Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb13 kur. 42-77
  • Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote
  • 2013 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
2013 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb13 kur. 42-77

Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote
[Picha katika ukurasa wa 42, 43]

ULIMWENGUNI POTE

  • IDADI YA NCHI 239

  • IDADI YA WAHUBIRI 7,782,346

  • JUMLA YA SAA ZILIZOTUMIWA KATIKA HUDUMA YA SHAMBAN1, 748,697,447

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 8,759,988

AFRIKA

  • IDADI YA NCHI 58

  • IDADI YA WATU 968,989,710

  • IDADI YA WAHUBIRI 1,312,429

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 2,999,639

Hakutaka Kutoa Mimba

Jijini Addis Ababa, mji mkuu wa Ethiopia, kulikuwa na mwanamke mwenye duka anayeitwa Saba. Siku moja, dada wawili walimfikia wakiwa na gazeti la Amkeni! ambalo lilikuwa likizungumzia kuhusu kutoa mimba. Saba aliwakaribisha ndani na huku akitokwa na machozi aliwaambia kwamba alikuwa akifikiria kutoa mimba. Walipokuwa wakizungumzia habari hiyo, wote watatu waliguswa sana na hisia hivi kwamba wakaanza kulia. Siku hiyo, Saba aliamua kutotoa mimba na kwa uthabiti akamwambia mume wake kwa nini ameamua kufikia uamuzi huo. Baada ya muda, akajifungua mtoto mrembo wa kike. Pia, alianza kujifunza Biblia na akabatizwa. Sasa Saba ni painia mwenye furaha. Mume wake pia alijifunza na kuwa ndugu yetu, na mnamo Aprili 2012, watoto wao wengine wawili walibatizwa pia.

‘Je, Itawezekana Kuzungumza Naye?’

[Picha katika ukurasa wa 44]

Kaokoland, Namibia: Machapisho ya kujifunzia Biblia yanawavutia watu wa kila rika. Broshua Msikilize Mungu Uishi Milele sasa inapatikana katika lugha 452!

Mwangalizi wa mzunguko nchini Ethiopia alikuwa akihubiri nyumba kwa nyumba akiwa pamoja na mhubiri mmoja. Katika nyumba fulani, walimkuta msichana wa kazi na kumuuliza ikiwa wangeweza kuzungumza na baba mwenye nyumba. Alipojibu kwamba hilo halingewezekana, walimuuliza ikiwa wangeweza kumpatia machapisho fulani ampelekee. Aliingia ndani ili kumuuliza, akarudi, na akasema kwamba alitaka kuyaona kwanza.

Hivyo akina ndugu walimpa magazeti ili akamwonyeshe. Baada ya dakika chache, alirudi na kusema kwamba alikubali kuyasoma. Kisha mmoja wa ndugu hao akasema,“Ikiwa hawezi kutoka nje, je, tunaweza kuingia ndani ili kuzungumza naye?” Kwa mara nyingine tena, msichana huyo akaenda kumuuliza. Wakati huu alikaa muda mrefu kidogo kuliko ilivyokuwa mwanzoni, na akina ndugu walikuwa wakijiuliza ikiwa angerudi au la. Hatimaye alirudi na kuwakaribisha ndani. Sasa akina ndugu wakaelewa kuwa mwenye nyumba, Yirgu, alikuwa mzee ambaye kwa miaka kumi alikuwa amelala kitandani, hakuweza kutoka kitandani au hata kukaa. Sababu iliyomfanya mfanyakazi huyo achukue muda mrefu ni kwamba alikuwa akimsaidia kuvaa na kusafisha chumba.

Akina ndugu wakamhubiria habari njema. Akiwa amevutiwa na mambo aliyosikia, Yirgu akakubali kujifunza Biblia. Kadiri funzo lilivyoendelea, ndivyo afya yake ilivyozidi kuimarika. Baada ya muda fulani, aliweza kutoka kitandani na kutembea akitumia kiti cha magurudumu. Punde si punde akaanza kuhudhuria mikutano na hivi karibuni alibatizwa katika kusanyiko la wilaya.

Vitabu vya Kanisa la Baba Yake

Calvin, ambaye anaishi nchini Zimbabwe, alikuwa na umri wa miaka minne baba yake alipokufa, akimwachia tu mkoba uliokuwa na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote, Buku la 1. “Shikamana na kanisa la vitabu hivi,” alimwambia Calvin. “Linafundisha kweli.”

Mama yake alipokufa, Calvin akaenda kuishi na nyanya yake. Kwa miaka tisa Calvin alikataa kwenda kwenye kanisa la nyanya yake, akisisitiza kwamba siku moja atalipata “kanisa” la vitabu ambavyo baba yake alimpatia.

Siku moja, nyanya ya mvulana huyo alikutana na dada yetu. Bila kujua kwamba alikuwa Shahidi, akamweleza dada huyo kwamba ana mjukuu mkaidi ambaye anakataa kwenda kanisani. Badala yake, kila siku ya Jumapili husoma kitabu ambacho baba yake alimwachia. Dada huyo akamuuliza jina la kitabu hicho. Nyanya huyo akasema anafikiri ni “moja ya vitabu vya kijinga vya Mashahidi wa Yehova.”

Dada huyo akasema angependa kuonana na mvulana huyo. Calvin alifurahi sana walipokutana. Bila kuchelewa, dada alianza kujifunza naye Biblia, akitumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? na mara moja Calvin akaanza kuhudhuria mikutano licha ya upinzani mkali kutoka kwa nyanya yake. Ameazimia kushikamana na kweli na anatazamia kwa hamu wakati ujao kwenye ufufuo ambako anatumaini kwamba ataungana na mama yake na baba yake. Calvin alibatizwa mnamo Agosti 2012.

“Mungu Unayemtumikia Ni Mwenye Nguvu”

Caro anaishi nchini Uganda. Mwezi mmoja tu baada ya kuanza kujifunza Biblia, Martin, mume wake, ambaye alikuwa mchawi, alianza kumpinga vikali. “Mizimu ya mababu haiingii ndani ya nyumba kwa sababu ya vitabu vyako,” akadai. Alimtendea vibaya na akamtishia kumuua ikiwa ataendelea kujifunza Biblia. Pia, akaacha kuitunza familia yake. Caro alibaki mtulivu, na kuitunza familia yake kwa chakula alicholima kwenye bustani yake, na akaendelea kutwaa ujuzi sahihi. Baadaye, ilipokuwa wazi kwamba uhai wake umo hatarini, Caro akakimbia. Alihangaika ili kujitegemeza. Hata hivyo, aliposikia kwamba watoto ni wagonjwa, alichukua pesa kidogo alizopata na kuwanunulia dawa.

Baada ya muda fulani, Caro alipigiwa simu na mume wake. “Ninataka urudi nyumbani,” akasema. “Nimeona kwamba Mungu unayemtumikia ana nguvu na amekuwa pamoja nawe. Ninataka uwaambie watu wale wanaokufundisha waje wanifundishe mimi pia. Kwa kweli, ninataka kubadili maisha yangu.” Martin alikuwa ameazimia. Sasa, familia hiyo ina umoja na furaha. Wote wawili Martin na Caro walibatizwa kwenye kusanyiko mwezi wa Agosti 2012.

Mhubiri Pekee Katika Mji wa Mbali

David alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova alipokuwa akiishi katika mji wa mbali kutoka kijijini kwao nchini Kenya. Hata hivyo, muda si muda, aliamua kurudi kijijini kwao Lokichar, ambacho kipo eneo la mbali kaskazini-magharibi mwa Kenya. Kutaniko lililokuwa karibu lilikuwa umbali wa kilometa 165 hivi katika mji wa Lodwar. Kwa miaka minne David hakuweza kuwasiliana vizuri na Mashahidi, hata hivyo, aliwahubiria majirani na watu wa ukoo, akiwaambia mambo aliyojifunza katika kipindi cha muda mfupi aliojifunza Biblia. Wengine waliitikia vizuri, na muda si muda David alikuwa akiongoza mafunzo kadhaa ya Biblia. Mnamo mwaka wa 2007 aliwasiliana na ndugu mjini Lodwar na akaendelea na funzo lake, akisafikiri mara mbili kwa mwezi akitumia pikipiki, teksi, na magari madogo ya abiria.

Kadiri ujuzi wake ulivyoongezeka, ndivyo David alivyoongeza bidii yake katika huduma. Akiwa bado hajabatizwa, alijenga “Jumba la Ufalme” la matope likiwa limeezekwa kwa nyasi karibu na nyumba yake, ambamo aliongoza mikutano na watu waliokuwa wakipendezwa. Hata hivyo, si kila mtu kijijini alifurahia kazi yake ya kuhubiri, na kwa miaka miwili alitukanwa na kupigwa. Katika pindi moja, wanakijiji fulani walimpiga bila sababu, wakimtuhumu kwa kuanzisha “ibada ya Shetani” kijijini mwao. Hata hivyo, baada ya David kuomba msaada wa kiongozi wa serikali, vurugu hizo zilikoma, na David akaendelea kuhubiri. “Kweli ni jambo muhimu zaidi katika maisha yangu,” akasema David. “Hata upinzani uwe mkubwa kadiri gani, hauwezi kunizuia.”

Mnamo 2009, David alibatizwa, na sasa anatumikia akiwa mtumishi wa huduma na painia wa kawaida. Yeye pamoja na mwanae mwenye umri wa miaka 15 ndio wahubiri pekee katika eneo hilo, lakini mnamo Aprili 2012, wanakijiji wapatao 60 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo, uliofanywa katika jumba la muda karibu na nyumba ya David.

“Tumia Maandiko Kuthibitisha Kwamba Amekosea”

Janet, dada painia wa kawaida nchini Ghana, alikuwa akisoma kitabu Biblia Inafundisha akiwa katika safari ndefu ya basi. Mhubiri mmoja wa dini aliingia ndani ya basi, akahubiri, kisha akawaomba abiria waanze kutoa sadaka kwa ajili ya huduma aliyoitoa. Janet akamwambia: “Unasema kwamba Yesu yuko sawa na Mungu. Basi ni nani aliyezungumza na Yesu alipokuwa akibatizwa?”

Mhubiri yule akasema,“Hilo ni fumbo.”

Janet akafungua sura ya 4 ya kitabu Biblia Inafundisha, akachagua maandiko kadhaa, na akawaomba abiria fulani wasome maandiko hayo. Akaeleza tofauti iliyopo kati ya Yesu na Mungu Mweza Yote, Yehova.

“Wewe ni mchawi,” akasema yule mhubiri.

Abiria waliposikia jambo hilo, wakaanza kumtetea Janet, wakisema, “Unapaswa kutumia Maandiko kuthibitisha kwamba amekosea badala ya kumwita mchawi.” Akiwa amekasirika, mhubiri yule akashuka kwenye kituo kilichofuata. Mwanamke mmoja kijana aliyekuwa amekaa karibu na Janet akamwambia hivi: “Nilifikiri kwamba Yehova ni jina la jengo la kanisa la Mashahidi. Sikujua kwamba ni jina la Mungu hadi ulipokuwa ukizungumza na yule mhubiri.”

Mazungumzo yakaendelea, na Janet akachukua namba ya simu ya yule mwanamke na akamwahidi kwamba atampigia. Mwanamke huyo alipofika nyumbani, akamsimulia nyanya yake habari hiyo. Nyanya yake pia alishangaa kusikia kwamba jina la Mungu ni Yehova. Baadaye Janet akapanga Mashahidi fulani waendelee kuzungumza na yule mwanamke na nyanya yake. Sasa wote wawili wanahudhuria mikutano.

AMERIKA

  • IDADI YA NCHI 57

  • IDADI YA WATU 946,087,916

  • IDADI YA WAHUBIRI 3,861,145

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 4,196,922

Aliipata Kweli Mahali Ambapo Hakutarajia

Walinzi wa gereza nchini Bolivia walikuwa wakipambana na Andrea mwenye umri wa miaka 20 ndani ya ua wa gereza huku Andrea akitukana matusi na kutoa vitisho. Kwa sababu alikuwa mkorofi na mwenye nguvu, watu walimwogopa. Leidy, ambaye ni Shahidi wa Yehova alikuwa amefungwa kwa sababu ya kushtakiwa kwa uwongo, hakumwogopa Andrea lakini alimwonea huruma. Kila asubuhi Leidy alikuwa na kawaida ya kusoma kwa sauti wimbo kutoka katika kitabu chetu cha nyimbo. Andrea aliposikia, akauliza, “Je, wewe ni Shahidi wa Yehova?”

[Picha katika ukurasa wa 50]

Peru: Kuwahubiria wakulima wanaoishi juu ya Bonde la Utcubamba

Leidy alipomjibu ndiyo, Andrea akasema: “Mama yangu ni Shahidi wa Yehova, na nilikuwa nikihudhuria naye mikutano. Alinifundisha Biblia.” Andrea akaanza kulia. Siku kadhaa zilizofuata, Leidy alikuwa na mazungumzo ya kiroho yenye kina na Andrea, na wakati wa kusikilizwa kwa kesi ya Andrea ulipofika, walisali pamoja ili kuomba msaada na mwongozo wa Yehova. Andrea aliachiliwa na akaendelea kujifunza kumhusu Yehova. Haraka akastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, na sasa anajiandaa kwa ajili ya ubatizo.

Leidy alitumia vizuri kufungwa kwake bila hatia na kabla hajatoka gerezani alikuwa ameanzisha mafunzo ya Biblia 21. Sasa hurudi gerezani siku tatu kwa wiki ili kufuatilia upendezi.

Walichochewa na Tovuti ya www.jw.org

Wenzi wa ndoa waliovaa vizuri wakiwa na watoto wao wawili wadogo walipoingia kwenye Jumba la Ufalme nchini Kanada Jumapili moja mwaka wa 2011, kila mmoja kutanikoni alifikiri kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova waliowatembelea kutoka jiji lingine. Dominic, mtumishi wa huduma katika kutaniko hilo, na mwanaume yule aliyetembelea walikumbukana mara moja. Dominic alikuwa amejifunza Biblia na mwanaume huyo miaka 17 iliyopita. Kwa muda wa miaka miwili iliyopita, Marc-André na mke wake, Josée, wamekuwa wakipakua magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika Tovuti ya www.jw.org na wakaonelea kwamba familia nzima inapaswa kwenda Jumba la Ufalme. Funzo la Biblia lilianzishwa mara moja, na familia hiyo ikaanza kuhudhuria mikutano yote. Baada ya miezi miwili tu tangu waanze kujifunza Biblia, familia hiyo ilianza kuwa na jioni ya Ibada ya Familia. Wanaendelea kufanya maendeleo mazuri, na Josée alitoa hotuba yake ya kwanza katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi mwezi Mei 2012.

‘Alinipatia Chakula Chake cha Mchana na Kofia’

Alipokuwa akihudhuria kusanyiko la wilaya mwaka wa 2010 nchini Chile, Marcelo mwenye umri wa miaka kumi alimwona mwanaume mmoja wa makamo aliyekaa kando yake ambaye hakuwa na chapisho lolote.

“Mtu huyu hana Biblia,” akamnong’oneza mama yake.

