Estonia
KARIBU Estonia! Nchi hii maridadi ya Baltiki ina mandhari zenye kupendeza sana kama vile misitu, maeneo ya malisho, na pwani zenye vijiji vyenye mpangilio mzuri, maziwa zaidi ya 1,400, na visiwa zaidi ya 1,500. Karibu nusu ya nchi ya Estonia imefunikwa kwa vichaka na miti mingi—ambayo ni masalio ya msitu wa kale uliofunika sehemu kubwa ya Ulaya. Nchi ya Estonia, ambayo ni kubwa kidogo kuliko Uswisi na Denmark, ni moja kati ya nchi ndogo zaidi barani Ulaya.
Utaona kwamba wakaaji wa nchi hii ndogo na maridadi, ambao ni wenye urafiki lakini wanyamavu, wana sifa fulani zenye kuvutia. Kwa ujumla, Waestonia wana elimu nzuri na wanapenda kusoma. Ingawa asilimia 30 hivi ya wakaaji wake wanazungumza Kirusi, Kiestonia ndiyo lugha rasmi. Hata hivyo, si rahisi kujifunza Kiestonia kwa sababu ni kigumu sana. Kwa mfano, Kiestonia kina maneno kadhaa yanayotumika kumaanisha “kisiwa,” ikitegemea umbo, ukubwa, na muda ambao kisiwa hicho kimekuwapo.
MSUKOSUKO WA KISIASA
Estonia imetawaliwa na nchi jirani zenye nguvu—moja baada ya nyingine. Mashujaa wa Ujerumani na majeshi ya Denmark yaliivamia nchi hiyo mapema katika karne ya 13, na baadaye Denmark, Lithuania, Norway, Poland, Sweden, na Urusi zilipigana kwa karne nyingi ili ziweze kuidhibiti Estonia.
Sweden nayo iliitawala Estonia kwa zaidi ya karne moja, kabla ya Urusi kuitwaa tena mwaka wa 1721. Baada ya kujitawala kwa kipindi kifupi kati ya mwaka wa 1918 na 1940, Estonia ilivamiwa na kutwaliwa na majeshi ya Muungano wa Sovieti. Katika mwaka wa 1941, Ujerumani ya Nazi iliiteka nchi hiyo lakini Muungano wa Sovieti ukaiteka tena mwaka wa 1944. Estonia ilikuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti kwa miaka 50 hivi, hadi mwaka wa 1991 wakati ilipojitenga na muungano huo na kuwa jamhuri ya kwanza ya Sovieti kujitangaza kuwa huru.
Matukio hayo yaliwaathiri jinsi gani Mashahidi wa Yehova nchini Estonia? Hali ilikuwa namna gani kwa watumishi wa Mungu wa kweli wakati wa utawala wenye kukandamiza wa Ujerumani na kipindi kigumu cha utawala wa Sovieti? Soma simulizi lenye kusisimua kuhusu imani, ujasiri wao, na jinsi walivyotumia busara wakati wa mateso makali.
MADHARA YA DINI ZA UWONGO
Wapiganaji wa kidini waliovamia Estonia katika karne ya 13 waliwalazimisha watu wakubali “Ukristo.” Lakini watu walijifanya tu kuwa wamegeuza imani yao. Baadaye, watu katika vijiji vizima walijitakasa kutokana na ubatizo huo kwa kujirushia maji wao wenyewe na pia nyumba zao, kisha wakarudia ibada yao ya kipagani. Watu hao waliendelea kuabudu vitu vya asili na kufuata desturi za kipagani, na pole kwa pole wakachanganya desturi hizo na mafundisho ya kanisa Katoliki.
Katika karne ya 17, Waestonia waligeuzwa imani na kuwa wafuasi wa Kanisa la Kilutheri, na baadaye Kanisa Othodoksi la Urusi likawa kanisa linaloungwa mkono na serikali. Mwaka wa 1925, kanisa hilo lilitenganishwa na serikali. Kulingana na uchunguzi fulani, asilimia 14 tu ya Waestonia ndio wanaodai kuwa dini ni muhimu katika maisha yao.
Hata hivyo, hivi majuzi, Waestonia wengi wanyofu wamekubali mafuta yenye kuponya ya Neno la Mungu, yaani, “fundisho lenye afya kulingana na habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:10, 11) Kwa sababu hiyo, tangu 1991 hesabu ya Mashahidi wa Yehova wanaotangaza Ufalme wa Mungu imeongezeka kutoka watu wasiozidi 1,000 mpaka watu zaidi ya 4,000. Lakini habari njema ilifika katika nchi ndogo ya Estonia jinsi gani?
“UNA MDOMO”
Walipokuwa Marekani mapema katika karne ya 20, Martin Kose na ndugu yake Hugo walipata vitabu fulani vilivyochapishwa na Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo). Martin alifurahia mambo aliyosoma lakini alihangaika kuhusu nchi ya kwao Estonia kwa sababu alijua hakukuwa na Wanafunzi wa Biblia huko. Alipopata anwani ya makao makuu yaliyo jijini New York katika broshua fulani, Martin alienda huko na kumweleza J. F. Rutherford hangaiko lake. Ndugu Rutherford ndiye aliyesimamia kazi ya Wanafunzi wa Biblia wakati huo.
“Nifanye nini?” Martin akauliza.
“Una mdomo, sivyo?” Ndugu Rutherford akamuuliza. “Basi rudi kwenu na uutumie.”
Martin alifanya hivyo! Mwaka wa 1923 alirudi Estonia na kuanza kuhubiri. Hivyo akawa Mwanafunzi wa Biblia wa kwanza nchini Estonia. Martin aliifundisha familia yake kweli za Biblia na mwana wake, Adolf, akawa mtumishi mwaminifu wa Mungu aliyewaimarisha akina ndugu katika nyakati ngumu walizokabili baadaye. Hugo, ndugu yake Martin, alipata kuwa Mwanafunzi wa Biblia pia, lakini hakurudi kuishi Estonia.
“HUTAKUWA MPWEKE”
Katika kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia jijini London mwaka wa 1926, Ndugu Rutherford aliomba watu wajitolee kwenda kuhubiri katika nchi za Baltiki. Albert West, Percy Dunham, na James Williams, walinyoosha mikono. Muda mfupi baadaye, waliwekwa rasmi kusimamia kazi ya kuhubiri habari njema nchini Estonia, Latvia, na Lithuania. William Dey, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi ya Ofisi ya Ulaya Kaskazini, iliyokuwa Denmark, alisafiri pamoja na Albert West mpaka Tallinn, jiji kuu la Estonia. Baada ya kumtafutia Albert chumba, Ndugu Dey alimpiga-piga begani na kumwambia: “Kwa heri, Albert. Hutakuwa mpweke. Hivi karibuni gazeti la Mnara wa Mlinzi litakuja!”
Makolpota, kama mapainia walivyoitwa wakati huo, walikuja kutoka Uingereza, Ujerumani, na nchi nyingine ili kusaidia. Hata hivyo, hawakuweza kukaa kwa muda mrefu kwa sababu ilikuwa vigumu kuongeza muda wa visa zao. Ilikuwa rahisi kwa makolpota kutoka Finland kukaa Estonia, kwa kuwa Kiestonia na Kifini ni lugha zinazofanana sana. Wahubiri kutoka nchi za kigeni walikuwa wengi na walipanda mbegu za Ufalme kwa bidii na kwa wingi. Wageni hao walikaribishwa kwa shauku na mara nyingi walipewa majina ya utani ikitegemea nchi za kwao. Kwa mfano, jina “Soome Miina” lilimaanisha Miina kutoka Finland, nalo jina “Londonist,” lilimaanisha mtu kutoka London.
OFISI YA TAWI YA KWANZA
Haikuwa rahisi kupata jengo linalofaa kutumiwa kama ofisi, na kwa kuwa wageni walionwa kuwa matajiri, walitozwa kodi ya juu. Hata hivyo, mwaka wa 1926 ofisi ya tawi ilifunguliwa katika jengo dogo jijini Tallinn, kwenye Barabara ya 17 Kreutzwaldi, na Albert West akawa mtumishi wa ofisi ya tawi. Vijitabu vya kwanza vya Kiestonia, kutia ndani kijitabu Millions Now Living Will Never Die!, vilitolewa mwaka huohuo.
Hilda Ang, mwanamke kijana raia wa Estonia, alisikia kuhusu kweli kutoka kwa rafiki zake. Alipoenda kwenye ofisi ya tawi kupata vitabu, ndugu fulani Mjerumani alimwomba amsaidie kutafsiri hotuba ya watu wote. Alikubali, na mwaka wa 1928 akaalikwa kufanya kazi kwenye ofisi hiyo kama mtafsiri. Baadaye aliolewa na ndugu Mwingereza, Alexander Brydson, aliyekuwa amehamia Estonia kuwa mhubiri wa wakati wote. Hilda alikuwa mtafsiri bora na mwenye bidii. Baadaye kazi yetu ilipopigwa marufuku, yeye na mume wake walilazimika kuondoka Estonia. Hata hivyo, Hilda aliendelea kutafsiri kisiri kwa miaka mingi akiwa ng’ambo. Yeye na mume wake walitumika wakiwa watumishi wa wakati wote kwa jumla ya miaka zaidi ya 100!
Mnamo 1928 Wanafunzi wa Biblia walichapisha kitabu chao cha kwanza cha Kiestonia, The Harp of God. Pia, kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, walichapisha Mnara wa Mlinzi, vitabu tofauti-tofauti saba, na vijitabu mbalimbali katika Kiestonia.
WAHUBIRI WA KWANZA
Makolpota walisafiri na kuhubiri maeneo makubwa kwa baiskeli na walilala popote walipopata mahali pa kulala—iwe ni katika nyumba za mashambani au juu ya marundo ya nyasi. Watu walikuwa maskini, lakini walipenda kusikiliza ujumbe wa Ufalme. Kwa sababu hiyo, wahubiri hao wa wakati wote walihubiri kwa furaha kati ya saa 150 mpaka 200 kwa mwezi. Mmoja wao alihubiri muda wa saa 239 mwezi fulani! Walikuwa watumishi wenye bidii, wajasiri, na wavumilivu. Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa dada mmoja alipoenda kuhubiri kwa mara ya kwanza:
“Je, unajua kuendesha baiskeli?” dada fulani mwenye bidii kutoka Finland akamuuliza.
“Ndiyo, ninajua,” dada huyo mpya akamjibu.
“Basi, twende Sarema,” akasema yule dada kutoka Finland kwa shauku, akirejelea kisiwa kikubwa zaidi cha Estonia, umbali wa kilomita 200 hivi.
Walipofika kwenye kijiji cha kwanza huko Sarema, yule dada kutoka Finland alipendekeza hivi: “Utaanzia hapa nami nitaanzia upande ule mwingine. Jioni, tukutane katikati ya kijiji.” Yule dada mpya hakuwa amewahi kuhubiri. Lakini alipobisha mlango wa kwanza, alihisi kwamba Yehova alikuwa anamsaidia na upesi akapata ujasiri na kuendelea kuhubiri kwa furaha.
Hellin Aaltonen (baadaye aliitwa Grönlund) alikutana na watu wa kisiwa cha Vormsi na kugundua kwamba walizungumza lugha asiyoijua.
“Je, mnazungumza Kiestonia?” akawauliza.
“Hapana, tunazungumza Kiswedi,” wakasema.
“Je, mna vitabu vya kusoma vya Kiswedi?” Hellin akawauliza.
“Hatujawahi kupata vitabu vya Kiswedi kwa mamia ya miaka,” wakajibu kwa kutia chumvi.
Alipotambua kwamba watu wa Vormsi walihitaji vitabu vya Kiswedi, Hellin aliamua kutembelea tena kisiwa hicho akiwa na Fanny Hietala, ambaye alizungumza Kiswedi.
“Tulichukua vitabu vyote vya Kiswedi vilivyokuwa kwenye ofisi na kwenda huko kwa mashua,” asema Hellin. “Kwa siku tatu, tuliwahubiria watu katika kisiwa chote na kuwaachia karibu vitabu vyote tulivyobeba. Miaka mingi baadaye, nilisikia kuhusu ndugu fulani kutoka Sweden aliyejifunza kweli kutoka katika vitabu alivyopata kisiwani Vormsi!” Mara nyingi wahubiri wa Ufalme waliona ukweli wa Mhubiri 11:6: “Asubuhi panda mbegu zako na mpaka jioni usiache mkono wako upumzike; kwa maana hujui ni wapi hii itafanikiwa.”
MATATIZO AMBAYO MAKOLPOTA WALIKABILI
Kazi ya makolpota haikuwa rahisi. Wakati wa baridi kali, waliteleza juu ya theluji au kutembea kwa miguu umbali wa kilomita 20 hadi 40 kwa siku. Kulikuwa na baridi kali na haikuwa rahisi kupata mahali pazuri pa kulala. Wangeweza tu kubeba chakula na vitu vingine vya lazima, kwa kuwa walibeba pia masanduku ya vitabu. Barabara zilikuwa hazipitiki kukiwa na mvua kubwa. Mara nyingi makolpota hao walilazimika kulala nje. Ili kuendelea na utumishi huo mgumu, walihitaji kuwa na nguvu za kutosha. Hata hivyo, wahubiri hao wenye kujitoa walihisi namna gani kuhusu utumishi wao?
“Sikukosa chochote muhimu,” asema Vilho Eloranta, ndugu mwenye bidii kutoka Finland aliyekuwa mhubiri wa wakati wote katika maeneo ya mbali kwa miezi mingi. “Mara nyingi, niliwapa watu vitabu, nao wakanipa chakula na mahali pa kulala. Sikuhitaji sana pesa. Jioni ilipofika, ningeanza kuomba mahali pa kulala. Ni wenye nyumba wachache waliokataa, hasa kama ingekuwa usiku au kama hakungekuwa na nyumba nyingine karibu.”
Vilho anaongeza kusema: “Nilihangaikia sana kuwapelekea watu ujumbe wa Ufalme hivi kwamba hata kukaa katika nyumba za hali ya chini hakukupunguza uradhi na shangwe niliyopata kutokana na kuhubiri.”
Ndugu na dada hao wenye bidii waliweka msingi kwa ajili ya ongezeko lililotokea miaka ya baadaye kwa kuwaachia watu vitabu vingi. Mnamo 1929, jumla ya vitabu na vijitabu 53,704 viligawanywa na wahubiri wachache.
“Estonia ilikuwa na makolpota wapatao 30,” asema Adolf Kose, “na walihubiri nchi nzima kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu.”
Matokeo ya kazi ya wahubiri hao wenye bidii bado yanaonekana. Kwa mfano, mapema miaka ya 1990, Mashahidi wa Yehova walikutana na Ruth, mwanamke mzee. Ujumbe wao haukuwa mpya kwake. Alikumbuka kwamba zaidi ya miaka 60 iliyokuwa imepita, alimsikiliza Mwanafunzi wa Biblia Mjerumani ambaye alimtembelea jirani yake mara kadhaa. Sasa, ingawa alikuwa kiziwi na mzee, Ruth aliitambua kweli, akakubali funzo la Biblia, na kubatizwa—miaka 70 hivi baada ya kuhubiriwa mara ya kwanza!
KAZI KATIKA OFISI YA TAWI MWANZONI
Katika siku hizo za mapema, ofisi ndogo ya tawi ilitumika pia kwa ajili ya makusanyiko. Kusanyiko la kwanza lililofanywa Juni 1928, lilihudhuriwa na watu 25, na 4 wakabatizwa. Mwaka uliofuata, ndugu 80 wa Finland walikuja kusaidia katika kusanyiko na kuhubiri.
Albert West, aliyekuwa mtumishi wa ofisi ya tawi nchini Estonia, alipewa mgawo wa kumsaidia William Dey, na baadaye akachukua mahali pake kama mtumishi wa ofisi ya tawi nchini Denmark. Ni nani angechukua mahali pa Ndugu West nchini Estonia? Wallace Baxter, kutoka Scotland alikuwa ndugu mwenye upendo na mcheshi. Kabla ya kujifunza kweli, alipigana katika jeshi la Uingereza nchini Ufaransa wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Mambo aliyoona na yale yaliyompata vitani yalikuwa kinyume cha mafundisho ya Yesu Kristo.
“Nilichanganyikiwa,” asema Ndugu Baxter, “na kutambua kwamba vita vyote vya binadamu havifai, hata adui awe nani. Niliamini kwamba watu wote ni ndugu na kuwa yeyote anayemtafuta Mungu, mwishowe atampata. Nilipokuwa nikifikiria mambo hayo, nilipiga magoti katika handaki langu na kuweka nadhiri kwa Mungu kwamba nikinusurika na kurudi nyumbani, nitamtumikia maisha yangu yote.”
Baxter alifanya hivyo. Baada ya kujifunza kweli, alianza kwa bidii utumishi wa wakati wote mwaka wa 1926. Miaka miwili baadaye alikubali mwaliko wa kutumika nchini Estonia, na huko akaendelea na bidii ileile. Aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa ofisi mwaka wa 1930, mwaka ambao Ndugu West aliondoka. Ofisi ya tawi ilihamishiwa kwenye Barabara ya 72 Suur Tartu, Tallinn, mwaka wa 1932, na mwaka uliofuata shirika la Watch Tower Bible and Tract Society likaandikishwa kisheria nchini Estonia.
UJUMBE WATANGAZWA KATIKA LUGHA MBALIMBALI
Mapema yapata mwaka wa 1927, Ndugu West alipata kibali cha kutoa hotuba kupitia kituo cha redio cha biashara jijini Tallinn. Hotuba aliyotoa, “Baraka za Milenia,” ilitafsiriwa katika Kiestonia. Hotuba hiyo iliwapendeza watu wengi, na vilevile ikatokeza ubishi. Hivyo, akina ndugu wakanyimwa kibali cha kutoa hotuba kupitia redio hadi mwaka wa 1929. Kisha, hotuba zikaanza kutolewa kwa ukawaida kupitia redio kila Jumapili. Hotuba hizo zilitolewa katika, Kiestonia, Kifini, Kiingereza, Kirusi, na mara kwa mara katika Kiswedi na Kijerumani, na angalau mara moja katika Kidenishi. Pia hotuba hizo ziliwavutia watu wengi na zingeweza kusikilizwa katika nchi za mbali kama Norway, Denmark, Sweden, Finland, na katika jiji la Leningrad (sasa ni St. Petersburg), Urusi. Katika mwaka wa utumishi wa 1932, hotuba 200 zilizotolewa zilichangia sana kutangazwa kwa jina la Yehova. Haishangazi kuwa zilichochea upinzani wa makasisi pia!
Makasisi hao walijua kuwa wenye mamlaka nchini Estonia waliogopa sana chochote kilichohusiana na Ukomunisti, hivyo wakawasingizia Mashahidi kuwa wanashirikiana na Wakomunisti. Wenye mamlaka walikuwa tayari kuchukua hatua haraka kukabiliana na lolote ambalo walihisi lingedhoofisha taifa lao, kwa hiyo, mwaka wa 1934, wakapiga marufuku hotuba hizo. Hata hivyo, si kila mtu aliyekubaliana na hatua hiyo. Mvulana fulani wa shule aliandika barua ifuatayo kwa Kiingereza:
Kwa Watch Tower na Hakimu Rutherford:
Ninasikitika kuwa serikali yetu ya Estonia imepiga marufuku hotuba zilizokuwa zikitolewa kupitia redio. Mimi ni mvulana, mwanafunzi wa shule. Wazazi wangu ni maskini: wanafanya kazi ngumu kuandaa mahitaji ya watoto wao. Lakini upendo wao kwa Bwana na tumaini analowapa huchangamsha nyuso zao. Nilikuwa mgonjwa sana wakati wa majira ya baridi kali, na hotuba hizo ndizo tu zilizonifariji. Machozi yangu yalikuwa machozi ya furaha. . . . Sasa nitapataje hotuba hizo? . . . Nilianza kujifunza Kiingereza, na hii ndiyo barua yangu ya kwanza katika lugha hiyo, ambayo nimeandika bila kutumia kamusi. . . . Ninakusalimu na kukutakia mema Hakimu Rutherford.
Ndugu Rutherford alimjibu mvulana huyo kwa kumwandikia barua ya kibinafsi na kumtumia baadhi ya hotuba zake zilizorekodiwa.
“GARI LA VITA LA UFALME WA MBINGUNI”
John North, kolpota mwenye bidii kutoka Uingereza, aliishi pamoja na familia yake katika nyumba iliyokokotwa na gari, alipokuwa akihubiri nchini Estonia. Jambo hilo liliwavutia watu wengi katika eneo lote la Estonia kusini. Gazeti fulani la habari lilisema hivi kuhusu nyumba hiyo: “Jijini Tartu Shirika [la Watch Tower] limetengeneza gari linalofanana na nyumba ili kulitumia kuzunguka nchi nzima na kufanya ibada. Wanawahubiria watu kutoka katika ‘gari la vita la Ufalme wa mbinguni’ na kugawa vitabu vinavyozungumzia Biblia. ‘Gari’ hilo lina wafanyakazi watano—mmishonari mkuu, mke wake, mtoto wao, na wanaume wawili wenye nguvu. Wanaume hao wawili wanaendesha baiskeli kwa haraka (kama Yehu), na wanaenda kila upande kuzunguka ‘gari’ hilo wakigawa vitabu.”
Wakati wa misukosuko ya kisiasa katikati ya miaka ya 1930, Nikolai Tuiman, aliyekuwa rubani wa jeshi, alitiwa gerezani kwa sababu ya kujihusisha na kikundi cha Kifashisti cha Estonia. Katika maktaba ya gereza, Nikolai alipata vitabu fulani vilivyoandikwa na J. F. Rutherford, ambavyo vilimsaidia kutambua kwamba hakupaswa kikitumaini kikundi hicho. Baada ya kuachiliwa, alisafiri hadi Tallinn, kwenye jengo ambalo anwani yake ilikuwa kwenye kitabu fulani cha mke wake kilichochapishwa na Mashahidi. Kwa msaada wa Ndugu Baxter, Nikolai alibadili maisha yake kabisa, akaacha shughuli za kisiasa, na kuwa Shahidi wa Yehova mwenye amani na bidii. Baadaye, kazi yetu ilipopigwa marufuku, Nikolai alilitegemeza sana kutaniko, akisaidia katika uchapaji uliokuwa ukifanywa kisiri. Alidumisha uaminifu wake katika miaka 15 hivi aliyokuwa uhamishoni Siberia.
Mtu mwingine ambaye pia alikuwa amejiingiza katika siasa na kukatishwa tamaa ni daktari aliyeitwa Artur Indus. Alisikia kuhusu kweli mara ya kwanza kabisa alipomtembelea Martin Kose nyumbani ili kumtibu. Ndugu Kose alimtia moyo Artur ajifunze Biblia, na kwa kuwa Artur alijua Kijerumani, Ndugu Kose alimwagizia vitabu vyote ambavyo vingeweza kupatikana katika lugha hiyo. Daktari huyo alisaidiwa na Martin kujifunza kweli, akajiweka wakfu kwa Yehova, na kubatizwa. Artur alikuwa daktari maarufu aliyeheshimiwa na pia akawa ndugu mwenye bidii na mwenye kuheshimiwa.
DALILI ZA MATESO
Miaka ya katikati ya 1930 ilikuwa na misukosuko mingi. Kwa sababu ya shinikizo kutoka Ujerumani ya Nazi na Kanisa Katoliki, kijitabu Righteous Ruler kilitwaliwa Januari 1935.
Mwaka huohuo, Waziri wa Mambo ya Ndani alifunga Shirika la Watch Tower nchini Estonia, akatwaa vitabu, na kuweka mali ya shirika hilo chini ya umiliki wa serikali. Ingawa vitabu vingi vilikuwa vimefichwa, karibu vitabu 76,000 vilitwaliwa. Kitendo hiki hakikukwamisha kazi yetu. Ndugu walifurahi na kushangaa wakati broshua mbili zilizokuwa zimetwaliwa zilipochapishwa kwenye magazeti mawili maarufu yenye jumla ya nakala 100,000. Ingawa tulipoteza vitabu, jina la Yehova lilitangazwa kwa kiwango kikubwa zaidi ya vile ambavyo lingetangazwa kama akina ndugu ndio wangegawa broshua hizo.
Wakati huohuo, kazi ya kuhubiri iliendelea, na kazi katika ofisi ikaanza tena. Vitabu kadhaa viliendelea kutwaliwa katika miaka iliyofuata. Hellin Aaltonen alikuwa akifanya kazi katika ofisi ya tawi wakati uvamizi fulani ulipofanywa.
“Polisi watatu vijana walikuja hasa kutwaa kijitabu Millions Now Living Will Never Die!” asema Dada Aaltonen, “lakini hatukuwa na nakala zozote. Walitoa vitabu vyote kwenye rafu na kuvitupa sakafuni. Ndugu Baxter hangeweza kufanya lolote, kwa kuwa walikuwa wanamwangalia kwa makini. Nilianza kupanga vile vitabu na bila kuonekana nikaenda kwenye dawati la Ndugu Baxter kuangalia kama kuna karatasi zozote ambazo polisi hao hawakupaswa kuziona. Niliona barua iliyokuwa na majina na anwani za wahubiri wote, nami nikaitupa kwenye kapu la takataka lililokuwa pembeni. Polisi hao walipoanza kupakia vitabu katika masanduku, msimamizi wao alichukua sanduku moja kwa kiburi na kulirusha kwa nguvu sana hivi kwamba mkono wake ulivunjika! Hivyo, polisi hao wakaondoka upesi kumpeleka hospitalini, nasi tukapata nafasi ya kupekua masanduku yote kabla hawajarudi.”
Ndugu Baxter anaongeza, “Polisi hao walirudi na walipokuwa wakipakia vitabu hivyo, nikamwona mmoja wao akiweka kitabu Deliverance kwenye mfuko wa koti lake. Mara kwa mara mimi nimejiuliza ni vitabu vingine vingapi ambavyo maofisa hao walichukua na kusoma?”
Hali ilikuwa yenye kuogopesha na isiyotabirika mwaka wa 1939. Idadi fulani ya majeshi ya Sovieti yaliruhusiwa kuingia Estonia. “Kila siku redio ilitangaza kwa mfululizo propaganda ya Wakomunisti,” akaandika Ndugu Baxter. “Watu walikuwa wenye udadisi mwingi, msisimuko, wasiwasi, na hata woga. Ndege za kivita za Sovieti zilizojaa askari wa miavuli, zilitoa ngurumo kali angani.” Je, hali hiyo ingesambaratisha kazi ya kuhubiri?
Licha ya msukosuko huo wote, katika mwaka wa 1940, watumishi waaminifu wa Yehova waliachia watu vitabu na vijitabu 59,776. Kazi hii kubwa ajabu ilifanywa na wahubiri 27 na mapainia 15 tu! Walifanya yote wawezayo wakati huo ambapo hawakuwa na vizuizi.
KUSANYIKO LA MWISHO BILA VIZUIZI
Ndugu walipanga kusanyiko jijini Tallinn, muda mfupi kabla ya utawala wa Sovieti kuanza, na kwa miaka 50 iliyofuata hawakuweza kukusanyika tena kwa uhuru. Walizungumzia makala katika Mnara wa Mlinzi kama vile “Theokrasi,” “Msimamo wa Kutounga Mkono Upande Wowote,” “Mitego,” na “Mwisho wa Dini.” Hicho kilikuwa chakula cha kiroho cha wakati unaofaa kilichowatayarisha watu wa Mungu kwa ajili ya mambo ambayo yangetokea baadaye.
Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa karibu kuikumba Estonia, na vingewaathiri ndugu zetu. Mnamo Juni 16, 1940, Muungano wa Jamhuri za Kisoshalisti za Sovieti uliagiza serikali ya Estonia iunde serikali mpya na kuwaruhusu wanajeshi zaidi wa Sovieti waingie Estonia. Chama cha Kikomunisti cha Estonia chenye washiriki wasiozidi 150 kilisajiliwa, na nchi ya Estonia ikatekwa na kuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti. Katika muda wa miezi kadhaa, maelfu ya Waestonia walipelekwa uhamishoni Siberia, na nyumba na mashamba yao ama yakaachwa, yakateketezwa, au kupewa Warusi waliovamia nchi hiyo. Maelfu ya wengine walijaribu kukimbia Estonia kwa mashua ndogo za uvuvi, wengi wao wakielekea Sweden. Wengi walifaulu, lakini wengine wakafa katika bahari iliyochafuka.
NDUGU WA MWISHO KUTOKA NCHI ZA NJE WAONDOKA
Estonia ilipoanza kutawaliwa na Wakomunisti, ofisi ya tawi ilifungwa tena. Na ingawa Ndugu Baxter na pia Alexander na Hilda Brydson walitaka kuendelea na mgawo wao, hali ilizidi kuwa hatari kwa ndugu wa nchi za nje kuendelea kukaa Estonia. Hivyo, Ndugu Rutherford akawashauri waondoke. Ndugu Baxter na Dunham na mke wake waliotoka Latvia walisafirishwa kwa gari-moshi kupitia Siberia na mwishowe wakafika Australia. Brydson na mke wake waliondoka mwaka mmoja baadaye, na kwenda Sweden. Ndugu Baxter aliyekuwa na tumaini la kwenda mbinguni, alitumika katika Halmashauri ya Tawi ya ofisi ya Australia hadi alipokufa Juni 21, 1994.a
Hali ingekuwa namna gani kwa ndugu wenyeji wachache baada ya ndugu wa nchi za nje kuondoka? Walikuwa wapya katika kweli, na walijikuta katikati ya vita vikali. Vita hivyo viliwavunja moyo na bidii yao ikapungua. Baada ya ripoti yao ya mwisho, mwaka wa 1941, hakukuwa na habari zozote kuwahusu kwa muda wa miaka 20 hivi.
MAJARIBU MAKALI YA IMANI
Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipopamba moto, majeshi ya Ujerumani yaliwafukuza Wasovieti na kuitwaa Estonia kuanzia 1941 mpaka 1944. Hata hivyo, hali ya ndugu zetu haikuwa bora. Jaan Pärrat, ndugu kiziwi alikuwa akihubiri jijini Tartu mwaka wa 1942, Wajerumani walipomkamata. Alishtakiwa kwa uchochezi na kufungwa gerezani. Kulingana na hati za gereza, msimamizi wa gereza lake aliagizwa “amrejeshe [Jaan Pärrat] ili aondolewe kwa njia fulani maalumu.” Hilo lilikuwa agizo la kumuua. Watu kadhaa walimwona akitolewa nje na kisha wakasikia milio ya risasi. Hakurudishwa wala kuonekana tena.
Ndiyo, huo ulikuwa wakati mgumu kwa akina ndugu. Kwanza jeshi la Sovieti kisha jeshi la Ujerumani lilitaka wanaume vijana wajiandikishe jeshini. “Ilitubidi tujifiche ili kuepuka kuandikishwa,” asema Adolf Kose. “Kama tungekamatwa, ingetubidi tuamue ama kutii amri ya kujiandikisha jeshini au kupigwa risasi. Kazi ya Ufalme iliathiriwa kwa sababu ilikuwa vigumu kufanya lolote.”
Mkondo wa vita ulibadilika tena. Jeshi la Sovieti liliwafukuza Wajerumani nchini Estonia mwishoni mwa mwaka wa 1944, na Estonia ikajipata tena chini ya utawala mkatili wa Sovieti. Vita na miaka ya ukandamizaji iliyofuata iliwaathiri sana Waestonia. Karibu robo yao waliuawa au wakapelekwa uhamishoni katika maeneo ya mbali ya Muungano wa Sovieti, au wakaikimbia nchi yao. Katika miaka iliyofuata, mamia ya maelfu ya Warusi walihamia Estonia, na kukawa na mchanganyiko mkubwa wa watu. Utawala wa Sovieti uliwaletea ndugu zetu majaribu makali, kama tutakavyoona.
NDUGU WA MSITUNI AWA SHAHIDI
Wakati huo, wafuasi wa kikundi cha wazalendo waliopinga utawala wa Sovieti waliitwa “Ndugu wa Msituni” (“Forest Brothers”) kwa sababu walijificha msituni. Kati yao kulikuwa na watu wengi wasio wafuasi wa kikundi hicho ambao pia walilazimika kujificha msituni kwa sababu Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti (KGB), lilitaka kuwakamata. Inakadiriwa kuwa nyakati nyingine, wanaume kati ya 15,000 na 20,000 walijificha msituni, baadhi yao wakitoweka kwa miaka mingi bila kukamatwa. Hata mtu wa mwisho kati yao hakupatikana hadi mwaka wa 1978! Je, yeyote kati ya Ndugu wa Msituni angekubali kweli na kuamua kuwa ndugu wa kiroho?
Erik Heinloo alijua yumo hatarini kwa kuwa alikuwa mtumishi wa Serikali ya Estonia. Muungano wa Sovieti ulipoiteka Estonia, Erik na mke wake Magda walijaribu mara nyingi kukimbilia Sweden kwa mashua. Mara ya mwisho, injini ya mashua iliharibika, na wakalazimika kurudi. Kwa miaka saba, Erik aliwaepa wenye mamlaka kwa kujificha msituni, lakini hatimaye alikamatwa. Kisha yeye na mke wake wakapelekwa kwenye kambi tofauti za wafungwa katika Muungano wa Sovieti.
Alipokuwa gerezani, Magda alikutana na Mashahidi wawili waliomweleza kuhusu tumaini la Ufalme. Magda alitambua mara moja kwamba alikuwa amepata kweli, hivyo akaanza kucheza dansi kwa furaha! Aliachiliwa mwaka wa 1956 na kubatizwa mwaka wa 1960. Miaka saba baada ya kuachiliwa, Erik naye alikubali kweli. Hatimaye, Ndugu wa Msituni akawa ndugu wa kiroho.
WASAKWA NA KUKAMATWA
Baada ya ndugu wa nchi za nje kulazimika kuondoka Estonia, ndugu jasiri na mwenye bidii, Martin Kose, alipewa mgawo wa kusimamia kazi kaskazini mwa Estonia. Eneo la kusini mwa Estonia lilisimamiwa na Friedrich Altpere, Mwestonia mrefu na mwenye adabu nzuri, aliyekuwa mwalimu wa Kiingereza katika shule ya sekondari. Katika miaka ya 1930, aliombwa atafsiri hotuba ya mmoja wa mapainia wa kigeni aliyekuwa amezuru Võru. Baada ya kufanya hivyo, alitambua kwamba amepata kweli. Alipopewa mgawo wa kusimamia eneo hilo la Estonia kusini, Friedrich alikuwa amefanya maendeleo na angeweza kuongoza kazi ya kuhubiri.
Migawo hiyo ilikuwa migumu kwa ndugu hao wawili kwa sababu hawakuwa na uzoefu mkubwa na hawakuweza kuwasiliana na tengenezo. Ingawa walikabili changamoto za kufanya kazi kisiri, ndugu hao walitumika kwa uaminifu kuanzia mwaka wa 1940 mpaka walipokamatwa mwishoni mwa mwaka wa 1948.
Halmashauri ya Utumishi iliundwa kuchukua mahali pa Martin Kose na Friedrich Altpere, nayo ilitia ndani Albert Kruus, Karl Talberg, na Artur Indus, huku Lembit Toom akiwekwa kuwa msaidizi. Iliwabidi ndugu katika halmashauri hiyo wafanye kazi kisiri. Ndugu Toom peke yake ndiye aliyeweza kusafiri kwa uhuru na kuvitembelea vikundi. Kwa nini? Alifanya kazi kwenye kinu cha upepo, na wakati hakukuwa na upepo wa kuendesha kinu hicho, alikuwa huru kufanya alichotaka.
Ndugu wenye majukumu nchini Estonia walihatarisha maisha yao ili kuwasaidia waabudu wenzao. Picha za wale waliofikiriwa kuwa viongozi zilibandikwa kwenye vituo vya gari-moshi, na walitendewa kama wahalifu. Maofisa wa KGB waliwaagiza maofisa wa usalama wanne hivi wapeleleze kila mmoja wa ndugu zetu wapole na wanyenyekevu. Ingawa hali ilikuwa ngumu kati ya miaka ya 1948 na 1951, Yehova alibariki jitihada za watumishi wake waliojitolea katika kazi ya kuhubiri. Kwa hiyo, idadi ya wahubiri iliongezeka na kuzidi 100.
‘WENYE KUJIHADHARI KAMA NYOKA, WASIO NA HATIA KAMA NJIWA’
Mambo yaliyowapata wanafunzi wa Yesu nchini Estonia yaliendelea kuthibitisha kuwa onyo hili la Bwana wao ni la kweli: “Jionyesheni wenyewe kuwa wenye kujihadhari kama nyoka na hata hivyo wasio na hatia kama njiwa. Jihadharini na watu; kwa maana watawapeleka mahakamani, nao watawapiga ninyi mijeledi katika masinagogi yao. Naam, mtakokotwa na kupelekwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, ili kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.” (Mt. 10:16-18) Lakini, baadhi ya ndugu wenye imani hawakuelewa kikamili kuwa si nyakati zote Yehova anatoa ulinzi dhidi ya ukandamizaji wa Shetani. (Ayu. 1:9-12; 2:3-6) Mashahidi fulani hawakuwa “wenye kujihadhari kama nyoka”—kama walivyopaswa kufanya—hivyo walikamatwa kwa urahisi na watesaji wakatili.
“Kuna mwanamume fulani aliyeonekana mwenye bidii na jasiri,” anakumbuka Adolf Kose. “Alipewa majukumu fulani kutanikoni na alipendwa sana na akina dada. Hata hivyo, akina ndugu walianza kumshuku na wakawaonya akina dada wasimpeleke katika maeneo yote ambapo mikutano ilifanyiwa.” Inasikitisha kuwa baadhi yao walipuuza onyo hilo, na mtu huyo aliweza kutoa habari nyingi sana kwa KGB.
“Katika mwaka wa 1950,” aeleza Lembit Toom, “tulipokea nakala fulani za Mnara wa Mlinzi kutoka Ujerumani, ambazo tulitaka kuwagawia ndugu zetu wote Wakristo nchini Estonia.”
Kusanyiko lilipangwa kufanywa kwenye ghala la kuhifadhia nyasi katika eneo fulani la siri. Maofisa wa KGB walipata kujua mipango yetu nao wakajitayarisha kuwakamata ndugu na dada wote. Waliwavizia na kuweka malori mawili yaliyojaa askari kwenye kituo cha gari-moshi ambapo ndugu hao wangeshukia. Mashahidi watatu walikuwa wamepanga kukutana na ndugu hao kwenye nguzo fulani ya maili katika barabara iliyoelekea mahali pa kusanyiko ili kuwaelekeza. Walipokuwa wakingoja, ndugu mmoja alisikia sauti fulani msituni na akaenda kuchunguza. Ghafula, akaona mtutu wa bunduki! Askari hao walimrudisha mahali ambapo wale ndugu wengine wawili walikuwa, na Mashahidi wote watatu wakakamatwa.
Wakati Lembit Toom na Ella Kikas (baadaye aliitwa Toom) walipotambua kwamba ndugu hao watatu wamekamatwa, walichukua hatua mara moja. Walipanda pikipiki ya Lembit na kuiendesha kwa kasi iwezekanavyo ili wafike kwenye kituo fulani kabla ya kile ambacho akina ndugu waliokuwa wakisafiri kwa gari-moshi walipaswa kushukia. Lembit na Ella walienda haraka kwenye kituo hicho, wakapanda kwenye gari-moshi, na kuwaambia ndugu hao washuke! Baadaye, gari-moshi hilo lilipofika kwenye kile kituo ambapo maofisa wa KGB walikuwa wakingoja, maofisa hao walivunjika moyo kukuta kwamba hakukuwa na Shahidi yeyote kwenye gari-moshi.
Wakati huohuo, ndugu wengine walitafuta eneo lingine ambapo kusanyiko lingefanywa. Kisha wakawaongoza wajumbe hao kwenye barabara isiyo na watu wengi. Walitembea umbali wa kilomita 10 kufika kwenye eneo hilo. Muda huo wote, askari walikuwa wakiendesha gari huku na huku kwenye barabara kuu wakiwatafuta wajumbe hao ambao walitoweka kiajabu. Kusanyiko hilo lilifanywa kwa amani na lilihudhuriwa na watu 111. Hali haikuwa changamfu kwa sababu wote walijua kuwa wangeweza kukamatwa wakati wowote. Programu ilitia ndani ripoti kuhusu ndugu na dada wa nchi nyingine, pamoja na mambo yaliyoonwa yenye kuimarisha imani kuhusu Mashahidi wa Yehova katika kambi za mateso za Nazi. Ingawa Mashahidi hao waliepuka kukamatwa wakati huo, bado wangekamatwa baadaye, kwa hiyo kusanyiko hilo liliandaa mwongozo muhimu na nguvu walizohitaji kukabili majaribu ya baadaye.
WAHOJIWA NA KUHUKUMIWA
Katika miezi michache iliyofuata, ndugu wote wenye majukumu walikamatwa mmoja baada ya mwingine. Wahubiri zaidi ya 70 walikamatwa pia, kutia ndani watu wengine waliokuwa na uhusiano wa aina fulani na Mashahidi wa Yehova. Watumishi wa Yehova wanaopenda amani walikabili mahojiano ambayo hayakuonekana kuwa na mwisho, huku wale waliokuwa huru wakijua kuwa wangeweza kukamatwa na kuhojiwa.
Kwa kawaida ndugu hao walihojiwa usiku na kwa miezi mingi, kwa hiyo, kwa muda mrefu hawakuweza kulala vizuri. Kwa sababu ya kukosa usingizi, walipata mfadhaiko wa akili uliowaathiri sana. Walihukumiwa bila kusikizwa mahakamani; waliambiwa tu hukumu yao—miaka 5 hadi 12 gerezani au kupelekwa kwenye kambi za kazi ngumu. Wengi wao walihukumiwa miaka kumi gerezani. Kosa lao? “Kueneza propaganda ya kupinga Serikali na uchochezi,” kulingana rekodi za serikali. Baadaye kidogo, sheria ilibadilika na Mashahidi wakaanza kuhukumiwa miaka 25 gerezani. Baada ya kuhukumiwa, August Pressraud mwenye miaka 63 alisema hivi kwa utani: “Ninaishukuru Mahakama tukufu kwa kunihukumu kifungo kirefu hivyo. Nilifikiri ningeishi kwa miaka 12 hivi. Lakini nimepewa robo ya karne!”
Baada ya kuhukumiwa, Mashahidi walipelekwa kwenye magereza au kambi za kazi ngumu zenye sifa mbaya kotekote katika Muungano wa Sovieti. Walipelekwa hasa Siberia na Mashariki ya Mbali au Kaskazini ya Mbali ya Urusi, ambako hali zilikuwa mbaya. Hawakuwa na tumaini la kurudi, na wafungwa wengi waliona ni afadhali kufa.
Hata ndugu wa uwongo walioshirikiana na wenye mamlaka waliteswa pia. Kwa mfano, ndugu wawili waliowafanyia maofisa wa KGB upelelezi walianza kuteswa baada tu ya kumaliza kazi yao. Wote wawili walipelekwa kwenye kambi za wafungwa. Yaonekana maofisa wa KGB hawakuwaheshimu hata kidogo ndugu hao waoga waliowapasha habari.b
MASHAHIDI WAPELEKWA SIBERIA
Kwa kuwa maofisa wa KGB walikuwa wamewakamata wale waliofikiriwa kuwa Mashahidi mashuhuri, waliazimia kumwondoa kila Shahidi wa Yehova aliyebaki. Walichukua hatua hiyo asubuhi na mapema, Aprili 1, 1951. Mambo yalipangwa vizuri sana hivi kwamba maeneo yote ya nchi (kutia ndani Latvia, Lithuania, na Ukrainia Magharibi) yalivamiwa wakati uleule.
Karibu Mashahidi wa Yehova wote, wengi wa watu wao wa ukoo, na hata watu wenye kupendezwa walikamatwa kutoka nyumbani kwao, wakakusanywa pamoja kwenye vituo kadhaa vya gari-moshi, na kuingizwa katika mabehewa ya mizigo. Waliruhusiwa kubeba chakula na vitu kadhaa vya kibinafsi, lakini vitu vyote vilivyobaki vilitwaliwa. Siku hiyo—bila kuhukumiwa wala maelezo yoyote—Waestonia 300 hivi walipelekwa Siberia kwa gari-moshi, wengi wao katika eneo la Tomsk, umbali wa kilomita 5,000 hivi.
VIJANA JASIRI
Corinna Ennika, mwenye miaka 17, na dada yake Ene, mwenye miaka 13, walikuwa wameenda kuwatembelea watu wa ukoo. Wazia jinsi walivyohangaika waliporudi nyumbani na kukuta nyumba yao imefungwa na mama yao ametoweka! Hata hivyo, walipojua kuwa mama yao amekamatwa, walitulia kidogo. Kwa nini?
“Angalau alikuwa hai!” Corinna anasema. “Tulipotambua kuwa huenda wengine pia walikuwa wamekamatwa, tuliwaza kwamba angalau Mama alikuwa pamoja na watu wa Yehova. Yehova alitutuliza na kututegemeza sana. Sikulia, wala Ene hakulia hata ingawa ana hisia nyepesi. Jumatatu (Siku ya 1) tulienda shuleni na hatukumtajia yeyote kuhusu kukamatwa kwa mama yetu.”
Corinna na Ene walikuwa watulivu hata wakati maofisa fulani walipokuja kuwachukua. “Katika behewa letu la gari-moshi, kila mtu alikuwa mtulivu,” Corinna anaongeza. “Dada fulani alitufariji, akituambia kuwa Yehova hawezi kuruhusu tuteseke kushinda uwezo wetu na kwamba tunahitaji kuamini ahadi yake kuwa atatusaidia.” Wasichana hao walitenganishwa na mama yao kwa zaidi ya miaka sita.
Hati fulani ya kuhamisha mtoto wa miezi sita ni uthibitisho kwamba watesaji hao waliwachukia Mashahidi bila sababu. Mtoto huyo alihamishwa kwa kuwa “adui wa Serikali.”
Uhamisho huo ulisababisha kihoro kingi, na wale waliohamishwa walifedheheshwa na kuvunjiwa heshima kwa kila njia. Kila asubuhi na jioni, watu wote walipaswa kushuka katika gari-moshi na kwenda kujisaidia, ingawa hakukuwa na vyoo. “Jambo hilo lilikuwa kinyume kabisa cha maadili na ubinadamu,” aeleza dada fulani. “Haingewezekana kuwatenganisha wanaume na wanawake. Watu wangepita karibu nasi, nao walinzi walisimama kila mahali kutuchunga.”
MAISHA HUKO SIBERIA—NA KIFO
Baada ya safari ngumu ya majuma mawili, watu waliohamishwa, pamoja na vitu vyao vichache, walishuka katika mabehewa yao na kukabili theluji. Wasimamizi wa shamba la ushirika lililokuwa karibu walikuja kuchagua wafanyakazi bora kwa ajili ya shamba lao, kama vile wenye mashamba walivyonunua wafanyakazi kwenye soko la watumwa.
Watu wengi walioishi Siberia walikuwa wahamishwa, na waliwahurumia wageni. Hivyo, kwa msaada wa waamini wenzao na wenyeji fulani wenye urafiki, ndugu waliohamishwa walianza maisha upya huko Siberia. Kwa kadiri fulani, baadhi yao waliweza kuishi maisha ya kawaida. Wachache kati yao hata walinufaika kiafya. Kwa mfano, dada wawili Waestonia waliokuwa na ugonjwa wa kifua kikuu walipona walipohamia Siberia, eneo ambalo ni kavu zaidi.
Lakini si kila mtu aliyenufaika. Mtoto mmoja alikufa kwenye gari-moshi, na Shahidi fulani mzee akafa kutokana na hali ngumu au kihoro. Ndugu fulani walilemaa kwa kukosa matibabu yanayofaa au kutokana na kazi ngumu. Wengine waliathiriwa na hali ngumu ya maisha, lishe mbaya, magonjwa, aksidenti, na baridi kali. Zaidi ya hayo, wengi waliumia moyoni kwa kutenganishwa na familia zao kwa miaka mingi na kutopokea kamwe barua kutoka kwa wapendwa wao.
“Kwa kuwa familia yetu ilitia ndani watoto na wanawake wachanga,” aeleza Tiina Kruuse, “tulipelekwa kwenye shamba la ushirika la watu maskini. Hata hawakuwa na chakula cha kutosha kwa ajili yao wenyewe na kwa ajili yetu. Wageni walitafuna maganda ya misonobari na mizizi inayoweza kulika, na mara nyingi walikunywa mchuzi wa upupu.”
Majira ya baridi huko Siberia ni marefu na yana baridi kali sana, ambayo wahamishwa Waestonia hakuwa wamezoea. Mara nyingi hata mambo ya kawaida kabisa, kama kulima viazi, hayakufaulu. Kwa wengi, mwaka wa kwanza uhamishoni ulikuwa mgumu na wenye njaa.
“Kiwango cha joto kilishuka hadi nyuzi 50 Selsiasi chini ya sufuri,” asema Hiisi Lember. “Kwa sababu hiyo, tuliweka kibanda cha kuku wetu chini ya kitanda ili asigande na kufa. Wengine hata walimweka ndama ndani ya nyumba iwapo alizaliwa wakati wa baridi kali.”
TWAHAMIA ENEO JIPYA KWA GHARAMA YA SERIKALI
Miaka kadhaa mapema, William Dey alikuwa amesema kuwa kama Muungano wa Sovieti ungeteka nchi za Baltiki, ndugu wangekuwa na maeneo mengi mapya ya kuhubiri. Maneno hayo yalikuwa ya kweli kabisa! Serikali ya Sovieti iliwasaidia sana Mashahidi wa Yehova kupanua kazi yao ya kuhubiri huko Siberia na maeneo mengine ya mbali kwa kuwapeleka uhamishoni. Ingawa Yehova aliruhusu Mashahidi wake wajaribiwe, watu wengi ambao hata hawakuwa wamesikia jina la Mungu walipata nafasi ya kujifunza kweli.
Kwa mfano, Lembit Trell, alikuwa amekamatwa kwa sababu ya kuipinga serikali. Alisikia kuhusu kweli mwaka wa 1948 kwa njia isiyo ya kawaida—akiwa katika chumba cha gereza jijini Tartu. Ofisa fulani wa jeshi la Urusi, aliyekuwa pia amezuiliwa, alimweleza kuhusu Mashahidi ambao alikutana nao katika chumba kingine gerezani. Ofisa huyo alimweleza kifupi mambo ambayo Mashahidi wanafundisha. Alimweleza kuwa serikali ya Mungu ndiyo suluhisho pekee, na kwamba hivi karibuni Mungu ataanza kuitawala dunia. Mambo hayo yalimpendeza Lembit.
Hatimaye, Lembit alipelekwa kwenye kambi ya wafungwa huko Vorkuta, eneo la mbali la Siberia kaskazini, karibu na Bahari ya Aktiki. Huko kambini aliwasikia Mashahidi wakizungumza kuhusu Biblia. Alipowakaribia, alitambua kwamba walikuwa wakizungumzia mambo yaleyale aliyokuwa ameyasikia kutoka kwa yule ofisa, hivyo akajiunga na mazungumzo yao.
“Kwa nini uko gerezani?” ndugu wakamuuliza Lembit.
“Nilikuwa nikipigania haki,” akajibu.
“Je, ulifaulu?” Shahidi mmoja akamuuliza.
Jibu lilikuwa wazi, lakini Lembit alijibu, “Hapana, sikufaulu.”
“Ona! Ulipigana ukiwa upande usiofaa,” ndugu fulani akamwambia Lembit. “Je, si afadhali upigane ukiwa upande unaofaa?” Kisha wakaanza kumweleza yale ambayo Biblia inasema kuhusu vita vya kiroho. Kadiri alivyowasikiliza, ndivyo Lembit alivyozidi kutambua kwamba alikuwa amepata kweli, na ndivyo alivyozidi kuona uhitaji wa kujiunga na upande wa Yehova wa vita vya kiroho.
Baada ya kuachiliwa, Lembit alirudi Estonia na kuanza kupigana vita vya kiroho. Sasa yeye ni painia wa kawaida. Maimu, mke wa Lembit, alipata kweli kwa njia kama hiyo; alianza kupendezwa na kweli alipozungumza na mfungwa mwenzake asiye Shahidi.
Kazi ya kuhubiri ilikuwa ngumu kwa ndugu ambao hawakujua Kirusi vizuri. Hata hivyo, mara nyingi ilikuwa rahisi kuanzisha mazungumzo kwa kutaja sababu iliyofanya wapelekwe uhamishoni Siberia. Jambo hilo liliwasaidia akina ndugu kuwa stadi katika mahubiri yasiyo rasmi. Isitoshe, walikuwa na wakati mwingi wa kuwahubiria wahamishwa Waestonia katika lugha yao ya mama. Dada mmoja aliyekuwa uhamishoni anakadiria kuwa Waestonia kati ya 15 na 20 walijifunza kweli kambini, na pia Warusi na Walithuania kadhaa.
JINSI YA KUPATA CHAKULA CHA KIROHO
Njia nyingi za kisiri zilitumiwa kuwapelekea Biblia na chakula cha kiroho Mashahidi waliokuwa gerezani na wale waliokuwa uhamishoni katika maeneo ya mbali. “Tulipokea kurasa za vitabu kwenye chupa za mafuta ya nguruwe au ya wanyama wengine,” anaeleza ndugu fulani. “Kwa kuwa mafuta hayo yalibadilika rangi na kuwa meupe kwa sababu ya baridi, karatasi haingeweza kuonekana kwa urahisi. Ingawa maofisa waliingiza kisu kwenye chupa hizo, ilikuwa vigumu kupata karatasi hiyo nyembamba, iliyobanwa kwenye upande wa ndani wa chupa.” Haikuwa rahisi kwa maofisa hao kupata chakula hicho cha kiroho kilichofichwa katika chupa za chakula halisi.
Pia vipande vidogo vya vitabu vingeshonwa kwenye kibeti au nguo, kufichwa kwenye katoni ya sabuni, au kushindiliwa ndani ya shimo kwenye sabuni. “Ningeweza kushindilia magazeti manne ya Mnara wa Mlinzi katika sabuni kwenye katoni,” anasema Ella Toom.
Ingawa barua zilikaguliwa, Mashahidi walijifunza jinsi ya kutumia maneno ya kawaida ili kweli za Biblia na maneno ya kitheokrasi yasitambuliwe. Kwa mfano, dada mmoja aliandika: “Tunatunzwa vizuri na Baba, pia, tuna kamba inayofikia maji kwenye kisima.” Alimaanisha kuwa “Baba,” yaani, Yehova, alikuwa akiwaandalia kiroho; kwamba walikuwa wanawasiliana na “kisima,” yaani, tengenezo la Yehova; na kuwa wangeweza kupata maji ya kweli ya uzima, yaani, vitabu vinavyotegemea Biblia.
Ingawa vitabu vingi vilinakiliwa kwa mkono tu, vingine vilichapwa kwa kutumia njia za hali ya chini. Walipokuwa wakinakili vitabu kwa mkono, Mashahidi walifurahi walipotengwa na wafungwa wengine kama adhabu ya kuhubiri. Kwa nini? “Hali ilikuwa nzuri nilipotengwa na wengine,” asema dada fulani. “Niliweza kutafsiri Mnara wa Mlinzi kwa kuwa sikusumbuliwa sana.” Hiyo ni mojawapo ya mbinu nyingi ambazo watesaji walitumia bila mafanikio na mara nyingi zilichangia kuendeleza kazi ya Ufalme!—Isa. 54:17.
UMUHIMU WA MIKUTANO
Nafasi za kuwa pamoja na Mashahidi wengine mikutanoni zilikuwa chache na zilithaminiwa sana. Corinna Ennika anaeleza jinsi yeye na dada mwingine walivyojipa ujasiri na kuondoka kazini kwa siku kadhaa bila ruhusa ili kuhudhuria mkutano. “Tuliondoka kazini jioni,” Corinna anaeleza, “na kutembea hadi kwenye kituo cha gari-moshi, umbali wa kilomita 25. Gari-moshi liliondoka saa nane usiku na tulisafiri kwa saa sita, kisha tukashuka na kutembea kwa miguu kilomita 10 ili kufika kwenye mkutano. Tulipata nyumba ambapo mkutano ulikuwa unafanyiwa, na hata kabla hatujaamua ni nani kati yetu ambaye angesema neno la siri la kujitambulisha, ndugu fulani alitoka nje, akatambua sisi ni akina dada, kisha akasema hivi kwa uchangamfu: ‘Hamjapotea. Karibuni ndani!’ Tulijifunza Mnara wa Mlinzi na kuimba nyimbo za Ufalme. Tulijengwa na kutiwa moyo sana.” Waliporudi kazini siku tatu baadaye, walifurahi kujua kuwa msimamizi wa shamba hakuwa hata amejua kuwa hawakuwako. Kuhudhuria mikutano ya kisiri kuliimarisha sana imani na ujasiri wa watumishi waaminifu wa Yehova.
Katika kisa kingine, ndugu fulani walikuwa wakifanya mkutano ndani ya gereza wakati walinzi walipoingia ghafula kutafuta vitabu. Ndugu mmoja aliyekuwa ameshika kurasa kadhaa mkononi, alichukua ufagio haraka na kuanza kufagia sakafu. Walinzi hao walitafuta lakini hawakupata chochote, hivyo wakaondoka. Wakati huohuo, yule ndugu aliendelea kufagia huku akiwa amezibana zile kurasa kwenye mpini wa ufagio!
NGUVU ZA UPENDO WA KWELI WA KIKRISTO
“Kwa miaka mitano nilifanya kazi katika migodi ya makaa ya mawe,” asema Adolf Kose. “Tulikuwa kaskazini mwa Mzingo wa Aktiki, ambako wakati wa baridi kali, mwangaza wa jua hauonekani. Kulikuwa na giza wakati tulipotoka ndani ya mgodi baada ya kumaliza zamu yetu. Kwa hiyo, hatukuona mwangaza wa jua kwa miezi mingi. Pia, hatukupata chakula cha kutosha. Hali hiyo iliathiri kumbukumbu langu na uwezo wangu wa kukumbuka wakati. Kwa sababu ya kazi ngumu, ukosefu wa chakula, na uchovu mwingi, tulikuwa na nguvu kidogo tu za kuzungumza kwa dakika chache kuhusu mambo ya kawaida. Hata hivyo, tulipozungumzia kweli za Ufalme, hatukuhisi uchovu. Tungeendelea kwa muda mrefu.”
Licha ya matatizo hayo yote, watu wa Yehova walijifunza kupendana bila ubinafsi. Ndugu Kose anaeleza, “Chochote tulichokuwa nacho au chochote ambacho mmoja wetu alipokea tulikigawa kwa usawa kati ya akina ndugu. Kila mmoja wetu alikuwa na uhitaji, kwa hiyo tulijifunza kugawana chochote tulichokuwa nacho.”—1 Yoh. 4:21.
Hata walinzi walipata kujua kuwa Mashahidi walisaidiana sikuzote. Aino Ehtmaa alipohamishwa kutoka kambi moja hadi nyingine, hakuwa na kijiko wala bakuli—vitu vilivyokuwa muhimu sana kambini.
“Usijali, ni sawa tu,” akasema msimamizi wa kambi, “dada zako watakupa unachohitaji.” Na walifanya hivyo. Mara nyingi, upendo kama huo wa Kikristo ulilitukuza jina la Yehova.
Hata hivyo, ushikamanifu wa akina ndugu uliendelea kujaribiwa. Kwa mfano, ingawa Dada Ehtmaa alikuwa amekaa katika kambi ya wafungwa kwa muda fulani, walinzi walimuuliza hivi kila wakati: “Je, bado unakataa kushirikiana nasi?” Bila shaka, walitaka ashirikiane nao kwa kuwapa habari za siri kuhusu Mashahidi wa Yehova.
Dada Ehtmaa alikuwa akiwajibu: “Mmeniweka katika kambi za wafungwa, na baba na mama yangu walikufa kwa sababu yenu, ninawezaje kushirikiana nanyi?”
Hata katika “vifungo vya gereza,” Mashahidi hao waliohamishwa waliendelea kuonyesha upendo kama wa Kristo kwa kuhubiri habari njema ya Ufalme walipoweza. Lakini wangewahubiria nani? Kwa kweli, mpango wa Sovieti wa kuwahamisha raia wasomi ambao hawakuwa Wakomunisti ‘uliwafungulia mlango kwa ajili ya neno.’ Ndugu na dada wengi walifurahia mazungumzo yenye matokeo mazuri pamoja na wasomi hao waliohamishwa, ambao huenda ingekuwa vigumu kwao kusikia au kukubali ujumbe wa Ufalme.—Kol. 4:2-4.
“Baadaye tulipelekwa kwenye kambi tofauti,” aeleza Ndugu Kose. “Ushahidi mkubwa ulikuwa ukitolewa katika kila chumba cha gereza. Wakati huo, niliweza kutoa ushahidi kwa njia kubwa zaidi ya vile nilivyoweza kufanya kabla ya kupelekwa kambini au tangu niachiliwe.”
Mashahidi wa Yehova walishambuliwa mfululizo miaka yote walipokuwa uhamishoni. Walinyang’anywa mali na uhuru wao, na kufedheheshwa kwa kila njia. Lakini waliwashinda watesaji wao kwa kudumisha mwenendo mzuri na hali nzuri ya kiroho.
WARUDI ESTONIA
Joseph Stalin alipokufa mwaka wa 1953, watu wengi waliomuunga mkono walihuzunika sana. Wakati huo, Ella Toom alikuwa katika chumba fulani gerezani pamoja na dada wengine sita. Mlinzi aliingia huku akilia na kuwaamuru wasimame na kusema maneno fulani ya kumtukuza Stalin. Walikataa kwa ujasiri.
Baada ya Stalin kufa, hali ya kisiasa ilianza kubadilika. Kuanzia mwaka wa 1956 mpaka 1957, Mashahidi wa Yehova duniani kote waliitumia serikali ya Sovieti barua nyingi sana kwa niaba ya ndugu zao waliokuwa uhamishoni. Mashahidi hao waliokuwa uhamishoni walisamehewa mmoja baada ya mwingine na kuruhusiwa kurudi nyumbani. Nao waliokuwa gerezani wakaachiliwa. Mashahidi fulani waliachiliwa punde tu baada ya Stalin kufa, lakini wengine walihitaji kungoja kwa muda fulani. Kwa mfano, familia ya Tuiman ilipelekwa uhamishoni mwaka wa 1951 lakini waliruhusiwa kurudi nyumbani mwaka wa 1965. Na ingawa ndugu zetu waliweza kurudi Estonia, bado walihitaji kutafuta mahali pa kuishi kwa kuwa mali yao yote ilitwaliwa walipoenda uhamishoni.
KUKUMBUKA YALIYOPITA
Vitisho, ukatili, kazi ngumu, na hali mbaya gerezani ziliwaathiri Mashahidi jinsi gani? Wengi wao waliendelea kuwa waaminifu na imara kiroho, hata walipokabili kifo. Mashahidi Waestonia wapatao 27 walifia gerezani au uhamishoni, kutia ndani Artur Indus, aliyetumika katika Halmashauri ya Utumishi nchini Estonia kabla ya kupelekwa uhamishoni. Friedrich Altpere alikufa punde tu baada ya kuachiliwa, yaelekea kwa sababu ya kazi ngumu. Imani ya watumishi wa Yehova ilijaribiwa vikali huko Siberia; lakini walijifunza mambo mengi, na walidumisha utimilifu wao. Kwa kweli, mateso hayo yaliimarisha sana imani na uvumilivu wao.—Yak. 1:2-4.
“Ndugu wote wenye majukumu walikuwa kwenye kambi za wafungwa,” anaeleza Viljard Kaarna, “na tuliendelea kuwasiliana nao. Kwa hiyo, tukiwa Siberia tulipata vitabu kwa ukawaida na tulikuwa imara kiroho. Tuliporudi Estonia, ilikuwa vigumu kupata chakula cha kiroho kwa ukawaida. Hatufikiri tungeendelea kuwa imara kiroho kama hatungepelekwa uhamishoni.”
Wahamishwa wengi wasio Mashahidi walitiwa uchungu sana na mateso waliyopata. Kwa upande mwingine, Mashahidi wa Yehova waliuona uhamisho wao kuwa jambo la kuwaimarisha kiroho.
“Tulijifunza utii kutokana na mambo tuliyoteseka,” asema Corinna Ennika. “Tulimtumaini Yehova na hatukujuta kamwe. Tulijifunza kwamba hatukuhitaji vitu vingi ili kuishi. Mimi na dada yangu Ene, tulikuwa tu na masanduku mawili madogo chini ya kitanda. Sasa tukihisi tunahitaji vitu vingi zaidi, tunatafakari jinsi hali zilivyokuwa uhamishoni. Wakati wa miaka yetu ya ujana—miaka 17 hadi 23—tulikuwa Siberia. Mara nyingi mimi hujiuliza ikiwa tungekuwa imara kiroho kama hatungepelekwa uhamishoni. Ninahisi kuwa wakati huo Siberia ndio mahali palipotufaa zaidi.”
Dada mwingine anasema, “Tulisahau upesi miaka mitano tuliyokuwa Siberia. Ni kana kwamba nilikuwa ninatazama sinema kwa saa kadhaa.”
Aino Ehtmaa anasema: “Sitasahau mianga ya kaskazini iliyoonekana kana kwamba inacheza dansi, siku zenye baridi kali ambapo umande kutoka baharini na katika mito ulifanyiza mawingu yenye rangi za kuvutia, siku ambapo jua halikutua kwa majuma mawili, na siku ambapo halikuchomoza kwa majuma mawili. Ninakumbuka stroberi mbichi ambazo ziliiva wakati wa majira mafupi ya kiangazi na bata-mwitu wa aktiki waliokula matawi madogo ya miti hiyo myembamba. Licha ya matatizo yote niliyopata, nilihisi kana kwamba nilikuwa nikitalii Siberia. Nilitambua kuwa, hata nikiwa Siberia, ninaweza kuwa mwenye furaha nikikaa karibu na Yehova.”
HALI MPYA, MBINU ZA ZAMANI
Baada ya ndugu kurudi Estonia kutoka Siberia, mateso hayakwisha. Polisi wa siri walitumia mbinu za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja kupata habari kuhusu tengenezo letu ili kuliharibia sifa.
Jüri Schönberg, aliyekuwa amekamatwa kwa kukataa kujiunga na jeshi, alichukuliwa katika kambi ya kazi ngumu na kuhojiwa vikali. Ofisa fulani wa KGB alikuwa amesafiri kutoka Kiev, Ukrainia, hadi Estonia ili kumshawishi Jüri ajiunge na KGB. Ofisa huyo alijaribu kumwonyesha kuwa vitabu vya Mashahidi wa Yehova vilipinga serikali na vilijaa makosa. Alimpa Jüri magazeti ya Mnara wa Mlinzi asome, lakini ingawa magazeti hayo yalionekana kuwa ya kweli, Jüri aliyakataa. Alikuwa na wasiwasi kuwa huenda yakawa magazeti bandia ambayo mara kwa mara KGB waliyatayarisha ili kuwachanganya Mashahidi. Kwa juma moja, ofisa huyo alimshinikiza Jüri kuanzia asubuhi mpaka jioni ili ashirikiane na KGB, lakini ndugu yetu akawa imara na kukataa kulegeza msimamo wake.
KUWASILIANA TENA NA “MAMA”
Ingawa lile Pazia la Chuma liliwazuia Waestonia wasiwasiliane na watu wa nchi nyingine, halingeweza kuzuia chakula cha kiroho kisiwafikie akina ndugu. Kwa miaka mingi akina ndugu walitumia vitabu vya miaka iliyopita. Hata hivyo, walipokuwa uhamishoni huko Siberia, Mashahidi Waestonia waliweza kukutana na ndugu kutoka maeneo mengine ya Muungano wa Sovieti. Waliporudi Estonia, waliendelea kuwasiliana kwa ujasiri na ndugu hao wa Muungano wa Sovieti na mara kwa mara, waliweza kupata chakula cha kiroho cha karibuni. Kwa mfano, kuanzia mwaka wa 1956, waliwasiliana na Ivan Dziabko na ndugu wengine kutoka Ukrainia na walipata vitabu kutoka kwao. Lakini waliwasiliana nao mara chache na walipata vitabu vichache. Mengi zaidi yalihitaji kufanywa, na muda si muda Yehova akabariki jitihada za ujasiri za ndugu zetu.
Chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza, ofisi ya tawi ya Finland ilifanya mipango ya kuwasaidia ndugu Waestonia kwa njia yenye utaratibu zaidi. Vilho Eloranta, aliyekuwa painia nchini Estonia miaka ya 1930, alipewa mgawo wa kuwasiliana nao. Katika ziara yake ya kwanza nchini humo, mapema miaka ya 1960, alikutana na Fanny Hietala. Baada ya hapo, ndugu wengi waliojifanya watalii walizuru Finland na walitumika kama wajumbe wa kusafirisha vitabu na barua na hivyo kusaidia kuendeleza mawasiliano. Hatimaye, ndugu wa Estonia walianza kuwasiliana na “Mama,” kama akina ndugu walivyoliita tengenezo la Yehova. Waliweza kutuma barua na ripoti za huduma ya shambani na waliweza kupokea vitabu kwenye mikanda ya filamu yenye maandishi madogo. Hata hivyo, kwa kuwa mambo hayo yalihitaji kufanywa kwa siri kabisa na kwa busara sana, mawasiliano yalifanywa mara mbili au tatu kwa mwaka.
Hugo Kose, Jr., binamu ya Adolf Kose, anayeishi Marekani, alizuru Estonia mara 15 kama mjumbe. Katika mojawapo ya ziara zake, walinzi wa mpakani walimpekua kwa makini lakini hawakupata chochote. Hata hivyo, alianza kuwa na wasiwasi walipomuuliza moja kwa moja alikuwa wa dini gani. Alipotambua kuwa walinzi hao hawakujua Kiingereza vizuri, Hugo alizungumza kwa haraka sana. Walinzi hao hawakutaka ijulikane kuwa hawajui Kiingereza kwa kumwomba azungumze polepole, kwa hiyo, simu ilipolia, walimwambia aondoke haraka kwa kuwa meli ilikuwa tayari kung’oa nanga. Hugo aliondoka mara moja!
Wale waliotumika kama wajumbe walijua kuwa mgawo wao ni muhimu sana, na waliuchukua kwa uzito. Nyakati zote walikuwa macho na walifahamu hatari ya kujiamini kupita kiasi. Ripoti za huduma ya shambani ziliandikwa kwa lugha ya siri ili mtu asiyehusika asiweze kuzisoma. Wajumbe hao walitambua kuwa wangeweza kuhatarisha maisha yao na ya wengine kwa kutokuwa macho. Nyakati nyingine, waliwaona maofisa wa KGB wakiwafuata. Kwa mfano, wakati Viljard Kaarna alipokuwa akingoja kifurushi kutoka kwa ndugu wawili, alimwona ofisa mmoja akiwapiga picha na kisha kuwafuata. Bila shaka, alikuwa akikusanya ushahidi ili kuutumia dhidi ya Mashahidi. Hata hivyo, katika miaka hiyo yote, ndugu hawakupoteza vitabu vyovyote, barua, wala ripoti.
USIMAMIZI WABORESHWA
Kwa muda fulani, kazi ya kuhubiri katika Muungano wa Sovieti ilisimamiwa na Halmashauri ya Nchi iliyokuwa Ukrainia. Zaidi ya hayo, ndugu kadhaa walikuwa waangalizi wa wilaya katika eneo hilo kubwa. Lakini sasa kazi ilikuwa inapanuka huko Estonia, na ilihitaji mtu wa kuisimamia. Adolf Kose, ndugu mnyamavu ambaye imani yake ilikuwa imeimarishwa na majaribu mbalimbali, alipewa mgawo wa kusimamia kazi nchini Estonia mwaka wa 1967. Baadaye, majukumu yake yaliongezwa yakatia ndani kushughulikia barua na ripoti za Latvia, Lithuania, Karelia, na Leningrad (sasa ni St. Petersburg), na Murmansk. Ndugu Kose pia alisaidia kupanga kazi ya uchapaji katika maeneo mbalimbali.
Ndugu Kose alifaulu jinsi gani kushughulikia majukumu hayo yote na pia kufanya kazi wakati wote pamoja na mke wake, Koidula, katika shamba la nguruwe karibu na mji wa Tapa? Ndugu Kose alibuni mashini fulani iliyorahisisha kazi yake kwa kiasi fulani. Kwa hiyo, aliweza kupata wakati wa kushughulikia migawo yake ya kiroho.
Baadaye, ndugu kama vile Viljard Kaarna, Lembit Toom, na Silver Silliksaar walisaidia kutembelea makutaniko nchini Estonia na nchi jirani katika Muungano wa Sovieti. Watu wanaozungumza Kirusi nchini Estonia walipoongezeka, Alexandr Yevdokimov alipewa mgawo wa kutembelea makutaniko ya Kirusi. Mwishowe, kazi ya kuchapa iligawanywa, na ndugu waliozungumza Kirusi wakaanza kuchapa vitabu vyao. Machapisho yao yalipofika yakiwa katika mikanda ya filamu, yalikuwa tayari katika Kirusi, hivyo, ndugu wangeweza kutumia filamu hizo kuchapisha nakala nyingi kwenye karatasi za picha. Hata hivyo, makutaniko yalipoongezeka, kazi hiyo ngumu ya kutokeza nakala iliachwa kwa kuwa haingeweza kutosheleza uhitaji uliokuwapo na ndugu wengi walihitajika kusaidia kuchapa katika maeneo kadhaa. Ingawa hawakuwa na vifaa vya kutosha, akina ndugu walikuwa wamechapa mamia ya nakala za vitabu tofauti-tofauti zaidi ya 20 kisiri. Kurasa zaidi ya milioni tano za vitabu vya Kiestonia na Kirusi zilitokezwa kwa mkono kati ya 1966 na 1989.
UMUHIMU WA KUWA MACHO
Wakati fulani polisi waliipekua nyumba ya ndugu wakijifanya kuwa wanatafuta pikipiki iliyoibwa. Hata hivyo, walienda moja kwa moja kwenye rafu ya vitabu, mahali ambapo kwa wazi mtu hawezi kuficha pikipiki! Bila shaka, walikuwa wakitafuta vitabu vilivyopigwa marufuku. Walivunjika moyo kama nini walipovikosa!
Akina ndugu waliwezaje kuficha vitabu hivyo visitambuliwe? Walipochapisha vitabu, mara nyingi walitumia majalada ya vitabu na magazeti ya zamani ya kilimwengu. Hivyo, nyumba zilipopekuliwa bila taarifa, machapisho hayo ya “zamani” hayakugunduliwa.
Mashahidi walitumia matukio ya pekee kama vile harusi, kuwa mbinu ya kuficha mikutano na makusanyiko yao. Kwa mfano, sherehe ya harusi ya Heimar na Elvi Tuiman iliendelea kwa siku mbili. Nyakati nyingine vikusanyiko hivyo, viliendelea kwa siku tatu au nne. Wazee wa makutaniko nchini Estonia waliwatia moyo wachumba wasialike watu wengi kwenye harusi zao. Vikundi vidogo havingeweza kuonekana kwa urahisi, havikuvuta uangalifu sana, na hivyo havingesababisha matatizo mengi.
NDUGU KUTOKA URUSI WAHAMIA ESTONIA
Mnamo 1970, Mashahidi wa zamani kutoka Ukrainia, Belarus, na sehemu nyingine za Muungano wa Sovieti walianza kuhamia Estonia. Kwa wengi wa ndugu hao, maisha nchini Estonia yalikuwa rahisi kuliko ilivyokuwa katika nchi zao, ambako walivumilia mateso makali.
Kwa msaada wa akina ndugu kama vile Nikolai Dubovinski kutoka Ukrainia, aliyetumika kwa muda mrefu akiwa mzee, kutaniko la kwanza la lugha ya Kirusi lilianzishwa mjini Tartu mnamo 1972 likiwa na wahubiri 50 hivi. Eneo la lugha ya Kirusi lilikuwa na ongezeko kubwa, na katika mwaka wa 2010, kulikuwa na makutaniko 27 yanayotumia lugha ya Kirusi na vikundi 4—yakifanyiza zaidi ya nusu ya wahubiri wote nchini Estonia.
NJIA MBALIMBALI ZA KUHUBIRI ISIVYO RASMI
Ndugu waliokuwa wakitumia lugha ya Kirusi walikuwa wenye bidii na ujasiri na hawakusita kuzungumza na watu katika vikao visivyo rasmi. Kwa mfano, wangeanzisha mazungumzo na watalii ambao walikuwa wakitembelea makanisa huko Tallinn na kuwahubiria. Mara nyingi watalii walifikiri kwamba mtu anayezungumza kuhusu Biblia alikuwa akiongoza watalii, hivyo walisikiliza kwa makini yale ambayo ndugu hao walisema.
Dada fulani walihubiri katika gari-moshi. Walikuwa wakinunua tiketi iliyowawezesha kusafiri kutoka Tartu kwenda Tallinn, kisha kurudi tena Tartu. Safari hiyo ya saa nane iliwapa nafasi nzuri ya kuanzisha mazungumzo pamoja na abiria na kuwahubiria habari njema.
Maria Pasechnick, ambaye alihamia Estonia kutoka Kazakhstan anasema hivi: “Nilisali ili nipate funzo la Biblia.” Baada ya kufikiria jambo hilo, aliamua kuwahubiria watu ambao alikuwa akingoja pamoja nao kwa muda mrefu kwenye foleni ndefu, akisubiri kununua chakula katika maduka.
Maria anaendelea kusema hivi: “Siku moja nilipokuwa nimepanga foleni, nilianza kuzungumza na mwanamke fulani, na hatua kwa hatua nikaanza kuelekeza mazungumzo katika Biblia. Mwanamke huyo hakupendezwa sana, lakini alinipeleka kwa rafiki zake na kunitambulisha kwao, kisha akaniacha niendelee na mazungumzo pamoja nao. Kwa hiyo, niliweza kuanzisha mafunzo manne ya Biblia. Mwanamke mmoja alibatizwa na kuwa Shahidi na anaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu.”
Kama ilivyo kila mahali leo, watumishi wengi wa Yehova waliweka mfano mzuri mahali walipofanya kazi. Kwa mfano, mratibu wa Chama cha Ukomunisti katika kampuni fulani ya umeme alidokeza kwamba Leonhard Nilsk hakuhitajika tena katika kampuni hiyo kwa sababu alikuwa mtu wa dini. Hata hivyo, msimamizi wa maabara ya umeme alisema hivi: “Je, tunawahitaji Wakomunisti walevi ambao hawatimizi majukumu yao au tunahitaji watu wa dini ambao wanajulikana kuwa waaminifu?” Pia, wafanyakazi wenzake walimtetea Leonhard kwa sababu ya sifa zake nzuri, na jambo hilo halikuzungumziwa tena. Kwa wazi mratibu wa chama alikuwa anajipendekeza kwa maofisa wa juu wa chama, na utawala wa Kikomunisti ulipoisha nchini Estonia, mratibu huyo wa chama alipoteza kazi yake.
KUTOA USHAHIDI CHINI YA MARUFUKU
Lembit Reile, ambaye sasa anatumika katika Halmashauri ya Tawi ya Estonia anasema hivi: “Nilipokuwa shuleni, nilikuwa nikizungumza kwa busara na wengi wa wanafunzi wenzangu. Nilikuwa nikimwalika kijana mmoja nyumbani kwetu, na kumhubiria kwa busara. Baada ya kumaliza shule, sikumwona tena kwa karibu miaka 20. Hivi karibuni, nilipokuwa nikitoa hotuba ya watu wote katika kutaniko la nyumbani kwetu, je, unaweza kukisia ni nani aliyekuwa miongoni mwa wasikilizaji? Ni yule mwanafunzi mwenzangu! Alikuwa akijifunza na Mashahidi wa Yehova, na muda mfupi baada ya ziara yangu katika kutaniko hilo, alibatizwa! Nilifurahi kama nini!”
Kwa sababu kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku, akina ndugu walihitaji kuwa macho walipohubiri. Mzee mmoja anaeleza jinsi walivyofanya hivyo: “Tulichunguza kwa makini watu waliotuzunguka na ambao tungeweza kuanzisha mazungumzo pamoja nao bila shida. Tulihitaji kuwa na busara sana tulipozungumza na watu tusiowajua. Baada ya muda, mara nyingi tungeweza kutambua ikiwa mtu alikuwa anawapasha habari maofisa wa KGB. Pia, ikiwa mtu alikuwa anazungumza sana au kwa sauti kubwa, tungekuwa na shaka. Kwa upande mwingine, ilikuwa salama kuzungumza na mtu mkimya. Mara nyingi tulianzisha mazungumzo na watu ambao hawakuunga mkono serikali ya Kikomunisti—watu walioitwa waasi, ambao walikuwa tayari kusikiliza maoni ya wengine.”
ZIARA YENYE KUTIA MOYO BUSTANINI
Baraza Linaloongoza lilipanga mmoja wa washiriki wake, Lloyd Barry, pamoja na Viv Mouritz, kutoka ofisi ya tawi ya Finland, wakutane na Adolf Kose, aliyekuwa akisimamia kazi nchini Estonia. Walikutana katika bustani huko Leningrad (sasa ni St. Petersburg).
Ndugu Mouritz anasema hivi kuhusu mkutano wao wa siri, “Mara ya kwanza Ndugu Kose alisita kuzungumza, na kwa tahadhari akainua gazeti lake kana kwamba analisoma. Lakini baada ya kuzungumza kwa muda, Adolf alishusha gazeti hilo, na akaanza kuongea kwa uhuru.”
Ndugu Barry alisema hivi, “Tulipomwalika kula pamoja nasi, alikataa akisema kwamba ilikuwa ni vizuri kukazia uangalifu mambo yaliyokuwa ya maana zaidi.”
Wakati Ndugu Kose alipoelezea wasiwasi wake kuhusu mateso na vizuizi ambavyo Mashahidi katika Muungano wa Sovieti walikuwa wanakabili, Ndugu Mouritz na Barry walimpa mapendekezo mengi yenye kutia moyo. Walimweleza hivi: “Hata katika nchi nyingine tunakabili majaribu pia. Majaribu hayo yanaonekana kuwa rahisi, lakini ni hatari zaidi! Tuna vishawishi vingi ambavyo ninyi hamvikabili, na tunapoteza watu wengi katika nchi za Magharibi kuliko hapa.”
Hiyo ilikuwa ziara ya wakati unaofaa na yenye kuimarisha sana kwa Ndugu Kose. Alikuja kugundua baadaye kwamba alikuwa anazungumza na mshiriki wa Baraza Linaloongoza, na kwa shangwe aliwasilisha habari zenye kutia moyo kutoka katika tengenezo la Yehova kwa wote walioendelea kudumisha utimilifu wao chini ya utawala wenye kukandamiza.
Baadaye Ndugu Barry aliandika hivi: “Tunawahurumia sana ndugu zetu katika Muungano wa Sovieti. Lilikuwa jambo zuri kukutana na Ndugu Kose na tulipokuwa tukiagana naye alitupa mkono na kutukumbatia, na hivyo tukamaliza mkutano wetu wenye kupendeza.”
VIJANA WASIMAMA IMARA SHULENI
Watumishi wa Yehova, hasa vijana, walikabili shinikizo la kuunga mkono mashirika ya kisiasa. Walichochewa washiriki katika utendaji uliokuwa kinyume cha dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia.
Ester Tamm anakumbuka hivi: “Siku moja nilipokuwa bado msichana mdogo shuleni, kila mwanafunzi darasani aliambiwa asimame, aende mbele, na aandike maneno fulani katika barua iliyokuwa ikimtakia dikteta, Joseph Stalin siku njema ya kuzaliwa.”
Ester alisimama lakini akakataa kwenda mbele. Badala yake, kwa heshima alisema kuwa hataandika chochote katika barua hiyo. Mwalimu alikasirika, lakini jambo la kushangaza ni kwamba baadhi ya wanafunzi wengine walimuunga mkono Ester na kwa ujasiri wakasema kuwa hawataandika chochote kwenye barua hiyo. Kwa hiyo, jambo hilo likaachwa.
Jambo lingine lilihusu kujifunga kitambaa chekundu shingoni kama ishara ya kuunga mkono Ukomunisti. Wale waliokataa kufanya hivyo walipewa maksi za chini au aina nyingine za adhabu. Ndugu na dada zetu vijana hawakulegeza msimamo wao, walionyesha uaminifu mshikamanifu uleule ulioonyeshwa na Danieli na waandamani wake katika Babiloni la kale.—Dan. 1:8.
MWANZO MPYA KABISA
Ukweli wa kwamba asilimia 7 tu ya watu ndio waliounga mkono Chama cha Kikomunisti unaonyesha kuwa Waestonia wengi hawakuunga mkono mfumo wa Sovieti. Watawala wa Estonia hawakutaka kufuata maagizo kutoka Moscow, na baadhi yao hata waliwasaidia Mashahidi. Kwa mfano, mnamo 1985 ofisa fulani alimfikia Lembit Toom na kumwambia hivi: “Ninajua kwamba wewe ni kama msimamizi miongoni mwa Mashahidi. Mnapofanya mikutano yenu, msiifanye wakati wa sherehe za Kiserikali.”
Lembit akamjibu, “Sawa, nitafikisha ujumbe huo.” Kwa kweli, maofisa wa KGB waliudhika Mashahidi walipofanya mikutano yao wakati wa sherehe za kiserikali. Inaonekana kwamba akina ndugu walikutana kwa njia iliyo wazi sana. Baada ya shauri hilo la kirafiki, walifanya mabadiliko.
Mwaka wa 1986, kulikuwa na mwanzo mpya kabisa wakati Muungano wa Sovieti ulipoanzisha sera yake ya perestroika, au marekebisho. Baraza Linaloongoza liliwatia moyo akina ndugu watumie nafasi na uhuru huo kupanga makusanyiko katika eneo la Ulaya ya Mashariki. Ndugu zetu katika Muungano wa Sovieti hawakuamini kwamba uhuru ungeweza kupatikana kabla ya Har–Magedoni. Mateso yote waliyopata yalikuwa bado katika kumbukumbu zao, na nyumba zao bado ziliendelea kupekuliwa.
WAALIKWA KUHUTUBIA WATU
Kwa sababu ya uhuru ulioongezeka, idadi ya watu waliopendezwa na dini na kujifunza Biblia ilizidi kuongezeka. Watu kwa ujumla walitaka kujua msimamo wa Mashahidi wa Yehova, na mashirika mbalimbali yaliwakaribisha akina ndugu wawahutubie watu kuhusu mambo tunayoamini.
Mmoja kati ya mialiko hiyo ulikuwa wenye kushangaza. Lembit Reile alikubali kukihutubia kikundi cha watu. Siku ilipofika, Ainar Ojarand, ambaye alikuwa amefanya mipango kuhusiana na hotuba hiyo, alikuwa akisikiliza redio huku akinyoa ndevu aliposikia tangazo hili: “Leo kwenye ukumbi wa Sakala Center kutakuwa na hotuba yenye kichwa ‘Biblia Inafundisha Nini?’” Huo ndio uliokuwa ukumbi mkubwa zaidi wa mikutano jijini Tallinn, ambako kwa kawaida Chama cha Kikomunisti kilikuwa kikifanyia mikutano! Karibu Ainar aangushe mashine yake ya kunyolea! Lakini hakuwa na njia ya kumtaarifu Lembit kwamba huo utakuwa mkutano mkubwa kuliko walivyofikiria—hadi walipokutana katika kituo cha basi.
Lembit anasema, “Ukumbi ulikuwa umejaa, na sikuwa nimewahi kuzungumza mbele ya watu wengi kama hao. Pia, sikuwa nimewahi kutumia kikuza sauti na wala kutoa hotuba nikiwa jukwaani. Baada ya kutoa sala fupi, nilimfikiria Paulo akiwa Areopago na kuanza kufikiria utangulizi. Kwa kuwa wasikilizaji wengi walikuwa walaji wa mboga za majani, nilianza hotuba yangu kwa kusema kwamba Mungu aliwapa wanadamu wa kwanza matunda na mboga za majani tu kwa ajili ya chakula. Waliruhusiwa kula nyama tu baada ya Gharika.”
Inaonekana kwamba utangulizi huo ulikuwa na matokeo mazuri kwa wasikilizaji, kwani baadaye watu wengi walitoa majina na anwani zao ili waweze kutumiwa vitabu vyetu vitakapopatikana. Kwa miaka mingi ndugu zetu walitoa hotuba mbele ya watu wengi shuleni, kwenye maktaba, na kwenye vituo vya utamaduni. Kwa hiyo, watu wengi wanaopenda uadilifu walitambua na kuikubali kweli.
KUWA MACHO KIROHO
Mnamo 1989, watumishi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti walianza kuwa na uhuru mwingi zaidi wa kidini, kwa hiyo, baadhi ya akina ndugu waliweza kusafiri hadi kwenye kusanyiko huko Poland. Hebu wazia jinsi akina ndugu walivyohisi kukusanyika kwa uhuru baada ya kukandamizwa kikatili kwa miaka mingi.
Ella Toom anasema hivi: “Tulifurahi sana! Tulilia sana! Kwa upande wetu kusanyiko hilo lilikuwa paradiso ya kiroho kwelikweli.”
Dada mmoja anasema hivi: “Tuliwasili Poland mapema, hivyo tukapelekwa kwenye mkutano katika Jumba la Ufalme. Nilipowaona akina ndugu na dada wakiingia katika Jumba la Ufalme, nilianza kulia. Hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kuingia katika Jumba la Ufalme.”
Mwaka huo, Theodore Jaracz na Milton Henschel, wa Baraza Linaloongoza, wakiambatana na Willi Pohl kutoka ofisi ya tawi ya Ujerumani, walisafiri kotekote katika Muungano wa Sovieti. Walitaka kukutana na ndugu ili kuwatia moyo na pia kuelewa hali ilivyokuwa. Mandhari ya ulimwengu ilikuwa inabadilika haraka, na bila kupoteza muda akina ndugu walitaka kutumia vizuri uhuru uliotokezwa na sera ya perestroika katika Muungano wa Sovieti. Huo ulikuwa wakati wa kupanga upya kazi ya Ufalme, na walianza na kazi ya kutafsiri.
Tangu 1983, Toomas (Tom) Edur, mchezaji wa zamani mwenye nguvu wa ligi ya mpira wa magongo mwenye asili ya Estonia, alikuwa akifanya kazi ya kutafsiri katika lugha ya Kiestonia katika ofisi ya tawi ya Kanada.c Wakati huo, machapisho hayo yaliandaliwa hasa kwa ajili ya Waestonia waliokuwa wakiishi ng’ambo. Lakini mwaka wa 1990, wakati kazi ilipoanza kupamba moto nchini Estonia, Toomas na mke wake, Elizabeth, walitumwa katika ofisi ya tawi ya Finland kusaidia kutafsiri machapisho yetu katika lugha ya Kiestonia. Muda mfupi baadaye walipelekwa nchini Estonia.
Kabla ya hilo, watafsiri mmoja-mmoja walikuwa wakitafsiri wakiwa sehemu tofauti-tofauti. Ilikuwa wazi sasa kwamba watafsiri wangenufaika wakifanya kazi pamoja, wakiwa katika kituo kimoja. Hivyo basi, watafsiri kadhaa walianza kufanya kazi wakiwa nyumbani kwa Lembit Toom huko Tartu. Hata hivyo, kwa kuwa haikuwa rahisi kupata kompyuta katika Muungano wa Sovieti, watafsiri hawakuwa na vifaa ambavyo vingewasaidia kufanya kazi yao vizuri. Lakini, hali ilianza kuwa nzuri baada ya ndugu fulani kutembelea ofisi ya tawi ya Marekani na kurudi na kompyuta mbili—huo ulikuwa mwanzo mzuri kwa utendaji wa idara ya tafsiri. Ni watafsiri wachache waliokuwa na ujuzi wa kutumia kompyuta na pia mfumo wa tengenezo wa Multilanguage Electronic Phototypesetting System (MEPS), hivyo, kazi hiyo haikuwa rahisi. Hata hivyo, walikuwa na hamu ya kujifunza na muda si muda wakaanza kufanya kazi nzuri.
KUSANYIKO LINGINE LENYE SHANGWE LAFANYWA NG’AMBO
Kadiri mamlaka ya Sovieti katika eneo la Ulaya Mashariki ilivyoendelea kupungua, ndivyo watu walivyozidi kufurahia uhuru. Kwa kweli, ndugu na dada 200 kutoka Estonia walipewa vibali vya kuhudhuria Kusanyiko la Wilaya lenye kichwa “Lugha Iliyo Safi,” huko Helsinki, Finland, Juni 1990.
Wajumbe kutoka Estonia waliposhuka katika mashua zilizowapeleka Finland, ndugu wa Finland walishangilia kwa nguvu hapo bandarini kwa muda wa nusu saa hivi! Watu ambao si Mashahidi walitaka kujua ni nini kilichokuwa kikiendelea na watu hao maarufu ni akina nani. Kwa kweli, mambo yalikuwa yamebadilika! Ndugu zetu wanyenyekevu ambao kwa miaka mingi walikuwa wametendwa vibaya na wenye mamlaka wa Sovieti, walikuwa wanakaribishwa kama mabingwa wa Olimpiki!
Jinsi ndugu wa Estonia walivyofurahi kusikia sehemu fulani ya programu ikitolewa katika Kiestonia na kupata machapisho mapya yaliyotolewa katika lugha yao ya asili! Ndugu mmoja ambaye ametumika kwa muda mrefu alisema hivi: “Tuliposhika mikononi mwetu kwa mara ya kwanza broshua katika lugha ya Kiestonia, ilikuwa ni kama kushika kito chenye thamani.”
Wajumbe kutoka Estonia walifurahia hata zaidi waliposikia tangazo lililotolewa katika hotuba ya mwisho. Msemaji alisema kwamba Baraza Linaloongoza limeidhinisha kutolewa kwa gazeti la Mnara wa Mlinzi mara mbili kwa mwezi likiwa na rangi kamili na litakuwa likichapishwa sambamba na toleo la Kiingereza, kuanzia Januari 1991! Wahudhuriaji wenye shangwe walisimama na kupiga makofi kwa muda mrefu. Baada ya kumaliza kupiga makofi, mtu mmoja kati ya wahudhuriaji aliuliza: “Je, kutakuwa na gazeti moja tu kwa kila kikundi cha funzo kama ilivyokuwa zamani? Au kila mtu atapata nakala yake?” Jibu la kwamba kila mmoja atapata nakala yake liliwafurahisha zaidi na kuwafanya waanze kupiga makofi tena.
Mara moja ofisi ya tawi ya Finland ilianza kuchapisha vitabu katika lugha ya Kiestonia na pia kutuma vitabu vya kuanzia mwaka wa 1990 vilivyokuwa vinapatikana. Zaidi ya kupokea msaada wa kiroho, Mashahidi wa Estonia waliopokea na kugawanya misaada mingi kutoka kwa akina ndugu wa nchi mbalimbali—msaada ambao ulihitajika sana kwa sababu ya hali ya uchumi.
KUSANYIKO LA KWANZA LILILOFANYWA KWA UHURU
Mara moja, tengenezo la Yehova lilitumia uhuru wa kidini ulioongezeka kuandaa makusanyiko ya wilaya kotekote katika Muungano wa Sovieti. Jinsi ndugu wa Estonia walivyofurahi kuandaa kusanyiko la kwanza kati ya makusanyiko ya wilaya yenye kichwa “Wapendao Uhuru [wa Kimungu],” lililofanywa jijini Tallinn, Julai 13-14, 1991!
Kusanyiko hilo lilikuwa pindi yenye shangwe hasa kwa baadhi ya wajumbe wenye umri mkubwa. Kwa nini? Kwa sababu mara ya mwisho walipohudhuria kusanyiko la wilaya kwa uhuru nchini Estonia ilikuwa mwaka wa 1940. Walifurahi kama nini kukusanyika kwa uhuru kwa mara nyingine baada ya miaka 50!
Akina ndugu waliozungumza Kirusi kutoka kaskazini-magharibi ya Muungano wa Sovieti, nchi za Baltiki, na Kaliningrad walikusanyika katika ukumbi wa Tallinn Linnahall (Ukumbi wa Jiji wa Maonyesho ya Muziki). Karibu na ukumbi huo, kuna ukumbi wa Jäähall (Ukumbi wa Barafu) ambapo watu 1,000 hivi walihudhuria programu hiyo katika lugha ya Kiestonia. Jumla ya watu katika kumbi zote mbili ilikuwa 4,808. Watu 447 walibatizwa. Hiyo ilikuwa pindi yenye kufurahisha sana!
Makusanyiko kama hayo yaliwasaidia wapya wajifunze kweli. Kwa mfano, Amalie, nyanya ya Leonhard Nilsk alikuwa akihudhuria ibada katika kanisa la Wasabato lakini alikuwa na shaka kuhusu mafundisho yao. Leonhard alimtia moyo nyanya yake achunguze kweli kwa kutumia Biblia. Hata hivyo, Amalie alichukua hatua baada ya kuhudhuria kusanyiko huko Tallinn mwaka wa 1991. Baada ya kuhudhuria siku ya kwanza, Amalie alisema kwamba hatarudi katika kanisa lake tena. Yale ambayo Leonhard alikuwa amemwambia Amalie hayakutosha—alihitaji kuona jinsi kweli inavyowaongoza watu wa Yehova. Alikubali kujifunza Biblia na baadaye akabatizwa.
NDOTO ZATIMIA
Kwa kuwa sasa watumishi wa Yehova hawakuwa wanateswa na kukandamizwa, haikuwa rahisi kwa wengine kuamini kwamba kulikuwa na uhuru wa kuabudu. Kwa mfano, ndugu mmoja aliyetumika akiwa mzee kwa miaka mingi, alikuwa ameingojea kwa hamu siku ambapo kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kitapatikana katika lugha ya Kiestonia. Katika mwaka wa 1991, kitabu hicho ndicho kilichokuwa cha kwanza kati ya vitabu vyetu kuchapishwa katika Kiestonia wakati wa kipindi kipya cha uhuru ulioongezeka.
Mzee huyo anasema, “Kwa kuwa sasa nilikuwa na kitabu hicho mikononi mwangu, sikuweza kuamini macho yangu. Nilipokuwa nikizungumzia kitabu hicho kwenye mkutano, nilishindwa kuzuia machozi. Kwa dakika fulani kila mtu alinyamaza, kwa kuwa hawakuamini masikio yao. Kisha vilio vya furaha vikafuatia! Akina ndugu walikuwa wakishangilia na kulia wakati uleule. Ilikuwa ni pindi isiyosahaulika. Kila wakati ninapoikumbuka mimi hutiririkwa na machozi.”
Mara nyingi akina ndugu walihisi ‘ni kama wanaota ndoto.’ (Zab. 126:1-6) Baada ya miaka mingi ya hali ngumu, wengi walishuhudia matokeo mazuri ya ahadi hii inayopatikana katika Neno la Mungu: “Katika majira yanayofaa tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—Gal. 6:9.
HATUA YA MAANA SANA KATIKA UTENDAJI WA KITHEOKRASI
Oktoba 31, 1991, ni tarehe ambayo ndugu na dada zetu wa Estonia wataendelea kuikumbuka sana. Hiyo ilikuwa tarehe ambayo kutaniko la kwanza la Mashahidi wa Yehova liliandikishwa kisheria nchini Estonia.
Wakati wa kupanga upya mambo ya kiroho ulikuwa umewadia. Watu wengi walipendezwa na habari njema, na walionyesha waziwazi kuwa wanavutiwa na Biblia na dini. Mafunzo ya Biblia yalihitaji kuongozwa, na pia mikutano ya kutaniko, makusanyiko ya pekee na ya mzunguko, na makusanyiko ya wilaya yalihitaji kupangwa vizuri. Watafsiri walihitaji vifaa vya kutosha ili waweze kufanya kazi yao iliyokuwa inazidi kuongezeka.
Wakati huohuo, wamishonari kutoka Gileadi walikuwa wameanza kuwasili, na walihitaji kutafutiwa nyumba zinazofaa. Pia, walihitaji kusaidiwa kupata viza na vibali vya kukaa nchini Estonia. Maofisa wa serikali walihitaji kujulishwa kuhusu msimamo wetu kuhusiana na mambo ya kisiasa. Vibali vya kujenga Majumba ya Ufalme vilihitajika pia.
Reino Kesk, ambaye wakati huo alikuwa akitumika akiwa mwangalizi wa mzunguko anasema, “Kwa sababu ya mambo ya msingi ya kitheokrasi yaliyohitaji kufanywa, miaka hiyo ilipita haraka sana kana kwamba ilikuwa miezi michache tu. Huo pia ulikuwa wakati wenye kusisimua. Watu waliipenda kweli na kuikubali haraka. Katika makutaniko mengi, wengi walitaka kubatizwa. Baadhi ya watu wanaopendezwa ambao walikuja kwenye kusanyiko bila kujua mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova, walifurahia hotuba na mara moja walitaka kubatizwa. Kulikuwa na mengi ya kufanya ili kuwasaidia!”
Estonia ilipokuwa chini ya utawala wa Sovieti, kazi ya kuhubiri ilisimamiwa na ofisi ya tawi ya Ujerumani. Mojawapo ya mbinu za siri za mawasiliano kati ya Ujerumani na Estonia ilikuwa kupitia ofisi ya tawi ya Finland. Sasa mipaka ikiwa imefunguliwa na mawasiliano kurahisishwa hata zaidi, ofisi ya tawi ya Finland ilianza kusimamia kazi ya kuhubiri nchini Estonia mwaka wa 1992.
WENYE BIDII NA HAMU ZAIDI!
Kwa sababu wengi walikuwa wanafanya maendeleo haraka, ilikuwa vigumu kuwajua wapya ambao walihitaji kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa. Kwa mfano, Tom Edur alipotembelea kikundi kipya asubuhi moja katika siku ya Ukumbusho wa Kifo cha Kristo, alishangaa kuona idadi kubwa ya watu waliojitokeza ili kwenda kuhubiri.
“Je, unamjua kila mtu hapa?” Tom akamuuliza ndugu mwenyeji.
Ndugu huyo akajibu, “Wengine si wahubiri.”
Hivyo, Tom akaongoza mkutano wa utumishi wa shambani na kisha akasema, “Labda baadaye nitazungumza na wale ambao bado si wahubiri.”
Wanafunzi wa Biblia wapatao kumi walijitokeza na kusema kwamba walikuwa wanataka kwenda kuhubiri. Baada ya Tom kuzungumza nao kuhusu matakwa ya msingi ya kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, wanawake watatu vijana walikiri kwamba bado hawakuwa wamejiuzulu katika makanisa yao. Tom aliwaeleza kwamba ikiwa wanataka kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, wanapaswa kuomba majina yao yaondolewe kwenye orodha ya washiriki wa makanisa yao. Hivyo ndivyo walivyofanya! Mara moja walienda kwenye kanisa lao, wakaomba majina yao yaondolewe kwenye orodha ya washiriki wa kanisa, na kisha wakajiunga na wengine katika kazi ya kuhubiri.
Mtu mmoja aliyekuwa katika mkutano huo wa utumishi alikuwa bado anavuta sigara. Ingemchukua muda kuacha zoea hilo, hivyo alirudi nyumbani akitazamia kuwa mhubiri baadaye.
Kwa kuwa sasa akina ndugu wangeweza kuhubiri bila kuzuiwa na serikali, walikuwa na hamu ya kutumia kila nafasi kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo. Wengine walikuwa na bidii sana hivi kwamba walihitaji kudumisha usawaziko katika mambo ya kiroho. Kwa mfano, alipokuwa akipitia maswali ya ubatizo pamoja na kijana fulani, Tom Edur alimuuliza ikiwa wazee walikuwa wamempa shauri lolote.
Yule kijana alijibu, “Ndiyo, wazee walinishauri kuwa mwangalifu kuhusu jinsi ninavyotumia wakati wangu.”
“Tatizo lilikuwa nini?” Tom akamuuliza.
Kijana akajibu, “Kwa sababu ya kutumia saa 150 katika utumishi wa shambani kila mwezi, nilikuwa nimepuuza mambo mengine ya kiroho. Wazee walinishauri kwamba kama ningehubiri saa 100, ningeweza kupata muda kwa ajili ya funzo la kibinafsi na kutayarisha mikutano.”
KUSANYIKO LENYE SHANGWE NCHINI URUSI
Tukio lingine muhimu katika historia ya kitheokrasi ni kusanyiko la kimataifa lililofanyika huko St. Petersburg, nchini Urusi, mnamo Juni 1992. Kwa wengi kati ya wajumbe 1,000 waliohudhuria kutoka Estonia, hiyo ilikuwa pindi nzuri ya kukutana tena na wafungwa wenzao na Mashahidi wengine waliokutana nao walipokuwa uhamishoni huko Siberia.
“Kusanyiko hilo lilipangwa kufanyika wakati unaofaa kabisa,” mjumbe mmoja anasema. “Tulikodi gari-moshi maalum kwa gharama ya chini kwa kutumia rubo za Urusi. Kisha, juma moja kabla ya kusanyiko, Estonia ikaanza kutumia krooni ya Estonia badala ya rubo. Kama tungekuwa nje ya Estonia juma hilo la kubadilisha pesa, hatungeweza kubadilisha pesa zetu. Hata hivyo, ingawa tulikuwa Estonia tuliruhusiwa kubadilisha kiasi kidogo tu cha pesa. Tungefanya nini na rubo ambazo hatukuweza kubadilisha? Kwa sababu rubo bado zilikuwa zinatumiwa nchini Urusi, akina ndugu walibeba rubo hizo kwenye kusanyiko na kuzitumbukiza katika masanduku ya michango. Zaidi ya hilo, kama kusanyiko lingefanywa juma moja baadaye, wakati sheria mpya za mipaka zilipotekelezwa, tungehitaji kupata viza kwa gharama ya juu ili kuvuka mpaka. Kusanyiko hilo lilifanywa wakati unaofaa kabisa kwa akina ndugu!”
Mmoja kati ya watu wengi walioguswa sana na kusanyiko hilo la kihistoria ni mwanamke fulani mwenye kupendezwa ambaye alipanga kusafiri pamoja na Mashahidi wa Estonia. “Sikuelewa vizuri muda wa kuondoka,” anasema. “Nilipofika kwenye kituo, gari-moshi lilikuwa tayari limeondoka. Lakini nilikuwa tayari nimelipa nauli. Ningefanya nini sasa? Nilisali kwa Yehova, nikimwomba anisaidie na kumwahidi kwamba nitafanya chochote niwezacho ili niweze kufika kusanyikoni.”
“Msimamizi wa kituo cha gari-moshi aliniambia kwamba ninapaswa kununua tiketi nyingine, lakini sikuwa na pesa za kutosha! Ghafla, nikaona kikundi cha watu wakiwasili. Wote walikuwa na shangwe na walivalia vizuri! Walikuwa Mashahidi kutoka kisiwa cha Sarema. Gari-moshi lao lilikuwa bado halijawasili, na hivyo ningeweza kutumia tiketi yangu kusafiri pamoja nao. Nilifarijika sana!
“Tulipokuwa tukisafiri Mashahidi waliimba nyimbo za Ufalme, ambazo zilinigusa sana. Nilijihisi kana kwamba nimekubalika kuwa mshiriki wa familia yao ya kiroho. Nilikaa nao muda wote wa kusanyiko na kuona kuwa walikuwa wanyofu na wenye upendo. Hilo liliondoa shaka zangu zote. Sasa ilikuwa wazi kwangu kwamba nilikuwa nimepata tengenezo la kidunia la Mungu.” Mwanamke huyo sasa anatumika akiwa painia wa kawaida pamoja na mume wake.
WALIO TAYARI KUFANYA KAZI WAKARIBISHWA
Kazi ya kuhubiri na kupanga mambo kulingana na tengenezo ilikuwa ikisonga haraka, na kulihitajika ndugu zaidi wenye uzoefu wa mambo ya kitheokrasi. Ni nani angejazia uhitaji huo wenye kuongezeka? Kama Isaya, wengi waliitikia na kusema: “Mimi hapa! Nitume mimi.”—Isa. 6:8.
Wamishonari wanne wa kwanza kutoka Gileadi, Vesa na Leena-Maria Edvik na pia Esa na Jaael Nissinen, walifika mnamo 1992. Reino na Lesli Kesk, waliokuwa wakifanya kazi ya kusafiri nchini Kanada kwa miaka 17, walikuwa kati ya wale waliopewa mgawo wa kutumika nchini Estonia. Kisha mnamo 1993, mapainia 20 kutoka Finland wakapewa mgawo wa kutumika katika eneo la lugha ya Kiestonia na Kirusi wakiwa mapainia wa pekee, na wamishonari wengine wanne wakawasili.
Baadaye, wamishonari walitumwa Estonia kutoka katika madarasa kadhaa ya Gileadi yaliyofuata, wakisababisha shangwe na shauku kubwa. Wamishonari fulani ambao hawakuwa wamezoezwa Gileadi pia walitumwa Estonia. Wamishonari na mapainia hao wenye bidii waliendelea kuimarisha msingi uliokuwa umewekwa kwa miaka mingi na ndugu na dada waaminifu nchini Estonia.
Zaidi ya hilo, karibu ndugu na dada 200 kutoka nchi za nje wamekuja kusaidia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Ukomavu wao wa kiroho umesaidia kuimarisha na kutegemeza makutaniko. Makutaniko mengi mapya yalianzishwa, na ndugu hao kutoka nchi za nje ndio waliokuwa wazee pekee katika makutaniko fulani hadi akina ndugu wenyeji walipofanya maendeleo ya kutosha kuweza kushughulikia majukumu zaidi.
Lembit Välja ni mmoja wa wale waliokuja kusaidia. Alizaliwa Estonia, akaokoka Vita vya Pili vya Ulimwengu, kisha akahamia Australia na kuwa Shahidi. Alipokuwa karibu kustaafu, aliamua kurudi Estonia mwaka wa 1990 kuwasaidia watu wengi waliotamani kuijua kweli. Anakumbuka kwamba wakati fulani, alikuwa akiongoza vikundi 18 vilivyokuwa na jumla ya wanafunzi wa Biblia 80 hivi. Vikundi hivyo vilikuwa vimetapakaa katika sehemu kubwa ya Estonia. Alitembelea vikundi hivyo kwa basi, mara nyingi akilala katika vituo vya basi ndani ya mfuko wake wa kulalia. Wanafunzi wake wa Biblia zaidi ya 50 walibatizwa, na akiwa na umri wa miaka 84, bado anaongoza mafunzo ya Biblia manne. Bidii na kujidhabihu kwake kumekuwa na matokeo makubwa—sasa kuna makutaniko na Majumba ya Ufalme katika miji mingi ambayo alikuwa akiitembelea.
Ndugu hao wenye kujitoa waliokuja kusaidia wamenufaika sana. Wengi wamesimulia kuhusu jinsi ambavyo wamejengwa kwa kuwajua wenyeji na njia yao ya maisha. Reino Kesk anasema hivi, “Inapanua mtazamo wako na kukusaidia kuona mambo kama Yehova anavyoyaona anapoutazama ulimwengu mzima.”
ZIARA ZA KWANZA ZA WAANGALIZI WA MZUNGUKO
Wakati huo wa ongezeko kubwa, ziara zenye kutia moyo za waangalizi wa mzunguko ziliyaimarisha sana makutaniko. Waangalizi wa mzunguko walifanya migawo yao kwa bidii sana na mara nyingi walitumia saa 15 kila siku katika utumishi wa shambani, wakihudhuria na kuongoza mikutano, na wakijibu maswali mengi ambayo akina ndugu walikuwa wakiuliza.
Mzunguko wa kwanza kuundwa ulitia ndani Estonia, Latvia, Lithuania, na Kaliningrad. Lugha nne zilikuwa zikitumiwa katika eneo hilo lililokuwa na makutaniko 46 na vikundi 12! Mwangalizi wa mzunguko pia alikuwa na migawo ya ziada ambayo ilichukua wakati wake mwingi, kama vile kushughulikia mambo ya usajili nchini Latvia na Lithuania. Sasa kuna mizunguko minne nchini Estonia pekee.
Lauri Nordling, ndugu mwenyeji ambaye alitumika akiwa mwangalizi wa mzunguko mwaka wa 1995, anasema, “Wahubiri walikuwa wakithamini sana ziara za waangalizi wa mzunguko. Mara nyingi tulipokutana kwa ajili ya mkutano wa utumishi wa shambani, chumba kilijaa watu. Wakati fulani chumba kidogo kilijaa ndugu na dada 70 hivi. Ikiwa ungerusha tofaa juu, halingeweza kufika sakafuni.”
CHANGAMOTO ZA KUJIFUNZA LUGHA MPYA
Ni changamoto kwa watu wengi kujifunza lugha mpya, na Kiestonia ni lugha ngumu kuijua vizuri. Kwa mfano, Markku Kettula, mmishonari mpya alikuwa akizungumza na mtu fulani kuhusu Yesu Kristo. Badala ya kusema Yesu ni Rahuvürst, yaani Mkuu wa Amani, alisema mara kadhaa kwamba Yesu ni rahuvorst—soseji ya amani. Ni baada tu ya Markku kufungua Biblia katika andiko la Isaya 9:6, ndipo mtu huyo alipogundua kwamba chanzo cha kweli cha amani si kitu kinachoweza kuliwa!
Dada painia alianza kujifunza Kirusi baada ya kuhamia Estonia. Alipokuwa akihubiri, alibisha bila kujua mlango wa mzee wa kutaniko ambaye hakumfahamu. Akiwa na kamusi mkononi, alianza kumhubiria. Ndugu huyo alijaribu kumweleza kuwa alikuwa mzee wa kutaniko. Mara moja dada huyo aliangalia neno “mzee” kwenye kamusi yake na kupata neno “-enye kuzeeka”.
“Ah,” dada akasema, “wewe si mzee sana! Isitoshe, katika Paradiso utakuwa kijana tena.” Baada ya kumwonyesha vitabu vya Mashahidi wa Yehova katika nyumba yake ndipo dada huyo akagundua kwamba ndugu huyo kwa kweli hakuwa anamaanisha kuwa amezeeka bali alikuwa mzee wa kutaniko.
HAKIMU ASIYEAMINI KUWA KUNA MUNGU AJIFUNZA KWELI
Wakati wa utawala wa Sovieti, Viktor Sen alikuwa amehukumiwa kifungo cha miaka miwili jela kwa sababu alikataa kujiunga na jeshi. Baada ya kukaa gerezani kwa mwaka mmoja, aliomba apelekwe Siberia kama mkaaji huru, jambo ambalo lingempa uhuru zaidi. Ombi lake lilipokuwa likisikilizwa, mahakimu walimkasirikia, hata hakimu mmoja alisema kwamba watu kama Viktor walipaswa kunyongwa au kupigwa risasi.
Miaka michache baadaye, katika kusanyiko, ndugu fulani alimtambulisha Viktor kwa kikundi fulani cha watu wenye kupendezwa na kumuuliza, “Je, unamtambua yeyote?”
“Hapana,” akajibu Viktor.
“Kweli?” ndugu huyo akamuuliza. Kisha, akamnyooshea kidole mmoja kati ya wale watu wenye kupendezwa, ambaye alikuwa ameaibika sana, na kumuuliza Viktor, “Je, humjui mwanamume huyu?
Viktor alikuwa hamkumbuki na alishangaa sana kujua kwamba mwanamume huyo alikuwa Yuri, mmoja kati ya mahakimu waliokuwa wakisikiliza ombi lake. Sasa alikuwa akijifunza Biblia na alikuwa katika kusanyiko pamoja na Viktor. Ni nini kilichobadilisha mtazamo wa Yuri kuelekea Mashahidi wa Yehova?
“Nililelewa katika familia isiyoamini kwamba kuna Mungu,” akaeleza Yuri. “Nilipokuwa shuleni, mara nyingi nilitoa hotuba kuhusu hatari ya dini. Kisha, miaka kadhaa baadaye, nikaketi mara chache kusikiliza wakati rafiki zangu walipokuwa wakijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Niligundua kwamba ingawa nilijua vema uwongo wa dini, sikujua chochote kuhusu Biblia. Hivyo, nikapendezwa kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia.”
Baada ya Yuri kubatizwa, alimwambia Viktor hivi: “Mara ya mwisho tulipokuwa mahakamani pamoja tuliketi pande mbili tofauti. Lakini tukishtakiwa kwa kosa lilelile tena, tutaketi upande mmoja! Sitakuwa hakimu wako wakati huo.” Yuri na Viktor ni wazee wa kutaniko jijini Tallinn.
UKUMBUSHO USIOWEZA KUSAHAULIKA
Ndugu aliyekuwa amehamia tu Estonia aliwakaribia Pavel na Margarita na kwa Kiestonia chake kibovu akasema, “Ikiwa mnataka uzima wa milele, mnapaswa kuja kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo leo jioni.” Mtu huyo na mke wake walivutiwa sana na wakaamua kuhudhuria.
Pavel na Margarita walikaribishwa kwa uchangamfu kwenye Ukumbusho. Lakini programu ilipokuwa ikiendelea walishtuka kidogo kumwona mtu akitembea katikati ya safu za viti akiwaangalia watu na kuandika habari fulani. Hawakujua kwamba alikuwa akihesabu tu watu waliokuwa wamehudhuria. Pavel na Margarita walianza kutia shaka kwa nini walihudhuria, lakini waliogopa kuondoka kwa sababu waliona kwamba wanaume wawili wakubwa walikuwa wakilinda milango. Bila kujua kwamba ndugu hao walikuwa wakaribishaji tu, Pavel na Margarita waliamua kwamba lingekuwa jambo la busara kutojaribu kuondoka.
Hata hivyo, hotuba ya Ukumbusho ilipoisha, Pavel na Margarita walifurahia sana walipomsikia msemaji akitangaza kuhusu mpango wa kujifunza Biblia nyumbani bila malipo kwa yeyote aliyetaka. Hofu ya Pavel na Margarita iliisha wakati akina ndugu walipojitambulisha kwao kwa uchangamfu, hivyo wenzi hao wa ndoa wakaomba funzo la Biblia. Kwa kuwa walikuwa wamepanga kuhama baada ya majuma wawili, waliomba ikiwa wangeweza kujifunza kila siku. Walipohamia kwenye makao yao mapya, kwa hamu waliwapigia simu akina ndugu waliokuwa wakiishi karibu nao, wakajitambulisha, na kuendelea na funzo la Biblia.
‘WAMESHUHUDIA MATENDO YENU MAZURI’
Mashahidi wa Yehova nchini Estonia wanaonyeshana upendo, kama wafanyavyo ndugu na dada zao ulimwenguni pote. (Yoh. 13:35) Wengine wanaona matendo hayo na wanavutwa katika ibada ya kweli.—1 Pet. 2:12.
Toivo alipewa kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu na dada aliyekuwa amemnyoa nywele kwenye kibanda fulani. Alipomaliza kukisoma, alitaka kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme, lakini alisita kwa kuwa alikuwa ameonywa kuhusu Mashahidi. Hivyo, aliamua kuwachunguza wakiwa kwenye Jumba la Ufalme bila kutoka katika gari lake. Alitaka kuona ni watu wa aina gani walioingia katika Jumba la Ufalme kabla ya mkutano na jinsi walivyoonekana walipotoka nje.
Alivutiwa kuona akina dada wakikumbatiana kwa shauku na aliweza kutambua waziwazi kuwa watu hao wanapendana kikweli. Kwa hamu alianza kuhudhuria mikutano na kujifunza Biblia. Alifanya maendeleo haraka na muda si muda akaanza kuhubiri kwa bidii. Sasa yeye ni Shahidi aliyebatizwa.
“YEHOVA AMEJIBU SALA YANGU!”
Mnamo 1997, Maria anayeishi katika kijiji kidogo cha Tootsi alipewa trakti Habari Njema za Ufalme Na. 35. Aliisoma trakti hiyo na kuiandikia ofisi ya tawi akiomba funzo la Biblia. Muda mfupi baadaye, Markku na Sirpa Kettula, wamishonari waliokuwa wakiishi Pärnu, wakaanza kujifunza Biblia pamoja na Maria. Baada ya muda mfupi, Maria alianza kuzungumza na wengine kuhusu kweli, na punde si punde binti-mkwe wake, Ingrid, na jirani ya Ingrid anayeitwa Malle wakajiunga na funzo hilo. Maria alipotaka kuanza kuhubiri, wazee walimtia moyo kwanza ahudhurie mikutano kwa ukawaida. Hata hivyo, kutaniko la karibu lilikuwa Pärnu, umbali wa kilomita 40, na hakuwa na pesa za kutosha kulipia nauli. Hivyo, baada ya kutiwa moyo na wamishonari, Maria alisali akimwomba Yehova msaada.
Wamishonari hao walipomtembelea tena, Maria alisema hivi kwa shangwe: “Yehova amejibu sala yangu!”
“Amejibu sala yako jinsi gani?” Markku na Sirpa wakamuuliza.
Kwa uchangamfu Maria akawajibu, “Nitawakusanya watu nyumbani kwangu, na mnaweza kupanga mikutano na kuanzisha kutaniko hapa. Kisha nitaweza kuhudhuria mikutano na pia kuanza kuhubiri.”
Wamishonari hawakutaka kumvunja moyo, lakini kwa busara wakamweleza kuwa kuanzisha kutaniko si rahisi kama anavyofikiri. Walimtia moyo ajaribu kuhudhuria mikutano huko Pärnu, angalau Jumapili.
Hivyo, Maria alisali tena kuhusu jambo hilo. Zaidi ya hilo, aliacha kununua magazeti ya habari ili ahifadhi pesa kwa ajili ya nauli. Muda si mrefu alikuwa na pesa za kutosha kuweza kuhudhuria mikutano mara nne kwa mwezi na akafurahi alipoanza kuhubiri. Hata hivyo, Maria angefurahia baraka nyingi hata zaidi.
Kwa kuwa kulikuwa na watu wengi waliotaka kujifunza Biblia huko Tootsi, wazee walipanga kuwe na funzo la kitabu, ambalo Maria, Ingrid, Malle, na watu wengine wenye kupendezwa wangeweza kuhudhuria. Miezi kadhaa tu baadaye, Maria na Malle walibatizwa, na Ingrid akabatizwa majira ya kiangazi yaliyofuata. Muda si mrefu mume wa Malle alibatizwa, na dada ya Malle akabatizwa wakati wa majira ya baridi kali yaliyofuata. Kikundi kidogo kinachositawi huko Tootsi kinafurahi kwamba trakti Habari za Ufalme Na. 35 ilifikisha kweli katika kijiji chao kidogo na kwamba wamepata baraka nyingi kutoka kwa Yehova zikiwa jibu la sala zao nyingi.
Kumekuwa na shangwe nyingi na matokeo mengi mazuri katika utendaji wa Ufalme katika miaka 20 iliyopita, kwani watu wengi wenye mioyo minyofu wameingia katika tengenezo la Yehova. Hata hivyo, watu hao wote ambao wanapenda uadilifu wangekusanyika wapi ili kuabudu na kufundishwa na Mungu wa kweli?
MAJUMBA YA UFALME YANAHITAJIKA HARAKA!
Jengo la kwanza la kufanyia mikutano lilijengwa katika mji wa Räpina, ulio kusini mwa Estonia, na akina ndugu walifanya mikutano katika jengo hilo kwa miaka mingi. Lakini ilikuwa wazi kwamba jitihada za akina ndugu wenyeji za kujenga mahali pao pa ibada hazingefanikiwa kwa sababu ya ongezeko la haraka la idadi ya wahubiri. Ofisi ya Uhandisi katika ofisi ya tawi ya Finland ilisaidia kwa kuchora ramani za Majumba ya Ufalme na majengo ya ofisi kwa ajili ya nchi za Baltiki. Ilikuwa shangwe iliyoje, mwaka wa 1993, wakati Jumba la Ufalme la kwanza lilipojengwa huko Maardu na kufuatiwa na mengine mengi baadaye.
Sasa kuna Majumba ya Ufalme 33 kwa ajili ya makutaniko 53 nchini Estonia. Akina ndugu wanafurahi kwamba wana Majumba ya Kusanyiko mawili—moja jijini Tallinn na lingine jijini Tartu. Yote mawili yalijengwa mwaka wa 1998.
Shahidi wa muda mrefu, Alexandra Olesyuk, anakumbuka: “Tulitamani sana kujenga Jumba la Ufalme jijini Tartu. Hivyo, tulipoombwa kwenda kusafisha mahali ambapo Jumba la Ufalme litajengwa, nilikuwa wa kwanza kwenda kusaidia, ingawa nilikuwa na umri wa miaka 79! Nilisafisha na kubeba vitu. Kila mara nilipopita kwa basi karibu na uwanja wa Jumba la Ufalme, nililia kwa shangwe. Nililia pia jumba hilo lilipokamilika.”
OFISI MPYA YA TAFSIRI
Kadiri idadi ya wahubiri ilivyoongezeka, ndivyo majengo makubwa zaidi yalivyohitajika ili kutosheleza mahitaji ya nchi na hasa kikundi cha watafsiri. Jengo fulani lililoonekana kuwa linafaa na ambalo halikuwa limekamilika, lilipatikana jijini Tallinn, kwenye Barabara ya 77 Herzeni (sasa Puhangu). Hata hivyo, jengo hilo lilihitaji marekebisho makubwa.
Ofisi ya tawi ya Finland iliandaa michoro ya ujenzi, vifaa, pesa, na wafanyakazi ili kukamilisha kazi hiyo. Bila msaada wao huenda ujenzi haungefaulu. Kwa mfano, wakati huo nchini Estonia vifaa vya ujenzi vilikuwa vya hali ya nchini au havikuwa vikipatikana. Zaidi ya hayo, ni ndugu wachache Waestonia waliokuwa na ujuzi wa kujenga ambao ulihitajika katika kazi hiyo. Hata hivyo, akina ndugu wenyeji walifundishwa hatua kwa hatua na kusaidiwa kupata uzoefu. Kufikia Februari 1994, sehemu ya kwanza ya majengo ya ofisi ilikuwa imemalizika. Mwaka huo, ndugu Toomas Edur, Reino Kesk, na Lembit Reile, waliwekwa rasmi katika Halmashauri ya Nchi ili kusimamia nchi zote tatu za Baltiki zilizokuwa chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Finland. Kwa kuwa vyumba zaidi vilihitajika, upanuzi ulifanywa mwaka wa 1997 na 1999.
Kampuni ya maji, ambayo wakati huo jengo lake lilikuwa kando ya ofisi ya tawi ilipendezwa na mpangilio wa bustani ya Betheli. Hivyo, kampuni hiyo ikakubali kupunguza bei ya maji ili akina ndugu wawasaidie kutengeneza bustani, ua, na mifumo yao ya taa. Hilo lilifanya jengo lao lionekane kama Betheli. Baadaye, waliuwazia akina ndugu jengo hilo kwa bei nzuri. Jengo hilo linatumiwa kama studio kwa ajili ya kurekodi drama na DVD, kutia ndani DVD za lugha ya ishara. Pia, sehemu fulani ya jengo hilo imerekebishwa kwa ajili ya Shule ya Mazoezi ya Kihuduma.
MAKUSANYIKO YA KIMATAIFA JIJINI TALLINN
Akina ndugu Waestonia walifurahia sana walipopata habari kwamba watakuwa wenyeji wa Kusanyiko la Kimataifa la “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” lililofanywa mwaka wa 1996. Makusanyiko mawili yaliyofanywa Tallinn yalikuwa kwa ajili ya wajumbe wanaozungumza lugha ya Kiestonia na Kirusi na pia akina ndugu kutoka Latvia na Lithuania. Wajumbe wengine walialikwa kutoka nchi 15. Makusanyiko hayo mawili ya siku tatu yalifanywa mwezi wa Agosti. Washiriki watano katika Baraza Linaloongoza—Ndugu Barber, Henschel, Jaracz, Schroeder, na Sydlik—walikuwapo ili kuwatia nguvu akina ndugu kwa hotuba zao. Kulikuwa na kilele cha wahudhuriaji 11,311 kwenye makusanyiko hayo, na watu wapya 501 waliojiweka wakfu wakabatizwa.
Kusanyiko hilo lilitoa ushahidi mzuri na kutangazwa sana na vyombo vya habari. Ripoti hizo zilitia ndani mahojiano ya dakika kumi katika televisheni. Mmiliki wa kituo fulani cha redio alirusha matangazo ambayo yaliwasifu sana Mashahidi kuwa “watu wema.”
Upendo wa kindugu ambao wajumbe walionyesha ulionekana wazi mwishoni mwa kila kusanyiko wakati wa kuagana. Mikono na vitambaa vingi vilivyopungwa-pungwa na machozi ya shangwe yaliyotiririka, yalionyesha hisia za waabudu wa kweli wa Yehova. Wote waliohudhuria walionyesha shukrani zao kwa, Yehova, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo na mkarimu, kwa kupiga makofi kwa muda mrefu baada ya sala ya mwisho. Makusanyiko hayo yanabaki kuwa matukio muhimu katika historia ya Mashahidi wa Yehova nchini Estonia.
ESTONIA YAWA NA OFISI YA TAWI TENA
Kati ya mwaka wa 1926 na 1940 kulikuwa na ofisi jijini Tallinn. Kisha, kuanzia 1994, kukawa na Ofisi ya Nchi iliyokuwa ikisimamia kazi chini ya uangalizi wa ofisi ya tawi ya Finland. Kulikuwa na mengi yaliyotimizwa na wengi walikuwa wakijiuliza kama Estonia ingekuwa na ofisi yake ya tawi kwa mara nyingine. Walipata jibu Machi 1, 1999, wakati Baraza Linaloongoza lilipowaweka Toomas Edur, Reino Kesk (sasa anatumika katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo), Lembit Reile, na Tommi Kauko kutumika katika Halmashauri ya Tawi ya Estonia. Sasa kuna watu 50 hivi wanaotumika katika ofisi ya tawi, wakishughulikia mahitaji ya watumishi wa Yehova washikamanifu na wenye bidii 4,300 nchini Estonia.
KUKABILI WAKATI UJAO KWA UHAKIKA
Watu wa Yehova nchini Estonia wanatazamia nini wakati ujao? Yehova hajawahi kushindwa kuwaongoza na kuwaimarisha watumishi wake washikamanifu. Kwa kweli, ndugu na dada ambao walidumisha utimilifu walipoteswa na Wanazi na Wasovieti nchini Estonia wameshuhudia utegemezo wa Yehova katika njia za ajabu zisizosahaulika. Wakishirikiana na ndugu na dada zao ulimwenguni pote, wanashangilia kwamba jina kuu la Yehova limetangazwa na kutakaswa hadi sehemu ya mbali sana ya jamhuri zilizokuwa chini ya Muungano wa Sovieti.—Mal. 1:11.
Wakati huohuo, bado kuna watu wengi wanyenyekevu na wanyofu nchini Estonia ambao wanataka kujifunza kuhusu Mungu wa kweli. Uhuru wa kidini uliopo sasa unawawezesha Mashahidi wa Yehova kutangaza hata zaidi habari njema za Ufalme wa Yehova.
[Maelezo ya Chini]
a Simulizi la maisha yake linapatikana katika ukurasa wa 373-376 wa gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1963 la Kiingereza.
b Hukumu zilizotolewa na hali katika magereza na kambi zimeelezwa katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2002, ukurasa wa 157 cha Kiingereza.
c Gazeti la Amkeni! la Februari 22, 1986 linaeleza sababu iliyofanya Ndugu Edur aache mchezo wa magongo na jinsi alivyofanya hivyo.
[Blabu katika ukurasa wa 172]
“Sikukosa chochote muhimu”
[Blabu katika ukurasa wa 204]
“Hali ilikuwa nzuri nilipotengwa na wengine”
[Sanduku katika ukurasa wa 168]
Maelezo Mafupi Kuhusu Estonia
Nchi
Estonia ni nchi maridadi, yenye watu wachache na misitu mikubwa yenye miti mirefu. Pia ina maziwa zaidi ya 1,400, mito na vijito karibu 7,000, na maeneo yenye majimaji yasiyoweza kukaa watu. Estonia ina visiwa zaidi ya 1,500 ambavyo vinafanyiza asilimia kumi ya nchi nzima. Sehemu kubwa ya nchi hiyo ni tambarare na haizidi mita 50 juu ya usawa wa bahari. Eneo la kusini-mashariki lina vilima-vilima maridadi.
Watu
Asilimia 68 ya watu wanaoishi nchini humo ni Waestonia, na asilimia 26 ni Warusi, na idadi inayobaki inatia ndani hasa Waukrainia, Wabelarusi, na Wafini. Dini zinazopatikana Estonia zinatia ndani dini ya Lutheri, Othodoksi, na dini nyingine zinazodai kuwa za Kikristo. Pia kuna Uislamu na dini ya Kiyahudi. Idadi kubwa ya watu hawashirikiani na dini yoyote.
Lugha
Lugha rasmi ni Kiestonia. Lugha hii iko katika kikundi kimoja na Kifini na Kihungaria. Watu wanaoongea Kirusi ni zaidi ya robo ya idadi ya watu kote nchini.
Chakula
Vyakula vinavyopendwa sana ni Leib (mkate mweusi), viazi, maboga yaliyotiwa siki, saladi ya kiazi sukari, na kabichi iliyochachishwa kwa chumvi. Vyakula vingine vinavyopendwa ni sült (nyama ya ndama iliyotayarishwa kwa jeli), rosolje (samaki aina ya heringi na viazi sukari), supu ya uyoga wa mwituni, nyama ya nguruwe, samaki, na nyama zilizokaushwa. Kitindamlo kinatia ndani kringel—aina ya mkate mtamu ulionyunyiziwa zabibu na njugu—na chapati za maji.
Hali ya hewa
Majira ya kiangazi hayana joto sana, nayo majira ya baridi hayana baridi kali. Wakati wa kiangazi, siku iliyo ndefu zaidi inakuwa na mwangaza wa jua kwa zaidi ya saa 19, na katika siku iliyo fupi zaidi, wakati wa majira ya baridi kali, jua huangaza kwa saa 6 tu. Ingawa maeneo ya pwani ya kusini-magharibi yanaweza kuwa na hali ya hewa yenye kupendeza ya Mediterania wakati wa kiangazi, kiwango cha joto katika majira ya baridi kinaweza kushuka hadi Selsiasi 20 chini ya sufuri.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 183, 184]
“Tulikuwa Kama Familia Moja”
ADOLF KOSE
ALIZALIWA 1920
ALIBATIZWA 1944
ALIKUFA 2004
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alifungwa katika kambi huko Siberia kuanzia mwaka wa 1951 hadi 1956. Alisaidia kupanga kazi ya kuhubiri katika nchi za Baltiki na maeneo ya kaskazini-magharibi ya Muungano wa Sovieti.
◼ ADOLF anasema, “Nilikamatwa mwaka wa 1950, na kupelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu iliyokuwa katika mji wa Inta, Siberia. Kwa mwaka mmoja na nusu, sikupata habari yoyote kumhusu mke na binti zangu wawili wadogo, ambao walikuwa wamepelekwa uhamishoni katika sehemu nyingine ya Siberia.
“Akina ndugu walikuwa na umoja wa kipekee. Tulikuwa kama familia moja. Tuligawana chakula cha kimwili na hata cha kiroho.
“Tuliporudi Estonia, tulikabili matatizo mengi. Tungewasiliana jinsi gani na ‘Mama,’ yaani, tengenezo letu? Tungedumisha umoja kati ya akina ndugu jinsi gani? Tungeendeleza kazi ya kuhubiri jinsi gani?
“Ili niweze kuwasiliana vizuri na wajumbe wa kusafirisha vitabu na barua, nilitaka kujifunza Kifini. Haikuwa rahisi kufanya hivyo kwa sababu hakukuwa na vitabu vya lugha wala kamusi zilizokuwa zinauzwa.
“Kuhusu uchapaji, ilikuwa hatia kuwa na taipureta isiyosajiliwa au kifaa cha kuchapia. Mtu yeyote aliyechapa vitabu vilivyopigwa marufuku, angefungwa kwa miaka saba. Pia, hiyo ilikuwa kazi ngumu kwa sababu haikuwa rahisi kupata vifaa vilivyohitajika. Baada ya kujaribu mbinu mbalimbali, mwishowe nilifaulu kubuni mbinu fulani ya uchapaji. Kwanza, nilitengeneza mashini ya kuchapia (ona picha chini). Kisha nikaitumia kuchapa maneno kwenye kitambaa chenye nta tulichotengeneza wenyewe. Nilipochapa, mashini hiyo ilitokeza mashimo kwenye nta. Tulichapa machapisho ya kwanza kwa wino uliotengenezwa kwa masizi na lami. Wakati wa kuchapa, wino huo wa kujitengenezea ulitiririka kupitia yale mashimo, na kisha kuacha maandishi kwenye karatasi iliyowekwa chini ya kile kitambaa chenye nta. Kazi hiyo ilikuwa ngumu, ilichukua wakati mwingi, na ingeweza kudhuru afya kwa sababu ya mvuke uliotokana na wino huo na kemikali nyingine hatari. Vyumba tulivyotumia havikuwa na hewa ya kutosha kwa sababu tulifunga madirisha yote ili kufanya kazi hiyo kwa siri.”
Hata wakati huo mgumu, Adolf alifuata kwa ujasiri miongozo yote iliyotolewa na tengenezo, nyakati zote akiwa na hakika kwamba Yehova atatoa majibu kwa wakati unaofaa. Alimtumikia Yehova akiwa na mtazamo na imani ileile, bila kuyumbayumba, hadi alipokufa mwaka wa 2004.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 186]
Barua kwa Stalin
Mnamo Juni 1949, ndugu waliokuwa wakisimamia kazi nchini Estonia waliandika barua kwa ujasiri wakazituma Moscow. Barua moja ilitumwa kwa Joseph Stalin, na nyingine kwa Nikolay Shvernik, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Muungano wa Jamhuri za Kisoshalisti za Sovieti.
Katika barua hizo ndugu waliomba Mashahidi wote wa Yehova waliokuwa wamekamatwa waachiliwe na mara moja mateso dhidi yao yasimamishwe. Barua hizo pia zilikuwa na onyo kali lililomlinganisha Stalin na Farao wa Misri ya kale aliyekataa kuwaruhusu Waisraeli waende kumtumikia Yehova kwa uhuru. (Kut. 5:1-4) Ndugu hao walisema hivi kwa ujasiri: “Tengenezo la Yehova Mungu . . . linapaswa kuruhusiwa kuwahubiria habari njema za Ufalme wa Yehova watu wote wanaoishi katika nchi zilizo katika Muungano wa Sovieti bila vizuizi vyovyote, la sivyo, Yehova ataangamiza kabisa Muungano huo na Chama cha Kikomunisti.”
“Tulitambua kuwa ulikuwa ujumbe wa kijasiri sana,” anasema Adolf Kose. “Hatukutaka kutuma barua hizo kutoka Tallinn, kwa kuwa tungeweza kugunduliwa. Hivyo, tukasafiri hadi Leningrad (St. Petersburg) ili kuzituma kutoka huko.”
Haijulikani kama Stalin mwenyewe alisoma barua hiyo, lakini hakuna shaka kwamba iliwafikia wenye mamlaka fulani. Ndugu fulani walipokuwa wakihojiwa, walionyeshwa nakala ya barua hiyo na ilikuwa imeandikwa: “Tengenezo hili lazima liangamizwe!” Muda si muda, ndugu walikamatwa na mateso yakaongezeka. Barua aliyotumiwa Shvernik inapatikana katika hifadhi ya nyaraka za kitaifa ikiwa na muhuri wa serikali.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 189]
Shirika la KGB na Tengenezo Letu
Mwishoni mwa miaka ya 1940, polisi wa siri walijitahidi sana kujua jinsi kazi ya Mashahidi wa Yehova ilivyopangwa. Watu fulani walijifanya kuwa wanapendezwa na kweli ili waweze kupata habari kwa ajili ya KGB. Chati hii, iliyopatikana katika jumba la kuhifadhi hati za serikali lililo Tallinn, inaonyesha kuwa KGB walikuwa na habari nyingi. Inatia ndani majina ya akina ndugu katika Halmashauri ya Utumishi, ndugu waliosimamia kazi katika majiji ya Estonia, na wale waliohusika katika kazi ya uchapaji.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 191]
Wapinzani Hawakuweza Kumnyamazisha
ELLA TOOM
ALIZALIWA 1926
ALIBATIZWA 1946
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alifungwa gerezani kwa jumla ya miaka 13 lakini akaachiliwa baada ya miaka 5 na miezi 6.
◼ ELLA anasema, “Wenye mamlaka waliniweka katika kifungo cha upweke kwa siku tatu ili kunilazimisha nikane imani yangu, na hivyo kuacha kuzungumza na watu kuhusu serikali ya Mungu, au mimi mwenyewe niache kuiamini. Maofisa hao walisema hivi kwa sauti kubwa: ‘Tutafanya yote tuwezayo kuhakikisha kwamba jina la Yehova halikumbukwi tena hapa Estonia! Utaenda kwenye kambi na wengine wataenda Siberia!’ Waliongeza kusema hivi kwa dharau: ‘Yehova wako yuko wapi?’ Nilikataa kuwa msaliti. Afadhali kuwa katika kambi pamoja na Mungu kuliko kuwa nyumbani bila Mungu. Hata nilipokuwa kambini, sikujiona kama mfungwa. Nilihisi kuwa Yehova aliruhusu nipelekwe huko ili nihubiri katika eneo hilo jipya.
“Katika kambi moja, nilikuwa nikienda matembezi kila siku na mtu fulani mwenye kupendezwa. Kisha siku moja tukaamua tusiende. Baadaye niligundua kuwa watu fulani wa dini wenye imani kali walipanga kunizamisha mtoni kwa sababu ya kazi yangu ya kuhubiri.” Wapinzani hawakuweza kumnyamazisha Ella na bado anamtumikia Yehova kwa uaminifu akiwa painia wa kawaida.d
[Maelezo ya Chini]
d Simulizi la maisha la Ella Toom linapatikana katika gazeti la Amkeni! la Aprili 2006 ukurasa wa 20-24.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 193, 194]
“Yehova, Mapenzi Yako na Yatendeke”
LEMBIT TOOM
ALIZALIWA 1924
ALIBATIZWA 1944
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Aliishi Estonia wakati Wajerumani walipoiteka nchi hiyo, kisha akapelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu huko Siberia kuanzia mwaka wa 1951 hadi 1956.
◼ LEMBIT alikuwa mmoja kati ya vijana wengi Mashahidi wa Yehova waliokataa kujiunga na jeshi la Ujerumani na hivyo akahitaji kujificha. Usiku mmoja maafisa wa polisi walivamia nyumba ambapo Lembit alikuwa akikaa. Walikuwa wamepata malalamiko kuwa kuna mtu wanayemtilia shaka ambaye anajificha katika shamba hilo. Lembit alificha kitanda chake mara moja na kutambaa akiwa nusu uchi na kujificha katika nafasi iliyokuwa kati ya msingi wa nyumba hiyo na sakafu ya mbao. Aliwasikia askari wakitembeatembea kwa kishindo kwenye sakafu juu tu ya kichwa chake.
Askari walimwelekezea bastola mwenye shamba hilo na kumwambia kwa sauti: “Kuna mtu anayejificha katika nyumba hii. Tunaweza kuingiaje chini ya sakafu?” Mtu huyo alinyamaza tu.
Askari huyo aliongeza kusema hivi kwa sauti: “Ikiwa mtu aliyejificha chini ya sakafu hatatoka, tutarusha gruneti humo!”
Kisha Lembit akaona mwangaza wa tochi zao walipokuwa wakijaribu kuchungulia chini. Lembit angeweza tu kusali, “Yehova, mapenzi yako na yatendeke.”
Lembit anasema: “Nilikuwa na mkazo mwingi sana wa akili, na nilitambaa hadi sehemu nyingine chini ya sakafu, nikiwa karibu kujisalimisha.”
Kisha, akalala chini na kutulia, na baada ya dakika chache zenye mkazo mwingi, polisi hao wakaondoka. Lembit alisubiri mahali alipokuwa kwa muda wa saa moja hivi ili kuhakikisha kuwa askari hao wameondoka kabisa. Kisha kabla ya mapambazuko, akaondoka katika nyumba hiyo ili kutafuta mahali pengine pa kujificha.
Wasovieti walipoiteka Estonia, Lembit alipata majaribu mengine. “Nilifungwa kwa miaka kumi katika kambi ya kazi ngumu huko Noril’sk, Siberia, umbali wa kilomita 8,000 kutoka Estonia. Kambini nilifanya kazi ngumu ya kuchimba madini ya nikeli. Maisha katika kambi hizo yalikuwa ya hali ya chini, na kazi ilikuwa yenye kuchosha sana. Katika eneo la kaskazini la Muungano wa Sovieti, juu ya Mzingo Aktiki, maisha ni magumu sana wakati wa majira ya baridi kali. Joto linaweza kupungua hadi Selsiasi 30 chini ya sufuri au hata chini zaidi. Kwa miezi miwili katika majira ya baridi kali, jua halichomozi.”
Baada ya miaka mitano ya kufanya kazi kama mtumwa, Lembit aliachiliwa huru, na katika mwaka wa 1957 akamwoa Ella Kikas. Kwa miaka mingi, Lembit amekuwa akisaidia katika kazi ya kutafsiri na kuchapa vitabu. Anafahamika kama mzee mwenye huruma, upendo, na ambaye sikuzote huwa tayari kutumia andiko fulani kuwaimarisha watumishi wenzake.e
[Maelezo ya Chini]
e Simulizi la maisha la Lembit Toom lilisimuliwa katika gazeti la Amkeni! la Februari 22, 1999, ukurasa wa 10-16.
[Picha]
Lembit na Ella Toom
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 199]
“Ni Mama Yako”
KARIN REILE
ALIZALIWA 1950
ALIBATIZWA 1965
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alizaliwa mama yake akiwa gerezani, lakini nyanya yake akamchukua na kumlea.
◼ “NILIZALIWA mama yangu, Maimu, akiwa gerezani kwa sababu ya shughuli zake za kisiasa,” anasema Karin. “Nilikuwa mtoto dhaifu, na kwa sababu ya baridi iliyokuwa gerezani, nilipatwa na nimonia iliyoathiri mapafu yangu mawili. Lakini sikufa kwa sababu nilisaidiwa na mfungwa mwingine, Laine Prööme, ambaye baadaye alijifunza Biblia.
“Wakati huo, watoto wa wafungwa wengi walipelekwa katika makao ya mayatima kotekote katika Muungano wa Sovieti ili wawasahau wazazi wao. Lakini mimi nilipelekwa kwa nyanya yangu. Mama yangu alipelekwa katika kambi ya wafungwa huko Mordvinia ambako alikutana na Ella Toom, dada mwenye ujasiri. Mama yangu alikubali kweli na akabatizwa akiwa huko.
“Kwa miaka mitano iliyofuata nililelewa na nyanya yangu. Siku moja bila kutazamia, mwanamke fulani nisiyemjua alikuja nyumbani kwetu. ‘Ni mama yako,’ nyanya yangu akaniambia. Nilichanganyikiwa sana, na ilinichukua miaka kadhaa kukubali hali hiyo.” Inafurahisha kwamba Karin na nyanya yake walikubali kweli pia.
Baadaye Karin alijifunza Kiingereza na akaanza kusaidia kutafsiri vitabu vyetu. Aliolewa na Lembit Reile, na sasa wanatumika pamoja katika ofisi ya tawi ya Estonia.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 201]
Jina la Mungu Katika Biblia ya Kiestonia
Katika mwaka wa 1686, Maandiko ya Kigiriki yalitafsiriwa katika lahaja ya watu wanaoishi kusini mwa Estonia na katika mwaka wa 1715 yakatafsiriwa katika lahaja ya watu wanaoishi kaskazini. Biblia nzima, Piibli Ramat, iliyochapishwa mwaka wa 1739, ilipatikana kwa urahisi kwa watu wa kawaida. Ilikuwa ya kipekee kwa sababu ilitumia jina la Mungu, Yehova, kila mahali ambapo jina hilo linapatikana katika Maandiko ya Kiebrania. Katika karne nyingi zilizofuata, jina hilo liliendelea kupatikana katika sehemu hizo za Biblia. Chapa ya mwaka wa 1988 ya Biblia ya Kiestonia inatumia jina la Mungu mara 6,867 katika Maandiko ya Kiebrania. Hivyo, Waestonia wengi wanajua kuwa jina la Mungu ni Yehova.
Hatua muhimu ilifikiwa Julai 3, 2009, katika kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova jijini Tartu, Estonia, wakati Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alipotangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kiestonia.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 202]
Vitabu Vilivyotengenezwa kwa Mikono
HELMI LEEK
ALIZALIWA 1908
ALIBATIZWA 1945
ALIKUFA 1998
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alifungwa na kupelekwa Siberia.
◼ HELMI alikamatwa kama mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kupelekwa Siberia, ambako alitengeneza kibeti kidogo cha kuwekea kijitabu cha kuandikia. Alishona kwenye kibeti hicho andiko lenye kutia moyo—Waroma 8:35: “Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je, ni dhiki au taabu au mateso au njaa au uchi au hatari au upanga?”
Helmi alipata vipande vya karatasi za rangi ya kahawia na kuzitumia kutengeneza kitabu. Aliandika maandiko yenye kutia moyo katika kitabu hicho. Ndugu wengi waliandika vitabu vizima-vizima kwa mkono, kwa kuwa vitabu vilivyochapwa havikuwa vingi.
Baada ya kurudi kutoka Siberia, Helmi aliwaambia maofisa hivi: “Ninawashukuru kwa kuwa mlinipeleka kuona milima yenye kupendeza ya Siberia—singeweza kupata pesa za kusafiri hadi huko!”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 209, 210]
Roho ya Kujidhabihu
FANNY HIETALA
ALIZALIWA 1900
ALIBATIZWA 1925
ALIKUFA 1995
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alihamia Estonia mwaka wa 1930, akawa painia, na kumlea mtoto yatima ambaye wazazi wake walikuwa Mashahidi.
◼ FANNY alibatizwa nchini Finland mwaka wa 1925 na kuanza utumishi wa wakati wote miaka miwili baadaye. Kwenye kusanyiko moja huko Helsinki, alikutana na William Dey, msimamizi wa Ofisi ya Ulaya Kaskazini. Ingawa walizungumza lugha tofauti, alimsikia Ndugu Dey akirudia-rudia neno “Estonia.” Alikisia kwamba ndugu huyo alitaka ahamie katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri, kwa hiyo, Fanny na mapainia wengine wakahamia Estonia mwaka wa 1930. Katika miaka iliyofuata, alitumia baiskeli yake kuhubiri habari njema katika majimbo kadhaa nchini Estonia, kutia ndani kisiwa cha Sarema.
Fanny hakuwahi kuolewa, lakini alimchukua na kumlea msichana yatima aliyeitwa Ester, ambaye wazazi wake walikufa akiwa na miaka minane. Baba ya msichana huyo alikuwa Shahidi. Fanny alimtunza kwa upendo na hatimaye Ester akawa Shahidi.
Wakomunisti walipoanza kuitawala Estonia, na mateso yakaanza, Fanny angeweza kurudi kwao Finland. Hata hivyo, alionyesha roho ya kujidhabihu kwa kutokiacha kikundi kidogo cha wahubiri wenyeji. Kwa sababu ya kuamua kubaki Estonia, Fanny alivumilia matatizo mengi na hali ya maisha ilikuwa mbaya. Hata hivyo, kwa kuwa alikuwa raia wa Finland, hakupelekwa uhamishoni Siberia.
Katika miaka ya 1950, Fanny alitumika kama mjumbe na alibeba barua na mikanda ya filamu yenye maandishi madogo kutoka Finland hadi Estonia. Alikuwa mwenye ujasiri na busara, na ingawa nyakati nyingi hali zilikuwa zenye kufadhaisha, hakuwahi kukamatwa. Kwa mfano, wakati mmoja alisafiri hadi Leningrad (St. Petersburg) kuchukua kifurushi cha mikanda ya filamu kilichokuwa kimeletwa na ndugu wa Finland. Alikuwa akutane naye katika bustani fulani. Fanny naye, alipaswa kupitisha kifurushi hicho haraka iwezekanavyo kwa ndugu wawili Waestonia. Hata hivyo, ndugu hao Waestonia walikuwa wamegundua kwamba wanafuatwa na polisi wa siri na hivyo wakajaribu kuondoka bila Fanny kuwaona. Lakini wapi! Fanny na yule ndugu wa Finland walitembea moja kwa moja wakielekea mahali ndugu hao walipokuwa. Kama Fanny angewasalimu au kujaribu kuwapa kile kifurushi, polisi hao wa siri wangejua mipango yao. Kwa kushangaza, Fanny aliwapita ndugu hao kana kwamba hakuwajua. Baadaye, waligundua kwamba Fanny hakuwaona, ingawa aliwajua vizuri sana! Kwa hiyo, polisi hao wa siri hakuweza kuwatambua wajumbe hao na baadaye ndugu Waestonia waliweza kupata kile kifurushi. Akiwa mjumbe, Fanny aliwasaidia akina ndugu nchini Estonia kupata chakula cha kiroho kwa ukawaida, na hakuna mikanda yoyote ya filamu ambayo polisi waliipata.
Dada huyu mwenye shauku alimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka 70 hadi alipokufa akiwa na umri wa miaka 95 na akiwa bado anaishi Estonia.
[Picha]
Kusafirisha chakula cha kiroho jijini Leningrad, 1966
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 213]
Watu Wanaosemwa Vibaya
Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu.” (Mt. 5:11) Kama vile Bwana wao alivyosema, Mashahidi wa Yehova wamekuwa watu wanaosemwa vibaya kwa chuki. Mashahidi walishutumiwa kwa uwongo kuwa tengenezo la kisiasa lililojihusisha na mambo ya kutaka kuipindua serikali na kufanya upelelezi. Hasa mwishoni mwa miaka ya 1950 na mwanzoni mwa miaka ya 1960, magazeti yalidai kuwa kazi yetu ilikuwa ikiongozwa na serikali ya Marekani na kwamba matajiri wa Marekani walikuwa wakitutumia ili kujinufaisha.
Silver Silliksaar alipokataa kujiunga na jeshi mwaka wa 1964, alishtakiwa kuwa msaliti wa nchi yake na kufungwa gerezani. Pia, sinema fupi kuhusu kesi yake, ambayo Wakomunisti waliongeza propaganda yao yenye kiburi, ilionyeshwa katika kumbi zote za sinema huko Estonia. Ndugu wengi waliokataa kujiunga na jeshi walifungwa miaka miwili au mitatu gerezani. Jüri Schönberg, Taavi Kuusk, na Artur Mikit walifungwa mara mbili kila mmoja—Ndugu Mikit alifungwa kwa jumla ya miaka mitano na nusu.
[Picha katika ukurasa wa 213]
Silver Silliksaar akiwa mahakamani kwa sababu ya imani yake
[Sanduku katika ukurasa wa 226]
Shule ya Huduma ya Kitheokrasi Yafanywa Kisiri
Wakati wa marufuku, ndugu hawakujua wangeweza kuwa na vitabu au Biblia kwa muda gani. Kwa hiyo, kando na kuwa na sehemu mbalimbali za kuficha vitabu hivyo, walijaribu kuweka akilini maandiko mengi iwezekanavyo.
Ndugu walipokusanyika kwa ajili ya tafrija, walitumia wakati huo kuzungumzia maandiko ya Biblia na kujaribu kuyaweka akilini. Wengine walitengeneza kadi ndogo zilizowasaidia kukumbuka maandiko hayo. Upande mmoja wa kadi hiyo ulikuwa na sura na mstari fulani wa Biblia, kama vile Mathayo 24:14, au swali fulani au jina la kitabu cha Biblia. Upande ule mwingine wa kadi hiyo waliandika maneno ya mstari huo au jibu la swali lililoulizwa.
Ndugu walitumia vitabu vyovyote vinavyotegemea Biblia ambavyo vilipatikana ili kuongoza mikutano. Kwa mfano, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilikuwa na madarasa ya kila juma, kazi za kufanyia nyumbani, maswali na majibu ya papohapo, na hata mitihani. Kulikuwa na pitio baada ya kila miezi mitatu na mtihani wa mwisho uliofanywa wakati wa majira ya kuchipua.
Mmoja wa wanafunzi anasema: “Moja kati ya kazi tulizopewa kila juma kufanyia nyumbani ilikuwa kuweka akilini maandiko matano ya Biblia, ambayo tulipaswa kuyasema bila kusoma, katika darasa lililofuata. Ninakumbuka mtihani wa mwisho mwaka wa 1988. Kulikuwa na kadi moja iliyosema: ‘Weka akilini maandiko 100 na kuyasema bila kusoma.’ Ingawa huenda ikaonekana kuwa jambo lisilo la kawaida, kila mtu alitamani kupata kadi hiyo. Migawo hiyo ilitusaidia hasa wakati wa kuhubiri kwa kuwa tulitumia Biblia hadharani mara chache sana.” Mnamo mwaka wa 1990, makutaniko ya Estonia yalifurahi kwa sababu hatimaye, yangeweza kuwa na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kama ndugu wengine ulimwenguni.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 236, 237]
“Utumishi wa Shambani Ulikuwa Wenye Kupendeza”
Wamishonari fulani wanaeleza mambo waliojionea wakiwa katika mgawo wao nchini Estonia:
Markku na Sirpa Kettula: “Eneo tulilogawiwa kuhubiri lilikuwa halijawahi kuhubiriwa. Utumishi wa shambani ulikuwa wenye kupendeza kwa kuwa watu walipendezwa sana na Biblia. Tulipofika Pärnu, wahubiri walikuwa 30 hivi. Sasa kuna makutaniko matatu.”
Vesa na Leena-Maria Edvik: “Maduka yalikuwa na bidhaa chache sana. Hivyo, badala ya kwenda madukani, watu walikuwa na wakati mwingi wa kuzungumzia Biblia. Tulipohubiri barabarani, watu walipanga mstari ili kupokea vitabu!”
Esa na Jaael Nissinen: “Unaweza kujifunza mambo mengi kutoka kwa watu wengine. Limekuwa pendeleo kuwajua wengi kati ya ndugu walioendelea kuwa waaminifu hata wakati wa majaribu makali.”
Anne na Ilkka Leinonen: “Siku baada ya siku, juma baada ya juma, eneo baada ya eneo, tulikutana na watu ambao hawajawahi kusikia ujumbe wa Biblia. Tulianza kuhubiri asubuhi na mapema hadi jioni sana na tulifurahia sana kuona ongezeko kubwa. Hatukuamini kuwa kufikia mwisho wa karne ya 20, tungekuwa na pendeleo la kuona ongezeko kama hilo. Hatutasahau miaka hiyo ya mapema.”
Richard na Rachel Irgens: “Watu walikuwa wakarimu sana na tulifurahia kuhubiri. Tulihubiri katika vijiji vilivyoko karibu na Ziwa Peipus. Hatukubeba chakula chochote kwa kuwa wenye nyumba walitukaribisha na kutupa chakula. Tuliona kuwa shauri la Yesu katika Mathayo 10:9, 10 linaweza kutumika hata sasa. Kuishi nchini Estonia kulitusaidia kujifunza umuhimu wa kukazia fikira mambo yaliyo muhimu na kutokengeushwa na yale yasiyo muhimu.”
[Picha]
Markku na Sirpa Kettula
Vesa na Leena-Maria Edvik
Anne na Ilkka Leinonen
Esa na Jaael Nissinen
Richard na Rachel Irgens
[Chati/Picha katika ukurasa wa 244, 245]
MFUATANO WA MATUKIO—Estonia
1920
1923 Martin Kose arudi Estonia ili kuhubiri.
1926 Ofisi ya tawi yafunguliwa jijini Tallinn.
Makolpota wa kigeni wawasili ili kusaidia katika kazi ya kuhubiri.
1928 Kusanyiko la kwanza lafanywa kwenye ofisi ya tawi.
1930
1933 Shirika la Watch Tower Bible and Tract Society laandikishwa kisheria.
1940
1940 Ndugu wa Estonia wafurahia kusanyiko la mwisho lililofanywa kwa uhuru, lakini kwa miaka 50 iliyofuata hawakuweza kukusanyika tena kwa uhuru.
1948 Mashahidi fulani wapelekwa gerezani na kwenye kambi za wafungwa katika Muungano wa Sovieti.
1949 Mashahidi wamwandikia Stalin barua ya malalamiko.
1950
1951 Mashahidi 300 hivi pamoja na wengi wa watu wao wa ukoo wapelekwa uhamishoni nchini Siberia.
1953 Stalin afa; Mashahidi waanza kuachiliwa huru.
1960
1970
1972 Kutaniko la kwanza la lugha ya Kirusi laanzishwa.
1980
1990
1991 Ofisi ya tafsiri yaanzishwa jijini Tartu.
Mashahidi wa Yehova wapata uhuru wa ibada.
Kusanyiko la kwanza kabisa katika Muungano wa Sovieti lafanywa jijini Tallinn.
1992 Wamishonari wa kwanza wa Gileadi wafika.
1993 Jumba la kwanza la Ufalme nchini Estonia lajengwa.
1994 Ofisi ya tafsiri yaanzishwa Tallinn.
1998 Majumba ya Kusanyiko yajengwa jijini Tallinn na Tartu.
1999 Estonia yawa na ofisi ya tawi tena.
2000
2000 Darasa la kwanza la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma lafanywa.
2009 Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yatangazwa nchini Estonia.
2010
[Grafu/Picha katika ukurasa wa 246]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Jumla ya Wahubiri
Jumla ya Mapainia
4,000
2,000
1990 2000 2010
[Ramani katika ukurasa wa 169]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
FINLAND
HELSINKI
Ghuba ya Finland
URUSI
St. Petersburg
LATVIA
RIGA
ESTONIA
TALLINN
Narva
Maardu
Tapa
Vormsi
Pärnu
Ziwa Võrtsjärv
Tartu
Räpina
Võru
Hiiumaa
Sarema
Ghuba ya Riga
Ziwa Peipus
Ziwa Pskov
[Picha katika ukurasa wa 162]
[Picha katika ukurasa wa 165]
Hugo na Martin Kose
[Picha katika ukurasa wa 166]
Albert West
[Picha katika ukurasa wa 167]
Ofisi ya tawi ya kwanza ilikuwa kwenye jengo hili
[Picha katika ukurasa wa 167]
Alexander na Hilda Brydson, miaka ya 1930
[Picha katika ukurasa wa 170]
Mapainia wa kwanza kutoka Finland, Jenny Felt na Irja Mäkelä
[Picha katika ukurasa wa 174]
Ofisi ya tawi ilihamishiwa kwenye Barabara ya 72 Suur Tartu, Tallinn, mwaka wa 1932
[Picha katika ukurasa wa 175]
Kaarlo Harteva akitoa hotuba kupitia redio
[Picha katika ukurasa wa 177]
John North na ‘gari lake la vita’
[Picha katika ukurasa wa 178]
Nikolai Tuiman
[Picha katika ukurasa wa 179]
Polisi walitwaa vitabu vingi sana
[Picha katika ukurasa wa 181]
1940: Kusanyiko la mwisho lililofanywa kabla ya utawala wa Sovieti
[Picha katika ukurasa wa 188]
Ndugu Kruus, Talberg, Indus, na Toom walikuwa katika Halmashauri ya Utumishi
[Picha katika ukurasa wa 200]
Maimu na Lembit Trell, 1957
[Picha katika ukurasa wa 212]
Ene na dada yake Corinna
[Picha katika ukurasa wa 218]
Sherehe ya harusi ya Heimar na Elvi Tuiman—kusanyiko lililofanywa kwa siku mbili
[Picha katika ukurasa wa 227]
Toomas na Elizabeth Edur
[Picha katika ukurasa wa 228, 229]
Makusanyiko ya Kukumbukwa
Wajumbe wakaribishwa kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Lugha Iliyo Safi” mjini Helsinki, Finland, mwaka wa 1990
Kusanyiko la Wilaya la “Wapendao Uhuru,” jijini Tallinn, Estonia, mwaka wa 1991
[Picha katika ukurasa wa 238]
Kusanyiko la kimataifa jijini St. Petersburg, Urusi, mwaka wa 1992
[Picha katika ukurasa wa 241]
Lauri na Jelena Nordling
[Picha katika ukurasa wa 243]
Reino na Lesli Kesk
[Picha katika ukurasa wa 247]
Yuri na Viktor
[Picha katika ukurasa wa 251]
Jumba la Ufalme la Maardu, na Jumba la Kusanyiko la Tartu
[Picha katika ukurasa wa 254]
Ofisi ya Tawi ya Estonia
Halmashauri ya Tawi, kuanzia kushoto hadi kulia: Tommi Kauko, Toomas Edur, na Lembit Reile