-
Afundisha Kuhusu Unyenyekevu Kwenye Pasaka ya MwishoYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 116
Afundisha Kuhusu Unyenyekevu Kwenye Pasaka ya Mwisho
MATHAYO 26:20 MARKO 14:17 LUKA 22:14-18 YOHANA 13:1-17
YESU ANAKULA PASAKA YAKE YA MWISHO PAMOJA NA MITUME
AFUNDISHA SOMO KWA KUWAOSHA MITUME MIGUU
Tayari Petro na Yohana wamefika Yerusalemu kufanya matayarisho kwa ajili ya Pasaka, kama Yesu alivyowaagiza. Baadaye, Yesu na wale mitume wengine kumi wanaelekea huko. Ni alasiri na jua linatua wakati Yesu na wanafunzi wake wanapoteremka kwenye Mlima wa Mizeituni. Hii ni mara ya mwisho kwa Yesu kuwa kwenye mlima huo mchana hadi atakapofufuliwa.
Baada ya muda mfupi, Yesu na wanafunzi wake wanafika jijini na kwenda kwenye nyumba ambamo watakula mlo wa Pasaka. Wanapanda ngazi na kwenda kwenye chumba kikubwa ghorofani. Humo wanapata matayarisho yote yakiwa yamefanywa kwa ajili ya mlo wao wa faragha. Yesu amekuwa akitazamia sana pindi hiyo kwa kuwa anasema: “Nimetamani sana kula Pasaka hii pamoja nanyi kabla sijateseka.”—Luka 22:15.
Desturi ya kupitisha vikombe kadhaa vya divai kati ya watu wanaokula pamoja mlo wa Pasaka ilianzishwa miaka mingi iliyopita. Sasa baada ya Yesu kupokea kikombe kimoja, anatoa shukrani na kusema: “Chukueni kikombe hiki na mkipitishe kutoka kwa mmoja mpaka kwa mwingine kati yenu, kwa maana ninawaambia, kuanzia sasa sitakunywa tena divai ya mzabibu mpaka Ufalme wa Mungu utakapokuja.” (Luka 22:17, 18) Ni wazi kwamba kifo chake kinakaribia.
Wakiwa wanaendelea na mlo wa Pasaka, jambo lisilo la kawaida linatokea. Yesu anasimama, anavua mavazi yake ya nje, na kuchukua taulo. Kisha anaweka maji katika beseni iliyo hapo karibu. Ilikuwa kawaida kwa mwenye nyumba kuhakikisha kwamba miguu ya wageni wake imeoshwa, labda na mfanyakazi. (Luka 7:44) Katika pindi hii, mwenye nyumba hayupo, basi Yesu anafanya kazi hiyo. Yeyote kati ya mitume wake angetumia fursa hiyo kufanya hivyo, lakini hakuna anayefanya hivyo. Je, labda ni kwa sababu bado wanashindana? Vyovyote vile, wanaaibika Yesu anapoosha miguu yao.
Yesu anapomfikia Petro, anakataa akisema: “Hutaosha kamwe miguu yangu.” Yesu anamjibu: “Nisipokuosha, wewe huna sehemu pamoja nami.” Petro anamwambia hivi kwa hisia: “Bwana, usioshe miguu yangu tu, bali pia mikono na kichwa changu.” Bila shaka, Petro anashangazwa na jinsi Yesu anavyomjibu: “Yeyote ambaye ameoga hahitaji kuoshwa zaidi ya miguu yake, yuko safi kabisa. Nanyi mko safi, lakini sio nyote.”—Yohana 13:8-10.
Yesu anawaosha miguu mitume wote 12, kutia ndani Yuda Iskariote. Baada ya kuvaa mavazi yake ya nje na kuketi tena mezani, Yesu anawauliza: “Je, mnaelewa jambo ambalo nimewafanyia? Ninyi huniita, ‘Mwalimu,’ na, ‘Bwana,’ nanyi hamjakosea, kwa maana ndivyo nilivyo. Kwa hiyo, ingawa mimi ni Bwana na Mwalimu, niliiosha miguu yenu, basi ninyi pia mnapaswa kuoshana miguu. Kwa maana nimewawekea kielelezo, ili mfanye kama nilivyowafanyia. Kwa kweli ninawaambia, mtumwa si mkuu kuliko bwana wake, wala yule aliyetumwa si mkuu kuliko yule aliyemtuma. Ikiwa mnajua mambo haya, mtakuwa wenye furaha mkiyatenda.”—Yohana 13:12-17.
Hilo ni somo zuri sana kuhusu kutumikia kwa unyenyekevu! Wafuasi wa Yesu hawapaswi kujitafutia mahali pa kwanza, wakifikiri kwamba wao ni watu muhimu na wanapaswa kuhudumiwa. Badala yake, wanapaswa kuiga mfano wa Yesu, si kwa kuwa na desturi ya kuoshana miguu, bali kwa kuwa tayari kutumikia kwa unyenyekevu na bila ubaguzi.
-
-
Mlo wa Jioni wa BwanaYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 117
Mlo wa Jioni wa Bwana
MATHAYO 26:21-29 MARKO 14:18-25 LUKA 22:19-23 YOHANA 13:18-30
YUDA ATAMBULISHWA KUWA MSALITI
YESU AANZISHA MLO WA UKUMBUSHO
Mapema jioni ya leo, Yesu aliwafundisha mitume wake somo la unyenyekevu kwa kuwaosha miguu. Sasa, inaelekea ni baada ya mlo wa Pasaka, anaponukuu maneno ya kinabii aliyosema Daudi: “Mtu niliyekuwa na amani naye, ambaye nilimwamini, aliyekuwa akila mkate wangu, amekiinua kisigino chake dhidi yangu.” Kisha anafafanua hivi: “Mmoja wenu atanisaliti.”—Zaburi 41:9; Yohana 13:18, 21.
Mitume wanatazamana na kila mmoja wao anauliza: “Bwana, je, ni mimi?” Hata Yuda Iskariote anauliza pia. Petro anamwambia Yohana ambaye amekaa kando ya Yesu hapo mezani, aulize mtu huyo ni nani. Basi Yohana anamuegemea Yesu na kumuuliza “Bwana, ni nani?”—Mathayo 26:22; Yohana 13:25.
Yesu anajibu hivi: “Ni yule ambaye nitampa kipande cha mkate ninachochovya.” Yesu anachovya kipande cha mkate katika bakuli lililo mezani na kumpa Yuda akisema: “Mwana wa binadamu anaenda zake, kama ilivyoandikwa kumhusu, lakini ole wake mtu atakayemsaliti Mwana wa binadamu! Ingekuwa afadhali kama mtu huyo hangezaliwa.” (Yohana 13:26; Mathayo 26:24) Kisha Shetani anamwingia Yuda. Tayari mwanamume huyu amepotoka, sasa anajitoa ili kufanya mapenzi ya Ibilisi na hivyo anakuwa “mwana wa maangamizi.”—Yohana 6:64, 70; 12:4; 17:12.
Yesu anamwambia Yuda: “Kile unachofanya, kifanye upesi zaidi.” Kwa kuwa Yuda ndiye aliyekuwa akitunza sanduku la pesa, baadhi ya mitume wanafikiri Yesu anamwambia: “‘Nunua vitu tunavyohitaji kwa ajili ya sherehe,’ au kwamba anapaswa kuwapa maskini kitu fulani.” (Yohana 13:27-30) Badala yake, Yuda anaenda kumsaliti Yesu.
Jioni hii ya mlo wa Pasaka, Yesu anaanzisha mlo mwingine tofauti kabisa. Anachukua mkate, anatoa sala ya shukrani, anaumega, na kuwapa mitume wake wale. Anasema: “Huu unamaanisha mwili wangu, ambao utatolewa kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.” (Luka 22:19) Mkate huo unapitishwa, nao mitume wanakula.
Sasa Yesu anachukua kikombe cha divai, anatoa sala ya shukrani, na kuwapitishia. Kila mmoja wao anakunywa kutoka kwenye kikombe ambacho Yesu anasema hivi kukihusu: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.”—Luka 22:20.
Basi, Yesu anaanzisha ukumbusho wa kifo chake ambao wafuasi wake wanapaswa kukumbuka siku ya Nisani 14 kila mwaka. Mwadhimisho huo utawakumbusha kile ambacho Yesu na Baba yake wamefanya ili kuwawezesha watu wenye imani wakombolewe kutoka kwa hukumu ya dhambi na kifo. Mwadhimisho huu ni mkuu kuliko Pasaka ilivyo kwa Wayahudi, kwa sababu unakazia kukombolewa kikweli kwa wanadamu wanaoamini.
Yesu anasema kwamba damu yake “itamwagwa kwa ajili ya wengi ili wasamehewe dhambi.” Kati ya wengi ambao watasamehewa ni mitume wake waaminifu na wengine walio kama hao. Hao ndio watakaokuwa pamoja naye katika Ufalme wa Baba yake.—Mathayo 26:28, 29.
-
-
Wabishana Kuhusu Aliye Mkuu ZaidiYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 118
Wabishana Kuhusu Aliye Mkuu Zaidi
MATHAYO 26:31-35 MARKO 14:27-31 LUKA 22:24-38 YOHANA 13:31-38
YESU ATOA USHAURI KUHUSU CHEO
YESU ATABIRI KWAMBA PETRO ATAMKANA
UPENDO UNAWATAMBULISHA WAFUASI WA YESU
Katika jioni yake ya mwisho pamoja na mitume wake, Yesu amewafundisha somo muhimu kuhusu unyenyekevu kwa kuwaosha miguu. Kwa nini jambo hilo linafaa? Ni kwa sababu wana udhaifu fulani. Wanampenda Mungu, lakini bado wanahangaika kuhusu aliye mkuu zaidi kati yao. (Marko 9:33, 34; 10:35-37) Udhaifu huo unaonekana tena jioni hii.
Mitume wanakuwa na “bishano kali kuhusu ni nani aliye mkuu zaidi kati yao.” (Luka 22:24) Bila shaka, Yesu anahuzunika sana anapoona wakibishana tena! Anafanya nini?
Badala ya kuwakemea mitume kwa sababu ya mtazamo na tabia yao, Yesu anajadiliana nao kwa subira: “Wafalme wa mataifa hupiga ubwana juu yao, na wale walio na mamlaka juu yao huitwa Wafadhili. Hata hivyo, ninyi hampaswi kuwa hivyo. . . . Kwa maana ni nani aliye mkuu zaidi, yule anayekula au yule anayehudumu?” Kisha Yesu anawakumbusha mfano ambao amewawekea sikuzote, anasema: “Lakini mimi ni kama mtu anayehudumu kati yenu.”—Luka 22:25-27.
Ingawa hawajakamilika, mitume wameshikamana na Yesu katika hali nyingi ngumu. Kwa hiyo, anasema: “Ninafanya agano pamoja nanyi, kama Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:29) Wanaume hao ni wafuasi washikamanifu wa Yesu. Anawahakikishia kwamba kupitia agano analofanya kati yake nao, watatawala pamoja naye katika Ufalme.
Ingawa mitume wana tazamio hilo zuri, wao bado ni wanadamu na hawajakamilika. Yesu anawaambia: “Shetani anataka kuwapata ninyi nyote ili awapepete kama ngano,” ambayo hutawanyika inapopepetwa. (Luka 22:31) Pia anawaonya hivi: “Ninyi nyote mtakwazika kuhusiana nami usiku wa leo, kwa maana imeandikwa: ‘Nitampiga mchungaji, nao kondoo wa kundi watatawanyika.’”—Mathayo 26:31; Zekaria 13:7.
Petro akiwa na uhakika anakataa akisema: “Hata wengine wote wakikwazika kuhusiana nawe, mimi sitakwazika kamwe!” (Mathayo 26:33) Yesu anamwambia Petro kwamba kabla jogoo hajawika mara mbili usiku huo, Petro atamkana. Hata hivyo, Yesu anasema: “Nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isidhoofike; nawe utakaporudi, watie nguvu ndugu zako.” (Luka 22:32) Lakini Petro anasema tena kwa ujasiri: “Hata nikilazimika kufa pamoja nawe, sitakukana kamwe.” (Mathayo 26:35) Wale mitume wengine wanasema vivyo hivyo.
Yesu anawaambia hivi wanafunzi wake: “Nipo pamoja nanyi muda kidogo zaidi. Mtanitafuta; na kama nilivyowaambia Wayahudi, ninawaambia ninyi pia, ‘Ninakoenda hamwezi kuja.’” Kisha anasema: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda, nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.”—Yohana 13:33-35.
Petro anapomsikia Yesu akisema kwamba atakuwa pamoja nao muda kidogo tu, anamuuliza: “Bwana, unaenda wapi?” Yesu anajibu: “Ninakoenda huwezi kunifuata sasa, lakini utanifuata baadaye.” Petro anashangaa kisha anasema: “Bwana, kwa nini siwezi kukufuata sasa? Nitatoa uhai wangu kwa ajili yako.”—Yohana 13:36, 37.
Sasa Yesu anazungumzia wakati ambapo aliwatuma mitume katika kampeni ya kuhubiri huko Galilaya bila mfuko wa pesa au mfuko wa chakula. (Mathayo 10:5, 9, 10) Anawauliza: “Je, mlikosa chochote?” Wanajibu: “Hapana!” Lakini watafanya nini katika siku zijazo? Yesu anawaagiza: “Yule aliye na mkoba wa pesa au mfuko wa chakula aubebe, na yule asiye na upanga, auze vazi lake la nje anunue upanga. Kwa maana ninawaambia mambo yaliyoandikwa kunihusu yatatimia, yaani, ‘Naye alihesabiwa pamoja na waasi sheria.’ Kwa maana hilo linatimia kunihusu.”—Luka 22:35-37.
Yesu anazungumzia wakati ambapo atatundikwa kwenye mti pamoja na watenda maovu, au waasi sheria. Baada ya hapo, wafuasi wake watateswa sana. Wanafikiri kwamba wako tayari nao wanasema: “Bwana, tazama! hapa pana panga mbili.” Anawaambia: “Inatosha.” (Luka 22:38) Panga mbili walizo nazo zitampa Yesu fursa ya kuwafundisha jambo lingine muhimu.
-
-
Yesu—Njia, Kweli, na UzimaYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 119
Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
YESU ANAENDA KUTAYARISHA MAHALI
ANAWAAHIDI WAFUASI WAKE MSAIDIZI
BABA NI MKUU KULIKO YESU
Akiwa bado katika chumba cha juu pamoja na mitume baada ya mlo wa ukumbusho, Yesu anawatia moyo hivi: “Mioyo yenu isitaabike. Iweni na imani katika Mungu; iweni na imani pia katika mimi.”—Yohana 13:36; 14:1.
Yesu anawapa mitume wake sababu itakayowasaidia wasiwe na wasiwasi atakapoondoka: “Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. . . . Nikienda na kuwatayarishia mahali, nitakuja tena nami nitawapokea nyumbani kwangu, ili mahali nilipo, ninyi pia muwe hapo.” Hata hivyo, mitume hawaelewi kwamba anazungumza kuhusu kwenda mbinguni. Tomasi anasema: “Bwana, sisi hatujui unakoenda. Tunawezaje kuijua njia?”—Yohana 14:2-5.
Yesu anajibu hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.” Mtu anaweza kuingia katika nyumba ya Baba yake wa mbinguni ikiwa tu atamkubali Yesu, mafundisho yake, na kuiga maisha yake. Yesu anasema: “Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.”—Yohana 14:6.
Filipo ambaye anasikiliza kwa makini, anatoa ombi hili: “Bwana, tuonyeshe Baba na hilo linatutosha.” Inaonekana Filipo anataka ishara fulani kutoka kwa Mungu, kama vile maono ambayo Musa, Eliya, na Isaya walipokea. Hata hivyo, mitume wana kitu bora kuliko maono hayo. Yesu anaonyesha jambo hilo anaposema: “Je, hata baada ya kuwa pamoja nanyi kwa muda mrefu hivyo, bado Filipo hujanijua? Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” Yesu anawakilisha kikamili utu wa Baba; kwa hiyo, kuishi pamoja na Yesu na kumtazama ni kama kumwona Baba. Bila shaka, Baba ni mkuu kuliko Mwana, kwa maana Yesu anasema: “Mambo ninayowaambia sisemi kwa kujitungia.” (Yohana 14:8-10) Mitume wanaona kwamba Yesu anampa sifa Baba yake kwa mambo yote anayofundisha.
Mitume wa Yesu wamemwona akifanya kazi za ajabu na wamemsikia akitangaza habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. Sasa anawaambia: “Yeyote anayeniamini atafanya pia kazi ambazo mimi hufanya; naye atafanya kazi kubwa kuliko hizi.” (Yohana 14:12) Yesu hamaanishi kwamba watafanya miujiza mikubwa kuliko ile aliyofanya. Hata hivyo, watafanya huduma yao kwa kipindi kirefu zaidi, katika eneo kubwa zaidi, na kuwahubiria watu wengi zaidi.
Yesu atakapoondoka hatawaacha peke yao, anawaahidi hivi: “Mkiomba jambo lolote katika jina langu, nitalifanya.” Isitoshe anasema: “Nitamwomba Baba, naye atawapa msaidizi mwingine awe pamoja nanyi milele, roho ya ile kweli.” (Yohana 14:14, 16, 17) Anawahakikishia kwamba watapokea msaidizi mwingine, yaani, roho takatifu. Jambo hilo linatokea siku ya Pentekoste.
Yesu anasema: “Bado muda kidogo nao ulimwengu hautaniona tena, lakini ninyi mtaniona, kwa sababu ninaishi, nanyi mtaishi.” (Yohana 14:19) Yesu atawatokea katika umbo la kimwili baada ya kufufuliwa, na pia, baadaye, atawafufua ili wawe pamoja naye mbinguni wakiwa viumbe wa roho.
Sasa Yesu anataja ukweli huu: “Yeyote aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye anayenipenda. Na yeyote anayenipenda atapendwa na Baba yangu, nami nitampenda na kujionyesha waziwazi kwake.” Kisha mtume Yuda, ambaye pia anaitwa Thadayo, anauliza: “Bwana, imekuwaje kwamba unakusudia kujionyesha waziwazi kwetu bali si kwa ulimwengu?” Yesu anamjibu hivi: “Ikiwa yeyote ananipenda, atalishika neno langu, naye Baba yangu atampenda . . . Yeyote asiyenipenda hayashiki maneno yangu.” (Yohana 14:21-24) Tofauti na wafuasi wake, ulimwengu hautambui kwamba Yesu ndiye njia, kweli, na uzima.
Yesu ataondoka, basi wanafunzi wake watakumbukaje mambo yote aliyowafundisha? Yesu anaeleza hivi:“Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba ataituma katika jina langu, hiyo itawafundisha mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” Mitume wameona jinsi roho takatifu ilivyo na nguvu, basi wanatiwa moyo na uhakikisho huo. Yesu anaongezea hivi: “Ninawaachia amani; ninawapa amani yangu. . . . Mioyo yenu isitaabike wala kuogopa.” (Yohana 14:26, 27) Basi wanafunzi hawapaswi kuwa na wasiwasi, kwa kuwa Baba ya Yesu atawaongoza na kuwalinda.
Baada ya muda mfupi, itathibitika wazi kwamba Mungu anawalinda. Yesu anasema: “Mtawala wa ulimwengu anakuja, naye hana uwezo juu yangu.” (Yohana 14:30) Ibilisi alifaulu kumwingia Yuda na kumwongoza. Lakini Yesu hana udhaifu unaoletwa na dhambi ambao Shetani anaweza kuutumia kumfanya amwasi Mungu. Wala Ibilisi hataweza kumzuia Yesu katika kifo. Kwa nini? Yesu anasema: “Ninafanya kama vile Baba alivyoniamuru.” Ana uhakika kwamba Baba yake atamfufua.—Yohana 14:31.
-
-
Kuzaa Matunda Kama Matawi na Kuwa Rafiki za YesuYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 120
Kuzaa Matunda Kama Matawi na Kuwa Rafiki za Yesu
MZABIBU WA KWELI NA MATAWI
JINSI YA KUENDELEA KUKAA KATIKA UPENDO WA YESU
Yesu amekuwa akiwatia moyo mitume wake waaminifu kwa mazungumzo yanayogusa moyo. Muda umesonga, labda ni usiku wa manane. Sasa Yesu anatoa mfano wenye kuchochea:
Anaanza hivi: “Mimi ndiye mzabibu wa kweli, naye Baba yangu ndiye mkulima.” (Yohana 15:1) Mfano wake unafanana na jambo lililosemwa karne nyingi mapema kuhusu taifa la Israeli, ambalo liliitwa mzabibu wa Mungu. (Yeremia 2:21; Hosea 10:1, 2) Hata hivyo, Yehova analikatilia mbali taifa hilo. (Mathayo 23:37, 38) Basi Yesu anazungumzia jambo jipya. Yeye ndiye mzabibu ambao baba yake amekuwa akiupalilia tangu alipomtia mafuta Yesu kwa roho takatifu mwaka wa 29 W.K. Lakini Yesu anaonyesha kwamba mzabibu huo haumwakilishi yeye peke yake, anaposema:
“[Baba yangu] huliondoa kila tawi ndani yangu lisilozaa matunda, naye hulisafisha kila tawi linalozaa matunda, ili lizae matunda zaidi. . . . Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa matunda likiwa peke yake lisipobaki katika mzabibu, vivyo hivyo hamwezi kuzaa matunda msipokaa katika muungano pamoja nami. Mimi ndiye mzabibu; nanyi ndio matawi.”—Yohana 15:2-5.
