Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
MACHI 1-7
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | HESABU 7-8
“Masomo Tunayojifunza Kutokana na Kambi ya Israeli”
it-1 497 ¶3
Kutaniko
Katika taifa la Israeli, wawakilishi waliopewa madaraka walitenda kwa niaba ya watu. (Ezr 10:14) Hivyo, ‘wakuu wa makabila’ walitoa matoleo baada ya hema la ibada kusimamishwa. (Hes 7:1-11) Pia, makuhani, Walawi, na “viongozi wa watu” walitia muhuri “mapatano thabiti” yaliyofanywa katika siku za Nehemia. (Ne 9:38–10:27) Wakati wa safari ya Waisraeli nyikani, wanaume 250 waliokuwa “wakuu wa kusanyiko, wanaume maarufu waliowekwa rasmi,” waliungana na Kora, Dathani, Abiramu, na Oni kumpinga Musa na Haruni. (Hes 16:1-3) Kupatana na mwongozo kutoka kwa Mungu, Musa aliwachagua wanaume 70 miongoni mwa wazee wa Israeli ambao walikuwa maofisa ili wamsaidie “kubeba mzigo wa watu” ambao hangeweza kuubeba peke yake. (Hes 11:16, 17, 24, 25) Mambo ya Walawi 4:15 inasema kuhusu “wazee wa kusanyiko,” na inaonekana kwamba wawakilishi wa watu walikuwa wazee wa taifa, viongozi wao, waamuzi wao, na wakuu wao.—Hes 1:4, 16; Yos 23:2; 24:1.
it-2 796 ¶1
Rubeni
Katika kambi ya Israeli, Warubeni, waliokuwa pamoja na watu wa kabila la Simeoni na Gadi, walikuwa upande wa Kusini wa hema la ibada. Taifa hilo liliposafiri, kundi la makabila matatu lililoongozwa na Warubeni lilifuata kundi la makabila matatu ya Yuda, Isakari, na Zabuloni. (Hes 2:10-16; 10:14-20) Makabila yalitoa matoleo yao kwa mpangilio huo siku ambayo hema la ibada lilizinduliwa.—Hes 7:1, 2, 10-47.
Hazina za Kiroho
it-1 835
Mzaliwa wa Kwanza
Kwa kuwa wana wazaliwa wa kwanza miongoni mwa Waisraeli ndio ambao wangekuja kuwa vichwa katika nyumba zao, waliwakilisha taifa lote. Yehova alilirejelea taifa lote kuwa “mzaliwa wangu wa kwanza.” Lilikuwa mzaliwa wa kwanza kwa msingi wa agano la Abrahamu. (Kut 4:22) Kwa sababu Yehova aliokoa uhai wao, aliamuru kwamba ‘kila mzaliwa wa kwanza wa kiume wa Waisraeli, mzaliwa wa kwanza wa kiume wa mwanadamu na mnyama,’ atakaswe kwa ajili yake. (Kut 13:2) Hivyo, wana wazaliwa wa kwanza walitolewa kwa Mungu.
MACHI 8-14
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | HESABU 9-10
“Jinsi Yehova Anavyowaongoza Watu Wake”
it-1 398 ¶3
Kambi
Kuhamisha kambi hiyo kubwa kutoka eneo moja hadi lingine kulikuwa wonyesho mkubwa zaidi wa utaratibu (Musa anataja maeneo 40 hivi waliyohamia kwenye Hesabu 33). Maadamu wingu lilikaa juu ya hema la ibada, kambi haikuhamishwa. Wingu liliposonga, kambi ilihamishwa. “Walipiga kambi kwa agizo la Yehova, na kwa agizo la Yehova waliondoka.” (Hes 9:15-23) Tarumbeta mbili za fedha ziliwatangazia wote waliopiga kambi maagizo hayo ya Yehova. (Hes 10:2, 5, 6) Milio ya pekee iliyobadilika-badilika ilikuwa ishara ya kuvunja kambi. Hilo lilitokea kwa mara ya kwanza “katika mwaka wa pili [1512 K.W.K.], mwezi wa pili, siku ya 20.” Sanduku la agano lilitangulia, likifuatwa na kundi la makabila matatu la kambi ya Yuda, Isakari, na Zabuloni kwa mfuatano huo. Kisha walifuatwa na Wagershoni na Wamerari waliobeba sehemu walizogawiwa za hema la ibada. Kisha wakafuatiwa na kundi la makabila matatu lililoongozwa na Rubeni, kisha Simeoni, halafu Gadi. Baada yao, Wakohathi walifuata waliobeba madhabahu, wakifuatiwa na kundi la makabila matatu la Efraimu, Manase, na Benjamini. Mwisho kabisa kulikuwa na kikosi cha nyuma cha kulinda kambi zote kilichoongozwa na kabila la Dani, pamoja na Asheri na Naftali. Hivyo, makundi mawili yaliyokuwa na watu wengi zaidi na yaliyokuwa yenye nguvu zaidi yalifanyiza kikosi cha mbele na cha nyuma.—Hes 10:11-28.
Hazina za Kiroho
it-1 199 ¶3
Kusanyiko
Umuhimu wa Kukusanyika. Umuhimu wa kukusanyika ili kunufaika kikamili kiroho kutokana na maandalizi ya Yehova unakaziwa kupitia Pasaka ya kila mwaka. Mwanamume yeyote aliyekuwa safi na ambaye hakuwa amesafiri, lakini akapuuza kusherehekea Pasaka alipaswa kuuawa. (Hes 9:9-14) Mfalme Hezekia alipowaita wakaaji wa Yuda na Israeli kwenda Yerusalemu kwa ajili ya kusherehekea Pasaka, ujumbe wake ulisema hivi kwa sehemu: “Watu wa Israeli, rudini kwa Yehova . . . Sasa msiwe wakaidi kama mababu zenu. Jinyenyekezeni kwa Yehova, nanyi mje mahali pake patakatifu ambapo amepatakasa milele, mumtumikie Yehova Mungu wenu, ili hasira yake inayowaka iwaondokee. . . . Yehova Mungu wenu ni mwenye huruma na rehema, naye hataugeuza uso wake mbali nanyi mkirudi kwake.” (2Nya 30:6-9) Kukataa kuhudhuria kungeonyesha mtu anamwasi Mungu. Ingawa Wakristo hawasherehekei sherehe kama vile Pasaka, kwa kufaa Paulo aliwasihi wasiache kukusanyika kwa ukawaida pamoja na watu wa Mungu, akisema hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukutana pamoja, kama wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile ikikaribia.”—Ebr 10:24, 25; ona KUTANIKO.
MACHI 15-21
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | HESABU 11-12
“Kwa Nini Uepuke Roho ya Kulalamika?”
it-2 719 ¶4
Ubishi
Kunung’unika. Kunung’unika huvunja moyo na hubomoa. Muda mfupi baada ya Waisraeli kutoka Misri, walinung’unika dhidi ya Yehova kwa kukosoa uongozi wa watumishi wake, Musa na Haruni. (Kut 16:2, 7) Baadaye, manung’uniko yao yalimvunja moyo sana Musa hivi kwamba akaomba kufa. (Hes 11:13-15) Kunung’unika kunaweza kuwa hatari sana kwa mnung’unikaji. Kwa maoni ya Yehova, mambo ambayo wanung’unikaji walisema dhidi ya Musa yalikuwa malalamiko ya kuasi uongozi wa Mungu mwenyewe. (Hes 14:26-30) Wengi walipoteza uhai wao kwa sababu ya kutafuta makosa.
Hazina za Kiroho
it-2 309
Mana
Ufafanuzi. Mana ilikuwa ‘nyeupe kama mbegu za mgiligilani’ na “ilionekana kama” utomvu wa mbedola, kitu kinachopenyeza mwanga kilicho kama nta kinachofanana na lulu. Ladha yake ilikuwa “kama ya keki bapa zenye asali” au “keki tamu iliyookwa kwa mafuta.” Baada ya kusagwa kwa jiwe la kusagia au kutwangwa kwenye kinu, mana ilichemshwa au ilitumiwa kuoka keki.—Kut 16:23, 31; Hes 11:7, 8.
MACHI 22-28
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | HESABU 13-14
Hazina za Kiroho
it-1 740
Nchi Ambayo Mungu Aliwapa Waisraeli
Kwa kweli, nchi ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilikuwa nchi nzuri sana. Musa alipowatuma wapelelezi wakachunguze Nchi ya Ahadi na wachukue baadhi ya mazao yake, walirudi wakiwa na tini, makomamanga, na tawi lenye kishada kimoja cha zabibu kilichokuwa kikubwa sana hivi kwamba wanaume wawili walihitajika kulibeba kwenye ufito! Licha ya kwamba waliogopa kwa sababu ya kukosa imani, walisema hivi waziwazi: Nchi hiyo “kwa kweli inatiririka maziwa na asali.”—Hes 13:23, 27.
APRILI 19-25
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | HESABU 22-24
“Yehova Anabadili Laana Kuwa Baraka”
it-2 291
Wazimu
Wazimu wa Kumpinga Yehova. Kwa upumbavu nabii Balaamu alitaka kutoa unabii dhidi taifa la Israeli ili apate pesa kutoka kwa Mfalme Balaki wa Moabu, lakini Yehova akapindua maneno yake na kuzuia jitihada zake. Mtume Petro aliandika kumhusu Balaamu ambaye “mnyama wa kubeba mizigo asiye na sauti alizungumza kwa sauti ya mwanadamu na kuzuia mwendo wa kiwazimu wa nabii huyo.” Mtume Petro alitumia neno la Kigiriki pa·ra·phro·niʹa kurejelea wazimu wa Balaamu. Neno hilo linatokeza wazo la “kurukwa na akili.”—2Pe 2:15, 16; Hes 22:26-31.
APRILI 26–MEI 2
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | HESABU 25-26
Hazina za Kiroho
it-1 359 ¶1-2
Mpaka
Hivyo, inaonekana kwamba mgawanyo wa ardhi kati ya makabila ulitegemea mambo mawili: matokeo baada ya kupiga kura, na ukubwa wa kabila. Huenda kura ilionyesha mahali ambapo kila kabila lingepewa urithi wa ardhi, na hivyo kuonyesha upande ambao urithi wao ungekuwa katika nchi, kwa mfano, Kaskazini, Kusini, Mashariki, Magharibi, kando ya bahari, au eneo la milimani. Uamuzi wa kura ulitoka kwa Yehova na hilo lingezuia makabila yasioneane wivu au kubishana. (Met 16:33) Kwa njia hiyo pia, Mungu angeongoza mambo ili hali za kila kabila zipatane na unabii unaopatikana kwenye Mwanzo 49:1-33 ambao mzee wa ukoo Yakobo alitoa alipokuwa akikaribia kufa.
Baada ya kupiga kura kufahamu eneo la kijiografia la kila kabila, kungekuwa na uhitaji wa kutambua ukubwa wa eneo lake kwa msingi wa sababu ya pili: idadi ya watu katika kabila hilo. “Mtaigawanya nchi hiyo kwa kura na kuimiliki kulingana na familia zenu. Kundi kubwa litapokea urithi mkubwa zaidi na kikundi kidogo kitapokea urithi mdogo. Kila mtu atapokea urithi wake mahali ambapo kura yake itaangukia.” (Hes 33:54) Uamuzi wa kura kuhusu upande wa kijiografia haungebadilika, hata hivyo, badiliko lingeweza kufanywa kuhusiana na ukubwa wa urithi. Kwa hiyo, eneo la Yuda lilipoonekana kuwa kubwa sana, lilipunguzwa kwa kuwagawia watu wa kabila la Simeoni maeneo ndani ya ardhi hiyo.—Yos 19:9.