Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jr sura 4 kur. 43-53
  • Jihadhari na Moyo Wenye Hila

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jihadhari na Moyo Wenye Hila
  • Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MIOYO YENYE HILA INAWEZA KUDANGANYA
  • JINSI YEHOVA ANAVYOTUFINYANGA
  • KUBALI KUFINYANGWA NA YEHOVA
  • Je, Kila Siku Unauliza, “Yehova Yuko Wapi?”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • “Siwezi Kunyamaza Kimya”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • Kitabu Cha Biblia Namba 26—Yeremia
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • “Uwaambie Neno Hili”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
Pata Habari Zaidi
Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
jr sura 4 kur. 43-53

SURA YA NNE

Jihadhari na Moyo Wenye Hila

1, 2. Kwa nini si rahisi kujua jinsi moyo wetu wa mfano ulivyo kikweli?

TUSEME kwamba ni asubuhi, ungali kitandani, kisha upate maumivu makali kifuani na kushindwa kupumua. Huenda ukawaza, ‘Yawezekana kwamba ni mshtuko wa moyo?’ Huwezi tu kupuuza hali hiyo. Lazima uchukue hatua mara moja. Huenda ukapiga simu gari la wagonjwa mahututi lije kukuchukua na kukukimbiza hospitalini. Daktari atakupima kwa uangalifu, akitumia mashini mbalimbali. Kupata matibabu haraka iwezekanavyo kwaweza kuokoa uhai wako.

2 Namna gani moyo wetu wa mfano? Si rahisi kujua jinsi ulivyo. Kwa nini? Biblia inasema: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” (Yer. 17:9) Kwa hiyo, moyo wetu unaweza kutudanganya na kutufanya tuamini kwamba hatuna tatizo lolote la kiroho, ijapokuwa wengine wanaona ishara na kutuhangaikia. Kwa nini tudanganyike? Huenda tukafumbwa macho na mwelekeo wetu wenyewe wa kutenda dhambi, hali kadhalika Shetani na ulimwengu huu mwovu. Ili kujua jinsi ya kuuchunguza moyo wetu, tunaweza kujifunza mengi kutokana na Yeremia na watu wa Yuda walioishi nyakati hizo.

3. Ni nini kimekuwa miungu kwa watu wengi?

3 Wayudea wengi walikuwa na mioyo mibovu kiroho. Walimwacha Mungu wa pekee wa kweli na kuanza kuabudu miungu ya Kanaani. Dhamiri yao haikuwasumbua hata kidogo. Yehova aliwaambia hivi waabudu hao: “Iko wapi miungu yako ambayo umejifanyia? Na isimame ikiwa inaweza kukuokoa wakati wa msiba wako. Kwa maana miungu yako imekuwa kama hesabu ya majiji yako.” (Yer. 2:28) Leo, huenda tusijione kuwa waabudu wa sanamu. Hata hivyo, kamusi moja inafafanua neno “mungu” kuwa “mtu au kitu chenye thamani kubwa.” Watu wengi ulimwenguni hutanguliza maishani mwao kazi, afya, familia, au hata wanyama vipenzi. Wengine huona michezo, watu mashuhuri, tekinolojia, kusafiri, au utamaduni wao kuwa mambo muhimu zaidi. Wengi hupuuza uhusiano wao na Muumba wao wakikimbizana na vitu hivyo. Je, Wakristo wa kweli wanaweza kuathiriwa na maoni hayo, kama vile watu wa Yuda katika siku za Yeremia walivyoathiriwa?

MIOYO YENYE HILA INAWEZA KUDANGANYA

4. Watu waliosema: “Neno la Yehova liko wapi? Na liingie, tafadhali,” walisema hivyo kutoka moyoni? Eleza.

4 Fikiria mistari inayozunguka maneno ya Yeremia kuhusu moyo kuwa hatari. Alitambua kwamba watu walikuwa wakisema: “Neno la Yehova liko wapi? Na liingie, tafadhali.” (Yer. 17:15) Lakini je, walikuwa wakisema hivyo kutoka moyoni? Sura hiyo ya kitabu cha Yeremia inaanza kwa kusema: “Dhambi ya Yuda imeandikwa kwa kalamu ya chuma. Imechongwa kwa ncha ya almasi juu ya bamba la moyo wao.” Tatizo kubwa lilikuwa kwamba Wayudea hao walikuwa ‘wakimtegemea mtu wa udongo, wakiufanya mwili wa nyama kuwa mkono wao, na moyo wao kumwacha Yehova.’ Walikuwa tofauti na wachache ambao walimtegemea Mungu awaongoze na kuwabariki.—Yer. 17:1, 5, 7.

5. Watu wa siku za Yeremia waliitikia jinsi gani maagizo ya Yehova?

5 Kilichokuwa katika mioyo ya wengi kilionekana wazi kutokana na jinsi walivyoitikia maneno ya Mungu. (Soma Yeremia 17:21, 22.) Kwa mfano, siku ya Sabato ilipaswa kuwa siku ya kupumzika kutokana na shughuli za kawaida na kufanya mambo ya kiroho. Watu walioishi siku hizo hawakupaswa kufanya shughuli zozote siku ya Sabato. Hata hivyo, matendo yao yalifunua yaliyokuwa moyoni mwao. “Hawakusikiliza wala kutega sikio lao, nao wakafanya shingo yao kuwa ngumu ili wasisikie na ili wasipokee nidhamu.” Ijapokuwa walijua sheria ya Mungu, walifanya wapendavyo—walifanya shughuli zao siku ya Sabato.—Yer. 17:23; Isa. 58:13.

6, 7. (a) Licha ya shauri kutoka kwa jamii ya mtumwa mwaminifu, huenda Mkristo akawa na maoni gani yasiyofaa? (b) Huenda hilo likaathiri jinsi gani kuhudhuria mikutano?

6 Leo, hatuko chini ya sheria ya Sabato. Hata hivyo, tunaweza kujifunza kutokana na jinsi watu hao walivyotenda, na kufunua yaliyokuwa moyoni mwao. (Kol. 2:16) Ili kufanya mapenzi ya Mungu, tumeondolea mbali mapendezi yetu ya kibinafsi. Tunatambua kwamba ni upumbavu kujichagulia wenyewe jinsi tunavyoweza kumpendeza Mungu. Pia, yamkini tumepata kujua wengi ambao wamejitahidi kufanya mapenzi ya Mungu na kwa kweli wakawa na uradhi maishani. Hivyo basi, tunaweza kupotoshwa jinsi gani?

7 Mkristo anaweza kufikiri kimakosa kwamba moyo wake hauwezi kamwe kumdanganya, kama wengi walivyofikiri katika siku za Yeremia. Kwa mfano, huenda mtu akasema, ‘Lazima nifanye kazi ili niruzuku familia yangu,’ jambo ambalo linaeleweka. Lakini namna gani akianza kufikiri, ‘Nahitaji kuongeza elimu ili kupata kazi nzuri zaidi’? Huenda hilo pia likaonekana kuwa wazo linalofaa, ambalo huenda likamfanya awaze: ‘Mambo yamebadilika siku hizi, mtu anahitaji kusoma hadi chuo cha ufundi au chuo kikuu ili asije akapoteza kazi.’ Bila kuwa mwangalifu, mtu anaweza kuanza kupuuza shauri lenye hekima, na lenye usawaziko kutoka kwa jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara kuhusu elimu ya ziada, na kuanza kukosa mikutano! Wengine wamefinyangwa na maoni ya ulimwengu kuhusu elimu. (Efe. 2:2, 3) Biblia inaonya hivi: “Msiige tabia na mienendo ya dunia hii.”—Rom. 12:2, Neno—Agano Jipya.a

Picha katika ukurasa wa 46

Je, moyo wako umekudanganya ukose mikutano?

8. (a) Ni mambo gani yanayoweza kumfanya Mkristo awe na kiburi? (b) Kwa nini haitoshi tu kujua mambo fulani kumhusu Mungu na mambo ambayo amefanya?

8 Ni kweli kwamba Wakristo fulani katika karne ya kwanza walikuwa na mali na hata labda walikuwa na umashuhuri fulani katika ulimwengu. Leo pia kuna Wakristo kama hao. Wanapaswa kuona jinsi gani mafanikio yao, nasi tunapaswa kuwa na maoni gani kuwaelekea? Yehova anajibu kupitia Yeremia. (Soma Yeremia 9:23, 24.) Badala ya kujisifu kwa sababu ya mafanikio ya kimwili, jambo la hekima ni kutambua kwamba jambo kuu ni kumjua Mwenye Enzi Kuu. (1 Kor. 1:31) Hivyo basi, inamaanisha nini kumfahamu na kumjua Yehova? Watu katika siku za Yeremia walijua jina la Mungu. Walijua pia mambo aliyofanya alipowakomboa mababu zao katika Bahari Nyekundu, walipokuwa wakiingia Nchi ya Ahadi, wakati wa Waamuzi, na wakati wa utawala wa wafalme waaminifu. Lakini kwa kweli hawakumjua Yehova wala kumwamini kikweli. Hata hivyo walisema: “Nimebaki bila hatia. Hakika hasira [ya Mungu] imeondoka juu yangu.”—Yer. 2:35.

Kwa nini ni muhimu kujua kwamba mioyo yetu ni yenye hila? Tunaweza kuchunguza mioyo yetu jinsi gani ili kujua jinsi Mchunguzaji Mkuu wa mioyo yetu anavyotuona?

JINSI YEHOVA ANAVYOTUFINYANGA

Picha katika ukurasa wa 48

Je, unamruhusu Yehova akufinyange?

9. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba watu wanaweza kubadili mtazamo wao, nao wanaweza kufanya hivyo jinsi gani?

9 Wayahudi ambao Yeremia aliwatangazia ujumbe wa Mungu walihitaji kubadili mtazamo wao. Hilo lingewezekana kwa sababu Mungu aliwaambia hivi wale ambao wangerudi kutoka uhamishoni: “Nitawapa moyo wa kunijua, kwamba mimi ni Yehova; nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao, kwa maana watarudi kwangu.” (Yer. 24:7) Badiliko kama hilo linawezekana leo pia. Isitoshe, huenda sisi pia tunahitaji kubadili moyo wetu wa mfano. Mambo matatu ni muhimu: kujifunza kwa bidii Neno la Mungu, kutambua mambo ambayo Mungu anatufanyia maishani, na kutumia mambo ambayo tumejifunza kumhusu. Tofauti na watu wa siku za Yeremia, tunapaswa kuwa tayari kumruhusu Mchunguzaji Mkuu auchunguze moyo wetu. Tunaweza kuuchunguza moyo wetu kwa kutegemea Biblia na pia kwa kutambua mambo ambayo Yehova ametufanyia. (Zab. 17:3) Ni jambo la hekima kama nini kufanya hivyo!

10, 11. (a) Kwa nini Yeremia alienda kwa mfinyanzi? (b) Ni nini kinachoamua jinsi Yehova anavyowafinyanga watu?

10 Shetani anataka kuwafinyanga watu wote wafanane, lakini Mungu anawafinyanga watu kulingana na mahitaji ya kila mmoja. Kwa mfano, fikiria kisa hiki alichojionea Yeremia. Siku moja, Mungu alimwagiza aende katika nyumba ya mfinyanzi. Mfinyanzi alikuwa akifanya kazi juu ya magurudumu ya kufinyangia. Chombo alichokuwa akifinyanga kilipoharibika, alikifinyanga kuwa chombo kingine. (Soma Yeremia 18:1-4.) Kwa nini Yeremia aliagizwa atazame mfinyazi akiwa kazini, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano huo?

11 Yehova alitaka kumwonyesha Yeremia na Waisraeli kwamba ana mamlaka ya kuwafinyanga watu na mataifa vyovyote apendavyo. Mungu anaufinyanga jinsi gani udongo? Tofauti na wanadamu, Yehova hakosei; wala kubadili-badili nia. Kwa kutegemea jinsi watu wanavyoitikia ufinyanzi, Yehova huamua atakavyowatumia.—Soma Yeremia 18:6-10.

12. (a) Yehoyakimu aliitikia jinsi gani ufinyanzi wa Yehova? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi kuhusu Yehoyakimu?

12 Hivyo basi, Yehova huwafinyanga watu jinsi gani? Kwanza kabisa, anatumia Biblia. Mtu anaposoma Neno la Mungu na kulifuata, anafunua utu wake, naye Mungu anamfinyanga. Na tuchunguze mfano wa Mfalme Yehoyakimu ili kuona jinsi watu wa siku za Yeremia walivyofinyangwa katika shughuli za kila siku maishani. Sheria ilisema kwamba mtu ‘hapaswi kumpunja mfanyakazi wa kukodiwa,’ lakini mfalme alifanya hivyo, akiwatumikisha Waisraeli wenzake wamjengee “nyumba yenye nafasi tele” bila mshahara. (Kum. 24:14; Yer. 22:13, 14, 17) Mungu alijaribu kumfinyanga Yehoyakimu akitumia neno Lake kupitia manabii. Lakini mfalme alifuata tamaa za moyo wake wenye hila. Alisema, “Sitatii” naye akaendelea kufuata njia aliyochagua tangu ujana wake. Hivyo, Mungu akasema: “[Yehoyakimu] atazikwa kwa maziko ya punda-dume, kwa kukokotwa na kutupwa.” (Yer. 22:19, 21) Ungekuwa upumbavu kama nini ikiwa tungesema: ‘Mimi nilizaliwa hivyo, siwezi kubadilika’! Leo, ingawa Mungu hatumi manabii kama Yeremia, anatupa mwongozo. Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara inatusaidia kuelewa na kutumia kanuni za Biblia. Huenda kanuni hizo zikahusu mambo ya kawaida maishani, kama vile mavazi na mapambo au muziki na kucheza dansi wakati wa arusi au matukio mengine. Je, tutaruhusu Neno la Mungu litufinyange?

13, 14. (a) Kwa nini Wayahudi waliokuwa na watumwa waliwaachilia? (b) Ni nini kilichofunua kilichokuwa katika mioyo yao?

13 Tuchukue mfano mwingine. Wababiloni walimtawaza Sedekia kuwa mfalme kibaraka wa Yuda. Ingawa Mungu alikuwa amemshauri kupitia Yeremia, Sedekia aliasi. (Yer. 27:8, 12) Wababiloni walizingira Yerusalemu. Mfalme na wakuu waliona inafaa kuchukua hatua na kutenda kulingana na Sheria ili wapate kibali cha Mungu. Akijua kwamba watumwa Waebrania wangeachiliwa huru katika mwaka wa saba wa utumwa wao, Sedekia alifanya agano la kuwaachilia. (Kut. 21:2; Yer. 34:14) Yerusalemu likiwa limezingirwa na adui, watu wakawaachilia watumwa wao!—Soma Yeremia 34:8-10.

14 Baadaye, majeshi ya Misri yakaja kuwasaidia wakaaji wa Yerusalemu, hatua iliyowafanya Wababiloni waondoke. (Yer. 37:5) Wale waliokuwa wamewaachilia watumwa wao wangefanya nini sasa? Waliwatumikisha tena kwa lazima. (Yer. 34:11) Wayahudi hao walipokuwa hatarini walijifanya wanashika sheria za Mungu, kana kwamba kufanya hivyo kungefunika mwenendo wao mbaya. Lakini hali ilipotulia, wakarudia njia zao za zamani. Licha ya kujifanya kwamba wanaishika Sheria, matendo yao ya baadaye yalionyesha kwamba mioyo yao haikutaka kufuata mwongozo wa Neno la Mungu na kufinyangwa kulingana nalo.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo ambayo Yeremia aliandika kuhusu mfinyanzi? Yehova anatufinyanga jinsi gani leo?

KUBALI KUFINYANGWA NA YEHOVA

15. Ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba tuko tayari kufinyangwa na Yehova?

15 Kutaniko la Yehova la ulimwenguni pote hutusaidia kuelewa kanuni mbalimbali za Biblia kuhusu mambo hususa. Kwa mfano, tunajua jinsi tunavyopaswa kutenda ikiwa ndugu fulani ametukosea. (Efe. 4:32) Huenda hata tukakiri kwamba shauri hilo la Biblia linafaa na ni lenye hekima. Lakini swali ni: Sisi ni udongo wa aina gani? Je, kwa kweli tutakubali kufinyangwa na Yehova? Ikiwa moyo wetu unaweza kufinyangwa, tutabadilika; Mfinyanzi Mkuu atatufinyanga tuwe chombo anachoweza kukitumia kutimiza kusudi lake. (Soma Waroma 9:20, 21; 2 Timotheo 2:20, 21.) Badala ya kuwa na moyo kama wa Yehoyakimu au Wayahudi waliokuwa na watumwa katika siku za Sedekia, tunapaswa kumruhusu Yehova atufinyange kwa ajili ya kusudi lenye kuheshimika.

16. Yeremia alitambua jambo gani muhimu?

16 Hata Yeremia mwenyewe alifinyangwa na Mungu. Nabii huyo alikuwa na mtazamo gani? Maneno yake yanaonyesha: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” Kisha akaomba: “Ee Yehova, nirekebishe.” (Yer. 10:23, 24) Vijana, je, mtamwiga Yeremia? Yaelekea mna maamuzi mengi ya kufanya siku za usoni. Vijana fulani hutaka ‘kuongoza hatua zao.’ Je, utamtegemea Mungu akuongoze unapofanya maamuzi? Kama Yeremia, utakiri kwa unyoofu kwamba wanadamu hawawezi kuongoza hatua zao? Kumbuka: Ukiutafuta mwongozo wa Mungu, yuko tayari kukufinyanga.

17-19. (a) Kwa nini Yeremia alifunga safari ndefu kwenda Efrati? (b) Utii wa Yeremia ulijaribiwa jinsi gani? (c) Yote ambayo Yeremia alifanya kuhusiana na mshipi yalitimiza nini?

17 Ili kuutimiza mgawo wake ifaavyo, Yeremia alipaswa kutii mwongozo wa Mungu. Kama ungekuwa Yeremia, je, ungefuata maagizo aliyopewa? Pindi moja, Yehova alimwambia Yeremia atafute mshipi wa kitani na ajifunge kiunoni. Kisha, Mungu akamwamuru asafiri mpaka Efrati. Ukitazama ramani, utaona kwamba alipaswa kusafiri kilomita 500 hivi. Baada ya kufika huko, Yeremia alipaswa kuuficha mshipi huo katika mpasuko wa mwamba kisha arudi Yerusalemu. Baadaye, Mungu alimwagiza afunge safari hiyo tena kwenda kuuchukua. (Soma Yeremia 13:1-9.) Kwa ujumla, huenda Yeremia alisafiri kilomita 1,900 hivi. Wachambuzi wa Biblia hudai haiwezekani kwamba alisafiri mbali hivyo, kwa miezi kadhaa.b (Ezra 7:9) Hata hivyo, hilo lilikuwa agizo la Mungu naye Yeremia alitii.

18 Wazia nabii huyo akipanda na kushuka milima ya Yudea, kisha akipitia jangwani kuelekea Efrati, ikitegemea njia aliyopitia. Kwa kusudi gani? Ili tu kwenda kuuficha mshipi wa kitani! Haikosi kutoweka kwake kwa muda mrefu kuliwashangaza jirani zake. Aliporudi, hakuwa na ule mshipi wa kitani. Kisha Mungu akamwambia afunge safari tena kwenda kuuchukua ule mshipi ambao sasa ulikuwa umeoza na “haufai jambo lolote.” Ingalikuwa rahisi kwake kusema: ‘Sasa imezidi. Sioni haja!’ Hata hivyo, kwa kuwa alikuwa amefinyangwa na Mungu, hakusema hivyo. Badala ya kulalamika, alifanya vile alivyoagizwa!

Picha katika ukurasa wa 53

Kwa nini tunapaswa kutii maagizo ya Yehova hata ikiwa hatuyaelewi?

19 Baada ya kwenda na kurudi mara ya pili, ndipo Mungu alipofafanua mambo. Baada ya Yeremia kufanya yote hayo, sasa angeweza kutangaza ujumbe huu muhimu: “Watu hawa wabaya wanaokataa kuyatii maneno yangu, wanaotembea katika ukaidi wa moyo wao na wanaoendelea kufuata miungu mingine ili kuitumikia na kuiinamia, pia watakuwa kama mshipi huu ambao haufai kwa jambo lolote.” (Yer. 13:10) Yehova alitumia njia bora kama nini ili kuwafundisha watu wake! Utii wa Yeremia wa kutoka moyoni katika jambo ambalo lilionekana kuwa dogo ulitimiza fungu muhimu katika jitihada za Yehova za kufikia mioyo ya watu wake.—Yer. 13:11.

20. Kwa nini huenda utii wako ukawashangaza wengi, lakini unaweza kuwa na uhakika gani?

20 Wakristo leo hawaagizwi watembee mamia ya kilomita ili watu wajifunze jambo fulani. Hata hivyo, je, inawezekana kwamba majirani na marafiki wanakushangaa au hata kukuchambua kwa sababu ya kuishi maisha ya Kikristo? Huenda wakashangazwa na mambo kama vile mavazi, elimu, kazi, au hata maoni yako kuhusu pombe. Je, utaazimia kufuata mwongozo wa Mungu kama Yeremia alivyofanya? Ukifanya maamuzi yanayoonyesha kwamba moyo wako unafinyangwa na Mungu, huenda ukapata nafasi za kutoa ushahidi mzuri. Vyovyote vile, ukitii mwongozo wa Yehova unaopatikana katika Neno lake na kukubali mwongozo anaotoa kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu utapata faida ya milele. Badala ya kuongozwa na moyo wenye hila, unaweza kuwa kama Yeremia. Hivyo basi, azimia kukubali kufinyangwa na Mungu; mwache akufanye kuwa chombo kwa ajili ya matumizi yenye heshima ili akutumie milele.

Kwa nini tunapaswa kupambana na mikazo ya Shetani, moyo wetu usio mkamilifu, na ulimwengu?

a Tafsiri ya NET Bible (2005) inasema: “Msipatanishwe na ulimwengu wa sasa.” Maelezo ya chini yanaongeza: “Inaonekana kwamba si lazima mtu achukue hatua ili ‘kupatanishwa’ na ulimwengu wa sasa, ni jambo linalotendeka, kwa kiasi fulani, pasipo hata mtu kufikiria. Hata hivyo, . . . huenda kwa kiasi fulani mtu akatambua na kukubali mabadiliko yanayoendelea. Yawezekana kwamba hali zote mbili zinahusika.”

b Wengine hudai kwamba mahali ambapo Yeremia alienda palikuwa karibu wala si Efrati. Kwa nini? “Msingi pekee wa kudai hivyo,” asema msomi mmoja, “ni kumwepusha nabii huyo na safari mbili ndefu kutoka Yerusalemu mpaka Efrati.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki