Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
© 2022 Christian Congregation of Jehovah’s Witnesses
JANUARI 16-22
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | 1 MAMBO YA NYAKATI 1-3
Hazina za Kiroho
it-1 911 ¶3-4
Majina ya Ukoo
Majina ya Wanawake. Wanawake walitajwa katika orodha ya majina ya ukoo hasa kulipokuwa na sababu ya kihistoria ya kufanya hivyo. Kwenye Mwanzo 11:29, 30, Sarai (Sara) ametajwa kwa sababu Mbegu iliyoahidiwa ingetokea kupitia yeye na si kupitia mke mwingine wa Abrahamu. Huenda Milka anatajwa kwenye mistari hiyo pia kwa sababu alikuwa nyanya ya Rebeka, mke wa Isaka, na hilo lilithibitisha kwamba Rebeka alikuwa wa ukoo wa Abrahamu kwa sababu Isaka hakupaswa kutafuta mke kutoka kwa watu wa mataifa mengine. (Mwa 22:20-23; 24:2-4) Kwenye Mwanzo 25:1, Ketura, jina la mke wa pili wa Abrahamu linatajwa. Hilo linaonyesha kwamba baada ya Sara kufa, Abrahamu alioa tena na kwamba nguvu zake za uzazi ziliendelea kuwa hai miaka 40 baada ya nguvu hizo kurudishwa kimuujiza na Yehova. (Ro 4:19; Mwa 24:67; 25:20) Hilo pia linatuonyesha uhusiano uliopo kati ya Israeli na mataifa mengine ya Kiarabu, kutia ndani Midiani.
Lea, Raheli, na masuria wa Yakobo pamoja na watoto wao wametajwa. (Mwa 35:21-26) Hilo linatusaidia kuelewa jinsi Mungu alivyoshughulika na wana hao baadaye. Kwa sababu kama hizo, majina ya wanawake wengine yanatajwa pia kwenye orodha za majina ya ukoo. Urithi ulipopitishwa kupitia wanawake, majina yao yaliwekwa kwenye orodha ya majina ya ukoo. (Hes 26:33) Bila shaka, Tamari, Rahabu, na Ruthu walikuwa wanawake wa pekee. Katika kila kisa, wanawake hao walifanya mambo yenye kutokeza na hivyo wakaja kuwa katika ukoo wa Masihi, Yesu Kristo. (Mwa 38; Ru 1:3-5; 4:13-15; Mt 1:1-5) Majina ya wanawake wengine waliotajwa kwenye orodha za majina ya ukoo yanapatikana kwenye 1 Mambo ya Nyakati 2:35, 48, 49; 3:1-3, 5.
FEBRUARI 6-12
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | 1 MAMBO YA NYAKATI 10-12
Hazina za Kiroho
it-1 1058 ¶5-6
Moyo
Kutumikia kwa “Moyo Kamili.” Moyo halisi hauwezi kufanya kazi ikiwa umegawanyika lakini moyo wa mfano unaweza kuwa umegawanyika. Daudi alisali hivi: “Unganisha moyo wangu ili niliogope jina lako,” kuonyesha kwamba moyo wa mtu unaweza kuwa umegawanyika inapohusu mambo anayopenda na mambo anayoogopa. (Zb 86:11) Mtu kama huyo anaweza kuwa na moyo “nusunusu”—anamwabudu Mungu akiwa vuguvugu. (Zb 119:113; Ufu 3:16) Mtu pia anaweza kuwa na “mioyo miwili” (tafsiri ya moja kwa moja ni kuwa na moyo na moyo), kwa kujaribu kuwatumikia mabwana wawili, au kwa kuzungumza kwa udanganyifu huku akitaka kuonekana kana kwamba anasema ukweli. (1Nya 12:33; Zb 12:2, maelezo ya chini) Yesu alipinga sana unafiki huo.—Mt 15:7, 8.
Mtu anayetaka kumpendeza Mungu hapaswi kuwa na moyo nusunusu au mioyo miwili lakini anapaswa kumtumikia kwa moyo kamili. (1Nya 28:9) Hilo linahitaji jitihada nyingi kwa sababu moyo wa mwanadamu ni hatari na una mwelekeo mbaya. (Yer 17:9, 10; Mwa 8:21) Mambo yanayoweza kutusaidia kudumisha moyo kamili ni: sala za kutoka moyoni (Zb 119:145; Omb 3:41), kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida (Ezr 7:10; Met 15:28), kushiriki kwa bidii kazi ya kuhubiri habari njema (linganisha Yer 20:9), na kushirikiana na wengine ambao wana moyo kamili kumwelekea Yehova.—Linganisha 2Fa 10:15, 16.