoea mema au mabaya. (Zaburi 51:6, NW) Akasema Sulemani: “Hata kwa mazoea yake mvulana hujifanya mwenyewe atambuliwe juu ya kama utendaji wake ni wenye kutakata na mnyoofu.” (Mithali 20:11, NW) Hivyo ndivyo ilivyokuwa juu ya Yakobo na Esau walipokuwa vijana. Kadiri wakati ulivyopita, mazoea ya Esau yalifanya ukosefu wake wa uthamini wa kiroho uonekane wazi. (Mwanzo 25:27-34; Waebrania 12:16) Hiyo imekuwa kweli pia kwa maelfu ambao walidai kuwa wanaitibari katika Yehova lakini wakathibitika kuwa wale ambao Biblia inaita “wazoeaji wa jambo lenye kujaa maumizo.” (Ayubu 34:8, NW) Mtunga zaburi aliandika hivi: “Wakati waovu wanapochipuka kama majani-majani na wazoeaji wote wa lililo la kujaa maumizo wanapochanuza, inakuwa hivyo ili kwamba wao wapate kuangamizwa kabisa milele.”—Zaburi 92:7, NW.
6. Kwa nini ni lazima sisi tudhihirishe itibari yetu katika Yehova sasa?
6 Hesabu ya watu waovu inapanda juu, na uangamivu wao utakuwa karibuni; Mungu hatavumilia watenda makosa kwa wakati usio dhahiri. (Mithali 10:29) Kwa hiyo ni lazima sisi tudhihirishe itibari yetu katika Yehova kwa kuzoea mambo tunayojifunza. “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mwema miongoni mwa mataifa,” Petro anahimiza. (1 Petro 2:12, NW) Basi, ni nini baadhi ya maeneo ambamo sisi tungeweza kufanya maendeleo?
Shughuli Zetu Pamoja na Wengine
7. Kwa nini ni lazima sisi tuwe na tahadhari katika shughuli zetu pamoja na “wale walio nje”?
7 Eneo moja lingeweza kuwa namna yetu ya kushughulika pamoja na wengine. Mithali 13:20, NW, inatahadharisha hivi: “Yeye ambaye anakuwa na shughuli pamoja na wapumbavu ataendewa na mambo vibaya.” Kwa kutotumia shauri hilo lililovuviwa, watu fulani wanajiruhusu wafahamiane kupita kiasi na walimwengu mmoja mmoja kazini na shuleni. Hivyo ndugu mmoja aliyeoa alikuja kuhusika katika mwenendo usio safi pamoja na mwanamke mmoja akiwa kazini. Alijiunga pia na wafanya kazi wenzake katika visafari vya kwenda sehemu za kwao za kunywea pombe, tokeo likiwa kwamba yeye alilewa. Kwa uhakika, sisi tunahitaji ‘kuendelea kutembea katika hekima kuelekea wale walio nje.’—Wakolosai 4:5, NW.
8. Ni jinsi gani watu fulani wangeweza kufanya maendeleo katika shughuli zao pamoja na Wakristo wenzao?
8 Lakini namna gani juu ya shughuli zetu pamoja na Wakristo wenzetu? Mathalani, tuseme kwamba wewe una deni la pesa za ndugu. Je! ungeweza kukawia-kawia bure tu kumlipa, ukisababu-sababu kwamba kwa kuwa ndugu yako anaonekana mwenye mali kidogo, wewe unazihitaji zaidi ya yeye? “Yule mwovu anakopa na halipi kurudisha,” inasema Zaburi 37:21, NW. Au ikiwa wewe ni mwajiri-kazi, je! wewe unatumia ile kanuni ya kwamba “Mfanya kazi anastahili mshahara wake” kuhusiana na kuwalipa waajiriwa-kazi Mashahidi? (1 Timotheo 5:18, NW) Paulo aliweza kusema hivi juu ya shughuli zake mwenyewe: “Tukiwa na utakatifu na weupe-moyo wa kuhofu Mungu . . . sisi tumejiendesha wenyewe katika ulimwengu, lakini hasa zaidi kuelekea ninyi.”—2 Wakorintho 1:12, NW.
Kuvalia na Kujipamba kwa Kiasi
9. Ni maelekeo gani katika kuvalia na kujipamba ambayo yameonwa na wazee fulani?
9 Mwangalizi-msafiri mmoja katika Ujeremani aliwasimulia Wakristo fulani wa huko kuwa ndicho “kizazi cha kuvaa viatu vya mpira wa tenisi” kwa sababu ya mavazi yao ya vivi hivi tu mikutanoni. Ofisi ya tawi iliongezea kwamba wahudhuriaji fulani wa mikutano ‘huukaribia mpaka wa kuvalia kizembe-zembe,’ ingawa ‘walio wengi sana wa ndugu zetu huvaa kwa kiasi.’ Bara jingine linaripoti vivyo hivyo kwamba “ukosefu wa usafi wa kibinafsi ni tatizo hapa . . . Ndugu fulani hawavai nguo zilizo safi. Wanaacha nywele zao bila kuchanuliwa na zikiwa chafu-chafu wakati wa kwenda mikutanoni au katika utumishi wa shambani.” Ni jambo la maana kama nini kwa watumishi wa Yehova kuwa nadhifu na safi katika kila jambo!—2 Wakorintho 7:1, NW.
10. (a) Ni kanuni gani inayopasa kuongoza uchaguzi wetu wa kuvalia na kujipamba? (b) Ni wakati gani huenda shauri likafaa, na inatupasa sisi tuitikie jinsi gani?
10 Sisi tunahitaji ‘kuvaa kwa kiasi, kwa ustahifu na ufaaji,’ hasa wakati wa kujitia katika utendaji mbalimbali wa kiroho. (1 Timotheo 2:9, New International Version) Suala si kama mtindo fulani ni wa kisasa kupita kiasi bali ni kama unafaa kwa mmoja anayedai kuwa mhudumu wa Mungu. (Warumi 12:2; 2 Wakorintho 6:3) Nguo za kivi-hivi mno au zenye kubana zinaweza kuondoa fikira kwenye ujumbe wetu. Ni wazi kabisa kwamba mitindo inayofanya kwa utovu wa adabu na kwa makusudi ili wanaume waonekane kama wanawake au kufanya wanawake waonekane kama wanaume haifai. (Linganisha Kumbukumbu 22:5.) Bila shaka, huenda desturi za mahali zikatofautiana, kulingana na hali ya hewa, mahitaji ya kikazi, na kadhalika, hivi kwamba kundi la Kikristo halifanyi sheria ngumu-ngumu na zilizokazwa sana ili zihusu udugu mzima wa ulimwenguni pote. Wala haiwapasi wazee kulazimisha mapendezi ya kibinafsi juu ya kundi la kondoo. Hata hivyo, ikiwa mtindo wa kujipamba wa mhubiri fulani wa Ufalme unasumbua kundi kwa ujumla au unaondoa fikira kwenye huduma, shauri la fadhili linafaa kutolewa. Je! wewe ungeitikia shauri kama hilo kwa unyenyekevu, ukidhihirisha itibari katika Yehova?—Waebrania 12:7.
Kumwitibari Mungu Awaandalie Riziki Watafutaji wa Ufalme
11. Ni jinsi gani watu fulani wamenaswa katika ufuatiaji wa vitu vya kimwili, na kwa nini hili si jambo la hekima?
11 “Endeleeni, basi kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi vitaongezwa kwenu ninyi.” (Mathayo 6:33, NW) Inasikitisha kama nini wakati watu fulani hawasikizi maneno hayo! Kwa kuimeza ile hekaya ya kujitafutia usalama wa kipesa, wao wanafuatia kwa ari utajiri, elimu ya kimwili, na kazi-maisha za kilimwengu, “wakiitibari katika njia yao ya kujidumisha.” (Zaburi 49:6, NW) Sulemani anaonya hivi: “Usijitaabishe ili kupata utajiri . . . Je! utavikazia macho vile ambavyo si kitu? Maana bila shaka mali hujifanyia mabawa, kama tai arukaye mbinguni.”—Mithali 23:4, 5.
12. Ni jinsi gani wale wanaofuatia utajiri ‘wanajichoma-choma mwili wote kwa maumivu mengi’?
12 Mtume Paulo anazidi kuonya hivi: “Kwa maana upendo wa pesa ndio mzizi wa namna zote za mambo yenye kudhuru, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo watu fulani wamepotezwa njia kutoka kwenye ile imani na wamejichoma-choma wenyewe mwili wote kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:10, NW) Katika hoji moja katika U.S.News & World Report, Dakt. Douglas LaBier alisema kwamba wanaume na wanawake wengi vijana wakiwa katika kufuatia utajiri “wanaripoti hisia za kukosa uradhi, kuwa na wasiwasi, kushuka moyo, kuhisi utupu wa kukosa kusudi, kurukwa na akili na kuona-ona njozi bandia, na pia malalamiko ya kimwili ya namna zote—maumivu ya kichwa, maumivu ya mgongo, matatizo ya tumbo, kutoweza kulala, matatizo ya kula.”
13. Kwa nini jambo bora zaidi ni kutosheka na “chakula na nguo”?
13 Wale wanaoitibari katika Yehova awaandalie riziki wanajiepushia maumivu na wasiwasi mwingi kwa kufanya hivyo. Ni kweli, kutosheka na “chakula na nguo” tu huenda kukamaanisha kuwa na kiwango cha maisha yaliyo ya kiasi zaidi. (1 Timotheo 6:8) Lakini “vitu vyenye kuthamanika havitakuwa na manufaa yo yote katika ile siku ya kiruu.” (Mithali 11:4, NW) Zaidi ya hilo, wakati sisi tunapoongeza utumishi wetu kwa Yehova, tunajitia katika mstari wa kupata ile “baraka ya Yehova” ambayo “hutajirisha, na yeye haongezi umivu lo lote pamoja nayo.”—Mithali 10:22, NW.
“Tafuta Amani na Uifuatie”
14, 15. (a) Ni masuala ya namna gani ambayo yamesumbua amani ya makundi nyakati fulani? (b) Amani inaweza kufuatiwa jinsi gani wakati hali za kutoafikiana zinapotukia?
14 Njia nyingine ambao sisi tunadhihirisha itibari yetu katika Yehova ni ‘kutafuta amani na kuifuatia’ miongoni mwa waitikadi wenzetu. (1 Petro 3:10-12, NW) Ingawa hivyo, nyakati fulani mambo madogo sana yanaruhusiwa kuwa chanzo cha ugomvi mchungu miongoni mwa akina ndugu: Upambaji wa Jumba la Ufalme, marekebisho katika maeneo ya kundi, migawo ya Funzo la Kitabu, kushughulikia ugavi wa magazeti na vitabu. Au, katika visa fulani, badala ya kutatua magombano ya kibinafsi au ya kibiashara katika ile roho ya Mathayo 18:15-17, akina ndugu wameacha kusemezana au wamesumbua kundi kwa mzozano wao.
15 Yakobo anasema hivi: “Tunda la uadilifu linapandiwa mbegu yalo chini ya hali zenye kujaa amani.” (Yakobo 3:18, NW) Kwa hiyo, kwa masilahi ya amani uwe mwenye mbetuko wa kuyaachia nafasi mapendezi au maoni ya wengine, hata kujinyima haki za kibinafsi. (Linganisha Mwanzo 13:5-12.) Mathalani, ikiwa makundi mawili yanashirikiana utumizi wa Jumba la Ufalme moja, kundi moja halipaswi kuchukua msimamo wa kwamba hilo ndilo “mwenyeji” wa jumba hilo na kwamba ndilo lenye mamlaka ya kuamrisha kiimla nyakati za mikutano au mambo mengineyo kwa kundi lile jingine. Kustahiana na kufanyiana ushirikiano kunapasa kuwepo sana.
16. Ni nini thamani ya kutambua utaratibu wa kitheokrasi katika maskani na katika kundi?
16 Magombano mengi yanaweza kuepukwa tunapofanya tu kutambua utaratibu wa kitheokrasi na kubaki tukiwa mahali petu patufaapo. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:22-27) Wakati wake wanapostahi matakwa ya waume zao, watoto maagizo ya wazazi wao, watumishi wa huduma mwelekezo kutoka kwa wazee, vitendo vyao ‘vinafanyiza kuweze kuwa na ukuzi wa kundi kwa ajili ya kujijenga lenyewe katika upendo.’ (Waefeso 4:16, NW) Ndiyo, inakubalika kwamba nyakati fulani waume, wazazi, na wazee hupungukiwa. (Warumi 3:23) Lakini je! kuasi, kulalamika, au kukinza mielekezo yenye makusudio mema kunaleta maendeleo kwenye hali hiyo? Ingekuwa afadhali kama nini kubaki mahali petu tulipogawiwa na Mungu na kutafuta amani!
Kujitahidi Wenyewe Katika Shamba
17. (a) Ni sababu gani ambazo watu fulani wanatoa kwa kuwa na ushiriki kidogo tu katika kazi ya kuhubiri? (b) Ni jinsi gani Yesu alivyowatia moyo Wakristo waitikie mifinyo ya leo?
17 Ingawa hivyo, mwito wa ushindani ulio mkubwa zaidi kwa wengi ni kutimiza ule utume wa Kikristo wa kuzihubiri habari njema. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Wengine wanakuwa na ushiriki kidogo tu katika utumishi wa shambani, labda wakitoa hoja ya kwamba mikazo ya kuchuma riziki na kulea jamaa inafanyiza iwe vigumu kwao kufanya zaidi. Ndiyo, inakubalika kwamba mikazo ya “siku za mwisho” inahitaji jitihada kubwa kuishinda. (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, Yesu alionya dhidi ya ‘kulemewa na masumbufu ya maisha.’ Kadiri ambavyo hali zinazidi kuharibika, Wakristo wanapaswa ‘kujiinua wenyewe wima na kuinua vichwa vyao juu.’ (Luka 21:28, 34, NW) Moja ya njia zilizo bora zaidi za ‘kusimama thabiti’ dhidi ya mashambulizi ya Shetani ni kuwa ‘nyayo zetu zikiwa zimevishwa vifaa vya habari njema’—kushiriki kwa ukawaida katika kuhubiri!—Waefeso 6:14, 15, NW.
18. Ni nini ingeweza kuwa ndiyo sababu ya watu fulani kujizuia wasiwe na ushiriki kamili katika ile kazi ya kuhubiri?
18 Kule nyuma katika siku ya Paulo, Wakristo wengi (angalau katika makundi fulani) walikuwa ‘wakitafuta masilahi yao wenyewe, si yale ya Kristo Yesu.’ (Wafilipi 2:21, NW) Je! jambo hili lingeweza kuwa kweli kuhusu watu fulani walio katikati yetu leo? Labda wao wana ukosefu wa rai ya kwamba kutafuta Ufalme ni kama yule mtu aliyepata “lulu moja ya thamani kubwa” ambayo yeye angedhabihu kitu cho chote ili awe nayo. (Mathayo 13:45, 46) Kwa kujiacha wapendezwe na mambo yao wenyewe, wao wanachagua kufanya mambo yale tu yasiyowatatiza sana na kutoa utumishi kidogo tu. Ingawa hivyo, kumbuka kwamba upendo kwa Yehova na mwanadamu mwenzao ndio husukuma Wakristo wa kweli kuhubiri, hata ikiwa kuanza kuongea na watu tusiowajua kunaenda dhidi ya mbetuko wetu wa kiasili.—Mathayo 22:37-39.
19. Kwa nini Yehova hafurahishwi na jitihada vugu-vugu, na ni jinsi gani sisi tungeweza kukadiria-kadiria utumishi wetu wenyewe kwake?
19 Ikiwa moyo hautusukumi kuhubiri, basi upendo wetu kwa Yehova na itibari yetu katika yeye inakaribia kulingana na hisia ndogo tu ya akilini. “Ujue Mungu wa baba yako na umtumikie kwa moyo kamili,” Daudi akahimiza Sulemani, “kwa maana Yehova anapekua mioyo yote, na yeye anatambua kila mbetuko wa fikira.” (1 Nyakati 28:9, AW) Yehova hapumbazwi na jitihada vuguvugu. Hata ushiriki wa ukawaida katika utumishi wa shambani haumridhishi yeye ikiwa sisi tunatoa kiasi kidogo tu cha yale ambayo tungaliweza kufanya kama ‘tungalikuwa tunajitahidi wenyewe kisulubu.’ (Luka 13:24, NW) Hivyo ni lazima kila Mkristo afanye mkadirio-kadirio wa kufuata haki juu ya ushiriki wake katika utumishi wa shambani na kujiuliza mwenyewe hivi: ‘Je! mimi kweli ninafanya yote ninayoweza?’ Labda marekebisho yanahitaji kufanywa katika mambo tunayotanguliza kwanza.
Twasukumwa ‘Kutenda Mema’ na Vielelezo vya Wengine
20. Kwa nini inafaa kuchunguza vielelezo vyema vinavyowekwa na Wakristo wenzetu?
20 Utumishi wetu kwa Mungu haufanywi kwa “ulinganisho pamoja na mtu yule mwingine.” (Wagalatia 6:4, NW) Hata hivyo, vielelezo vyema vya wengine vinaweza mara nyingi kutusukuma tufanye mengi zaidi. Mtume Paulo mwenyewe alisema hivi: “Mwe waigaji wa mimi, hata kama vile mimi nilivyo wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1, NW) Basi, fikiria ni wakati mwingi kadiri gani ambao ndugu zetu wanatumia kila mwezi katika utumishi wa shambani. Katika United States, saa za wastani kwa wahubiri zimeinuka kutoka saa 8.3 katika 1979 zikawa saa 9.7 katika 1987! Ndugu zetu wamekuwa wathibitifu katika kuongezea wakati wanaotumia katika shamba. Je! hiyo ni kweli kuhusu wewe?
21. Ni nini kimeongoza wengi waingie kazi ya painia? Toa kielezi.
21 Kwa kusukumwa na vielelezo vyenye bidii vya wengine, watu wengi kadiri isivyopata kuwa wakati mwinginewo wanaingia kazi ya painia wa kawaida. Katika California (U.S.A.) dada mmoja kijana jina lake Angela alipokea toleo la kazi yenye kushawishi, kutia na uanachuo kwenye koleji ya uchaguzi wake. Badala ya kuifanya, Angela alichagua huduma ya wakati wote. Sababu yake ilikuwa nini? “Kwa kushirikiana pamoja na mapainia wengi, ningeweza kuona wakiwa na shangwe na uradhi wenye kina kirefu si kuhusiana na wenyewe tu bali pia katika uhusiano wao pamoja na Yehova. Mimi nilitaka kuwa na shangwe na uradhi huu wenye kina kirefu.”
22. Ni nini manufaa za kuzoea mambo uliyojifunza?
22 Je! wewe unataka “shangwe na uradhi wenye kina kirefu”? Basi “itibari katika Yehova na utende mema”! Acha yale unayojua yakusume wewe kutenda yote yote uwezayo katika utumishi wa Yehova. Kuyazoea mambo uliyojifunza kutafanya mwendeleo wako wa kiroho udhihirike kwa wote na kutanufaisha wengine kwa njia yenye kuokoa uhai. (1 Timotheo 4:15, 16, AW) Kwa hiyo, wote na waitikie maneno ya Paulo kwenye Wafilipi 4:9, W: “Mambo ambayo wewe ulijifunza na pia ukayakubali na kuyasikia na kuyaona kuhusiana na mimi, yazoee haya; na yule Mungu wa amani atakuwa pamoja na wewe.”
Mawazo ya Kupitia
◻ Itikio letu linapasa kuwa nini kuhusu kuchungulia ndani ya kioo cha Neno la Mungu?
◻ Ni jinsi gani sisi tungeweza kufanya maendeleo katika namna yetu ya kushughulika pamoja na wengine?
◻ Kwa nini si jambo la hekima kufuatia vitu vya kimwili?
◻ Ni jinsi gani sisi tunaweza kutafuta amani katika kundi?
◻ Ni nini kinachopaswa kutusukuma tuwe na ushiriki kamili katika utumishi wa shambani?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Haitoshi kuona dosari na mawaa ya kiroho. Ni lazima tufanye kitendo cha kuzisahihisha!
[Picha katika ukurasa wa 18]
Mara nyingi wale wanaofuatia utajiri hujiletea wenyewe “maumivu mengi”