Zamani, kusafiri kwa kutumia barabara kulichukua muda mrefu, kulichosha, na kugharimu pesa nyingi kuliko kusafiri kwa mashua. Hata hivyo, ili kufika sehemu nyingi, njia pekee ilikuwa kutembea kwa miguu.
Msafiri angeweza kutembea kilomita 30 hivi kwa siku. Angekumbana na hali ngumu kama vile jua kali, mvua, baridi, au kushambuliwa na wezi. Mtume Paulo alisema kwamba aliposafiri, ‘mara nyingi alikabili hatari za kutokana na mito, hatari za kutokana na wezi.’—2 Kor. 11:26.
Milki ya Roma ilikuwa na barabara nyingi nzuri za mawe. Kando ya barabara kuu, kulikuwa na nyumba za wageni kila baada ya umbali wa safari ya siku moja hivi kwa miguu. Karibu nusu ya safari, kulikuwa na hoteli ambazo mtu angeweza kupata chakula au mahitaji mengine ya msingi. Waandishi wa enzi hizo walitaja kwamba hoteli na nyumba hizo za wageni zilikuwa chafu, zilijaa watu, viroboto na zilikuwa na joto sana. Hazikuheshimika na zilipendwa na watu wanaotenda mambo mabaya. Mara nyingi, wahudumu wa sehemu hizo waliwaibia wasafiri na walitoa huduma za ukahaba.
Bila shaka Wakristo waliepuka sehemu hizo kadiri walivyoweza. Hata hivyo, waliposafiri kwenda sehemu ambazo hawakuwa na watu wa ukoo au marafiki, walilazimika kukaa humo.