SOMO LA 44
Kutumia Maswali Vizuri
MASWALI huhusisha wasikilizaji kwa sababu yanahitaji majibu ya mdomo au ya kimoyomoyo. Maswali yanaweza kukusaidia kuanzisha mazungumzo na kuyafurahia. Ukiwa msemaji na mwalimu, unaweza kutumia maswali kuamsha upendezi wa mtu, kumsaidia mtu asababu kuhusu habari fulani, au kukazia jambo unalosema. Maswali mazuri yanawasaidia wengine kufikiri badala ya kusikiliza tu. Uwe na kusudi fulani akilini, na uulize maswali kwa njia inayokusaidia kutimiza kusudi hilo.
Ili Kuendeleza Mazungumzo. Unapokuwa katika utumishi wa shambani, uwe macho kuona pindi za kuwaomba watu maoni yao ikiwa hawaoni ubaya kuulizwa maswali.
Mashahidi wengi huanzisha mazungumzo yenye kupendeza kwa kuuliza swali kama, “Je, umewahi kufikiria . . . ?” Wakichagua swali ambalo watu wengi wanalifikiria sana, hakika watafurahia utumishi wa shambani. Hata kama mtu hajawahi kusikia swali ambalo umeuliza, bado linaweza kuchochea fikira zake. Tunaweza kuzungumzia mambo mengi kwa kuuliza maswali kama “Unaonaje . . . ?” na “Je, unaamini . . . ?”
Mweneza-evanjeli Filipo alimwendea ofisa wa makao ya kifalme kutoka Ethiopia ambaye alikuwa akisoma kwa sauti unabii wa Isaya. Filipo akamwuliza: “Je, wewe kwa hakika wajua [au, unaelewa] unayoyasoma?” (Mdo. 8:30) Swali hilo lilimwezesha Filipo amweleze kweli kuhusu Yesu Kristo. Mashahidi wengine leo wametumia swali kama hilo kuzungumza na watu ambao wametamani sana kuelewa vizuri kweli ya Biblia.
Watu wengi husikiliza wakipewa nafasi ya kutoa maoni. Baada ya kuuliza swali, sikiliza kwa makini. Uwe mwenye fadhili badala ya kuchambua jibu la mtu huyo. Mpongeze kutoka moyoni inapowezekana. Pindi moja, Yesu alimpongeza mwandishi mmoja ambaye ‘alijibu kwa kutumia akili,’ akamwambia: ‘Hauko mbali na ufalme wa Mungu.’ (Mk. 12:34) Hata kama hukubaliani naye, unaweza kumshukuru kwa kujieleza. Maneno yake yanaweza kukuonyesha mambo unayohitaji kufikiria unapozungumza naye kweli ya Biblia.
Ili Kutokeza Mambo Muhimu. Ikiwa unahutubia watu au unazungumza na mtu, jaribu kutumia maswali yanayoelekeza kwenye mambo muhimu. Hakikisha unauliza maswali ambayo kwa kweli wasikilizaji wangependa kujua majibu yake. Pia unaweza kutumia maswali yanayochochea fikira kwa sababu majibu yake si wazi. Ukitua kifupi baada ya kuuliza swali, inaelekea wasikilizaji watasikiliza kwa hamu zaidi mambo yanayofuata.
Pindi moja nabii Mika alitumia maswali kadhaa. Baada ya kuuliza juu ya takwa la Mungu kwa waabudu wake, nabii huyo aliuliza maswali mengine manne, labda kila swali likiwa na jibu. Maswali hayo yote yanawasaidia wasomaji kutazamia majibu yenye ufahamu wa ndani ambayo nabii huyo anamalizia mazungumzo. (Mika 6:6-8) Je, unaweza kufanya hivyo unapofundisha? Ebu jaribu.
Ili Kusababu Juu ya Habari. Maswali yanaweza kutumiwa kuwasaidia wengine waelewe sababu zinazotolewa. Yehova alifanya hivyo alipotoa matangazo mazito dhidi ya Israeli kama tunavyoona katika Malaki 1:2-10. Kwanza aliwaambia: “Nimewapenda ninyi.” Hawakuthamini upendo huo, akawauliza: “Je, Esau siye ndugu yake Yakobo?” Kisha Yehova akataja hali ya ukiwa ya Edomu ili kuthibitisha kwamba kwa sababu ya uovu wao, Mungu hakupenda taifa hilo. Kisha akaendelea kutoa mifano na kuuliza maswali ili kukazia jinsi ambavyo Israeli limeshindwa kuitikia vizuri upendo wake. Baadhi ya maswali hayo yanaulizwa kana kwamba ni makuhani wasio waaminifu wanayauliza. Mengine ni maswali ambayo Yehova anawauliza makuhani. Mazungumzo hayo yanatugusa moyo na kuvuta uangalifu wetu, na kusababu kunakotumiwa ni wazi kabisa, na ujumbe unaotolewa hauwezi kusahaulika.
Wasemaji wengine huuliza maswali mazuri kwa njia hiyo. Hata ingawa wasikilizaji hawatarajiwi kujibu, wao huyafikiria, kana kwamba wanashiriki katika mazungumzo hayo.
Tunapoongoza mafunzo ya Biblia, tunatumia njia inayomfanya mwanafunzi ashiriki. Bila shaka kuna faida zaidi ikiwa mwanafunzi hasomi tu majibu ambayo yamechapwa. Kwa sauti ya fadhili, tumia maswali ya ziada kusababu na mwanafunzi. Unapozungumzia mambo makuu, mtie moyo atumie Biblia kujibu. Pia unaweza kumwuliza: “Jambo tunalozungumzia linapatanaje na jambo hili jingine ambalo tumejifunza? Kwa nini ni muhimu? Jambo hili liguse maisha yetu kwa njia gani?” Kutumia maswali kwa njia hiyo ni bora kuliko kueleza imani yako au wewe mwenyewe kufafanua jambo kwa urefu mno. Kwa njia hiyo, unamsaidia mwanafunzi kutumia ‘nguvu za kufikiri’ kumwabudu Mungu.—Rom. 12:1.
Ikiwa mwanafunzi haelewi jambo fulani, uwe na subira. Labda anajaribu kulinganisha jambo unalosema na mambo ambayo ameamini kwa miaka mingi. Huenda ikafaa kuzungumzia jambo hilo kwa njia tofauti. Lakini nyakati nyingine unahitaji kusababu tu naye. Tumia Maandiko sana. Tumia mifano. Hali kadhalika, tumia maswali rahisi yanayomsaidia kusababu kwa msingi wa uthibitisho uliopo.
Ili Kutambua Hisia za Moyoni. Watu wanapojibu maswali, nyakati nyingine hawaonyeshi hisia zao za moyoni. Wanaweza tu kukupa majibu ambayo wanafikiri unataka. Unahitaji ufahamu. (Mit. 20:5) Kama Yesu, mwulize hivi: “Je, unaamini hili?”—Yn. 11:26.
Wanafunzi wengi wa Yesu walipokasirika na kumwacha kwa sababu ya jambo alilosema, Yesu aliwaomba mitume maoni yao. Akawauliza: “Nyinyi hamtaki kwenda pia, je, mwataka?” Petro akaonyesha hisia zao za moyoni, akasema: “Bwana, tutaenda zetu kwa nani? Wewe una semi za uhai udumuo milele; na sisi tumeamini na tumekuja kujua kwamba wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.” (Yn. 6:67-69) Pindi nyingine, Yesu aliwauliza wanafunzi wake: “Watu wanasema Mwana wa binadamu ni nani?” Kisha akauliza swali ambalo lingeonyesha maoni yao ya moyoni. “Ingawa hivyo, nyinyi mwasema mimi ni nani?” Petro akasema: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”—Mt. 16:13-16.
Unapoongoza funzo la Biblia, inaweza kufaa kutumia njia hizo kushughulikia hali fulani. Unaweza kumwuliza hivi: “Wanafunzi wenzako (au wafanyakazi wenzako) wanaonaje jambo hili?” Kisha uulize: “Wewe unalionaje?” Ukijua hisia za kweli za mtu, inakuwa rahisi kumsaidia sana ukiwa mwalimu.
Ili Kutia Mkazo. Unaweza kutumia maswali pia kukazia mawazo. Mtume Paulo alifanya hivyo katika Waroma 8:31, 32: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, nani atakayekuwa dhidi yetu? Yeye ambaye hakumwachilia hata Mwana wake mwenyewe bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, kwa nini pia yeye pamoja naye hatatupa sisi kwa fadhili vitu vingine vyote?” Ona kwamba kila swali linategemea maneno anayotangulia kutaja.
Nabii Isaya alionyesha usadikisho thabiti baada ya kuandika hukumu ya Yehova dhidi ya mfalme wa Babiloni, akiongezea kusema: “Maana BWANA wa majeshi amekusudia, naye ni nani atakayelibatili? na mkono wake ulionyoshwa, ni nani atakayeugeuza nyuma?” (Isa. 14:27) Maswali kama hayo huonyesha kwamba jambo linalotajwa haliwezi kukanushwa. Jibu halihitajiwi.
Ili Kufichua Fikira Zisizofaa. Maswali ambayo yamefikiriwa vizuri pia yanasaidia sana kufichua kufikiri kusikofaa. Kabla ya Yesu kumponya mtu fulani, aliwauliza Mafarisayo na wanasheria swali hili: “Je, yaruhusika kisheria kuponya siku ya sabato au sivyo?” Baada ya kumponya, akawauliza swali jingine: “Ni nani kati yenu, ikiwa mwana wake au fahali aanguka ndani ya kisima, hatamtoa nje mara hiyo siku ya sabato?” (Luka 14:1-6) Yesu hakutarajia wamjibu wala hawakumjibu. Maswali hayo yalifichua fikira zao zisizofaa.
Nyakati nyingine, hata Wakristo wa kweli wanaweza kufikiri isivyofaa. Katika karne ya kwanza, wengine katika Korintho walikuwa wakishtaki ndugu zao mahakamani ili kusuluhisha matatizo ambayo wao wenyewe walipaswa kuyasuluhisha kati yao. Mtume Paulo alifanyaje? Aliuliza maswali mengi hususa ili kurekebisha fikira zao.—1 Kor. 6:1-8.
Ukifanya mazoezi, unaweza kujifunza kutumia maswali vizuri. Lakini kumbuka kuonyesha heshima, hasa unapozungumza na watu wenye umri mkubwa, watu ambao huwafahamu, na wenye mamlaka. Tumia maswali kufundisha kweli ya Biblia kwa njia inayovutia.