Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Waangalizi wa Mzunguko Wanatusaidiaje?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 17

      Waangalizi wa Mzunguko Wanatusaidiaje?

      Mwangalizi wa mzunguko na mke wake

      Malawi

      Mwangalizi wa mzunguko akiongoza mkutano wa utumishi wa shambani

      Kikundi cha utumishi

      Mwangalizi wa mzunguko akihubiri hadharani

      Huduma ya shambani

      Mwangalizi wa mzunguko akiwa kwenye kikao pamoja na wazee wa kutaniko

      Mkutano wa wazee

      Biblia huwataja mara kadhaa Barnaba na mtume Paulo. Wanaume hao walikuwa waangalizi wanaosafiri, wakiyatembelea makutaniko ya karne ya kwanza. Kwa nini? Walihangaikia kikweli hali ya ndugu zao wa kiroho. Paulo alisema kwamba alitaka ‘kurudi akawatembelee akina ndugu’ ili aone jinsi wanavyoendelea. Alikuwa tayari kusafiri mamia ya kilometa kwenda kuwaimarisha. (Matendo 15:36) Hiyo ndiyo tamaa ya waangalizi wa mzunguko leo.

      Wanakuja kututia moyo. Kila mwangalizi wa mzunguko hutembelea makutaniko 20 hivi. Yeye hukaa katika kila kutaniko kwa muda wa juma moja, mara mbili kila mwaka. Tunaweza kufaidika sana kutokana na uzoefu wa ndugu hao na wake zao pia, ikiwa wameoa. Wanajitahidi kuwafahamu vizuri vijana kwa wazee, nao wana hamu ya kuandamana pamoja nasi katika huduma ya shambani na kwa wale tunaojifunza nao Biblia. Waangalizi hao huandamana pamoja na wazee kufanya ziara za uchungaji. Ili kutuimarisha, wao hutoa hotuba zenye kutia moyo katika mikutano na makusanyiko.—Matendo 15:35.

      Wanapendezwa na wote kutanikoni. Waangalizi wa mzunguko wanapendezwa sana na hali ya kiroho ya makutaniko. Wao hufanya mkutano pamoja na wazee na watumishi wa huduma ili kuzungumzia maendeleo ambayo yamefanywa na kuwapa mapendekezo kuhusu jinsi ya kushughulikia majukumu yao. Wanawasaidia mapainia kupata mafanikio katika huduma yao, nao hufurahia kuwajua wapya na kusikia kuhusu maendeleo yao ya kiroho. Kila mmoja wa ndugu hao hujitoa kwa hiari akiwa “mfanyakazi mwenzi kwa ajili ya faida [yetu].” (2 Wakorintho 8:23) Tunapaswa kuiga imani yao na roho yao ya kujitoa kufanya mapenzi ya Mungu.—Waebrania 13:7.

      • Kwa nini waangalizi wa mzunguko hutembelea makutaniko?

      • Unaweza kufaidika jinsi gani kutokana na ziara zao?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Tia alama katika kalenda yako tarehe ya ziara ijayo ya mwangalizi wa mzunguko katika kutaniko lenu ili usikose kusikiliza hotuba zake kwenye Jumba la Ufalme. Ikiwa ungependa yeye au mke wake awepo wakati mnapojifunza Biblia juma hilo ili upate kumfahamu, mjulishe yule unayejifunza naye Biblia.

  • Tunawasaidiaje Ndugu Zetu Wakati wa Taabu?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 18

      Tunawasaidiaje Ndugu Zetu Wakati wa Taabu?

      Mashahidi wa Yehova wakitoa msaada baada ya janga katika Jamhuri ya Dominika

      Jamhuri ya Dominika

      Wajitoleaji wakijenga upya Jumba la Ufalme nchini Japani

      Japani

      Shahidi wa Yehova akimfariji mtu baada ya janga nchini Haiti

      Haiti

      Janga linapotokea, mara moja Mashahidi wa Yehova hupanga kuwasaidia ndugu zao ambao wanahitaji msaada. Jitihada hizo huonyesha upendo wa kweli tulio nao. (Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:17, 18) Tunatoa msaada katika njia zipi?

      Tunatoa msaada wa kifedha. Njaa kali ilipotokea Yudea, Wakristo wa karne ya kwanza huko Antiokia waliwatumia ndugu zao wa kiroho msaada wa kifedha. (Matendo 11:27-30) Vivyo hivyo, tunaposikia kwamba ndugu zetu katika sehemu nyingine za dunia wanakabili hali ngumu, tunatuma fedha kupitia kutaniko letu ili kuwasaidia.—2 Wakorintho 8:13-15.

      Tunatoa huduma zinazohitajika. Wazee wanaotumikia katika eneo lililokumbwa na janga hujitahidi kuwasiliana na kila mshiriki wa kutaniko na kuhakikisha wote wako salama. Halmashauri ya kutoa misaada inaweza kuratibu kugawanywa kwa chakula, maji safi ya kunywa, nguo, makao, na matibabu. Mashahidi wengi wenye ujuzi hujitolea kusafiri kwa gharama zao wenyewe ili kushiriki katika kazi hiyo ya kutoa misaada au kurekebisha nyumba na Majumba ya Ufalme yaliyoharibiwa. Umoja tunaofurahia tukiwa tengenezo na uzoefu ambao tumepata kwa kufanya kazi pamoja, hutuwezesha kupanga mambo haraka uhitaji unapotokea. Ijapokuwa sisi huwasaidia “wale ambao ni ndugu zetu katika imani,” tunawasaidia wengine pia iwezekanapo, haidhuru dini yao.—Wagalatia 6:10.

      Tunatoa msaada wa kiroho na faraja. Waliokumbwa na janga mara nyingi huhitaji faraja. Katika nyakati hizo, tunatiwa nguvu na Yehova, “Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Tunafurahia kuzungumza pamoja na wale walio katika hali hizo kuhusu ahadi za Biblia zinazowahakikishia kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utakomesha majanga yote yanayosababisha uchungu na kuteseka.—Ufunuo 21:4.

      • Kwa nini Mashahidi huitikia haraka majanga yanapotokea?

      • Ni ujumbe gani wa kiroho wenye kufariji tunaoweza kuzungumzia na watu waliokabili hali ngumu?

  • Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara Ni Nani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 19

      Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara Ni Nani?

      Yesu akizungumza na wanafunzi wake
      Shahidi wa Yehova akijifunza machapisho ya Biblia

      Sote tunafaidika na chakula chetu cha kiroho

      Washiriki wawili wa baraza linaloongoza la Mashahidi wa Yehova

      Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alifanya mazungumzo ya faragha pamoja na wanafunzi wake wanne—Petro, Yakobo, Yohana, na Andrea. Yesu alipokuwa akitabiri ishara ya kuwapo kwake katika siku za mwisho, aliuliza swali muhimu: “Kwa kweli ni nani mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi asimamie watumishi wake wa nyumbani na kuwapa chakula chao kwa wakati unaofaa?” (Mathayo 24:3, 45; Marko 13:3, 4) Yesu alikuwa akiwahakikishia wanafunzi wake kwamba akiwa “bwana” wao, angewaweka rasmi wale ambao wangekuwa wakiwaandalia wafuasi wake chakula cha kiroho katika siku za mwisho. Watu hao wangekuwa akina nani?

      Ni kikundi kidogo cha wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta. “Mtumwa” huyo huhusianishwa hasa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Anawaandalia waabudu wenzake chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Tunamtegemea mtumwa huyo mwaminifu aendelee kutuandalia “kipimo [chetu] cha chakula kwa wakati unaofaa.”—Luka 12:42.

      Anasimamia nyumba ya Mungu. (1 Timotheo 3:15) Yesu alimpa mtumwa jukumu zito la kusimamia kazi ya sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Kazi hiyo inatia ndani kutunza mali zake, kuelekeza utendaji wa kuhubiri, na kutufundisha kupitia makutaniko. Kwa hiyo, ili kutuandalia kile tunachohitaji wakati tunapokihitaji, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anatuandalia chakula cha kiroho kupitia machapisho tunayotumia katika huduma, na pia kupitia mikutano na makusanyiko.

      Mtumwa huyo ni mwaminifu kwa kushikamana na kweli za Biblia na utume wa kuhubiri habari njema, naye ni mwenye busara katika kutunza kwa hekima mali za Kristo duniani. (Matendo 10:42) Yehova anabariki kazi ya mtumwa huyo kwa maandalizi mengi ya kiroho na ongezeko.—Isaya 60:22; 65:13.

      • Ni nani aliyewekwa na Yesu kuwalisha wanafunzi wake kiroho?

      • Ni katika njia gani mtumwa huyo ni mwaminifu na mwenye busara?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki