Jinsi Unavyoweza Kujibu Vizuia-Mazungumzo Vikitokea
Maelezo: Matarajio ya watu ya uzima hutegemea mtazamo wao kwa Yehova Mungu na Ufalme wake mikononi mwa Kristo Yesu. Ujumbe wa Ufalme wa Mungu unavutia, nao unaelekeza kwenye tumaini pekee linalotegemeka kwa ajili ya wanadamu. Ni ujumbe unaobadili maisha. Tunataka kila mtu ausikie. Tunafahamu kwamba ni wachache tu watakaoupokea na kuuthamini, lakini tunajua kwamba angalau watu wanahitaji kuusikia ili wafanye uchaguzi wa jambo wanalojua. Hata hivyo, si kila mtu aliye tayari kusikiliza, nasi hatujaribu kumlazimisha. Lakini tukiwa na utambuzi mara nyingi inawezekana kuvigeuza vizuia-mazungumzo viwe nafasi za mazungumzo zaidi. Hii ni mifano ambayo baadhi ya Mashahidi wenye uzoefu wametumia wakijitahidi kutafuta wanaostahili. (Mt. 10:11) Hatupendekezi kwamba ukariri moyoni lolote la majibu haya bali uweke wazo akilini, ulitie katika maneno yako mwenyewe na kulieleza kwa njia inayoonyesha kwamba unapendezwa kikweli na mtu unayesema naye. Unapofanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba wale ambao mioyo yao ina mwelekeo unaofaa watasikiliza na kuthamini yale ambayo Yehova anafanya ili kuwavuta kwenye maandalizi yake ya upendo ya kupata uzima.—Yoh. 6:44; Mdo. 16:14.
‘MIMI SIPENDEZWI’
● ‘Hebu nikuulize, Unamaanisha kwamba hupendezwi na Biblia, au hupendezwi na dini kwa ujumla? Nauliza hivyo kwa sababu tumekutana na watu wengi ambao wakati mmoja walikuwa watu wa dini lakini hawaendi tena kanisani kwa sababu wanaona unafiki mwingi katika makanisa (au, wanaona kwamba dini ni biashara tu; au, hawaoni inafaa dini kujiingiza katika siasa; n.k.). Biblia pia haikubali matendo hayo, nayo huandaa msingi pekee unaotuwezesha kuutazamia wakati ujao tukiwa na uhakika.’
● ‘Ikiwa unamaanisha kwamba hupendezwi na dini nyingine, ninaelewa hilo. Lakini inaelekea unapendezwa na wakati ujao tunaoweza kutazamia kwa sababu ya hatari ya vita vya nyukilia (au, jinsi tunavyoweza kuwalinda watoto wetu ili wasitumie vibaya dawa za kulevya; au linaloweza kufanywa kuhusu uhalifu ili tusiogope kutembea barabarani; n.k.). Je, unaona kuna tarajio lolote la kupata utatuzi wa kweli?’
● ‘Je, ni kwa sababu tayari una dini . . . Hebu niambie, Je, unafikiri kuna wakati ambapo watu wote watakuwa katika dini moja? . . . Ni nini kinachozuia jambo hilo lisitendeke? . . . Ili hilo lifaulu, ni msingi gani unaohitajiwa?’
● ‘Ninaweza kuelewa jambo hilo. Miaka michache iliyopita nilikuwa na maoni kama hayo. Lakini nilisoma jambo fulani katika Biblia lililonisaidia niwe na maoni tofauti. (Mwonyeshe mtu huyo lilikuwa nini.)’
● ‘Ungependa nikuonyeshe katika Biblia jinsi unavyoweza kuwaona tena wapendwa wako waliokufa (au, kusudi la kweli la maisha; au, jinsi inavyoweza kutusaidia kuziunganisha familia zetu; n.k.)?’
● ‘Ikiwa unamaanisha kwamba hupendi kununua kitu, hebu nikutulize akili. Mimi sifanyi biashara. Lakini je, unapenda kuwa na nafasi ya kuishi katika paradiso duniani, bila magonjwa na uhalifu, ukiwa na jirani wanaokupenda kwelikweli?’
● ‘Je, wewe hujibu hivyo sikuzote Mashahidi wa Yehova wanapokutembelea? . . . Je, umewahi kujiuliza kwa nini tunaendelea kuwatembelea watu au jambo tunalotaka kusema? . . . Kwa ufupi, sababu ya kuja kukuona ni kwamba ninajua jambo fulani ambalo wewe unapaswa kulijua pia. Kwa nini usisikilize mara hii tu?’
‘SIPENDEZWI NA DINI’
● ‘Ninaelewa maoni yako. Kusema kweli, makanisa hayaufanyi ulimwengu huu kuwa mahali salama zaidi pa kuishi, sivyo? . . . Hebu nikuulize, Umekuwa na maoni hayo sikuzote? . . . Lakini unamwamini Mungu?’
● ‘Kuna watu wengi walio na maoni kama yako. Dini haijawasaidia kamwe. Hiyo ni moja ya sababu ambazo zinafanya tukutembelee—kwa sababu makanisa hayajawaambia watu ukweli kumhusu Mungu na kusudi lake zuri ajabu kwa wanadamu.’
● ‘Lakini nina uhakika kwamba unapendezwa na maisha yako ya baadaye. Je, unajua kwamba Biblia ilitabiri hali zilizo ulimwenguni leo? . . . Nayo inaonyesha yatakayotokea baadaye.’
● ‘Je, umekuwa na maoni hayo sikuzote? . . . Una maoni gani kuhusu wakati ujao?’
‘MIMI SIPENDEZWI NA MASHAHIDI WA YEHOVA’
● ‘Watu wengi hutuambia hivyo. Je, umewahi kujiuliza kwa nini watu kama mimi hujitolea kuwatembelea watu hata ingawa tunajua kwamba huenda watu wengi wasitukaribishe? (Taja mambo makuu katika Ezekieli 9:1-11, ukieleza kwamba, ikitegemea jinsi watu wanavyoitikia ujumbe wa Ufalme, kila mtu ‘anatiwa alama’ ili aje kuokolewa katika dhiki kuu au aje kuharibiwa na Mungu.)’
● ‘Ninaelewa jambo hilo, kwa sababu mimi pia nilikuwa na maoni hayo. Lakini, bila kupendelea, nikaamua kumsikiliza mmoja wao. Ndipo nikagundua kwamba sikuwa nimeambiwa ukweli kuwahusu. (Taja shtaka moja la uwongo ambalo watu wengi hutumia kisha ueleze tunayoamini.)’
● ‘Muda mfupi uliopita nilimwambia jambo hilohilo Shahidi mmoja aliyekuja kunitembelea. Lakini kabla hajaondoka niliuliza swali ambalo niliamini kwamba hawezi kulijibu. Ungependa kulijua swali hilo? . . . (Kwa mfano: Kaini alitoa wapi mke wake?)’ (Pendekezo hili litumiwe tu na wale ambao walipatwa na jambo hilo.)
● ‘Ikiwa wewe ni mtu wa dini, ninaelewa unachomaanisha. Bila shaka dini yako ni muhimu kwako. Lakini nafikiri utakubali kwamba sote tunapendezwa na (taja kichwa kinachofaa).’
● ‘Basi bila shaka una dini yako mwenyewe. Tafadhali, ungependa kuniambia ni dini gani hiyo? . . . Sisi hufurahia kuzungumza na watu wa dini yako. Una maoni gani kuhusu (taja kichwa chako cha mazungumzo)?’
● ‘Ndiyo, naelewa hilo. Tumekutembelea kwa sababu tungependa kuona watu wakiishi pamoja kwa amani. Tumechoka kusikia kila siku habari za vita na kuteseka. Nadhani wewe pia unahisi hivyo. . . . Lakini ni nini kinachoweza kuleta mabadiliko yanayohitajiwa? . . . Tumepata kitia-moyo katika ahadi za Biblia.’
● ‘Asante kwa kunijulisha maoni yako. Tafadhali unaweza kuniambia jambo linalofanya usipendezwe nasi? Je, ni yale tunayokuonyesha katika Biblia, au ni kwa sababu tumekuja kukutembelea?’
‘NINA DINI YANGU MWENYEWE’
● ‘Hebu niambie, Je, dini yako inafundisha kwamba kuna wakati ambapo watu wanaopenda mema wataishi milele duniani? . . . Hilo ni jambo lenye kuvutia, sivyo? . . . Limo humu katika Biblia. (Zab. 37:29; Mt. 5:5; Ufu. 21:4)’
● ‘Ninakubali kwamba kila mtu anapaswa kujifanyia uamuzi kuhusiana na jambo hili. Lakini je, unajua kwamba Mungu mwenyewe anatafuta watu wa aina fulani ili wawe waabudu wake wa kweli? Ona hapa katika Yohana 4:23, 24. Inamaanisha nini kumwabudu Mungu “kwa kweli”? . . . Mungu ametupa msaada gani ili tuweze kujua lililo kweli na lisilo kweli? . . . (Yoh. 17:17) Hebu ona jinsi ilivyo muhimu kwetu binafsi. (Yoh. 17:3)’
● ‘Je, umekuwa mtu wa dini maisha yako yote? Unafikiri wanadamu watapata kuungana katika dini moja? . . . Nimefikiria jambo hilo sana kwa sababu ya maneno yaliyoandikwa katika Ufunuo 5:13. . . . Tunahitaji kufanya nini ili tupatane na jambo hilo?’
● ‘Nilikuwa nikitumaini kumwona mtu kama wewe anayependezwa na mambo ya kiroho. Watu wengi leo hawapendi mambo ya kiroho. Una maoni gani kuhusu ahadi ya Biblia kwamba Mungu ataondoa uovu wote na kuifanya dunia hii iwe mahali ambapo watu wanaopenda uadilifu peke yao wataishi? Je, jambo hilo ni zuri kwako?’
● ‘Je, unajihusisha sana na mambo ya kanisa? . . . Je, siku hizi kanisa hujaa watu wakati wa ibada? . . . Je, unaona kwamba wafuasi wengi wanaonyesha tamaa ya moyo mnyoofu ya kutumia Neno la Mungu katika maisha ya kila siku? (Au, Je, unaona kwamba washiriki wana maoni yanayolingana kuhusu utatuzi wa matatizo yanayoukabili ulimwengu?) Sisi tumeona kwamba kuna faida ya kujifunza Biblia nyumbani.’
● ‘Inaonekana umeridhika na dini yako. Lakini watu wengi hawaridhiki na hali zilizo ulimwenguni. Labda wewe pia unaona hivyo, sivyo? . . . Ulimwengu unaelekea wapi?’
● ‘Je, wewe hupenda kusoma Biblia? . . . Je, unapata wakati wa kuisoma kwa ukawaida?’
● ‘Asante kwa kuniambia hivyo. Ninaamini utakubali kwamba, hata tuwe wa dini gani, sote tunapendezwa sana na amani ya ulimwengu (au, njia za kuwalinda watoto wetu wasipatwe na mavutano mabaya; au kuwa na ujirani ambamo watu wanapendana kikweli; au, kuwa na uhusiano mzuri pamoja na watu wengine, na hilo linaweza kutokeza tatizo wakati kila mtu anahisi yuko chini ya mkazo).’
● ‘Ninafurahi kujua kwamba unapenda dini. Watu wengi leo hawachukui dini kwa uzito. Hata wengine hufikiri hakuna Mungu. Lakini, kulingana na yale ambayo umefundishwa, unafikiri Mungu ni mtu wa aina gani? . . . Ona kwamba Biblia inatuonyesha jina lake. (Kut. 6:3; Zab. 83:18)’
● ‘Yesu alipowatuma wanafunzi wake wakahubiri, aliwaambia waende katika kila sehemu ya dunia, na hivyo wangewakuta watu wengi ambao wana dini tofauti. (Mdo. 1:8) Lakini alijua kwamba wale walio na njaa na kiu ya uadilifu wangesikiliza. Ni ujumbe gani hasa ambao alisema ungetangazwa wakati wetu? (Mt. 24:14) Ufalme huo unamaanisha nini kwetu?’
‘TAYARI SISI NI WAKRISTO HAPA KWETU’
● ‘Ninafurahi kusikia hivyo. Basi bila shaka unajua kwamba Yesu mwenyewe alifanya kazi kama hii, akiwatembelea watu katika nyumba zao, naye aliwaagiza wanafunzi wake pia wafanye hivyo. Unajua habari walizohubiri? . . . Hizo ndizo habari ambazo tumekuja kuzungumzia leo. (Luka 8:1; Dan. 2:44)’
● ‘Basi nina hakika utaona uzito wa mambo ambayo Yesu alisema hapa katika Mahubiri ya Mlimani. Alitaja mambo waziwazi lakini pia alionyesha upendo aliposema . . . (Mt. 7:21-23) Basi, tunahitaji kujiuliza hivi, Nayajua kadiri gani mapenzi ya Baba wa mbinguni? (Yoh. 17:3)’
‘NINA SHUGHULI’
● ‘Basi nitasema kwa ufupi sana. Nilikuja kuzungumza nawe jambo moja tu muhimu. (Eleza mambo makuu ya mazungumzo yako ukitumia sentensi mbili hivi.)’
● ‘Ni sawa. Nitapenda kukutembelea wakati mwingine ambao unakufaa zaidi. Lakini kabla sijaondoka, ningependa kusoma andiko moja tu linalotupatia jambo muhimu la kufikiria.’
● ‘Ninaelewa. Mimi pia ni mama (au, mfanyakazi; au mwanafunzi) nami nina shughuli nyingi. Kwa hiyo nitasema kwa ufupi. Sote tunakabiliwa na hali nzito. Biblia inaonyesha kwamba tunakaribia sana wakati ambapo Mungu atauharibu mfumo wa mambo wa sasa ulio mbovu. Lakini kuna watu watakaookoka. Swali ni, Mimi na wewe tunapaswa kufanya nini ili tuwe kati yao? Biblia inajibu swali hilo. (Sef. 2:2, 3)’
● ‘Hiyo ndiyo sababu hasa iliyonifanya nikutembelee. Sote tuna shughuli nyingi sana hivi kwamba nyakati nyingine mambo muhimu kwelikweli maishani hupuuzwa, sivyo? . . . Nitasema kwa ufupi, lakini naamini utapendezwa na andiko hili moja tu. (Luka 17:26, 27) Sote hatutaki kujikuta katika hali hiyo, kwa hiyo tunahitaji kutafuta wakati katika maisha yetu yenye shughuli nyingi ili tufikirie mambo ambayo Biblia inasema. (Toa kichapo.)’
● ‘Je, itakufaa zaidi tukirudi baada ya nusu saa hivi, baada ya kuwatembelea jirani zako?’
● ‘Basi sitachukua muda mrefu. Labda nitakutembelea siku nyingine. Lakini kabla sijaondoka, ningependa nikupe kichapo hiki. (Mpe toleo la mwezi huo.) Kichapo hiki kina masomo yatakayokufahamisha majibu ya Biblia kwa maswali kama (taja swali moja au mawili tu).’
● ‘Pole kwa kuwa nimekutembelea wakati usiofaa. Labda unajua kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilitaka kuzungumza na wewe jambo muhimu kutoka katika Biblia. Lakini kwa kuwa huna wakati wa kusikiliza sasa, ningependa kukupa trakti hii, inayozungumzia (taja kichwa). Itakuchukua muda mfupi tu kuisoma trakti hii, lakini itakupendeza sana.’
● ‘Ninaelewa jambo hilo. Inaonekana hakuna wakati wa kutosha kufanya kila jambo. Lakini umepata kujiuliza jinsi ambavyo maisha yangekuwa tofauti ikiwa ungeishi milele? Najua jambo hili huenda likasikika kuwa geni. Lakini acha nikuonyeshe andiko moja tu la Biblia linaloeleza jinsi jambo hilo linavyowezekana. (Yoh. 17:3) Kwa hiyo, jambo tunalohitaji kufanya sasa ni kupata ujuzi huu kumhusu Mungu na Mwana wake. Ndiyo sababu tunawaachia watu vichapo hivi.’
‘KWA NINI MNAWATEMBELEA WATU MARA NYINGI?’
● ‘Kwa sababu tunaamini kwamba tunaishi katika siku za mwisho zinazotajwa katika Biblia. Tunaona kwamba ni muhimu kwetu sote kufikiria yatakayotokea baada ya hizi hali za sasa. (Taja jambo moja au mawili yaliyotukia hivi karibuni au hali za sasa.) Swali ni, tunahitaji kufanya nini ikiwa tunataka kuuokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo?’
● ‘Kwa sababu tunampenda Mungu na jirani zetu. Sote tunapaswa kufanya hivyo, sivyo?’
‘TAYARI NAIJUA VIZURI KAZI YENU’
● ‘Ninafurahi sana kusikia hivyo. Je, una mtu wa ukoo au rafiki ambaye ni Shahidi? . . . Hebu nikuulize: Unaamini tunayofundisha kutoka katika Biblia, yaani, kwamba tunaishi katika “siku za mwisho,” kwamba hivi karibuni Mungu atawaharibu waovu, na kwamba dunia hii itakuwa paradiso ambamo watu wanaweza kuishi milele wakiwa na afya kamilifu katikati ya jirani wanaopendana kwelikweli?’
‘HATUNA PESA’
● ‘Sisi hatuombi pesa. Lakini tunawatolea watu funzo la Biblia nyumbani bila malipo. Moja la masomo hayo ni (tumia kichwa cha sura fulani kutoka katika kichapo kinachotolewa wakati huu). Je, nitumie dakika chache niwaonyeshe jinsi linavyofanywa? Haitawagharimu hata shilingi moja.’
● ‘Sisi tunapendezwa na watu, wala hatupendezwi na pesa zao. (Endelea na mazungumzo. Waonyeshe kichapo kimoja na ueleze jinsi kinavyoweza kuwasaidia. Wakionyesha upendezi wa kweli na kuahidi kwamba watakisoma, waachie. Ikiwa inafaa, eleza jinsi kazi yetu ya ulimwenguni pote ya kuhubiri inavyogharimiwa.)’
MTU AKISEMA, ‘MIMI NI MBUDHA’
● Usikate shauri kwamba imani za mtu huyo ni sawa na za Wabudha wengine wote. Mafundisho ya Buddha hayaeleweki na watu huyafasiri kwa njia zao mbalimbali. Ubudha wa Japan ni tofauti sana na Ubudha wa Asia ya Kusini-Mashariki. Pia watu wana maoni mbalimbali. Hata hivyo, kwa ujumla huenda mambo yafuatayo yakakusaidia: (1) Ubudha hautambui Mungu wa nje, Muumba aliye mtu. Lakini Wabudha wengi huabudu sanamu na masalio ya Buddha. (2) Siddhartha Gautama, aliyepewa jina Buddha, alikuja kuonwa kuwa mfano bora wa kidini kwa wafuasi wake, ili wamwige. Aliwatia watu moyo wapate ujuzi kwa kujifunza habari ya wanadamu kutokana na maoni ya kibinadamu, pia aliwatia watu moyo waondoe kabisa chanzo cha kuteseka kwa kuitawala akili ili kuondoa tamaa zote za dunia. Alifundisha kwamba kwa njia hiyo huenda mtu akafikia Nirvana, ajiondolee kabisa kule kuzaliwa upya katika mwili mwingine. (3) Wabudha huabudu mababu wao wa kale, kwa sababu wanawaona hao kuwa chanzo cha uhai wao.
Mapendekezo ya mazungumzo: (1) Unaposema na Wabudha, kazia kwamba wewe si sehemu ya Jumuiya ya Wakristo. (2) Wabudha wanaheshimu “vitabu vitakatifu,” na kwa sababu hiyo kwa ujumla wao huiheshimu Biblia. Badala ya kukazia falsafa ya Buddha, toa ujumbe mzuri wa Biblia. Wajulishe kwamba Biblia si falsafa tu ya wanadamu bali ni Neno lenye mamlaka la Yehova Mungu, Muumba wa wanadamu. Uliza kwa heshima ikiwa unaweza kuwaonyesha jambo lenye kupendeza katika kitabu hicho kitakatifu, Biblia. (3) Wabudha wengi hupendezwa na amani na maisha ya familia nao hutaka kuishi maisha ya uadilifu. Mara nyingi wao hupenda kuzungumzia lolote kati ya mambo hayo. (4) Onyesha kwamba Biblia inataja serikali ya uadilifu ya mbinguni juu ya dunia kuwa ndiyo njia pekee ya kuondoa matatizo yanayowakabili wanadamu. Inaeleza wakati ujao wa dunia na tarajio zuri ajabu la kuishi milele katika paradiso duniani. (5) Unaweza kutaja kwamba Biblia inaeleza mwanzo wa uhai, maana ya uhai, hali ya wafu na tumaini la ufufuo, sababu ya kuwapo kwa uovu. Kutoa kweli zilizo wazi za Neno la Mungu kwa njia yenye fadhili kutafanya mioyo ya watu walio mfano wa kondoo iitikie vizuri.
Kijitabu cha Kiingereza In Search of a Father kiliandikwa hasa kwa ajili ya Wabudha wenye mioyo minyoofu.
MTU AKISEMA, ‘MIMI NI MHINDU’
● Unapaswa kujua kwamba falsafa ya Kihindu ni ngumu kufahamika. Huenda utaona inasaidia kukumbuka mambo haya: (1) Uhindu hufundisha kwamba mungu Brahman ana maumbo matatu—Brahma Muumba, Vishnu Mhifadhi, na Siva Mwangamizaji. Lakini Wahindu hawaamini kwamba kuna mungu ambaye ana utu wake mwenyewe. (2) Wahindu huamini kwamba vitu vyote vya asili vina nafsi isiyokufa kamwe, kwamba nafsi hiyo huwa na mizunguko isiyo na mwisho ya kuzaliwa upya katika mwili mwingine, kwamba matendo (Karma) huamua mwili ambamo nafsi hiyo itazaliwa tena, kwamba kufunguliwa kutoka katika “gurudumu hilo lisilo na mwisho” kunawezekana tu kwa kuzima tamaa zote za mwili, na kwamba hilo likitimizwa, nafsi hiyo itaungana na roho ya ulimwengu wote. (3) Kwa ujumla, Wahindu huheshimu dini nyingine. Wahindu huamini kwamba, ijapokuwa dini mbalimbali hufundisha mafundisho yanayopingana, zote huongoza kwenye kweli ileile.
Badala ya kujaribu kushughulikia falsafa ngumu ya Kihindu, toa kweli zenye kuridhisha zinazopatikana katika Biblia Takatifu. Maandalizi ya upendo ya Yehova ya kupata uzima yako wazi kwa watu wa aina zote, na kweli zilizo wazi katika Neno lake zitaifikia mioyo ya wale wanaoona njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu. Ni Biblia pekee inayotoa tumaini lenye msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao; ni Biblia pekee inayotoa majibu yenye kuridhisha kwelikweli kwa maswali muhimu yanayowakabili wanadamu wote. Wape nafasi ya kusikia majibu hayo. Ni jambo linalopendeza kwamba wimbo wa Kihindu Rig-Veda, 10. 121, una kichwa “Kwa Mungu Asiyejulikana.” Katika hali fulani huenda ukaona inafaa kutaja wimbo huo kwa njia inayofanana na ile ambayo mtume Paulo alitaja madhabahu yenye maandishi “Kwa Mungu Asiyejulikana” katika Athene. (Mdo. 17:22, 23) Inapendeza kujua kwamba, jina la mungu wa Wahindu, Vishnu, bila herufi “V,” ni Ish-nuh, ambalo katika Kikaldayo humaanisha “mwanamume Noa.” Taja yale ambayo Biblia inasema kuhusu maana ya Gharika ya duniani pote katika siku za Noa. Wale wanaosumbuliwa na tarajio la kuzaliwa upya katika mwili mwingine kusiko na mwisho huenda wakasaidiwa na habari iliyo katika ukurasa wa 152, 153, chini ya kichwa “Kuzaliwa Upya Katika Mwili Mwingine.”
Vijitabu The Path of Divine Truth Leading to Liberation na From Kurukshetra to Armageddon—And Your Survival vina habari itakayowasaidia sana Wahindu wenye mioyo minyoofu.
MTU AKISEMA, ‘MIMI NI MYAHUDI’
● Kwanza, chunguza uone jinsi mtu huyo anavyojiona kuwa Myahudi. Wengi wao hawafuati dini. Kwa wengi wao, kuwa Myahudi kunamaanisha tu kabila lake.
Haya ni mambo machache ambayo ni vizuri kukumbuka: (1) Wayahudi wa kidini wanaona ni marufuku kutamka jina la Mungu. (2) Wayahudi wengi wanaiona “Biblia” kuwa kitabu cha Wakristo, lakini ukitaja “Maandiko ya Kiebrania,” “Maandiko,” au “Torati,” tatizo hilo halitokei. (3) Mapokeo ni sehemu kuu ya imani yao nayo huonwa na Wayahudi wengi wa kidini kuwa yana mamlaka inayolingana na Maandiko. (4) Huenda wakamhusisha Yesu Kristo na mateso ambayo Wayahudi walipata mikononi mwa Jumuiya ya Wakristo kwa kutumia jina la Yesu. (5) Mara nyingi wanaamini kwamba Mungu anawataka Wayahudi waishike Sabato, imani inayotia ndani kuacha kugusa pesa siku hiyo.
Ili kuanzisha mazungumzo kwa mambo mnayokubaliana, unaweza kusema: (1) ‘Labda utakubali kwamba, bila kujali malezi yetu, sote tunakabili magumu yaleyale katika ulimwengu wa leo. Je, unaamini kwamba kwa kweli kutakuwako utatuzi wenye kudumu wa matatizo makubwa yanayokikabili kizazi hiki? (Zab. 37:10, 11, 29; Zab. 146:3-5; Dan. 2:44)’ (2) ‘Sisi si sehemu ya Jumuiya ya Wakristo na hatuamini Utatu bali tunamwabudu Mungu wa Abrahamu. Hasa tunapendezwa na ukweli wa kidini. Je, ni sawa nikikuuliza jinsi unavyojua kilicho cha kweli, hasa kwa vile kuna tofauti kubwa za imani kati ya Wayahudi? . . . (Kum. 4:2; Isa. 29:13, 14; Zab. 119:160)’ (3) ‘Tunapendezwa na ahadi ya Mungu kwa Abrahamu kwamba kupitia uzao wake watu wa mataifa yote watabarikiwa. (Mwa. 22:18)’
Mtu huyo akionyesha kwamba hamwamini Mungu, muulize ikiwa amekuwa na maoni hayo sikuzote. Kisha labda zungumzia sababu gani Mungu ameruhusu uovu na kuteseka. Kumbukumbu za mateso makubwa waliyotendewa na Wanazi zimewafanya Wayahudi wengi wahangaikie jambo hilo.
Ikiwa unazungumzia umuhimu wa kutumia jina la Mungu, chunguza kwanza ujue maoni ya mtu huyo kuhusu jambo hilo. Eleza kwamba andiko la Kutoka 20:7 linakataza kulitumia jina la Mungu kwa njia isiyofaa, lakini halikatazi kulitumia kwa heshima. Ndipo toa sababu kwa kutumia maandiko kama Kutoka 3:15 (au Zaburi 135:13); 1 Wafalme 8:41-43; Isaya 12:4; Yeremia 10:25; Malaki 3:16.
Unapozungumza kuhusu Masihi: (1) Sema kwanza kuhusu baraka za wakati ujao chini ya utawala wake, badala ya utambulisho wake. (2) Kisha toa sababu kwa kutumia maandiko yanayomtaja Masihi ambaye ni mtu. (Mwa. 22:17, 18; Zek. 9:9, 10; Dan. 7:13, 14) (3) Labda unaweza kuzungumzia safari mbili za kuja kwa Masihi. (Eleza tofauti iliyo kati ya Danieli 7:13, 14 na Danieli 9:24-26.) (4) Unapomtaja Yesu, fanya hivyo ukikazia hali yenye kuendelea ya kusudi la Mungu. Taja kwamba Yesu alipofundisha, wakati ulikuwa umekaribia wa Mungu kuruhusu hekalu la pili liharibiwe, lisijengwe upya kamwe. Lakini Yesu alikazia utimizo wa Sheria na wa Manabii na wakati ujao wenye utukufu ambapo hayo yangewaelekeza watu wenye imani.