Yesu amewaahidi wanafunzi wake kwamba baada ya yeye kuondoka, atamtuma msaidizi, yaani, roho takatifu. Baada ya siku hamsini na moja, mitume na watu wengine wanapokea roho hiyo, na basi wanakuwa matawi ya mzabibu huo. Na “matawi” yote yanapaswa kubaki katika muungano na Yesu. Ili kutimiza jambo gani?
Anaeleza hivi: “Yeyote anayekaa katika muungano pamoja nami, nami katika muungano pamoja naye, huyo huzaa matunda mengi; kwa maana bila mimi hamwezi kufanya lolote kamwe.” Matawi hayo—wafuasi wake waaminifu—wangezaa matunda mengi, kwa kuiga sifa za Yesu, na kuwahubiria wengine kuhusu Ufalme wa Mungu, na kufanya wanafunzi wengi. Namna gani mtu asipobaki katika muungano na Yesu na akose kuzaa matunda? Yesu anaeleza hivi: “Ikiwa yeyote hakai katika muungano pamoja nami, atatupwa.” Kwa upande mwingine, Yesu anasema: “Mkikaa katika muungano pamoja nami, na maneno yangu yakae ndani yenu, ombeni chochote mnachotaka nanyi mtapewa.”—Yohana 15:5-7.
Sasa Yesu anazungumzia jambo ambalo amelitaja mara mbili—kushika amri zake. (Yohana 14:15, 21) Anafafanua njia muhimu ambayo wanafunzi wake wanaweza kuthibitisha kwamba wanafanya hivyo: “Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu, kama vile ambavyo nimeshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake.” Hata hivyo, zaidi ya kumpenda Yehova Mungu na Mwana wake kuna mengi yanayohusika. Yesu anasema: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda. Hakuna mtu aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu atoe uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya mambo ninayowaamuru.”—Yohana 15:10-14.
Baada ya saa chache, Yesu ataonyesha upendo wake kwa kuutoa uhai wake kwa ajili ya wote wanaomwamini. Mfano wake unapaswa kuwachochea wafuasi wake waonyeshane upendo kama huo wa kujidhabihu. Upendo huo ndio utakaowatambulisha, kama Yesu alivyosema hapo awali: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.”—Yohana 13:35.
Mitume wanapaswa kutambua kwamba Yesu anawaita “rafiki.” Anaeleza sababu ya kuwaita hivyo: “Nimewaita rafiki, kwa sababu nimewajulisha mambo yote niliyosikia kutoka kwa Baba yangu.” Huo ni uhusiano wenye thamani sana—kuwa marafiki wa karibu wa Yesu na kujua mambo ambayo Baba alimwambia! Hata hivyo, ili wafurahie uhusiano huo, ni lazima ‘waendelee kuzaa matunda.’ Ikiwa watafanya hivyo, Yesu anasema: “hata mkimwomba Baba jambo lolote katika jina langu, [atawapa].”—Yohana 15:15, 16.
Upendo kati ya “matawi” hayo, yaani, wanafunzi wake, utawasaidia kuvumilia mambo yatakayotokea. Anawaonya kwamba ulimwengu utawachukia. Ingawa hivyo, anawafariji hivi: “Ikiwa ulimwengu unawachukia, kumbukeni kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, . . . kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia.”—Yohana 15:18, 19.
Akieleza zaidi sababu itakayofanya ulimwengu uwachukie, Yesu anaongezea hivi: “Watawatendea mambo yote haya kwa ajili ya jina langu, kwa sababu hawamjui Yule aliyenituma.” Yesu anasema kwamba miujiza yake, inawahukumu wale wanaomchukia: “Kama singefanya kati yao kazi ambazo hakuna mwingine aliyezifanya, hawangekuwa na dhambi; lakini sasa wameniona, nao wamenichukia mimi na pia Baba yangu. Kwa kweli, chuki yao inatimiza unabii.—Yohana 15:21, 24, 25; Zaburi 35:19; 69:4.
Yesu anaahidi tena kutuma msaidizi, roho takatifu. Wafuasi wake wote wanaweza kupata nguvu hizo na zinaweza kuwasaidia kuzaa matunda, yaani, ‘kutoa ushahidi.’—Yohana 15:27.
-
-
“Jipeni Moyo! Mimi Nimeushinda Ulimwengu”Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 121
“Jipeni Moyo! Mimi Nimeushinda Ulimwengu”
BAADA YA MUDA MFUPI MITUME HAWATAMWONA TENA YESU
HUZUNI YA MITUME ITAGEUKA KUWA SHANGWE
Yesu na mitume wake wanakaribia kuondoka kwenye chumba cha juu ambapo walikula mlo wa Pasaka. Baada ya kuwahimiza vya kutosha, Yesu anaongezea hivi: “Nimewaambia mambo haya ili msikwazike.” Kwa nini ushauri huo uliwafaa? Anawaambia hivi: “Watu watawafukuza katika masinagogi. Kwa kweli, saa inakuja ambayo kila mtu atakayewaua atafikiri kwamba amemtolea Mungu utumishi mtakatifu.”—Yohana 16:1, 2.
Huenda habari hizo zinafanya mitume wawe na wasiwasi. Ingawa hapo awali Yesu alikuwa amesema kwamba ulimwengu utawachukia, hakuwa amewaambia moja kwa moja kwamba watauawa. Kwa nini? Yesu anasema: “Sikuwaambia mambo haya mwanzoni, kwa sababu nilikuwa pamoja nanyi.” (Yohana 16:4) Sasa anawaonya kabla hajaondoka. Jambo hilo litawasaidia wasikwazike baadaye.
Yesu anaendelea kusema: “Ninaenda kwa Yule aliyenituma; na bado hakuna hata mmoja wenu anayeniuliza, ‘Unaenda wapi?’” Mapema jioni hiyo walikuwa wameuliza mahali anakoenda. (Yohana 13:36; 14:5; 16:5) Lakini sasa, wakiwa wameogopa kwa sababu alitaja kuhusu kuteswa, wanalemewa na huzuni. Hivyo, hawaulizi zaidi kuhusu utukufu atakaopata au jambo hilo litamaanisha nini kwa waabudu wa kweli. Yesu anasema hivi: “Kwa sababu nimewaambia mambo haya, mioyo yenu imejaa huzuni.”—Yohana 16:6.
Kisha Yesu anaeleza hivi: “Ninaenda zangu kwa faida yenu. Kwa maana nisipoenda, msaidizi hatakuja kwenu; lakini nikienda, nitamtuma kwenu.” (Yohana 16:7) Yesu akifa na kwenda mbinguni ndipo wanafunzi wake watakapopokea roho takatifu, ambayo ataituma kama msaidizi wa watu wake mahali popote duniani.
Roho takatifu “[itauthibitishia] waziwazi ulimwengu kuhusu dhambi na kuhusu uadilifu na kuhusu hukumu.” (Yohana 16:8) Naam, kosa la ulimwengu la kutomwamini Mwana wa Mungu litafunuliwa. Yesu atakapopaa mbinguni atatoa uthibitisho hakika wa uadilifu wake na ataonyesha kwa nini Shetani, “mtawala wa ulimwengu,” anastahili kuhukumiwa.—Yohana 16:11.
Yesu anaendelea kusema: “Bado nina mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili kwa sasa.” Atakapomimina roho takatifu, itawaongoza kwenye “kweli yote,” nao wataweza kuishi kulingana na kweli hiyo.—Yohana 16:12, 13.
Mitume wanashangaa Yesu anaposema hivi: “Baada ya muda kidogo hamtaniona tena, na baada ya muda kidogo mtaniona.” Wanaulizana anamaanisha nini. Yesu anatambua kwamba wanataka kumuuliza kuhusu jambo hilo, basi anaeleza hivi: “Kwa kweli ninawaambia, mtalia na kuomboleza, lakini ulimwengu utashangilia; mtahuzunika, lakini huzuni yenu itageuka kuwa shangwe.” (Yohana 16:16, 20) Yesu anapouawa siku inayofuata alasiri, viongozi wa kidini wanashangilia, lakini wanafunzi wanaomboleza. Kisha huzuni yao inageuka kuwa shangwe Yesu anapofufuliwa! Nao wanazidi kuwa na shangwe anapomimina juu yao roho takatifu ya Mungu.
Akilinganisha hali ya mitume na mwanamke aliye na uchungu wa kuzaa, Yesu anasema: “Mwanamke anapokuwa akizaa anahisi huzuni kwa sababu saa yake imefika, lakini baada ya kumzaa mtoto hakumbuki tena dhiki hiyo kwa sababu anashangilia kwamba mtu amezaliwa ulimwenguni.” Yesu anawatia moyo mitume wake kwa kusema: “Ninyi pia mnahuzunika sasa; lakini nitawaona tena na mioyo yenu itashangilia na hakuna mtu atakayeondoa shangwe yenu.”—Yohana 16:21, 22.
Kufikia sasa, mitume hawajatoa ombi lolote kamwe katika jina la Yesu. Sasa anasema: “Siku hiyo mtamwomba Baba katika jina langu.” Kwa nini watafanya hivyo? Si kwa sababu Baba hataki kujibu. Kwa kweli, Yesu anasema: “Baba mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu mmenipenda . . . nikiwa mwakilishi wa Mungu.”—Yohana 16:26, 27.
Huenda maneno ya Yesu yenye kutia moyo yamewapa mitume ujasiri wa kusema hivi: “Kwa hiyo, tunaamini kwamba ulitoka kwa Mungu.” Hivi karibuni uhakika huo utajaribiwa. Kwa kweli, Yesu anafafanua jambo litakalotokea: “Tazama! Saa inakuja, na kwa kweli imefika, wakati kila mmoja wenu atatawanyika na kwenda nyumbani kwake, nanyi mtaniacha peke yangu.” Lakini anawahakikishia hivi: “Nimewaambia mambo haya ili kupitia kwangu muwe na amani. Ulimwenguni mtapata dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:30-33) Si kwamba Yesu anawakimbia. Ana uhakika kwamba wao pia wanaweza kuushinda ulimwengu, kama yeye alivyofanya, kwa kutimiza kwa uaminifu mapenzi ya Mungu licha ya jitihada za Shetani na ulimwengu wake za kuvunja utimilifu wao.
-
-
Sala ya Mwisho ya Yesu Katika Chumba cha JuuYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 122
Sala ya Mwisho ya Yesu Katika Chumba cha Juu
MATOKEO YA KUMJUA MUNGU NA MWANA WAKE
UMOJA KATI YA YEHOVA, YESU, NA WANAFUNZI
Akichochewa na upendo wake mwingi kwa mitume wake, Yesu amekuwa akiwatayarisha kabla hajaondoka. Sasa anatazama mbinguni na kusali hivi kwa Baba yake: “Mtukuze mwana wako ili mwana wako akutukuze, kama vile ulivyompa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili awape uzima wa milele wote ambao umempa.”—Yohana 17:1, 2.
Kwa kweli, Yesu anatambua kwamba kumpa Mungu utukufu ndilo jambo muhimu zaidi. Lakini tumaini ambalo Yesu anataja linafariji sana—uzima wa milele! Akiwa amepokea “mamlaka juu ya wote wenye mwili,” Yesu anaweza kuwaletea wanadamu wote faida za fidia. Ingawa hivyo, ni wachache tu watakaopata baraka hiyo. Kwa nini ni wachache? Kwa sababu Yesu atawaletea baraka za fidia wale tu wanaotenda kulingana na jambo ambalo sasa Yesu anataja: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.
Lazima mtu amjue Baba na Mwana kwa undani, na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja nao. Anapaswa kuwa na maoni kama yao. Isitoshe, anapaswa kujitahidi kuiga sifa zao zisizo na kifani anaposhughulika na wengine. Anapaswa kuelewa kwamba jambo muhimu zaidi ni kutukuzwa kwa jina la Mungu, kisha jambo la pili ni wanadamu kupata uzima wa milele. Sasa Yesu anaendelea na mazungumzo yake.
“Nimekutukuza duniani, kwa kuwa nimemaliza kazi uliyonipa nifanye. Sasa Baba, nitukuze kando yako kwa utukufu niliokuwa nao kando yako kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:4, 5) Naam, Yesu anaomba kurudishwa katika utukufu wa mbinguni kupitia ufufuo.
Hata hivyo, Yesu hasahau mambo ambayo ametimiza katika huduma yake. Anasali hivi: “Nimelifunua jina lako kwa watu ulionipa kutoka ulimwenguni. Walikuwa wako, nawe ukanipa, nao wamelishika neno lako.” (Yohana 17:6) Katika huduma yake, Yesu alifanya mengi zaidi ya kulitamka tu jina la Mungu, Yehova. Aliwasaidia mitume wake waelewe kile kinachowakilishwa na jina hilo, yaani, sifa za Mungu na jinsi anavyoshughulika na wanadamu.
Mitume wamemjua Yehova, jukumu la Mwana wake, na mambo ambayo Yesu amefundisha. Yesu anasema hivi kwa unyenyekevu: “Nimewapa maneno uliyonipa, nao wameyakubali na kwa hakika wamejua kwamba nilikuja nikiwa mwakilishi wako, nao wameamini kwamba ulinituma.”—Yohana 17:8.
Kisha Yesu anataja tofauti kati ya wafuasi wake na ulimwengu wa wanadamu kwa ujumla: “Siombi kwa ajili ya ulimwengu, bali ninawaombea wale ulionipa, kwa sababu ni wako . . . Baba Mtakatifu, walinde kwa sababu ya jina lako ambalo umenipa, ili wawe kitu kimoja kama vile sisi tulivyo kitu kimoja. . . . Nimewalinda na hakuna hata mmoja wao aliyeangamizwa ila yule mwana wa maangamizi,” yaani, Yuda Iskariote, ambaye anaendelea na mipango ya kumsaliti Yesu.—Yohana 17:9-12.
“Ulimwengu umewachukia,” Yesu anaendelea kusali. “Sikuombi uwatoe ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14-16) Mitume na wanafunzi wengine wako ulimwenguni, yaani, jamii ya wanadamu inayotawaliwa na Shetani, lakini wanapaswa kujitenga na ulimwengu na uovu wake. Jinsi gani?
Wanapaswa kuendelea kuwa watakatifu, wakiwa wametengwa kwa ajili ya kumtumikia Mungu, kwa kufuata kweli zilizo katika Maandiko ya Kiebrania na kweli ambazo Yesu mwenyewe amefundisha. Yesu anasali hivi: “Watakase kupitia ile kweli; neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Baada ya muda, baadhi ya mitume wataandika vitabu vilivyoongozwa na roho ya Mungu ambavyo vitakuwa sehemu ya “kweli” inayoweza kumtakasa mtu.
Lakini baadaye kuna wengine ambao watakubali “kweli.” Basi Yesu anasali “si kwa ajili ya Hawa tu [yaani, wale walio hapo], bali pia wale [wanaomwamini] kupitia neno lao.” Yesu anaomba nini kwa ajili yao wote? “Wawe kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe Baba umo katika muungano nami, nami nimo katika muungano nawe, ili wao pia wawe katika muungano nasi.” (Yohana 17:20, 21) Kihalisi, Yesu na Baba yake si mtu mmoja. Wao ni kitu kimoja katika maana ya kwamba wanakubaliana katika mambo yote. Yesu anasali kwamba wafuasi wake wafurahie umoja huo.
Muda mfupi kabla ya hapo, Yesu alikuwa amemwambia Petro na wenzake kwamba alikuwa anaenda kuwatayarishia mahali, akimaanisha huko mbinguni. (Yohana 14:2, 3) Sasa Yesu anataja jambo hilo katika sala: “Baba, ninataka wale ambao umenipa wawe pamoja nami mahali nilipo, ili waone utukufu wangu ambao umenipa, kwa sababu ulinipenda kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu.” (Yohana 17:24) Kwa hiyo, anathibitisha kwamba zamani za kale—kabla Adamu na hawa hawajazaa watoto—Mungu alimpenda mwana wake mzaliwa wa pekee, ambaye alikuja kuwa Yesu Kristo.
Yesu anamalizia sala yake kwa kusisitiza jina la Baba yake na upendo wa Mungu kwa mitume na kwa wengine ambao watakubali ile “kweli,” anaposema: “Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda uwe ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”—Yohana 17:26.
-
-
Yesu Anasali Akiwa na Huzuni NyingiYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 123
Yesu Anasali Akiwa na Huzuni Nyingi
MATHAYO 26:30, 36-46 MARKO 14:26, 32-42 LUKA 22:39-46 YOHANA 18:1
YESU KATIKA BUSTANI YA GETHSEMANE
JASHO LAKE NI KAMA MATONE YA DAMU
Yesu anamaliza kusali akiwa na mitume wake waaminifu. Kisha ‘baada ya kuimba sifa, wanaenda kwenye Mlima wa Mizeituni.’ (Marko 14:26) Wanaelekea upande wa mashariki kwenye bustani inayoitwa Gethsemane, ambako Yesu amezoea kwenda.
Baada ya kufika kwenye sehemu hiyo maridadi yenye miti ya mizeituni, Yesu anawaacha nyuma mitume wanane. Labda wanabaki karibu na mwingilio wa bustani hiyo, kwa maana anawaambia hivi: “Ketini hapa, mimi naenda pale kusali.” Yesu anaenda na mitume watatu—Petro, Yakobo, na Yohana—anaingia ndani zaidi katika bustani. Anahuzunika sana na kuwaambia hivi wale mitume watatu: “Nimehuzunika sana, kiasi cha kufa. Kaeni hapa na mwendelee kukesha pamoja nami.”—Mathayo 26:36-38.
Yesu anasonga mbali kidogo, kisha ‘anaanguka chini na kuanza kusali.’ Anamwomba nini Mungu katika kipindi hiki kigumu? Anasali hivi: “Baba, mambo yote yanawezekana kwako; niondolee kikombe hiki. Lakini si kama ninavyotaka, bali unavyotaka.” (Marko 14:35, 36) Anamaanisha nini? Je, anakimbia jukumu lake la kutoa fidia? Hapana!
Akiwa mbinguni, Yesu alijionea jinsi Waroma walivyowatesa sana watu na kuwaua. Sasa akiwa mwanadamu, aliye na hisia nyororo na anayeweza kuhisi uchungu, Yesu anaogopa jambo litakalompata. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ni kuwa anahuzunika kwa sababu anahisi kwamba akifa kama mhalifu anaweza kuliletea suto jina la Baba yake. Baada ya saa chache, atatundikwa kwenye mti kama mtu aliyemkufuru Mungu.
Baada ya kusali kwa muda mrefu, Yesu anarudi na kuwakuta wale mitume watatu wakiwa wamelala usingizi. Anamwambia hivi Petro: “Je, hamngeweza kukesha pamoja nami hata kwa saa moja? Endeleeni kukesha na kusali bila kuacha, ili msiingie katika majaribu.” Yesu anatambua kwamba mitume pia wamekuwa na mkazo, na muda umesonga sana. Anaongezea hivi: “Bila shaka, roho inataka lakini mwili ni dhaifu.”—Mathayo 26:40, 41.
Kisha Yesu anaondoka kwa mara ya pili na kumwomba Mungu amwondolee “kikombe hiki.” Anaporudi, anawakuta tena wale mitume watatu wakiwa wamelala, ingawa wanapaswa kuwa wakisali kwamba wasiingie katika majaribu. Yesu anapozungumza nao, ‘hawajui la kumjibu.’ (Marko 14:40) Yesu anaondoka mara ya tatu, kisha anapiga magoti na kusali.
Yesu anahangaishwa sana na jinsi kifo chake kama mhalifu kitakavyoliletea suto jina la Baba yake. Ingawa hivyo, Yehova anasikiliza sala ya Mwana wake, na pindi moja Mungu anamtuma malaika ili amtie nguvu. Hata hivyo, Yesu haachi kumsihi Baba yake, bali anaendelea “kusali kwa bidii zaidi.” Ana mkazo mwingi sana wa kihisia. Yesu amebeba jukumu zito sana! Uhai wake mwenyewe wa milele na uhai wa wanadamu wenye imani unahusika. Hata ‘jasho lake linakuwa kama matone ya damu yakidondoka chini.’—Luka 22:44.
Yesu anaporudi kwa mitume wake mara ya tatu, anawakuta tena wakiwa wamelala usingizi. Anawaambia hivi: “Mnalala na kupumzika wakati kama huu! Tazama! Saa imekaribia ya Mwana wa binadamu kusalitiwa mikononi mwa watenda dhambi. Simameni twende. Tazama! Msaliti wangu amekaribia.”—Mathayo 26:45, 46.
-
-
Kristo Asalitiwa na KukamatwaYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 124
Kristo Asalitiwa na Kukamatwa
MATHAYO 26:47-56 MARKO 14:43-52 LUKA 22:47-53 YOHANA 18:2-12
YUDA AMSALITI YESU KATIKA BUSTANI
PETRO AMKATA MTU SIKIO
YESU AKAMATWA
Ni usiku wa manane. Makuhani wamekubali kumlipa Yuda vipande 30 vya fedha ili amsaliti Yesu. Basi Yuda anaongoza kundi kubwa la wakuu wa makuhani na Mafarisayo kwenda kumtafuta Yesu. Wako pamoja na kikundi cha wanajeshi Waroma walio na silaha na kamanda wa jeshi.
Inaonekana Yesu alipomwambia Yuda aondoke kwenye mlo wa Pasaka, alienda moja kwa moja kwa wakuu wa makuhani. (Yohana 13:27) Waliwakusanya maofisa wao na kikundi cha wanajeshi. Huenda Yuda aliwapeleka kwanza kwenye chumba ambacho Yesu na mitume wake walisherehekea Pasaka. Lakini sasa kundi hilo limevuka Bonde la Kidroni na wanaelekea kwenye bustani. Mbali na silaha, wamebeba mienge na taa, wakiwa wameazimia kumpata Yesu.
Yuda anapoongoza kundi hilo kupanda Mlima wa Mizeituni, ana uhakika kwamba anajua mahali atakapompata Yesu. Katika juma lililotangulia, Yesu na mitume wake walipokuwa wakienda Yerusalemu na kurudi Bethania, mara kwa mara walisimama katika bustani ya Gethsemane. Lakini sasa ni usiku, na huenda Yesu amefichwa na kivuli cha mizeituni iliyo katika bustani. Basi, wanajeshi ambao huenda hawajawahi kumwona Yesu, watamtambuaje? Yuda atawapa ishara ili kuwasaidia. Anasema hivi: “Yule nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni na kuondoka naye akiwa chini ya ulinzi.”—Marko 14:44.
Yuda anaongoza kundi hilo kuingia katika bustani, kisha anamwona Yesu na mitume wake naye anamwendea moja kwa moja. Yuda anasema: “Salamu, Rabi!” Kisha anambusu kwa wororo. Yesu anamuuliza: “Mwenzangu, umekuja kufanya nini?” (Mathayo 26:49, 50) Yesu anajibu swali alilouliza kwa kusema: “Yuda, unamsaliti Mwana wa binadamu kwa busu?” (Luka 22:48) Lakini Yesu haendelei na mazungumzo hayo!
Sasa Yesu anakuja kwenye mwangaza wa zile taa na mienge na kuuliza: “Mnamtafuta nani?” Umati unamjibu: “Yesu Mnazareti.” Kwa ujasiri Yesu anasema: “Ni mimi.” (Yohana 18:4, 5) Bila kujua jambo litakalotokea, wanaume hao wanaanguka chini.
Badala ya kutumia fursa hiyo kukimbilia gizani, Yesu anawauliza tena wanamtafuta nani. Wanaposema tena, “Yesu Mnazareti,” anasema hivi kwa utulivu: “Niliwaambia ni mimi. Basi, ikiwa mnanitafuta mimi, waacheni wanaume hawa waende.” Hata katika kipindi hiki kigumu, Yesu anakumbuka jambo alilosema mapema, kwamba hatampoteza hata mmoja. (Yohana 6:39; 17:12) Yesu amekuwa pamoja na mitume wake waaminifu na hajampoteza hata mmoja, isipokuwa “mwana wa maangamizi”—Yuda. (Yohana 18:7-9) Basi, sasa anaomba wafuasi wake washikamanifu waachwe waende.
Wanajeshi wanaposimama na kumkaribia Yesu, mitume wanatambua jambo linaloendelea. Wanauliza: “Bwana, tuwashambulie kwa upanga?” (Luka 22:49) Kabla Yesu hajajibu, Petro anachukua upanga mmoja kati ya panga mbili walizo nazo mitume. Anamshambulia Malko, mtumwa wa kuhani mkuu, na kulikata sikio lake la kulia.
Yesu analigusa sikio la Malko, na kuponya kidonda hicho. Kisha anafundisha somo muhimu, anamwamuru hivi Petro: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wote wanaochukua upanga wataangamia kwa upanga.” Yesu yuko tayari kukamatwa, kwa kuwa anauliza hivi: “Maandiko yanayosema lazima itendeke hivi yatatimizwaje?” (Mathayo 26:52, 54) Kisha anaongezea hivi: “Je, sipaswi kukinywa kikombe ambacho Baba amenipa?” (Yohana 18:11) Yesu anakubaliana na mapenzi ya Mungu kwake, hata kufikia hatua ya kufa.
Yesu anauliza umati hivi: “Je, mmekuja kunikamata mkiwa na mapanga na marungu kana kwamba mimi ni mwizi? Siku baada ya siku nilikuwa nikiketi hekaluni nikifundisha lakini hamkunikamata. Lakini yote haya yametokea ili kutimiza mambo yaliyoandikwa na manabii.”—Mathayo 26:55, 56.
Kikosi cha wanajeshi, kamanda wa jeshi, na maofisa wa Wayahudi wanamkamata Yesu na kumfunga. Mitume wanapoona hivyo, wanakimbia. Hata hivyo, “kijana fulani”—labda ni mwanafunzi Marko—anabaki katika umati ili kumfuata Yesu. (Marko 14:51) Umati unamtambua kijana huyo, nao wanajaribu kumkamata, analazimika kuacha vazi lake la kitani na kukimbia.
-
-
Yesu Apelekwa kwa Anasi, Kisha kwa KayafaYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 125
Yesu Apelekwa kwa Anasi, Kisha kwa Kayafa
MATHAYO 26:57-68 MARKO 14:53-65 LUKA 22:54, 63-65 YOHANA 18:13, 14, 19-24
YESU APELEKWA KWA KUHANI MKUU WA ZAMANI ANASI
SANHEDRINI YAFANYA KESI ISIYO HALALI
Baada ya Yesu kufungwa kama mhalifu, anapelekwa kwa Anasi, ambaye alikuwa kuhani mkuu wakati mvulana Yesu alipowashangaza walimu hekaluni. (Luka 2:42, 47) Baadaye, baadhi ya wana wa Anasi walitumikia wakiwa wakuu wa makuhani, lakini sasa mkwe wake, Kayafa, ndiye aliye na cheo hicho.
Yesu akiwa nyumbani kwa Anasi, Kayafa anapata muda wa kuwakusanya washiriki wa Sanhedrini. Mahakama hiyo yenye washiriki 71 inatia ndani kuhani mkuu na wengine waliowahi kuwa na cheo hicho.
Anasi anamhoji Yesu “kuhusu wanafunzi wake na kuhusu mafundisho yake.” Yesu anamjibu hivi: “Nimezungumza na ulimwengu hadharani. Sikuzote nilifundisha katika sinagogi na hekaluni, ambapo Wayahudi wote hukusanyika, nami sikusema jambo lolote kwa siri. Kwa nini unaniuliza? Waulize wale waliosikia nilichowaambia.”—Yohana 18:19-21.
Ofisa aliyesimama hapo karibu anampiga Yesu kofi usoni na kumkemea hivi: “Je, hivyo ndivyo unavyomjibu mkuu wa makuhani?” Lakini Yesu akijua kwamba hajafanya kosa, anajibu hivi: “Ikiwa nimesema vibaya, toa ushahidi kuhusu kosa hilo; lakini ikiwa nimesema jambo lililo sawa, kwa nini unanipiga?” (Yohana 18:22, 23) Kisha Anasi anaagiza Yesu apelekwe kwa mkwe wake, Kayafa.
Kufikia sasa washiriki wote wa Sanhedrini—kuhani mkuu wa sasa, wazee wa watu, na waandishi—wamekusanyika. Wamekutana nyumbani kwa Kayafa. Si halali kufanya kesi kama hiyo usiku wa Pasaka, lakini jambo hilo haliwazuii kutimiza kusudi lao baya.
Hiki ni kikundi kisichofuata haki. Baada ya Yesu kumfufua Lazaro, Sanhedrini iliamua kwamba Yesu anapaswa kuuawa. (Yohana 11:47-53) Na siku chache zilizopita, viongozi wa kidini walipanga njama ya kumkamata Yesu na kumuua. (Mathayo 26:3, 4) Naam, hata kabla kesi yake haijaanza, tayari Yesu amehukumiwa kifo!
Zaidi ya kufanya mkutano usio halali, kuhani mkuu na washiriki wengine wa Sanhedrini wanatafuta mashahidi watakaotoa ushahidi wa uwongo katika kesi ya Yesu. Wanawapata wengi, lakini ushahidi wao unatofautiana. Mwishowe, wawili wanajitokeza na kusema: “Tulimsikia akisema, ‘Nitaliangusha chini hekalu hili lililojengwa kwa mikono, na kwa siku tatu nitajenga lingine ambalo halijajengwa kwa mikono.’” (Marko 14:58) Hata hivyo, bado watu hao hawakubaliani kabisa.
Kayafa anamuuliza hivi Yesu: “Kwa nini hujibu? Watu hawa wanashuhudia nini kukuhusu?” (Marko 14:60) Yesu anakaa kimya anapokabili mashtaka hayo ya uwongo kutoka kwa mashahidi ambao mashtaka yao yanatofautiana. Basi Kuhani Mkuu Kayafa anatumia mbinu nyingine.
Kayafa anajua kwamba Wayahudi hawakubaliani na mtu yeyote anayedai kuwa Mwana wa Mungu. Hapo awali, Yesu alipomwita Mungu Baba yake, Wayahudi walitaka kumuua kwa sababu walidai kwamba alikuwa “akijifanya kuwa sawa na Mungu.” (Yohana 5:17, 18; 10:31-39) Kayafa anajua jambo hilo, basi kwa ujanja anamwamuru Yesu hivi: “Ninakuapisha mbele za Mungu aliye hai utuambie kama wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu!” (Mathayo 26:63) Bila shaka, Yesu alisema kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. (Yohana 3:18; 5:25; 11:4) Asipofanya hivyo sasa, hilo linaweza kuonyesha kwamba anakana kuwa yeye ni Mwana wa Mungu na kwamba ndiye Kristo. Basi Yesu anasema: “Mimi ndiye; nanyi mtamwona Mwana wa binadamu akiwa ameketi kwenye mkono wa kuume wa nguvu, akija pamoja na mawingu ya mbinguni.”—Marko 14:62.
Papo hapo, Kayafa anayararua mavazi yake na kusema: “Amekufuru! Tunahitaji mashahidi wengine wa nini? Tazama! Sasa mmemsikia akikufuru. Mnaonaje?” Sanhedrini inatoa hukumu hii isiyo ya haki: “Anastahili kufa.”—Mathayo 26:65, 66.
Kisha wanaanza kumdhihaki Yesu na kumpiga ngumi. Wengine wanampiga makofi usoni na kumtemea mate usoni. Baada ya kuufunika uso wake na kumpiga makofi, wanamdhihaki hivi: “Toa unabii! Ni nani aliyekupiga?” (Luka 22:64) Huyu ni Mwana wa Mungu anayetendewa vibaya katika kesi isiyo halali inayofanywa usiku!
-
-
Akanwa Nyumbani kwa KayafaYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 126
Akanwa Nyumbani kwa Kayafa
MATHAYO 26:69-75 MARKO 14:66-72 LUKA 22:54-62 YOHANA 18:15-18, 25-27
PETRO AMKANA YESU
Yesu anapokamatwa katika bustani ya Gethsemane, mitume wanamwacha na kukimbia kwa woga. Hata hivyo, wawili kati yao wanaacha kukimbia. Nao ni Petro “na mwanafunzi mwingine,” labda ni mtume Yohana. (Yohana 18:15; 19:35; 21:24) Wanaweza kumfikia Yesu atakapopelekwa nyumbani kwa Anasi. Anasi anapoagiza Yesu apelekwe kwa Kuhani Mkuu Kayafa, Petro na Yohana wanafuata kwa mbali. Huenda wanahangaika kwa sababu wanahofia uhai wao wenyewe na kile kitakachompata Bwana wao.
Yohana anafahamiana na kuhani mkuu, kwa hiyo anaingia katika ua wa nyumba ya Kayafa. Petro anabaki mlangoni hadi Yohana anaporudi kuzungumza na kijakazi anayelinda mlango. Kisha Petro anaruhusiwa kuingia.
Usiku huo kuna baridi, kwa hiyo wale walio ndani ya ua wamewasha moto wa makaa. Petro anakaa pamoja nao ili aote moto anaposubiri ‘kuona’ matokeo ya kesi ya Yesu. (Mathayo 26:58) Sasa kwa sababu ya mwangaza wa moto, yule mlinzi wa mlango aliyemruhusu Petro aingie anamwona vizuri. “Wewe pia ni mmoja wa wanafunzi wa mtu huyu, sivyo?” anauliza. (Yohana 18:17) Si msichana huyo peke yake anayemtambua Petro na kudai kwamba alikuwa pamoja na Yesu.—Mathayo 26:69, 71-73; Marko 14:70.
Jambo hilo linamshtua Petro. Anajaribu kujificha, hata anaondoka na kwenda mlangoni. Basi Petro anakana kwamba alikuwa pamoja na Yesu, pindi fulani anasema: “Simjui wala sielewi unachosema.” (Marko 14:67, 68) Pia anaanza “kulaani na kuapa,” akimaanisha kwamba yuko tayari kuapa kwamba anasema ukweli na kuadhibiwa ikiwa anadanganya.—Mathayo 26:74.
Wakati huohuo, kesi ya Yesu inaendelea, labda katika sehemu fulani ya nyumba ya Kayafa iliyo juu ya ua. Petro na wengine wanaosubiri chini wanaweza kuwaona mashahidi mbalimbali wakiingia na kutoka ili kutoa ushahidi.
Petro anapomkana Yesu, matamshi yake ya Kigalilaya yanaonyesha kwamba anadanganya. Isitoshe, mtu fulani katika kikundi hicho ni mtu wa ukoo wa Malko, ambaye alikatwa sikio na Petro. Basi anamuuliza hivi Petro: “Nilikuona katika bustani pamoja naye, sivyo?” Petro anapokana mara hii ya tatu, jogoo anawika, kama ilivyotabiriwa.—Yohana 13:38; 18:26, 27.
Wakati huo, huenda Yesu yuko ghorofani akitazama uani. Bwana anageuka na kumtazama Petro moja kwa moja, jambo ambalo lazima linamuumiza sana Petro. Anakumbuka jambo ambalo Yesu alisema saa chache tu awali walipokuwa katika chumba cha juu. Wazia jinsi Petro anavyohisi anapotambua kile alichofanya! Petro anaenda nje na kuanza kulia kwa uchungu.—Luka 22:61, 62.
Jambo hilo linawezekanaje? Petro ambaye alikuwa na uhakika kwamba ni mshikamanifu na yuko imara kiroho, angewezaje kumkana Bwana wake? Watu wanapotosha ukweli, na Yesu anahukumiwa kuwa mhalifu mbaya. Ingawa Petro angemtetea mtu huyo asiye na hatia, alimkana Yule aliye na “maneno ya uzima wa milele.”—Yohana 6:68.
Jambo hilo la kuhuzunisha lililompata Petro linaonyesha kwamba hata mtu mwenye imani na aliyejitoa kabisa anaweza kuanguka ikiwa hajajitayarisha vizuri kwa ajili ya majaribu au vishawishi visivyotarajiwa. Mambo yote yaliyompata Petro yanapaswa kuwa onyo kwa watumishi wote wa Mungu!
-