Hata baada ya baraza linaloongoza la karne ya kwanza kutatua suala la tohara, watu fulani waliodai kuwa Wakristo walikaidi uamuzi uliotolewa. Mtume Paulo aliwaita Wayudaiza, ‘ndugu wa uwongo’ waliotaka “kupotosha habari njema kuhusu Kristo.”—Gal. 1:7; 2:4; Tito 1:10.
Inaonekana lengo la ndugu hao wa uwongo lilikuwa kuwatuliza Wayahudi ili wasipinge vikali Ukristo. (Gal. 6:12, 13) Ndugu hao wa uwongo walidai kwamba ili mtu aonwe kuwa mwadilifu lazima ashike Sheria ya Musa kuhusu mambo kama vile chakula, tohara, na sherehe za Kiyahudi.—Kol. 2:16.
Haishangazi kwamba watu walioshikilia maoni hayo hawakuwa huru kushirikiana na waabudu wenzao kutoka kwa Watu wa Mataifa. Inasikitisha kwamba hata watu wenye kuheshimika katika kutaniko la Kikristo, ambao walikuwa na asili ya Kiyahudi, walionyesha mtazamo huo usiofaa. Kwa mfano, ndugu kutoka kutaniko la Yerusalemu walipoenda Antiokia, walijitenga na ndugu zao wa Mataifa. Hata Petro ambaye alikuwa akishirikiana kwa uhuru na Watu wa Mataifa kabla ya wakati huo, alijitenga—hata hakutaka kula pamoja nao. Alitenda kinyume kabisa na kanuni ambayo mwanzoni yeye mwenyewe aliitetea. Ndiyo sababu Petro alipata shauri kali kutoka kwa Paulo.—Gal. 2:11-14.