Uwezo wa Neno Lenye Fadhili
“Moyo uliolemewa na hangaiko, jinsi unavyoweza kufarijiwa na neno lenye fadhili!”—Mithali 12:25, Knox.
WAKRISTO hawalindwi kabisa kutokana na taabu. Nyakati nyingine wao hupatwa na hangaiko kwa sababu ya kuishi katika hizi “nyakati za hatari.”—2 Timotheo 3:1.
Tunapopatwa na msiba kama huo, ni baraka kama nini kusikia maneno yenye fadhili kutoka kwa rafiki mwaminifu-mshikamanifu! “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu,” yasema Biblia. (Mithali 17:17) Mtu mwaminifu Ayubu alijulikana kuwa rafiki wa aina hiyo. Hata Elifazi alisema hivi kumhusu: “Mtu alipojikwaa, akawa dhaifu na kuchoka, maneno yako yalimtia moyo akasimame.”—Ayubu 4:4, Today’s English Version.
Hata hivyo, Ayubu mwenyewe alipohitaji kitia-moyo, Elifazi na waandamani wake hawakutamka maneno yenye fadhili. Wao walimlaumu Ayubu kwa ajili ya taabu yake, wakidokeza kwamba ni lazima alikuwa na kosa fulani la siri. (Ayubu 4:8) The Interpreter’s Bible chaeleza hivi: “Kile Ayubu ahitajicho ni huruma ya moyo wa kibinadamu. Yeye apokea tu mfululizo wa misemo ya kidini ya kurudiwa-rudiwa yaliyo ‘kweli’ kabisa na yanayovutia kabisa na maadili yaleyale.” Ayubu alivunjika moyo sana kwa kusikia hotuba za Elifazi na waandamani wake hivi kwamba alilazimika kupaza sauti hivi: “Je, mtanichukiza nafsi yangu hata lini, na kunivunja-vunja kwa maneno?”—Ayubu 19:2.
Tusimfanye kamwe mtumishi mwenzetu wa Mungu alie kwa dhiki kwa sababu ya maneno yetu yasiyo na maana na yasiyo ya fadhili. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 24:15.) Mithali moja ya Biblia yaonya hivi: “Yale uyasemayo yaweza kuokoa uhai au kuuharibu; kwa hiyo ni lazima ukubali matokeo ya maneno yako.”—Mithali 18:21, TEV.
Kwa kutambua uwezo wa usemi, na tufuate kielelezo cha mtume Paulo. Alipokuwa Makedonia, yeye alikuwa ‘akiwafariji kwa maneno mengi.’—Matendo 20:2.