Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
© 2023 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
NOVEMBA 6-12
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 13-14
“Mtu Akifa, Je, Anaweza Kuishi Tena?”
Jitihada Yetu ya Kuishi Muda Mrefu Zaidi
HATA leo ni wachache wawezao kupinga maneno hayo kuhusu ufupi wa maisha, ingawa yaliandikwa miaka ipatayo 3,500 iliyopita. Sikuzote watu hawaridhiki kufurahia upeo wa maisha kwa muda mfupi tu, kisha kuzeeka na kufa. Hivyo, njia za kurefusha maisha zimeongezeka katika historia yote.
Wakati wa Yobu Wamisri walikula mapumbu ya wanyama katika jitihada ambazo hazikufua dafu za kurudia ujana wao. Lengo moja kuu la tiba ya kurefusha maisha ya enzi za kati lilikuwa kutokeza dawa ambayo ingeweza kurefusha maisha. Waliofuatia tiba ya kurefusha maisha waliamini kwamba dhahabu iliyotokezwa na wanadamu ingesababisha uhai usioweza kufa na kwamba kulia sahani za dhahabu kungerefusha maisha. Wachina wa kale waliofuata dini ya Tao walifikiri kwamba wangeweza kugeuza maumbile ya mwili kwa kutumia mbinu kama kutafakari, mazoezi ya kupumua, na utaratibu maalum wa kula na hivyo kufikia hali ya kutoweza kufa.
Mvumbuzi Mhispania aitwaye Juan Ponce de León anajulikana kuwa alitafuta kwa udi na uvumba chemchemi ya ujana. Daktari fulani wa karne ya 18 alipendekeza katika kitabu chake, Hermippus Redivivus, kwamba mabikira wachanga wawekwe katika kijumba wakati wa masika na pumzi zao zikusanywe katika chupa na kutumiwa kama dawa ya kurefusha maisha. Ni wazi kwamba hakuna hata moja ya mbinu hizo iliyofanikiwa.
Je, Mti Uliokatwa Unaweza Kuchipuka Tena?
HUENDA mzeituni ukaonekana hauvutii sana unapolinganishwa na mwerezi maridadi wa Lebanoni. Hata hivyo, mzeituni una uwezo wenye kustaajabisha sana wa kuhimili hali ngumu. Inakadiriwa kwamba mizeituni fulani imekuwapo kwa miaka 1,000 hivi. Mizizi ya mzeituni ni mirefu sana hivi kwamba inaweza kuusadia mti huo kukua tena hata kama shina la mti huo limekufa. Ikiwa mizizi hiyo iko hai, basi mti huo utachipuka tena.
Mwanaume mwaminifu Ayubu alikuwa na uhakika kwamba hata kama angekufa, angeishi tena. (Ayu. 14:13-15) Alitumia mfano wa mti, labda ule wa mzeituni, ili kuonyesha uwezo wa Mungu wa kumfufua. “Kwa maana hata kwa ajili ya mti kuna tumaini,” akasema Ayubu. “Ukikatwa, utachipuka tena.” Mvua inaponyesha baada ya ukame mkali, mabaki ya mzeituni ulionyauka kabisa yanaweza kuchipuka tena kutoka kwenye mizizi yake na kutokeza ‘matawi kama mmea mpya.’—Ayu. 14:7-9.
“Utaitamani Sana”
Maneno ya Ayubu yanatusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyotupenda: Ana uhusiano wa kipekee na wale ambao kama Ayubu, hujiweka mikononi mwake na kumruhusu awafinyange ili wawe watu wenye kupendeza machoni pake. (Isaya 64:8) Yehova anawathamini sana waabudu wake waaminifu. ‘Anatamani’ washikamanifu wake waliokufa. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “-tamani” pasipo shaka ni “mojawapo ya maneno mazito zaidi ya kuonyesha hamu kubwa,” asema msomi mmoja. Ndiyo, Yehova anawakumbuka waabudu wake na pia anatamani kuwafufua.
Hazina za Kiroho
it-1 191
Majivu
Majivu yalitumiwa kurejelea kitu ambacho hakina maana au thamani yoyote. Kwa mfano, Abrahamu alisema hivi mbele za Yehova, “mimi ni mavumbi na majivu.” (Mwa 18:27; ona pia Isa 44:20; Ayu 30:19) Naye Ayubu alifananisha misemo ya wafariji wake wa uwongo na “methali za majivu.”—Ayu 13:12.
NOVEMBA 13-19
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 15-17
“Elifazi Anaonyesha Jinsi Ambavyo Hatupaswi Kuwafariji Wengine”
Kataa Mawazo Yasiyofaa!
Katika hotuba zote tatu, Elifazi alionyesha wazo la kwamba Mungu ni mwenye kudai mengi mno hivi kwamba hakuna jambo watumishi wake wanalofanya linalompendeza. Elifazi alimwambia Ayubu hivi: “Hata watumishi wake, Mungu hana imani nao; na malaika wake huwaona wana kosa.” (Ayubu 4:18, BHN) Baadaye Elifazi alisema hivi kumhusu Mungu: “Yeye hana imani na watakatifu wake, na mbingu zenyewe kwa kweli si safi machoni pake.” (Ayubu 15:15) Naye akauliza: “Je, Mweza-Yote anapendezwa kwa vyovyote kwa kuwa wewe ni mwadilifu?” (Ayubu 22:3) Bildadi alikubaliana na maoni hayo kwa kuwa alisema hivi: “Kuna hata mwezi, nao si mwangavu; nazo nyota zenyewe si safi machoni pake [Mungu].”—Ayubu 25:5.
Tunapaswa kujihadhari ili tusiathiriwe na kufikiri kwa namna hiyo. Kunaweza kutufanya tufikiri kwamba Mungu anatudai mambo mengi mno. Kufikiri kwa njia hiyo kunahatarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Isitoshe, tukiathiriwa na kufikiri kwa namna hiyo, tutaitikiaje tunapotiwa nidhamu? Badala ya kukubali rekebisho kwa unyenyekevu, huenda moyo wetu ‘ukawa na ghadhabu juu ya Yehova’ na hata tunaweza kumwekea kinyongo. (Methali 19:3) Hakika hilo linaweza kuharibu uhusiano wetu pamoja na Mungu.
Iga Unyenyekevu na Wororo wa Yesu
16 Maneno yetu ya wororo. Upendo wetu mwororo kuelekea wengine hutuchochea ‘kusema kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 The.5:14) Tunaweza kusema nini ili kuwatia moyo watu hao? Tunaweza kuwafariji kwa kuwaonyesha kwamba tunawajali na kuwahangaikia kikweli. Tunaweza kuwapongeza kwa unyoofu ili kuwasaidia waone sifa zao nzuri na uwezo wao. Tunaweza kuwakumbusha kwamba Yehova aliwavuta kwa Mwana wake, kwa hiyo lazima wawe ni wenye thamani machoni pake. (Yoh. 6:44) Tunaweza kuwahakikishia kwamba Yehova anawajali sana watumishi wake “waliovunjika moyo” au “waliopondwa roho.” (Zab. 34:18) Maneno yetu ya wororo yanaweza kuwaponya wale wanaohitaji faraja.—Met. 16:24.
Hazina za Kiroho
Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ayubu
7:9, 10; 10:21; 16:22—Je, maneno hayo yanaonyesha kwamba Ayubu hakuamini ufufuo? Ayubu anazungumza mambo ambayo yangetukia ikiwa angekufa. Kwa hiyo, alimaanisha nini? Huenda maneno yake yanamaanisha kwamba iwapo angekufa, watu walioishi katika siku zake hawangemwona tena. Hawangemtambua wala yeye hangeweza kurudi nyumbani kwake wala kutambuliwa tena hadi wakati wa Mungu uliowekwa. Pia, huenda Ayubu alimaanisha kwamba hakuna mtu anayeweza kutoka Sheoli bila kusaidiwa. Maneno ya Ayubu 14:13-15 yanaonyesha wazi kwamba Ayubu aliamini kutakuwa na ufufuo siku zijazo.
NOVEMBA 20-26
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 18-19
“Usiwaache Kamwe Waabudu Wenzako”
Masomo Tunayojifunza Kutokana na Machozi ya Yesu
9 Unaweza kuwategemeza wanaoomboleza. Yesu hakulia tu na Martha na Maria, bali pia aliwasikiliza na kuwafariji. Tunaweza kuwatendea vivyo hivyo wale wanaoomboleza. Dan, mzee wa kutaniko anayeishi Australia, anasema hivi: “Baada ya kufiwa na mke wangu nilihitaji utegemezo. Wenzi kadhaa wa ndoa walikuwa tayari kunisikiliza mchana na usiku. Waliniruhusu niomboleze na hawakuaibika nilipotoa machozi. Pia, walitoa msaada hususa kama vile kuosha gari langu, kuninunulia bidhaa, na kunipikia chakula ilipokuwa vigumu kwangu kufanya mambo hayo. Na walisali pamoja nami mara kwa mara. Walithibitika kuwa marafiki wa kweli na ‘ndugu ambao wamezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.’”— Met. 17:17.
Mpendwa Wako Anapomwacha Yehova
16 Endeleeni kuwategemeza washiriki wa familia walio waaminifu. Wanahitaji upendo na kitia moyo chenu sasa kuliko wakati mwingine wowote. (Ebr. 10:24, 25) Nyakati nyingine, washiriki wa familia wa mtu aliyetengwa na ushirika wamehisi kwamba baadhi ya watu kutanikoni hawashirikiani nao kama awali. Usiruhusu jambo hilo litokee! Vijana ambao wazazi wao wameiacha kweli wanahitaji hasa kupongezwa na kutiwa moyo. Maria, ambaye mume wake alitengwa na ushirika na kuiacha familia yake anasema hivi: “Baadhi ya marafiki wangu walikuja nyumbani na kupika chakula na walijiunga nami katika funzo letu la familia. Walihisi maumivu yangu na kulia pamoja nami. Walinitetea wakati porojo zisizo za kweli zilipoenezwa. Kwa kweli, walinitia moyo sana!”—Rom. 12:13, 15.
Je! Wewe Wajitahidi Kufikia?
20 Baraza la wazee lapaswa kung’amua kwamba mfuto huenda ukasababisha mkazo kwa aliyekuwa mwangalizi au mtumishi wa huduma, hata ikiwa yeye aacha pendeleo hilo kwa kujitolea. Ikiwa yeye hakutengwa na ushirika, lakini wazee waona kwamba ndugu huyo ameshuka moyo, wao wapaswa kuandaa usaidizi wa kiroho wenye upendo. (1 Wathesalonike 5:14) Wapaswa kumsaidia ang’amue kwamba yuahitajiwa katika kundi. Hata ikiwa shauri limetakiwa, huenda usiwe ni muda mrefu sana kabla mwanamume mnyenyekevu mwenye shukrani hajapokea mapendeleo zaidi ya utumishi katika kundi.
Hazina za Kiroho
Uwezo wa Neno Lenye Fadhili
Hata hivyo, Ayubu mwenyewe alipohitaji kitia-moyo, Elifazi na waandamani wake hawakutamka maneno yenye fadhili. Wao walimlaumu Ayubu kwa ajili ya taabu yake, wakidokeza kwamba ni lazima alikuwa na kosa fulani la siri. (Ayubu 4:8) The Interpreter’s Bible chaeleza hivi: “Kile Ayubu ahitajicho ni huruma ya moyo wa kibinadamu. Yeye apokea tu mfululizo wa misemo ya kidini ya kurudiwa-rudiwa yaliyo ‘kweli’ kabisa na yanayovutia kabisa na maadili yaleyale.” Ayubu alivunjika moyo sana kwa kusikia hotuba za Elifazi na waandamani wake hivi kwamba alilazimika kupaza sauti hivi: “Je, mtanichukiza nafsi yangu hata lini, na kunivunja-vunja kwa maneno?”—Ayubu 19:2.
Tusimfanye kamwe mtumishi mwenzetu wa Mungu alie kwa dhiki kwa sababu ya maneno yetu yasiyo na maana na yasiyo ya fadhili. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 24:15.) Mithali moja ya Biblia yaonya hivi: “Yale uyasemayo yaweza kuokoa uhai au kuuharibu; kwa hiyo ni lazima ukubali matokeo ya maneno yako.”—Mithali 18:21, TEV.
NOVEMBA 27–DESEMBA 3
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 20-21
“Uadilifu Haupimwi kwa Utajiri”
Kuwa Tajiri kwa Mungu
12 Yesu alisema kwamba kuwa tajiri kwa Mungu ni tofauti kabisa na kujiwekea hazina za vitu vya kimwili, au kujitafutia utajiri wa kimwili. Hivyo, Yesu alikuwa akisema kwamba hangaiko letu kuu maishani halipaswi kuwa kukusanya utajiri wa kimwili au kufurahia vitu tulivyo navyo. Badala yake, tunapaswa kutumia mali zetu kwa njia ambayo itaboresha, au kujenga, uhusiano wetu pamoja na Yehova. Tukifanya hivyo, bila shaka tutakuwa matajiri kwa Mungu. Kwa nini? Kwa sababu tutaweza kupata baraka nyingi kutoka kwake. Biblia inatuambia hivi: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Methali 10:22.
Hazina za Kiroho
Kumshinda Shetani na Kazi Zake
19 Ni jambo la kupendeza kwamba mtumishi wa Mungu Ayubu alilazimika kukabili “mawazo yenye usumbufu” ambayo Shetani aliwasilisha kupitia Elifazi na Sofari. (Ayubu 4:13-18, NW; 20:2, 3) Kwa hiyo Ayubu alipatwa na “uchungu,” uliomfanya aseme ‘maneno ya haraka’ kuhusu “vitisho” vinavyopata akili yake. (Ayubu 6:2-4; 30:15, 16) Elihu alimsikiliza Ayubu kwa ukimya na kumsaidia kwa moyo mweupe aone maoni yenye hekima sana ya Yehova kuhusu mambo. Vilevile leo, wazee wenye ufahamu huonyesha kwamba wao hujali waliopatwa na pigo kwa kutowaongezea “mkazo” watu kama hao. Badala ya kufanya hivyo, kama Elihu, wao huwasikiliza kwa saburi na kisha kutumia mafuta yenye kufariji ya Neno la Mungu. (Ayubu 33:1-3, 7, NW; Yakobo 5:13-15) Hivyo mtu yeyote ambaye hisia zake za moyoni husumbuliwa na masumbufu, yaliyo ya kweli au ya kuwaziwa, au ‘atishikaye katika ndoto na kwa maono’ kama Ayubu alivyokuwa, aweza kupata faraja ya Kimaandiko yenye kutuliza katika kutaniko.—Ayubu 7:14; Yakobo 4:7.
DESEMBA 4-10
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 22-24
“Je, Mwanadamu Anaweza Kuwa na Faida kwa Mungu?”
Kataa Mawazo Yasiyofaa!
Wazo la kwamba Mungu ni mwenye kudai mengi mno linahusiana sana na maoni ya kwamba Mungu huona wanadamu kuwa bure kabisa. Hotuba ya tatu ya Elifazi ina swali hili: “Je, mwanamume anaweza kuwa na faida kwa Mungu mwenyewe, kwamba mtu mwenye ufahamu awe na faida kwake?” (Ayubu 22:2) Elifazi alikuwa akimaanisha kwamba Mungu huona mwanadamu kuwa bure kabisa. Vivyo hivyo, Bildadi alisema hivi: “Mwanadamu anayeweza kufa anawezaje kuwa upande wa haki mbele za Mungu, au, mtu aliyezaliwa na mwanamke anawezaje kuwa safi?” (Ayubu 25:4) Kulingana na maoni hayo, Ayubu, mwanadamu duni anayeweza kufa, angewezaje kudai kuwa mwadilifu mbele za Mungu?
Watu fulani leo wanajiona kuwa hawafai. Huenda wanahisi hivyo kwa sababu ya malezi yao, matatizo ya maisha, au kwa sababu ya chuki kuelekea jamii au kabila lao. Lakini Shetani na roho wake waovu pia wanafurahia kumfanya mtu ahisi kwamba hafai. Wanapomfanya ahisi kwamba Mungu Mweza-Yote hafurahii chochote anachofanya, inakuwa rahisi sana kwa mtu huyo kuvunjika moyo. Baada ya muda, mtu huyo anaweza kupeperushwa, na hata kujiondoa kwa Mungu aliye hai.—Waebrania 2:1; 3:12.
Uzee na magonjwa hutuwekea vizuizi. Huenda ikaonekana tunatimiza tu sehemu ndogo sana katika utumishi wa Ufalme tukilinganisha na yale tuliyofanya tulipokuwa vijana wenye nguvu na afya nzuri. Ni muhimu kutambua kwamba Shetani na roho wake waovu wanataka tuhisi kwamba Mungu hafurahii yale tunayofanya. Tunapaswa kukataa kufikiri kwa namna hiyo.
Somo la Jinsi ya Kushughulika na Matatizo
Waandamani wake watatu walimvunja moyo Ayubu hata zaidi kwa kusema mawazo yao ya kibinafsi badala ya hekima ya kimungu. Elifazi hata alifikia hatua ya kusema kwamba ‘Mungu hana imani katika watumishi wake’ na kwamba kwa kweli ilikuwa mamoja kwa Yehova iwe Ayubu alikuwa mwadilifu au la. (Ayubu 4:18; 22: 2, 3, NW) Ni vigumu kuwazia maneno yenye kuvunja moyo—au yaliyo ya uongo zaidi—kuliko hayo! Haishangazi kwamba baadaye Yehova aliwakemea Elifazi na waandamani wake kwa ukufuru huo. “Ninyi hamkunena yaliyo sawa katika habari zangu,” yeye akasema. (Ayubu 42:7) Lakini dai lenye madhara zaidi lilikuwa lije bado.
Vijana Wanaofurahisha Moyo wa Yehova
10 Kama Biblia inavyoonyesha, Shetani alitilia shaka uaminifu wa Ayubu na pia wengine wote wanaomtumikia Mungu, kutia ndani wewe. Naam, Shetani alimwambia Yehova hivi alipokuwa akizungumza kuwahusu wanadamu kwa ujumla: “Yote aliyo nayo mtu [si Ayubu tu bali mtu yeyote] atayatoa kwa ajili ya uhai wake.” (Ayubu 2:4) Je, unaona jinsi unavyohusika katika suala hilo muhimu? Kama inavyoonyeshwa na Mithali 27:11, Yehova anasema kwamba unaweza kumpa msingi wa kumjibu Shetani anayemlaumu. Wazia Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu anakusihi wewe utoe jibu kuhusiana na suala kuu lililopo. Hilo ni daraka na pendeleo kubwa sana. Je, unaweza kutimiza yale ambayo Yehova anakusihi ufanye? Ayubu aliyatimiza. (Ayubu 2:9, 10) Ndivyo alivyofanya Yesu na vilevile wengine wengi tangu zamani, kutia ndani vijana. (Wafilipi 2:8; Ufunuo 6:9) Unaweza kufanya vivyo hivyo. Hata hivyo, unapaswa kujua kwamba ni lazima uunge mkono upande mmoja katika suala hilo. Kupitia mwenendo wako utaonyesha kwamba unatetea lawama ya Shetani au jibu la Yehova. Utatetea nini?
Yehova Anakujali!
11 Je, uchaguzi wako ni muhimu machoni pa Yehova? Je, uaminifu ambao watu wengi wameonyesha hautoshi kumpa sababu ya kumjibu Shetani? Ibilisi alidai kwamba hakuna mtu anayemtumikia Yehova kwa sababu ya kumpenda, dai ambalo limekwisha thibitishwa kuwa la uwongo. Lakini bado Yehova anataka uunge mkono upande wake katika suala la enzi kuu kwa sababu anakujali. Yesu alisema hivi: “Si jambo la kutamanika kwa Baba yangu aliye mbinguni kwa mmoja wa wadogo hawa kuangamia.”—Mathayo 18:14.
12 Ni wazi kwamba, Yehova anapendezwa na uchaguzi wako. Jambo muhimu zaidi ni kwamba anaathiriwa nao. Biblia inaonyesha wazi kwamba Yehova ana hisia ambazo huchochewa na mwenendo mzuri au mbaya wa binadamu. Kwa mfano, Yehova ‘alihuzunika,’ Waisraeli walipomwasi tena na tena. (Zaburi 78:40, 41) Kabla ya Gharika ya siku za Noa, wakati ‘maovu ya mwanadamu yalipokuwa makubwa,’ Yehova ‘alihuzunika moyo.’ (Mwanzo 6:5, 6) Fikiria maana ya jambo hilo. Ukiamua kuwa na mwenendo mbaya, utamhuzunisha Muumba wako. Hiyo haimaanishi kwamba Mungu ni dhaifu au anaongozwa na hisia tu. Badala yake anakupenda na kukujali. Kwa upande mwingine, unapofanya yanayofaa unafurahisha moyo wa Yehova. Yeye hufurahi kwa sababu anapata sababu nyingine ya kumjibu Shetani, na pia kwa sababu anaweza kukupa thawabu. Ndivyo anavyotaka kufanya. (Waebrania 11:6) Yehova Mungu ni Baba mwenye upendo kama nini!
Hazina za Kiroho
Tumia Miradi ya Kiroho ili Kumtukuza Muumba Wako
Fikiria jinsi Yehova alivyotimiza kazi ya kuumba ulimwengu hasa kusudi lake la uumbaji ilipohusu dunia. Maneno, “ikawa jioni, ikawa asubuhi,” yanaonyesha kwamba Yehova ndiye aliamua urefu wa vipindi vya uumbaji. (Mwanzo 1:5, 8, 13, 19, 23, 31) Mwanzoni mwa kila kipindi cha uumbaji, alijua waziwazi mradi au kusudi lake kwa siku hiyo ya uumbaji. Naye Mungu akatimiza kusudi lake la kuumba vitu. (Ufunuo 4:11) ‘Nafsi ya Yehova mwenyewe ina tamaa, naye ataifanya,’ akasema mzee wa ukoo Ayubu. (Ayubu 23:13) Yehova alifurahi kama nini kuona “kila kitu alichokuwa amefanya” na kukitangaza kuwa “chema sana”!—Mwanzo 1:31.
Ili tutimize miradi yetu, sisi pia tunapaswa kuwa na tamaa kuu ya kuifikia. Ni nini kitakachotusaidia kukuza tamaa hiyo kuu? Hata wakati dunia ilipokuwa bila umbo, na ukiwa, Yehova angeweza kuona kimbele jinsi ambavyo ingekuwa baadaye—johari maridadi katika anga ambayo ingemletea heshima na utukufu. Vivyo hivyo, tamaa yetu ya kutimiza yale ambayo tumeazimia kufanya inaweza kukuzwa kwa kutafakari matokeo na manufaa ya kutimizwa kwa mradi huo. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kuhusiana na Tony, mwenye umri wa miaka 19. Hakusahau kamwe kile kilichomvutia alipotembelea ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ulaya Magharibi. Tangu wakati huo na kuendelea, Tony alikuwa akifikiria swali hili: ‘Mtu huhisije anapoishi na kutumika mahali kama hapa?’ Tony hakuacha kamwe kufikiria uwezekano wa kutumika Betheli, naye aliendelea kujitahidi kufikia mradi huo. Alifurahi sana wakati miaka kadhaa baadaye ombi lake la kutumika kwenye ofisi ya tawi lilipokubaliwa.
DESEMBA 11-17
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 25-27
“Si Lazima Uwe Mkamilifu Ili Uwe Mtimilifu”
it-1 1210 ¶4
Utimilifu
Ayubu. Inaelekea Ayubu aliishi katika kipindi fulani baada ya kifo cha Yosefu na kipindi hicho Musa alikuwa hai. Ayubu anarejelewa kuwa mwanamume ambaye “alikuwa mtu mnyoofu [Kiebrania, tam] na mtimilifu; alimwogopa Mungu na kuepuka uovu.” (Ayu 1:1; ona AYUBU.) Ni wazi kwamba utimilifu wa mwanadamu ni sehemu ya suala zito lililo katika ya Yehova Mungu na Shetani kwa sababu Mungu alimuuliza Adui yake kumhusu Ayubu, adui huyo alipoingia kwenye mkutano wa malaika mbele za Yehova. Shetani alidai kwamba Ayubu alimwabudu Mungu si kwa sababu anampenda bali kwa ajili ya faida za kibinafsi. Hivyo, alitilia shaka utimilifu wa Ayubu. Ingawa Shetani aliruhusiwa kuharibu mali za Ayubu na kuwaua watoto wake bado alishindwa kabisa kuvunja utimilifu wa Ayubu. (Ayu 1:6–2:3) Kisha, alidai kwamba Ayubu alikuwa mbinafsi na angeweza kuvumilia kupoteza mali zake na watoto wake ilimradi tu aokoe ngozi yake. (Ayu 2:4, 5) Ayubu alipigwa na ugonjwa mbaya sana uliomsababishia maumivu makali, naye mke wake akamvunja moyo, na marafiki wake waliosema mambo ambayo yalikuwa kinyume na viwango na kusudi la Mungu wakamshushia hadhi Ayubu na kumkashifu. (Ayu 2:6-13; 22:1, 5-11) Hata hivyo, Ayubu alisema kwamba hatakana utimilifu wake. “Mpaka nitakapokufa, sitaukana utimilifu wangu! Nitadumisha uadilifu wangu, nami sitauacha kamwe; moyo wangu hautanihukumu maadamu ninaishi.” (Ayu 27 5, 6) Kwa sababu Ayubu alidumisha utimilifu wake alithibitisha kwamba Adui ya Mungu alikuwa mwongo.
Dumisha Utimilifu Wako!
3 Inapohusu watumishi wa Mungu, utimilifu unamaanisha kumpenda Yehova kwa moyo wetu wote na kushikamana naye kabisa, hivi kwamba tunatanguliza mapenzi yake katika maamuzi yetu yote. Fikiria jinsi neno hilo linavyotumiwa katika Biblia. Maana moja ya msingi ya neno “utimilifu” katika Biblia ni: kamili, bila kasoro, au nzima. Kwa mfano, Waisraeli walimtolea Yehova dhabihu za wanyama, na Sheria ilisema kwamba wanyama hao walipaswa kuwa bila kasoro. (Law. 22:21, 22) Watu wa Mungu hawakuruhusiwa kutoa mnyama asiye na mguu, sikio, au jicho; wala hawakupaswa kutoa mnyama mgonjwa. Yehova alitaka mnyama huyo awe kamili, bila kasoro, au ugonjwa wowote. (Mal. 1:6-9) Tunaweza kuelewa kwa nini Yehova alitaka Waisraeli wamtolee dhabihu isiyo na kasoro au iliyo kamili. Tunaponunua bidhaa fulani, iwe ni tunda, kitabu, au kifaa, hatungependa kununua tunda lililooza au kitabu kisicho na kurasa zote au kifaa ambacho hakina sehemu zote. Tungependa kununua bidhaa iliyo kamili, isiyo na kasoro, au nzima. Yehova anahisi vivyo hivyo inapohusu upendo na ushikamanifu wetu kwake. Ni lazima upendo na ushikamanifu wetu kwake uwe kamili, bila kasoro, au upungufu wowote.
4 Je, tunapaswa kufikiri kwamba ili tuwe watimilifu ni lazima tuwe wakamilifu? Huenda tukahisi kwamba tumepungukiwa au tuna kasoro nyingi sana. Hata hivyo, hatuhitaji kuwa na wasiwasi. Fikiria sababu hizi mbili. Kwanza, Yehova hakazii fikira kasoro zetu. Neno lake linatuambia hivi: “Ikiwa ungekuwa unatazama tu makosa, Ee Yah, basi ni nani, Ee Yehova, angeweza kusimama?” (Zab. 130:3) Yehova anajua kwamba sisi si wakamilifu, sisi ni wanadamu wenye dhambi, naye hutusamehe mara nyingi. (Zab. 86:5) Pili, Yehova anajua uwezo wetu, naye hatarajii tutimize mambo yanayopita uwezo wetu. (Soma Zaburi 103:12-14.) Basi ni katika maana gani tunaweza kuwa kamili, bila kasoro, na bila upungufu wowote machoni pake?
5 Kwa watumishi wa Yehova, siri ya kuwa watimilifu ni upendo. Ni lazima upendo wetu kwa Mungu na ujitoaji wetu mshikamanifu kwake akiwa Baba yetu wa mbinguni uwe kamili, bila kasoro, au upungufu wowote. Ikiwa upendo wetu kwake utadumu ukiwa hivyo hata tunapojaribiwa, basi sisi ni watimilifu. (1 Nya. 28:9; Mt. 22:37) Wafikirie tena Mashahidi watatu waliotajwa mwanzoni. Kwa nini walitenda kama walivyotenda? Je, yule msichana mdogo anachukia kufurahia maisha akiwa shuleni, au je, yule ndugu kijana angependa kuaibishwa anapohubiri nyumba kwa nyumba, au yule ndugu mwenye familia je, angependa kupoteza kazi yake? Bila shaka, hapana. Badala yake, wanajua kwamba Yehova ana viwango vya uadilifu, na wamekazia akilini mwao kumpendeza Baba yao wa mbinguni. Upendo wao kwake huwachochea kumtanguliza katika kila uamuzi wanaofanya. Hivyo, matendo yao yanathibitisha kwamba wao ni watimilifu.
Hazina za Kiroho
Tumepangwa Kitengenezo Kulingana na Kitabu cha Mungu
3 Uumbaji unathibitisha kwamba hakuna aliye na utaratibu kama Mungu. Biblia inasema hivi: “Kwa hekima Yehova mwenyewe aliuweka msingi wa dunia. Aliziweka mbingu imara kwa utambuzi.” (Met. 3:19) Tunajua tu “kingo za njia [za Mungu],” na “mnong’ono . . . wa jambo lililosikiwa juu yake.” (Ayu. 26:14) Ingawa tunajua mambo machache sana kuhusu sayari, nyota, na makundi ya nyota, tunatambua kwamba vitu vilivyo angani vimepangwa kwa utaratibu wa ajabu. (Zab. 8:3, 4) Makundi ya nyota yana mamilioni ya nyota, na zote zinasonga kwa utaratibu. Inastaajabisha sana kwamba sayari zinazunguka jua kwa mpangilio kana kwamba zinatii sheria za barabarani! Kwa kweli, mpangilio tata wa ulimwengu unatusaidia kuona kwamba Yehova, “[aliyezifanya] mbingu kwa uelewaji” pamoja na dunia, anastahili sifa, ushikamanifu, na ibada yetu.—Zab. 136:1, 5-9.
DESEMBA 18-24
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 28-29
“Je, Unajulikana kwa Sifa Kama za Ayubu?”
Waonyeshe Fadhili-Upendo Wenye Uhitaji
19 Masimulizi ya Biblia tuliyozungumzia pia yanakazia kwamba fadhili-upendo zinapaswa kuonyeshwa wale ambao hawawezi kujitimizia mahitaji yao. Abrahamu alihitaji msaada wa Bethueli ili kuendeleza ukoo wake. Naye Yakobo alihitaji msaada wa Yosefu ili mwili wake upelekwe Kanaani. Naomi pia alihitaji msaada wa Ruthu ili kupata mrithi. Abrahamu, Yakobo, na Naomi hawangeweza kutimiza mahitaji yao bila kusaidiwa. Vivyo hivyo leo, fadhili-upendo zinapaswa hasa kuonyeshwa wale wenye uhitaji. (Mithali 19:17) Tunapaswa kumwiga mzee wa ukoo Yobu, ambaye alijali ‘maskini aliyelilia msaada, yatima asiyekuwa na wa kumsaidia’ na pia wale “waliokuwa karibu kuangamia.” Yobu pia ‘aliwafanya wajane waone tena furaha moyoni’ na akawa ‘macho kwa kipofu na miguu kwa viwete.’—Ayubu 29:12-15, BHN.
it-1 655 ¶10
Mavazi
Mavazi yalitumiwa kwa njia nyingine za mfano pia. Kama tu sare ama mavazi fulani ya pekee yanavyoonyesha kwamba mtu ni wa shirika fulani, au anaunga mkono jambo fulani, vivyo hivyo, mavazi yanatumiwa kwa njia ya mfano katika Biblia kumtambulisha mtu na msimamo anaochukua na pia mambo anayofanya ili kuunga mkono msimamo wake, kama mfano uliotolewa na Yesu kuhusu vazi la ndoa unavyoonyesha. (Mt 22:11, 12; ona VAZI LA KICHWANI; KIATU.) Kwenye Ufunuo 16:14, 15, Bwana Yesu Kristo anatoa onyo kwamba mtu hapaswi kulala kiroho ili asije akanyang’anywa utambulisho wake akiwa shahidi mwaminifu wa Mungu wa kweli. Jambo hilo ni hatari sana kwa kuwa “vita vya siku kuu ya Mungu Mweza-Yote” vinakaribia.
Majina Yana Maana
Hatukujichagulia majina tuliyopewa tulipozaliwa. Hata hivyo, sisi wenyewe ndio tunaoamua tutakuwa na sifa gani. (Methali 20:11) Hebu jiulize: ‘Yesu na mitume wangenichagulia jina gani ikiwa wangepewa nafasi ya kufanya hivyo? Ni jina gani ambalo lingeeleza vizuri sifa yangu kuu?’
Tunapaswa kufikiria swali hilo kwa uzito. Kwa nini? “Ni afadhali kuchagua jina badala ya utajiri mwingi,” akaandika Mfalme Sulemani mwenye hekima. (Methali 22:1) Kwa kweli, tukijipatia jina zuri, au sifa nzuri katika jamii, tumepata kitu cha thamani. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ni kwamba tukijifanyia jina zuri mbele za Mungu, tutapata hazina ya kudumu. Jinsi gani? Mungu anaahidi kwamba ataandika katika “kitabu cha kumbukumbu” majina ya wale wanaomwogopa, na atawapa uzima wa milele.—Malaki 3:16; Ufunuo 3:5; 20:12-15.
Hazina za Kiroho
Tabasamu Ni Yenye Manufaa Kwako!
Je, kweli kutabasamu hubadili hali ya mambo? Je, wakumbuka wakati tabasamu ya mtu fulani ilipokufanya uhisi kitulizo au kukufanya uhisi umestarehe? Au mtu alipokosa kutabasamu kukakufanya uwe na wasiwasi au hata kuhisi umepuuzwa? Naam, tabasamu hubadili hali ya mambo. Huwa na matokeo kwa yule anayetabasamu na yule ambaye ameonyeshwa tabasamu. Yobu, anayetajwa katika Biblia alisema hivi kuhusu adui zake: “Kama nikiwacheka [“nikatabasamu nao,” NW] hawakuamini; wala hawakuangusha nuru ya uso wangu.” (Ayubu 29:24, Zaire Swahili Bible) “Nuru” ya uso wa Yobu huenda ilirejezea furaha au uchangamfu.
DESEMBA 25-31
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | AYUBU 30-31
“Jinsi Ayubu Alivyodumisha Usafi wa Kiadili”
Usiruhusu Macho Yako Yaone Mambo Yasiyofaa!
8 Tamaa ya macho na ya mwili inaweza pia kuwa na uvutano mbaya juu ya Wakristo wa kweli. Kwa hiyo, Neno la Mungu linatutia moyo tujitie nidhamu kuhusu mambo tunayoona na kutamani. (1 Kor. 9:25, 27; soma 1 Yohana 2:15-17.) Mwanamume mwadilifu Ayubu alitambua kwamba kuna uhusiano wenye nguvu kati ya kuona na kutamani. Alisema hivi: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu. Basi nawezaje kukaza fikira kwa bikira?” (Ayu. 31:1) Ayubu hakukataa tu kumgusa mwanamke kwa njia potovu lakini hangeruhusu hata akili yake ifikirie jambo kama hilo. Yesu alikazia kwamba ni lazima tulinde akili zetu kutokana na mawazo mapotovu aliposema hivi: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mt. 5:28.
Fikiria ‘Mwisho Baadaye’
Kabla ya kuchukua hatua ya kwanza kufuata barabara yenye ishara “Usiingie,” jiulize, ‘Inanielekeza wapi?’ Kufikiria jinsi ‘mwisho baadaye’ unavyoweza kuwa kunatosha kukuzuia usifuate njia inayoweza kuwa na matokeo mabaya. UKIMWI na magonjwa mengine ya zinaa, mimba zisizotakikana, utoaji-mimba, mahusiano yaliyoharibika, na dhamiri zilizochafuka ni matokeo mabaya yanayowapata wale wanaopuuza ishara hizo. Mwisho wa barabara kwa wanaojihusisha katika ukosefu wa maadili unaelezwa waziwazi na mtume Paulo.”—1 Wakorintho 6:9, 10.
Vijana—Mwongozwe na Neno la Mungu
15 Unafikiri ushikamanifu wako kwa Mungu utajaribiwa zaidi wakati gani—je, ni wakati unapokuwa na wengine au unapokuwa peke yako? Ni kweli kwamba unapokuwa shuleni au kazini, inaelekea kwamba ulinzi wako wa kiroho unakuwa imara. Unakuwa macho kuona hatari yoyote ya kiroho. Lakini unapostarehe na kuacha kujilinda ndipo unapokuwa katika hatari kubwa zaidi ya kushambuliwa kiadili.
16 Kwa nini unapaswa kumtii Yehova hata unapokuwa peke yako? Kumbuka jambo hili: Unaweza kuumiza hisia za Yehova au kuufanya moyo wake ushangilie. (Mwa.6:5, 6; Met. 27:11) Yehova anafurahishwa au kuumizwa na matendo yako kwa sababu ‘anakujali.’ (1 Pet. 5:7) Anataka umsikilize ili ujifaidi mwenyewe. (Isa. 48:17, 18) Watumishi fulani wa Yehova katika Israeli la kale walipopuuza mashauri yake, walimfanya ahisi uchungu. (Zab. 78:40, 41) Kwa upande mwingine, Yehova alimpenda sana nabii Danieli, kwa kuwa malaika alimwita “mtu mwenye kutamanika sana.” (Dan. 10:11) Kwa nini? Kwa sababu Danieli aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu si mbele ya watu tu bali pia akiwa peke yake.—Soma Danieli 6:10.
Hazina za Kiroho
Ustadi wa Kusikiliza kwa Upendo
Waandamani wa Ayubu walisikiliza angalau hotuba zake kumi. Na bado, Ayubu alisema hivi: “Laiti ningekuwa na mtu wa kunisikiliza!” (Ayubu 31:35) Kwa nini alisema hivyo? Kwa sababu kusikiliza kwao hakukumfariji. Hawakumjali Ayubu wala hawakutaka kuelewa hisia zake. Kwa kweli, hawakuwa na hisia-mwenzi kama wasikilizaji wenye huruma. Mtume Petro anashauri hivi: “Ninyi nyote iweni na akili zinazopatana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo, wanyenyekevu katika akili.” (1 Petro 3:8) Tunaweza kuonyeshaje hisia-mwenzi? Njia moja ni kwa kujali hisia za yule mtu mwingine na kujitahidi kumwelewa. Tunaweza kuonyesha kwamba tunajali kwa kusema maneno yenye huruma kama vile “haikosi kuwa uliumia sana” au “haikosi ulihisi kwamba hukueleweka.” Njia nyingine ni kusema kwa maneno yako mwenyewe mambo ambayo mtu huyo anakwambia. Hilo linaonyesha kwamba umeelewa yale anayosema. Kusikiliza kwa upendo kunamaanisha kusikiliza maneno na hata hisia zinazowasilishwa.