Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
JANUARI 1-7
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 1-3
“Ufalme wa Mbinguni Umekaribia”
nwtsty habari za utafiti—Mt 3:1, 2
kuhubiri: Neno la Kigiriki linamaanisha hasa “kutoa tangazo ukiwa mjumbe wa hadharani.” Linakazia namna tangazo hilo linavyofanywa: kwa kawaida ni tangazo linalofanywa waziwazi na hadharani badala ya kutolewa kama hotuba mbele ya kikundi cha watu.
Ufalme: Neno la Kigiriki ba·si·leiʹa linaonekana kwa mara ya kwanza, linamaanisha serikali ya kifalme, eneo linalotawaliwa na watu wanaotawaliwa na mfalme. Neno hilo linalopatikana mara 162 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, linapatikana mara 55 katika masimulizi ya Mathayo na mara nyingi zaidi linarejelea ufalme wa mbinguni wa Mungu. Mathayo anatumia neno hilo mara nyingi sana hivi kwamba Injili yake inaweza kuitwa Injili ya Ufalme.
Ufalme wa mbinguni: Maneno hayo yanaonekana mara 30 hivi na yanapatikana katika Injili ya Mathayo tu. Injili za Marko na Luka zinatumia maneno “Ufalme wa Mungu,” kuonyesha kwamba “Ufalme wa Mungu” uko katika mbingu za kiroho na unatawala kutoka huko.—Mt 21:43; Mk 1:15; Lu 4:43; Da 2:44; 2Ti 4:18.
umekaribia: Linatumiwa kuashiria kwamba Mfalme wa wakati ujao wa Ufalme wa Mbinguni alikuwa karibu kutokea.
nwtsty picha
Mavazi na Mwonekano wa Yohana Mbatizaji
Yohana alivaa vazi lililofumwa kwa manyoya ya ngamia na kiunoni alijifunga mshipi wa ngozi ambao ungeweza kutumiwa kubeba vitu vidogovidogo. Nabii Eliya alivaa vazi kama hilo. (2Fa 1:8) Mavazi yaliyofumwa kwa manyoya ya ngamia yalitengenezwa kwa kitambaa kigumu na kwa kawaida yalivaliwa na maskini. Tofauti na hilo, matajiri walivalia mavazi laini yaliyotengenezwa kwa hariri au kitani. (Mt 11:7-9) Kwa kuwa Yohana alikuwa Mnadhiri tangu alipozaliwa, inawezekana kwamba nywele zake hazikuwahi kukatwa. Kwa hiyo, kutokana na mavazi yake na jinsi alivyoonekana, huenda mtu angetambua mara moja kwamba aliishi maisha rahisi na alijitoa kikamili kufanya mapenzi ya Mungu.
Nzige
Neno “nzige” linalotumiwa katika Biblia linaweza kumaanisha aina yoyote ya panzi wenye vipapasio vifupi, hasa panzi wanaohamahama wakiwa katika makundi. Kulingana na uchunguzi uliofanywa jijini Jerusalem, asilimia 75 ya mwili wa nzige hao wa jangwani una virutubisho vya protini. Leo nzige wanapoliwa katika Mashariki ya Kati, kichwa, miguu, mabawa, na tumbo huondolewa. Sehemu ya kifua huliwa ikiwa mbichi au ikiwa imepikwa. Inasemekana kwamba wana ladha kama ya uduvi au kaa na wana protini nyingi sana.
Asali ya Mwituni
Picha zinaonyesha mzinga wa nyuki uliotengenezwa na nyuki wa mwituni (1) na sega lililojaa asali (2). Inawezekana kwamba asali ambayo Yohana alikula ilitengenezwa na jamii ya nyuki wa mwituni wanaojulikana kama Apis mellifera syriaca, ambao ni nyuki wa asili wa eneo hilo. Jamii hii ya nyuki inaweza kustahimili kuishi katika maeneo makame na yenye joto ya nyika ya Yudea lakini hawafai kufugwa kwa sababu wanawashabulia wanadamu. Hata hivyo, mapema katika karne ya tisa K.W.K., watu walioishi Israeli walifuga nyuki kwenye mizinga ya udongo wa mfinyanzi. Mabaki mengi ya mizinga hiyo iligunduliwa katikati ya eneo ambalo huenda zamani lilikuwa la mjini (sasa linajulikana kama Tel Rehov), lililoko katika Bonde la Yordani. Asali iliyopatikana katika mizinga hii ilitengenezwa na jamii ya nyuki ambao inaonekana walihamishwa kutoka katika eneo ambalo sasa ni Uturuki.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mt 1:3
Tamari: Mwanamke wa kwanza kati ya wanawake watano wanaotajwa katika orodha ya Mathayo ya ukoo wa Masihi. Wale wengine wanne ni Rahabu na Ruthu ambao wote wawili hawakuwa Waisraeli (mst. 5); Bath-sheba, “mke wa Uria” (mst. 6); na Maria (mst. 16). Inawezekana wanawake hao walitiwa ndani ya orodha hiyo ya ukoo inayotaja wanaume tu kwa sababu kuna jambo la pekee katika njia ambayo kila mmoja wao alikuja kuwa nyanya (bibi) ya Yesu.
nwtsty habari za utafiti—Mt 3:11
ninawabatiza: Au “ninawazamisha.” Neno la Kigiriki ba·ptiʹzo linamaanisha “kuchovya; kutumbukiza.” Marejeo mengine ya Biblia yanaonyesha kwamba kubatiza kunahusisha kuzamisha kabisa. Katika kisa kimoja, Yohana alikuwa akibatiza katika eneo la Bonde la Yordani karibu na Salimu “kwa sababu kulikuwa na maji mengi huko.” (Yoh 3:23) Filipo alipokuwa akimbatiza towashi Mwethiopia, wote wawili “wakaingia ndani ya maji.” (Mdo 8:38) Neno hilohilo la Kigiriki linatumiwa katika Septuajinti kwenye 2Fa 5:14 linapoeleza kwamba Naamani “[alijitumbukiza] mara saba katika Mto Yordani.”
JANUARI 8-14
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 4-5
“Mambo Tunayojifunza Kutokana na Mahubiri ya Yesu ya Mlimani”
nwtsty habari za utafiti—Mt 5:3
Wenye furaha: Si hali ya kuchangamka tu, kama mtu anavyohisi anapoburudika. Badala yake, linapotumiwa kuwahusu wanadamu, neno hilo linamaanisha hali anayokuwa nayo mtu aliyebarikiwa na Mungu na anayefurahia kibali chake. Neno hilo linatumiwa pia kueleza jinsi Mungu na Yesu walivyo katika utukufu wa mbinguni.—1Ti 1:11; 6:15.
wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho: Neno la Kigiriki linalorejelewa “wale wanaotambua,” kihalisi linamaanisha, “wale ambao ni maskini (wenye uhitaji; fukara; ombaomba),” katika muktadha huu linatumiwa kuwahusu wale wenye uhitaji na wanaotambua kabisa kwamba wana uhitaji huo. Neno hilohilo lilitumiwa kumhusu Lazaro ambaye alikuwa “ombaomba” anayetajwa katika Lu 16:20, 22. Katika Kigiriki maneno hayo ambayo yanatafsiriwa katika tafsiri fulani kuwa wale ambao ni “maskini wa roho” yanatokeza wazo la watu ambao wanatambua kabisa umaskini wao wa kiroho na kwamba wanamhitaji Mungu sana.
nwtsty habari za utafiti—Mt 5:7
wenye rehema: Neno linalotumiwa katika Biblia kurejelea “wenye rehema” na “rehema” halihusu tu kusamehe au kuwa na huruma unapohukumu. Mara nyingi linatumiwa kuelezea hisia za huruma na kuwasikitika wengine ambazo humchochea mtu kuchukua hatua ya kuwasaidia wenye uhitaji.
nwtsty habari za utafiti—Mt 5:9
wanaofanya amani: Wale ambao huleta amani mahali ambapo inakosekana na si tu kudumisha amani.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mt 4:9
kunifanyia tendo la ibada: Kitenzi cha Kigiriki kinachoweza kurejelea “kuabudu” kinatumiwa hapa katika njeo inayoonyesha kitendo kisichorudiwa, kinachofanyika mara moja na kupita. Kurejelewa kwa kitenzi hicho, yaani, “[fanya] tendo la ibada” kunaonyesha kwamba Ibilisi hakumwomba Yesu amfanyie ibada kwa ukawaida au kwa kuendelea; alitaka amfanyie “tendo [moja tu] la ibada.”
nwtsty habari za utafiti—Mt 4:23
kufundisha . . . kuhubiri: Kufundisha kunatofautiana na kuhubiri katika maana ya kwamba mwalimu anafanya mengi zaidi ya kutangaza ujumbe; anafunza, anafafanua, anatumia hoja zenye ushawishi, na kutoa uthibitisho.
JANUARI 15-21
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 6-7
“Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme”
nwtsty habari za utafiti—Mt 6:24
mtumwa: Kitenzi cha Kigiriki kinarejelea kufanya kazi ya mtumwa, kinamaanisha mtu anayemilikiwa na bwana mmoja tu. Yesu hapa alikuwa akieleza kwamba Mkristo hawezi kumpa Mungu ujitoaji kamili ambao anastahili na wakati huohuo ajitoe kutafuta mali za kimwili.
nwtsty habari za utafiti—Mt 6:33
Endeleeni . . . kuutafuta: Kitenzi cha Kigiriki kilichotumiwa kinaonyesha tendo la kuendelea na kinaweza pia kuandikwa “Tafuta bila kuacha.” Wafuasi wa kweli wa Yesu hawautafuti Ufalme kwa muda fulani na kisha kwenda kufanya mambo mengine. Badala yake, sikuzote wanapaswa kuutanguliza katika maisha yao.
Ufalme: Baadhi ya hati za kale za Kigiriki zinasema “Ufalme wa Mungu.”
wake: Inarejelea Mungu, “Baba wa mbinguni” anayetajwa katika Mt 6:32.
uadilifu: Wale wanaotafuta uadilifu wa Mungu wanafanya mapenzi yake na wako tayari kufuata viwango vyake vya mema na mabaya. Fundisho hili ni tofauti kabisa na fundisho la Mafarisayo, ambao walifikiria kuanzisha uadilifu wao wenyewe.—Mt 5:20.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mt 7:28, 29
ukashangazwa: Kitenzi cha Kigiriki kilichotumiwa hapa kinaweza kumaanisha “kustaajabu sana kiasi cha kupigwa na bumbuazi.” Kitenzi hicho kinachoonyesha tendo linaloendelea kinaashiria kwamba umati haungeweza kusahau maneno yake.
njia yake ya kufundisha: Maneno hayo yanarejelea jinsi Yesu alivyofundisha, yaani, mbinu alizotumia kufundisha, zilizotia ndani mambo aliyofundisha, maagizo yote ya Mahubiri ya Mlimani.
si kama waandishi wao: Badala ya kunukuu maneno ya marabi walioheshimiwa, kama ilivyokuwa desturi ya waandishi, Yesu anazungumza akiwa mwakilishi wa Yehova, kama mtu mwenye mamlaka, mafundisho yake yakitegemea Neno la Mungu.—Yoh 7:16.
JANUARI 22-28
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 8-9
“Yesu Aliwapenda Watu”
nwtsty habari za utafiti—Mt 8:3
akamgusa: Sheria ya Musa iliagiza wagonjwa wa ukoma watengwe ili kuwalinda watu wengine wasiambukizwe ugonjwa huo. (Law 13:45, 46; Hes 5:1-4) Hata hivyo, viongozi wa dini ya Kiyahudi, walitunga sheria za ziada. Kwa mfano, hakuna mtu yeyote aliyeruhusiwa kusimama umbali wa mikono 4 hivi, yaani, karibu mita 1.8 kutoka kwa mgonjwa wa ukoma. Lakini kulipokuwa na upepo mkali, hakuna aliyeruhusiwa umbali wa mikono 100, yaani, karibu mita 45. Sheria kama hizo zilifanya watu wenye ukoma wadharauliwe. Mapokeo yanamsifu rabi mmoja ambaye alijificha alipowaona wenye ukoma na rabi mwingine ambaye aliwatupia mawe ili wasimkaribie. Kwa upande mwingine, Yesu alisikitishwa sana na kuugua kwa mtu huyo mwenye ukoma hivi kwamba akafanya jambo ambalo Wayahudi wengine hawangeweza hata kuwazia kulifanya—alimgusa mwanamume huyo. Alifanya hivyo, hata ingawa angeweza kumponya mtu huyo mwenye ukoma kwa kusema neno moja tu.—Mt 8:5-12.
Ninataka: Yesu hakukubali tu ombi hilo bali alionyesha tamaa kubwa ya kutaka kumtimizia ombi lake, akionyesha kwamba hakufanya hivyo ili kutimiza wajibu tu.
nwtsty habari za utafiti—Mt 9:10
akila: Au “akiwa ameketi mezani.” Kuketi mezani, au kuegemea mezani, pamoja na mtu fulani kulionyesha urafiki wa karibu pamoja na mtu huyo. Hivyo, Wayahudi katika siku za Yesu, kwa kawaida hawangeweza kamwe kuketi mezani, au kula chakula pamoja na watu ambao si Wayahudi.
wakusanya kodi: Wayahudi wengi walikusanya kodi kwa niaba ya watawala Waroma. Watu waliwachukia Wayahudi hao kwa sababu mbali tu na kushirikiana na taifa la kigeni lililochukiwa, wakusanya kodi hao waliwadhulumu watu kwa kutoza pesa nyingi zaidi kuliko kiwango cha kodi kilichowekwa. Kwa ujumla, Wayahudi waliwaepuka wakusanya kodi, kwa sababu waliwaona kuwa sawa na watenda dhambi na makahaba.—Mt 11:19; 21:32.
nwtsty habari za utafiti—Mt 9:36
akausikitikia: Kitenzi cha Kigiriki splag·khniʹzo·mai kilichotumiwa hapa kinahusiana na neno “matumbo” (splagʹkhna), kinaashiria hisia za ndani kabisa, hisia yenye nguvu sana. Ni mojawapo ya maneno yenye nguvu zaidi katika Kigiriki linaloelezea hisia ya huruma.
JANUARI 29–FEBRUARI 4
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 10-11
“Yesu Aliwaburudisha Watu”
nwtsty habari za utafiti—Mt 10:29
shore: Neno la Kigiriki strou·thiʹon linaonyesha udogo na linamaanisha ndege mdogo wa aina yoyote, lakini mara nyingi lilitumiwa kuwarejelea shore, ndege wa bei ya chini zaidi ambaye aliuzwa kwa ajili ya chakula.
kwa sarafu ya thamani ndogo: Tnn., “kwa sarafu moja ya asarioni,” ambayo ilikuwa sawa na mshahara wa mtu ambaye alifanya kazi ya dakika 45. (Angalia Nyongeza B14.) Katika kisa hiki, wakati wa safari yake ya tatu kwenda Galilaya, Yesu alisema kwamba shore wawili waliuzwa kwa sarafu moja ya asarioni. Pindi nyingine, mwaka mmoja hivi baada ya wakati huo, Yesu alipokuwa katika huduma yake huko Yudea, alisema kwamba shore watano wangeweza kununuliwa kwa sarafu mbili. (Lu 12:6) Tunapolinganisha masimulizi hayo, tunajifunza kwamba shore walikuwa na thamani ndogo sana kwa wafanyabiashara hivi kwamba yule shore wa tano angeweza kutolewa bila malipo yoyote.
hata nywele zote za vichwa vyenu zimehesabiwa: Inasemekana kwamba kichwa cha mwanadamu kina wastani wa nywele zaidi ya 100,000. Kwa Yehova kujua kihususa hata mambo madogo kadiri hiyo kunatuhakikishia kwamba anamjali sana kila mfuasi wa Kristo.
nwtsty picha
Shore
Shore walikuwa ndege wa gharama ya chini zaidi waliouzwa kwa ajili ya chakula. Shore wawili wangeweza kununuliwa kwa mshahara ambao mtu alipata kwa kufanya kazi dakika 45. Neno la Kigiriki linaweza kumaanisha aina mbalimbali za ndege wadogo, kutia ndani shore wa kawaida wa nyumbani (Passer domesticus biblicus) na shore wa Hispania (Passer hispaniolensis), ambao bado wanapatikana kwa wingi nchini Israel.
nwtsty habari za utafiti—Mt 11:28
kulemewa na mizigo: Wale ambao Yesu aliwakaribisha wamfuate walikuwa ‘wakilemewa na mizigo’ ya mahangaiko na taabu. Ibada yao kwa Yehova ilikuja kuwa mzigo mzito kwa sababu ya desturi za wanadamu ambazo ziliongezwa katika Sheria ya Musa. (Mt 23:4) Hata Sabato, ambayo ilikusudiwa kuwaburudisha, ilikuja kuwa mzigo kwao.—Kut 23:12; Mk 2:23-28; Lu 6:1-11.
nami nitawaburudisha: Neno la Kigiriki “kuburudisha” linaweza kurejelea kupumzika (Mt 26:45; Mk 6:31) na pia kitulizo kutokana na kazi ngumu ili kurudia hali ya kawaida na kupata nguvu tena (2Ko 7:13; Flm 7). Muktadha unaonyesha kwamba kuchukua “nira” ya Yesu (Mt 11:29) kungehusisha utumishi na si kupumzika. Kitenzi cha kutenda kinachomwonyesha Yesu kuwa chanzo cha burudisho hilo kinaonyesha wazo la kuwarudishia na kuwapa tena nguvu watu waliochoka ili wapate tena tamaa ya kuchukua nira yake ambayo ni laini na nyepesi.
nwtsty habari za utafiti—Mt 11:29
Chukueni nira yangu: Yesu alitumia neno “nira” kwa njia ya mfano katika maana ya kujitiisha chini ya mamlaka na kufuata mwongozo. Ikiwa alikuwa akifikiria nira yenye sehemu mbili, ambayo sehemu moja Yesu alipewa na Mungu ili abebe, basi angeweza kuwaalika wanafunzi wake wabebe nira pamoja naye na angewasaidia. Katika kisa hicho maelezo hayo yanaweza kusemwa: “Tubebe nira yangu pamoja.” Ikiwa nira hiyo ilikuwa ile ambayo Yesu mwenyewe aliwapa wengine wachukue, basi inarejelea kujitiisha chini ya mamlaka ya Kristo na kufuata mwongozo wake tukiwa wanafunzi wake.