-
Hekalu Lasafishwa TenaYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 103
Hekalu Lasafishwa Tena
MATHAYO 21:12, 13, 18, 19 MARKO 11:12-18 LUKA 19:45-48 YOHANA 12:20-27
YESU AULAANI MTINI NA KULISAFISHA HEKALU
LAZIMA YESU AFE ILI WENGI WAPATE UZIMA
Yesu na wanafunzi wake wamelala siku tatu huko Bethania tangu walipofika kutoka Yeriko. Sasa, asubuhi na mapema Jumatatu, Nisani 10, wanaelekea Yerusalemu. Yesu anahisi njaa. Basi anapoona mtini, anaenda kwenye mtini huo. Je, anapata tini zozote?
Sasa ni mwishoni mwa Machi, lakini msimu wa tini utakuwa Juni. Hata hivyo, ule mtini una majani, kwa kuwa umechipua mapema. Basi, Yesu anafikiri kwamba huenda kuna tini za mapema. Hata hivyo, hapati tini zozote. Majani yameufanya mtini huo uonekane kana kwamba una tini. Kisha Yesu anasema: “Mtu yeyote asile matunda yako tena kamwe.” (Marko 11:14) Papo hapo, ule mtini unaanza kunyauka, na maana ya jambo hilo itajulikana kesho yake asubuhi.
Baada ya muda mfupi, Yesu na wanafunzi wake wanafika Yerusalemu. Anaenda katika hekalu, ambalo alikuwa amelikagua alasiri siku iliyotangulia. Leo, anafanya mengi zaidi ya kulikagua; anachukua hatua kama ile aliyochukua miaka mitatu mapema kwenye Pasaka ya mwaka wa 30 W.K. (Yohana 2:14-16) Pindi hii, Yesu anawafukuza “wale [wanaouza] na kununua hekaluni.” Pia, anazipindua “meza za wale [wanaobadili] pesa na viti vya wale [wanaouza] njiwa.” (Marko 11:15) Hata hamruhusu mtu yeyote anayebeba kitu apitie katikati ya ua wa hekalu kuelekea sehemu nyingine ya jiji.
Kwa nini Yesu anawachukulia hatua kali wale wanaobadili pesa na kuuza wanyama hekaluni? Anasema: “Je, haikuandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa ajili ya mataifa yote’? Lakini mmeifanya kuwa pango la wanyang’anyi.” (Marko 11:17) Anawaita watu hao wanyang’anyi kwa sababu wanawatoza bei ya juu sana watu wanaonunua wanyama kwa ajili ya dhabihu. Yesu anaona shughuli zao kuwa upunjaji, au unyang’anyi.
Bila shaka, wakuu wa makuhani, waandishi, na watu mashuhuri wanasikia kuhusu jambo ambalo Yesu amefanya, nao wanaanzisha upya jitihada za kutaka kumuua. Hata hivyo, wanakabili tatizo. Hawajui jinsi ya kumuua Yesu, kwa sababu umati unakusanyika ili kumsikiliza.
Si Wayahudi tu waliokuja kwa ajili ya Pasaka, bali pia watu waliogeuzwa imani na kufuata dini ya Wayahudi. Kati yao kuna Wagiriki ambao wamekuja kuabudu kwenye sherehe hiyo. Wanaenda kuzungumza na Filipo, labda wakivutiwa na jina lake la Kigiriki, nao wanaomba kumwona Yesu. Huenda Filipo hajui kama jambo hilo linafaa, basi anashauriana na Andrea. Wawili hao wanazungumza na Yesu kuhusu jambo hilo, na inaonekana bado Yesu yuko hekaluni.
Yesu anajua kwamba atakufa baada ya siku chache, basi huu si wakati wa kukutana na watu wenye udadisi au wakati wa kutafuta umashuhuri. Anawajibu mitume hao wawili kwa kutumia mfano, akisema: “Saa imefika ya Mwana wa binadamu kutukuzwa. Kwa kweli ninawaambia, mbegu ya ngano isipoanguka kwenye udongo na kufa, hubaki ikiwa mbegu moja tu; lakini ikifa, huzaa matunda mengi.”—Yohana 12:23, 24.
Huenda mbegu moja ya ngano ikaonekana kuwa na thamani ndogo. Hata hivyo, ikipandwa kwenye udongo na “kufa” ikiwa mbegu moja, inaweza kuota na baada ya muda kumea na kuwa shina lenye mbegu nyingi. Vivyo hivyo, Yesu ni mtu mmoja mkamilifu. Hata hivyo, ikiwa atakuwa mwaminifu kwa Mungu mpaka kifo, atakuwa njia ya kuwapatia uzima wa milele wengi walio na roho kama hiyo ya kujidhabihu. Basi, Yesu anasema: “Yeyote anayeupenda sana uhai wake huuangamiza, lakini yeyote anayeuchukia uhai wake katika ulimwengu huu ataulinda kwa ajili ya uzima wa milele.”—Yohana 12:25.
Yesu hajifikirii tu yeye mwenyewe, kwa maana anasema: “Ikiwa yeyote anataka kunihudumia, basi anifuate na mahali nilipo ndipo mhudumu wangu atakapokuwa pia. Ikiwa yeyote anataka kunihudumia, Baba atamheshimu.” (Yohana 12:26) Ni thawabu iliyoje! Wale wanaoheshimiwa na Baba watatawala pamoja na Kristo katika Ufalme.
Anapofikiria kuhusu mateso mengi na kifo chenye maumivu kinachomsubiri, Yesu anasema: “Sasa ninataabika, nami niseme nini? Baba, niokoe kutoka katika saa hii.” Lakini Yesu hataki kuepuka kufanya mapenzi ya Mungu. Anaongezea hivi: “Hata hivyo, ndiyo sababu nimekuja kwenye saa hii.” (Yohana 12:27) Yesu anakubaliana na yote ambayo Mungu amekusudia, kutia ndani kifo chake cha kujidhabihu.
-
-
Wayahudi Wasikia Sauti ya Mungu—Je, Wataonyesha Imani?Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 104
Wayahudi Wasikia Sauti ya Mungu—Je, Wataonyesha Imani?
WATU WENGI WASIKIA SAUTI YA MUNGU
MSINGI WA HUKUMU
Akiwa katika hekalu siku ya Jumatatu, Nisani 10, Yesu anazungumza kuhusu kifo chake kinachokaribia. Akihangaikia jinsi jina la Mungu litakavyohusika, Yesu anasema: “Baba, litukuze jina lako.” Sauti yenye nguvu kutoka mbinguni inajibu: “Nimelitukuza nami nitalitukuza tena.”—Yohana 12:27, 28.
Watu walio hapo karibu wanashangaa. Baadhi yao wanafikiri kwamba wamesikia mngurumo. Wengine wanasema: “Malaika ameongea naye.” (Yohana 12:29) Hata hivyo, wametoka tu kumsikia Yehova akizungumza! Na hii si mara ya kwanza kwa wanadamu kusikia sauti ya Mungu kuhusiana na Yesu.
Miaka mitatu na nusu mapema, Yesu alipobatizwa, Yohana Mbatizaji alisikia Mungu akisema hivi kumhusu Yesu: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” Baadaye kwenye Pasaka ya mwaka wa 32 W.K., Yesu aligeuka sura mbele ya Yakobo, Yohana, na Petro. Wanaume hao watatu walimsikia Yehova akisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali. Msikilizeni.” (Mathayo 3:17; 17:5) Lakini sasa, mara hii ya tatu, Yehova anazungumza kwa njia ambayo wengi wanaweza kumsikia!
Yesu anasema: “Sauti hii imesikika, si kwa ajili yangu, bali kwa ajili yenu.” (Yohana 12:30) Ni uthibitisho kwamba kwa kweli yeye ni Mwana wa Mungu, Masihi aliyetabiriwa.
Isitoshe, maisha ya Yesu ya uaminifu yanaonyesha jinsi wanadamu wanavyopaswa kuishi na pia yanathibitisha kwamba Shetani Ibilisi, mtawala wa ulimwengu, anastahili kuangamizwa. Yesu anasema: “Sasa ulimwengu huu unahukumiwa; sasa mtawala wa ulimwengu huu atatupwa nje.” Badala ya kuwa hasara, kifo cha Yesu kinachokaribia kitakuwa ushindi. Jinsi gani? Anaeleza hivi: “Na bado mimi, nikiinuliwa kutoka duniani, nitawavuta watu wa namna zote kwangu.” (Yohana 12:31, 32) Kupitia kifo chake kwenye mti, Yesu atawavuta watu kwake, na hivyo kufungua njia ya kupata uzima wa milele.
Umati unaposikia Yesu akisema kuhusu ‘kuinuliwa,’ wanasema: “Tulisikia kutoka katika Sheria kwamba Kristo hudumu milele. Kwa nini unasema kwamba lazima Mwana wa binadamu ainuliwe? Huyo Mwana wa binadamu ni nani?” (Yohana 12:34) Licha ya uthibitisho mwingi, kutia ndani kusikia sauti ya Mungu, wengi wao hawamkubali Yesu kuwa ndiye Mwana wa kweli wa binadamu, Masihi aliyeahidiwa.
Kama alivyofanya wakati uliopita, Yesu anajirejezea kuwa “nuru.” (Yohana 8:12; 9:5) Anauhimiza hivi umati: “Nuru itakuwa miongoni mwenu kwa muda kidogo zaidi. Tembeeni wakati bado mna nuru, ili giza lisiwazidi nguvu . . . Wakati mna nuru, iweni na imani katika nuru ili muwe wana wa nuru.” (Yohana 12:35, 36) Kisha Yesu anaondoka, kwa sababu hapaswi kufa siku ya Nisani 10. Siku ya Pasaka Nisani 14 ndipo ‘atakapoinuliwa,’ yaani, atatundikwa kwenye mti.—Wagalatia 3:13.
Tunapochunguza huduma ya Yesu, ni wazi kwamba unabii ulikuwa ukitimia Wayahudi walipokosa kumwamini. Isaya alikuwa ametabiri kwamba macho ya watu yangepofushwa na mioyo yao ingekuwa migumu hivi kwamba hawangegeuka ili waponywe. (Isaya 6:10; Yohana 12:40) Naam, Wayahudi wengi wanakataa kwa ukaidi uthibitisho kwamba Yesu ndiye Mkombozi wao aliyeahidiwa, njia ya uzima.
Nikodemo, Yosefu wa Arimathea, na watawala wengi ‘kwa kweli wanamwamini’ Yesu. Lakini je, watatenda kwa imani, au wataogopa, iwe ni kwa sababu wanaogopa kufukuzwa katika sinagogi au kwa sababu ‘wanaupenda utukufu wa wanadamu’?—Yohana 12:42, 43.
Yesu anaeleza maana ya kumwamini: “Yeyote anayeniamini, haniamini mimi tu bali pia Yule aliyenituma; na yeyote anayeniona mimi anamwona pia Yule aliyenituma.” Kweli ambazo Mungu alimwagiza Yesu afundishe na ambazo Yesu anaendelea kuzitangaza ni muhimu sana hivi kwamba anasema: “Yeyote anayenipuuza na hapokei maneno yangu, ana wa kumhukumu. Neno ambalo nimesema ndilo litakalomhukumu katika siku ya mwisho.”—Yohana 12:44, 45, 48.
Kisha Yesu anamalizia kwa kusema: “Sijasema kwa uamuzi wangu mwenyewe, bali Baba aliyenituma amenipa amri kuhusu jambo la kutangaza na la kusema. Pia, ninajua kwamba amri yake inamaanisha uzima wa milele.” (Yohana 12:49, 50) Yesu anajua kwamba baada ya muda mfupi atamwaga damu yake iwe dhabihu kwa ajili ya wanadamu wanaomwamini.—Waroma 5:8, 9.
-