Usishindwe na Hangaiko
“MSIHANGAIKE kamwe juu ya siku ifuatayo, kwa maana siku ifuatayo itakuwa na mahangaiko yayo yenyewe. Waitosha kila siku ubaya wayo yenyewe.” (Mathayo 6:34) Bila shaka, shauri hilo lililotolewa na Yesu Kristo lafaa kwetu sisi ambao twaishi katika jamii yenye mbio-mbio na yenye mkazo.
Ingawa hivyo, je, kwa kweli yawezekana kwetu kutohangaikia matatizo, maamuzi, wajibu, na madaraka yetu? Mamilioni ya watu wameshuka moyo, wamesononeka, na kulemewa na mambo. Hiyo ndiyo sababu kuuza dawa za kutuliza na kupoza maumivu ni biashara yenye kuchuma mamilioni ya dola.
Mahali pa Kuweka Mpaka
Tunahitaji kupanga na kujitayarishia wajibu wetu mbalimbali, migawo, maamuzi, na matatizo—yawe ya haraka au yasiwe ya haraka. Biblia hututia moyo ‘tuketi na kupiga hesabu ya gharama’ kabla ya kuanza shughuli yoyote kubwa. (Luka 14:28-30) Hilo latia ndani kufikiria kwa makini mambo tuwezayo kuchagua kufanya, tukichanganua athari ziwezazo kusababishwa na matokeo, na kukadiria gharama kuhusiana na wakati, nguvu, na pesa.
Ingawa mtu apaswa kufikiria kwa makini yale yawezayo kutukia, haiwezekani wala haisaidii kujaribu kufikiria kila jambo liwezalo kutukia baadaye. Kwa mfano, kwa ajili ya usalama wa familia, huenda ukafikiria utakachofanya endapo moto utatokea nyumbani mwako. Huenda ukanunua na kuweka vifaa vya kugundua moshi na vya kuzima moto. Huenda ukapanga na kufanya mazoezi ya kutumia njia za kuponyokea kwa kutokea sehemu mbalimbali za nyumba. Lakini, nini iliyo tofauti kati ya kupanga kwa hekima na kwa busara, na kuhangaika kupita kiasi bila sababu? Hangaiko hilo huanza unapoanza kuwa na maumivu makali moyoni kuhusu hali mbalimbali za kudhania tu, ambazo nyingi huenda zikatokana na kuwaza sana. Mawazo yenye kusumbua huenda yakakushinda nguvu, yakikusadikisha kwamba lazima uwe ulipuuza jambo fulani au haujafanya yote yahitajiwayo ili kulinda familia yako. Maumivu hayo makali ya kujiletea yanaweza kukulemea akili sana hivi kwamba huenda yakakukosesha usingizi.
Musa Akiwa Mbele ya Farao
Yehova Mungu alimpa nabii wake Musa mgawo mgumu. Kwanza, Musa aliwajibika kwenda kwa Waisraeli na kuwasadikisha kwamba Yehova alikuwa amemweka rasmi ili awaongoze kutoka Misri. Halafu, Musa aliwajibika kwenda mbele ya Farao na kumwomba awaruhusu Waisraeli waondoke. Hatimaye, Musa aliwajibika kuongoza mamilioni ya watu kupitia nyikani hadi kwenye nchi iliyokaliwa na watu wenye uhasama. (Kutoka 3:1-10) Mambo hayo yote yangeweza kuwa yenye kuogofya sana, lakini je, Musa aliruhusu daraka hilo lijaze akili yake kwa hangaiko lisilofaa?
Ni wazi kwamba Musa alihangaikia masuala kadhaa. Yeye alimwuliza Yehova hivi: “Nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n’nani? niwaambie nini?” Yehova alimpa jibu. (Kutoka 3:13, 14) Musa pia alihangaikia kile ambacho kingelitokea ikiwa Farao angelikataa kumwamini. Kwa mara nyingine tena, Yehova alimjibu nabii huyo. Tatizo moja la mwisho—Musa alikiri kwamba hakuwa “msemaji mwenye ufasaha.” Jambo hilo lingeweza kutatuliwaje? Yehova aliagiza Aroni awe msemaji wa Musa.—Kutoka 4:1-5, 10-16, NW.
Akiwa ametayarishwa kwa kujibiwa maswali yake na akiwa na imani katika Mungu, Musa alifanya yale Yehova aliyomwamuru. Badala ya kujitesa kwa mawazo yenye kuogofya kuhusu yale ambayo yangeliweza kutukia alipokabili Farao, Musa “alifanya vivyo hivyo.” (Kutoka 7:6, NW) Kama angeruhusu mahangaiko yamshinde, hayo yangeliweza kudhoofisha imani na ujasiri aliohitaji ili kutekeleza mgawo wake.
Njia ya Musa yenye usawaziko ya kushughulikia mgawo wake ni kielelezo cha kile ambacho mtume Paulo alikiita “utimamu wa akili.” (2 Timotheo 1:7; Tito 2:2-6) Kama Musa hangelitumia utimamu wa akili, ukubwa wa mgawo wake ungeliweza kwa urahisi kumlemea sana hivi kwamba, yaelekea angeliukataa.
Kudhibiti Mawazo Yako
Je, wewe hutendaje unapokabiliwa na mitihani ya imani au majaribu katika maisha yako ya kila siku? Je, wewe una mwelekeo wa kupatwa na hofu ya ghafula ukifikiria tu vizuizi na magumu yaliyoko mbele? Au una maoni yenye usawaziko kuyaelekea? Sawa na vile ambavyo watu fulani wangesema, ‘Usivuke daraja kabla ya kulifikia.’ Huenda kusiwe na uhitaji wa kuvuka daraja hilo la kudhania tu! Hivyo, mbona usumbuliwe na jambo ambalo huenda lisitokee kamwe? Biblia husema: “Uzito [“Hangaiko,” NW] katika moyo wa mtu huuinamisha.” (Mithali 12:25) Mara nyingi tokeo ni kwamba mtu anakawia kufanya uamuzi fulani, akiahirisha mambo hadi kuchelewa mno.
Jambo lililo baya zaidi ni madhara ya kiroho ambayo hangaiko lisilofaa huenda likatokeza. Yesu Kristo alionyesha kwamba kuthamini “neno la ufalme” kwaweza kusongwa kabisa na nguvu za udanganyifu wa mali na “hangaiko la mfumo huu wa mambo.” (Mathayo 13:19, 22) Kama vile miiba iwezavyo kuzuia miche isifikie ukomavu na kuzaa matunda, ndivyo hangaiko lisilodhibitiwa liwezavyo kutuzuia tusifanye maendeleo ya kiroho na kuzaa matunda yanayomletea Mungu sifa. Maumivu hayo makali ya kujiletea, ambayo ni yenye kuharibu, yamefanya watu wengine hata wasijiweke wakfu kwa Yehova. Wao huhangaika, ‘Vipi ikiwa sitatenda kupatana na wakfu wangu?’
Mtume Paulo alituambia kwamba katika vita yetu ya kiroho, tunajitahidi sana kuingiza “kila fikira katika utekwa ili kuifanya iwe tiifu kwa Kristo.” (2 Wakorintho 10:5) Adui wetu mkuu, Shetani Ibilisi, angefurahi sana kutumia mahangaiko yetu ili kutuvunja moyo na kutudhoofisha kimwili, kihisia-moyo, na kiroho. Yeye ni stadi katika kutumia shaka ili kunasa wasio na hadhari. Hiyo ndiyo sababu Paulo pia aliwaonya Wakristo “[wa]siruhusu mahali kwa ajili ya Ibilisi.” (Waefeso 4:27) Akiwa “mungu wa huu mfumo wa mambo,” Shetani amefaulu “[ku]pofusha akili za wasioamini.” (2 Wakorintho 4:4) Na tusimruhusu kamwe adhibiti akili zetu!
Msaada Upo
Mtoto anaweza kumwendea baba mwenye upendo na kupata mwongozo na faraja anapokabili matatizo. Vivyo hivyo, tunaweza kumwendea Baba yetu wa kimbingu, Yehova, na matatizo yetu. Kwa kweli, Yehova hutualika tumtwike mizigo yetu na mahangaiko yetu pia. (Zaburi 55:22) Kama mtoto ambaye hahangaikii tena matatizo yake baada ya kupata uhakikisho kutoka kwa baba yake, yatupasa tumtwike Yehova mizigo yetu na pia kumwachia hiyo mizigo.—Yakobo 1:6.
Sisi humtwikaje Yehova mahangaiko yetu? Andiko la Wafilipi 4:6, 7 lajibu: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” Naam, kwa kuitikia sala na dua zetu za bidii, Yehova anaweza kutupa utulivu wa ndani unaolinda akili zetu zisisumbuliwe na mahangaiko yasiyo ya lazima.—Yeremia 17:7, 8; Mathayo 6:25-34.
Ingawa hivyo, ili kutenda kupatana na sala zetu, hatupaswi kujitenga kimwili au kiakili. (Mithali 18:1) Badala yake, yapendekezwa kwamba tufikirie kanuni na miongozo ya Biblia inayohusiana na tatizo letu, hivyo tukiepuka kutegemea akili zetu wenyewe. (Mithali 3:5, 6) Wachanga kwa wazee vilevile waweza kutumia Biblia na vichapo vya Watch Tower ili kupata habari kwa wingi juu ya kufanya maamuzi na kushughulika na matatizo. Kwa kuongezea, katika kutaniko la Kikristo, tumebarikiwa kuwa na wazee wenye hekima na uzoefu na pia Wakristo wengine wakomavu ambao wako tayari sikuzote kuzungumza nasi. (Mithali 11:14; 15:22) Mara nyingi wale ambao hawahusiki kihisia-moyo katika matatizo yetu, na walio na maoni sawa na ya Mungu kuyahusu, wanaweza kutusaidia kuwa na maoni tofauti kuelekea matatizo yetu. Na ingawa hawatatufanyia maamuzi, wanaweza kuwa chanzo kikuu cha kitia-moyo na utegemezo.
‘Mtumainie Mungu’
Hakuna mtu awezaye kukana kwamba kila siku sisi hupata mkazo wa kutosha tunaposhughulika na matatizo yetu yaliyo halisi bila ya kuyazidisha kwa kuhangaikia yale ya kudhania tu. Ikiwa hangaiko juu ya kile kiwezacho kutukia latutia hofu au wasiwasi, basi acheni tumwendee Yehova kwa sala na dua. Acheni tutegemee Neno lake na tengenezo lake kwa mwongozo, hekima, na utimamu wa akili. Tutaona kwamba hata hali gani itokee, msaada wapatikana wa kuishughulikia.
Akiwa na moyo mzito na hangaiko, mtunga-zaburi aliimba: “Mbona nasononeka hivyo moyoni? Kwa nini nahangaika hivyo? Nitamtumainia Mungu, maana nitamsifu tena Mungu, aliye msaada wangu na Mungu wangu.” (Zaburi 42:11, Biblia Habari Njema) Acheni hizo ziwe hisia zetu za moyoni.
Naam, pangia yale ambayo kwa kufaa yaweza kutarajiwa, na kumwachia Yehova yale yasiyotarajiwa. “[Tupeni] hangaiko lenu lote juu yake, kwa sababu yeye huwajali nyinyi.”—1 Petro 5:7.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Kama Daudi, je, wewe humtwika Yehova mizigo na mahangaiko yako?