Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be uku. 4-uku. 8 fu. 1
  • Karibu Kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Karibu Kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Vichwa vidogo
  • Jinsi ya Kufaidika Kabisa
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be uku. 4-uku. 8 fu. 1
Picha katika ukurasa wa 5

Karibu Kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi

KATIKA nchi zaidi ya 200 duniani kote, mamilioni ya wanafunzi wanafaidika kila juma na elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Wengine ni wapya katika shule, hali wengine wameshiriki kwa miaka mingi. Shule hii inaongozwa katika sehemu mbalimbali zipatazo makumi ya maelfu. Hata uwe unaishi wapi duniani, unaweza kushiriki katika programu hiyo hiyo ya elimu. Watu wa umri wowote ule, kabila lolote lile, na wenye elimu yoyote ile wanapokea mafundisho haya ya kitheokrasi bila malipo.

Shule hii ilipoanzishwa katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1943, kusudi lake lilikuwa hili: “Kuwatayarisha ‘wanaume wote waaminifu,’ wale ambao wamelisikia Neno la Mungu na kuthibitisha kwamba wanaliamini, ‘ili waweze kufundisha wengine’ . . . kwa kusudi la kufanya kila mmoja . . . awe na uwezo zaidi wa kutangaza tumaini lake.” (Course in Theocratic Ministry, uku. 4) Shule hii bado ina kusudi hilo hilo.

Kwa kuwa tuna zawadi ya usemi tuliopewa na Mungu, tunaweza kuutumiaje kwa njia bora zaidi? Biblia inajibu: “Kila mwenye pumzi na amsifu BWANA.” (Zab. 150:6) Tunapofanya hivyo, tunamfurahisha Baba yetu wa mbinguni. Tunamthibitishia kwamba tunamshukuru kwa moyo kwa sababu ya wema wake na upendo wake. Si ajabu kwamba sikuzote Wakristo hutiwa moyo ‘wamtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani’! (Ebr. 13:15) Tunakukaribisha uwe mwanafunzi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ili upate msaada wa kuboresha uwezo wako wa kutumia vipawa vyako ili kumsifu Yehova.

Ingawa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inakazia kusoma mbele ya watu na vilevile uwezo wa kusema na kufundisha, ina faida nyinginezo. Unaposhiriki, utasaidiwa kukuza mambo muhimu kama vile uwezo wa kusoma, kusikiliza na kukumbuka mambo, kujifunza, kufanya utafiti, kuchanganua habari na kuzipanga, kuzungumza na wengine, kujibu maswali, na kuandika mawazo yako. Biblia yenyewe pamoja na vichapo vinavyoitegemea vitakuwa msingi wa funzo na maelezo na hotuba zitakazotolewa katika shule. Unaposoma kweli zenye thamani zinazopatikana katika Neno la Mungu, utajifunza kuona mambo jinsi Mungu anavyoyaona. Hiyo inaweza kukufaidi sana katika kila sehemu ya maisha yako. Katika karne ya 20, mwalimu mmoja wa chuo kikuu, William Lyon Phelps, aliandika hivi kuhusu faida ya Neno la Mungu: “Kwa kweli kila mtu ambaye ameijua Biblia vizuri anaweza kuitwa mwenye elimu. . . . Naamini kwamba kuijua Biblia bila masomo ya chuo kuna thamani kuliko masomo ya chuo bila Biblia.”

Jinsi ya Kufaidika Kabisa

Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 4

Bila shaka, ni lazima wewe mwanafunzi ujitahidi ili ufaidike kabisa na elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mtume Paulo alimhimiza hivi Timotheo, mshirika wake Mkristo: “Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote.” (1 Tim. 4:15) Unaweza kujitahidi kwa njia zipi zenye manufaa?

Ikiwezekana, hudhuria Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kila juma. Tumia vizuri kitabu hiki, Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Andika jina lako vizuri katika nafasi ambayo imeandaliwa kwenye ukurasa wa mbele wa kitabu. Beba kitabu hiki nyakati zote unapohudhuria shule. Kitabu hiki kina mazoezi vilevile. Piga mstari mambo muhimu unayosoma humu ndani ambayo unaona yatakusaidia. Unapojifunza wakati wa mazungumzo katika shule, tumia nafasi kubwa zilizo pembeni kuandika mambo unayoweza kutumia.

Programu iliyochapwa ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi itaandaliwa kando. Pia programu hiyo itakuwa na habari zaidi zinazoonyesha jinsi shule hiyo itakavyoongozwa. Huenda ikafaa uweke programu yako katika kitabu hiki ili uweze kuipata kwa urahisi.

Unapojitayarishia shule kila juma, ukumbuke kwamba Biblia ndicho kitabu kikuu cha mafundisho. Jambo kuu kwanza ni usomaji wa Biblia ambao umepangwa juma hilo. Pia utafaidika ukisoma mapema habari za sehemu mbalimbali za programu.

Huenda kukawa na fursa za wasikilizaji kushiriki wakati wa shule. Zitumie vizuri. Kushiriki katika mazungumzo hayo ni njia muhimu ya kukumbuka mambo unayosikia na kuweza kuyatumia maishani mwako mwenyewe.

Bila shaka, wanafunzi wote watapata nafasi za kutoa hotuba au maonyesho mbele ya kutaniko. Tumia vizuri kila mojawapo ya nafasi hizo. Jitahidi kufanya maendeleo katika sifa yoyote ya usemi ambayo unagawiwa. Utapewa mashauri ili uzidi kufanya maendeleo. Pokea msaada huo kwa njia nzuri. Andika katika kitabu chako madokezo unayoweza kutumia ili ufanye maendeleo. Kwa kuwa ni vigumu kujiona jinsi wengine wanavyokuona, madokezo na mashauri yanayotolewa kwa upendo na kwa kutegemea Biblia yanaweza kuchangia sana maendeleo yako. Na ndivyo ilivyo hata kama umekuwa katika shule kwa miaka mingi.—Mit. 1:5.

Je, ungependa kufanya maendeleo ya haraka zaidi? Wewe mwenyewe ukichukua hatua zinazofaa, unaweza kufaulu. Soma mapema kila hotuba ya wanafunzi. Kama kuna uhitaji wa msemaji wa badala, utaweza kujitolea, na hivyo upate uzoefu zaidi. Wengine wanapotoa hotuba, sikiliza kwa makini jinsi wanavyozitoa. Kila mmoja wetu hujifunza kutoka kwa mwenzake.

Kwa kuongezea, unaweza kufanya maendeleo haraka zaidi kwa kusoma mapema kitabu hiki ikiwa hali zinaruhusu. Baada ya kujifunza vizuri mambo yaliyo katika masomo 15 yanayofuata, sasa shughulikia sehemu ya “Programu Inayokusaidia Kuwa Msemaji na Mwalimu Bora,” inayoanzia ukurasa wa 78. Kwanza, jifunze kila somo kisha ufanye mazoezi yaliyoorodheshwa humo. Tumia mambo unayojifunza katika huduma yako. Kufanya hivyo kunaweza kuharakisha maendeleo yako ukiwa msemaji na mwalimu bora wa Neno la Mungu.

Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi itakusaidia kutimiza jambo muhimu zaidi maishani. Kwa kuwa tuko hai kwa mapenzi ya Mungu, tunapomsifu tunaonyesha tunatambua kusudi letu halisi la sisi kuwa hai. Yehova Mungu anastahili sifa bora zaidi. (Ufu. 4:11) Elimu tunayopokea katika shule hii ni njia ya kutimiza jambo hilo ili tuweze kufikiri kwa njia ya wazi, kutenda kwa hekima, na kueleza kwa njia bora kweli za ajabu za Neno la Mungu lililopuliziwa.

MAMBO AMBAYO SHULE HII INASHUGHULIKIA

  • Kila juma kuna programu ya kusoma, kujifunza, na kufanya utafiti kuhusu Biblia

  • Mafundisho juu ya kusoma mbele ya watu na vilevile uwezo wa kusema na kufundisha

  • Kushiriki katika mazungumzo katika shule

  • Nafasi za kushughulikia mgawo mbele ya kutaniko

  • Msaada wa kibinafsi ili ufanye maendeleo

USTADI MBALIMBALI UNAOZINGATIWA

  • Kusikiliza na kukumbuka

  • Kusoma kibinafsi

  • Kujifunza

  • Kufanya utafiti

  • Kuchanganua na kupanga habari

  • Kuzungumza na wengine

  • Kujibu maswali

  • Kuandika mawazo yako

MSINGI WA KUJENGEA

Uwezo wa kuwasiliana vizuri na watu ni ustadi. Si watu wote wana ustadi huo. Vitabu vingi vimetayarishwa kuwasaidia watu kuwasiliana kwa njia bora. Lakini, Muumba, Yule aliyewapa wanadamu uwezo wa kusema, anajua mengi kuhusu kusema na kufundisha kuliko mtaalamu yeyote wa mambo ya usemi. Mwana wake mzaliwa wa pekee alishirikiana naye akiwa Stadi wa Kazi kufanyiza ubongo wa binadamu na viungo vya usemi na hata maajabu mengine yote ya uumbaji.

Malaika walipoumbwa, kisha wanadamu kufuata, huyo Mwana alikuwa Neno la Mungu na Mungu alimtumia kuwasiliana nao. (Mit. 8:30; Yn. 1:1-3) Mwana huyo alitumwa duniani akiwa Bwana Yesu Kristo. Maandiko yaliyoongozwa kwa roho yanasema hivi juu yake: “Umati ulishangaa juu ya njia yake ya kufundisha.” Na wale waliomsikia walishuhudia hivi: “Hajasema kamwe mtu mwingine kama hivi.” (Mt. 7:28; Yn. 7:46) Basi, kuna sababu nzuri ya Yesu kuitwa Mwalimu zaidi ya mara 40 katika vitabu vya Injili. Tunaweza kujifunza mengi kutoka kwake kuhusu kusema na kufundisha.

Pia Biblia inatuonyesha jinsi Yehova Mungu alivyotumia wanaume na wanawake wa malezi tofauti-tofauti kutimiza mapenzi yake. Baadhi yao walitangaza ujumbe mfupi-mfupi lakini wenye nguvu sana. Wengi hawakuhutubu mbele ya watu wengi, lakini kwa uaminifu walitoa ushahidi kuhusu Mungu wa kweli na kusudi lake. Inaelekea kwamba wengi wao hawakuwa wasemaji wenye ufasaha lakini Mungu alibariki jitihada zao. Tunaweza kujifunza kutokana na habari ambazo Biblia inatuambia kuhusu jinsi walivyotimiza huduma yao.—Zab. 68:11.

Bila shaka, Biblia si kitabu kinachofundisha hasa kusema mbele ya watu. Lakini wale wanaoisoma kwa utambuzi wanapata mambo yenye thamani sana yanayoweza kuwasaidia wawe wasemaji wazuri na walimu bora. Kitabu hiki Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kinajaribu kutimiza kusudi hilo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki