Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb11 kur. 74-161
  • Papua New Guinea

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Papua New Guinea
  • 2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • WATANGAZAJI WA MAPEMA WA HABARI NJEMA
  • KUHUBIRI KATIKA “KIJIJI KIKUBWA”
  • “NJOO UWAFUNDISHE WATU WANGU”
  • MAKUSANYIKO YASIYOSAHAULIKA
  • KUTUMIA PICHA KUHUBIRI
  • KUPANUA KAZI YA KUHUBIRI
  • WENGINE WASIKIA HABARI NJEMA
  • KUKABILIANA NA MADHEHEBU YA WAABUDU-MALI
  • KUCHAPISHA VICHAPO VYA BIBLIA
  • KAZI YA KUHUBIRI YAENEA KASKAZINI
  • OFISI YA TAWI INAANZISHWA
  • ‘WAPIGENI MARUFUKU MASHAHIDI’
  • KUHUBIRI KWENYE NYANDA ZA JUU
  • KUHUBIRI KWA SUBIRA KUNALETA MATOKEO
  • MBEGU YA UFALME ILIYOPANDWA YATOKEZA MATUNDA
  • MBEGU ZINAKUA KATIKA MAENEO YA MBALI
  • WAMISHONARI ZAIDI WAFIKA
  • KAZI YA UJENZI YACHOCHEA MAENDELEO
  • NJIA MBALIMBALI ZA KUHUBIRI
  • KAZI YA MZUNGUKO KWENYE MTO SEPIK
  • KUSHINDANA MWELEKA NA ROHO WAOVU
  • KUWAFUNDISHA WATU KUSOMA NA KUANDIKA
  • KWELI YA BIBLIA HUBADILI MAISHA
  • KUHESHIMU ZAWADI YA MUNGU YA NDOA
  • WATOTO WANAOMLETEA SIFA MUUMBA WAO
  • JITIHADA ZA KUHUDHURIA MAKUSANYIKO YA KIKRISTO
  • KIELELEZO KIZURI CHA WAMISHONARI
  • VITA VYA WENYEWE KWA WENYEWE BOUGAINVILLE
  • VOLKANO YAHARIBU RABAUL
  • KAZI YA KUTAFSIRI INASONGA MBELE
  • SHULE YA UTUMISHI WA PAINIA INAWANUFAISHA WENGI
  • KUKUA PAMOJA KATIKA UPENDO
2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb11 kur. 74-161

Papua New Guinea

ZAMANI—katika kipindi cha miaka mingi—watu wengi sana walihamia kusini kupitia Asia wakitafuta makao mapya. Kwenye upande wa mashariki wa Visiwa vya Malay, walifika New Guinea, kisiwa cha kitropiki ambacho ndicho kisiwa cha pili kwa ukubwa ulimwenguni pote.a Walitembea kwenye ufuo wake, wakiishi kando ya vinamasi, misitu, na kwenye visiwa vinavyozunguka. Wengine walipanda juu mlimani wakaishi kwenye nyanda za juu zenye joto na zilizo na mabonde makubwa na udongo wenye rutuba.

Watu hao hawakuwa wa taifa moja bali walitoka katika makabila zaidi ya elfu moja ambayo yalipigana mara nyingi. Walikuwa na utamaduni mbalimbali, walivalia mavazi ya pekee, na kuzungumza zaidi ya lugha 800. Vikundi vingi viliishi pamoja katika vijiji vilivyolindwa bila kuwa na mawasiliano na watu wengine ulimwenguni. Wengi waliamini kwamba maeneo ya mbali ambayo hawangeweza kuona yalikuwa ya roho waovu na mababu ambao wangeweza kuathiri maisha ya watu kwa njia nzuri au mbaya. Kila kitu walichofanya maishani kilitegemea hasa kutuliza roho hizo.

Sura za watu zilitofautiana sana ingawa walifanana katika jambo moja tu. Akizungumza kuhusu jambo hilo, Jorge de Meneses, ofisa wa serikali ya Ureno aliyekuwa akizuru eneo hilo mnamo 1526, alikiita kisiwa hicho Ilhas dos Papuas, jina linalomaanisha “Nchi ya Watu Wenye Nywele za Kipilipili.” Baharia Mhispania Ynigo Ortiz de Retes aliona kwamba watu wa visiwa hivyo walifanana na wakazi wa nchi ya Guinea, Afrika Magharibi, kwa hiyo akaita kisiwa hicho Nueva Guinea, au New Guinea.

Katika karne ya 19, wakoloni kutoka Ulaya waligawanya kisiwa hicho katika maeneo matatu. Waholanzi, waliofika kwanza, walichukua upande wa magharibi, ambao leo ni sehemu ya Indonesia. Waingereza na Wajerumani waligawanya sehemu ya mashariki mara mbili ikawa British New Guinea upande wa kusini (ambao baadaye uliitwa Papua) na upande wa kaskazini ukawa German New Guinea (ambao baadaye uliitwa New Guinea). Baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, maeneo hayo mawili yakawa chini ya udhibiti wa Australia. Mwishowe, mnamo 1975, Papua na New Guinea zikaungana kufanyiza taifa huru la Papua New Guinea.b

Leo, bado Papua New Guinea inajaribu kwenda sambamba na maendeleo ya kiteknolojia ya ulimwengu wa sasa. Baadhi ya raia wa nchi hiyo wanaishi katika majiji ya kisasa wakizungukwa na vitu vya kisasa. Hata hivyo, watu 4 kati ya 5 wanaishi vijijini, ambako hakuna mabadiliko makubwa ambayo yamefanyika katika muda wa miaka mia moja iliyopita na ambako kuwa na nguruwe ni ishara ya utajiri, watu hulipa mahari, kuwasiliana na pepo kumeenea, na watu wanazingatia sana kuwa washikamanifu kwa ukoo wao.

Hata hivyo, katika miaka ya hivi karibuni, nchi hiyo yenye unamna-namna imekuwa na mabadiliko mengine muhimu ambayo yamewagusa watu wa makabila yote na kuboresha maisha yao katika njia nyingi sana. Ni mabadiliko ya kiroho yanayotokana na kujifunza na kufuata kweli zinazopatikana katika Neno la Mungu, Biblia.—Rom. 12:2.

WATANGAZAJI WA MAPEMA WA HABARI NJEMA

Kweli ya Biblia ilifika Papua New Guinea mnamo 1932 wakati ambapo painia Mwingereza anayeitwa Peck alitua huko akielekea Malaya (ambayo sasa ni Malasia). Kwa kuwa hakuwa mtu wa kupoteza nafasi zinazojitokeza, Peck alitumia majuma kadhaa akiwahubiria wenyeji. Aliwaachia vichapo vingi sana kabla ya kuelekea kwenye mgawo wake.

Miaka mitatu baadaye, mapainia saba wakiwa kwenye mashua yenye injini inayoitwa Lightbearer walitia nanga huko Port Moresby ili kurekebisha injini yao iliyokuwa imeharibika. Walikaa huko kwa mwezi mzima, wakihubiri kwa bidii katika eneo lote la Port Moresby na maeneo ya karibu. Mmoja wao aliyeitwa Frank Dewar, ambaye alikuwa mwanamume mwenye nguvu kutoka New Zealand, alitembea kuingia ndani zaidi ya kisiwa hicho kufikia umbali wa kilomita 50 hivi kutoka ufuoni akiwa amebeba mzigo mzito wa vitabu vya Biblia na kuwaachia wakazi wa eneo hilo.

Heni Heni Nioki, aliyekuwa mchawi wa kabila la Koiari alipata baadhi ya vichapo hivyo. Baada ya hapo, kweli za Biblia ambazo alijifunza zilikaa moyoni mwake zikisubiri Mashahidi wa Yehova warudi na kutia maji kilichokuwa kimepandwa.—1 Kor. 3:6.

Katika miaka ya mwishomwisho ya 1930, painia mwingine alishiriki katika kazi ya kuhubiri ya muda mrefu akifanya hivyo katika miji mikubwa ya Papua New Guinea, kutia ndani visiwa vya New Britain, New Ireland, na Bougainville. Aliacha vichapo vingi sana vya Biblia. Lakini kabla ya wengine kuendeleza kazi hiyo, eneo hilo lilihusika katika Vita vya Pili vya Ulimwengu.

KUHUBIRI KATIKA “KIJIJI KIKUBWA”

Katika Septemba 22, 1951, miaka 12 baadaye, Tom Kitto, Mwaustralia mrefu mwenye umri wa miaka 47, alitua kwa ndege huko Port Moresby, eneo lenye joto jingi na unyevunyevu. Alikuwa amekubali mwito uliowataka wajitoleaji waanze kuhubiri katika visiwa vya Pasifiki. Mke wake, Rowena, alijiunga naye majuma sita baadaye. Eneo lao lilikuwa nchi yote ya Papua New Guinea.

Kitto na mke wake walitambua kwamba watu wengi kutoka Ulaya walikuwa na ubaridi kuelekea ujumbe wa Ufalme. Kisha wakakutana na Geoff Bucknell, Mwaustralia mwenzao ambaye alikuwa amefifia kutoka kwenye kweli alipokuwa kijana. Geoff alikubali kujifunza na baadaye akawa Shahidi mwaminifu, pamoja na mke wake, Irene.

Kisha Tom na Rowena wakahamia Hanuabada, jina linalomaanisha “Kijiji Kikubwa” katika lugha ya wenyeji ya Motu. Kijiji hicho kilifika hadi kwenye Bandari ya Port Moresby na kilikuwa na mamia ya nyumba zilizotengenezwa juu ya nguzo za mbao na kuunganishwa na vijia virefu vya mbao vinavyofika hadi ufuoni. “Watu walituzunguka ili wasikilize habari njema,” anaandika Rowena. “Watu wengi sana walipendezwa hivi kwamba tulirudi kila jioni kuongoza mafunzo ya Biblia, tulikosa kurudi jioni mbili tu katika miezi miwili.” Tom anaongeza hivi: “Tumaini la ufufuo na kuishi katika paradiso duniani liliwavutia sana watu hawa. Wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo na polisi wa eneo hilo walijaribu kuwafanya waache kujifunza, lakini waliendelea kuwa imara. Kweli ilikuwa imeingia ndani sana ya mioyo yao.”

Raho na Konio Rakatani, Oda Sioni, Geua Nioki na mume wake, Heni Heni aliyekuwa amepata vichapo kutoka kwa wahubiri waliowasili katika mashua inayoitwa Lightbearer miaka 16 mapema, ni baadhi ya wale ambao walichukua msimamo imara kwa ajili ya kweli. Punde si punde, watu 30 hivi walikuwa wakihudhuria mikutano kwa ukawaida katika nyumba ya Heni Heni. “Wanaume waliketi upande mmoja na wanawake upande ule mwingine katika chumba hicho,” anakumbuka Oda Sioni, ambaye alikuwa kijana wakati huo. “Wanawake walivalia sketi za nyasi na hawakuwa na blauzi na waliwabeba watoto katika mifuko yenye kuvutia iliyofumwa kwa nyuzi na ilining’inizwa kwenye nguzo za chumba hicho. Baada ya kuwanyonyesha watoto, waliwatia ndani ya mifuko hiyo na kuibembeza polepole hadi watoto walipolala.”

Tom Kitto aliongoza mikutano hiyo akisaidiwa na mtafsiri. Nyakati nyingine mambo yalienda mrama. “Katika mkutano mmoja, ndugu ya Heni Heni, Badu Heni, alikuwa akitafsiri,” anaeleza Don Fielder, aliyefika huko katika mwaka wa 1953. “Mwanzoni ilionekana kwamba mambo yalikuwa shwari, kwa kuwa Badu alitafsiri maneno ya Tom na hata aliiga ishara zake. Baadaye tu ndipo Badu alimwambia Tom kuwa hakuelewa chochote ambacho alikuwa akisema. Alisema tu kweli alizokuwa amejua hapo awali na kuiga ishara za Tom ili ionekane kwamba hivyo ndivyo hotuba ilivyosema.” Licha ya hali hizo ngumu, kikundi hicho kilikua upesi, na baada ya muda kikundi cha pili kilianzishwa katika nyumba ya Raho Rakatani, ambayo pia ilikuwa kwenye kijiji cha Hanuabada.

“NJOO UWAFUNDISHE WATU WANGU”

Mapema katika mwaka wa 1952, Bobogi Naiori, chifu wa eneo la Koiari ambaye pia alikuwa mchawi maarufu, alimtembelea Heni Heni, kwani alikuwa wantok wake, au mtu wa kabila lake, na akahudhuria mkutano katika nyumba yake. Kwa kuwa alivutiwa na mambo aliyoona na kusikia, baadaye Bobogi alimwendea Tom Kitto na kumsihi: “Tafadhali, njoo uwafundishe watu wangu kuhusu kweli!”

Muda mfupi baadaye, Tom na Rowena walisafiri kwa gari lao kuukuu kupitia barabara za udongo kufika nyumbani kwa Bobogi huko Haima, kijiji kidogo kilicho umbali wa kilomita 25 hivi kaskazini ya Port Moresby. Tom aliwahubiria wanakijiji waliokuwa wamekusanyika na Bobogi akatafsiri. Kuanzia wakati huo, watu 30 hivi wakaanza kujifunza Biblia.

Baadaye katika mwezi huo, kikundi kilichokuwa huko Haima kilijenga jumba dogo kwa ajili ya mikutano ya Kikristo. “Jumba hilo lilikuwa na kiunzi cha mbao, paa lililoezekwa kwa nyasi, na kuta zilizofika kiunoni zilizofumwa kwa mianzi,” anakumbuka Elsie Horsburgh ambaye baadaye alihudhuria mikutano huko. “Ndani kulikuwa tu na viti vya mbao, taa ya mafuta, na ubao mweusi mdogo.” Jengo hilo la hali ya chini likawa Jumba la Ufalme la kwanza nchini Papua New Guinea.

Bobogi alitaka watu wa kabila yake walioishi katika milima ya karibu wasikie habari njema. Kwa hiyo, yeye na Tom walitembea kwenye barabara iliyokuwa kwenye mwinuko mkali hadi kwenye uwanda wa juu wa Sogeri. Baada ya muda mfupi walikuwa wakijifunza na zaidi ya watu 90 katika vijiji vitatu huko.

Utendaji kama huo haungekosa kuonwa na wenye mamlaka. Huko Ioadabu, ofisa wa serikali aliingia mahali ambapo mikutano ilikuwa ikifanyiwa na kuamuru aelezwe ni nani aliyekuwa amewaruhusu Mashahidi wa Yehova kuwafundisha wanakijiji. Pia polisi waliwahoji baadhi ya watu wanaopendezwa kuhusu kazi yetu. Makasisi fulani wa kijiji na wamiliki wa mashamba waliwatisha akina ndugu kwamba watawaumiza.

Chini ya hali hizo zenye mkazo, baadhi ya watu wanaopendezwa waliacha kujifunza. Hata hivyo, wachache walisimama imara. Mnamo 1954, ubatizo wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova kufanywa nchini Papua New Guinea ulifanywa katika Mto Laloki huko Haima, na wanafunzi 13 wa Biblia wakabatizwa. Mmoja wao alikuwa Bobogi, ambaye alisema hivi: “Hata ikiwa watu wote wa Koiari wataacha kweli, mimi sitafanya hivyo, kwa sababu ninajua hii ndiyo kweli.” Kupatana na maneno yake, Bobogi alidumisha utimilifu wake, akitumika kwa uaminifu akiwa mzee katika Kutaniko la Haima hadi alipokufa katika mwaka wa 1974.

MAKUSANYIKO YASIYOSAHAULIKA

Mnamo Julai 1955, John Cutforth, mmishonari Mkanada aliyekuwa akitumika huko Australia, aliwasili Port Moresby na kuwa mwangalizi wa kwanza wa mzunguko. Mara moja, John alipenda eneo hilo, utamaduni, na watu wake. Hakujua kwamba angetumika nchini Papua New Guinea kwa zaidi ya miaka 35.

John alifika akiwa na sinema inayoitwa The New World Society in Action, masimulizi yaliyoonyesha utaratibu wa tengenezo na makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Wakati wa ziara yake ya majuma matatu, alionyesha sinema hiyo mara 14 nyakati nyingine mbele ya mamia ya wahudhuriaji au hata mbele ya watu 2,000 hivi. Watu wengi sana waliifurahia, hiyo ikiwa mara ya kwanza kwa wengine wao kutazama sinema yoyote.

Ziara ya John ilifikia mwisho wakati wa kusanyiko la mzunguko la siku moja huko Haima. “Wanaotaka kubatizwa walipoombwa wasimame, . . . watu 70 walisimama!” anakumbuka Tom Kitto. “Mioyo yetu ilijawa na shangwe tulipoona ndugu 40 na dada 30 wakisimama msituni kwenye ukingo wa mto wakiwa tayari kuonyesha wakfu wao kwa Yehova.”

Mwaka uliofuata, akina ndugu walipanga kuwa na kusanyiko la pili la mzunguko huko Haima. Bobogi, chifu wa kijiji, alipewa mgawo wa kutayarisha mahali pa kusanyiko na chakula kwa ajili ya wote waliotazamiwa kuhudhuria. Siku tatu kabla ya kusanyiko, John (Ted) Sewell, mwangalizi mpya wa mzunguko kutoka Australia, alikutana na Bobogi kuzungumzia matayarisho hayo.

“Umejenga nini?” akauliza Ted moja kwa moja.

“Hakuna,” Bobogi akamjibu.

“Bobogi, leo ni Alhamisi (Siku ya 4) na kusanyiko ni Jumapili!” Ted akasema kwa mshangao.

“Ni kweli, ndugu,” akajibu Bobogi. “Tutatayarisha kila kitu Jumamosi.”

Ted alishangaa na kurudi Port Moresby akiwa na uhakika kwamba hakutakuwa na utaratibu wowote katika kusanyiko hilo.

Jumapili hiyo alielekea Haima akiwa na wasiwasi kuona ni nini ambacho kingetukia. Kulikuwa na mabadiliko makubwa kama nini! Chini ya mti mkubwa kulikuwa na jukwaa la mbao mbele ya eneo kubwa lililokuwa limefyekwa. Mbali kidogo kulikuwa na maeneo ya kupikia, ambako nguruwe, wallaby, mbawala, hua, samaki, viazi vikuu, na viazi vitamu vilikuwa vikichomwa. Birika za chai zilikuwa zikichemka. Watu walichangamana kwa furaha katika eneo la kula lililotengenezwa kwa vifaa vilivyopatikana msituni. Bobogi alisimama katikati ya hekaheka hizo zote, bila wasiwasi wowote. Ted alistaajabu sana!

“Bobogi, ulijifunzia wapi kufanya mambo haya yote?” akamwuliza.

“Oh, niliona mambo yote haya katika sinema ile ambayo John Cutforth alituonyesha mwaka uliopita,” Bobogi akajibu.

Zaidi ya watu 400 kutoka katika makabila manane walihudhuria kusanyiko hilo, na 73 wakabatizwa. Miaka iliyofuata, kusanyiko hilo likaja kuitwa kusanyiko la Bobogi.

KUTUMIA PICHA KUHUBIRI

Mnamo 1957, John Cutforth alihamia kabisa Papua New Guinea na kuwa mwangalizi anayesafiri huko. Tangu ziara yake ya kwanza, alikuwa amefikiria sana njia bora zaidi ya kuwahubiria wenyeji, kwa kuwa wengi wao hawakujua kusoma na kuandika. Sasa alikuwa tayari kutumia mbinu yake.

Alipokuwa akitoa hotuba mbele ya kutaniko au kikundi cha mbali, John aliandika jina lake na la mtafsiri kwenye ubao mweusi. Kisha, akaelekeza kidole mbinguni, na kuwauliza wasikilizaji, “Mungu, jina lake nani?” Akaandika jibu lao, “Yehova” na “Zaburi 83:18” juu ya ubao huo. Chini yake upande wa kushoto, aliandika kichwa “Ulimwengu wa Kale” na kuchora wanaume wawili wakipigana, mtu akilia, kaburi, na “Waroma 5:12.” Upande wa kulia, akaandika kichwa “Ulimwengu Mpya” na kuchora wanaume wawili wakisalimiana kwa mikono, mtu akitabasamu, kaburi lililofutwa, na “Ufunuo 21:4.” Baadaye, alitoa hotuba yenye kusisimua ili kueleza michoro yake. Kisha akawakaribisha wasikilizaji wasimame mbele na kurudia hotuba yake. Walipokuwa wameelewa, aliwaambia wachore picha hizo kwenye karatasi na kuzitumia katika kazi ya kuhubiri.

Mahubiri hayo yaliyokuja kuitwa “Mahubiri ya Kwanza ya Picha” yalikuwa na matokeo makubwa sana katika kazi ya kuhubiri nchini Papua New Guinea. Mahubiri mengine ya picha yalifuata. “Tulitumia saa nyingi kunakili picha hizo za mahubiri kwenye vitabu vya kuandikia shuleni. Kila mwanafunzi wa Biblia alipata nakala ambayo alitumia kuwafundisha wengine,” anasema Lena Davison aliyetumika katika nchi hiyo kwa miaka 47. Watoto walichora picha kwenye vitabu vyao na wakafurahia sana kuvipaka rangi.

Mbinu hiyo ya kufundisha ilitumiwa pia katika mikutano ya kutaniko. “Michoro kwenye ubao ilitumiwa sana wakati wa Mikutano ya Watu Wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi, na hilo likawasaidia sana wale ambao hawakujua kusoma,” anaeleza Joyce Willis, painia kutoka Kanada aliyekaa zaidi ya miaka 40 nchini Papua New Guinea. Mahubiri ya picha yaliyochorwa juu ya turubai yalitumiwa pia katika makusanyiko. “Picha hizo kubwa zilipendwa sana na zilikazia mafundisho muhimu katika akili za wasikilizaji,” anasema Mike Fisher aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko huko. “Picha nyingi kati ya hizo ziliishia katika nyumba za wahubiri waliokuwa katika maeneo ya mbali, ambao walizitumia kuwahubiria wageni.”

Miaka mingi baadaye, watu wengi zaidi walipojifunza kusoma na kuandika na vichapo vyenye picha vikapatikana kwa wingi, mahubiri ya picha yakaacha kutumiwa.

KUPANUA KAZI YA KUHUBIRI

Mwishoni mwa miaka ya 1950, Waaustralia wengi wenye bidii walihamia Papua New Guinea, wakiwa na hamu ya kuhubiri habari njema. Zaidi ya hilo, watu wengi waliojifunza kweli huko Port Moresby walirudi kwenye vijiji vyao wakiwa na ujumbe wa Ufalme. Kwa hiyo, habari njema ikaenea upesi kote nchini.

Mnamo 1957, David Walker, ndugu Mwaustralia mwenye umri wa miaka 26 aliyekuwa akiishi huko Port Moresby, alisikia kwamba watu katika kijiji jirani cha Manu Manu na katika eneo la Gabadi walikuwa wanapendezwa na kweli. David aliacha kazi yake, akaanza kufanya upainia wa pekee, na akahubiri katika eneo hilo kwa mwaka mzima akiwa peke yake. Wengine waliendeleza alipoachia, na sasa kuna kutaniko na Jumba la Ufalme huko Manu Manu.

Wakati huohuo, Don Fielder alikutana na wavuvi kadhaa waliopendezwa na kweli alipokuwa akihubiri kwenye soko la Koki huko Port Moresby. Wanaume hao walikuja kutoka Hula, kijiji cha pwani karibu kilomita 100 upande wa mashariki. Ili kuwasaidia wao na familia zao, Don, pamoja na Athol (Dap) Robson na watu wengine wenye kupendezwa waliokuwa wenyeji wa Hula, walielekea huko kwa kutumia mtumbwi mpya wa Don wenye urefu wa mita 8. Walikaa huko Hula kwa siku tatu na kuanzisha kikundi kidogo cha kujifunza.

Muda mfupi baadaye, Don alihamia Hula na akatumika akiwa painia wa pekee pamoja na mke wake Shirley, na binti yao Debbie mwenye umri wa miaka miwili. “Tulijenga nyumba ndogo na kuanza kuhubiri katika vijiji vitano vya eneo hilo,” anaeleza Don. “Hilo lilihusisha kutembea umbali wa kilomita 12 kwenda na kurudi kila siku. Ilikuwa kazi yenye kuchosha lakini ilituburudisha kiroho kwani tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia na punde tukawa na wahubiri wapya wanane waliohubiri pamoja nasi.”

Kazi ya kuhubiri ya Don na Shirley ilimkasirisha sana kasisi wa Kanisa la United la eneo hilo, ambaye alimshinikiza mwenye shamba awaamuru waondoe nyumba yao kutoka kwenye shamba lake. “Watu wa kijiji cha karibu waliposikia jambo hilo, walikasirika sana kwa sababu hawakutaka tuondoke,” anasema Don. “Watu 20 hivi walitusaidia kuhamisha nyumba yote kutia ndani msingi wake, hadi kwenye shamba lingine lililokuwa la kijiji chao.”

Kasisi huyo aliyekasirika hakukata tamaa. Alijitahidi kuwashinikiza wenye mamlaka wa Port Moresby watupige marufuku tusijenge nyumba yetu popote katika wilaya hiyo. “Badala ya kuondoka katika mgawo wetu,” anasema Don, “tulimwomba Alf Green, fundi stadi wa mbao, achukue mbao za nyumba hiyo yetu na kujenga chumba kidogo juu ya mtumbwi wetu. Kisha tukatia nanga katika kinamasi cha mikoko karibu na mlango wa mto uliokuwa karibu. Tuliishi na kufanya upainia tukiwa mahali hapo penye mbu wengi na mamba kwa miaka miwili na nusu iliyofuata.” Binti yao wa pili Vicki alipozaliwa, Don na familia yake walirudi Port Moresby. Baadaye walitumika katika kazi ya mzunguko, na Don akatumika kwenye Halmashauri ya Tawi.

WENGINE WASIKIA HABARI NJEMA

Kufikia wakati huo, huko Port Moresby, Lance na Daphne Gosson walianza kujifunza na vijana kadhaa waliotoka kwenye kijiji cha pwani cha Kerema kilichoko kilomita 225 hivi magharibi ya Port Moresby. Wanaume hao waliporudi nyumbani kwa ajili ya likizo, Lance na Jim Chambliss waliamua kuwatembelea kwa majuma mawili na hivyo kufikisha habari njema huko Kerema.

“Kijiji chote kilikusanyika ili kutusikiliza,” akaandika Lance. “Wakati tulipokuwa tukizungumza, kasisi wa Sosaiti ya Wamishonari ya London aliingia ghafula na kumshambulia mtafsiri wetu na kumpiga ngumi mara kadhaa kabla ya wanakijiji kumzuia. Alisisitiza kwamba watu wa eneo hilo hawakutaka tuwe katika eneo lao na akatuamuru tuondoke eneo ‘lake.’ Basi tukasema kwamba wale waliotaka kutusikiliza watufuate hadi upande ule mwingine wa kijiji, na wale wengine wabaki naye. Kijiji chote kilitufuata.

“Asubuhi iliyofuata, tulienda kumwona mkuu wa wilaya ili turipoti kile kilichokuwa kimetendeka. Njiani tulikutana na mwanamke aliyekuwa mgonjwa sana. Tulimwambia kwamba tungempeleka hospitali, lakini aliogopa kwenda. Baada ya kumbembeleza sana alikubali kuandamana nasi. Tulimwacha na daktari kisha tukaenda kumwona mkuu wa wilaya ambaye kwa wazi hakufurahi kutuona. Hata alitushtaki kwa ukali kwamba tuliwafundisha watu wasikubali matibabu! Hata hivyo, wakati huohuo daktari yule wa hospitali aliingia na kumsikia akitushtaki hivyo. Alimwambia mkuu huyo kwamba tulikuwa tumemsadikisha mwanamke mgonjwa aende hospitalini akatibiwe. Kwa kupendeza, mkuu huyo aliomba msamaha mara moja. Alituambia kwamba kasisi Mkatoliki wa eneo hilo alikuwa amemtembelea na kumwambia uwongo kuhusu imani yetu. Alitupa polisi wawili waliojihami watulinde ili tusishambuliwe tena. Ilikuwa ajabu kwetu kuwa na polisi wawili wenye bunduki wakiketi pamoja nasi katika mafunzo yetu ya Biblia!”

Punde tu baada ya hapo, Waaustralia wawili vijana, Jim Smith na Lionel Dingle, walipewa mgawo wa kwenda Kerema kuwa mapainia wa pekee. Mara moja walianza kujifunza Kitairuma, lugha ya eneo hilo. “Tulisema neno katika lugha ya Motu, na wanafunzi wetu wa Biblia walituambia neno linalopatana nalo katika Kitairuma nasi tukaliandika,” anaeleza Jim. “Kwa njia hiyo, tulikuwa na maneno kadhaa ambayo yalitusaidia kufanyiza msamiati uliotusaidia kutoa utangulizi rahisi wa habari za Biblia. Watu wa eneo hilo walishangaa kutusikia tukizungumza lugha yao, kwa kuwa hakuna mzungu yeyote katika wilaya yote ambaye angeweza kufanya hivyo. Baada ya miezi mitatu tulikuwa tukiongoza mikutano ya kila juma katika Kitairuma pande zote za Ghuba ya Kerema.”

Baadaye, painia mwingine kijana kutoka Australia, Glenn Finlay, alichukua mahali pa Jim na Lionel na akahubiri peke yake kwa miezi 18 huko Kerema. “Ulikuwa wakati mgumu sana kwangu,” anasema Glenn, “na nyakati nyingine nilijiuliza ikiwa nilikuwa nikitimiza jambo lolote kupitia kazi yangu. Lakini tukio fulani lenye kunyenyekeza lilibadili maoni yangu.

“Mmoja wa wanafunzi wangu wa Biblia alikuwa mzee anayeitwa Hevoko, aliyekuwa mwokaji katika kijiji hicho. Hakujua kusoma wala kuandika na baada ya miezi kadhaa alikuwa ameelewa kweli chache tu za msingi. Nilijiuliza ikiwa kulikuwa na faida yoyote kumfundisha. Kisha asubuhi moja, nilipokaribia nyumba yake, nilisikia sauti yake na nikasimama ili nisikilize. Hevoko alikuwa akisali kwa sauti kwa Yehova, akimshukuru kutoka moyoni kwa sababu amemfundisha ukweli kuhusu jina na Ufalme wake. Sala hiyo ya unyoofu ilinikumbusha kwamba Yehova hutazama mioyo ya watu, si akili. Anajua vizuri ni nani wanaompenda.”—Yoh. 6:44.

KUKABILIANA NA MADHEHEBU YA WAABUDU-MALI

Mnamo 1960, mapainia wa pekee wengine wawili kutoka Australia, Stephen Blundy na Allen Hosking, walihamia kijiji cha Savaiviri kilichoko kilomita 50 hivi mashariki ya Kerema. Baada ya kuishi katika hema kwa miezi mitatu, Stephen na Allen walihamia katika nyumba ndogo ya msituni iliyokuwa katika shamba la minazi lililozungukwa na kinamasi kikubwa.

Savaiviri lilikuwa eneo linalojulikana sana kwa sababu ya madhehebu yake ya waabudu-mali. Madhehebu hiyo ilianza jinsi gani? Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, wenyeji walistaajabishwa na utajiri, au mali, ambazo askari-jeshi wageni walikuwa nazo. Kisha vita vilikwisha, na wanajeshi wakafunga virago vyao na kuondoka. Wanakijiji fulani walisema kwamba kwa kuwa mali hizo zilikuwa zimetoka mbali sana mahali wasipoweza kuona—kwa kuwa wanaamini kuwa pepo wanaishi mahali pasipoonekana—basi mababu zao waliokufa walikuwa wakiwatumia mali hizo lakini wanajeshi hao ndio waliokuwa wakizuia. Ili kuwajulisha pepo uhitaji wao, watu waliigiza vita na kujenga gati zenye nguvu ili kujitayarishia kwa ajili ya siku hiyo tukufu wakati ambapo mali mpya zingefika.

Baada ya muda, Stephen na Allen walikuwa wakijfunza na washiriki 250 hivi wa madhehebu hiyo, kutia ndani kiongozi wao na baadhi ya “mitume kumi na wawili” wake. “Wengi kati ya watu hao walikubali kweli,” anasema Stephen. “Kwa kweli, ofisa mmoja wa serikali alituambia baadaye kwamba kazi yetu ya kuhubiri iliwasaidia sana kumaliza madhehebu hiyo ya waabudu-mali huko Savaiviri.”

KUCHAPISHA VICHAPO VYA BIBLIA

Upesi mapainia hao wa zamani waliona umuhimu wa kutafsiri vichapo vya Biblia katika lugha za eneo hilo. Lakini, wangeweza jinsi gani kuchapisha vichapo katika lugha 820 tofauti-tofauti?

Mnamo 1954, Tom Kitto alichukua hatua ya kwanza kwa kupanga akina ndugu wenyeji watafsiri sura moja ya kitabu “Let God Be True”c katika lugha ya Motu, ambayo ndiyo lugha ya eneo la Port Moresby. Zaidi ya nakala 200 za sura hiyo yenye kichwa “Dunia Mpya” zilisambazwa zikiwa kama vijitabu, na watu wengi sana waliozungumza Kimotu walifurahi sana.

Maeneo mapya yalipofunguka, mapainia walifanya kazi ngumu na kwa muda mrefu kutafsiri vichapo katika lugha nyingine za kienyeji. Jim Smith anaeleza hivi: “Kwa kuandika maneno mapya, nilifanya kazi kubwa sana kutokeza kamusi ya Kitairuma na maandishi kuhusu sarufi, ambayo tulitumia kutafsiri makala za funzo la Mnara wa Mlinzi. Mara nyingi nilifanya kazi hadi usiku nikipiga chapa makala zilizotafsiriwa ili kuwapa watu watakaohudhuria mikutano. Baadaye nilitafsiri trakti na kijitabu katika Kitairuma. Vichapo hivyo vya mapema viliwasaidia watu wengi wa Kerema kujifunza kweli.”

Vichapo vingine vilitokezwa katika Kihula na Kitoaripi. Kwa kuwa ilikuwa vigumu sana kuchapisha vichapo katika kila lugha, akina ndugu walikazia fikira zao kwenye lugha mbili zilizotumiwa katika biashara—Hiri Motu na Tok Pisin. Hiri Motu, ni lugha ya Motu iliyorahisishwa, ambayo ilizungumzwa na watu wengi wanaoishi kwenye pwani ya Papua. “Tulifanya kazi nyingi ya kuboresha maandishi ya lugha hiyo,” anasema Don Fielder. “Kwa kweli, Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vya Kihiri Motu vilisaidia sana kuboresha lugha hiyo ili iweze kueleweka leo.” Kitok Pisin—mchanganyiko wa Kiingereza, Kijerumani, Kikuanua, na lugha nyingine—kinazungumzwa na watu wengi katika nyanda za juu, maeneo ya pwani, na visiwani upande wa kaskazini mwa Papua New Guinea. Kazi ya kuhubiri ilianza jinsi gani katika eneo hilo kubwa?

KAZI YA KUHUBIRI YAENEA KASKAZINI

Mnamo Juni 1956, Ken na Rosina Frame, mapainia waliokuwa wametoka tu kuoana walikuwa Mashahidi wa kwanza kuhamia New Ireland, kisiwa kimoja kati ya Visiwa vya Bismarck vilivyoko kaskazini-mashariki mwa Papua New Guinea. Ken, aliyekuwa mhasibu, alifanya kazi katika kampuni kubwa huko Kavieng, mji mkuu wa kisiwa hicho. “Kabla ya kuondoka Sydney,” Ken anaeleza, “tulishauriwa kwamba tuwaache watu watuzoee kabla ya kuanza kuhubiri hadharani. Rosina alikuwa mshonaji stadi wa nguo na baada ya muda mfupi alikuwa na wateja wengi. Tuliwahubiria kwa njia isiyo rasmi, na baada ya muda kukawa na kikundi kidogo cha watu waliopendezwa ambao walikutana kwa siri nyumbani kwetu mara moja kwa juma.

“Miezi 18 baadaye, mwangalizi wa mzunguko, John Cutforth, alitutembelea na kuuliza ikiwa angeonyesha sinema yenye kichwa The Happiness of the New World Society. Nilizungumza na mmiliki wa jumba la sinema, naye akakubali kuonyesha sinema yetu ya bila malipo. Lazima wafanyakazi wake waliwaambia watu wengine kuhusu sinema hiyo kwani tulipofika kwenye jumba hilo, lango lake lilikuwa limejaa watu, na tulihitaji msaada kutoka kwa polisi ili tufaulu kuingia ndani. Zaidi ya watu 230 walikuja kuitazama, bila kuhesabu watu waliochungulia kwenye madirisha yaliyokuwa wazi. Baada ya hapo tulihubiri waziwazi.”

Mnamo Julai 1957, kutaniko lilianzishwa huko Rabaul, New Britain, mji maridadi wa bandarini uliokuwa katikati ya milima miwili ya volkano hai. Kutaniko la Rabaul lilikutana nyuma ya nyumba iliyokodishwa na mapainia wa pekee. “Zaidi ya watu 100 walikuja kwenye nyumba hiyo kila usiku ili kujifunza Biblia,” anasema painia Norm Sharein. “Tuliwapanga katika vikundi vya watu 20 hivi na kuwafundisha kwa kutumia taa za mafuta chini ya miti.”

Kutaniko lilipokuwa na kusanyiko la kwanza la mzunguko, watu saba walibatizwa ufuoni. Mara moja watano kati yao wakawa mapainia. Lakini ni wapi ambapo wangetumika vizuri zaidi? Ofisi ya tawi ya Australia ilitoa jibu—Madang.

Huko Madang, mji ulioko kaskazini-mashariki mwa pwani, “mashamba” yalikuwa tayari kuvunwa. (Yoh. 4:35) Kwa kweli, kikundi hicho kidogo cha wahubiri hakingeweza kushughulikia watu wote waliopendezwa. Painia Mkanada Matthew Pope na familia yake walipofika na kununua nyumba yenye vyumba kadhaa upande wa nyuma, njia ilifunguka ya kuwatuma mapainia wengi zaidi huko.

Mapainia wanane waliwasili kutoka Rabaul na wakaishi katika sehemu mbalimbali za Wilaya ya Madang. Mmoja wao, Tamul Marung, alinunua baiskeli na kusafiri kwa kutumia mashua hadi Basken, kijiji cha nyumbani kwao, kilomita 48 kaskazini ya Madang. Baada ya kuhubiri huko Basken, alipanda baiskeli yake na kurudi Madang, akihubiri njiani. Kisha alirudi Basken, akaanzisha kutaniko, na kufanya upainia kwa miaka mingine 25. Katika kipindi hicho, alioa na akapata watoto. Baadaye, binti na mpwa wake wa kike walitumika Betheli.

Wakati huo, huko Madang, John na Lena Davison walikutana na Kalip Kanai, mwalimu wa shule katika kijiji kidogo cha Talidig, kilichoko katikati ya Basken na Madang. Baada ya muda, John na Lena walikuwa wakisafiri hadi Talidig wakajifunze na Kalip na watu wake wa ukoo. Hilo lilimkasirisha mkaguzi wa shule aliyekuwa Mkatoliki, naye akawaamuru polisi wamfukuze Kalip na watu wake wa ukoo kutoka nyumbani kwao. Bila kuvunjika moyo, kikundi hicho kilihamia katika kijiji cha karibu cha Bagildig, na mwishowe kikawa kutaniko kubwa. Baadaye walijenga Jumba kubwa la Ufalme ambalo lilitumiwa kwa ajili ya makusanyiko. Sasa kuna makutaniko saba na vikundi viwili katika Wilaya ya Madang.

Huku maendeleo yakitukia huko Madang, Jim Baird pamoja na John na Magdalen Endor walikuwa wakipata matokeo mazuri huko Lae, mji mkubwa wa pwani ulioko kilomita 210 hivi upande wa kusini-mashariki. “Tulijifunza na watu wengi nyumbani kwetu kila usiku. Baada ya miezi sita wanafunzi kumi wa Biblia waliandamana nasi katika utumishi,” anakumbuka John. Baadaye katika mwaka huo zaidi ya watu 1,200 walihudhuria maonyesho ya sinema yenye kichwa The New World Society in Action iliyoonyeshwa katika jumba la sinema la Lae. Wengi waliohudhuria walikuwa vibarua ambao walipeleka habari njema waliporudi kwenye vijiji vyao vya mbali vya milimani.

Ndani zaidi kutoka Lae, wahubiri wenye bidii walikuwa wakifanya kazi nzuri. Huko Wau, Jack Arifeae, mwenye mwili mkubwa na aliyekuwa na bidii nyingi ya kumtumikia Yehova, alianzisha kutaniko nyumbani kwake. Watu 30 hivi wa kabila la Kukukuku—ambalo wakati fulani liliogopwa kwa kula nyama ya wanadamu—walikuwa wakijifunza Biblia na kufanya maendeleo ya kiroho.

Wakati huohuo, katika eneo jirani la Bulolo, Wally na Joy Busbridge walihubiri kwa bidii hivi kwamba wasimamizi wa Misheni ya Makabila Mapya wakakasirika, kwa kuwa waliona eneo hilo kuwa miliki yao. Kwa sababu ya kushinikizwa na kanisa hilo, mwajiri wa Wally alimwambia, “Uache dini yako, au utafute kazi nyingine.” Wally na Joy walihamia Lae na wakaendelea kuhubiri. Baadaye walianza utumishi wa wakati wote na wakatumika katika kazi ya kuzunguka kwa miaka mingi.

Popondetta, mji mdogo ulio kusini-mashariki ya Lae, ulihubiriwa habari njema na Jerome na Lavinia Hotota ambao walirudi kwenye mkoa wa nyumbani kwao kutoka Port Moresby. Jerome alikuwa na bidii sana na alitumia Maandiko kwa ushawishi, naye Lavinia alikuwa mwanamke mwenye fadhili ambaye alipendezwa sana kibinafsi na wengine. Kama ilivyotarajiwa, walipoanza tu kuhubiri askofu Mwanglikana pamoja na wengi wa wafuasi wake walifika nyumbani kwao na kuwaambia waache. Lakini Jerome na Lavinia hawakutishika. Waliendelea kuhubiri na wakaanzisha kutaniko dogo lenye bidii.

Kufikia mwaka wa 1963, habari njema ilikuwa imehubiriwa hadi Wewak, mji ulio mbali kwenye pwani ya kaskazini ya Papua New Guinea. Karl Teynor na Otto Eberhardt, wajenzi wawili Wajerumani, walijenga hospitali ya Wewak mchana na wakajifunza na zaidi ya watu 100 wakati wa jioni na miisho ya juma. Kazi yao ya kuhubiri ilimkasirisha sana kasisi Mkatoliki wa eneo hilo hivi kwamba akakusanya umati wenye ghasia na kutupa pikipiki za Karl na Otto baharini. Mtu mmoja aliyeshirikiana na kasisi huyo, kiongozi mashuhuri wa kijiji, alikuwa na mwana ambaye baadaye alikuja kuwa Shahidi. Kwa sababu ya kuvutiwa na mabadiliko aliyoona katika maisha ya mwana wake, mtazamo wa mtu huyo ulibadilika naye akawaruhusu Mashahidi wahubiri katika vijiji vilivyokuwa chini ya udhibiti wake.

OFISI YA TAWI INAANZISHWA

Huku makasisi wakijaribu kuwadhibiti Mashahidi, akina ndugu walichukua hatua za “kuithibitisha kisheria habari njema” kwa njia kubwa. (Flp. 1:7) Kwa sababu hiyo, Mei 25, 1960, shirika la International Bible Students Association, linalotumiwa kisheria na Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingi, liliandikishwa rasmi na serikali. Hilo liliwawezesha akina ndugu kupata ardhi ya serikali ambayo wangeweza kujenga Majumba ya Ufalme na majengo mengi ambayo yanahitajika ili kutegemeza kazi ya Ufalme.

Baadaye katika mwaka huo, ofisi ya tawi ya Watch Tower Society ilianzishwa pia huko Papua New Guinea. John Cutforth aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa ofisi ya tawi. Hata hivyo, kwa kuwa hakukuwa na maeneo mengi ya kukodi, ofisi hiyo ingekuwa wapi?

Jibu lilipatikana wakati Jim na Florence Dobbins walipowasili. Jim alikuwa ametumika kwenye Jeshi la Wanamaji la Marekani huko Papua New Guinea wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Baadaye, Jim na Florence walijifunza kweli na wakajiwekea mradi wa kupanua utumishi wao. “Mnamo 1958, ndugu kutoka Port Moresby alitutembelea nyumbani kwetu huko Ohio na kutuonyesha picha za Papua New Guinea,” anaeleza Jim. “Baadaye tuligundua kwamba alikuwa ameacha picha moja bila kujua. Picha hiyo ilikuwa na mandhari maridadi zaidi ambazo tumewahi kuona. ‘Tutamtumia picha hiyo,’ mke wangu akasema. Lakini mimi nikamwambia, ‘Hapana, acha tumpelekee.’”

Mwaka mmoja baadaye, Jim na Florence, pamoja na binti zao, Sherry na Deborah, walihamia kwenye nyumba ndogo ya mawe huko Six Mile, katika eneo la Port Moresby. Muda mfupi baada ya hapo, Jim akaanza kuzungumza na John Cutforth kuhusu mahali ambapo ofisi ya tawi ingekuwa.

“Nimetafuta kila mahali huku Port Moresby ambapo tunaweza kuwa na ofisi ya tawi, lakini hakuna sehemu inayopatikana,” akasema John.

“Namna gani nyumba yetu?” Jim akamwambia. “Mnaweza kutumia vyumba vitatu vya mbele, na mimi na familia yangu tutaishi nyuma.”

Mipango ilifanywa, na Septemba 1, 1960, nyumba ya akina Dobbin ikaandikishwa kisheria kuwa ofisi ya tawi ya kwanza nchini Papua New Guinea.

‘WAPIGENI MARUFUKU MASHAHIDI’

Wapinzani wetu hawakufurahia maendeleo hayo. Kuanzia 1960 na kuendelea, muungano wa makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo, shirika la kuwategemeza wanajeshi waliostaafu na wanajeshi wengine wa Australia (Returned Services League, RSL), na vyombo vya habari vilianza kampeni iliyopangwa ya kuwavunjia heshima na kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova.

Mambo yalifikia kilele wakati ambapo karatasi iliyochapishwa kuhusu msimamo wetu juu ya kutiwa damu mishipani iliposambazwa kwa madaktari, makasisi, na maofisa wa serikali. Kama kawaida, makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo ndio waliokuwa wa kwanza kusema. Agosti 30, 1960, gazeti South Pacific Post lilikuwa na kichwa “Makanisa Yakasirishwa na Suala la Damu.” Katika makala inayokuwa ndani, viongozi wa kanisa walisema kuwa Mashahidi ni “wapinga-Kristo [na] maadui wa Kanisa.”

Makala zilizofuata zilidai kwa uwongo kwamba Mashahidi wa Yehova ni wachochezi na kwamba mafundisho yao yaliwachochea watu wasiende shuleni, wasilipe kodi, wajiunge na madhehebu ya waabudu-mali, na wasidumishe usafi. Ripoti nyingine za uwongo ziliwashtaki kwa kutumia vibaya kupatwa kwa jua ili kuwaogopesha na “kuwadhibiti wenyeji wasio na elimu.” Gazeti moja hata liliwazomea Mashahidi kwa “kuishi, kula, na kufanya kazi pamoja na wanakijiji.” Gazeti South Pacific Post liliwachambua kwa kufundisha kwamba “watu wote wako sawa” na likadai kwamba Mashahidi ni “tisho kubwa kuliko Ukomunisti.”

Mwishowe, Machi 25, 1962, RSL iliwaomba wenye mamlaka wakoloni wawapige Mashahidi marufuku. Hata hivyo, serikali ya Australia ilikataa waziwazi ombi hilo. “Tangazo hilo lilikuwa na matokeo mazuri katika nchi yote,” anasema Don Fielder. “Watu wenye akili zilizofunguka wangeweza kuona kwamba madai ya wapinzani hayakuwa ya kweli.”

KUHUBIRI KWENYE NYANDA ZA JUU

Katika mwezi huohuo, Tom na Rowena Kitto walitoka Port Moresby na kufunga safari ngumu ya majuma kadhaa. Walikuwa wakielekea maeneo ambayo hayajahubiriwa kwenye nyanda za juu za New Guinea.

Miaka 30 mapema, Waaustralia waliokuwa wakitafuta dhahabu waliingia kwenye nyanda hizo na kugundua karibu watu milioni moja ambao hawakuwa wamewahi kuwasiliana na sehemu nyingine za dunia. Wenyeji hao waliopigwa na butwaa walidhani wanaume hao wazungu walikuwa roho za mababu wao waliokuwa wamefufuka.

Baada tu ya watu hao waliokuwa wakitafuta dhahabu, wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walifuata. “Wamishonari hao waliposikia kwamba tunaenda huko, waliwaamuru wanakijiji wasitusikilize,” anasema Rowena. “Lakini onyo lao lilitusaidia sana. Watu hao wa nyanda za juu—ambao kwa kawaida ni wadadisi—walikuwa wakitusubiri kwa hamu tufike.”

Tom na Rowena walifungua duka dogo huko Wabag, kilomita 80 kaskazini-magharibi ya mji wa Mlima Hagen. “Makasisi waliwaagiza wafuasi wao wasinunue chochote kutoka kwetu, wasituuzie, au hata kuzungumza nasi na wakawashinikiza waombe tunyang’anywe ardhi yetu,” anasema Tom. “Hata hivyo, baada ya muda, wanakijiji hao waliona kwamba tulikuwa tofauti na wazungu wengine ambao waliwafahamu. Jambo lililoonekana wazi ni kwamba tuliwatendea kwa fadhili. Kwa kweli, mara nyingi matendo yetu ya fadhili yaliwafanya walie machozi na wakasema kwamba walitaka tuendelee kuishi huko!”

KUHUBIRI KWA SUBIRA KUNALETA MATOKEO

Kuanzia mwaka wa 1963 na kuendelea, Mashahidi kutoka nchi nyingine walihamia kwenye nyanda za juu ili kusaidia katika upanuzi wa kazi ya kuhubiri. Wakisonga polepole kutoka mashariki hadi magharibi, hao akina ndugu na dada walihubiri katika eneo lote, wakianzisha vikundi na makutaniko katika maeneo mengi.

Huko Goroka, kwenye Mkoa wa Nyanda za Juu za Mashariki, kutaniko dogo lilikutana nyumbani kwa mtu fulani. Baadaye, walijenga mahali pa kukutania kwa kutumia vifaa walivyopata msituni. Kisha, mnamo 1967, walijenga Jumba la Ufalme lenye kuvutia lililokuwa na viti 40. “Nilitania kwamba tutajaza viti hivyo wakati wa Har–Magedoni,” anasema George Coxsen, aliyetumika kwenye nyanda za juu kwa miaka kumi. “Nilikosea kama nini! Katika muda wa miezi 12, watu wengi sana walikuwa wakihudhuria mikutano hivi kwamba tulihitaji kuanzisha kutaniko la pili!”

Mbali zaidi upande wa mashariki, karibu na Kainantu, Norm Sharein alijifunza Biblia na zaidi ya wanakijiji 50 ambao walikuja nyumbani kwake kila siku. Baadaye, mapainia Berndt na Erna Andersson walitunza kikundi hicho kwa muda wa miaka miwili na nusu. “Mara nyingi watu hawakuoga, walivalia mavazi machache, hawakujua kusoma na kuandika, na walijihusisha sana na uchawi,” anaeleza Erna. “Hata hivyo, kwa sababu ya kusaidiwa kwa subira na upendo, baadhi yao walianza kukariri na kueleza maandiko 150.”

Berndt na Erna walikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na kikundi hicho. “Tulipopewa mgawo wa kwenda Kavieng, wanawake walinizunguka wakilia, na kuomboleza kwa sauti kubwa!” anasema Erna. “Mmoja baada ya mwingine, walishika mikono yangu na kunigusa usoni huku machozi yao yakitiririka. Tena na tena, nilirudi ndani ya nyumba na kulia huku Berndt akijaribu kuwatuliza, lakini hawangeweza kufarijika. Mwishowe, tulipoanza kuondoka, umati mkubwa ulifuata gari letu lilipokuwa likiteremka mlimani, wanawake wakilia kwa sauti kubwa. Bado mimi hushindwa na hisia ninapoeleza jinsi nilivyohisi siku hiyo. Tunatamani kama nini kuwaona watu hao tuliowapenda sana katika ulimwengu mpya!” Mapainia wengine waliendeleza kazi ya Berndt na Erna, na kutaniko zuri likaanzishwa huko Kainantu.

MBEGU YA UFALME ILIYOPANDWA YATOKEZA MATUNDA

Kufikia mwanzoni mwa miaka ya 1970, kikundi kidogo cha Mashahidi kilikuwa kimeanza kwenye mji wa Mlima Hagen, kilomita 130 hivi magharibi ya Goroka. Mji huo ulijulikana sana kwa ajili ya soko lake la kila juma, ambalo liliwakusanya pamoja maelfu ya watu kutoka vijiji vya mbali. “Tuliwaachia watu vichapo vingi sana katika soko hilo,” anasema Dorothy Wright painia asiye na woga. Watu hao waliporudi kwenye vijiji vyao, ujumbe wa Ufalme ulienda pamoja nao, na ukapenya katika maeneo ya mbali ambayo wahubiri hawangeweza kufika wakati huo.

Baadaye, Jim Wright, mwana wa Dorothy, pamoja na painia mwenzake, Kerry Kay-Smith walipewa mgawo wa kwenda Banz, wilaya ya kukuza chai na kahawa katika bonde maridadi la Wahgi mashariki ya Mlima Hagen. Huko walikabili upinzani mkali kutoka kwa makanisa, ambayo yaliwachochea watoto wawatupie mawe na kuwafukuza kutoka vijijini mwao. Kerry alipohamia kwenye mgawo mwingine, Jim alibaki Banz, akifanya upainia akiwa peke yake. Anakumbuka hivi: “Mara nyingi nilijilaza kitandani usiku katika nyumba yangu ndogo ya nyasi nikisali, ‘Yehova, ninafanya nini hapa?’ Miaka mingi baadaye ndipo tu nilipopata jibu la swali hilo.

“Katika mwaka wa 2007, nilisafiri kutoka Australia kwenda Banz ili nihudhurie kusanyiko la wilaya,” Jim anasema. “Karibu na mahali ambapo ile nyumba yangu ya nyasi ilikuwa, sasa kulikuwa na Jumba jipya la Ufalme ambalo lingeweza kupanuliwa na kuwa Jumba la Kusanyiko ambalo lingeweza kutoshea watu 1,000. Nilipoingia katika eneo hilo, ndugu mmoja alinikimbilia, akanishika, na kuanza kulia begani mwangu. Mwishowe, ndugu huyo anayeitwa Paul Tai, alipoacha kulia, alinieleza kwamba nilikuwa nimejifunza na baba yake miaka 36 iliyopita. Baadaye Paul alisoma vitabu ambavyo baba yake alitumia kujifunza na akaikubali kweli. Aliniambia kwamba anatumika akiwa mzee.

“Wakati wa kusanyiko hilo, nilihojiwa jukwaani na nikaeleza mateso ambayo tulivumilia zamani huko Banz,” akasema Jim. “Karibu kila mtu aliyekuwa akisikiliza alitokwa na machozi. Baada ya programu baadhi ya akina ndugu walikuja wakanikumbatia na kuomba msamaha huku wakitokwa na machozi. Walipokuwa wavulana, walikuwa wamenifukuza kutoka kijijini mwao huku wakinitupia mawe na kunitusi. Isitoshe, mmoja wao, Mange Samgar—ambaye sasa ni mzee—ndiye kasisi wa Kilutheri aliyekuwa amewachochea wafanye hivyo! Kusanyiko hilo lilikuwa wakati mzuri kama nini wa kukutana tena!”

MBEGU ZINAKUA KATIKA MAENEO YA MBALI

Ingawa watu wengi nchini Papua New Guinea walijifunza kweli kwa sababu ya kuzungumza moja kwa moja na Mashahidi, wengine waliipata kutokana na mbegu za kweli zilizojipenyeza hadi katika maeneo ya mbali. (Mhu. 11:6) Kwa mfano, karibu na mwaka wa 1970, ofisi ya tawi ilianza kupokea ripoti za utumishi wa shambani kutoka kwa mtu asiyejulikana, aliyekuwa katika kutaniko lisilojulikana, na katika kijiji kisichojulikana kwenye Mto Sepik ulio mbali sana. Ofisi ya tawi ilimwomba Mike Fisher, mwangalizi wa mzunguko, achunguze jambo hilo.

“Ili kufika kwenye kijiji hicho, nilisafiri saa kumi kwa mtumbwi wenye injini kupitia mto mwembamba uliopita katikati ya msitu uliojaa mbu,” anaeleza Mike. “Mwishowe, nilifika jioni sana, na nikakutana na mtu huyo aliyekuwa ametengwa na ushirika miaka mingi mapema katika eneo lingine. Alirudi katika kijiji chake, akatubu dhambi zake, na kuanza kuwahubiria watu. Zaidi ya watu 30 katika kijiji hicho walijiita Mashahidi wa Yehova na wengine wao walistahili kubatizwa. Muda mfupi baadaye, mtu huyo aliyetubu alirudishwa, na kikundi hicho kikatambuliwa rasmi na ofisi ya tawi.”

Katika mwaka wa 1992, mwangalizi mwingine wa mzunguko, Daryl Bryon, aligundua kwamba kuna kijiji fulani cha mbali ambako ilisemekana kuwa watu wanapendezwa na kweli. “Ili kufika kwenye kijiji hicho, nilisafiri kwa gari kwa kilomita 80, nikatembea katika msitu mkubwa kwa saa nzima na nusu, kisha nikasafiri kwa mtumbwi nikipiga makasia dhidi ya mkondo wa maji kwa saa nyingine moja,” Daryl anaeleza. “Nilishangaa sana kuona kwamba kwenye ukingo wa mto, katikati ya milima mirefu, kulikuwa na jengo jipya lenye ubao uliosema ‘Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.’

“Kulikuwa na watu 25 hivi wanaopendezwa ambao walikutana katika jumba hilo kila Jumapili ili kujifunza kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Kwa kuwa walidai kuwa Mashahidi, niliwauliza ikiwa walitafuna tambuu. ‘Hapana,’ walinijibu. ‘Tuliacha kufanya hivyo mwaka mmoja uliopita tulipojifunza kweli!’ Nilifurahi kama nini wakati ofisi ya tawi ilipoongeza kikundi hicho kwenye mzunguko wangu.”

WAMISHONARI ZAIDI WAFIKA

Katika miaka ya 1980 na 1990, utendaji katika eneo la Papua New Guinea uliongezeka wakati wamishonari waliozoezwa kwenye Shule ya Gileadi, wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, na mapainia wa pekee kutoka Australia, Finland, Japani, Kanada, Marekani, New Zealand, Sweden, Ufilipino, Uingereza, Ujerumani, na nchi nyingine walipowasili. Mara nyingi hilo lilithibitika kuwa baraka maradufu, kwa kuwa baadaye baadhi ya wahubiri hao walioa na wakaungwa mkono na wenzi wenye bidii kama wao.

Wengi walipowasili nchini, walihudhuria madarasa ya lugha kwa miezi miwili au mitatu ili kujifunza Kitok Pisin au Kihiri Motu. Wanafunzi walijifunza lugha kila asubuhi kisha wakaenda utumishi kila alasiri ili kutumia mambo waliyokuwa wamejifunza. Mazoezi hayo yaliwasaidia wengi wao kuongoza mafunzo ya Biblia na kutoa hotuba baada ya miezi michache tu.

Kujifunza lugha mpya kuliwasaidia pia kuwa na subira na hisia-mwenzi walipowafundisha watu ambao hawakujua kusoma au kuandika. Kwa sababu hiyo, waliwasaidia watu wengi wanaopendezwa wajifunze mambo ya msingi yanayohitajika ili kusoma Neno la Mungu. (Isa. 50:4) Matokeo ni kwamba idadi ya wahubiri iliongezeka kutoka 2,000 katika mwaka wa 1989 kufikia 3,000 hivi katika mwaka wa 1998, ongezeko la asilimia 50 katika muda wa miaka tisa tu!

Ingawa wengi kati ya wahubiri hao baadaye walilazimika kuondoka Papua New Guinea kwa sababu ya afya au sababu nyingine, waliacha urithi wa kudumu. Kwa kweli, watu hao wapendwa bado wanakumbukwa sana kwa uaminifu wao na matendo yao ya upendo.—Ebr. 6:10.

KAZI YA UJENZI YACHOCHEA MAENDELEO

Kadiri idadi ya wahubiri wa Ufalme ilivyozidi kuongezeka, ndivyo kulivyokuwa na uhitaji wa Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na upanuzi wa ofisi ya tawi. Uhitaji huo ulishughulikiwa jinsi gani?

Kabla ya mwaka wa 1975, Wizara ya Ardhi ya serikali ilitenga ardhi kwa ajili ya matumizi ya kidini. Makanisa yaliyotaka yaliomba ardhi na kueleza sababu yao mbele ya Tume ya Ardhi ya serikali. Mwombaji aliyefaulu alipewa ardhi hiyo bila malipo lakini alihitaji kujenga katika kipindi fulani cha wakati.

Mnamo 1963, licha ya upinzani mkali kutoka kwa makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, shirika la International Bible Students Association lilipata ardhi nzuri sana huko Port Moresby. Ardhi hiyo ilikuwa na mandhari yenye kuvutia sana ya soko la Koki na Bahari ya Matumbawe yenye maji safi kabisa. Baadaye, ofisi ya tawi yenye orofa mbili na Jumba la Ufalme lilijengwa katika ardhi hiyo. Mbinu hiyohiyo ilitumiwa kupata ardhi zaidi huko Port Moresby ili kujenga Majumba ya Ufalme ya Sabama, Hohola, Gerehu, na Gordon.

Mwanzoni, ardhi ya Gordon, ambayo iko mahali maarufu sana karibu na kitovu cha mji, ilikuwa imetengwa kwa ajili ya ujenzi wa kanisa kuu la Waanglikana. “Hata hivyo, tulipokuwa mbele ya Tume ya Ardhi, mwenyekiti alimwambia kasisi Mwanglikana kwamba tume hiyo haikufurahishwa na jinsi kanisa hilo lilikuwa limejikusanyia ardhi nyingi na mara nyingi liliitumia kwa sababu za kibiashara,” anaeleza Ron Fynn, aliyetumika huko Papua New Guinea kwa miaka 25. “Mwenyekiti huyo alisema pia kwamba Waanglikana hawatapokea tena ardhi nyingine hadi tume hiyo itakaporidhika kwamba wanatumia ardhi ambayo tayari wamepewa kama ilivyokusudiwa.

“Baada ya kusema hivyo, mwenyekiti alinigeukia na kuniuliza tulitaka ardhi gani. Nilimwambia kwamba tulitaka ardhi iliyokuwa imepewa Waanglikana hapo Gordon. Kasisi huyo Mwanglikana alisimama upesi ili kupinga, lakini mwenyekiti alimwamuru aketi. Kisha nikamaliza nilichotaka kusema. Kila mtu alishangaa kusikia kamati hiyo ikisema kwamba kutaniko letu limepewa ardhi hiyo.”

Jumba la Ufalme na ofisi ya tawi yenye orofa nne zilijengwa kwenye ardhi hiyo. Ofisi hiyo ya tawi iliwekwa wakfu Desemba 12, 1987. Eneo la awali huko Koki liliuzwa. Kati ya mwaka wa 2005 na 2010, jengo lenye orofa nne la makazi, Jumba la Ufalme, na ofisi ya tafsiri zimeongezwa kwenye majengo hayo ya ofisi ya tawi. Majengo hayo yaliwekwa wakfu Mei 29, 2010.

Leo, kuna Majumba 89 ya Ufalme na mahali pengine ambapo mikutano inafanywa nchini kote. Katika maeneo mengi ya vijijini bado sehemu za kukutania zinajengwa kwa vifaa vilivyotolewa msituni. Hata hivyo, katika miji mikubwa vifaa vya kisasa ndivyo vinavyotumiwa katika ujenzi. Mengi kati ya majumba hayo mapya yamejengwa chini ya usimamizi wa programu ya kujenga Majumba ya Ufalme katika nchi zisizo na uwezo mkubwa wa kifedha, ambayo imekuwa ikifanya kazi nchini Papua New Guinea tangu mwaka wa 1999.

UVUMILIVU LICHA YA HALI NGUMU

Dini mbalimbali zilizo huko Papua New Guinea zilikuwa na mkataba usio rasmi wa mahali ambapo kila dini ilipaswa kuendesha shughuli zake. Kila kikundi cha kanisa kilikuwa na eneo lake na ilitarajiwa kwamba dini nyingine hazitaingilia eneo hilo. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova huwahubiria habari njema watu wote wanaotaka kusikiliza, haidhuru wanaishi wapi. Viongozi wa kidini walikasirika sana kwa kuwa Mashahidi walifanya hivyo na pia kwa sababu watu wengi walisikiliza kweli.

“Baada ya kuhamia kisiwa kidogo cha Kurmalak, kilicho kwenye mkoa wa West New Britain, mtu wa kwanza aliyenitembelea alikuwa kasisi wa Kianglikana,” anasema Norm Sharein. “‘Huna ruhusa ya kuhubiri katika eneo langu,’ akasema. ‘Watu hawa tayari ni Wakristo!’

“Baadaye nilimwona mtu mmoja niliyekuwa nikijifunza naye Biblia akipiga makasia ya mtumbwi wake kwa kasi katika mvua nyingi na bahari iliyochafuka akielekea ufuoni. Kwa kweli, alikuwa akihatarisha uhai wake kwa kusafiri katika hali hiyo mbaya ya hewa. Alivuta mtumbwi wake kwenye ufuo na, huku akipumua kwa nguvu, akaniambia kwamba Wakatoliki waliojaa katika mashua moja wakiongozwa na mwalimu wao wa katekisimu, walikuwa wakija kunipiga. Sikuwa na mahali pa kukimbilia, kwa hiyo nikamwomba Yehova anipe hekima na nguvu.

“Mashua hiyo ilipowasili, wanaume 15 hivi walishuka, wakiwa na nyuso zilizopakwa rangi nyekundu—jambo lilionyesha wazi kwamba walitaka kunidhuru. Badala ya kungoja waje kwangu, nilienda kukutana nao. Mapema nilikuwa na woga, lakini sasa sikuhisi woga. Nilipowakaribia, walinitukana wakifikiri kwamba hilo lingenichochea kupigana nao, lakini nilibaki nikiwa mtulivu.

“Pia, kati ya watu waliokusanyika mahali hapo, kulikuwa na mwanamume mwingine mzee ambaye nilijifunza naye Biblia, naye ndiye aliyemiliki kisiwa hicho. Akiwa na nia nzuri, aliwaambia hivi wanaume hao: ‘Mashahidi wa Yehova hawapigani. Hebu mpigeni mjionee wenyewe!’

“‘Sasa mtu huyu yuko upande wa nani?’ nilijiuliza, nikitamani anyamaze.

“Baada ya kuzungumza nao kwa dakika kadhaa, niliwaomba waondoke, na kama ishara ya kwamba sikuwa na uhasama wowote, nilimnyoshea kiongozi wao mkono wangu wa kulia. Akiwa ameshangaa, aliwatazama wenzake, nao wakamtazama. Kisha akanisalimu. Hilo lilifanya kila mtu astarehe, na sote tukasalimiana. Baadaye waliondoka na nikatulia sana! Nilikumbuka maneno ya Paulo kwa Timotheo: ‘Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, . . . akiendelea kujizuia chini ya uovu.’”—2 Tim. 2:24.

Berndt Andersson anakumbuka kwamba katika kijiji kimoja kilichokuwa mlimani, kasisi mmoja wa Kilutheri na kikundi chenye ghasia cha wanaume 70 hivi kutoka kijiji kingine walijaribu kuwafukuza Mashahidi na kuharibu Jumba lao la Ufalme. Wanaume hao walishangaa Berndt alipoenda kukutana nao. Alimkaribia kasisi huyo na kumwuliza kwa nini misheni ya Kilutheri inasema kwamba Mungu anaitwa Anutu, jina la kienyeji ambalo lilianza kutumiwa na Wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kasisi huyo alisema kwamba jina hilo linapatikana katika Biblia, hivyo Berndt akamwomba amwonyeshe linapatikana wapi. Kasisi huyo alifungua Biblia yake, na aliposhindwa kulipata, Berndt akamwomba asome Zaburi 83:18. Baada ya kumsaidia kupata andiko hilo, kasisi alianza kulisoma kwa sauti. Alipofikia jina Yehova, alifunga Biblia yake na kusema kwa sauti, “Huo ni uwongo!” Aligundua kwamba tayari alikuwa ameishutumu Biblia yake mwenyewe. Baada ya kisa hicho, wafuasi wake wengi walibadili mtazamo wao kuwaelekea Mashahidi.

Nyakati nyingine wapinzani wa kidini waliteketeza Majumba ya Ufalme yaliyojengwa kwa nyasi, kama ilivyotukia katika kijiji cha Agi, katika Mkoa wa Milne Bay. Hata hivyo, katika kisa hicho, mmoja wa watu walioteketeza jumba hilo, alikuwa mlevi wakati huo, na alijuta sana. Baadaye aliwafikia akina ndugu na kukubali kujifunza Biblia, naye akawa painia. Isitoshe, alikubaliwa kuishi katika nyumba ya mapainia iliyokuwa kando ya jumba hilo lililojengwa upya. Hivyo akawa mtunzaji wa jumba lililojengwa mahali palepale alipoteketeza lile la kwanza!

Leo, mateso yanayochochewa na dini yamepungua. “Tumeingia katika kipindi cha amani,” anasema Craig Speegle. “Lakini bado tunakabili tatizo lingine—jeuri ambayo mara nyingi husababishwa na majambazi na wezi wanaoitwa raskol. Kwa hiyo, katika maeneo hatari, akina ndugu wanahubiri katika vikundi wakiwa karibu-karibu.”

“Inasaidia unapojitambulisha kuwa Shahidi,” wanasema wamishonari Adrian na Andrea Reilly. “Iwe unaenda kununua vitu au unahubiri, ni jambo la hekima kubeba vichapo,” anasema Adrian. “Ni kweli kwamba huenda vichapo hivyo visikulinde, lakini vinaweza kukusaidia kujitambulisha kuwa mhudumu wa Yehova. Pindi moja gari langu liliharibika katika eneo hatari huko Lae. Nilikuwa peke yangu, na muda si muda genge la vijana walioonekana kuwa hatari lilinizunguka. Hata hivyo, wawili kati yao walinitambua kwa kuwa nilikuwa nimezungumza nao kuhusu Biblia. Kwa sababu hiyo waliwaambia wale wengine wasinidhuru. Hivyo badala ya kuniibia au kunidhuru, nilishangaa vijana hao wote walipolisukuma gari langu umbali wa nusu kilomita hadi kwenye makao ya wamishonari.”

Katika kisa kingine, dada mmoja alikuwa sokoni wakati raskol waliokuwa wamejihami kwa visu walipomnong’onezea hivi, “Tupatie mkoba wako.” Mara moja aliwapa mkoba, nao wakakimbia. Baada ya dakika chache, walirudi, wakamwomba msamaha, na kumpa mkoba wake ukiwa na kila kitu ndani. Kwa nini? Walipofungua mkoba huo, waliona Biblia na kitabu Kutoa Sababu na wakahisi vibaya kwamba walimwibia.”

NJIA MBALIMBALI ZA KUHUBIRI

“Tulihubiri mahali popote tulipopata watu,” anakumbuka Elsie Thew, ambaye alitumika huko Papua New Guinea akiwa na Bill, mume wake, kuanzia mwaka wa 1958 hadi 1966. “Tulizungumza na watu vijijini, nyumbani, shambani, sokoni, na katika njia za vichakani. Tulizungumza na wavuvi katika fuo na kingo za mito. Mwanzoni tulipoanza kuhubiri katika eneo hilo, tulibeba ramani ya dunia yote ili tuweze kuwaonyesha watu waliokuwa sehemu za mbali sana mahali tulipotoka. Hilo lilikuwa muhimu kwa sababu tuliwasili kwa ndege, na kwa kuwa wanakijiji wengi hawakujua mengi kuhusu sehemu nyingine za dunia, walidhani tulianguka kutoka mbinguni! Kwa hiyo tuliwaonyesha kwamba tulitoka sehemu nyingine ya dunia ileile ambayo wao wanaishi.”

Njia pekee ya kufikia vijiji vingi vilivyotapakaa kwenye pwani ndefu na kingo za mito ya Papua New Guinea ni kwa mashua au mtumbwi. Steve Blundy anakumbuka hivi: “Ndugu Daera Guba, kutoka Hanuabada, Port Moresby alikuwa mzee kwa umri lakini mwenye uzoefu mwingi wa kutumia mashua. Chini ya nyumba yake, kulikuwa na magogo mawili yaliyokuwa na shimo katikati, kwa hiyo mimi na painia mwenzangu tulimsaidia kupata mbao alizohitaji kutengeneza puapua, aina fulani ya mashua yenye matanga. Matanga yake yalitengenezwa kwa chandarua. Daera akiwa nahodha na ndugu wengine wawili au watatu kutoka Hanuabada wakiwa mabaharia, tulisafiri mara kadhaa hadi kwenye vijiji vya pwani karibu na Port Moresby.”

Mwishoni mwa miaka ya 1960, Berndt Andersson alikuwa akitumika huko New Ireland, kisiwa maridadi kilicho kilomita 650 hivi kaskazini-mashariki ya nchi kavu. Berndt anaandika hivi: “Watu waliotoka visiwa vidogo vilivyokuwa karibu walituomba tuwatembelee. Hata hivyo, ili tufanye hivyo, tulihitaji mashua, lakini hatungeweza kuinunua kwa sababu rudishio letu la gharama lilikuwa dogo sana. Tulikuwa na mbao chache lakini hizo hazingetosha kutengeneza mashua. Kwa hiyo tulisali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. Kisha bila kutarajia kabisa, ndugu mmoja kutoka Lae alitutumia dola 200 [za Australia] kama mchango wa kutusaidia kutembelea visiwa vya mbali. Kwa hiyo, tuliweza kujenga mashua ambayo tuliiita Pioneer. Hata hivyo, haikuwa na injini. Kwa mara nyingine tena, ndugu huyo akatupa pesa za kununua injini ndogo. Sasa tungeweza kutembelea visiwa hivyo maridadi!”

Karibu na mwaka wa 1990, Jim Davies, ambaye alikuwa mwangalizi wa mzunguko, pamoja na ndugu wengine watatu, walifanya mipango ya kuhubiri katika kambi ya wakimbizi iliyokuwa upande wa juu wa Mto Fly karibu na mpaka wa Indonesia. Akina ndugu walikuwa wametutafutia mahali pa kulala katika nyumba ya mwanamke mmoja aliyependezwa ambaye mume wake alikuwa msimamizi wa pili katika kambi hiyo. “Safari ya kuelekea upande wa juu wa Mto Fly ilichukua karibu saa mbili tukitumia mtumbwi uliokuwa na injini,” anasema Jim. “Saa tatu hivi asubuhi, tuliwasili mahali pasipokuwa na miti msituni, tukaona barabara ya mchanga iliyoelekea kwenye kambi iliyokuwa mbali. Tulingojea usafiri hapo.

“Hatimaye, saa kumi na moja jioni, gari moja lilitokea. Tuliweka mizigo yetu na kuketi, kisha baada ya kusafiri umbali wa mita 90 hivi, usukani wa gari hilo ulivunjika! Bila wasiwasi, dereva alitambua tatizo, akatafuta waya fulani, akainama chini ya gari na kufunga pamoja vipande vilivyoachana. Nilijiambia, ‘Waya huo hautadumu.’ Lakini nilikuwa nimekosea. Kwa saa tano, waya huo ulishikilia vipande vya gari hilo lililoendeshwa kwa magurudumu yote manne kwa sababu barabara ilikuwa mbovu. Mara kwa mara tulikwama kwenye matope na ilibidi tusukume gari hilo. Tuliwasili saa nne usiku tukiwa tumechoka na tumejaa matope.

“Kwa siku tatu, tulihubiri kwenye kambi hiyo ambayo ilikuwa imeenea katika eneo kubwa la msitu, na tukawaachia watu vichapo vyote tulivyokuwa navyo. Pia tulikutana na mtu mmoja aliyekuwa ametengwa na ushirika, naye akatueleza kwamba angependa kumrudia Yehova. Baadaye tulifurahi kusikia kwamba alirudi. Pia mke wake na baadhi ya watoto wao sasa ni Mashahidi. Pia yule mwanamke mwenye kupendezwa pamoja na mume wake ambao walitupa mahali pa kulala sasa ni Mashahidi.”

KAZI YA MZUNGUKO KWENYE MTO SEPIK

Mto Sepik ulio na urefu wa kilomita zaidi ya 1,100 ni kama nyoka mkubwa mwenye rangi ya kahawia aliyejipindapinda kutoka milimani hadi baharini. Katika sehemu fulani, mto huo ni mpana sana hivi kwamba ni vigumu kuona ukingo ulio ng’ambo ile nyingine. Mto huo ni njia kuu inayotumiwa na ndugu wengi kutia ndani waangalizi wa mzunguko na wake zao. Na tuambatane na mwangalizi mmoja pamoja na mke wake wanapotembelea makutaniko yaliyo kandokando ya mto huo mkubwa.

Warren Reynolds anaandika hivi: “Asubuhi na mapema, mimi na mke wangu, Leann, tunaelekea mji wa Wewak tukiwa tumefunga boti yetu ya alumini yenye urefu wa mita 3.5 juu ya gari letu. Baada ya kusafiri kwa saa tatu katika gari linaloendeshwa kwa magurudumu yote manne, tunaegesha gari hilo kando ya mto kwa siku chache na kusafiri sehemu ya juu ya mto huo ili kuwatembelea wahubiri 30 hivi wanaoishi katika vijiji vinne kando ya vijito vya Mto Sepik.

“Huku boti yetu ikiwa imepakiwa vitu, tunawasha injini yake na kuelekea upande wa juu wa mto. Baada ya saa moja, tunageuka na kuingia Mto Yuat, ambao ni kijito cha Mto Sepik, na kusafiri kwa saa mbili nyingine kabla ya kufika kijiji cha Biwat. Tunakaribishwa kwa uchangamfu na akina ndugu na wanafunzi wao wa Biblia, baadhi yao wanavuta boti yetu ufuoni na mmoja anaiweka nyumbani kwake. Baada ya kufurahia mlo wa ndizi na tui, sote tunafunga safari ya saa mbili kwa miguu kupitia msitu wenye vinamasi, wahubiri hao wakituongoza huku wakiwa wamebeba mizigo yetu. Hatimaye tunafika kwenye kijiji kidogo kinachoitwa Dimiri, ambapo tunakata kiu kwa tui, kisha katika nyumba iliyotengenezwa kwa vitu vinavyopatikana msituni na iliyojengwa juu ya nguzo za mbao, tunatayarisha mahali pa kulala na kuweka chandarua cha kujikinga na mbu. Baada ya kula viazi vikuu vilivyopikwa, tunaenda kulala.

“Wahubiri 14 wanaishi katika vijiji vitatu katika eneo hilo. Kwa siku chache zinazofuata, tunahubiri kila kijiji na kupata watu wengi wanaopendezwa. Pia tunafurahia kuona wanafunzi wawili wa Biblia wakihalalisha ndoa yao na kustahili kuwa wahubiri wa Ufalme. Wale wahubiri wengine wanaandaa karamu ya harusi ya viazi vikuu, sago, mboga fulani za majani, na kuku wawili.

“Siku ya Jumapili tunafurahia kuwa na hudhurio la wanakijiji 93 kwenye hotuba ya watu wote! Baada ya mkutano, saa za adhuhuri, mikoba yetu ikiwa imejaa, tunafunga safari ya kurudi Biwat, tunaacha mizigo yetu katika nyumba ya mwanafunzi fulani wa Biblia na kuanza kuhubiri. Watu wengi wanakubali vichapo vyetu; na baadhi yao wanakubali kujifunza Biblia. Usiku huo, katika nyumba ya mwanafunzi mmoja wa Biblia, tunaketi karibu na moto huku moshi ukifukuza mbu.

“Mapema siku inayofuata, tunarudi kwenye boti yetu, tunaisukuma mtoni na kuanza safari katika ukungu wa asubuhi huku tukifurahia ndege na samaki wanaoruka majini. Tunapishana na familia kwenye vyelezo vya mianzi wakienda kuuza bidhaa zao sokoni.

“Tunaporudi kwenye gari letu, tunajaza mafuta kwenye injini ya boti na kujaza maji ya kunywa ndani ya mitungi yetu na kupakia vitu vingine tutakavyohitaji. Kisha tukaelekea mtoni tena kuanza safari ya kuwatembelea wahubiri 14 huko Kambot. Tunawasili saa mbili baadaye tukiwa tumelowa kabisa kwa sababu ya mvua. Kutoka Kambot, tunaelekea upande wa juu wa mto huo, kwenye kijiji kimoja kikubwa kilichokuwa pande zote mbili za mto. Wakati huu boti yetu imejaa wahubiri. Tunawahubiria watu hao wenye uthamini hadi jioni. Tunapokuwa tukirudi, tunawahubiria watu ambao wamesimama kwenye gati za mianzi zilizokuwa zikielea majini. Walituona asubuhi tukielekea upande wa juu kwa hiyo wamekuwa wakitusubiri turudi. Kwa kuwa watu wengi katika eneo hili la mbali hawana pesa, wanakijiji wanatushukuru kwa kuwatembelea na kwa trakti ambazo tumewapa, kwa kutupa vyakula mbalimbali—nazi, maboga, samaki waliokaushwa, na ndizi. Jua linaposhuka, tunarudi Kambot na kuanza kupika vyakula hivyo.

“Huko Kambot, mahali pa kukutania pamejengwa juu ya nguzo ndefu za mbao kama nyumba zote katika eneo hilo zinavyojengwa. Wakati wa majira ya mvua, eneo hilo lote linapofurika, watu huendesha mitumbwi yao hadi kwenye mlango wa mahali pa mkutano. Katika siku ya mwisho ya ziara yetu, watu 72, kutia ndani wengine ambao wametembea kwa saa tano ili kufika mahali hapo, wanahudhuria hotuba ya watu wote.

“Baada ya kurudi kwenye gari letu na kufunga boti juu ya paa, tunaanza safari ya saa tatu kurudi nyumbani. Tukiwa njiani, tunatafakari kuhusu ndugu na dada zetu wapendwa wanaoishi kandokando ya Mto Sepik. Pia tunafikiria kuhusu jinsi Yehova anavyowapenda, kama inavyoonyeshwa kupitia jitihada ambazo tengenezo lake linafanya ili walishwe vizuri kiroho. Ni pendeleo kama nini kuwa sehemu ya familia hii nzuri!”

KUSHINDANA MWELEKA NA ROHO WAOVU

Ingawa idadi kubwa ya wakazi wa Papua New Guinea wanadai kuwa Wakristo, wengi wao pia hufuata imani za kitamaduni, kutia ndani kuabudu mababu waliokufa na kuogopa roho waovu. Kitabu kimoja kinasema kwamba katika miaka ya hivi karibuni, “watu wengi wameanza tena kupendezwa na uchawi na ulozi.” Hivyo, bado watu husema kwamba magonjwa na kifo husababishwa na wachawi au roho za mababu waliokufa.

Katika mazingira kama hayo, kweli ya Biblia huwaweka watu huru kikweli. Hata baadhi ya wachawi wametambua nguvu ya Neno la Mungu, wakaacha mazoea yao, na kukubali kweli. Fikiria mifano miwili:

Soare Maiga aliishi katika kijiji kilichokuwa kilomita 50 hivi kutoka Port Moresby na aliogopwa sana kwa sababu ya nguvu zake za kiuchawi. Hata hivyo, alitaka sana kujua kuhusu imani ya Mashahidi wa Yehova, kwa hiyo alijiunga na kikundi kimoja kilichokuwa kikijifunza Biblia. Punde si punde, alikubali kweli na akaacha mazoea yake ya zamani. Lakini kila mara alipojaribu kutupa vitu vyake vya kuwasiliana na pepo, vitu hivyo vilirudi kwa njia ya ajabu! Hata hivyo, Soare alikuwa ameazimia ‘kumpinga Ibilisi,’ kwa hiyo siku moja alitia vitu hivyo ndani ya mkoba, akatia jiwe ndani ya mkoba huo, kisha akaenda huko Port Moresby na kuutupa baharini. (Yak. 4:7) Vitu hivyo havikurudi tena. Baada ya hilo, mtu huyo jasiri akawa Shahidi mwenye bidii wa Mungu wa kweli, Yehova.

Kora Leke alitumia uchawi na miti-shamba kuwatibu wagonjwa. Hata hivyo, alipoanza kujifunza Biblia, alijitahidi sana kuacha roho aliyekuwa akimsaidia katika uchawi wake. Kama Soare, Kora alikuwa ameazimia kuachana na roho waovu, na alifaulu kwa msaada wa Yehova. Baadaye, alitumika akiwa painia wa kawaida na kisha painia wa pekee. Hata sasa ingawa yeye ni mzee na miguu yake ni dhaifu, ndugu huyo mshikamanifu anaendelea kuwaeleza jirani zake habari njema.

Kora alifika kwa njia gani mahali ambapo alipenda kukaa akihubiri? Akina ndugu walimpeleka kwa toroli (wheelbarrow) ambayo ndiyo iliyokuwa njia pekee iliyofaa wakati huo. Baadaye, ndugu fulani mbunifu katika ofisi ya tawi alimtengenezea kiti cha magurudumu akitumia kiunzi kilichotengenezwa kwa chuma cha kiti cha kawaida, magurudumu ya baiskeli, na chandarua. Kora angeweza kujisukuma mwenyewe kwa kiti hicho kipya na amekitumia kikamili! Wazee kama yeye ni kielelezo chenye kuchochea kama nini, kwani wanaufurahisha sana moyo wa Yehova!—Met. 27:11.

KUWAFUNDISHA WATU KUSOMA NA KUANDIKA

Andiko la Waroma 15:4 linasema: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi.” Ni wazi basi kwamba Mungu anataka watu wake wajue kusoma na kuandika. Kama ambavyo tayari tumetaja, Mashahidi wa Yehova huko Papua New Guinea wamejitahidi sana kuwafundisha watu kusoma na kuandika.

Bila shaka, inaweza kuwa vigumu, hasa kwa wazee, kujifunza kusoma na kuandika, lakini mwanafunzi akiwa na bidii, atafanikiwa. Kwa kweli, Neno la Mungu linaweza kuwavuta hata watu wa hali ya chini sana na wale ambao hawajui kusoma na kuandika hata kidogo.

Fikiria kisa cha Save Nanpen, kijana aliyeishi karibu na chanzo cha Mto Sepik. Save alipohamia Lae, aliona maisha tofauti sana na kwa mara ya kwanza, akaona utamaduni wa nchi za Ulaya. Isitoshe, alikutana na Mashahidi wa Yehova ambao walimwambia kuhusu tumaini la Ufalme. Save aliguswa sana na mambo aliyosikia, akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na muda si muda, akastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Hata hivyo, alisitasita kuchukua hatua iliyofuata, yaani, kubatizwa. Kwa nini? Alikuwa amemwambia Yehova kwamba hangebatizwa hadi atakapoweza kujisomea Biblia. Kwa hiyo akajifunza kwa bidii na kufikia miradi yake ya kiroho.

Bado watu wengi hawajui kusoma na kuandika, lakini shule za serikali zimeanzishwa katika sehemu nyingi, na watoto wa Mashahidi wanahudhuria shule hizo. Kwa kweli, vijana wetu wameweka mfano mzuri wa kujifunza kusoma na kuandika, na ni kwa sababu hasa ya jitihada za wazazi na mazoezi yanayotolewa katika mikutano ya kutaniko, kama vile Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.

KWELI YA BIBLIA HUBADILI MAISHA

Mtume Paulo aliandika: “Silaha za vita vyetu si za kimwili, bali ni zenye nguvu kwa Mungu kwa ajili ya kupindua ngome zenye nguvu.” (2 Kor. 10:4) Nyakati nyingine, andiko moja tu linaweza kuwa na nguvu sana, kama kisa cha mwanamke mmoja anayeitwa Elfreda, kinavyoonyesha. Baada ya Elfreda kuonyeshwa jina la Mungu katika Biblia yake ya Kiwedau, alichunguza jambo hilo katika ensaiklopedia moja, na kitabu hicho kilimthibitishia yale ambayo Biblia ilisema kuhusu jina la Mungu. Alijiambia, ‘Mashahidi wa Yehova wanafundisha kweli.’ Hata hivyo, mume wake, Armitage, hakutaka uhusiano wowote na Mashahidi. Alikuwa mlevi na alitafuna tambuu na kuvuta tumbaku, na pia alikuwa na hasira kali.

Baada ya kustaafu huko Lae, Armitage, pamoja na Elfreda, walihamia Alotau katika Mkoa wa Milne Bay, ambako hakukuwa na Mashahidi. Wakiwa huko, Elfreda aliandikisha magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na kujifunza Biblia kupitia barua pamoja na Kaylene Nilsen, ambaye alikuwa painia. Kaylene anasema: “Kila juma, Elfreda alinitumia majibu kupitia barua.”

Baadaye, wahitimu wa Gileadi, Geordie na Joanne Ryle, walitumwa Milne Bay, nao walimtembelea Elfreda ili wamtie moyo na kuhubiri pamoja naye. Geordie anasema: “Armitage aliniomba nijifunze Biblia pamoja naye. Kwa sababu ya sifa yake mbaya, nilishuku nia yake. Lakini baada ya kujifunza naye kwa mwezi moja, niliona kwamba alikuwa na moyo mnyoofu. Baadaye alibatizwa na akawa mtumishi wa huduma.” Sasa vizazi vitatu vya familia yake ni Mashahidi, na mjukuu wake, Kegawale Biyama, ambaye alinukuliwa hapo awali, ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi huko Port Moresby.

Walipokuwa wakihubiri huko Hula, Don na Shirley Fielder walijifunza Biblia na Alogi na Renagi Pala. “Alogi alikuwa mwizi na kila mara alikuwa akipigana na watu,” anaandika Don. “Aliugua ugonjwa fulani uliofanya ngozi yake iwe mbaya sana, na sehemu ya mdomo wake ilikuwa na kidonda kibaya. Yeye na mke wake walitafuna tambuu, kwa hiyo mianya iliyokuwa katikati ya meno yao myeusi ilikuwa myekundu kama damu. Mtu hangetarajia kwamba Alogi angevutiwa na kweli. Hata hivyo, yeye na mke wake walipendezwa na kweli na wakahudhuria mikutano yetu, na kuketi nyuma.

“Katika muda wa miezi sita,” anasema Don, “Alogi alifanya mabadiliko yenye kushangaza. Aliacha kuiba, kupigana, na ugomvi, halafu yeye na Renagi wakawa nadhifu na wakaanza kutoa maelezo katika mikutano. Pia walianza kuwahubiria wengine habari njema. Wenzi hao na watu wengine wachache wakawa ndio wahubiri wa kwanza katika eneo la Hula.”

Abel Warak aliyeishi New Ireland aliugua ukoma. Kwa sababu ya ugonjwa huo, miguu na mikono yake ilikuwa imekufa ganzi. Alipokutana na Mashahidi kwa mara ya kwanza, Abel hangeweza kutembea na hakuwa na tamaa ya kuishi. Hata hivyo, ukweli ilibadili kabisa mtazamo wake na kumfanya awe mwenye shangwe na nguvu. Baada ya muda, akawa painia. Ili apate lishe bora zaidi, Abel alikuwa akivua samaki, lakini kwa kuwa miguu yake ilikuwa imekufa ganzi, hangeweza tena kutembea kwenye matumbawe. Hivyo akina ndugu walimnunulia buti zilizokuwa zikifika magotini. Pia alijifunza kuendesha baiskeli ambayo ilimwezesha kusafiri mbali kuhubiri habari njema. Nyakati nyingine, hata alisafiri umbali wa kilomita 100 kutembelea watu waliopendezwa, na pindi moja, alisafiri umbali wa kilomita 145 kwenda kumwalika kwenye Ukumbusho mtu aliyependezwa.

Nyakati nyingine, “kumjua Yehova” kumewasaidia hata watu wenye tabia za kinyama wafanye mabadiliko makubwa. (Isa. 11:6, 9) Kwa mfano, katika mwaka wa 1986, watu 60 hivi kutoka vijiji viwili vilivyokuwa karibu na Banz walikuja kwenye kusanyiko la wilaya huko Lae na kuketi kwenye viti vya mbele. Watu hao walioishi sehemu za mlimani walikuwa maadui kwa muda mrefu na walipigana mara kwa mara. Lakini baada ya kusikia habari njema kutoka kwa mapainia wa pekee, waliamua kuishi pamoja kwa amani. Visa kama hivyo hutukumbusha maneno yanayopatikana kwenye Zekaria 4:6: “‘Si kwa jeshi, wala kwa nguvu, bali kwa roho yangu,’ Yehova wa majeshi amesema.” Roho hiyohiyo pia iliwachochea watu wengi wanyoofu waishi kupatana na viwango vya Biblia vya maadili.

KUHESHIMU ZAWADI YA MUNGU YA NDOA

Katika nchi nyingi, desturi za huko na pia dini zinazodai kuwa za Kikristo hupuuza maoni ya Biblia kuhusu ndoa. (Mt. 19:5; Rom. 13:1) Ndivyo ilivyo hata huko Papua New Guinea. Kwa hiyo, ili kumpendeza Yehova, watu wengi waliokuwa wakiishi pamoja bila kuoana kisheria au wale wenye wake wengi walihitaji kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yao. Fikiria mfano wa Francis na mke wake, Christine.

Francis alipojiuzulu kutoka jeshini, yeye na mke wake walitengana. Christine na watoto wao wawili walirudi kwa wazazi wake katika Kisiwa cha Goodenough, Mkoa wa Milne Bay, naye akarudi Mlima Hagen. Baadaye, Francis alianza kuishi na mwanamke mwingine aliyekuwa na watoto. Walihudhuria Kanisa la Assemblies of God. Baada ya muda, mwanamke aliyekuwa akiishi na Francis alitembelewa na Mashahidi na akaanza kujifunza Biblia. Kisha Francis pia akapendezwa na muda si muda wote wawili wakaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo.

Francis alitaka kuwa mhubiri wa Ufalme, kwa hiyo alihitaji kusuluhisha matatizo yake ya ndoa. Baada ya kufikiria jambo hilo kupitia sala, alilizungumzia pamoja na mwanamke aliyekuwa akiishi naye. Mwanamke huyo na watoto wake walihamia nyumba nyingine, na Francis akaenda kumwona Christine, ambaye walikuwa wametengana kwa miaka sita. Christine na watu wake wa ukoo walishangaa sana kumwona Francis. Akitumia Maandiko, Francis aliwaeleza wote kwamba alitaka kufanya yaliyo sawa machoni pa Yehova. Kisha akamwomba mke wake arudi naye hadi Mlima Hagen pamoja na watoto wao ili wawe familia tena. Kila mtu alishangaa jinsi Francis alivyokuwa amebadilika sana. Christine alikubali ombi la mume wake, naye Francis akawalipa watu wa ukoo wa mke wake kiasi fulani cha pesa kwa kuitunza familia yake kwa zaidi ya miaka sita iliyokuwa imepita.

Christine aliporudi Mlima Hagen, yeye pia alianza kujifunza Biblia, lakini kwanza alihitaji kujifunza kusoma na kuandika. Pia aliacha kutafuna tambuu na kuvuta tumbaku. Wenzi hao wa ndoa sasa ni watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu.

WATOTO WANAOMLETEA SIFA MUUMBA WAO

Kwa kufuata kwa ujasiri dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia, watoto wengi huko Papua New Guinea wametoa ushahidi mzuri. Kwa mfano, mapema katika mwaka wa 1966, mwalimu mmoja wa shule ya msingi aliwaambia watoto saba wa Mashahidi wa eneo hilo kwamba walipaswa kusalimu bendera wakati wa sherehe ambazo zingefanywa juma lililofuata. Siku hiyo ilipofika, watoto wote saba walikataa kusalimu bendera mbele ya wanafunzi 300 hivi. Kwa sababu hiyo, walifukuzwa shuleni, hata ingawa wazazi wao walikuwa wameandika barua wakiomba watoto wao wasihusishwe katika sherehe hizo. Mzee mmoja kutoka kutaniko la huko aliandika barua kwa maofisa wa serikali huko Papua New Guinea na Australia kuhusu jambo hilo.

Mnamo Machi 23, Msimamizi wa Serikali ya Australia huko Papua New Guinea aliwapigia simu wakuu wa shule hiyo na kuagiza kwamba watoto hao warudishwe shuleni mara moja. Ibada ya kweli ilikuwa imepata ushindi mdogo wa kisheria. Leo, serikali ya Papua New Guinea inaendelea kuheshimu haki ya watoto ya kukataa kusalimu bendera kwa sababu ya dhamiri.

“Watoto na wanaonyonya” wanaweza kumsifu Yehova katika njia nyingine pia. (Mt. 21:16) Fikiria mfano wa Naomi kutoka sehemu za mlimani ambaye wazazi wake, Joe na Helen, hawakuwa Mashahidi. Naomi alipokuwa na umri wa miaka mitatu hivi, aliishi kwa mwaka mmoja hivi na shangazi yake, yaani dada ya Helen, ambaye ni Shahidi mwenye bidii huko Lae. Shangazi yake alikuwa akimbeba Naomi ndani ya mfuko ulioning’inizwa kwenye bega lake kila mara alipoenda mahubiri. Kwa njia hiyo, Naomi alijua tumaini la Ufalme, na pia shangazi yake alitumia sana picha katika Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia.

Naomi aliporudi kwa wazazi wake, alichukua kichapo cha Mashahidi, akatoka nje ya nyumba, na kubisha mlango wao kwa sauti ya juu. “Ingia ndani,” wazazi wake wakamwambia. Alipoingia tena ndani, msichana huyo mdogo alisema hivi: “Habari. Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na nimekuja kuzungumza nanyi kuhusu Biblia.” Huku Joe na Helen wakimtazama kwa mshangao, Naomi aliendelea kusema: “Biblia inasema kwamba Paradiso itakuwa juu ya dunia; na Mfalme mmoja, Yesu, atatawala juu yetu. Kila kitu kinachotuzunguka kimefanywa na Yehova.”

Joe na Helen walipigwa na butwaa. “Jamani majirani wetu watasema nini!” Joe akamwambia mke wake. “Tafadhali kesho mfungie ndani.”

Siku iliyofuata, wazazi wake walipokuwa wameketi nje ya nyumba yao, Naomi aligonga kwa sauti ukuta wa chumba chake cha kulala. “Njoo huku nje,” Joe akamwambia. Naomi alitoka na kuanzisha mazungumzo: “Habari. Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na nimekuja kukuhubiria. Watu wazuri wataishi milele duniani. Lakini watu ambao hukasirika na kufanya mambo mabaya hawataishi katika Paradiso.” Wakiwa wamechanganyikiwa, Helen alianza kulia, huku Joe akiondoka kwa hasira kwenda kulala.

Usiku huo, kwa sababu ya udadisi, Joe alianza kusoma Biblia yake nzee ya tafsiri ya King James Version na akapata jina Yehova. Asubuhi iliyofuata, badala ya kwenda kazini, aliwaandikia Mashahidi barua kisha akasafiri kwa gari umbali wa kilomita 40 ili kuipeleka kwenye Jumba la Ufalme huko Mlima Hagen.

Akina ndugu waliwatembelea Joe na Helen na kupanga kuanza kujifunza nao Biblia kwa ukawaida. Pia walimfundisha Helen kujua kusoma. Hatimaye, wote wawili, Joe na Helen walibatizwa, na Helen aliwafundisha wanafunzi wengine wa Biblia kujua kusoma. Yote hayo kwa sababu msichana mdogo alimsifu Yehova!

JITIHADA ZA KUHUDHURIA MAKUSANYIKO YA KIKRISTO

Katika sehemu fulani za dunia, akina ndugu hutumia barabara zenye hewa chafu na msongamano wa magari au reli za chini ya ardhi zilizojaa watu ili kufika kwenye mikutano na makusanyiko ya Kikristo. Lakini nchini Papua New Guinea mara nyingi watu wanakabili tatizo la ukosefu wa barabara nzuri na usafiri. Hivyo, familia nyingi hulazimika kusafiri mwendo fulani kwa miguu au kwa mtumbwi au kwa njia zote mbili. Kwa mfano, kila mwaka wahubiri pamoja na watoto wao hutembea kwa zaidi ya kilomita 160 kupitia milima iliyochongoka na yenye kuteleza ili kuhudhuria kusanyiko la wilaya huko Port Moresby. Wakati wa safari hiyo ngumu inayochukua juma moja, wao hupita kwenye Njia ya Kokoda, ambapo vita vikali vilipiganwa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Wao hubeba vyakula, vyombo vya kupikia, nguo, na vifaa vingine wanavyohitaji kwa ajili ya kusanyiko.

Kwa kawaida, ndugu kutoka Kisiwa cha Nukumanu husafiri umbali wa kilomita 800 kuelekea magharibi ili kuhudhuria makusanyiko ya wilaya ya kila mwaka huko Rabaul. “Ili wafike kwa wakati,” anasema Jim Davies, “nyakati nyingine wao huanza safari majuma sita kabla ya kusanyiko kwa sababu huduma za boti hazitegemeki. Usafiri pia wakati wa kurudi nyumbani hautegemeki. Pindi moja, boti pekee iliyokuwa ikielekea Nukumanu iligeuza njia na kuelekea Australia ili ikarekebishwe, kisha wenye boti hiyo wakakosa pesa. Kwa sababu hiyo, iliwachukua akina ndugu miezi sita kurudi nyumbani! Huenda hicho ni kisa cha pekee, lakini ni kawaida kwa wahubiri kucheleweshwa kwa majuma kadhaa na hivyo kulazimika kuishi na Mashahidi wengine au watu wa ukoo.”

KIELELEZO KIZURI CHA WAMISHONARI

Inaweza kuwa vigumu kwa wamishonari kuzoea maisha ya hali ya chini kuliko yale waliyokuwa nayo nyumbani. Lakini wengi wamefanya mabadiliko hayo, na wakazi wa nchi wanakotumika huthamini sana wanapofanya hivyo. Mwanamke mmoja huko Papua New Guinea alisema hivi kuhusu dada wawili wamishonari waliokuwa wakijifunza pamoja naye, “Ngozi yao ni nyeupe, lakini mioyo yao ni kama yetu.”

Wamishonari fulani hutumika katika kazi ya kuzungukia makutaniko. Ili kutembelea makutaniko, huenda wakatumia usafiri wowote unaopatikana. Mambo yalikuwa hivyo kwa Edgar Mangoma. Mizunguko aliyotembelea ilitia ndani Mto Fly na Ziwa Murray. “Nilipotembelea makutaniko mawili yaliyo kando ya ziwa, nilisafiri kwa mitumbwi ambayo nyakati nyingine ilikuwa na injini au nyakati nyingine haikuwa nayo. Niliposafiri kwa mtumbwi ambao haukuwa na injini, ingenichukua saa nane kutoka kutaniko moja hadi lile lingine. Kwa kawaida, ndugu watatu au wanne waliandamana nami, ili warudi na mtumbwi baada ya kunifikisha nilikokuwa nikienda. Niliwathamini sana ndugu hao!”

Kielelezo kizuri cha wamishonari, kutia ndani unyenyekevu na upendo wao kwa watu, ulikuwa na matokeo mazuri. Mwangalizi mmoja wa mzunguko anasema hivi: “Wanakijiji walishangaa kuniona nikiishi na watu wanaopendezwa na kula pamoja nao. Hata baadhi yao wameniambia: ‘Wewe unamwabudu Mungu kwa njia inayofaa. Makasisi wetu hawashirikiani nasi kama vile wewe unavyofanya.’”

Je, dada wamishonari wanaotumika Papua New Guinea huona ikiwa vigumu kuzoea maisha ya huko? “Kwa miezi michache ya kwanza ilikuwa vigumu kwangu,” anasema Ruth Boland, ambaye aliambatana na mume wake, David, katika kazi ya kusafiri. “Mara nyingi nilijihisi siwezi kuendelea. Lakini ninafurahi kwamba sikuacha, kwa kuwa nimekuja kuwathamini na kuwapenda ndugu na dada. Mimi na mume wangu hatukujifikiria sana bali tuliwafikiria wengine. Kwa kweli, shangwe tuliyopata haina kifani. Hatukuwa na vitu vya kimwili, lakini tulikuwa matajiri kiroho. Na tuliona jinsi ambavyo Yehova alibariki kazi ya kuhubiri habari njema na pia maisha yetu. Usipokuwa na vitu vya kimwili, unamtegemea Yehova zaidi na kupata baraka zake.”

VITA VYA WENYEWE KWA WENYEWE BOUGAINVILLE

Mnamo 1989, harakati za muda mrefu za Kisiwa cha Bougainville kujipatia uhuru zililipuka na kuwa vita vya wenyewe kwa wenyewe. Wakati wa vita hivyo vya miaka 12, watu 60,000 hivi walitoroka makwao, na 15,000 walikufa. Kulikuwa na wahubiri wengi waliotoroka makwao, na wengi wao walihamia sehemu nyingine za Papua New Guinea.

Muda mfupi kabla ya kuhama kisiwa hicho, Dan Ernest, ambaye ni painia alikamatwa na wanajeshi wa Bougainville Revolutionary Army (BRA) na kupelekwa kwenye bohari kubwa. Dan anakumbuka hivi: “Ndani ya bohari hiyo kulikuwa na jenerali wa BRA aliyevalia sare zilizojaa medali na alikuwa na upanga.

“Aliniuliza, ‘Wewe ni Dan Ernest?’

“Nikajibu, ‘Ndiyo.’

“‘Nasikia wewe ni jasusi wa Papua New Guinea Defence Force,’ akasema.

“Nilianza kumweleza kwamba Mashahidi wa Yehova hawajihusishi katika mapigano ya nchi, lakini akanikatiza na kusema: ‘Tunajua hilo! Tulikuwa tukiwatazama. Dini nyingine ziliunga mkono upande wowote ulioshinda. Ni dini yenu tu ambayo haikuunga mkono upande wowote.’ Kisha akasema: ‘Watu wetu wamehangaishwa sana na vita hivi na wanahitaji ujumbe wenu wenye kufariji. Tungependa uendelee kuhubiri huku Bougainville. Lakini ikiwa utalazimika kuondoka, nitahakikisha kwamba utalindwa pamoja na mali yako.’ Majuma mawili baadaye, mimi na mke wangu tulipopewa mgawo mpya wa upainia kwenye Kisiwa cha Manus, jenerali huyo alitupa ulinzi kama alivyokuwa ameahidi.”

Ofisi ya tawi ilijitahidi sana kuwasiliana na ndugu katika eneo lililokumbwa na vita na, ingawa wanajeshi wa majini waliweka vizuizi barabarani, waliweza kuwatumia vyakula, dawa, na vichapo. Mwangalizi mmoja wa mzunguko aliyetembelea eneo hilo aliripoti hivi: “Madhara ya vita yanaonekana kila mahali, lakini bado ndugu na dada wanaendelea kuhubiri na kukutana. Pia mafunzo mengi ya Biblia yanaongozwa.”

Hatimaye, katika mwaka wa 2001, pande zilizokuwa zikipigana zilifikia mkataba wa amani ambao ulifanya Bougainville na visiwa vilivyo karibu kuwa maeneo huru. Kwa sasa, hakuna Shahidi anayeishi katika Kisiwa cha Bougainville, lakini Kisiwa cha Buka kilicho karibu kina kutaniko lenye wahubiri 39.

VOLKANO YAHARIBU RABAUL

Jiji la Rabaul lina bandari kubwa ambayo ni shimo kubwa lililotokezwa na volkano zamani. Mnamo Septemba 1994, matundu yaliyokuwa kwenye pande za bandari hiyo yalilipuka, yakaharibu Rabaul na kubadili maisha ya watu katika jimbo hilo. Jumba la Ufalme na makao ya wamishonari yaliyokuwa kando yake yaliharibiwa, lakini hakuna ndugu yeyote aliyekufa. Hata hivyo, ndugu moja aliyekuwa na matatizo ya moyo alikufa alipokuwa akikimbia mlipuko huo. Akina ndugu wote walienda maeneo yaliyokuwa kilomita kadhaa kutoka eneo hilo kwa kutii maagizo ambayo kwa miaka kadhaa yalikuwa yamebandikwa kwenye ubao wa matangazo wa Jumba la Ufalme.

Mara moja, ofisi ya tawi ilichukua hatua za kuwasaidia wale waliokuwa wameathiriwa na kuratibu mipango ya kutoa misaada. Nguo, vyandarua vya mbu, dawa, petroli, dizeli, na vitu vingine vilivyotolewa kama mchango vilitumwa, kutia ndani mchele na miyugwa kutoka kutaniko lililokuwa karibu. Kwa kweli, mpango wa kutoa misaada ulifanikiwa sana hivi kwamba wakuu wa serikali wa mahali hapo na watu wengine waliusifu.

Mwishowe, Kutaniko la Rabaul liliacha kuwepo. Siku mbili baada ya mlipuko huo, wahubiri 70 hivi na watoto wao walikusanyika katika shule moja ya ufundi ambayo haikuwa na watu. Wazee walipowasili, wahubiri waliuliza, “Funzo la kitabu litaanza saa ngapi?” Naam, licha ya hali ngumu, ndugu hawakuacha kukutanika na kuhubiri. (Ebr. 10:24, 25) Wengi wa akina ndugu walihamia kwenye vikundi vilivyokuwa karibu, na matokeo yakawa kwamba kikundi kimoja kikawa kutaniko.

Wakuu wa serikali katika jimbo hilo waliahidi dini zote ambazo majengo yao yaliharibiwa kwamba zitapewa uwanja katika mji wa Kokopo ulio kilomita 24 kutoka Rabaul. Hata hivyo, Mashahidi hawakupewa uwanja wowote ilhali dini nyingine zilipewa. Kisha, miaka saba hivi baada ya mlipuko huo, ndugu mmoja kutoka Afrika alianza kufanya kazi katika wizara ya uchoraji ramani ya mji. Alipoona jinsi Mashahidi walivyotendewa isivyo haki, mara moja akawapa uwanja unaofaa huko Kokopo na akawasaidia kujaza fomu ya maombi, ambayo ilikubaliwa. Kikundi cha wajenzi waliojitolea kilisaidia kujenga Jumba la Ufalme na makao ya wamishonari. Kwa kweli, ukosefu wa haki waliofanyiwa hapo awali uligeuka kuwa baraka. Jinsi gani? Uwanja ambao dini zile nyingine zilipewa ulikuwa juu ya mlima. Lakini uwanja ambao Mashahidi walipewa ulikuwa mahali pazuri katikati ya mji.

KAZI YA KUTAFSIRI INASONGA MBELE

“Katika nchi iliyo na zaidi ya lugha 800, ni muhimu kuwa na lugha moja au zaidi ambazo watu wanaweza kutumia kuwasiliana,” anasema Timo Rajalehto, ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi na msimamizi wa Idara ya Tafsiri. “Lugha rahisi zinazotumiwa katika biashara, kama vile Kitok Pisin na Kihiri Motu zinafaa kwa kusudi hilo. Ni rahisi kujifunza lugha hizo, na pia zinatumiwa katika shughuli za kila siku. Lakini haziwasilishi kwa njia inayofaa hoja ngumu. Kwa hiyo, mara nyingi watafsiri wetu hushindwa kueleza maneno mengine magumu.

“Kwa mfano, tuligundua kwamba hakuna neno la Kitok Pisin linaloweza kutafsiri kwa kufaa neno ‘kanuni.’ Kwa hiyo, watafsiri wetu waliunganisha maneno mawili ya lugha ya Tok Pisin ili kufanyiza neno stiatok (maneno ya kuelekeza), ambalo hufafanua jinsi ambavyo kanuni zinafanya kazi kwa kuwaelekeza watu katika njia inayofaa. Neno hilo lilianza kutumiwa na vyombo vya habari na sasa linatumiwa na watu wengi wanaozungumza Kitok Pisin.”

Gazeti Mnara wa Mlinzi lilianza kuchapishwa katika lugha ya Motu mwaka wa 1958, na katika lugha ya Tok Pisin mwaka wa 1960. Makala za funzo zilichapishwa huko Sydney, Australia, kwenye kurasa mojamoja ambazo ziliunganishwa kwa kibanio na kisha kusafirishwa kwa meli hadi Port Moresby. Katika mwaka wa 1970, kurasa ziliongezwa zikawa 24, na nakala zaidi ya 3,500 zilichapishwa. Gazeti Amkeni! lenye kurasa 24 lilichapishwa kwa mara ya kwanza katika lugha ya Tok Pisin mnamo Januari 1972. Kwa sasa, ofisi ya tawi hutayarisha gazeti Mnara wa Mlinzi mara mbili kwa mwezi na gazeti Amkeni! mara nne kwa mwaka katika lugha ya Tok Pisin na toleo la funzo la Mnara wa Mlinzi kila mwezi na toleo la watu wote mara nne kwa mwaka katika lugha ya Hiri Motu.

“Hivi majuzi, tulitafsiri baadhi ya trakti katika lugha mpya, kutia ndani lugha ya Enga, Jiwaka, Kuanua, Melpa, na Orokaiva,” anasema Timo Rajalehto. “Kwa kuwa watu wanaozungumza lugha hizo huzungumza pia lugha ya Tok Pisin au Kiingereza, au lugha zote mbili, kwa nini hilo lilifanywa? Tulitaka kuona jinsi ambavyo watu wataitikia ujumbe wa Ufalme katika lugha yao ya kienyeji. Je, watavutiwa na kweli na wawe na maoni yanayofaa kuwaelekea Mashahidi?

“Jibu la wazi ni ndiyo! Kwa kweli, kumekuwa na maelezo mengi mazuri kuhusu jambo hilo. Mafunzo ya Biblia yameanzishwa, na hata watu fulani ambao hapo awali walitupinga wamebadili mtazamo wao kuwaelekea Mashahidi. Watu wanapopata kichapo katika lugha yao ya kienyeji, jambo hilo huwa na matokeo mazuri.”

Kwa sasa, Idara ya Tafsiri ina watu 31, kutia ndani vikundi vya kutafsiri lugha ya Hiri Motu na Tok Pisin. Mnamo Desemba 2009, wote walifurahia kuhamia ofisi mpya za utafsiri.

SHULE YA UTUMISHI WA PAINIA INAWANUFAISHA WENGI

Kwa watumishi wengi wa Yehova, kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia ni tukio muhimu maishani mwao. Shule hiyo huwasaidia mapainia kukua kiroho na pia huwazoeza kuwa mapainia bora. Hebu ona maelezo ya baadhi ya wale ambao wamehudhuria shule hiyo.

Lucy Koimb: “Shule hiyo imenisaidia kuona kwamba jambo muhimu ninaloweza kufanya maishani ni kuwa katika utumishi wa wakati wote.”

Michael Karap: “Kabla ya kuhudhuria shule hiyo, nilikuwa na ziara nyingi za kurudia lakini sikuwa na mafunzo ya Biblia. Sasa ninaongoza mafunzo mengi ya Biblia!”

Ben Kuna: “Shule hiyo ilinisaidia kufikiria kama vile Yehova anavyofikiria.”

Siphon Popo: “Sijawahi kujifunza kwa bidii sana hivyo maishani mwangu! Nilijifunza kutokuwa na haraka ninapojifunza.”

Julie Kine: “Shule hiyo ilinifunza kuwa na maoni yanayofaa kuhusu vitu vya kimwili. Hatuhitaji vitu vingi kama watu wanavyosema tunahitaji.”

Dan Burks, ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi, alisema hivi: “Mapainia wanapopata matokeo, wao huwa na furaha na bidii zaidi. Tuna hakika kwamba Shule ya Utumishi wa Painia itaendelea kuwanufaisha mapainia wengi katika nchi hii. Bila shaka, wahubiri wengine na watu katika eneo hunufaika pia.”

KUKUA PAMOJA KATIKA UPENDO

Yesu Kristo alisema: “Wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:35) Nchini Papua New Guinea, upendo wa Kikristo umewaunganisha watu licha ya tofauti za lugha, jamii, tamaduni za kikabila, na tofauti za kiuchumi. Watu wenye mioyo minyoofu wanapoona upendo wa aina hiyo, wanachochewa kusema, “Mungu yupo pamoja nanyi.”

Maneno hayo yalisemwa na Mange Samgar aliyetajwa awali, ambaye ni dereva wa basi na zamani alikuwa kasisi wa kanisa la Kilutheri huko Banz. Ni nini kilichomfanya aseme hivyo? Kutaniko moja lilikodisha moja ya basi za Mange ili kuhudhuria kusanyiko la Wilaya huko Lae. “Akitaka kujua kuhusu Mashahidi, Mange aliandamana nao,” wanasema Steve na Kathryn Dawal, waliokuwa kwenye uwanja wa kusanyiko basi hilo lilipowasili. “Mange alivutiwa sana na utaratibu na umoja wa kijamii na kikabila miongoni mwa watu wa Yehova. Kufikia wakati aliporudi nyumbani katika basi lililojaa Mashahidi, alikuwa amesadikishwa kwamba amepata kweli. Baadaye, yeye na mwana wake walikuja kuwa wazee Wakristo.”

Dada Hoela Forova, mwanamke mjane aliyekuwa painia wa kawaida, alikuwa akimtunza mama yake ambaye pia alikuwa mjane, na walihitaji pesa haraka za kujenga nyumba mpya. Pindi mbili, alimpa mtu wa ukoo pesa za kununua mbao, lakini hakuona tena pesa hizo wala mbao. Wakijua shida aliyokuwa nayo, Mashahidi wa eneo hilo walimjengea nyumba kwa siku tatu tu. Kwa siku hizo tatu, Hoela alilia mara kwa mara kwa sababu ya upendo huo mwingi wa akina ndugu. Ujenzi huo ulitoa ushahidi mzuri. Shemasi wa kanisa moja alisema hivi kwa mshangao, “Watu ambao hawaombi-ombi pesa na ambao kazi yao ni kutembea-tembea wakiwa wamebeba mikoba wanaweza jinsi gani kujenga nyumba kwa siku tatu!”

Mtume Yohana aliandika hivi: “Watoto wadogo, acheni tupendane, si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yoh. 3:18) Kwa sababu ya upendo huo ambao umeonyeshwa katika njia mbalimbali, kazi ya kuhubiri nchini Papua New Guinea inaendelea kusonga mbele. Wahubiri 3,672 waliongoza mafunzo ya Biblia 4,908, na watu 25,875 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mwaka wa 2010—huo ni uthibitisho wenye nguvu kama nini wa baraka za Yehova!—1 Kor. 3:6.

Miaka 70 hivi iliyopita, kikundi kidogo cha ndugu na dada wenye ujasiri walitembelea nchi hiyo yenye kustaajabisha ili kupeleka kweli inayowaweka watu huru. (Yoh. 8:32) Kwa makumi ya miaka iliyofuata, Mashahidi wengi nchini humo na kutoka nchi za kigeni walijiunga nao katika kazi ya kuhubiri. Mbele yao kulikuwa na vizuizi vingi ambavyo vilionekana haviwezi kushindwa: misitu mikubwa, vinamasi vyenye mbu wanaosababisha malaria, barabara mbovu, na hata sehemu nyingine hazikuwa na barabara, na vilevile umaskini, vita vya kikabila, zoea la kuwasiliana na pepo, na nyakati nyingine upinzani mkali kutoka kwa viongozi na wafuasi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Pia akina ndugu walikabiliana na tatizo la kuwafundisha watu kusoma na kuandika na pia kuwahubiria maelfu ya watu waliozungumza lugha zaidi ya 800! Jitihada zao za kujidhabihu katika kazi ya kuhubiri Ufalme zimethaminiwa sana na wale ambao wameendeleza kazi waliyoanzisha.

Ingawa hivyo, bado watumishi wa Yehova wanakabili mengi ya matatizo hayo huko Papua New Guinea. Lakini mambo yote yanawezekana kwa Mungu. (Mk. 10:27) Kwa hiyo, wakimtegemea kabisa, ndugu na dada katika nchi hiyo wana hakika kwamba Yehova atabadilisha lugha ya watu wengi zaidi wanaopenda uadilifu na “kuwapa lugha safi, ili wote waliitie jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega.”—Sef. 3:9.

[Maelezo ya Chini]

a Greenland ndicho kisiwa kikubwa zaidi ulimwenguni. Australia huonwa kuwa bara, si kisiwa.

b Katika simulizi hili lote, tutatumia jina la sasa Papua New Guinea badala ya majina hayo ya awali.

c Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwi tena.

[Blabu katika ukurasa wa 88]

“Bobogi, ulijifunzia wapi kufanya mambo haya yote?”

[Blabu katika ukurasa wa 100]

‘Alikubali kuonyesha sinema yetu bila malipo’

[Blabu katika ukurasa wa 104]

“Uache dini yako, au utafute kazi nyingine”

[Blabu katika ukurasa wa 124]

Walipofungua mkoba na kuona kilichokuwa ndani, walihisi vibaya kwamba walimwibia

[Blabu katika ukurasa wa 149]

“Ngozi yao ni nyeupe, lakini mioyo yao ni kama yetu”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 80]

Maelezo Mafupi Kuhusu Papua New Guinea

Nchi

Papua New Guinea hufanyiza nusu ya upande wa mashariki wa kisiwa cha New Guinea. Nchi hiyo inatia ndani visiwa vidogo 151 na ukubwa wake unazidi kidogo ule wa nchi ya Morocco. Sehemu ya ndani zaidi ya nchi hiyo ina milima yenye miamba; upande wa pwani una misitu mikubwa ya mvua na vinamasi.

Watu

Asilimia 99 ya wakaaji wake milioni 6.7 ni Wapapua na Wamelanesia. Waliobaki ni Wapolinesia, Wachina, na Wazungu. Wengi wao ni wa dini zinazodai kuwa za Kikristo.

Lugha

Papua New Guinea ndiyo nchi yenye lugha nyingi zaidi duniani kwani kuna lugha 820—hiyo ni asilimia 12 ya lugha zote ulimwenguni. Mbali na lugha zao za kienyeji, watu wengi huzungumza Kitok Pisin, Kihiri Motu, au Kiingereza.

Kazi

Asilimia 85 hivi ya wakaaji wa nchi hiyo huishi maisha ya kitamaduni, nao hupanda mboga kwenye mashamba madogo katika vijiji vidogo. Kahawa na chai hukuzwa kwenye nyanda za juu kama mazao ya biashara. Madini, gesi, na petroli, na pia bidhaa zinazotoka katika misitu huchangia uchumi wa nchi hiyo.

Chakula

Vyakula vikuu vinatia ndani viazi vitamu, miyugwa, mihogo, sago, na ndizi ambazo huliwa zikiwa hazijapikwa au zimepikwa. Mboga, matunda, na vilevile pia nyama na samaki waliotiwa kwenye mikebe hupendwa sana. Nyama ya nguruwe huliwa katika pindi za pekee.

Hali ya hewa

Kuna majira mawili—majira ya mvua kidogo na majira ya mvua nyingi. Kwa sababu Papua New Guinea iko karibu na ikweta, kuna joto na unyevunyevu katika sehemu za pwani, lakini kuna baridi kwenye nyanda za juu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 83, 84]

“Niliacha Kuwa Mwenye Haya”

ODA SIONI

ALIZALIWA 1939

ALIBATIZWA 1956

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Painia wa kwanza kati ya wenyeji wote wa Papua New Guinea. Sasa anatumika akiwa painia wa pekee katika Kutaniko la Hohola Motu, huko Port Moresby.

◼ DADA yangu mkubwa alipowaona Tom na Rowena Kitto wakihubiri kwenye vijia vya mbao vya kijiji cha Hanuabada, aliniambia nihudhurie mikutano yao ili niweze kuchunguza hiyo “dini mpya.” Wakati huo mikutano ilikuwa ikifanywa nyumbani mwa Heni Heni Nioki, aliyekuwa akijifunza Biblia.

Nilikuwa na umri wa miaka 13 na nilikuwa mwenye haya sana. Nilienda nyumbani kwa Heni Heni ambako wanakijiji 40 hivi walikuwa wamekusanyika, na nikaketi kimya nyuma ya kila mtu nikiwa nimefunika uso wangu kwa mikono. Nilifurahia mambo niliyosikia na hivyo nikarudi tena na tena. Baada ya muda, Heni Heni akaniomba nimtafsirie Tom Kitto kutoka Kiingereza hadi Kimotu, lugha iliyozungumzwa na wengi kati ya waliohudhuria.

Miaka kadhaa baadaye, nilipoanza kufanya kazi katika hospitali ya karibu nikiwa na mradi wa kuwa daktari, John Cutforth alizungumza nami faraghani na kuniambia hivi, “Ukiwa daktari wa kitiba, utawasaidia watu kimwili, lakini ukiwa ‘daktari’ wa kiroho, unaweza kuwasaidia kupata uzima wa milele.” Juma hilohilo nikaanza kufanya upainia.

Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa huko Wau. Nilikuwa nimetembelea mji huo na nikapata watu kadhaa wanaopendezwa na kweli. Mwanamume mmoja anayeitwa Jack Arifeae, aliniomba nikahubiri katika kanisa la Kilutheri la eneo hilo. Nilichagua kuzungumzia sheria ya Mungu kuhusu damu. Watu 600 waliohudhuria walinisikiliza kwa makini, kwa kuwa wengi wao waliamini kwamba iwapo wangekula damu ya mtu mwingine basi roho yake ingetawala mwili wao. Kasisi alikasirika sana na kuwaambia wasikilizaji kwamba hawapaswi kushirikiana nami hata kidogo. Lakini wengi wao walifurahia mambo waliyosikia na wakafanya maendeleo ya kiroho.

Mwaka mmoja hivi baadaye, nilipewa mgawo huko Manu Manu, kilomita 50 hivi kaskazini-magharibi ya Port Moresby. Nilikutana na chifu wa eneo hilo, Tom Surau ambaye aliniomba nihubiri katika kijiji chake. Baada ya kujifunza na wanakijiji kwa siku tatu, walivunja-vunja sanamu yao ya mbao ya Bikira Maria na kuitupa ndani ya mto.

Watu waliokuwa wakiishi eneo la chini zaidi walikusanya vipande hivyo na kuvipeleka kwa makasisi Wakatoliki katika kijiji chao, wakisema, “Wamemwua Maria!” Makasisi wawili walikuja kwangu. Mmoja wao alinijia moja kwa moja na kunipiga ngumi usoni na pete yake ikanikata usoni. Wanakijiji walipokuja kunisaidia, makasisi hao walitoroka.

Nilisafiri hadi Port Moresby ili jeraha langu likashonwe na ili nipige ripoti kwa polisi. Baadaye, makasisi hao walilazimika kulipa faini na wakaondolewa katika wadhifa wao. Wakati huo, nilirudi kijijini na kuanzisha kikundi katika eneo hilo la mbali. Kwa msaada wa Yehova, niliacha kuwa mwenye haya.

[Picha]

Mikutano ya kwanza ilifanywa katika nyumba ya Heni Heni

[Sanduku katika ukurasa wa 86]

Mfumo wa Wantok

Neno wantok, linalomaanisha “usemi mmoja” katika Kitok Pisin, linahusiana na muungano wenye nguvu wa kitamaduni unaowaunganisha watu wa kabila moja wanaozungumza lugha moja. Muungano huo unahusisha wajibu na mapendeleo fulani. Kwa mfano, watu wanatazamiwa kushughulikia mahitaji ya kimwili ya waliozeeka au wale wasio na kazi au wasioweza kufanya kazi katika kabila lao. Hilo husaidia sana katika nchi isiyoweza kuwasaidia kifedha watu wasio na uwezo.

Lakini mfumo huo pia una matatizo yake. Kwa mfano, mwanafunzi wa Biblia anapochukua msimamo kwa ajili ya kweli, watu wengine katika familia wanaweza kumtenga. Katika hali kama hizo, wapya wanapaswa kumtegemea Yehova iwapo wanapoteza kazi au kwa sababu fulani wanapatwa na uhitaji wa kimwili. (Zab. 27:10; Mt. 6:33) “Mfumo wa wantok unaweza pia kuwapa akina ndugu matatizo ya kushirikiana kwa njia isiyofaa na watu wa ukoo ambao si Mashahidi, kutia ndani wale ambao wametengwa na ushirika,” anasema Kegawale Biyama ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi. “Pia, wakati wa uchaguzi wa kisiasa, Mashahidi ambao ni watu wa ukoo wa mgombezi wa kiti fulani wanashinikizwa wavunje msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote.” Bila shaka, Mashahidi hao hawavunji msimamo wao.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 91]

Alipendwa na Watu Wengi

Alipokuwa akitumika akiwa mmishonari huko Papua New Guinea, John Cutforth alipendwa na watu wengi. Hebu ona mambo ambayo baadhi ya wamishonari wenzake na wengine waliotumika pamoja naye walisema kumhusu.—Met. 27:2.

Erna Andersson: “John alituambia hivi: ‘Mmishonari halisi huwa mambo yote kwa watu wa namna zote. Ikiwa watu wanakukaribisha uketi kwenye kisiki cha mti, keti, hawana kiti kingine bora kuliko hicho. Wakikupa kitanda kilichotengenezwa kwa njia isiyopendeza sana, kubali na ukilalie, kimetengenezwa kwa fadhili. Wakikupa chakula kisicho cha kawaida, kula, kwa sababu kimetayarishwa kwa upendo.’ John aliweka mfano bora sana wa mmishonari mwenye kujidhabihu.”

Awak Duvun: “Wakati wa utawala wa wakoloni, John aliwafundisha watu kihalisi kwamba hakupaswi kuwa na ubaguzi kati ya watu weusi na weupe! Mara nyingi alisema, ‘Hakuna tofauti kati ya mtu mweusi na mzungu!’ Aliwapenda watu wote.”

Peter Linke: “Alasiri moja, baada ya kusafiri mchana kutwa, John alifika nyumbani kwetu Goroka, akiwa amejawa na vumbi na uchovu. Lakini baada ya chakula cha jioni akasema, ‘Sijamsaidia mtu yeyote leo’ kisha akatoka nje na kutokomea kwenye giza la jioni na kwenda kuitembelea familia moja ili kuwatia moyo. Sikuzote aliwafikiria wengine. Sote tulimpenda.”

Jim Dobbins: “John alitufunza jinsi ya kuishi maisha rahisi na kufundisha kwa njia rahisi, kwa kutumia mifano ambayo watu wangeweza kuelewa kama vile Yesu alivyofanya. Tulipofanya hivyo tuliweza kuwasiliana na wale ambao hawakujua kusoma na kuandika.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 101]

‘Hatutaacha Kamwe’

KALIP KANAI

ALIZALIWA 1922

ALIBATIZWA 1962

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa miongoni mwa ya watu wa kwanza kuikubali kweli katika eneo la Madang. Limesimuliwa na mwana wake, Ulpep Kalip.

◼ BABA yangu alikuwa mtu mnyenyekevu na alifikiria mambo kwa uzito. Alipokabili tatizo, angesikiliza kwa makini kisha achanganue jambo hilo kabla ya kutoa maoni yake.

Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nililazwa hospitalini huko Madang kwa sababu papa aliukata mguu wangu. Baba yangu alipokuwa akinitembelea, alikutana na John Davison. “Katika ulimwengu mpya,” John alisema, “Yehova anaweza kumpa mwana wako mguu mpya.” Baba yangu alipendezwa sana, hivyo akaanza kujifunza Biblia kwa bidii, na muda mfupi baadaye akawa na imani yenye nguvu.

Kwa sababu baba yangu pamoja na watu wa familia yake walikuwa wamejiuzulu kutoka Kanisa Katoliki, polisi walichochewa watufukuze kutoka nyumbani mwetu. Nyumba zetu 12, zilizozungukwa na bustani zenye maua, zilikuwa bado hazijamaliza mwaka mmoja tangu zilipojengwa. Polisi walitupa mienge juu ya paa za nyasi, ambazo ziliteketea. Tulikimbia ili kuokoa mali zetu, lakini majivu yenye moto pamoja na moshi ulitushinda nguvu na kutufanya tutoke nje. Tulilia sana tulipoona nyumba zetu zikiteketea na kuwa majivu.

Tukiwa na majonzi mengi tulitembea hadi Bagildig, kijiji jirani, ambako chifu wa kijiji hicho alikubali kwa fadhili tuhamie na kuishi kwenye kibanda kimoja. Tulipokuwa huko, baba yetu alituambia: ‘Yesu aliteswa. Kwa hiyo sisi pia tunatarajia kuteswa, lakini hatutaacha kamwe kushikilia imani yetu!’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 107, 108]

Alishukuru Kwamba Alienda Shule “Isiyofaa”

MICHAEL SAUNGA

ALIZALIWA 1936

ALIBATIZWA 1962

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alianza upainia wa pekee mnamo Septemba 1964 na ametumika akiwa painia wa pekee kwa muda mrefu zaidi kuliko mtu mwingine yeyote huko Papua New Guinea.

◼ MNAMO 1959, nilihamia Rabaul ili kuendeleza masomo yangu. Niliposikia kwamba Mashahidi walikuwa na shule yao, nilienda nyumbani kwa “mwalimu” wao, Lance Gosson, nikifikiri kwamba nilikuwa ninaenda kuhudhuria shule ya ufundi. Lance alinikaribisha nihudhurie funzo la Biblia lililokuwa likifanywa kila Jumatano. Ingawa sikuwa nimeelewa vizuri alimaanisha nini, nilikubali mwaliko wake. Nilifurahia sana yale niliyojifunza, hasa kujua kwamba jina la Mungu ni Yehova na kwamba kutakuwa na “mbingu mpya na dunia mpya.” (2 Pet. 3:13) Nilibatizwa asubuhi ya Julai 7, 1962, nikiwa na furaha sana kwamba nilikuwa nimeenda kwenye shule “isiyofaa.”

Siku hiyohiyo, nilihudhuria mkutano wa wale waliotaka kushiriki katika utumishi wa upainia. Kiongozi wa mkutano huo, John Cutforth, aliyekuwa pia mwangalizi wa wilaya, alikazia kwamba mashamba yalikuwa meupe kwa ajili ya mavuno na kwamba wafanyakazi zaidi walihitajika. (Mt. 9:37) Mara tu hali ziliponiruhusu nilijiandikisha kuwa painia wa likizo, kama vile mapainia wasaidizi walivyoitwa wakati huo. Mnamo Mei 1964, niliwekwa kuwa painia wa kawaida, na katika mwezi wa Septemba nikawa painia wa pekee.

Ninakumbuka pindi moja nilikuwa nikihubiri karibu na Rabaul. Mwanamume mmoja Mtolai aliniomba Biblia yangu ili aishike na kujisomea mwenyewe andiko fulani. Nilipompa, aliirarua vipande-vipande na kuitupa chini. Badala ya kumkasirikia, niliripoti kisa hicho kwa kamanda wa polisi, ambaye alimtuma afisa mmoja wa polisi amkamate bwana huyo mara moja. Kamanda huyo alimwambia yule bwana: “Wewe ni mtu mbaya. Ulivunja sheria ya Mungu na ya serikali. Kesho lazima umnunulie mtu huyo Biblia mpya, la sivyo utafungwa jela.” Baada ya hayo kamanda huyo aliniambia nirudi kwenye kituo hicho cha polisi saa 4 kamili asubuhi iliyofuata ili nichukue pesa za kununua Biblia nyingine. Nilipofika kesho yake, pesa zilikuwa tayari. Tangu wakati huo, watu wengi Watolai wamejifunza kweli.

Katika pindi nyingine, nilikuwa pamoja na kikundi cha Mashahidi tukigawa trakti Habari za Ufalme katika eneo la magharibi ya Wewak. Mashahidi wale wengine walinitangulia. Hata hivyo, kiongozi mmoja wa kijiji, aliwaona akina ndugu wakigawa nakala za trakti hiyo na kuzikusanya. Ni kana kwamba alijua kwamba nilikuwa nikiwafuata kwa sababu alisimama katikati ya barabara na kuningoja, mikono yake ikiwa kiunoni huku akiwa ameshika zile nakala za Habari za Ufalme. Nilimuuliza ikiwa kulikuwa na shida yoyote. Akanikabidhi trakti zile na kusema, “Mimi ndiye ninayesimamia eneo hili, na sitaki kukuona ukigawa makaratasi haya.”

Nikazichukua kutoka kwake. Wakati huo wanakijiji walikuwa wamekusanyika mahali pale. Niliwatazama na kuwauliza, “Ikiwa mnataka kulima mashamba yenu au kwenda kuvua samaki, je, mnahitaji kupata ruhusa rasmi?”

“Hapana!” akasema mwanamke mmoja.

Kisha nikawauliza, “Mngependa kusoma trakti hizi?”

“Ndiyo,” wakasema. Kwa hiyo nikawagawia tena zile trakti za Habari za Ufalme bila upinzani wowote. Hata hivyo, nilihitaji kujitetea baadaye mbele ya jopo la wazee 20 wa kijiji. Jambo la kupendeza ni kwamba 18 kati yao walikubali tuendelee na kazi yetu ya kuhubiri.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 112]

‘Je, Wamekula Moyo Wako?’

AIOKOWAN

ALIZALIWA 1940

ALIBATIZWA 1975

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mmoja kati ya watu wa kwanza kutoka Enga kujifunza kweli.

◼ WAKATI Tom na Rowena Kitto walipofika Wabag, Mkoa wa Enga, wamishonari wenyeji walieneza habari za uwongo kuwahusu. Kwa mfano, wamishonari hao walidai kwamba Tom na Rowena waliifukua miili ya wafu na kuila. Uvumi huo uliniogopesha sana.

Siku moja Tom alimwuliza baba yangu ikiwa alijua msichana fulani ambaye angeweza kumsaidia mke wake kufanya kazi za nyumbani. Baba alimweleza kwamba ningekuwa tayari kufanya hivyo. Niliogopa sana, lakini baba alinilazimisha nifanye kazi hiyo.

Baadaye, Tom na Rowena waliniuliza, “Unafikiri ni nini huwapata watu wanapokufa?”

“Watu wazuri huenda mbinguni,” nilijibu.

“Je, ulisoma hivyo katika Biblia?” waliuliza.

“Sijawahi kwenda shule, kwa hiyo sijui kusoma,” nikajibu.

Walianza kunifundisha kusoma, na pole kwa pole nilianza kuelewa kweli za Biblia. Nilipoacha kuhudhuria Kanisa Katoliki, mmoja wa viongozi wa kanisa hilo aliniuliza: “Kwa nini uliacha kuja kanisani? Je, wazungu hao wawili wamekula moyo wako?”

“Ndiyo,” nikajibu, “nimewapa moyo wangu wa mfano kwa sababu ninajua kwamba wananifundisha kweli.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 117]

“Nipe Kuku Mmoja, Nacho Kitakuwa Chako”

AWAIWA SARE

ALIZALIWA 1950

ALIBATIZWA 1993

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alijifunza kweli akiwa eneo la mbali. Sasa anatumika katika Kutaniko la Mundip akiwa mtumishi wa huduma.

◼ NILIPOKUWA nikiishi na rafiki yangu mmoja, niliona kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Nilisoma sura kadhaa ndani yake na nikamwuliza ikiwa angenipa kiwe changu. “Nipe kuku mmoja, nacho kitakuwa chako,” alijibu.

Nilimpa kuku mmoja, nami nikaenda na kitabu hicho nyumbani na kukisoma kwa makini. Muda mfupi baadaye, nilianza kuwaeleza wengine kuhusu mambo mazuri niliyokuwa nimejifunza, ingawa wazee wa kanisa waliniita mara mbili na kuniamuru niache kuhubiri!

Muda mfupi baadaye, niliandikia ofisi ya tawi barua nikiwauliza jinsi ningekutana na Mashahidi wa Yehova katika eneo langu. Walinipa anwani za Alfredo de Guzman, ambaye alinialika nihudhurie kusanyiko la wilaya huko Madang.

Nilifika kwenye kusanyiko nikiwa nimevalia nguo zilizopasuka-pasuka ambazo kwa kawaida nilivalia huko msituni na nikiwa na ndevu zangu nyeusi nilizokuwa nimeachilia. Licha ya hali yangu kila mtu alinitendea kwa fadhili na heshima. Programu ilipokuwa ikiendelea nilianza kulia kwa sababu yale niliyosikia yalinigusa moyo. Siku iliyofuata, nilifika kusanyikoni nikiwa nimenyoa ndevu zangu.

Baada ya kusanyiko, Alfredo alinitembelea kijijini mwangu. Alihitaji kusafiri kwa saa mbili kwa gari kutoka Madang, kisha atembee kwa miguu kwa saa tano. Familia yangu pamoja na marafiki walimwuliza maswali mengi, na alijibu yote akitumia Biblia.

Leo Kutaniko la Mundip lina wahubiri 23, na zaidi ya watu 60 wanahudhuria mikutano.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 125, 126]

“Utajitetea Jinsi Gani?”

MAKUI MAREG

ALIZALIWA 1954

ALIBATIZWA 1986

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alifanya upainia akiwa peke yake kwa miaka mingi kwenye kisiwa kisichokuwa na Mashahidi.

◼ MNAMO 1980, painia mmoja alinipa trakti nikiwa Madang na nikaenda nayo hadi nyumbani katika Kisiwa cha Bagabag, umbali wa saa sita ukisafiri kwa kutumia mashua. Nilipendezwa sana na yale niliyosoma na nikaiandikia ofisi ya tawi barua ili nipate habari zaidi. Muda mfupi baadaye nilipokea barua kutoka kwa Badam Duvun, painia aliyeishi Madang, akinikaribisha kuhudhuria kusanyiko la wilaya. Nilimtembelea kwa majuma mawili na nikaanza kujifunza Biblia. Pia nilihudhuria mikutano yote katika Jumba la Ufalme la eneo hilo. Niliporudi nyumbani, niliendelea kujifunza, lakini kupitia barua.

Muda mfupi baadaye, nilianza kujifunza Biblia na familia 12 katika Kisiwa cha Bagabag. Tulifanya mikutano kwa ukawaida katika nyumba ya mjomba wangu, kwa kutumia njia ileile ya kujifunza Biblia niliyokuwa nimeona huko Madang. Baba yangu aliyekuwa na cheo cha juu katika Kanisa la Kilutheri, alikasirishwa sana na jambo hilo. “Mimi ninamjua Yahweh lakini simjui Yehova,” alifoka. Nilifungua Biblia yangu ya Kitok Pisin na kumwonyesha maelezo ya chini yanayopatikana katika andiko la Kutoka 3:15, ambayo yanaeleza kuhusu jina la Mungu. Baba yangu hakuwa na la kusema.

Alinipeleka mara tatu mbele ya viongozi wa kanisa ili niitetee imani yangu. Mkutano mmoja kati ya hiyo ulifanywa katika kanisa kubwa zaidi kwenye kisiwa hicho. Zaidi ya watu mia moja walihudhuria. Kila mtu alikuwa na wasiwasi. Mwenyekiti aliniuliza, “Utajitetea jinsi gani?” “Ninataka tu kufanya kama Mathayo 6:33 inavyosema na kuutanguliza Ufalme wa Mungu,” nikajibu huku nikiwa nimeshikilia Biblia yangu kwa nguvu. Baba yangu alisimama kwa ghafula na kwa hasira nyingi akasema hivi kwa sauti kubwa, “Unajaribu kutufundisha?” Mjomba wangu mmoja alisimama ili anipige, lakini mtu fulani wa ukoo akamzuia mara moja. Fujo zikaanza katika mkutano huo. Mwishowe, niliambiwa niondoke.

Hata hivyo, matatizo yangu hayakuishia hapo. Mwanamke mmoja aliyekuwa akihudhuria mikutano yetu alikuwa na mtoto mgonjwa, kisha mtoto huyo akafa. Watu fulani katika kijiji chetu walisema eti mimi ndiye niliyesababisha kifo hicho kwa sababu ya kumfundisha mwanamke huyo dini mpya. Baba yangu alichukua chuma na kunifukuza kutoka nyumbani. Nilikimbilia Madang pamoja na shangazi yangu Lamit Mareg, ambaye pia alikuwa amekubali kujifunza Biblia. Muda mfupi baadaye, sote wawili tulibatizwa.

Kisha, baba yangu akawa mgonjwa sana. Nilimkaribisha nyumbani kwangu Madang na kumtunza hadi alipokufa. Katika kipindi hicho, alikuwa na maoni tofauti kuelekea dini yangu. Kabla hajafa, alinisihi nirudi kwenye Kisiwa cha Bagabag na kuwahubiria wakaaji wa huko. Nilifanya hivyo katika mwaka wa 1987. Kwa fadhili, watu wangu wa ukoo walinijengea nyumba ndogo, na kwa miaka 14 nilikuwa Shahidi pekee katika kisiwa hicho. Kwa miaka 12 kati ya ile niliyokuwa huko, nilitumika nikiwa painia wa kawaida.

Baadaye, nilirudi Madang ili nifanye upainia pamoja na Lamit. Mnamo 2009, watu sita kutoka Kisiwa cha Bagabag walisafiri hadi Madang ili kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Sijawahi kuolewa na ninafurahi sana kwamba nimetumia useja wangu kumtumikia Yehova kikamili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 141, 142]

Yehova Alinichukua

DORAH NINGI

ALIZALIWA 1977

ALIBATIZWA 1998

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alijifunza kweli alipokuwa msichana na akatengwa na familia yake. Baadaye alianza kufanya upainia na sasa anatumika katika ofisi ya tawi.

◼ NILIPOKUWA na umri wa miaka 17, nilipata nakala ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Upesi niligundua kwamba nilikuwa nimepata kitu cha pekee sana. Nilitambua kwamba kitabu hicho kilikuwa cha Mashahidi wa Yehova kwa kuwa nilipokuwa na umri wa miaka minne, Mashahidi wawili walikuwa wamezungumza na mimi kuhusu ahadi ya Mungu ya Paradiso duniani.

Muda mfupi baada ya kupata kitabu Kuishi Milele, wazazi walionilea waliniambia kwamba kwa kuwa walikuwa na watoto wao watano, nilihitaji kurudi kwa familia yangu, ambayo iliishi kwenye mji wa pwani wa Wewak. Nilipofika huko niliishi na baba mdogo.

Nikiwa na hamu ya kukutana na Mashahidi, nilitafuta Jumba la Ufalme na nikafika huko ndugu mmoja alipokuwa akitangaza wimbo wa mwisho. Hata hivyo, mmishonari mmoja kutoka Marekani anayeitwa Pam alipanga tujifunze Biblia pamoja. Nilifurahia kabisa mambo niliyokuwa nikijifunza, lakini baada tu ya kujifunza mara tatu, tukawa na mzozo na baba mdogo.

Nilipokuwa nikirudi nyumbani baada ya mkutano wa Jumapili, niliona moshi nje ya nyumba ya baba mdogo. Alikuwa akiteketeza vitu vyangu vyote, kutia ndani vitabu vyangu vya kujifunzia Biblia. Aliponiona, alipaaza sauti, “Ikiwa unataka kuabudu pamoja na watu hao, basi acha wao wakutunze.” Kwa kuwa sikuruhusiwa kuishi hapo tena, sikuwa na la kufanya ila kwenda nyumbani kwa wazazi wangu wa asili, walioishi katika kijiji kilichokuwa umbali wa saa mbili kutoka Wewak unaposafiri kwa gari.

Nilipomkaribia baba yangu, aliwaambia hivi wadogo wangu huku nikisikia: “Huyu msichana ni nani? Sisi hatumjui. Aliacha kuwa mtoto wetu alipokuwa na miaka mitatu.” Nilielewa jambo alilokuwa akisema kwamba yeye pia hakutaka niishi kwake; kwa hiyo niliondoka na kuishi mahali popote ambapo ningeweza.

Miaka miwili hivi baadaye, ndugu wawili waliokuwa mapainia wa pekee walikutana nami katika kijiji cha wazazi wangu. Niliwaambia, “Tafadhali mwambieni Pam kwamba sijasahau mambo aliyonifundisha, lakini sina uwezo wa kuja kumwona.” Hata hivyo, muda mfupi baada ya hapo nilikutana na Pam huko Wewak na tukaanza tena kujifunza. Wakati huo, niliishi na familia tatu tofauti, lakini kwa sababu ya kushirikiana na Mashahidi nilifukuzwa katika kila nyumba. Kwa fadhili, Pam alifanya mipango ili niishi na familia fulani ya Mashahidi huko Wewak. Nilibatizwa katika mwaka wa 1998 na nikawa painia wa kawaida mnamo Septemba 1999. Nilialikwa kufanya kazi Betheli mnamo 2000 na nimekuwa na pendeleo la kufanya kazi na kikundi cha watafsiri wa Kitok Pisin.

Ingawa niliumia sana kwa kuwa familia yangu ilinifukuza, nimebarikiwa sana kupata familia ya kiroho. Moja ya maandiko ninayopenda sana ni Zaburi 27:10 inayosema hivi: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.”

[Picha]

Vichapo vya Kitok Pisin

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 147, 148]

“Yehova Ndiye Mwalimu Wetu Mkuu Zaidi”

JOHN TAVOISA

ALIZALIWA 1964

ALIBATIZWA 1979

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alipokuwa mtoto aliteswa kikatili na walimu na wanafunzi wenzake na akalazimika kuacha shule baada ya kusoma kwa miaka miwili tu. Sasa anatumika akiwa mwangalizi wa mzunguko.

◼ NILIZALIWA katika kijiji cha Govigovi kwenye Mkoa wa Milne Bay. Baba yangu alianza kujifunza Biblia nilipokuwa na umri wa miaka saba na alinifundisha mambo aliyokuwa akijifunza.

Huo ndio wakati nilipoanza masomo yangu kwenye shule ya umma. Walimu wangu wawili, ambao walikuwa Waanglikana, walipogundua kwamba nilikuwa nikishirikiana na Mashahidi, walianza kunitesa. Wanafunzi wengine wakafanya hivyo pia, nyakati nyingine wakinipiga kwa fimbo. Kwa sababu hiyo nililazimika kuacha shule baada ya miaka miwili tu.

Mwaka mmoja hivi baadaye, nilikutana na mmoja kati ya walimu hao sokoni. “Wewe ni mwanafunzi mwerevu na ungefanya vizuri sana shuleni,” akaniambia. “Lakini kwa sababu ya dini yako, utakuwa mtumishi wa wanafunzi wenzako.” Nilipomwambia baba yangu kile ambacho mwalimu huyo alikuwa amesema, aliniambia maneno yenye kutia moyo sana. “Ikiwa ulimwengu hautakuelimisha,” akasema, “Yehova atafanya hivyo.”

Baba na ndugu mmoja painia wa pekee walinisaidia nipate elimu yenye thamani zaidi ya zote—ujuzi unaoongoza kwenye uzima wa milele. (Yoh. 17:3) Lugha yangu ya mama ni Dawawa, lakini walinifundisha Biblia katika Kihiri Motu, ambayo ilikuwa lugha yangu ya pili, na pia katika Kitok Pisin, ambayo ikawa lugha yangu ya tatu. Nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 15. Miaka miwili baadaye nikawa painia.

Mnamo 1998, nilialikwa kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Wakati huo sikujua Kiingereza vizuri. Kwa hiyo, ili nijitayarishe kwa ajili ya shule hiyo, ofisi ya tawi iliniambia nishirikiane na kutaniko la Kiingereza huko Port Moresby. Kwa hiyo, Kiingereza kikawa lugha yangu ya nne.

Baada ya kuhitimu, nilitumwa katika Kutaniko la Alotau kwenye Mkoa wa Milne Bay. Miezi sita baadaye, nilishangaa na kufurahi sana nilipowekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko. Mzunguko wangu wa kwanza ulitia ndani New Britain, New Ireland, Kisiwa cha Manus, na visiwa vingine vya karibu. Katika mwaka wa 2006, nilimwoa Judy, na tukawa mapainia wa pekee kwa mwaka mmoja, na baada ya hapo tukaendelea na kazi ya mzunguko.

Ninapoyazuru makutaniko, mara nyingi mimi huwaambia vijana: “Yehova ndiye Mwalimu wetu mkuu zaidi. Kwa hiyo mwache akufundishe, kwa sababu anaweza kukusaidia upate mafanikio ya kweli maishani.” Kwa kweli, hilo ni somo muhimu sana ambalo nimejifunza.

[Picha]

Nikiwa na mke wangu, Judy

[Chati/Picha katika ukurasa wa 156, 157]

MFUATANO WA MATUKIO—Papua New Guinea

1930

1935 Mapainia wakiwa ndani ya meli ya Sosaiti inayoitwa Lightbearer wakihubiri huko Port Moresby.

1940

1950

1951 Tom na Rowena Kitto wanawasili Port Moresby.

1956 Mapainia wanahamia New Ireland na New Britain.

1957 John Cutforth anatoa hotuba akitumia picha.

1960

1960 Shirika la International Bible Students Association laandikishwa.

1962 Tom na Rowena Kitto wanahamia maeneo ya milimani ya New Guinea.

1965 Ofisi ya tawi yajengwa huko Koki, Port Moresby.

1969 Kusanyiko la Kimataifa la “Amani Duniani” linafanywa huko Haima, Papua.

1970

1975 Papua na New Guinea zaungana kufanyiza Papua New Guinea.

1977-1979 Umati wenye fujo unaharibu Majumba ya Ufalme kwenye Mkoa wa Milne Bay.

1980

1987 Ofisi mpya ya tawi inawekwa wakfu.

1989 Vita vya wenyewe kwa wenyewe vinaanza kwenye Kisiwa cha Bougainville.

1990

1991 Mnara wa Mlinzi linachapishwa katika Kitok Pisin na Kihiri Motu wakati uleule na la Kiingereza.

1994 Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali yaanza kutenda.

1994 Milipuko ya volkano yaharibu Rabaul, New Britain.

1999 Dawati la Ujenzi wa Majumba ya Ufalme linaanzishwa kwenye ofisi ya tawi.

2000

2002 Jumba la Kusanyiko linajengwa huko Gerehu, Port Moresby.

2010

2010 Kuwekwa wakfu kwa ofisi ya tawi baada ya upanuzi.

2020

[Grafu/Picha katika ukurasa wa 118]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Jumla ya Wahubiri

Jumla ya Mapainia

3,500

2,500

1,500

500

1955 1965 1975 1985 1995 2005

[Ramani katika ukurasa wa 81]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

PAPUA NEW GUINEA

PORT MORESBY

Wewak

Mto Sepik

Kambot

Dimiri

Biwat

Mto Yuat

Wabag

Mlima Hagen

Banz

Bonde la Wahgi

NYANDA ZA JUU ZA NEW GUINEA

Ziwa Murray

Mto Fly

Basken

Talidig

Bagildig

Madang

Goroka

Kainantu

Lae

Bulolo

Wau

Kerema

Savaiviri

Ghuba ya Papua

Popondetta

Njia ya Kokoda

Hula

Agi

Govigovi

Alotau

BAHARI YA MATUMBAWE

Kisiwa cha Manus

Visiwa vya Bismarck

BAHARI YA BISMARCK

Kisiwa cha Bagabag

New Britain

Rabaul

Kokopo

Kisiwa cha Kurmalak

New Ireland

Kavieng

BAHARI YA SOLOMON

Kisiwa cha Goodenough

Kisiwa cha Buka

Kisiwa cha Bougainville

Kisiwa cha Nukumanu

Ikweta

Haima

Six Mile

Hanuabada

Bandari ya Port Moresby

Soko la Koki

Uwanda wa Sogeri

Ioadabu

[Picha katika ukurasa wa 74]

[Picha katika ukurasa wa 77]

“Lightbearer”

[Picha katika ukurasa wa 78]

Wahubiri wa kwanza wenyeji, kuanzia kushoto kuelekea kulia: Bobogi Naiori, Heni Heni Nioki, Raho Rakatani, na Oda Sioni

[Picha katika ukurasa wa 79]

Kijiji cha Hanuabada na sehemu fulani ya Port Moresby inaonekana upande wa nyuma

[Picha katika ukurasa wa 82]

Shirley na Don Fielder kabla tu ya kuwasili Papua New Guinea

[Picha katika ukurasa wa 85]

Jumba la Ufalme la kwanza nchini huko Haima, Port Moresby

[Picha katika ukurasa wa 87]

John Cutforth

[Picha katika ukurasa wa 89]

Hotuba ya picha

[Picha katika ukurasa wa 90]

Kulia: John Cutforth akifundisha kwa kutumia picha; chini: ndugu akibeba ubao wenye picha ili akahubiri katika vijiji vya mbali

[Picha katika ukurasa wa 92]

Alf Green, David Walker, na Jim Smith

[Picha katika ukurasa wa 93]

Kushoto: Shirley, Debbie, na Don Fielder; kulia: Don akiwa katika mtumbwi wake

[Picha katika ukurasa wa 96]

Jim Smith na Glenn Finlay

[Picha katika ukurasa wa 97]

Stephen Blundy akivuka Ghuba ya Kerema

[Picha katika ukurasa wa 99]

Rosina na Ken Frame

[Picha katika ukurasa wa 102]

Matthew na Doris Pope

[Picha katika ukurasa wa 103]

Nyumba ya Magdalen na John Endor ndipo mahali pa kwanza ambapo mikutano ilifanyiwa huko Lae

[Picha katika ukurasa wa 109]

Nyanda za juu

[Picha katika ukurasa wa 110]

Tom na Rowena Kitto wakiwa mbele ya duka lao dogo na nyumba yao huko Wabag

[Picha katika ukurasa wa 113]

Erna na Berndt Andersson

[Picha katika ukurasa wa 114]

Kerry Kay-Smith na Jim Wright

[Picha katika ukurasa wa 115]

Mike Fisher akiwa kwenye Mto Sepik

[Picha katika ukurasa wa 123]

Jumba la Ufalme huko Agi liliteketezwa lakini likajengwa upya na kupanuliwa

[Picha katika ukurasa wa 127]

Elsie na Bill Thew

[Picha katika ukurasa wa 128]

“Puapua” ikiwa majini

[Picha katika ukurasa wa 128]

Mashua inayoitwa “Pioneer” iliyotengenezwa na Berndt Andersson

[Picha katika ukurasa wa 131]

Kusafiri kwenye Mto Sepik

[Picha katika ukurasa wa 132, 133]

Kushoto: Mwangalizi wa mzunguko Warren Reynolds na mke wake, Leann, wakitembelea kijiji cha Biwat; juu: akitoa hotuba ya watu wote alipotembelea kijiji cha Dimiri

[Picha katika ukurasa wa 135]

Kora Leke

[Picha katika ukurasa wa 135]

Soare Maiga

[Picha katika ukurasa wa 136]

Save Nanpen

[Picha katika ukurasa wa 139]

Geordie na Joanne Ryle

[Picha katika ukurasa wa 145]

Baadhi ya watoto waliofukuzwa shuleni kwa kukataa kusalimu bendera

[Picha katika ukurasa wa 152, 153]

Kushoto: Eneo la Rabaul, volkano Tavurvur ikiwa mbali; chini: Jumba la Ufalme la Rabaul lililoharibiwa mwaka wa 1994

[Picha katika ukurasa wa 155]

Kikundi cha watafsiri, 2010

[Picha katika ukurasa wa 161]

Ofisi ya Tawi ya Papua New Guinea

Halmashauri ya Tawi: Dan Burks, Timo Rajalehto, Kegawale Biyama, Craig Speegle

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki