Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
MACHI 5-11
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 20-21
“Yeyote Anayetaka Kuwa Mkubwa Kati Yenu Lazima Awe Mhudumu Wenu”
nwtsty picha
Sokoni
Masoko fulani, kama lililoonyeshwa hapa, yalikuwa kandokando ya barabara. Mara nyingi wachuuzi walipanga bidhaa nyingi sana barabarani hivi kwamba waliwazuia wapita-njia wasitembee kwa uhuru. Wenyeji wangenunua bidhaa za kawaida, vyombo vya udongo, vyombo vya glasi vya bei ghali, na pia mazao ya shambani. Kwa kuwa hakukuwa na friji, watu walihitaji kwenda sokoni kila siku. Mnunuzi angeweza kupata habari zilizoletwa na wachuuzi au wageni wengine, watoto walicheza, na watu wasio na kazi wangesubiri kuajiriwa. Huko sokoni, Yesu aliwaponya wagonjwa na mtume Paulo alihubiri. (Mdo 17:17) Kwa upande mwingine, waandishi na Mafarisayo wenye kiburi walipenda kutambuliwa na kusalimiwa katika maeneo hayo yenye watu wengi.
nwtsty habari za utafiti—Mt 20:20, 21
mama ya wana wa Zebedayo: Huyo ni mama ya mtume Yakobo na Yohana. Simulizi la Marko linasema kwamba Yakobo na Yohana ndio waliomfikia Yesu. Inaonekana wao ndio chanzo cha ombi hilo, lakini walifanya hivyo kupitia mama yao, Salome, ambaye inaelekea alikuwa shangazi ya Yesu.—Mt 27:55, 56; Mk 15:40, 41; Yoh 19:25.
mmoja upande wako wa kuume na mwingine upande wako wa kushoto: Pande zote mbili zinawakilisha heshima na mamlaka, lakini sikuzote upande wenye heshima zaidi ni upande wa kulia.—Zb 110:1; Mdo 7:55, 56; Ro 8:34.
nwtsty habari za utafiti—Mt 20:26, 28
mhudumu: Au “mtumishi.” Mara nyingi, Biblia inatumia neno la Kigiriki di·aʹko·nos kurejelea mtu ambaye haachi kuwahudumia wengine kwa unyenyekevu. Neno hilo linatumiwa kumfafanua Kristo (Ro 15:8), wahudumu au watumishi wa Kristo (1Ko 3:5-7; Kol 1:23), watumishi wa huduma (Flp 1:1; 1Ti 3:8), na vilevile watumishi wa nyumbani (Yoh 2:5, 9) na maofisa wa serikali (Ro 13:4).
si kuhudumiwa, bali kuhudumu: Au “si kutumikiwa, bali kutumikia.”
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mt 21:9
Tunaomba umwokoe: Tnn., “Hosanna.” Neno hilo la Kigiriki linatokana na maneno ya Kiebrania yanayomaanisha “tunaomba, umwokoe” au “mwokoe, tafadhali.” Hapa maneno hayo ni ombi linalotolewa kwa Mungu kwa ajili ya wokovu au ushindi; linaweza kutafsiriwa, “tafadhali mpe wokovu.” Baadaye, ombi hilo likaja kutumika katika sala na nyimbo. Maneno hayo ya Kiebrania yanapatikana katika Zb 118:25, ambayo ilikuwa sehemu ya Zaburi za Haleli zilizoimbwa wakati wa Pasaka. Kwa hiyo, ilikuwa rahisi kukumbuka maneno hayo katika pindi hii. Njia moja ambayo Mungu alijibu sala ya kumwokoa Mwana wa Daudi ilikuwa kwa kumfufua kutoka kwa wafu. Katika andiko la Mt 21:42, Yesu mwenyewe ananukuu Zb 118:22, 23 na kutumia maneno hayo kumhusu Masihi.
Mwana wa Daudi: Maneno yanayoonyesha kutambua nasaba ya Yesu na fungu lake akiwa Masihi aliyeahidiwa.
MACHI 12-18
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 22-23
“Tii Zile Amri Mbili Kuu Zaidi”
nwtsty habari za utafiti—Mt 22:37
moyo: Unapotumiwa kwa njia ya mfano, neno hilo linarejelea yule mtu wa ndani. Hata hivyo, linapotajwa pamoja na “nafsi” au “akili,” linachukua maana hususa zaidi kumaanisha hasa hisia na tamaa za mtu. Maneno hayo matatu (moyo, nafsi, na akili) hayatofautiani kabisa katika maana; yanatumiwa kwa kupishana ili kukazia kwa nguvu kadiri iwezekanavyo uhitaji wa kuwa na upendo kamili kwa Mungu.
nafsi: Au “mtu mwenyewe.”
akili: Yaani, uwezo wa kufikiri. Mtu anapaswa kutumia uwezo wake wa kufikiri ili kumjua Mungu na kukua katika upendo wake kwa Yehova. (Yoh 17:3, maelezo ya chini; Ro 12:1) Katika nukuu hilo la Kum 6:5, maandishi ya awali ya Kiebrania yalitumia maneno matatu, yaani, ‘moyo, nafsi, na nguvu.’ Hata hivyo, katika simulizi la Kigiriki la Injili ya Mathayo, neno “akili” limetumiwa badala ya “nguvu.” Huenda mambo kadhaa yalichangia kutumiwa kwa neno hilo tofauti. Kwanza, ingawa Kiebrania cha awali hakikuwa na neno hususa kwa ajili ya “akili,” mara nyingi neno la Kiebrania “moyo” lilitumiwa kutokeza wazo hilo. Neno hilo linapotumiwa kwa njia ya mfano linarejelea yule mtu wa ndani, kutia ndani fikira, hisia, mitazamo, na mambo yanayomchochea mtu. (Kum 29:4; Zb 26:2; 64:6; soma habari za utafiti—moyo katika mstari huu.) Kwa sababu hiyo, mahali ambapo Kiebrania kinatumia neno “moyo,” mara nyingi Septuajinti ya Kigiriki inatumia neno la Kigiriki “akili.” (Mwa 8:21; 17:17; Met 2:10; Isa 14:13) Sababu nyingine ambayo huenda ilimfanya Mathayo atumie neno la Kigiriki “akili” badala ya “nguvu” aliponukuu Kum 6:5 ni kwamba neno la Kiebrania lililotafsiriwa “nguvu [au, “uwezo,” maelezo ya chini]” linaweza kutia ndani nguvu za kimwili na uwezo wa kiakili. Vyovyote vile, mawazo hayo yanayopishana kati ya maneno ya Kiebrania na ya Kigiriki yanaweza kutusaidia kuelewa kwa nini waandikaji wa Injili hawatumii maneno yaleyale wanaponukuu Kumbukumbu la Torati.
nwtsty habari za utafiti—Mt 22:39
Ya pili: Jibu la moja kwa moja ambalo Yesu alimpa Farisayo liliandikwa kwenye Mt 22:37, lakini sasa Yesu hajibu tu swali la kwanza bali anataja amri ya pili (Law 19:18), na kufundisha kwamba amri hizo mbili zinategemezana na kwamba Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.—Mt 22:40.
jirani: Neno la Kigiriki “jirani” (tnn., “aliye karibu”) linaweza kuhusisha watu wengi zaidi ya wale wanaoishi karibu. Linaweza kuhusisha mtu yeyote ambaye unachangamana naye.—Lu 10:29-37; Ro 13:8-10.
nwtsty habari za utafiti—Mt 22:40
Sheria . . . Manabii: Neno “sheria” linarejelea vitabu vya Biblia vya Mwanzo hadi Kumbukumbu la Torati. “Manabii” ni neno linalorejelea vitabu vya kinabii katika Maandiko ya Kiebrania. Hata hivyo, maneno hayo yanapotajwa pamoja yanaweza kumaanisha Maandiko yote ya Kiebrania.—Mt 7:12; 22:40; Lu 16:16.
hutegemea: Kitenzi cha Kigiriki kinachomaanisha kihalisi “kuning’inia” kimetumiwa hapa kwa njia ya mfano kumaanisha “kutegemea kitu kingine; kutegemezwa na.” Kwa hiyo, Yesu anaonyesha si Sheria tu yenye Amri Kumi inayotegemea upendo bali ni Maandiko yote ya Kiebrania.—Ro 13:9.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mt 22:21
Kaisari vitu vya Kaisari: Jibu la Yesu hapa, na pia katika masimulizi yanayolingana ya Mk 12:17 na Lu 20:25, ndiyo mistari pekee ambapo Yesu alimtaja maliki wa Roma. “Vitu vya Kaisari” vinatia ndani malipo kwa ajili ya huduma za serikali na vilevile heshima na ujitiisho unaopaswa kuonyeshwa kwa mamlaka hizo.—Ro 13:1-7.
Mungu vitu vya Mungu: Hivi vinatia ndani kumwabudu kwa moyo wote, kumpenda kwa nafsi yote, na kumtii kikamili na kwa ushikamanifu.—Mt 4:10; 22:37, 38; Mdo 5:29; Ro 14:8.
nwtsty habari za utafiti—Mt 23:24
ambao huchuja mbu lakini hummeza ngamia: Mbu ni mmoja kati ya wanyama wadogo zaidi wasio safi ambao Waisraeli waliwafahamu. Ngamia ni kati ya wale wakubwa zaidi. (Law 11:4, 21-24) Yesu alitia chumvi na pia alitumia tamathali ya usemi aliposema kwamba viongozi wa kidini walichuja vinywaji vyao ili wasitiwe unajisi na mbu, lakini wakati huohuo walipuuza kabisa mambo mazito zaidi ya Sheria, kitendo ambacho kililingana na kummeza ngamia.
MACHI 19-25
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | MATHAYO 24
“Endelea Kuwa Macho Kiroho Katika Siku za Mwisho”
it-2 279 ¶6
Upendo
Upendo wa Mtu Unaweza Kupoa. Yesu Kristo alipowaambia wafuasi wake kuhusu mambo ya wakati ujao, alisema kwamba upendo (a·gaʹpe) wa wengi wanaodai kumwamini Mungu ungepoa. (Mt 24:3, 12) Mtume Paulo alisema kwamba sehemu moja ya ishara ya nyakati za hatari ni kwamba watu wangekuwa “wenye kupenda pesa.” (2Ti 3:1, 2) Hivyo, ni wazi kwamba mtu anaweza kuacha kukazia fikira kanuni zinazofaa na aanze kupenda mambo yasiyofaa. Hilo linaonyesha wazi umuhimu wa kuonyesha na kuboresha upendo wetu kwa kutafakari Neno la Mungu na kuishi kulingana na kanuni Zake.—Efe 4:15, 22-24.
Kutafuta Hazina za Kiroho
nwtsty habari za utafiti—Mt 24:8
maumivu ya taabu: Maneno hayo ya Kigiriki kihalisi yanarejelea maumivu makali ambayo mtu hupata wakati wa kuzaa. Ingawa hapa yametumiwa kurejelea mahangaiko, uchungu, na kuteseka kwa ujumla, huenda yakawa yanadokeza kwamba katika kipindi kinachotangulia dhiki kuu inayotajwa katika Mt 24:21, matatizo na mateso yataongezeka, yatakuwa makali zaidi, na yatakuwa ya muda mrefu zaidi kama tu maumivu ya kuzaa.
nwtsty habari za utafiti—Mt 24:20
wakati wa majira ya baridi kali: Kuwepo kwa mvua kubwa, mafuriko, na baridi wakati wa majira hayo kungefanya iwe vigumu kupata chakula na makao.—Ezr 10:9, 13.
siku ya Sabato: Katika maeneo kama Yudea, vizuizi vilivyohusiana na sheria ya Sabato vingefanya iwe vigumu kwa mtu kusafiri kwenda mbali au kubeba mizigo; pia, malango ya jiji yalifungwa siku ya Sabato.—Soma Mdo 1:12 na Nyongeza B12.