Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • mwbr18 Februari kur. 1-3
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2018
  • Vichwa vidogo
  • FEBRUARI 5-11
  • FEBRUARI 12-18
  • FEBRUARI 19-25
  • FEBRUARI 26–MACHI 4
Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2018
mwbr18 Februari kur. 1-3

Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha

FEBRUARI 5-11

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty Habari za Utafiti—Mt 12:20

utambi unaofifia: Taa ndogo iliyotumiwa nyumbani ilitengenezwa kwa udongo na kujazwa mafuta ya zeituni. Utambi wa kitani ulifyonza mafuta ili taa iendelee kuwaka. Msemo wa Kigiriki “utambi unaofifia” huenda ulirejelea utambi unaotoa moshi kwa sababu bado una moto lakini mwangaza wa taa unafifia au umezimwa. Unabii wa Isaya 42:3 ulitabiri kwamba Yesu angekuwa mwenye huruma; kamwe hangezima tumaini dogo la watu wa hali ya chini na waliokandamizwa.

FEBRUARI 12-18

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 14-15

nwtsty habari za utafiti—Mt 14:21

na pia wanawake na watoto wadogo: Ni Mathayo tu anayewataja wanawake na watoto anaporipoti muujiza huu. Inawezekana kwamba jumla ya watu waliolishwa kimuujiza ilikuwa zaidi ya 15,000.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Mt 15:7

wanafiki: Neno la Kigiriki hy·po·kri·tesʹ hapo awali lilirejelea waigizaji Wagiriki (na baadaye Waroma) ambao walifunika nyuso zao kwa kinyago ambacho kilisaidia kukuza sauti ya mwigizaji. Neno hilo lilikuja kutumiwa kwa njia ya mfano kuhusu mtu yeyote anayeficha nia yake au utu wake kwa kuigiza au kujifanya ana nia nzuri. Yesu hapa anawaita viongozi wa dini ya Kiyahudi “wanafiki.”—Mt 6:5, 16.

nwtsty habari za utafiti—Mt 15:26

watoto . . . mbwa wadogo: Kwa kuwa Sheria ya Musa ilisema kwamba mbwa walikuwa kati ya wanyama ambao si safi, mara nyingi Maandiko yanatumia neno hilo kuonyesha dharau. (Law 11:27; Mt 7:6; Flp 3:2; Ufu 22:15) Hata hivyo, katika masimulizi ya Marko (7:27) na Mathayo, Yesu anatumia neno linaloonyesha udogo, linalomaanisha “mbwa mdogo” au “mbwa wa nyumbani”, ili kupunguza makali ya ulinganifu aliotumia. Inawezekana Yesu alitumia neno lililorejelea wanyama vipenzi ambao walifugwa nyumbani kwa watu ambao hawakuwa Wayahudi. Kwa kuwalinganisha Waisraeli na “watoto” na watu wasio Wayahudi na “mbwa wadogo,” huenda Yesu alikuwa akionyesha wanaopaswa kutangulizwa. Katika nyumba iliyokuwa na watoto na pia mbwa, watoto wangelishwa kwanza.

FEBRUARI 19-25

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Mt 16:18

Wewe ni Petro, na juu ya mwamba huu: Neno la Kigiriki peʹtros ni jina la kiume linalomaanisha “kipande cha mwamba; jiwe.” Hapa linatumiwa kama jina rasmi (Petro), jina la Kigiriki ambalo Yesu alimpa Simoni. (Yoh 1:42) Jina la kike peʹtra linarejelea “mwamba,” na linaweza kumaanisha jabali, au mwamba. Neno hili la Kigiriki linapatikana pia katika Mt 7:24, 25; 27:60; Lu 6:48; 8:6; Ro 9:33; 1Ko 10:4; 1Pe 2:8. Ni wazi kwamba Petro mwenyewe hakujiona kuwa mwamba ambao Yesu angejenga kutaniko juu yake, kwa kuwa aliandika katika 1Pe 2:4-8 kwamba Yesu ndiye aliyetabiriwa zamani kuwa “jiwe la pembeni la msingi,” lililochaguliwa na Mungu mwenyewe. Vivyo hivyo, mtume Paulo alimrejelea Yesu kuwa “msingi” na “mwamba wa kiroho.” (1Ko 3:11; 10:4) Kwa hiyo, Yesu alikuwa akicheza na maneno, ni kana kwamba alikuwa akisema: ‘Wewe, ambaye ninakuita Petro, yaani, Kipande cha Mwamba, umefahamu utambulisho wa Kristo, “mwamba huu,” yule atakayekuwa msingi wa kutaniko la Kikristo.’

kutaniko: Hii ndiyo mara ya kwanza ambapo neno la Kigiriki ek·kle·siʹa linaonekana. Linatokana na maneno mawili ya Kigiriki, ek, linalomaanisha “nje,” na ka·leʹo, linalomaanisha “kuita.” Linarejelea kikundi cha watu kilichoitwa au kukusanywa pamoja kwa ajili ya kusudi maalumu au kazi fulani. (Angalia Kamusi.) Katika muktadha huu, Yesu alikuwa akitabiri kuanzishwa kwa kutaniko la Kikristo, lililofanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta, ambao wakiwa “mawe yaliyo hai [wanajengwa] kuwa nyumba ya kiroho.” (1Pe 2:4, 5) Neno hili la Kigiriki lilitumiwa mara nyingi katika Septuajinti kwa kuwa linalingana na neno la Kiebrania linalomaanisha “kutaniko,” ambalo mara nyingi linarejelea taifa lote la watu wa Mungu. (Kum 23:3; 31:30) Katika Mdo 7:38, Waisraeli ambao waliitwa kutoka Misri walirejelewa kuwa “kutaniko.” Vivyo hivyo, Wakristo ambao “[wanaitwa] kutoka katika giza” na ambao “[wamechaguliwa] kutoka ulimwenguni” wanafanyiza “kutaniko la Mungu.”—1Pe 2:9; Yoh 15:19; 1Ko 1:2.

nwtsty habari za utafiti—Mt 16:19

funguo za Ufalme wa mbinguni: Katika Biblia, watu ambao walipewa funguo iwe kihalisi au kwa njia ya mfano, walikuwa wamekabidhiwa mamlaka fulani. (1Nya 9:26, 27; Isa 22:20-22) Kwa hiyo neno “ufunguo” likaja kuwakilisha mamlaka na wajibu. Petro alitumia “funguo” hizo kuwafungulia Wayahudi (Mdo 2:22-41), Wasamaria (Mdo 8:14-17), na Watu wa Mataifa (Mdo 10:34-38) nafasi ya kupokea roho ya Mungu ili wawe na tumaini la kuingia katika Ufalme wa mbinguni.

FEBRUARI 26–MACHI 4

HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 18-19

nwtsty habari za utafiti—Mt 18:6, 7

jiwe la kusagia ambalo huzungushwa na punda: Au “jiwe kubwa la kusagia.” Tnn., “jiwe la kusagia la punda.” Jiwe kama hilo, ambalo huenda lilikuwa na kipenyo cha mita 1.2 hadi 1.5, lilikuwa zito sana hivi kwamba lilihitaji kuzungushwa na punda.

vikwazo: Maana ya awali ya neno la Kigiriki skanʹda·lon, lililotafsiriwa ‘kikwazo,’ huenda ilikuwa mtego; wengine wanadai kwamba ilirejelea kijiti katika mtego ambapo chambo kiliwekwa. Katika maana pana, neno hilo lilirejelea kizuizi ambacho kingeweza kumfanya mtu ajikwae au kuanguka. Kwa njia ya mfano, neno hilo linarejelea tendo au hali inayomwongoza mtu kufuata njia isiyofaa, kujikwaa au kuanguka kimaadili, au kuanguka katika dhambi. Katika Mt 18:8, 9, kitenzi kinachofanana na hicho, yaani, skan·da·liʹzo, kinachotafsiriwa ‘-fanya ukwazike,’ kinaweza pia kurejelea “kuwa mtego; sababisha ufanye dhambi.”

nwtsty picha

Jiwe la Kusagia

Jiwe la kusagia lilitumiwa kusaga nafaka na kukamua mafuta ya zeituni. Mawe fulani ya kusagia yalikuwa madogo na yangeweza kuzungushwa kwa mkono, lakini mengine yalikuwa makubwa na yangeweza kuzungushwa tu na mnyama. Inawezekana Samsoni alilazimishwa na Wafilisti kuzungusha jiwe kubwa kama hilo. (Amu 16:21) Mawe ya kusagia yaliyozungushwa na wanyama hayakuwa tu katika Israeli bali pia katika maeneo mengi ya Milki ya Roma.

Jiwe la Kusagia la Juu na la Chini

Jiwe kubwa la kusagia kama linaloonyeshwa hapa lilizungushwa na mnyama wa kufugwa kama vile punda, na lilitumiwa kusaga nafaka au kukamua zeituni. Jiwe la juu la kusagia lingeweza kuwa na kipenyo cha mita 1.5 na lilizungushwa juu ya jiwe la chini lililokuwa kubwa zaidi.

nwtsty habari za utafiti—Mt 18:9

Gehena: Neno hili linatokana na neno la Kiebrania geh hin·nomʹ, linalomaanisha “bonde la Hinomu,” ambalo lilikuwa upande wa Magharibi na Kusini mwa jiji la kale la Yerusalemu. (Ona Nyongeza B12, ramani “Yerusalemu na Maeneo Jirani.”) Kufikia siku za Yesu, bonde hilo lilikuwa mahali pa kuchomea takataka, kwa hiyo neno “Gehena” liliwakilisha kwa njia inayofaa uharibifu kamili.

nwtstg Kamusi

Gehena

Neno la Kigiriki linalorejelea Bonde la Hinomu, lililokuwa upande wa kusini magharibi wa jiji la kale la Yerusalemu. (Yer 7:31) Neno hilo lilitumiwa kinabii kurejelea mahali ambapo maiti zilitupwa. (Yer 7:32; 19:6) Hakuna uthibitisho kwamba wanyama au wanadamu walitupwa katika Gehena ili wateswe au kuchomwa moto wakiwa hai. Kwa hiyo mahali hapo hapangeweza kufananisha mahali pasipoonekana ambapo nafsi za wanadamu zinateswa milele katika moto halisi. Badala yake, Yesu na wanafunzi wake walitumia neno “Gehena” kufananisha adhabu ya milele ya “kifo cha pili,” yaani, maangamizi ya milele, uharibifu.—Ufu 20:14; Mt 5:22; 10:28.

nwtsty habari za utafiti—Mt 18:10

huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni: Au “wanaweza kuingia kwa Baba yangu.” Kwa kuwa wanaweza kuingia mbele ya kuwapo kwa Mungu, ni viumbe wa roho tu wanaoweza kuuona uso wa Mungu.—Kut 33:20.

Kutafuta Hazina za Kiroho

nwtsty habari za utafiti—Mt 18:22

mara 77: Tnn., “sabini mara saba.” Neno hili la Kigiriki linaweza kumaanisha ama “70 na 7” (mara 77) au “70 kuzidisha kwa 7” (mara 490). Katika Mwa 4:24 tafsiri ya Septuajinti inatumia neno hilohilo la Kiebrania “mara 77,” na hivyo kuunga mkono matumizi ya msemo “mara 77.” Licha ya jinsi neno hilo lilivyoeleweka, kurudiwa kwa namba saba kulikuwa sawa na “bila kikomo” au “bila mwisho.” Kwa kubadili mara 7 ambazo Petro alikuwa ametaja kuwa mara 77, Yesu alikuwa akiwajulisha wafuasi wake kwamba hawakupaswa kuweka kiwango cha kuwasamehe wengine. Tofauti na hilo, Talmudi ya Babiloni (Yoma 86b) inasema hivi: “Mtu akikosea mara ya kwanza, mara ya pili na ya tatu anasamehewa, lakini mara ya nne hapaswi kusamehewa.”

nwtsty habari za utafiti—Mt 19:7

cheti cha kumfukuza: Au “cheti cha talaka.” Kwa kutaka mtu ambaye anafikiria kutoa talaka atayarishe hati ya kisheria na ikiwezekana azungumze na wazee, Sheria ilimpa mtu huyo muda wa kufikiria upya uamuzi huo mzito. Kusudi la Sheria hiyo lilikuwa kuzuia talaka zilizotolewa ovyoovyo na kuwapa wanawake kiwango fulani cha ulinzi wa kisheria. (Kum 24:1) Lakini katika siku za Yesu, viongozi wa kidini walifanya iwe rahisi kutoa talaka. Mwanahistoria wa karne ya kwanza Yosefo, ambaye alikuwa Farisayo aliyemtaliki mke wake, alipendekeza kwamba talaka ingeweza kutolewa “kwa sababu yoyote ile (na wanaume wana sababu nyingi).”

nwtsty picha

Cheti cha Talaka

Cheti hiki cha talaka kinachosemekana kuwa cha mwaka wa 71 au 72 W.K., kiliandikwa kwa Kiaramu. Kilipatikana upande wa kaskazini wa Wadi Murabbaat, kwenye mto uliokauka katika Jangwa la Yudea. Cheti hicho kinasema kwamba katika mwaka wa sita wa uasi wa Wayahudi, Yosefu, mwana wa Naqsan, alimtaliki Miriamu, binti ya Yonathani ambaye alikuwa akiishi katika jiji la Masada.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki