SOMO LA 18
Kutumia Biblia Kujibu Maswali
TUNAPOULIZWA maswali yanayohusu imani yetu, maisha yetu, maoni yetu juu ya matukio ya nyakati zetu, na tumaini letu la wakati ujao, sisi hujitahidi kutumia Biblia kujibu. Kwa nini? Kwa sababu Biblia ni Neno la Mungu. Imani yetu inategemea Biblia. Maisha yetu yanategemea Biblia. Maoni yetu kuhusu matukio ya ulimwengu yanategemea Biblia. Tumaini letu la wakati ujao linategemea kabisa ahadi za Biblia zilizopuliziwa.—2 Tim. 3:16, 17.
Tunafahamu sana uzito wa jina letu. Sisi ni Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:12) Kwa hiyo, tunapojibu maswali, tunayajibu kulingana na maoni ya Yehova tunayopata katika Neno lake lililopuliziwa wala hatujibu kulingana na falsafa za wanadamu. Ingawa ni kweli kwamba kila mmoja wetu ana maoni yake kuhusu mambo mbalimbali, sisi huacha Neno la Mungu lirekebishe maoni yetu kwa sababu tunasadiki kabisa kwamba Neno hilo ndilo kweli. Bila shaka, Biblia inaturuhusu kuwa na maoni tofauti-tofauti katika masuala mengi. Badala ya kushurutisha wengine wafuate maoni yetu, sisi tunapenda kufundisha watu kanuni za Maandiko, na hivyo tunawaruhusu wawe na uhuru wa kuchagua kama sisi. Kama mtume Paulo, sisi hujaribu “kukuza utii kwa njia ya imani.”—Rom. 16:26.
Andiko la Ufunuo 3:14 linasema kwamba Yesu Kristo ni “shahidi mwaminifu na wa kweli.” Alijibu maswali na kukabiliana na hali kwa njia gani? Nyakati nyingine alitumia mifano iliyofanya watu wafikiri. Nyakati nyingine aliuliza yule mwenye kuuliza swali jinsi anavyofahamu andiko fulani. Mara nyingi alinukuu maandiko, alitaja jinsi maandiko yanavyosema, au aliyarejelea. (Mt. 4:3-10; 12:1-8; Luka 10:25-28; 17:32) Katika karne ya kwanza, kwa kawaida vitabu vya kukunjwa vya Maandiko vilihifadhiwa katika masinagogi. Hakuna jambo linaloonyesha kwamba Yesu alikuwa na vitabu vyake mwenyewe vya kukunjwa, lakini alijua sana Maandiko na aliyarejelea mara nyingi alipokuwa akifundisha wengine. (Luka 24:27, 44-47) Kwa kweli angeweza kusema kwamba yale aliyofundisha hayakutokana na ubuni wake. Alisema mambo aliyosikia kutoka kwa Baba yake.—Yn. 8:26.
Tunataka kuiga mfano wa Yesu. Hakuna mmoja wetu ambaye amewahi kumsikia Mungu akisema, kama alivyomsikia Yesu. Lakini Biblia ni Neno la Mungu. Tukiitumia kujibu maswali, tunaepuka kujielekezea fikira. Tunaonyesha tumeazimia kabisa kufuata maoni ya Mungu kuhusu kweli badala ya kutoa maoni ya wanadamu wasiokamilika.—Yn. 7:18; Rom. 3:4.
Bila shaka, tamaa yetu si kutumia tu Biblia bali ni kuitumia kwa njia inayomfaidi zaidi msikilizaji. Tunataka asikilize bila kuwa na maoni yenye ubaguzi. Kwa kutegemea maoni yake, unaweza kutaja mambo yanayotokana na Biblia kwa kusema: “Je, hukubali kwamba maneno ya Mungu ndiyo muhimu zaidi?” Au unaweza kusema: “Je, unajua kwamba Biblia inazungumzia swali hili hasa?” Ikiwa unazungumza na mtu ambaye haamini Biblia, unaweza kutumia utangulizi tofauti kidogo. Unaweza kusema: “Ebu nikueleze unabii huu wa kale.” Au unaweza kusema: “Kitabu ambacho kimeenezwa zaidi katika historia kinasema hivi . . . ”
Nyakati nyingine, unaweza kutaja tu jinsi andiko fulani linavyosema. Lakini, ikiwezekana ni afadhali zaidi kufungua Biblia na kuisoma. Mwonyeshe mtu huyo andiko hilo katika Biblia yake hali ikiruhusu. Kutumia Biblia moja kwa moja kwa njia hiyo mara nyingi hugusa sana mioyo ya watu.—Ebr. 4:12.
Wazee Wakristo wana wajibu wa kipekee wa kutumia Biblia wanapojibu maswali. Mojawapo ya sifa za kumstahilisha mtu awe mzee ni “kushika kwa imara lile neno la uaminifu kwa habari ya usanifu wa kufundisha kwake.” (Tito 1:9) Mshiriki wa kutaniko anaweza kufanya maamuzi mazito maishani baada ya kushauriwa na mzee. Ni muhimu shauri litegemee Maandiko. Mfano ambao mzee anaweka unaweza kuwa na uvutano sana juu ya jinsi wengine wanavyofundisha.