-
Tunaweza Kusaidiaje Kudumisha Jumba Letu la Ufalme?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 26
Tunaweza Kusaidiaje Kudumisha Jumba Letu la Ufalme?
Estonia
Zimbabwe
Mongolia
Puerto Riko
Kila Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova linawakilisha jina takatifu la Mungu. Kwa hiyo, ni pendeleo na ni sehemu muhimu ya ibada yetu takatifu kushiriki kulidumisha likiwa safi, nadhifu, na katika hali nzuri. Wote wanaweza kushiriki.
Jitolee kufanya usafi baada ya mikutano. Kila baada ya mkutano, ndugu na dada hujitolea kwa furaha kufanya usafi kwenye Jumba la Ufalme. Mara moja kila juma, usafi wa kina hufanywa. Mzee au mtumishi wa huduma hutoa maelekezo, kwa kawaida akifuata orodha ya mambo yanayopaswa kufanywa. Ikitegemea uhitaji, watu hujitolea kufagia, kusafisha sakafu, kupangusa vumbi, kupanga viti, kusafisha vyoo, kusafisha madirisha na vioo, kutupa takataka, au kufanya usafi wa nje. Angalau mara moja kwa mwaka, siku maalumu hutengwa ya kufanya usafi mkubwa. Tunapowahusisha watoto wetu kufanya usafi, tunawafundisha kuheshimu mahali petu pa ibada.—Mhubiri 5:1.
Jitolee kufanya marekebisho yanapohitajika. Kila mwaka Majumba ya Ufalme hukaguliwa nje na ndani. Kwa kutegemea ukaguzi huo marekebisho hufanywa ili kuepuka gharama zisizo za lazima baadaye. (2 Mambo ya Nyakati 24:13; 34:10) Jumba la Ufalme safi na lililotunzwa vizuri ni mahali panapofaa pa kumwabudia Mungu wetu. Tunaposhiriki katika kazi hii, tunaonyesha tunampenda Yehova na pia mahali petu pa ibada. (Zaburi 122:1) Jambo hilo linawavutia watu wengine pia katika eneo.—2 Wakorintho 6:3.
Kwa nini hatupaswi kupuuza mahali petu pa ibada?
Ni mipango gani ambayo hufanywa ili kudumisha usafi katika Jumba la Ufalme?
-
-
Maktaba ya Jumba la Ufalme Inaweza Kutunufaisha Jinsi Gani?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 27
Maktaba ya Jumba la Ufalme Inaweza Kutunufaisha Jinsi Gani?
Israeli
Jamhuri ya Cheki
Benin
Visiwa vya Cayman
Je, ungependa kufanya utafiti ili uielewe Biblia vizuri zaidi? Je, ungependa kujua mengi zaidi kuhusu andiko, mtu, eneo, au jambo lolote katika Biblia? Au, je, ungependa kujua ikiwa Neno la Mungu linaweza kukusaidia kushughulikia jambo fulani linalokuhangaisha? Ikiwa ndivyo, unaweza kutumia maktaba ya Jumba la Ufalme.
Kuna vifaa vya utafiti. Labda huna machapisho yote ya Biblia ya Mashahidi wa Yehova katika lugha yako. Hata hivyo, maktaba ya Jumba la Ufalme ina machapisho mengi ya karibuni. Huenda pia kukawa na tafsiri mbalimbali za Biblia, kamusi, na vitabu vya marejeo. Unaweza kutumia maktaba hiyo kabla au baada ya mikutano. Ikiwa kuna kompyuta huenda ikawa na programu ya Watchtower Library. Programu hiyo ina machapisho mengi na ni rahisi kuitumia kufanya utafiti kuhusu jambo lolote, neno, au hata andiko la Biblia.
Inasaidia wanafunzi katika Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo. Unaweza kutumia maktaba ya Jumba la Ufalme unapotayarisha migawo yako. Mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ndiye msimamizi wa maktaba. Yeye ana jukumu la kuhakikisha machapisho mapya yanawekwa na kupangwa vizuri. Yeye au yule anayejifunza Biblia pamoja nawe anaweza kukuonyesha namna ya kutafuta habari unayohitaji. Hata hivyo, hatupaswi kuchukua vitabu vya maktaba ya Jumba la Ufalme na kwenda navyo. Pia, tunapaswa kutunza vitabu hivyo na kuepuka kuvichora au kuvitia alama yoyote.
Biblia inaeleza kwamba ili “[tupate] ujuzi kumhusu Mungu” ni lazima tuutafute kama tunavyotafuta “hazina zilizofichika.” (Methali 2:1-5) Maktaba ya Jumba la Ufalme inaweza kukusaidia kutimiza jambo hilo.
Ni vifaa gani vya utafiti vinavyopatikana katika maktaba ya Jumba la Ufalme?
Ni nani anayeweza kukusaidia kutumia maktaba hiyo vizuri?
-
-
Ni Habari Gani Zinazopatikana Kwenye Tovuti Yetu?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 28
Ni Habari Gani Zinazopatikana Kwenye Tovuti Yetu?
Ufaransa
Poland
Urusi
Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake hivi: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili waone matendo yenu mema na kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:16) Hiyo ndiyo sababu tunatumia teknolojia ya kisasa, kutia ndani Intaneti. Tovuti yetu, jw.org, ni kituo rasmi chenye taarifa kuhusu imani na utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Mambo hayo yanatia ndani nini?
Majibu ya Biblia ya maswali ambayo huulizwa kwa ukawaida. Unaweza kupata majibu ya maswali muhimu ambayo watu hujiuliza. Kwa mfano trakti, Je, Kuteseka Kutaisha? na Je, Kweli Wafu Wataishi Tena? zinapatikana kwenye mtandao katika lugha zaidi ya 600. Pia unaweza kupata Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha zaidi ya 130 pamoja na vifaa vya kukusaidia kujifunza Biblia, kutia ndani kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? na matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Machapisho mengi yanaweza kusikilizwa au kusomwa kwenye mtandao au hata kupakuliwa kama MP3, PDF, au EPUB. Hata unaweza kuchapisha kurasa kadhaa za kusoma na mtu anayependezwa katika lugha yake! Video zinapatikana katika lugha nyingi za ishara. Pia, unaweza kupakua drama za Biblia na muziki mtamu unaoweza kusikiliza unapopumzika.
Habari za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova. Pia kwenye tovuti kuna habari za karibuni kuhusu kazi yetu ya ulimwenguni pote, matukio yanayowahusu Mashahidi wa Yehova, na jitihada zetu za kutoa misaada. Unaweza kupata taarifa kuhusu makusanyiko yajayo na anwani za ofisi zetu za tawi.
Kupitia njia hizi tunaangaza nuru ya kweli kwa mapana na marefu. Watu wa kila bara, kutia ndani Antaktika, wanafaidika. Tunasali “neno la Yehova lizidi kuenea upesi” duniani kote kwa utukufu wa Mungu.—2 Wathesalonike 3:1.
Tovuti ya jw.org inawasaidiaje watu wengi kujifunza Biblia?
Ungependa kuchunguza nini katika tovuti yetu?
-