Je! Wewe Wajitahidi Kufikia?
“Ikiwa mwanamume yeyote anajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi, yeye anatamani kazi nzuri.”—1TIMOTHEO 3:1, NW.
MASHAHIDI WA YEHOVA wana malengo yafaayo ambayo huelekezwa na kutekelezwa kwa njia ya kimungu. Hiyo haishangazi, kwa kuwa Mungu wao ana malengo ya kuheshimika na sikuzote hutimiza makusudi yake. (Isaya 55:8-11) Watumishi wa Yehova hawapaswi kuwa kama wale watu wasio na lengo zuri ambao huishi kivyao tu bila kufanya mengi ya kunufaisha mtu yeyote isipokuwa wao wenyewe. Jambo la umaana mkubwa kwa Mashahidi wa Mungu ni kutimiza lile lengo la kuheshimika la kupiga mbiu juu ya ujumbe wa Ufalme na kushiriki na wengine maarifa yenye kutoa uhai ya Neno la Mungu.—Zaburi 119:105; Marko 13:10; Yohana 17:3.
2 Katika tengenezo la Yehova, kuna malengo mengine ya kuheshimika pia. Mtume Paulo alitaja moja la haya alipoandika hivi: “Taarifa hiyo ni ya uaminifu. Ikiwa mwanamume yeyote anajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi, yeye anatamani kazi nzuri.” Mwanamume wa jinsi hiyo ataka kutimiza jambo fulani kwa faida ya wengine. Atamani “kazi nzuri,” si maisha ya starehe na utukufu. Tafsiri nyingine husema: “Ni kweli kabisa kusema kwamba mwanamume awekaye moyo wake juu ya uongozi ana tamaa ya makubwa yenye kusifika.”—1 Timotheo 3:1, Phillips.
Hatari kwa Wazee
3 Ni kwa njia gani mwanamume awekaye moyo wake juu ya kuwa mwangalizi wa Kikristo alivyo na “tamaa ya makubwa yenye kusifika”? Basi, tamaa ya makubwa ni tamaa yenye idili ya kufikia lengo hususa. Ni kweli kwamba kuna tamaa za makubwa za kuheshimika na zisizoheshimika. Lakini ikiwa mwanamume hujitahidi kwa unyenyekevu kufikia cheo cha mwangalizi kwa sababu ataka kutumikia wengine, utumishi wake hutolewa kwa matilaba za unyoofu na waweza kutokeza baraka za kiroho. Lakini yuahitaji kulinda moyo wake.—Mithali 4:23.
4 Watu fulani wenye tamaa ya makubwa hutafuta utukufu. Wengine hutaka kutawala wanadamu wenzao. Pupa ya umashuhuri au mamlaka ni kama mzizi uliooza ambao waweza kusababisha hata mti wenye sura ya afya ubwagike chini. Mkristo pia angeweza kujiacha ashindwe na tamaa hiyo ya makubwa yenye kuchochewa vibaya. (Mithali 16:18) “Mimi nililiandikia kundi jambo fulani,” akasema mtume Yohana, “lakini Diotrefe, ambaye hupenda kuwa na mahali pa kwanza miongoni mwao [“ambaye hutaka kuwa kichwa cha kila jambo,” Phillips], hapokei chochote kutoka kwetu kwa staha. Hiyo ndiyo sababu, mimi nikija, nitafanya ukumbuko wa kazi zake ambazo yeye aendelea kufanya, akipayuka-payuka juu yetu kwa maneno maovu. Pia, bila kutosheka na mambo haya, wala yeye hawapokei akina ndugu kwa staha, na wale wanaotaka kuwapokea yeye hujaribu kuwazuilia na kuwatupa nje ya kundi.” (3 Yohana 9, 10, NW) Tamaa ya makubwa ya Diotrefe haikuwa ya Kikristo. Kiburi na kufuatia mamlaka kwa tamaa ya makubwa juu ya wengine ni mambo yasiyo na nafasi miongoni mwa wafuasi wa kweli wa Yesu.—Mithali 21:4.
5 Mwangalizi Mkristo ambaye hutunza wa-jibu wake kwa matilaba ifaayo hatafuatia tamaa za makubwa ya ubinafsi. Atafikiria kazi hii nzuri ya uangalizi wa Kikristo kuwa pendeleo lenye kupewa na Mungu na atachunga kundi la kondoo za Mungu “si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi.” (1 Petro 5:2, 3) Ndiyo, waangalizi wapaswa kulinda dhidi ya kusitawisha kiburi na kutafuta kutumia uwezo vibaya.
6 Mzee hapaswi kupiga ubwana juu ya Wakristo wengine, kwa maana yeye ni mfanya kazi mwenzao, si ‘bwana-mkubwa juu ya imani yao.’ (2 Wakorintho 1:24, NW) Mitume fulani walipotafuta umashuhuri, Yesu alisema: “Mnajua kwamba watawala wa mataifa hutawala watu wao kwa mabavu [hupiga ubwana juu yao, NW] na wakuu hao huwamiliki watu wao. Lakini kwenu isiwe hivyo, ila yeyote anayetaka kuwa mkuu kati yenu sharti awe mtumishi wa wote; na anayetaka kuwa wa kwanza kati yenu sharti awe mtumishi wenu. Jinsi hiyohiyo, Mwana wa Mtu hakuja kutumikiwa bali kutumikia na kutoa maisha yake kuwa fidia ya watu wengi.” (Mathayo 20:20-28, HNWW) Mzee siye Mchungaji Mkuu bali ni mchungaji wa chini tu. Akipiga ubwana juu ya kundi la kondoo, yeye adhihirisha roho ya kiburi. Hasa madhara yangetokea kama angeshawishi wengine wamsaidie kuendeleza zaidi tamaa zake za kiburi cha makubwa. Yasema mithali moja: “Kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa BWANA [Yehova, NW]; hakika, hatakosa adhabu.”—Mithali 16:5.
7 Kwa hiyo wazee Wakristo wapaswa ‘kunyenyekea chini ya mkono wa Mungu ulio hodari.’ Kiburi hufunga njia ya mafaa ya kiroho, kwa maana ni wanyenyekevu peke yao walio na hali ifaayo ya moyo na akili kuweza kufanya mapenzi ya kimungu. “Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.” (1 Petro 5:5, 6) Ndiyo, Yehova huwabariki walio na akili za unyenyekevu. Ni kutokana na hao kwamba wanaume wastahilio huwekwa watumikie wakiwa wazee Wakristo.
8 Historia ya ki-siku-hizi ya Mashahidi wa Yehova imejaa masimulizi ya utumishi wa unyenyekevu uliotolewa na watu mmoja mmoja wenye kumcha Mungu. Mathalani, fikiria W. J. Thorn mwenye tabia pole, ambaye wakati mmoja alikuwa piligrimu, au mwangalizi anayesafiri, na mfanya kazi wa Betheli kwa muda mrefu. Kuhusu yeye, Mkristo mmoja alisema: “Mimi sitasahau kamwe kamwe taarifa moja iliyosemwa na Ndugu Thorn ambayo imenisaidia hadi leo hii. Alisema, nami namnukuu, ‘Wakati wowote nianzapo kujifikiria sana, mimi husubiri kidogo na kusema: “Ewe kavumbi katiti. Una nini cha kujivunia?”’” Lo, hiyo ni sifa ya kupongezeka kama nini ambayo wazee na wengine wapaswa kuionyesha! Kumbuka, “thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha BWANA [Yehova, NW] ni utajiri, na heshima [utukufu, NW], nayo ni uzima.”—Mithali 22:4.
Tamaa ya Kupewa na Mungu Kutumikia
9 Je! tamaa ya kutumikia kuwa mwangalizi ni ya kupewa na Mungu? Ndiyo, kwa maana roho ya Yehova ndiyo huandaa kichocheo, moyo mkuu, na imara ya kumtolea yeye utumishi mtakatifu. Kwa kielelezo, ilikuwaje wafuasi wa Yesu wenye kunyanyaswa waliposali wapate ujasiri wa kuhubiri? “Mahali ambapo walikuwa wamekusanyika pamoja palitikiswa; na mmoja kwa wote wakajazwa roho takatifu na wakawa wakisema neno la Mungu kwa ujasiri.” (Matendo 4:27-31, NW) Kwa kuwa roho takatifu ilitokeza matokeo ya jinsi hiyo, yaweza pia kuchochea mtu ajitahidi kufikia.
10 Ingeweza kuwa ni kwa nini Mkristo mkomavu hajitahidi kufikia? Huenda akawa ni mwanamume wa kiroho lakini ahisi kuwa hatoshelei. (1 Wakorintho 2:14, 15) Bila shaka, twapaswa kuwa na maoni ya kiasi juu yetu wenyewe, tukiwa na habari juu ya mipaka yetu. (Mika 6:8) Badala ya kufikiri kwa kimbelembele kwamba sisi ndio tustahilio zaidi kwa daraka fulani, ni vema kukumbuka kwamba “hekima ipo pamoja na wenye kiasi.” (Mithali 11:2, NW) Lakini twapaswa pia kung’amua kwamba ikiwa Mungu atupa sisi pendeleo la utumishi, yeye atatugawia pia imara ihitajiwayo ili kulitekeleza. Kama alivyosema Paulo: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”—Wafilipi 4:13.
11 Huenda Mkristo asijitahidi kufikia kwa sababu yeye ahisi kwamba hana hekima ya kutosha kutoa shauri. Basi, labda aweza kupata hekima kwa kuwa mwanafunzi wa Neno la Mungu mwenye bidii ya uendelevu zaidi, na kwa uhakika apaswa kusali apate hekima. Yakobo aliandika: “Mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa. Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yo yote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku. Maana mtu kama yule asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa Bwana [Yehova, NW]. Mtu wa nia mbili husita-sita katika njia zake zote.” (Yakobo 1:5-8) Katika kujibu sala, Mungu alimpa Sulemani “moyo wa hekima na uelewevu” uliomwezesha kupambanua kati ya mema na mabaya anapohukumu. (1 Wafalme 3:9-14, NW) Kisa cha Sulemani kilikuwa cha pekee, lakini kwa funzo la bidii ya uendelevu na msaada wa Mungu, wanaume waliokabidhiwa daraka la kundi waweza kushauri wengine kwa uadilifu. “BWANA [Yehova, NW] huwapa watu hekima; kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu.”—Mithali 2:6.
12 Kadiri fulani ya hangaiko huenda ikazuia mwanamume asijitahidi kufikia. Huenda akafikiri kwamba angekuwa hawezi kubeba daraka zito la kuwa mzee. Hata Paulo alikiri hivi: “Kuna lile ambalo hunijia mbio siku kwa siku, hangaiko kwa ajili ya makundi yote.” (2 Wakorintho 11:28, NW) Lakini mtume alijua la kufanya anapopatwa na hangaiko, kwa maana aliandika hivi: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Ndiyo, sala na tumaini katika Mungu vyaweza kusaidia kutuliza hangaiko.
13 Ikiwa hangaiko fulani laendelea, mwanamume aliye na wasiwasi juu ya kujitahidi kufikia angeweza kusali kama Daudi: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu [yenye kuon-doa utulivu, NW]; uone kama iko njia iletayo majuto [maumivu, NW] ndani yangu, ukaniongoze katika njia ya milele.” (Zaburi 139:23, 24) Hata tuwe tuna mawazo gani “yenye kuondoa utulivu” au ‘yenye kutia wasiwasi,’ Mungu aweza kutusaidia tukabiliane nayo ili tuweze kufanya maendeleo ya kiroho. (Ona The New International Version.) Wazo hilo limewekwa vizuri katika zaburi nyingine: “Niliposema: ‘Hakika wayo wangu utaenda kwa kuyumbayumba,’ fadhili-upendo zako mwenyewe, O Yehova, ziliendelea kunitegemeza. Mawazo yangu yenye kuondoa utulivu yalipokuwa mengi ndani yangu, maliwazo yako mwenyewe yalianza kuikumbatia-kumbatia nafsi yangu.”—Zaburi 94:18, 19, NW.
Tumikia kwa Mteremo kama Apendavyo Yehova
14 Ikiwa mwanamume Mkristo ashindwa kujitahidi kufikia kwa sababu ya hangaiko, hisia za kukosa utoshelevu, au ukosefu wa kichocheo, hakika ingefaa kusali apate roho ya Mungu. Yesu alisema: “Ikiwa nyinyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, lo! jinsi Baba aliye katika mbingu atakavyowapa roho takatifu kwa wingi zaidi wale wanaomwomba!” (Luka 11:13, NW) Kwa kuwa amani na kujidhibiti yamo miongoni mwa matunda ya roho, roho hiyo yaweza kutusaidia tukabiliane na hangaiko au hisia za kukosa utoshelevu.—Wagalatia 5:22, 23.
15 Namna gani ukosefu wa kichocheo? Tukiwa Wakristo waliobatizwa, twahitaji kusali kwamba Mungu atufanye tutende yampendezayo. Daudi alisihi hivi: “Nifanye mimi nijue njia zako mwenyewe, O Yehova . . . Nifanye mimi nitembee katika ukweli wako na unifundishe.” (Zaburi 25:4, 5, NW) Sala za jinsi hii zitatusaidia tuepuke kijia kibaya, nasi twaweza kusali kwa njia kama hiyo ikiwa hatuna kichocheo cha kujitahidi kufikia. Twaweza kumwomba Yehova atufanye tutake kukubali mapendeleo ya utumishi. Kwa uhakika, tukisali ili tupate roho ya Mungu na kuacha nafasi wazi ya kuelekezwa nayo, bila shaka tutajifanya tupatikane ikiwa twatolewa mapendeleo ya utumishi. Ingawaje, watumishi wa Mungu hawangetaka kukinza roho yake kwa njia yoyote.—Waefeso 4:30.
16 Tukiwa na “akili ya Kristo,” twapata upendezo katika kufanya mapenzi ya kimungu. (1 Wakorintho 2:16, NW) Yesu alikuwa na mtazamo ule ule kama mtunga zaburi, aliyesema: “Kuyafanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; naam, sheria yako imo moyoni mwangu.” (Zaburi 40:8) Kristo alisema: “Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako,” na hilo lilifikia hatua ya kifo juu ya mti wa mateso. (Waebrania 10:9, 10) Tamaa ya kufanya kila jambo liweze-kanalo katika utumishi wa Yehova huandaa kichocheo imara cha kujitahidi kufikia daraka la kundi.
Tazama Kwenye Wakati Ujao
17 Kwa sababu ya matatizo ya afya na sababu nyinginezo, watu fulani ambao hapo kwanza walitunza wajibu wa maana katika kundi hawana mapendeleo hayo sasa. Hawapaswi kuvunjika moyo. Twajua kwamba wanaume wengi waaminifu wasioweza tena kutumikia kikamili kama walivyofanya wakati mmoja wangali wanasimama imara wakiwa washika-ukamilifu. (Zaburi 25:21) Kwa kweli, wazee wanyenyekevu wa muda mrefu waweza kuendelea kufanya ujuzi wao upatikane kwa kubaki katika baraza la wazee. Ingawa wao wawekewa kizuizi na uzee au manyonge fulani, hawahitaji kuondoka cheoni. Kwa sasa, acheni kila Shahidi wa Yehova alithamini sana pendeleo lipitalo yote, lile la ‘kuongea juu ya utukufu wa umaliki wa Mungu’ la kuwa wategemezaji wa jina lake takatifu.—Zaburi 145:10-13, NW.
18 Ikiwa wewe ulikuwa mzee au mtumishi wa huduma wakati mmoja lakini sasa hutumikii katika nafasi hiyo, uwe na uhakika kwamba Mungu angali akujali, na labda wakati ujao atakujalia mapendeleo fulani yasiyotarajiwa. (1 Petro 5:6, 7) Ikiwa wewe wahitaji kufanya marekebisho fulani, uwe na nia ya kukiri kosa na kulitengeneza kwa msaada wa Mungu. Watu fulani ambao wamefutwa wasiwe wazee wamechukua maoni yasiyo ya Kikristo, na wachache wamekuwa wasiotenda au wameangukia mbali kutoka kwenye ukweli. Lakini ni jambo la hekima kama nini kuwa kama wale ambao wamedhihirisha roho nzuri! Mathalani, mzee mmoja aliyekuwa ametumikia kwa miaka mingi katika Amerika ya Kati alipofutwa, alisema: “Mimi nina maumivu sana kuwa nilipoteza pendeleo ambalo nimelithamini kwa muda mrefu sana. Lakini nitajitahidi kwa njia yoyote ambayo akina ndugu wataka kunitumia na nijitahidi kupata tena mapendeleo yangu ya utumishi.” Baada ya muda, ndugu huyo alipendelewa kutumikia tena akiwa mzee.
19 Ikiwa wewe ulifutwa usiwe mzee au mtumishi wa huduma, basi dumisha roho ya unyenyekevu. Epuka maoni ya uchungu mkali ambayo yangekukosesha ustahili wa mapendeleo ya wakati ujao. Roho ya kimungu huvuta staha. Badala ya kuvunjika moyo, fikiria jinsi Yehova anavyobariki huduma yako au watu wa nyumba yako. Jenga familia yako kiroho, uwazuru walio wagonjwa, na uwatie moyo wanyonge. Juu ya yote, thamini sana pendeleo lako la kusifu Mungu na kupiga mbiu ya habari njema ukiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.—Zaburi 145:1, 2; Isaya 43:10-12.
20 Baraza la wazee lapaswa kung’amua kwamba mfuto huenda ukasababisha mkazo kwa aliyekuwa mwangalizi au mtumishi wa huduma, hata ikiwa yeye aacha pendeleo hilo kwa kujitolea. Ikiwa yeye hakutengwa na ushirika, lakini wazee waona kwamba ndugu huyo ameshuka moyo, wao wapaswa kuandaa usaidizi wa kiroho wenye upendo. (1 Wathesalonike 5:14) Wapaswa kumsaidia ang’amue kwamba yuahitajiwa katika kundi. Hata ikiwa shauri limetakiwa, huenda usiwe ni muda mrefu sana kabla mwanamume mnyenyekevu mwenye shukrani hajapokea mapendeleo zaidi ya utumishi katika kundi.
21 Ikiwa wewe wajitahidi kufikia, huenda ikawa lazima ungoje kwa muda fulani kabla ya kupokea mapendeleo zaidi ya utumishi. Usikose subira. Musa alingoja kwa miaka 40 kabla Mungu hajamtumia wakati wa kuwaweka huru Waisraeli kutoka utumwa wa Kimisri. (Matendo 7:23-36) Kabla ya kuwekwa awe mwandamizi wa Musa, Yoshua alitumikia kwa muda mrefu akiwa hadimu wake. (Kutoka 33:11; Hesabu 27:15-23) Daudi alingoja kwa muda fulani kabla hajawekwa juu ya kiti cha ufalme cha Israeli. (2 Samweli 2:7; 5:3) Petro na Yohana Marko yaonekana walipitia vipindi vya kutakaswa. (Mathayo 26:69-75; Yohana 21:15-19; Matendo 13:13; 15:36-41; Wakolosai 4:10) Kwa hiyo ikiwa sasa wewe huna wajibu wa kundi, huenda Yehova akawa anakuruhusu ufinyangwe kwa kupata ujuzi mwingi zaidi. Vyovyote vile, tafuta msaada wa Mungu wakati ujitahidipo kufikia, naye huenda akakubariki kwa mapendeleo zaidi ya utumishi. Kwa sasa, fanya kazi kwa bidii ya uendelevu ili ustahili daraka la kundi na udhihirishe roho ya Daudi, aliyejulisha hivi: “Kinywa changu kitazinena sifa za BWANA [Yehova, NW]; wote wenye mwili na walihimidi jina lake takatifu milele na milele.”—Zaburi 145:21.
Wewe Ungejibuje
◻ Ni hatari gani ambazo wazee Wakristo wapaswa kulinda dhidi yazo?
◻ Ni nini kiwezacho kusaidia wale wasiojitahidi kufikia kwa sababu ya hangaiko au hisia za kukosa utoshelevu?
◻ Ni nini kiwezacho kuchochea mtu ajifanye kupatikana kwa ajili ya daraka la kundi?
◻ Waliokuwa wazee na watumishi wa huduma hapo zamani wapaswa kutazama kwenye wakati ujao wakiwa na maoni gani?
[Maswali ya Funzo]
1. Jambo lenye umaana mkubwa zaidi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ni kutimiza lengo gani?
2. Ni lengo gani la wanaume Wakristo lililotajwa na Paulo kwenye 1 Timotheo 3:1?
3, 4. Kwa nini mwanamume anayejitahidi kufikia kuwa mwangalizi apaswa kulinda moyo wake?
5. Waangalizi wapaswa kutunza wajibu wao wakiwa na maoni gani?
6. Kwa nini ni lazima mzee asipige ubwana juu ya watu wa Mungu?
7, 8. (a) Kwa nini yahitajiwa kabisa wazee Wakristo wawe wanyenyekevu? (b) Toa kielelezo cha mzee mnyenyekevu.
9. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba tamaa ya mtu kutumikia kuwa mwangalizi ni ya kupewa na Mungu?
10. (a) Ni nini sababu moja ambayo huenda mwanamume Mkristo asiwe anajitahidi kufikia? (b) Mungu akitujalia pendeleo la utumishi, twaweza kuwa na uhakika juu ya nini?
11. Ni jambo gani laweza kufanywa na Mkristo ambaye hajitahidi kufikia kwa sababu yeye ahisi kwamba hana hekima ya kutosha kutoa shauri?
12. Ikiwa mwanamume hajitahidi kufikia kwa sababu ya hangaiko, ni nini liwezalo kumsaidia?
13. Mwanamume angeweza kusali jinsi gani ikiwa ana wasiwasi juu ya kujitahidi kufikia?
14. Kwa nini mwanamume asiyejitahidi kufikia apaswa kusali apate roho takatifu ya Mungu?
15. Ni sala za aina gani ambazo zaweza kusaidia wale wasio na kichocheo cha kujifanya wapatikane kwa ajili ya mapendeleo ya utumishi?
16. Ni maoni gani huandaa kichocheo imara cha kujitahidi kufikia daraka la kundi?
17. (a) Kwa nini wanaume ambao sasa hawatumikii kikamili kama walivyokuwa wakifanya wakati mmoja hawapaswi kuvunjika moyo? (b) Ni nini lililo pendeleo kubwa kupita yote?
18. (a) Ikiwa mzee au mtumishi wa huduma amefutwa, huenda nini kikahitajiwa? (b) Ni maoni gani mazuri aliyoonyesha mzee mmoja aliyefutwa?
19. Ni ushauri gani ufaao ambao wapewa kwa ndugu ambaye amefutwa asiwe mzee au mtumishi wa huduma?
20. Ni jinsi gani huenda baraza la wazee likaweza kusaidia aliyekuwa mwangalizi au mtumishi wa huduma?
21. Ni nani waliongoja mapendeleo ya utumishi, na ni jambo gani ladokezwa kwa wale wanaoyangoja leo?
[Picha katika ukurasa wa 19]
W. J. Thorn aliweka kielelezo kizuri akiwa mzee mnyenyekevu
[Picha katika ukurasa wa 21]
Kama Yesu, je! wewe una nia ya kufanya kila jambo liwezekanalo katika utumishi wa Yehova?