Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jinsi Machapisho Yetu Yanavyoandikwa na Kutafsiriwa
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 23

      Jinsi Machapisho Yetu Yanavyoandikwa na Kutafsiriwa

      Ndugu akifanya kazi kwenye idara ya Uandikaji, Marekani.

      Idara ya Uandikaji, Marekani

      Kikundi cha watafsiri nchini Korea Kusini

      Korea Kusini

      Mwanamume nchini Armenia akiwa ameshika kitabu kilichotafsiriwa na Mashahidi wa Yehova

      Armenia

      Msichana nchini Burundi akiwa ameshika kitabu kilichotafsiriwa na Mashahidi wa Yehova

      Burundi

      Mwanamke nchini Sri Lanka akiwa ameshika magazeti yaliyotafsiriwa na Mashahidi wa Yehova

      Sri Lanka

      Ili tufanikiwe kutangaza “habari njema” katika “kila taifa na kabila na lugha na watu,” tunachapisha vitabu na magazeti katika lugha zaidi ya 750. (Ufunuo 14:6) Kazi hiyo yote inafanywaje? Tuna waandishi katika nchi mbalimbali na vilevile vikundi vya watafsiri. Wote hao ni Mashahidi wa Yehova.

      Makala ya kwanza huandikwa katika Kiingereza. Baraza Linaloongoza husimamia kazi ya Halmashauri ya Uandikaji katika makao yetu makuu. Halmashauri hii huratibu kazi za waandikaji wanaoishi katika makao makuu na pia wale walio katika baadhi ya ofisi za tawi. Kwa sababu Halmashauri ya Uandikaji inatumia waandikaji wa nchi mbalimbali, machapisho yetu huwapendeza watu wa mataifa yote.

      Makala hutumwa kwa watafsiri. Baada ya kuandikwa na kuidhinishwa, makala hutumwa kwa vikundi vya watafsiri duniani kote. Watafsiri hao hujitahidi kuchagua “maneno sahihi ya kweli” yanayotafsiri maana kamili katika lugha yao.—Mhubiri 12:10.

      Kompyuta huharakisha kazi. Kompyuta haiwezi kufanya kazi zinazofanywa na waandikaji na watafsiri. Hata hivyo, kazi hiyo inaweza kuharakishwa kwa kutumia kamusi zilizo kwenye kompyuta, pamoja na vifaa vingine vya kufanyia utafiti. Mashahidi wa Yehova walibuni programu ya kompyuta inayoitwa Multilanguage Electronic Publishing System (MEPS). Programu hiyo huwezesha maandishi yaliyotafsiriwa katika mamia ya lugha kuunganishwa pamoja na picha, na kuyatayarisha kwa ajili ya uchapishaji.

      Kwa nini tunafanya kazi yote hiyo ya uchapishaji, hata katika lugha zinazozungumzwa na watu wachache tu? Kwa sababu ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:3, 4.

      • Machapisho yetu huandikwa jinsi gani?

      • Kwa nini tunatafsiri machapisho yetu katika lugha nyingi sana?

  • Kazi Yetu ya Ulimwenguni Pote Inagharimiwaje?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 24

      Kazi Yetu ya Ulimwenguni Pote Inagharimiwaje?

      Mtu akitoa mchango wa hiari
      Mashahidi wa Yehova wakihubiri

      Nepal

      Wajitoleaji wa ujenzi wa Majumba ya Ufalme nchini Togo

      Togo

      Wajitoleaji wakifanya kazi katika ofisi ya tawi ya Uingereza

      Uingereza

      Tengenezo letu linachapisha na kusambaza mamia ya mamilioni ya Biblia na machapisho mengine kila mwaka bila malipo. Tunajenga na kurekebisha Majumba ya Ufalme na ofisi za tawi. Tunatunza maelfu ya Wanabetheli na wamishonari, na pia kutoa msaada wakati wa majanga. Kwa hiyo, huenda ukajiuliza, ‘Kazi yote hii inagharimiwaje?’

      Hatukusanyi sadaka wala fungu la kumi. Ingawa gharama za kutegemeza kazi ya kuhubiri habari njema ni kubwa, hatuombi-ombi fedha. Zaidi ya miaka 100 iliyopita, toleo la pili la Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba tunaamini Yehova ndiye anayetusaidia na kwamba ‘hatutawaomba-omba watu au kuwasihi watutegemeze,’ nasi hatujawahi kufanya hivyo!—Mathayo 10:8.

      Kazi yetu inategemezwa kwa michango ya hiari. Watu wengi wanathamini kazi yetu ya kufundisha Biblia, nao hutoa michango ili kuiunga mkono. Mashahidi wenyewe wanatumia wakati, nguvu, fedha, na rasilimali zao nyingine ili kutimiza mapenzi ya Mungu duniani kote. (1 Mambo ya Nyakati 29:9) Kuna masanduku ya michango katika Majumba ya Ufalme na makusanyikoni, na wote wanaopenda wanaweza kutoa michango ya hiari. Pia, michango inaweza kutolewa kupitia tovuti yetu ya jw.org. Sehemu kubwa ya fedha tunazopokea ni michango ya watu wa kawaida ambao si matajiri, kama yule mjane maskini ambaye Yesu alimsifu. Mjane huyo alitumbukiza sarafu mbili ndogo kwenye sanduku la hazina la hekalu. (Luka 21:1-4) Kwa hiyo mtu yeyote anaweza “kuweka kando kitu fulani” kwa ukawaida ili atoe mchango “kama alivyoazimia moyoni mwake.”—1 Wakorintho 16:2; 2 Wakorintho 9:7.

      Tuna hakika kwamba Yehova ataendelea kuchochea mioyo ya wale wanaotaka ‘kumheshimu kwa vitu vyao vyenye thamani,’ kwa kuunga mkono kazi ya Ufalme, ili mapenzi yake yatendeke.—Methali 3:9.

      • Ni nini kinachofanya tengenezo letu liwe tofauti na dini nyinginezo?

      • Michango inatumika jinsi gani?

  • Majumba ya Ufalme Yanajengwa Jinsi Gani na Kwa Nini?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 25

      Majumba ya Ufalme Yanajengwa Jinsi Gani na Kwa Nini?

      Wajitoleaji wa Ujenzi wa Majumba ya Ufalme Nchini Bolivia

      Bolivia

      Jumba la Ufalme nchini Nigeria kabla ya kujengwa upya
      umba la Ufalme nchini Nigeria baada ya kujengwa upya

      Nigeria, kabla na baada

      Jumba la Ufalme likijengwa nchini Tahiti

      Tahiti

      Kama jina lenyewe linavyoonyesha, fundisho kuu la Biblia katika majumba yetu ni Ufalme wa Mungu. Hicho ndicho kilichokuwa kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu.—Luka 8:1.

      Ni mahali pa ibada ya kweli katika eneo. Hapo ndipo kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme huratibiwa. (Mathayo 24:14) Majumba ya Ufalme yanatofautiana kwa ukubwa na muundo, na hayana madoido. Majumba mengi hutumiwa na zaidi ya kutaniko moja. Ili kwenda sambamba na ongezeko la idadi ya makutaniko, katika miaka ya karibuni tumejenga makumi ya maelfu ya Majumba ya Ufalme (wastani wa majumba matano kila siku). Jambo hilo limewezekanaje?—Mathayo 19:26.

      Yanajengwa kwa kutegemea michango. Michango hutumwa kwenye ofisi ya tawi ili makutaniko yanayohitaji kujenga au kukarabati Jumba la Ufalme yaweze kuitumia.

      Hujengwa na wajitoleaji wa matabaka mbalimbali ambao hawalipwi mshahara. Katika nchi nyingi Vikundi vya Ujenzi wa Majumba ya Ufalme vimeanzishwa. Vikundi vya watumishi na wajitoleaji wa ujenzi husafiri kutoka kutaniko moja hadi jingine na wakati mwingine kwenda kwenye maeneo ambayo ni vigumu kuyafikia, ili kusaidia makutaniko kujenga Majumba ya Ufalme. Katika nchi nyingine, Mashahidi wanaostahili husimamia ujenzi na ukarabati wa Majumba ya Ufalme katika eneo walilogawiwa. Ingawa wajitoleaji wengi wenye ustadi husaidia wakati wa ujenzi, washiriki wa kutaniko hujitolea kwa wingi. Roho ya Yehova pamoja na jitihada za nafsi yote za watu wake hufanikisha kazi hiyo.—Zaburi 127:1; Wakolosai 3:23.

      • Kwa nini mahali petu pa ibada panaitwa Jumba la Ufalme?

      • Inawezekanaje kujenga Majumba ya Ufalme Ulimwenguni pote?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki