Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
MACHI 14-20
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | 1 SAMWELI 14-15
“Kutii Ni Bora Kuliko Dhabihu”
it-2 521 ¶2
Utii
Hakuna kitu kinachoweza kubadilishwa na utii, huwezi kupata kibali cha Mungu bila kutii. Samweli alimwambia hivi Mfalme Sauli: “Je, Yehova hupendezwa zaidi na dhabihu za kuteketezwa na dhabihu nyinginezo kuliko kuitii [aina ya sha·maʽʹ] sauti ya Yehova? Tazama! Kutii [kihalisi, kusikiliza] ni bora kuliko dhabihu, na kusikiliza kuliko mafuta ya kondoo dume.” (1Sa 15:22) Kukosa kutii ni kukataa neno la Yehova, ni kuonyesha kwamba mtu haamini, hatumaini, wala hana imani katika neno hilo na Chanzo chake. Hivyo yule anayekosa kutii hana tofauti na mtu anayefanya uaguzi au kuabudu sanamu. (1Sa 15:23; linganisha Ro 6:16.) Maneno ya kukubali jambo hayana maana yoyote ikiwa mtu hatatenda kwa njia inayohitajika; kukosa kutenda kunathibitisha mtu hana imani au heshima kuelekea chanzo cha maagizo aliyopewa. (Mt 21:28-32) Wale wanaotosheka kwa kusikia tu na kukubali katika akili zao kweli ya Mungu, lakini hawatendi kulingana na kweli hiyo, wanajidanganya kwa mawazo ya uwongo na hawapati baraka yoyote. (Yak 1:22-25) Mwana wa Mungu alionyesha wazi kwamba hata wale wanaofanya mambo yanayofanana na yale yaliyoamriwa, lakini wanafanya hivyo kwa njia isiyofaa au kwa nia mbaya, hawawezi kamwe kuingia katika Ufalme bali watakataliwa kabisa.—Mt 7:15-23.
Hazina za Kiroho
it-1 493
Huruma
Kukubali kushinikizwa kuonyesha huruma kinyume na mapenzi ya Mungu, kunaweza kuwa na madhara makubwa. Tunaweza kuona hilo kutokana na kilichompata Mfalme Sauli. Wakati ulikuwa umefika wa kutekeleza hukumu ya Mungu dhidi ya Waamaleki, ambao walikuwa watu wa kwanza kuwashambulia Waisraeli bila sababu walipokuwa wakitoka Misri. Sauli aliamriwa asiwahurumie. Lakini kwa sababu ya kushinikizwa na raia wake, hakutekeleza kikamili amri ya Yehova. Kwa hiyo, Yehova alimkataa Sauli asiwe mfalme. (1Sa 15:2-24) Kusitawisha uthamini wenye kina kwamba njia za Yehova ni sahihi na kuendelea kutanguliza ushikamanifu kwake, kunaweza kumzuia mtu asifanye makosa kama ya Sauli, na hivyo kupoteza kibali cha Mungu.
MACHI 21-27
Hazina za Kiroho
it-2 871-872
Sauli
Ilikuwa baada ya hapo na baada ya Daudi kutiwa mafuta akiwa mfalme wa wakati ujao wa Israeli ambapo roho ya Yehova ilimwacha Sauli. Kuanzia wakati huo na kuendelea “roho mbaya kutoka kwa Yehova ilikuwa ikimtesa.” Kwa kuwa alimwondolea Sauli roho yake, Yehova aliiruhusu roho mbaya imwingie, na hivyo kumnyima Sauli amani ya akili na kuchochea hisia, fikira, na mawazo mabaya ndani yake. Sauli alipokosa kumtii Yehova, alionyesha kwamba ana mwelekeo mbaya wa akili na moyo, na roho ya Mungu haingeweza kumlinda Sauli dhidi ya mwelekeo huo. Hata hivyo, kwa kuwa Yehova alikuwa ameruhusu “roho mbaya” ichukue mahali pa roho yake na imsumbue Sauli, ingeweza kusemwa ni “roho mbaya kutoka kwa Yehova,” hivi kwamba watumishi wa Sauli waliiita “roho mbaya kutoka kwa Mungu.” Kwa kufuata pendekezo la mmoja wa watumishi wake, Sauli alimwomba Daudi awe mwanamuziki wa makao ya mfalme ili amtulize anaposumbuliwa na “roho mbaya.”—1Sa 16:14-23; 17:15.
MACHI 28–APRILI 3
Hazina za Kiroho
it-2 695-696
Nabii
Ingawa waliwekwa rasmi ya roho ya Yehova, haielekei kwamba manabii walizungumza kila wakati wakiongozwa na roho ya Mungu. Badala yake, roho ya Mungu ‘ilikuja juu yao’ pindi fulani, na kuwafunulia ujumbe uliopaswa kutangazwa. (Eze 11:4, 5; Mik 3:8) Hilo lilikuwa na nguvu juu yao iliyowachochea kuzungumza. (1Sa 10:10; Yer 20:9; Amo 3:8) Si kwamba walifanya mambo ambayo hayakuwa ya kawaida tu, bali pia mwonekano na matendo yao yalionyesha bidii na hisia ambazo hazikuwa za kawaida. Hilo linaweza kueleza kinachomaanishwa na maneno watu fulani ‘kutenda kama manabii.’ (1Sa 10:6-11; 19:20-24; Yer 29:24-32; linganisha Mdo 2:4, 12-17; 6:15; 7:55) Umakini wao na bidii yao yenye ujasiri katika kutekeleza utume wao ungewafanya wengine wauone mwenendo wao kuwa wa ajabu au hata usiopatana na akili, kama vile nabii alivyoonwa na wakuu wa majeshi wakati ambapo Yehu alitiwa mafuta. Hata hivyo, wakuu hao walipotambua mwanamume huyo alikuwa nabii, walikubali ujumbe wake kwa uzito. (2Fa 9:1-13; linganisha Mdo 26:24, 25) Pindi ambayo Sauli alikuwa akimkimbiza Daudi, Sauli alipofanywa ‘kutenda kama nabii,’ alivua nguo zake na kulala “mchana wote na usiku huo wote akiwa uchi,” naye Daudi akaweza kukimbia. (1Sa 19:18–20:1) Hilo halimaanishi kwamba mara nyingi manabii walikaa uchi. Biblia inaonyesha jambo tofauti. Katika visa viwili vingine ambavyo manabii walikaa uchi, kulikuwa na kusudi. Walifanya hivyo ili kuonyesha jambo fulani lililohusiana na unabii wao. (Isa 20:2-4; Mik 1:8-11) Sababu ya Sauli kuwa uchi haielezwi. Huenda hilo lilikuwa ni kuonyesha alikuwa mwanadamu wa kawaida tu, au kuonyesha kwamba ananyang’anywa mavazi yake ya kifalme, au kuonyesha kuwa hana nguvu dhidi ya mamlaka na nguvu za Yehova, au kuonyesha jambo lingine.