“Tumia hiyo yako kusoma naye,” mama yake akamjibu. Hivyo, Marcelo akamsogelea mwanaume huyo anayeitwa Victor na kusoma Biblia yake pamoja naye akifungua maandiko yote yaliyotajwa. Kipindi cha pumziko kilipoanza, Marcelo alimgeukia mama yake na kumwambia,“Hana chakula cha mchana.” Mama yake akapendekeza kwamba ashiriki chakula chake pamoja na Victor. Hivyo, Marcelo akampa mwanaume huyo mkate na kikombe cha chai. Victor alipokuwa akila chakula cha mchana, Marcelo alikuwa akimwonyesha maandiko yote ya Biblia aliyokuwa akiyakumbuka.

Kufikia alasiri, jua lilikuwa kali sana. Marcelo akamgeukia tena mama yake na kusema, “Hana kofia.”

Mama yake akamjibu, “Mpe kofia yako.” Hivyo, akampa. Baada ya programu kuisha, Marcelo na Victor wakaagana.

Katika kusanyiko la wilaya mwaka uliofuata, Marcelo aliangalia huku na huku ili kuona ikiwa Victor amekuja. Alifurahi sana alipomwona, na wakati huu alikuwa amevaa tai! Victor alipomwona Marcelo, akatangaza hivi: “Nipo hapa leo kwa sababu ya kijana huyu. Mwaka jana, nilipewa mwaliko wa kuhudhuria kusanyiko, na nilikuja. Kijana huyu alishiriki pamoja nami Biblia yake, chakula chake cha mchana, na alinipa kofia yake. Sasa ninajifunza Biblia!” Victor, sasa ni mhubiri ambaye hajabatizwa.

Mwandishi wa Habari Ampongeza

Katika makala yake, mwandishi maarufu sana nchini Venezuela alieleza mambo yaliyompata alipohitaji huduma za mteja katika kampuni ya simu ya taifa ambako alikuwa amepiga ili asaidiwe jambo fulani la kiufundi. Mfanyakazi aliyepokea alimjibu kwa ufupi na bila adabu, kwa hiyo hakupata msaada wowote. Alipopiga mara ya pili alijibiwa na kijana aliyejitambulisha kwa jina la “Misael” ambaye alijibu maswali yake kwa adabu na kwa ufanisi. Mwanamke huyo aliandika hivi: “Fadhili, heshima, utayari wa kusaidia, na roho ya ushirikiano ambayo kijana huyo alionyesha muda wote wa mazungumzo yetu kwenye simu yalikuwa mambo ya pekee sana. Kwa sababu ya msaada wake, niliweza kutatua tatizo na pia nilijifunza jinsi ya kushughulikia jambo kama hilo wakati ujao.”

Mwanamke huyo alipompongeza, kijana huyo alieleza kwamba yeye akiwa Shahidi wa Yehova, anajitahidi kuwatendea jirani zake katika njia ambayo Yesu alifundisha. Mwandishi huyo akaomba kuzungumza na msimamizi wa Misael na akampongeza mfanyakazi wake kwa huduma bora anayotoa. Katika makala yake, aliandika kwamba Misael ni Mvenezuela na Shahidi wa Yehova mwenye mfano mzuri wa kuigwa. Alimalizia makala yake kwa kusema: “Tunahitaji watu kama Misael katika maeneo yote ambayo huduma za jamii hutolewa.”

“Msiwe Wakaidi!”

[Picha katika ukurasa wa 54]

Mexico City, Mexico: Mengi kati ya mafunzo ya Biblia zaidi ya milioni moja nchini Mexico yalianzishwa kwa sababu ya mahubiri ya barabarani

Gabriela mwenye umri wa miaka kumi na tano, ambaye ni kiziwi, alifurahi sana kubatizwa kwenye kusanyiko la wilaya la lugha ya ishara lililofanywa Oktoba 2011 nchini Ekuado. Alisisimka sana hivi kwamba aliporudi shuleni siku ya Jumatatu, alimwomba mwalimu wake ikiwa angeweza kutoa tangazo fupi kwa wanafunzi wenzake. Mwalimu huyo alikubali, kisha Gabriela akasimama mbele ya darasa na kwa shauku akaanza kusema kwa lugha ya ishara: “Ningependa kuwatangazia kwamba Ijumaa, Jumamosi, na Jumapili iliyopita, nilikuwa kwenye kusanyiko ambako nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Pia, ningependa kuwaambia kwamba tunaishi karibu na mwisho wa mfumo huu wa mambo. Wakati uliobaki ni mfupi! Ni vizuri mfanye mabadiliko haraka. Kwa hiyo msiwe wakaidi. Mwogopeni Mungu!” Wanafunzi wenzake walivutiwa sana.

Baadaye siku hiyo, wakati wa chakula cha mchana, Katty, Shahidi kiziwi asiyetenda, alimwendea Gabriela na kumuuliza kuhusu kusanyiko. Gabriela alijibu hivi kwa unyofu: “Lilikuwa zuri! Hata hivyo, sasa nikiwa Shahidi ambaye amebatizwa, ninataka kubaki mwaminifu kwa Yehova. Hivyo lazima nikujulishe kwamba siwezi kuendelea kuwa rafiki yako kwa sababu wewe unaishi maisha mapotovu. Nikiendelea kuwa rafiki yako nitaathiri uhusiano wangu pamoja na Mungu. Unahitaji kubadilika. Ni muhimu usali kwa Yehova na pia kuzungumza na wazee. Najua unaweza kufanya mabadiliko na kuwa mtu mzuri.” Unyofu wa Gabriela na himizo lake lenye upendo vilimsaidia Katty, kwani alizungumza na wazee, akapata msaada wa kiroho, na akaanza tena kushiriki katika huduma.

Alitumia Kompyuta ya Mwalimu Wake

Wanafunzi wote darasani walikuwa wakimuuliza dada mwenye umri wa miaka 16 nchini Marekani kuhusu dini yake, lakini hakuwa na chapisho lolote, wala Biblia. Akitaka kutumia maandiko kujibu maswali ya wanafunzi wenzake, aliazima kompyuta ya mwalimu wake na kufungua Tovuti ya www.jw.org. Si tu kwamba alijibu maswali yao yote bali pia aliwaonyesha jinsi ya kutumia tovuti hiyo. Aliwaeleza kwamba wakati wowote wakiwa na maswali ya Biblia na hakuna Mashahidi karibu wanaoweza kuwasaidia, wanaweza kutembelea Tovuti hiyo ili kupata majibu. Kadiri wiki ilivyosonga, alitambua kwamba wanafunzi wenzake walikuwa na maswali machache kuliko awali. Alipowauliza kwa nini, baadhi yao walijibu kwamba wamekuwa wakifungua kwa ukawaida Tovuti hiyo kupitia simu zao. Hata mwalimu wake amekuwa akifanya hivyo!

ASIA NA MASHARIKI YA KATI

  • IDADI YA NCHI 48

  • IDADI YA WATU 4,222,869,785

  • IDADI YA WAHUBIRI 674,608

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 662,736

Mapigano Kati ya Vijiji Yaepukwa

Wakiwa njiani kuelekea msibani, kikundi cha Mashahidi kilisafiri kupitia kijiji fulani kidogo nchini Indonesia. Painia mmoja aliwaona vijana fulani kandokando ya barabara. Alizungumza nao na kuwaachia broshua Msikilize Mungu Uishi Milele. Baada ya muda fulani, dada mmoja alipita mahali hapo akiwa anarudi nyumbani. Mwanaume fulani aliyekuwa ameshika mkononi broshua Sikiliza Uishi, akamkaribia na kumshukuru kwa kuwapa watoto wake broshua hiyo. “Broshua hii imeokoa maisha ya watoto wangu!” akamwambia. Dada huyo ambaye hakujua mwanzo wa habari hiyo, akauliza ni nini kilichokuwa kimetokea. Baba huyo akaeleza kwamba vijana hao walikuwa wamepanga kuvamia kijiji fulani. Kulingana na desturi ya eneo hilo, walidhamiria kulipiza kisasi kwa sababu rafiki yao alipigwa. Hata hivyo, wavulana hao waliposoma broshua hiyo, wakajifunza kwamba watu wanaopigana na wengine hawatarithi Paradiso inayokuja. Kwa hiyo wakatulia, wakaachana na mpango wao, na kurudi nyumbani. Mapigano hatari ambayo yangetokea yaliepukwa kwa sababu ya ujumbe wa Biblia ulio kwenye broshua hiyo.

Mvaaji wa Mavazi ya Jinsia Nyingine Abadilika

[Picha katika ukurasa wa 56]

Shau Kei Wan, Hong Kong: Kumhubiria mwanamke kijana sokoni

Rek alilelewa kwenye familia ya kawaida nchini Kambodia, hata hivyo tangu utotoni, yeye na mdogo wake pacha walijihisi kuwa wao ni wa jinsia ya kike. Walichezea wanasesere na walipenda kuvaa nguo za kike. Mama yao alichanganyikiwa na kuaibika na hakujua jinsi ambavyo angewazuia. Waliondoka kwenda shuleni wakiwa wamevaa kama wavulana lakini wangevaa nguo za kike mara moja wakifika shuleni. Walipofika umri wa miaka 16, mapacha hao walijiunga na mashindano ya urembo kwa ajili ya watu wanaovaa mavazi ya jinsia nyingine na wafanyabiashara ya burudani waliona kipaji chao. Jambo hilo lilifanya waonyeshwe katika vipindi vya televisheni na vya ucheshi. Baada ya muda mfupi, Rek akawa mgoni wa jinsia moja na akawa akishirikiana na watu wengine wanaovaa mavazi ya jinsia nyingine.

Mama ya Rek akaanza kwenda kanisani na kumlazimisha Rek aende pamoja naye. Ingawa alikubali kuvaa nguo za kiume, alikataa kukata nywele zake ndefu. Mara kwa mara kasisi alitoa maneno ya kumdhalilisha Rek na kudhihaki mtindo wake wa maisha. Licha ya hayo, Rek alifikiri kwamba angejifunza Biblia katika kanisa hilo. Wiki ya kwanza, aliamka alfajiri na mapema na kuendesha baiskeli umbali wa kilomita kadhaa ili kwenda kanisani, hata hivyo kasisi akamwambia kwamba hangeweza kumfundisha. Rek aliudhika sana kasisi huyo alipokosa kabisa kufika wiki ya pili.

Hata hivyo, Rek alipofika nyumbani, pacha wake alimwambia kwamba kuna mwanamke fulani aliwatembelea na alikuwa tayari kujifunza nao Biblia bila malipo. Alikuwa amewaachia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Mapacha hao wakaanza kujifunza Biblia pamoja na dada huyo na mume wake. Baada ya miezi sita, mdogo wa Rek alihisi kwamba hayuko tayari kubadili mtindo wake wa maisha, hivyo akaacha kujifunza. Kwa upande mwingine, Rek, aliguswa sana na andiko la 1 Wakorintho 6:9, 10 na aliona waziwazi ni jambo gani alilopaswa kufanya. Kwa kujifunza kwa bidii, kusoma Biblia, sala, na kuhudhuria mikutano, aliweza kusafisha maisha yake. Mama ya Rek pia anajifunza na anafanya maendeleo mazuri. Rek alipobatizwa, mama yake alisema hivi huku akitokwa na machozi, “Nimefurahi sana kuona mwanangu anabatizwa akiwa mwanaume.” Sasa Rek anatumikia akiwa painia wa kawaida.

Mtu Anayewasiliana na Pepo Abadili Njia Zake

Or-Ya alikuwa mtu mwenye mazoea ya kuwasiliana na pepo, mganga wa kienyeji, mshauri, na mbashiri. Wenzi wa ndoa ambao ni mapainia wa pekee wanaotumikia Haifa, nchini Israeli, walikutana naye wakiwa katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Aliwasalimia kwa maneno haya: “Ikiwa ni kuhusu Mungu, ingieni ndani!” Nyumba yake ilikuwa imejaa vitu vinavyohusiana na kuwasiliana na pepo na mafumbo. Mwanamke huyo alidai kwamba alipokea jumbe kutoka kwa Mungu, baadhi ya jumbe hizo alipokea kupitia “roho” ya rabi aliyekufa.

Alivutiwa sana na mpango wa kujifunza Biblia kupitia kitabu Biblia Inafundisha. Siku mbili tu kabla ya wenzi hao wa ndoa kufika nyumbani kwake, mwanamke huyo alikuwa amesali kwa Mungu akimwomba amtume mtu ambaye angemfundisha Biblia bila kutegemea ufafanuzi wowote wa kirabi. Mwezi huohuo, aliuliza, “Je, kuna watu wengine ambao wana imani kama yenu?” Alihudhuria mkutano wa kutaniko na alivutiwa na uchangamfu na upendo alioonyeshwa. Amekuwa akihudhuria kwa ukawaida tangu wakati huo.

“Mna miezi miwili tu ya kuniandaa kwa ajili ya ubatizo!”

Baada ya kujifunza kwa miezi miwili, Or-Ya aliuliza kuhusu kusanyiko lililofuata: “Je, si kwamba kwenye makusanyiko mtu anaweza kubatizwa? Ikiwa ndivyo, basi mna miezi miwili tu ya kuniandaa kwa ajili ya ubatizo!” Hatua ya kwanza aliyochukua ilikuwa kutupa vitu vyote alivyotumia kuwasiliana na pepo. Kisha akaacha kazi ya kuwasiliana pepo na kuanza kuwahubiria wengine, akiwapa kitabu Biblia Inafundisha na magazeti wagonjwa na wateja wake wote wa zamani. Alipokuwa akiumwa, alikataa kutumia njia zake za zamani za kuponya. Kuacha kazi yake ya zamani kulimfanya asiwe na kipato chochote kwa miezi minne. Hata hivyo, aliweka masharti fulani kuhusu kazi, yaani, angefanya kazi siku nne katika wiki, saa sita kwa siku, ili awe na wakati kwa ajili ya mambo ya kitheokrasi. Hatimaye alipata kazi iliyomfaa. Kisha akauza nyumba yake kubwa na kupanga nyumba ndogo.

Hatimaye, Or-Ya alistahili kubatizwa, lakini wiki moja kabla ya kusanyiko, mguu wake mmoja ulivunjika. Hata hivyo bila wasiwasi wowote akabatizwa, lakini mguu wake ukiwa umefungwa plasta. Leo Or-Ya ni mhubiri mtendaji, anawahubiria wateja wake wa zamani na kuongoza mafunzo ya Biblia.

Mshiriki wa Dhehebu Apata Kweli

Ndugu wawili mapacha ambao ni viziwi walianza kujifunza Biblia katika eneo la mbali la milimani nchini Filipino. Wote wawili walikuwa waumini wa dhehebu lililoamini kwamba silaha haziwezi kuwadhuru washiriki wa dhehebu hilo ikiwa watakuwa wamevaa hirizi na skafu ili kujilinda. Walikuwa wamezoezwa kutumia visu, mapanga, na bunduki na walikuwa wameshiriki katika mapigano mengi ya milimani dhidi ya vikundi vya waasi. Dhehebu hilo liliwaruhusu wajifunze Biblia kwa sharti la kwamba Mashahidi hao hawatawalazimisha kuliacha dhehebu hilo.

