Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bt sura 15 kur. 117-123
  • “Kuyaimarisha Makutaniko”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kuyaimarisha Makutaniko”
  • “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Turudi Tukawatembelee Akina Ndugu” (Mdo. 15:36)
  • “Wakagombana kwa Ukali” (Mdo. 15:37-41)
  • “Alishuhudiwa Vema” (Mdo. 16:1-3)
  • “Kuimarishwa Katika Imani” (Mdo. 16:4, 5)
  • “Mtoto Wangu Mpendwa na Mwaminifu Katika Bwana”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Timotheo—Alikuwa Tayari na Mwenye Nia ya Kutumikia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Marko ‘Mwenye Faida kwa Ajili ya Huduma’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Timotheo—“Mtoto Halisi Katika Imani”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
bt sura 15 kur. 117-123

SURA YA 15

‘Kuyaimarisha Makutaniko’

Waangalizi wa mzunguko huyasaidia makutaniko yawe na imani yenye nguvu

Matendo 15:36–16:5

1-3. (a) Paulo anasafiri na nani, na mwandamani huyo ni mtu wa aina gani? (b) Tutajifunza nini katika sura hii?

WANAPOVUKA milima na mabonde kutoka mji mmoja hadi mwingine, mtume Paulo anamfikiria kijana anayesafiri pamoja naye. Kijana huyo ni Timotheo mwenye umri wa miaka 20 hivi. Kadiri kijana huyo anavyotembea katika safari hii ndivyo anavyokuwa mbali zaidi na nyumbani kwao. Kadiri siku inavyopita, ndivyo wanavyozidi kuwa mbali na majiji ya Listra na Ikoniamu. Ni mambo gani yatakayotokea? Huenda Paulo alijua kwa sababu hii ni safari yake ya pili ya umishonari. Anajua kwamba kutakuwa na hatari na matatizo mengi. Timotheo atatendaje atakapokabili hali hizo?

2 Paulo anamwamini Timotheo, labda kuliko Timotheo anavyojiamini. Matukio ya karibuni yalimfanya Paulo aone umuhimu wa kuchagua mwandamani anayefaa. Paulo anajua kwamba kazi ya kutembelea makutaniko na kuyatia nguvu, inahitaji waangalizi walio thabiti na wenye nia moja. Kwa nini? Huenda sababu moja ni kutoelewana kati ya Paulo na Barnaba kulikosababisha mgawanyiko.

3 Katika sura hii tutajifunza mengi kuhusu njia bora ya kutatua kutoelewana. Pia, tutajua ni kwa nini Paulo alichagua kusafiri na Timotheo, nasi tutajifunza mengi kuhusu kazi muhimu inayotimizwa na waangalizi wa mzunguko.

“Turudi Tukawatembelee Akina Ndugu” (Mdo. 15:36)

4. Paulo alikusudia kufanya nini katika safari yake ya pili ya umishonari?

4 Katika sura iliyotangulia tuliona jinsi ndugu wanne, Paulo, Barnaba, Yuda, na Sila, walivyolitia nguvu kutaniko la Antiokia kwa kulijulisha uamuzi wa baraza linaloongoza kuhusu suala la tohara. Paulo alifanya nini baadaye? Alimwendea Barnaba akiwa na mikakati mipya ya safari, akamwambia: “Turudi tukawatembelee akina ndugu katika kila jiji ambalo tulitangaza neno la Yehova tuone jinsi wanavyoendelea.” (Mdo. 15:36) Paulo hakuwa akipendekeza wawatembelee Wakristo hao wapya kirafiki tu. Kitabu cha Matendo kinaonyesha wazi kusudi halisi la safari ya pili ya umishonari ya Paulo. Kwanza, kuyajulisha makutaniko maagizo yaliyotolewa na baraza linaloongoza. (Mdo. 16:4) Pili, akiwa mwangalizi wa mzunguko, Paulo alikuwa ameazimia kuyajenga makutaniko kiroho, na kusaidia kuimarisha imani yao. (Rom. 1:11, 12) Tengenezo la Mashahidi wa Yehova linafanyaje hivyo leo?

5. Baraza Linaloongoza huwasiliana na makutaniko na kuyatia moyo jinsi gani?

5 Leo, Kristo anatumia Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova kuongoza kutaniko lake. Kupitia barua, machapisho ya mtandaoni na yaliyochapishwa, mikutano, na njia nyingine, ndugu hao watiwa-mafuta huyaongoza na kuyatia moyo makutaniko ulimwenguni pote. Pia, Baraza Linaloongoza hujitahidi kudumisha mawasiliano pamoja na kila kutaniko. Ili kufanya hivyo, wanatumia waangalizi wa mzunguko. Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi maelfu ya wazee wanaostahili ulimwenguni pote kuwa waangalizi wa mzunguko.

6, 7. Waangalizi wa mzunguko wana majukumu gani?

6 Waangalizi wa mzunguko leo huwahangaikia na kuwatia moyo wote katika makutaniko wanayotembelea. Jinsi gani? Kwa kufuata kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza kama Paulo. Alimhimiza hivi mwangalizi mwenzake: “Lihubiri neno; fanya hivyo kwa uharaka katika nyakati zinazofaa na nyakati ngumu; karipia, kemea, himiza, kwa subira yote na ustadi wa kufundisha. . . . Fanya kazi ya mweneza-injili.”​—2 Tim. 4:2, 5.

7 Waangalizi wa mzunguko—pamoja na wake zao ikiwa wameoa—hutii maneno hayo kwa kushiriki katika huduma ya shambani pamoja na wahubiri wa kutaniko wanalotembelea. Kwa sababu wao ni walimu stadi, na wanapenda huduma, mfano wao unawachochea ndugu na dada. (Rom. 12:11; 2 Tim. 2:15) Waangalizi wa mzunguko huonyesha upendo usio na ubinafsi na kujidhabihu. Huwatumikia wengine kwa hiari, nyakati nyingine wanasafiri wakati ambapo kuna hali mbaya ya hewa na hata katika maeneo yenye hatari. (Flp. 2:3, 4) Pia, waangalizi wa mzunguko hutia moyo, hufundisha, na kuonya makutaniko kupitia hotuba zinazotegemea Biblia. Ni vizuri kwa wote kutanikoni kutafakari mfano mzuri wa waangalizi hao na kujitahidi kuiga imani yao.​—Ebr. 13:7.

“Wakagombana kwa Ukali” (Mdo. 15:37-41)

8. Barnaba aliitikiaje mwaliko wa Paulo?

8 Barnaba alikubali pendekezo la Paulo la ‘kuwatembelea akina ndugu.’ (Mdo. 15:36) Wawili hao walifanya kazi bega kwa bega wakisafiri pamoja, na tayari walijua maeneo na watu waliohitaji kutembelewa. (Mdo. 13:2–14:28) Kwa hiyo, huenda waliona ingefaa wasafiri pamoja kwa ajili ya mgawo huo. Hata hivyo, tatizo likatokea. Andiko la Matendo 15:37 linasema: “Barnaba alikuwa ameazimia kwenda na Yohana, aliyeitwa Marko.” Barnaba hakuwa akitoa pendekezo. “Alikuwa ameazimia” waende pamoja binamu yake, Marko, katika safari hiyo ya umishonari.

9. Kwa nini Paulo na Barnaba hawakuelewana?

9 Paulo hakukubali. Kwa nini? Masimulizi yanasema: “Lakini Paulo hakutaka waende pamoja naye [Marko], kwa sababu alikuwa amewaacha huko Pamfilia na hakuenda pamoja nao kwenye kazi.” (Mdo. 15:38) Marko alikuwa amesafiri pamoja na Paulo na Barnaba katika safari yao ya kwanza ya umishonari lakini hakuendelea na safari hiyo mpaka mwisho. (Mdo. 12:25; 13:13) Mwanzoni katika safari yao ya kwanza, wakiwa Pamfilia, Marko aliuacha mgawo wake na kurudi nyumbani Yerusalemu. Biblia haisemi ni kwa nini aliondoka, lakini inaonekana kwamba mtume Paulo alimwona Marko kuwa mtu asiyechukua mambo kwa uzito. Huenda Paulo alikuwa na mashaka kuhusu kutegemeka kwa Marko.

10. Kutoelewana kati ya Paulo na Barnaba kulisababisha nini, na matokeo yalikuwa nini?

10 Hata hivyo, Barnaba alikuwa ameazimia kwenda na Marko. Na Paulo alikataa kwenda naye. Matendo 15:39 inasema: “Ndipo wakagombana kwa ukali hivi kwamba wakaachana.” Barnaba akapanda meli kuelekea Kipro, kisiwa cha nyumbani kwao, akiwa pamoja na Marko. Naye Paulo akaenda zake. Masimulizi hayo yanasema: “Paulo akamchagua Sila na kuondoka baada ya akina ndugu kumkabidhi kwenye fadhili zisizostahiliwa za Yehova.” (Mdo. 15:40) Wakasafiri pamoja ‘kupitia Siria na Kilikia, wakiyaimarisha makutaniko.’​—Mdo. 15:41.

11. Ni sifa gani zinazohitajiwa ili kudumisha urafiki na mtu aliyetukosea?

11 Huenda masimulizi hayo yakatukumbusha hali yetu ya kutokamilika. Paulo na Barnaba walikuwa wamewekwa rasmi kuwa wawakilishi wa pekee wa baraza linaloongoza. Inaonekana baadaye Paulo aliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa baraza hilo. Hata hivyo, ingawa Paulo na Barnaba walikuwa ndugu wazuri sana, wakati huu walishindwa kudhibiti hasira yao. Je, wangeruhusu hali hiyo ivunje kabisa urafiki wao? Ingawa hawakuwa wakamilifu, Paulo na Barnaba walikuwa wanyenyekevu, na walikuwa na akili ya Kristo. Ndiyo sababu baada ya muda mfupi, walionyesha roho ya undugu wa Kikristo na kusameheana. (Efe. 4:1-3) Baadaye, Paulo na Marko walifanya kazi pamoja katika migawo mingine ya Kikristo.a—Kol. 4:10.

12. Kama Paulo na Barnaba, waangalizi wanapaswa kuwa na sifa gani?

12 Tukio hilo moja halimaanishi kwamba Barnaba na Paulo walikuwa na utu huo. Barnaba alikuwa mwenye upendo na mkarimu sana hivi kwamba badala ya mitume kumwita kwa jina lake, Yosefu, walikuwa wakimwita Barnaba, yaani, “Mwana wa Faraja.” (Mdo. 4:36) Paulo alikuwa mpole na mwenye upendo mwororo. (1 The. 2:7, 8) Waangalizi Wakristo leo, kutia ndani waangalizi wa mzunguko, wanapaswa kujitahidi kuwa wanyenyekevu na kuwatendea wazee wenzao na kundi zima kwa wororo.​—1 Pet. 5:2, 3.

“Alishuhudiwa Vema” (Mdo. 16:1-3)

13, 14. (a) Timotheo alikuwa nani, na alikutana jinsi gani na Paulo? (b) Kwa nini Paulo alipendezwa na Timotheo? (c) Timotheo alipewa mgawo gani?

13 Katika safari yake ya pili ya umishonari, Paulo alienda Galatia, mkoa wa Roma, ambako makutaniko kadhaa yalikuwa yameanzishwa. Mwishowe, “akafika Derbe na pia Listra.” Simulizi hilo linaendelea kusema hivi: “Huko kulikuwa na mwanafunzi aliyeitwa Timotheo, mama yake alikuwa Myahudi aliyekuwa mwamini, lakini baba yake alikuwa Mgiriki.”​—Mdo. 16:1.b

14 Inaonekana kwamba, Paulo alikuwa amekutana na familia ya Timotheo alipotembelea eneo hilo karibu mwaka wa 47 W.K. Baada ya miaka miwili au mitatu hivi, wakati wa safari yake ya pili, Paulo alipendezwa kwa njia ya pekee na kijana Timotheo. Kwa nini? Kwa sababu Timotheo “alishuhudiwa vema na akina ndugu.” Sifa nzuri za Timotheo zilijulikana kutanikoni kwao na hata katika makutaniko mengine. Masimulizi ya Matendo yanasema kwamba akina ndugu wa Listra na Ikoniamu, waliokuwa umbali wa kilomita 30 hivi, walijua sifa nzuri za Timotheo. (Mdo. 16:2) Wakiongozwa na roho takatifu, wazee walimpa kijana Timotheo mgawo mzito wa kusafiri pamoja na Paulo na Sila ili kufanya kazi nao.​—Mdo. 16:3.

15, 16. Timotheo aliwezaje kupata sifa nzuri?

15 Timotheo alipataje sifa nzuri hivyo akiwa kijana? Je, ni kwa sababu alikuwa na akili nyingi, sura nzuri, au vipawa vyake? Mara nyingi wanadamu huvutiwa na mambo kama hayo. Hata nabii Samweli alidanganyika wakati fulani kwa kuangalia mwonekano wa nje. Hata hivyo, Yehova alimkumbusha: “Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona ndani ya moyo.” (1 Sam. 16:7) Timotheo alikuwa na sifa za ndani zilizowavutia Wakristo wenzake.

16 Miaka kadhaa baadaye, mtume Paulo alirejelea sifa fulani za Timotheo. Paulo alitaja mtazamo wake mzuri, upendo wake wa kujidhabihu, na bidii yake katika kushughulikia migawo ya kiroho. (Flp. 2:20-22) Timotheo alijulikana pia kwa kuwa na ‘imani isiyo na unafiki.’​—2 Tim. 1:5.

17. Vijana wanawezaje kumwiga Timotheo?

17 Leo, vijana wengi humwiga Timotheo kwa kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu. Wanajifanyia jina zuri pamoja na Yehova na watu wake, hata wakiwa na umri mdogo. (Met. 22:1; 1 Tim. 4:15) Wanaonyesha imani isiyo na unafiki. (Zab. 26:4) Hivyo, vijana wengi, kama Timotheo, wanaweza kutimiza mengi katika kutaniko. Wanapostahili kuwa wahubiri wa habari njema na hatimaye kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, wao huwatia moyo wote wanaompenda Yehova!

“Kuimarishwa Katika Imani” (Mdo. 16:4, 5)

18. (a) Paulo na Timotheo walilisaidiaje baraza linaloongoza wakiwa wahudumu wanaosafiri? (b) Makutaniko yalipata baraka gani?

18 Paulo na Timotheo walifanya kazi pamoja kwa miaka mingi. Wakiwa wahudumu wanaosafiri, walifanya mambo mbalimbali waliyoagizwa na baraza linaloongoza. Biblia inasema: “Walipokuwa wakipita katika majiji, walikuwa wakiwapa maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu ili wayashike.” (Mdo. 16:4) Bila shaka makutaniko yalifuata mwongozo wa mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu. Kwa sababu ya kutii “makutaniko yakaendelea kuimarishwa katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”​—Mdo. 16:5.

19, 20. Kwa nini Wakristo wanapaswa kuwatii “wale wanaoongoza”?

19 Leo pia Mashahidi wa Yehova hupata baraka nyingi wanapofuata mwongozo wa “wale wanaoongoza” kati yao. (Ebr. 13:17) Kwa kuwa tamasha ya ulimwengu huu inabadilika, Wakristo wanapaswa kukubali na kujitiisha chini ya mwongozo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45; 1 Kor. 7:29-31) Tukifanya hivyo tutaepuka madhara ya kiroho na kubaki bila doa kutokana na ulimwengu.​—Yak. 1:27.

20 Waangalizi Wakristo leo kutia ndani washiriki wa Baraza Linaloongoza si wakamilifu kama walivyokuwa Paulo, Barnaba, Marko na wazee wengine watiwa mafuta wa karne ya kwanza. (Rom. 5:12; Yak. 3:2) Hata hivyo, Baraza Linaloongoza linategemeka kwa sababu linashikamana kabisa na Neno la Mungu na kufuata mfano uliowekwa na mitume. (2 Tim. 1:13, 14) Matokeo ni kwamba makutaniko yanatiwa nguvu na kuimarishwa katika imani.

TIMOTHEO ATUMIKA “KATIKA KUENDELEZA HABARI NJEMA”

Paulo alithamini sana kazi nzuri iliyofanywa na Timotheo. Baada ya kufanya kazi pamoja kwa miaka 11 hivi, Paulo aliandika hivi kuhusu Timotheo: “Sina mtu mwingine aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mahangaiko yenu. . . . Ninyi mnajua jinsi alivyojithibitisha mwenyewe, kwamba kama mtoto na baba yake alitumikia pamoja nami katika kuendeleza habari njema.” (Flp. 2:20, 22) Timotheo alijitolea ili kuendeleza kazi ya kuhubiri, na kwa sababu hiyo Paulo alimpenda sana naye ni mfano mzuri sana kwetu.

Timotheo.

Inaonekana kwamba Timotheo, ambaye baba yake alikuwa Mgiriki na mama yake Myahudi, alilelewa Listra. Tangu utotoni, Timotheo alikuwa amefundishwa Maandiko na mama yake, Eunike, na nyanya yake Loisi. (Mdo. 16:1, 3; 2 Tim. 1:5; 3:14, 15) Huenda Eunike, Loisi, na Timotheo walikubali kuwa Wakristo, Paulo alipotembelea Listra kwa mara ya kwanza.

Paulo aliporudi miaka kadhaa baadaye, Timotheo, ambaye huenda alikuwa na umri wa miaka 20 hivi wakati huo, “alishuhudiwa vema na akina ndugu huko Listra na Ikoniamu.” (Mdo. 16:2) Roho ya Mungu iliongoza kutolewa kwa “unabii” kumhusu kijana huyo, na kulingana na unabii huo, Paulo na wazee wengine walipendekeza Timotheo afanye utumishi wa pekee. (1 Tim. 1:18; 4:14; 2 Tim. 1:6) Alipaswa kwenda pamoja na Paulo akiwa mmishonari. Timotheo angeiacha familia yao na pia alikubali kutahiriwa ili Wayahudi wasiwe na sababu yoyote ya kulalamika.​—Mdo. 16:3.

Timotheo alisafiri sana. Alihubiri pamoja na Paulo na Sila huko Filipi, halafu akahubiri Beroya akiwa na Sila, kisha akahubiri Thesalonike akiwa peke yake. Walipokutana tena katika jiji la Korintho, Timotheo alimjulisha Paulo kuhusu upendo na uaminifu wa Wathesalonike licha ya dhiki walizokabili. (Mdo. 16:6–17:14; 1 The. 3:2-6) Paulo aliposikia habari mbaya kuhusu kutaniko la Korintho, alifikiria kumtuma Timotheo aende Korintho ili akawasaidie. (1 Kor. 4:17) Baadaye, Paulo akiwa Efeso aliwatuma Timotheo na Erasto waende Makedonia. Paulo aliwaandikia Waroma akiwa Korintho na alikuwa pamoja na Timotheo, aliyekuwa amerudi tena Korintho. (Mdo. 19:22; Rom. 16:21) Hayo ni baadhi ya maeneo ambayo Timotheo alienda ili kutimiza migawo yake.

Inaonekana kwamba Timotheo alisita kwa kiasi fulani kutumia mamlaka yake, ndiyo sababu Paulo alimtia moyo hivi: “Usiruhusu kamwe mtu yeyote audharau ujana wako.” (1 Tim. 4:12) Hata hivyo, Paulo alimwamini Timotheo naye alimtuma aende katika kutaniko lililokuwa na matatizo na kumwagiza: “Uwaamuru watu fulani wasifundishe mambo tofauti.” (1 Tim. 1:3) Pia, Paulo alimpa Timotheo mamlaka ya kuwaweka rasmi waangalizi na watumishi wa huduma katika makutaniko.​—1 Tim. 5:22.

Paulo alimpenda sana Timotheo kwa sababu ya sifa zake nzuri. Maandiko yanaonyesha kwamba kijana huyo alikuwa kama mwana kwa sababu alishirikiana na Paulo kwa ukaribu, uaminifu na kwa upendo. Paulo aliandika kwamba anakumbuka machozi ya Timotheo, anatamani kumwona, na anasali kwa ajili yake. Pia, akiwa kama baba mwenye kujali, Paulo alimpa Timotheo ushauri kuhusu ‘ugonjwa wake wa mara kwa mara’​—huenda ulikuwa ugonjwa wa tumbo.​—1 Tim. 5:23; 2 Tim. 1:3, 4.

Paulo alipofungwa kwa mara ya kwanza huko Roma, Timotheo alikuwa pamoja naye. Timotheo pia alifungwa kwa muda fulani. (Flm. 1; Ebr. 13:23) Ni wazi kwamba wanaume hao walipendana kikweli, kwa sababu Paulo alipotambua kwamba anakaribia kufa, alimtumia Timotheo ujumbe huu: “Jitahidi kabisa ili uje kwangu upesi.” (2 Tim. 4:6-9) Maandiko hayasemi ikiwa Timotheo alifika kabla ya Paulo kufa, na kumwona tena mshauri wake mpendwa.

MARKO APATA MAPENDELEO MENGI

Injili ya Marko inasimulia kwamba wale waliomkamata Yesu walijaribu pia kumkamata “kijana fulani” aliyeponyoka, “akakimbia akiwa uchi.” (Marko 14:51, 52) Kwa kuwa Marko, ambaye pia anaitwa Yohana Marko, ndiye peke yake aliyeandika kuhusu tukio hilo, huenda kijana huyo ni yeye mwenyewe. Ikiwa ndivyo, basi Marko alikuwa amekutana kibinafsi na Yesu.

Marko akisikiliza na kuandika mwanamume mzee anapoongea.

Miaka 11 hivi baadaye, Herode Agripa alipokuwa akiwatesa Wakristo, “watu wengi” waliokuwa washiriki wa kutaniko la Yerusalemu walikuwa wamekusanyika katika nyumba ya Maria, mama ya Marko, wakisali. Petro alienda katika nyumba hiyo alipofunguliwa kimuujiza kutoka gerezani. (Mdo. 12:12) Hivyo, inawezekana kwamba Marko alilelewa katika nyumba ambayo baadaye ilitumiwa kwa ajili ya mikutano ya Kikristo. Huenda aliwafahamu wanafunzi wa mwanzoni wa Yesu, nao walimsaidia sana kufanya maendeleo ya kiroho.

Marko alitumikia bega kwa bega na waangalizi kadhaa wa kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. Inaonekana mgawo wake wa kwanza ulikuwa katika jiji la Antiokia ya Siria alipotumikia pamoja na binamu yake, Barnaba, na mtume Paulo. (Mdo. 12:25) Barnaba na Paulo walipoanza safari yao ya kwanza ya umishonari, Marko alisafiri pamoja nao, kwanza walienda Kipro kisha Asia Ndogo. Wakiwa huko, Marko akarudi Yerusalemu kwa sababu zisizojulikana. (Mdo. 13:4, 13) Baada ya Barnaba na Paulo kutoelewana kwa sababu ya Marko, kama inavyosimuliwa katika Matendo sura ya 15, Marko na Barnaba waliendelea na kazi ya umishonari katika kisiwa cha Kipro.​—Mdo. 15:36-39.

Inaonekana kufikia mwaka wa 60 au 61 W.K., tayari walikuwa wametatua kutoelewana kwao kwa sababu Marko anatajwa kwa mara nyingine kwamba alikuwa akitumikia pamoja na Paulo jijini Roma. Paulo aliyekuwa mfungwa katika jiji hilo, aliliandikia hivi kutaniko la Kolosai: “Aristarko, mateka mwenzangu anawatumia salamu zake, na pia Marko, binamu ya Barnaba, (ambaye mlipokea maagizo ya kumkaribisha ikiwa atakuja kwenu).” (Kol. 4:10) Kwa hiyo, Paulo alikuwa akifikiria kumtuma Yohana Marko aende Kolosai, akamwakilishe.

Kati ya mwaka 62 na 64 hivi, Marko alitumikia pamoja na mtume Petro katika jiji la Babiloni. Kama tulivyoona katika Sura ya 10 ya kitabu hiki, walikuwa na uhusiano wa karibu, kwa kuwa Petro anamwita kijana huyo “Marko, mwanangu.”​—1 Pet. 5:13.

Mwishowe, mwaka wa 65 W.K. hivi, mtume Paulo alipofungwa kwa mara ya pili jijini Roma, alimwandikia hivi Timotheo, mtumishi mwenzake aliyekuwa Efeso: “Mchukue Marko uje pamoja naye, kwa maana ni mwenye faida kwangu katika huduma.” (2 Tim. 4:11) Bila shaka Marko alikubali mwaliko huo na kurudi Roma. Ndiyo sababu Barnaba, Paulo, na Petro walimthamini sana kijana huyo!

Pendeleo kubwa zaidi la Marko ni lile la kuongozwa na roho ya Yehova kuandika masimulizi ya Injili. Inaaminika kwamba Marko alipata habari nyingi kutoka kwa mtume Petro. Kuna mambo yanayounga mkono wazo hilo. Kwa mfano, masimulizi ya Marko yanataja mambo fulani hususa ambayo yangeweza kusimuliwa tu na mtu aliyejionea matukio hayo, kama vile Petro. Hata hivyo, inaonekana Marko aliandika Injili yake akiwa Roma bali si akiwa Babiloni pamoja na Petro. Marko anatumia maneno mengi ya Kilatini na kutafsiri maneno ya Kiebrania ili watu wasio Wayahudi waelewe kwa urahisi. Kwa hiyo inaonekana aliandika hasa kwa ajili ya Watu wa Mataifa.

a Ona sanduku lenye kichwa “Marko Apata Mapendeleo Mengi.”

b Ona sanduku lenye kichwa “Timotheo Atumika ‘Kuendeleza Habari Njema’.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki