SOMO LA 45
Mifano Inayofundisha
MIFANO ni njia yenye nguvu sana ya kufundisha. Mara nyingi inavutia wasikilizaji na kuvuta uangalifu wao. Inachochea fikira za watu. Inachochea hisia na inaweza kugusa dhamiri na mioyo. Nyakati nyingine, unaweza kutumia mifano kushinda tatizo fulani. Pia mifano husaidia sana kukumbuka mambo. Je, wewe hutumia mifano unapofundisha?
Tamathali ni semi fupi ambazo zinaweza kufanya mtu apige picha dhahiri akilini. Ukichagua semi za tamathali kwa makini, maana yake inakuwa wazi. Lakini mwalimu mzuri anaweza kuzifafanua kwa ufupi ili kutia mkazo. Biblia imejaa mifano ambayo unaweza kujifunza.
Anza na Tashbihi na Sitiari. Tashbihi ni tamathali rahisi sana za usemi. Ikiwa unajifunza kutumia mifano, inaweza kufaa kuanza na semi hizi. Kwa kawaida semi hizo hutangulizwa na neno “kama” au “mfano wa.” Tashbihi hulinganisha vitu viwili vilivyo tofauti kabisa lakini vyenye ufanani fulani. Biblia imejaa tamathali zinazotaja mimea, wanyama, na vitu kama nyota na pia mambo yanayohusu wanadamu. Zaburi 1:3 inatuambia kwamba mtu anayesoma Neno la Mungu kwa ukawaida ni “kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji,” mti unaozaa matunda na usionyauka. Mtu mwovu anatajwa kuwa “kama simba” anayeotea windo. (Zab. 10:9) Yehova alimwahidi Abrahamu kwamba mbegu yake ingekuwa nyingi “kama nyota za mbinguni” na “kama mchanga ulioko pwani.” (Mwa. 22:17) Yehova alisema hivi kuhusu uhusiano wa karibu aliokuwa nao na taifa la Israeli: “Kama vile mshipi unavyoshikamana na viuno vya mtu,” ndivyo Alivyofanya Israeli na Yuda kushikamana na Yeye.—Yer. 13:11.
Sitiari pia hukazia ufanano ulioko kati ya mambo mawili yaliyo tofauti kabisa. Lakini sitiari ina mkazo zaidi. Sitiari ni maneno yanayoonyesha kitu fulani kuwa kitu kingine. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nyinyi ndio nuru ya ulimwengu.” (Mt. 5:14) Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi alipokuwa akieleza madhara ya kuongea bila kufikiri: “Ulimi ni moto.” (Yak. 3:6) Daudi alimwimbia hivi Yehova: “Ndiwe genge langu na ngome yangu.” (Zab. 31:3) Kwa kawaida sitiari nzuri haihitaji kufafanuliwa. Ufupi wake hukazia uzito wake. Sitiari inaweza kuwasaidia wasikilizaji kukumbuka jambo kuliko maelezo tu.
Utiaji chumvi wa jambo fulani hutumiwa katika mazungumzo, lakini ni lazima utumiwe kwa busara ama sivyo unaweza kueleweka vibaya. Yesu alitumia tamathali ya aina hiyo kutaja jambo ambalo hatuwezi kusahau alipouliza: “Kwa nini wautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe?” (Mt. 7:3) Kabla ya kujaribu kutumia tamathali ya aina hii, jifunze kutumia tashbihi na sitiari.
Tumia Mifano. Badala ya kutumia tamathali za usemi, unaweza kufundisha kwa kutumia mifano ya hadithi au ya mambo halisi yaliyotendeka. Mara nyingi watu hupita kiasi wanapotumia mifano, kwa hiyo uitumie kwa busara. Mifano inapaswa kutumiwa kutegemeza mambo ambayo kweli ni muhimu, na itumiwe kwa njia inayofanya jambo kuu likumbukwe, wala si kusimulia tu hadithi.
Ingawa si lazima mifano yote iwe mambo yaliyotokea kihalisi, inapasa kuonyesha mitazamo au hali halisi za maisha. Kwa hiyo, Yesu alipokuwa akifundisha jinsi ya kuwatendea watenda-dhambi wenye kutubu, alitoa mfano wa mtu aliyefurahi sana kupata kondoo wake aliyepotea. (Luka 15:1-7) Mtu fulani hakuelewa vizuri amri ya Sheria ya kumpenda jirani. Yesu akamsimulia hadithi ya Msamaria mmoja aliyemsaidia mtu aliyejeruhiwa baada ya kuhani na Mlawi kukosa kumsaidia. (Luka 10:30-37) Ukijifunza kuwa makini kuona mitazamo na matendo ya watu, unaweza kutumia vizuri njia hii ya kufundisha.
Nabii Nathani alimkaripia Mfalme Daudi kwa kusimulia hadithi aliyobuni. Hadithi hiyo ilifaa sana kwa sababu ilimfanya Daudi asiweze kujitetea. Hadithi hiyo ilimhusu tajiri mmoja aliyekuwa na kondoo wengi na maskini mmoja aliyekuwa na kondoo mmoja tu wa kike ambaye alimtunza sana. Daudi aliwahi kuwa mchungaji, basi alielewa kabisa hisia za yule mwenye kondoo mmoja. Daudi akashikwa na ghadhabu ya haki dhidi ya yule tajiri aliyemnyakua kondoo yule mmoja wa maskini. Kisha Nathani akamwambia Daudi wazi: “Wewe ndiwe mtu huyo”! Moyo wa Daudi ukaguswa, akatubu kweli. (2 Sam. 12:1-14) Ukifanya mazoezi, unaweza kushughulikia hali ngumu kwa njia nzuri.
Maandiko yana mifano mingi inayosaidia sana kufundisha. Yesu alifanya hivyo kwa maneno machache aliposema: “Mkumbukeni mke wa Loti.” (Luka 17:32) Yesu alirejelea “siku za Noa” alipofafanua kindani ishara ya kuwapo kwake. (Mt. 24:37-39) Katika Waebrania sura ya 11, mtume Paulo aliwataja kwa majina wanaume na wanawake 16 waliokuwa mifano mizuri ya imani. Unapoifahamu Biblia vizuri, utaweza kutumia mifano mingi mizuri sana katika Maandiko inayozungumzia matukio na watu.—Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11.
Nyakati nyingine inaweza kufaa kukazia jambo kwa kusimulia tukio fulani halisi la nyakati zetu. Lakini, hakikisha unatumia mambo yaliyoonwa ambayo yamethibitishwa na kuepuka yale ambayo yanaweza kumwaibisha msikilizaji yeyote au epuka mambo yenye ubishi ambayo hayahusiani na habari unayozungumzia. Pia kumbuka kwamba jambo lililoonwa linapasa kutimiza kusudi fulani. Usisimulie mambo madogo-madogo yanayoweza kukengeusha watu kutoka kwenye kusudi lako.
Je, Mfano Huo Unaeleweka? Mfano wowote unaotumia unapasa kutimiza kusudi fulani. Je, mfano huo utatimiza kusudi hilo kama huonyeshi jinsi unavyohusiana na habari unayozungumzia?
Yesu alisema wanafunzi wake ni “taa ya ulimwengu,” akafafanua kwa ufupi jinsi taa inavyotumiwa na jinsi usemi huo unavyohusiana na daraka lao. (Mt. 5:15, 16) Baada ya Yesu kutoa mfano wa kondoo aliyepotea, alitaja shangwe inayotokea mbinguni mtu mmoja mwenye dhambi akitubu. (Luka 15:7) Na baada ya Yesu kusimulia ile hadithi ya Msamaria mwenye ujirani, alimwuliza yule mtu swali hususa kisha akamshauri. (Luka 10:36, 37) Katika hali tofauti, Yesu aliwafafanulia watu wanyenyekevu waliotaka kujua mfano kuhusu aina mbalimbali za udongo na ule wa magugu shambani, lakini hakuufafanulia umati mifano hiyo. (Mt. 13:1-30, 36-43) Siku tatu kabla ya kufa, Yesu alitoa mfano unaohusu walimaji wa shamba la mizabibu waliokuwa wauaji. Hakueleza maana ya mfano huo kwa sababu hakukuwa na haja. “Makuhani wakuu na Mafarisayo . . . wakajua kwamba alikuwa akisema juu yao.” (Mt. 21:33-45) Kwa hiyo, mfano wako, maoni ya wasikilizaji, na kusudi lako ni muhimu katika kuamua iwapo utaeleza maana ya mfano huo na kadiri utakavyoufafanua.
Kukuza uwezo wa kutumia mifano vizuri huchukua muda, lakini kuna baraka. Mifano mizuri huvutia akili na kugusa moyo. Matokeo ni kwamba ujumbe wako unakuwa na uzito ambao hauwezi kutokezwa na maneno tu.