Bila shaka, akina ndugu waliwatia moyo mapacha hao kufanya maamuzi yao wenyewe yanayotegemea mambo waliyokuwa wakijifunza katika Biblia. Mmoja wa mapacha hao alihisi kwamba hangeweza kufanya marekebisho yanayohitajika maishani mwake ili kumtumikia Mungu kwa njia inayokubalika. Hata hivyo, yule mwingine, aliendelea kujifunza. Ili kumtia moyo, ndugu aliyejifunza naye alifungua Biblia na kufafanua hivi kwa lugha ya ishara: “Jina lako, Samuel, liko kwenye Biblia. Samweli wa kwenye Biblia alimtumikia Mungu wa kweli, Yehova, hadi alipokuwa mzee sana. Wewe pia unaweza kumtii Yehova kwa uaminifu.” Jambo hilo liligusa moyo wa Samuel. “Ikiwa jina langu liko kwenye Biblia,” akaeleza, “Basi mimi pia lazima niwe upande wa Yehova.” Alilijulisha dhehebu hilo kwamba anaondoka kwenye milima hiyo, kisha alichoma hirizi zote na vifaa vyake vyote vya kuwasiliana na pepo na akafanya maendeleo haraka. Samuel sasa ni mtumishi wa Yehova ambaye amebatizwa, na anawasaidia kwa bidii viziwi wengine wajifunze kweli ya Biblia.

Mtoto Anakabili Mateso

[Picha katika ukurasa wa 61]

Erdenet, Mongolia: Mwanamke anayeishi katika eneo la mbali lililotambarare, akiongozwa funzo

Rajiv anaishi katika kijiji fulani cha mbali kaskazini mwa India. Alipokuwa na miaka 9 katika darasa la nne, mwalimu wake ambaye ni Shahidi wa Yehova, aliwafundisha watoto viwango vya maadili akitumia kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Rajiv alikubali habari hizo na akaanza kuishi kulingana na mambo hayo. Alimwambia mwalimu wake kwamba alikuwa ameacha kupigana na wanafunzi wenzake na alikuwa akila chakula chake cha mchana na wale ambao hawakuwa na chakula.

Kadiri alivyojifunza mengi zaidi kuhusu ahadi ya Paradiso duniani, alianza kuwaambia wengine kuhusu habari njema hizo kijijini kwake na wakati akisafiri kwenye treni. Jambo hilo liliwaudhi na kuwaaibisha wazazi wake. Walimwambia aache kuongea kuhusu Yehova na Yesu. Alipoendelea, walianza kumpiga, mama yake angeficha nguo zake ili akirudi kutoka shuleni asiwe na nguo za kuvaa kwenda kuzungumza na watu kuhusu tumaini lake jipya. Wazazi wake hawakumruhusu alale kwenye kitanda chake, na hawakumpa chakula. Hatua hizo ziliposhindwa, walimwita kuhani ili abadili kufikiri kwa mvulana huyo.

Kuhani huyo alikaa siku kadhaa kwenye nyumba hiyo na alijaribu kumlazimisha Rajiv aisujudie sanamu. Rajiv aliposema kwamba sanamu hiyo ni jiwe tu na haikuwa mungu aliye hai, kuhani huyo akajibu kwamba mvulana huyo anapaswa ‘aone zaidi ya kile anachoona katika sanamu hiyo.’ Kwa kufanya hivyo tu ndipo “angemwona” mungu katika sanamu hiyo. Rajiv alichukua kipande cha karatasi na kuandika juu yake “rupia 100.” Akampa kuhani karatasi hiyo na kumwomba akanunue chokoleti kadhaa na kumrudishia chenji. Kuhani huyo akasema kwamba yeye si mjinga, kwani hicho kilikuwa kipande cha karatasi tu na hakikuwa na thamani yoyote. “Ikiwa utaangalia zaidi ya kile unachoona kwenye karatasi hiyo,” akajibu Rajiv, “basi utaona pesa halisi kwenye kipande hicho cha karatasi.” Kwa hasira, kuhani huyo akainamisha kwa nguvu kichwa cha mvulana huyo mbele ya sanamu. Rajiv akasema: “Umekiinamisha kwa nguvu kichwa changu mbele ya sanamu hii, hata hivyo hutaweza kamwe kunifanya nilegeze msimamo wangu.” Mwishowe kuhani akaondoka, akisema kwamba haikuwezekana kumbadili mvulana huyo na ikiwa angeendelea kukaa zaidi, basi hata yeye mwenyewe angepoteza imani yake. Kisha wazazi wa Rajiv wakamhamishia shule nyingine. Hata hivyo hajaacha kuzungumza na mtu yeyote ambaye atasikiliza mambo anayosema kumhusu Yehova na ahadi ya Paradiso. Sasa akiwa na umri wa miaka kumi, anaendelea kumtegemea Yehova ili amsaidie kuimarisha imani yake.

Aliipata Biblia Aliyokuwa Akiitafuta

Larisa alipokuwa akimhubiria muuzaji wa duka la vitabu nchini Armenia, mwanamke fulani aliingia na kumuuliza muuzaji huyo ikiwa kulikuwa na Biblia ya “Ulimwengu Mpya.” Muuzaji huyo akasema kwamba hakuwa na Biblia ya aina hiyo hata hivyo angemuuzia tafsiri fulani ya Kiarmenia. “Je, inaeleweka kwa urahisi?” mteja huyo akauliza. Muuzaji akasoma mistari michache na kusema, “Inaonekana inaeleweka.” Akiwa hajaridhika, mteja huyo akasisitiza kwamba alihitaji kupata Biblia ya “Ulimwengu Mpya.” Ghafla Larisa akakumbuka kwamba alikuwa na Biblia yake ya Kiarmenia kwenye pochi yake. Alimwonyesha mwanamke huyo na kumwomba asome kichwa. Mwanamke huyo akasoma, “Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.” Ilikuwa ndiyo Biblia aliyokuwa akiitafuta!

Mteja huyo alieleza kwamba binti yake na mkwe wake walio nchini Ugiriki walikuwa wameanza tu kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa bado hawakuwa wamejifunza Kigiriki, walimwomba mama yao awapelekee Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiarmenia atakapowatembelea tena. Dada yetu akampa huyo mwanamke Biblia hiyo na akamwambia, “Tafadhali wapelekee hii na uwaambie kwamba ni zawadi kutoka kwa Yehova.” Mwanamke huyo alifurahi hata zaidi Larisa alipojitolea kumsaidia ajifunze Biblia pia. Walipeana namba za simu ili kwamba mwanamke huyo aanze kujifunza mara tu arudipo kutoka Ugiriki.

ULAYA

  • IDADI YA NCHI 47

  • IDADI YA WATU 738,679,198

  • IDADI YA WAHUBIRI 1,595,888

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 841,260

Alirudisha Pochi

Nina, dada ambaye ni painia wa kawaida nchini Bosnia, anajifunza na familia ya Waromani. Siku moja alipokuwa akitembea kwenye mtaa fulani, msichana mwenye umri wa miaka kumi wa familia hiyo aliokota pochi ambayo ndani yake kulikuwa na pesa, kadi za mkopo, na hati kadhaa. Kabla ya kujifunza kweli, angeona kuokota pochi hiyo kuwa zawadi yenye thamani, hata hivyo baada ya kushauriwa na mama yake, aliamua kuipeleka pochi hiyo polisi. Uamuzi huo haukuwa wa kawaida kwa kuwa familia hiyo ilikuwa maskini na hata hawakuwa na pesa za kutosha ili kununua mkate. Karibu muda wa saa mbili baada ya kumkabidhi ile pochi polisi aliyepigwa na butwaa, walipigiwa simu wakiombwa warudi kituo cha polisi. Mwenye pochi hiyo alikuwa akiwasubiri ili awashukuru na kuwapa zawadi. Aliwapa pesa inayolingana na dola 30 za Marekani, ambazo ni sawa na mshahara wa siku mbili.

Alivutiwa na Kichwa

[Picha katika ukurasa wa 64]

Gjógv, Visiwa vya Faroe: Visiwa hivi vilikuwa na kilele cha wahubiri 118 katika mwaka wa 2012

Nihad, ambaye anaishi nchini Bosnia, alikuwa amemaliza utumishi wa shambani. Alipofika kwenye gari lake, alimkuta mwanaume fulani amesimama pembeni ya gari hilo. Nihad alipomsalimia, mwanaume huyo akamwambia: “Samahani, nimeona gazeti fulani kwenye gari lako lenye kichwa ‘Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri.’ Kwa kweli ningependa kupata nakala ya gazeti hilo. Nimekuwa nikisubiri mahali hapa kwa saa moja hivi ili mwenye gari atokee. Je, naweza kuipata tafadhali? Nihad alifurahi kumpa gazeti hilo na akatumia nafasi hiyo pia kumhubiria.

Wafanyakazi wa Meli Wafarijiwa

Wenzi wa ndoa fulani wanaohubiri katika eneo la bandari ya Rotterdam nchini Uholanzi walipotembelea meli fulani ya mizigo, walikutana na wafanyakazi wenye huzuni wa meli hiyo. Huku akitokwa na machozi, mhandisi mkuu akawaambia kwamba meli hiyo ilikuwa imekumbana na mlolongo wa majanga, karibu meli hiyo igongane na meli nyingine, na ilikuwa imeharibika. Hivyo akauliza, “Je, mnaweza kusali kwa ajili yetu?” Wenzi hao wa ndoa waliamua kuwatolea wafanyakazi hao hotuba ya Biblia ili kuwatia moyo. Saa moja jioni ya siku iliyofuata, wahubiri hao wakiwa na wenzi wa ndoa wengine wawili walikaribishwa sehemu ya mbele ya meli hiyo. Kulikuwa na watu 15 kati ya wafanyakazi 16 wa meli hiyo waliokusanyika hapo. Baada ya sala ya kufungua, ndugu alitoa hotuba yenye kichwa “Misiba—Je, Ni Kazi ya Mungu?” Wafanyakazi hao waliweza kusoma maandiko ya Biblia yaliyotajwa kwa sababu wahubiri hao walikuwa wamebeba Biblia za ziada na walimsaidia kila mmoja kutafuta maandiko. Baada ya sala ya kumalizia, wafanyakazi wote walibaki wakiwa wameketi na kuzungumza na akina ndugu. Wafanyakazi hao walijihisi nafuu na kutoa shukrani. Mmoja wao alisema, “Jambo hili ni jibu la sala zetu.” Wafanyakazi hao walichukua vitabu 20, pia Biblia na machapisho mengine. Baadaye nahodha wa meli hiyo akawakabidhi wahubiri hao bahasha yenye dola 200 za Marekani zikiwa mchango kwa ajili ya machapisho waliyopata.

Alisali Ili Aweze Kusaidia

Irene, anayeishi nchini Sweden, aliandika hivi: “Nina umri wa miaka 80, na kwa sababu ya maumivu siwezi kutoka kwenda utumishi wa shambani. Nilisali kwa Yehova anisaidie ili niweze kumsaidia mtu fulani niliyemtembelea zamani na ambaye sasa atakuwa tayari kuwa na mazungumzo au kutembelewa.

“Siku moja, simu yetu ya mezani iliita, na mume wangu akapokea. Mwanamke aliyepiga akamwambia: ‘Samahani, ninyi ndio watu pekee ambao ninaweza kuwakumbuka, ndiyo sababu nimewapigia. Je, mke wako angependa kunitembelea ili tuzungumzie Neno la Mungu? Nilijifunza miaka 15 au 20 iliyopita, lakini mume wangu ambaye amekufa, wakati huo alinipinga hivyo nikaacha kujifunza.’

“Nilikumbuka kwamba nilimtembelea mwanamke huyo nikiwa na dada mwingine, ambaye ndiye aliyejifunza naye. Jambo lililonishangaza ni kwamba, mwanamke huyo alinikumbuka mimi. Nikiwa nimefurahi, nilifanya mipango ya kukutana naye. Tangu wakati huo, tumekuwa tukijifunza kila wiki. Alihudhuria Ukumbusho na hotuba ya pekee. Pia, amekuwa akihudhuria mikutano. Ninamshukuru Yehova kila siku kwa kujibu sala yangu.”

Hakuna Sanduku kwa Ajili ya Chokoleti

Sergio, mwenye umri wa miaka nane, ambaye anaishi nchini Italia, alitaka kuwathibitishia wazee kwamba alikuwa tayari kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Siku moja, alienda na baba yake, ambaye alihitaji kurekebisha kufuli kwa ajili ya wenzi fulani wa ndoa wenye umri wa miaka 70 hivi. Sergio alibeba magazeti kadhaa. “Baba yangu alipokuwa akifanya kazi,” anaeleza, “Nilimpatia mwanaume wa nyumba hiyo magazeti niliyokuwa nayo, ambaye alishangazwa hivi kwamba akamwita mke wake na kumwonyesha magazeti hayo. Kisha nikaandika majina yao, anwani, na namba yao ya simu ili niweze kuwarudia wakati mwingine. Mke wake ndiye aliyenipa habari zote hizo na akanipa pakiti kubwa ya chokoleti.” Siku chache baadaye, Sergio na mmoja wa wazee wa kutaniko wakawarudia wenzi hao wa ndoa. Sergio aligonga kengele na mama mwenye nyumba hiyo alipojibu, alieleza kwamba alitaka kuwapatia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Mwanamke huyo alikubali kitabu hicho. Akampa Sergio pakiti nyingine ya chokoleti. “Nisingeweza kuweka chokoleti uliyonipa kwenye sanduku la michango, kwa hiyo niliila,” akasema Sergio, ambaye aliongezea kusema hivi, “Hatimaye wazee walielewa ni kadiri gani nilitaka kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa.”

Kasisi Alitaka Kujifunza Zaidi

Simeon alikuwa kasisi wa kanisa lililo kwenye mji wa Gurkovo, nchini Bulgaria, mahali ambako hakuna Mashahidi. Kujifunza kwake Biblia kulimfanya atambue tofauti kati ya mambo ambayo Biblia inafundisha na yale ambayo kanisa linafundisha. Siku moja, alipata baadhi ya magazeti yetu alipokuwa akisafiri kwa treni. Simeon alifurahi kujifunza kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli na kwamba hakuna Utatu. Akiwa na hamu ya kujifunza zaidi, aliandika barua kwa ofisi ya tawi na makanisa yote aliyoyajua. Kanisa moja tu lilijibu barua yake, likimwambia kwamba aache kuhangaikia “mambo hayo ya kipuuzi.” Tofauti na hilo, ofisi ya tawi ilipanga Mashahidi wawili wasafiri karibu kilomita 35 kutoka Kazanlŭk. Walianza kujifunza Biblia pamoja na Simeon na familia yake. Simeon alipenda mambo aliyokuwa akijifunza, na akawakaribisha majirani na marafiki zake ili wahudhurie funzo. Baada ya muda mfupi watu 25 walikuwa wakihudhuria funzo la Biblia kila wiki. Baada ya kuhudhuria moja ya mazungumzo ya Biblia kwa mara ya kwanza, jirani mwenye umri wa miaka 75 alisema hivi huku akitokwa na machozi, “Katika saa moja nimeelewa mengi zaidi kuliko miaka 30 niliyoenda kanisani.” Karibu watu 60 wanahudhuria mikutano ambayo ndugu kutoka Kazanlŭk wanaongoza mjini Gurkovo kila mwezi, na watu 79 walihudhuria Ukumbusho.

“Katika saa moja nimeelewa mengi zaidi kuliko miaka 30 niliyoenda kanisani”

“Tafadhali Fuata Njia Hiyohiyo ya Maisha”

Valya, dada mwenye umri wa miaka 15 nchini Ukrainia, alimwona mwalimu wake amekuja shuleni akiwa amevaa nguo nyeusi na alikuwa akilia. Baada ya kujua kwamba mama ya mwalimu huyo alikuwa amekufa, Valya aliamua kumfariji kwa kutumia maandiko yanayohusu ufufuo. Valya alichukua Biblia na broshua mbili, Ni Nini Hutupata Tunapokufa? na Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, kisha akaamua kwamba baada ya vipindi vya masomo kwisha, angemwendea mwalimu huyo. Alisema: “Nilipokuwa nikisubiri kwenye mlango wa ofisi yake, nilikuwa na wasiwasi sana, hivyo nikasali kwa Yehova ili anisaidie.”

Valya alipoingia ofisini, mwalimu huyo akamuuliza, “Unataka nini?”

“Ninataka kukufariji kwa sababu ninaelewa jinsi unavyohisi. Miaka kadhaa iliyopita babu yangu alikufa.”

[Picha katika ukurasa wa 68]

Georgia: Kuhubiri kwenye shamba la mizabibu

Mwalimu huyo aliguswa sana na jinsi ambavyo Valya alivyomhangaikia. Huku akilia, alisema kwamba si watu wake wa ukoo wala wafanyakazi wenzake waliomwonyesha huruma ya kutoka moyoni kama hiyo. Kisha Valya alisoma na kuelezea andiko la Ufunuo 21:3, 4, baada ya hapo mwalimu huyo alikubali broshua zile, akasema, “Wewe uko tofauti sana na wanafunzi wengine.”

Valya akamwambia, “Ninajitahidi kusoma Biblia na kuishi kulingana na yale ninayosoma, na ninawasikiliza wazazi wangu.”

Kutokana na ombi la mwalimu huyo, baadaye Valya alimletea Biblia na kitabu Biblia Inafundisha. Mwalimu huyo alimshukuru tena na kumwambia Valya hivi: “Dini yako ndiyo dini ya kweli, na una wazazi wazuri sana ambao wanakufundisha mambo sahihi. Tafadhali fuata njia hiyohiyo ya maisha.”

Alikosea Namba ya Simu

Katika siku ya kwanza ya kusanyiko la wilaya la mwaka 2011 lililofanywa Malakasa, nchini Ugiriki, Natalie alimpigia simu baba yake ili kumjulisha juu ya basi linaloenda kwenye viwanja vya kusanyiko. Hata hivyo, alikosea namba ya simu, na hakuna aliyepokea. Muda mfupi baadaye, mtu ambaye alikuwa amepigiwa simu kimakosa aliiona namba na akapiga ili kujua ni nani aliyempigia. Hata hivyo, programu ya kusanyiko ilikuwa imeanza, ingawa Natalie alikuwa amekusudia kuizima simu yake, kwa namna fulani alipokea simu hiyo. Kwa hiyo, bila mwenyewe kujua, mwanaume huyo aliweza kusikiliza sehemu ya hotuba ya mwenyekiti, ambayo iliamsha upendezi wake.

Baadaye, mwanaume huyo alituma ujumbe mfupi, akiuliza: “Wewe ni nani? Je, wewe ni kasisi?” Kipindi cha asubuhi kilipoisha, Natalie aliona ujumbe huo na kujibu hivi: “Mimi si kasisi. Mimi ni Shahidi wa Yehova, na ninahudhuria kusanyiko.”

[Picha katika ukurasa wa 71]

Pittenweem, Scotland: Kuhubiri bandarini

Mwanaume huyo akapiga tena simu siku ya Jumamosi ili kuuliza ikiwa bado kusanyiko lilikuwa likiendelea. Baba ya Natalie alimhubiria na baada ya hapo mwanaume huyo akasema, “Katika dakika chache, hotuba ambayo nilisikiliza kupitia simu ilijibu maswali mengi ambayo yamekuwa yakinisumbua.” Familia ya mwanaume huyo ilikuwa ikisumbuliwa na mashetani na hawakujua kabisa hao roho ni nani na kwa nini walikuwa wakiwasumbua. Mwanaume huyo akasema: “Sijawahi kuwa na nia ya kuongea na Mashahidi wa Yehova hadi sasa, lakini ikiwa inawezekana, ningependa kuzungumza na mwanaume aliyetoa hotuba.”

Bila shaka iliwezekana. Mwanaume huyo alikuja kwenye kusanyiko siku ya Jumapili na alishangazwa sana na mambo aliyoona—familia zilizovaa vizuri na zenye furaha. Hakukuwa na takataka chini, hakuna lugha chafu, hakuna aliyevuta sigara. “Sikuwahi kufikiri kwamba watu kama ninyi mko katika sayari hii!” akasema. “Nahisi kana kwamba nimeingia katika ulimwengu mwingine.” Baba ya Natalie alimpeleka kwenye ofisi ya mwenyekiti, ambako alizungumza na mwenyekiti. Kusanyiko lenyewe na majibu aliyopewa vilimvutia sana mwanaume huyo. Alikubali kitabu Biblia Inafundisha, Biblia, na baadhi ya magazeti, na mipango ikafanywa kwa ajili ya ziara ya kurudia.

OCEANIA

  • IDADI YA NCHI 29

  • IDADI YA WATU 38,495,300

  • IDADI YA WAHUBIRI 94,924

  • IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 59,431

“Sijawahi Kamwe Kusikia Wimbo Mzuri Kama Huo”

Katika kisiwa cha Savaii, Samoa, wanafunzi huanza siku kwa shule nzima kuimba wimbo wa kidini. Hata hivyo Celina, mwenye miaka mitano, na Levaai, mwenye miaka sita, kwa heshima walimwambia mkuu wa shule kwamba hawangeimba wimbo huo kwa sababu wao ni Mashahidi wa Yehova. Kukataa kuimba wimbo huo kungefanya wapate adhabu kali. Hata hivyo, kwa kweli mkuu huyo alifikiri kwamba angeweza kuwaaibisha watoto hao hivi kwamba wakubali kuimba, hivyo akasema, “Sawa, ikiwa hamwezi kuimba wimbo wetu, basi imbeni wimbo wenu mmoja.” Hivyo, Celina na Levaai waliimba wimbo namba 111, “Ataita,” ambao walikuwa wamejifunza hivi karibuni kwenye jioni ya Ibada ya Familia. Walipomaliza, mkuu huyo wa shule alikuwa akitokwa na machozi. Akasema: “Huo ni wimbo mzuri sana ambao sijawahi kamwe kuusikia. Tafadhali imbeni tena.” Wakaimba tena. Kisha akawaambia, “Kuanzia sasa na kuendelea, nitawaomba mwimbe, si nyimbo zetu, bali zenu.”

“Kuanzia sasa na kuendelea, nitawaomba mwimbe, si nyimbo zetu, bali zenu”

Katika Maisha Yake Yote Alisali kwa Yesu

[Picha katika ukurasa wa 72]

Timor-Leste: Nchi hii ambayo zamani iliharibiwa na vita imekuwa na ongezeko la asilimia 9 la wahubiri

Mwanaume mmoja nchini Fiji ambaye alikuwa mhudumu wa kanisa katika eneo lao aliamua kuketi na kusikiliza katika funzo la mtu mwingine. Wakati wa funzo, alisikia kwamba Yesu si Mungu. Alisumbuliwa sana na jambo hilo hivi kwamba hakuweza kupata usingizi. Alipoona kusumbuka huko, mke wake akamwambia, “Usirudi tena kuwasikiliza watu hao!” Hata hivyo, hakuweza kuliondoa jambo hilo akilini mwake. Wiki iliyofuata, alihudhuria tena funzo la Biblia. Siku chache baada ya funzo hilo la pili na hata kabla yeye mwenyewe hajaanza kujifunza, alienda kanisani kwake na kuacha kazi yake ya kuhudumu. Jambo hilo liliwashtua na kuwakasirisha watu wake wa ukoo na waumini kanisani. Si kwamba alikuwa akiliacha kanisa tu, bali pia alikuwa akijiuzulu kazi yenye mshahara mzuri. Angeweza kuona kwa urahisi katika Biblia kweli kumhusu Yesu, hata hivyo haikuwa rahisi kwake kusali kwa Yehova kwa sababu katika maisha yake yote amekuwa akisali kwa Yesu. Baada ya miezi mingi, hatimaye aliweza kusali kwa Yehova. Sasa anawahubiria wengine habari njema na kuwasaidia wamjue na kumpenda Yehova.

Jumuiya Ndogo Yaikubali Kweli

Watu 62 tu ndio wanaoishi katika kisiwa cha Makatea kilicho Pasifiki Kusini. Kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Tahiti linawafundisha watu hao kuhusu Yehova. Mafunzo tisa ya Biblia huongozwa kwa ukawaida kwa njia ya simu. Watu 15 wanakutana kwenye nyumba ya mmoja wa wanafunzi wa Biblia na kusikiliza mikutano, ambayo inafanywa nchini Tahiti. Kati ya wale wanaojifunza Biblia sasa kuna msichana ambaye alikuwa nguzo muhimu katika kanisa lake na alitarajiwa kuwekwa rasmi kuwa mhudumu wa kike. Muda mfupi uliopita, alirudi kanisani kwake ili kuwaeleza ni kwa nini ameacha kwenda kanisani. Alitumia Biblia kuonyesha kwamba mwanamke hapaswi kufundisha kutanikoni. Pia, alielezea jukumu la Yesu Kristo na maana ya Mlo wa Jioni wa Bwana, ambao unapaswa kuadhimishwa mara moja kwa mwaka na si kila Jumapili. Zaidi ya hayo, aliwaeleza kwamba ni watu 144,000 tu ndio watakaokuwa na Kristo mbinguni na wao tu ndio wanaopaswa kula mkate na kunywa divai ya Ukumbusho. Akichochewa na mfano wake, mwanamke mwingine aliliacha kanisa na sasa anajifunza Biblia kwa ukawaida na Mashahidi.

Familia Ilikubali Mwaliko

Katika jitihada za kuwaalika watu wasiotenda wahudhurie Ukumbusho wa kifo cha Kristo, wazee wawili katika Visiwa vya Solomoni walimtembelea Joshua, ambaye hajawahi kuhudhuria mikutano tangu mwaka 1998. Akiwa pamoja na watu 20 wa familia yake, Joshua alitembea kwa saa mbili ili kuhudhuria Ukumbusho. Joshua alitokwa na machozi kwa namna ambavyo kutaniko liliwakaribisha kwa uchangamfu. Watu wengi katika familia walikuja pia kwenye hotuba ya pekee, ambapo baada ya hotuba waliwaambia wazee kwamba wangependa kujifunza Biblia. Mipango ilifanywa ili kujifunza na watu 15 kati yao.

Alijua Jibu

Kati ya visiwa zaidi ya 1,000 katika eneo linalosimamiwa na ofisi ya tawi ya Guam, kuna visiwa zaidi ya 100 vinavyokaliwa. Hata hivyo, ni visiwa 13 tu vilivyo karibu na kutaniko. Kwa sababu visiwa vingi havijawahi kutembelewa na Mashahidi wa Yehova, akina ndugu wanaendelea kutafuta njia za kuwafikia watu hao. Mnamo Aprili 2012, kikundi cha akina ndugu kilisafiri kwa mashua hadi kwenye kisiwa cha Polowat, moja kati ya visiwa vilivyo mbali sana. Polowat ni kisiwa ambacho hakina mawasiliano na sehemu nyingine za ulimwengu. Wanaume wanajifunga mashuka kiunoni, wanatengeneza mitumbwi, na maisha yao yanategemea kilimo.

Mmoja kati ya wahubiri walioenda kisiwani hapo alimuuliza hivi kijana fulani, “Ni nini hutupata tunapokufa?”

“Ninajua jibu la swali hilo!” kijana huyo akajibu. Kisha akasimama na kuchukua kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani katika lugha ya Kichuukese kilichokuwa kwenye rafu yake, na akafungua kwenye ukurasa wa yaliyomo. Akifungua kwenye sura ya 8 yenye kichwa, “Inakuwaje Wakati wa Kufa?” akaeleza kwa shauku mambo ambayo amejifunza kwenye kitabu hicho.

[Picha katika ukurasa wa 75]

Kingston, Kisiwa cha Norfolk: Kuhubiri kwenye barabara kuu, Quality Row

Hata hivyo, alipataje kitabu hicho? Mwaka 2009, wahubiri walio katika kisiwa kikuu cha Chuuk walihubiri kwenye bandari mbalimbali wakijitahidi kuwafikia watu waliokuwa wakisafiri kwenda visiwa vya mbali na kuwapa vitabu Kuishi Milele. Mtu fulani aliyekuwa akienda Polowat alikubali kubeba boksi la vitabu ili akawape jirani zake, kijana huyo alikuwa miongoni mwa majirani hao.

Kabla ya kuondoka Polowat, akina ndugu walimtembelea tena kijana huyo mara kadhaa ili kumtia moyo na kumwonyesha jinsi ya kunufaika na mpango wa kujifunza. Pia, walimfundisha jinsi ya kutafuta maandiko na kuandika mambo makuu katika sehemu za pambizoni mwa kitabu chake.

Jinsi inavyotia moyo kujua kwamba hata katika visiwa vya mbali mahali ambako hakuna televisheni, redio, magazeti, au Intaneti, machapisho yetu yanawasaidia watu wajifunze kweli katika lugha zao za asili!

Risasi Tatu, Sababu Tatu

Anna alikuwa mhubiri ambaye hajabatizwa alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi wakati vita vya wenyewe kwa wenyewe vilipopamba moto kisiwani Bougainville nchini Papua New Guinea. Mnamo 1991 alikuwa miongoni mwa kikundi cha Mashahidi wakubwa sita na watoto saba kutoka katika Kutaniko la Arawa ambao walilazimika kukimbilia msituni wakiwa na vitu vichache tu. Kwa miaka miwili, waliishi kwenye mahame huku wakitafuta chakula. Walifanya mikutano yao kwa kutumia vitabu viwili tu walivyokuwa navyo, Biblia ya Anna na kitabu Wenye Umoja Katika Ibada ya Mungu wa Pekee wa Kweli. Walisali pamoja, waliimba nyimbo za Ufalme, na kuwahubiria watu waliokutana nao.

Wanajeshi wa jeshi la mapinduzi waliwapata na wakataka akina ndugu wawili katika kikundi hicho wajiunge na jeshi, hata hivyo waliwaheshimu Mashahidi kwa sababu ya msimamo wao wa kutojiingiza katika mambo ya kisiasa. Pindi moja mwanajeshi fulani alimwonyesha Anna risasi tatu na kumwambia, “Usipokubali nikuoe, nitakuua.” Anna akampa sababu tatu—sababu moja kwa kila risasi—kwa nini hangekubali kuolewa naye, sababu kuu zaidi ni kwamba Biblia inasema kuoa au kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Mwanaume huyo akageuka na kuondoka.

“Hakuna jambo linaloweza kusimamisha kazi ya Yehova, hata vita vya wenyewe kwa wenyewe haviwezi”

Mwaka 2012, baada ya kusikia kwamba kuna uhitaji wa wahubiri wa Ufalme mjini Arawa, Anna, ambaye sasa ni painia wa kawaida, alirudi Arawa pamoja na mwandamani wake ili kusaidia kuanzisha kikundi. Aliulizwa ikiwa ilimsumbua kurudi katika eneo ambalo aliona mauaji ya halaiki na kukabiliana na mambo mengi magumu wakati wa vita. Alijibu hivi: “Ninahisi shangwe. Hakuna jambo linaloweza kusimamisha kazi ya Yehova, hata vita vya wenyewe kwa wenyewe haviwezi.”

‘Umekiinamisha kichwa changu mbele ya sanamu hii, hata hivyo hutaweza kamwe kunifanya nilegeze msimamo wangu’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki