-
Kaburi Tupu—Yesu Yuko Hai!Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 134
Kaburi Tupu—Yesu Yuko Hai!
MATHAYO 28:3-15 MARKO 16:5-8 LUKA 24:4-12 YOHANA 20:2-18
YESU AFUFULIWA
MATUKIO KWENYE KABURI LA YESU
AWATOKEA WANAWAKE KADHAA
Wale wanawake wanashtuka sana wanapokuta kaburi likiwa tupu! Maria Magdalene anakimbia kwenda kwa “Simoni Petro na yule mwanafunzi mwingine, ambaye Yesu alimpenda,” yaani, mtume Yohana. (Yohana 20:2) Hata hivyo, wale wanawake wengine walio kwenye kaburi wanamwona malaika. Na ndani ya kaburi kuna malaika mwingine, ambaye “amevaa kanzu nyeupe.”—Marko 16:5.
Mmoja wa wale malaika anawaambia hivi: “Msiogope, kwa maana ninajua mnamtafuta Yesu aliyeuawa kwenye mti. Hayupo hapa, kwa maana amefufuliwa kama alivyosema. Njooni, tazameni mahali alipokuwa amelala. Basi nendeni upesi mkawaambie wanafunzi wake kwamba alifufuliwa kutoka kwa wafu, na tazama! anawatangulia kwenda Galilaya.” (Mathayo 28:5-7) Basi wale wanawake “wakitetemeka huku wakiwa wamelemewa na hisia,” wanakimbia kwenda kuwajulisha wanafunzi.—Marko 16:8.
Kufikia sasa, Maria amewapata Petro na Yohana. Akiwa anahema, anawaambia: “Wamemwondoa Bwana kaburini, nasi hatujui wamemlaza wapi.” (Yohana 20:2) Petro na Yohana wanaondoka mbio. Yohana anakimbia haraka zaidi naye anafika kwenye kaburi kwanza. Anachungulia ndani na kuviona vitambaa, lakini haingii ndani.
Petro anapofika, anaingia ndani moja kwa moja. Anaona vitambaa vya kitani na kitambaa kilichotumiwa kufunga kichwa cha Yesu. Sasa Yohana anaingia ndani naye anaamini ripoti ya Maria. Licha ya mambo ambayo Yesu alikuwa amesema, hakuna yeyote kati yao anayetambua kwamba amefufuliwa. (Mathayo 16:21) Wanarudi nyumbani wakiwa wamechanganyikiwa. Lakini Maria, ambaye amerudi kwenye kaburi, anabaki hapo.
Wakati huohuo, wale wanawake wengine wako njiani kwenda kuwajulisha wanafunzi kwamba Yesu amefufuliwa. Wakiwa wanakimbia kwenda kuwajulisha, Yesu anakutana nao na kusema: “Siku njema!” Wanaanguka miguuni pake na “kumsujudia.” Kisha Yesu anasema: “Msiogope! Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu ili waende Galilaya, na huko wataniona.”—Mathayo 28:9, 10.
Hapo awali, kulipokuwa na tetemeko la ardhi na malaika wakatokea, wanajeshi waliokuwa kaburini ‘walitetemeka, wakawa kama wafu.’ Baada ya kurudiwa na nguvu, waliingia jijini na “kuwajulisha wakuu wa makuhani mambo yote yaliyotokea.” Kisha makuhani wakashauriana na wazee wa Wayahudi. Wakaamua kuwahonga wanajeshi hao ili wafiche jambo hilo na waseme: “Wanafunzi wake walikuja usiku wakamwiba tulipokuwa tumelala usingizi.”—Mathayo 28:4, 11, 13.
Wanajeshi Waroma wanaweza kuuawa ikiwa watalala wanapolinda, basi makuhani wanawaahidi hivi: “Na gavana akisikia [uwongo wao kwamba walikuwa wamelala], sisi tutamwelezea jambo hilo, nanyi hamtahitaji kuwa na wasiwasi.” (Mathayo 28:14) Wanajeshi wanachukua hongo na kufanya kama wanavyoambiwa na makuhani. Basi habari za uwongo kwamba mwili wa Yesu uliibiwa zinaenea sana kati ya Wayahudi.
Bado Maria Magdalene anaomboleza kaburini. Anapoinama na kuchungulia ndani ya kaburi, anawaona malaika wawili wakiwa wamevaa mavazi meupe! Mmoja ameketi mahali ambapo kichwa cha Yesu kilikuwa kimelazwa na mwingine miguuni. Wanamuuliza: “Mwanamke, kwa nini unalia?” Maria anawajibu: “Wamemwondoa Bwana wangu, nami sijui wamemlaza wapi.” Maria anapogeuka anamwona mtu mwingine. Mtu huyo anarudia swali walilouliza malaika na kuongezea hivi: “Unamtafuta nani?” Akifikiri kwamba ni mtunza-bustani, Maria anasema: “Bwana, ikiwa umemchukua, niambie umemlaza wapi, nami nitamwondoa.”—Yohana 20:13-15.
Kwa kweli, Maria anazungumza na Yesu aliyefufuliwa, lakini pindi hiyo hamtambui. Hata hivyo, Yesu anaposema, “Maria!” anamtambua kupitia njia ambayo amekuwa akizungumza naye. Maria anasema hivi kwa shangwe: “Raboni!” (maana yake “Mwalimu!”) Lakini akiogopa kwamba Yesu yuko karibu kupaa mbinguni, Maria anamshika. Basi Yesu anamwambia hivi: “Acha kuning’ang’ania, kwa maana bado sijapanda kwenda kwa Baba. Lakini nenda kwa ndugu zangu, nawe uwaambie, ‘Ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu.’”—Yohana 20:16, 17.
Maria anakimbia kwenda mahali ambapo mitume na wale wanafunzi wengine wamekusanyika. Anawaambia hivi: “Nimemwona Bwana!” na hivyo kuongezea simulizi lake kwenye mambo ambayo wamesikia kutoka kwa wale wanawake wengine. (Yohana 20:18) Ingawa hivyo, ‘wanayaona maneno hayo kama upuuzi.’—Luka 24:11.
-
-
Yesu Aliyefufuliwa Awatokea WengiYesu—Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 135
Yesu Aliyefufuliwa Awatokea Wengi
YESU ATOKEA BARABARANI KUELEKEA EMAU
AWAFUNGULIA WANAFUNZI WAKE MAANDIKO TENA NA TENA
TOMASI AACHA KUWA NA SHAKA
Siku ya Jumapili, Nisani 16, wanafunzi wameshuka moyo. Hawaelewi kwa nini kaburi liko tupu. (Mathayo 28:9, 10; Luka 24:11) Baadaye siku hiyo, Kleopa na mwanafunzi mwingine wanaondoka Yerusalemu kwenda Emau, umbali wa kilomita 11 hivi.
Wakiwa wanatembea, wanazungumzia jambo lililotokea. Kisha mtu fulani anajiunga nao. Anawauliza “Ni mambo gani haya mnayojadiliana huku mkitembea?” Kleopa anajibu: “Je, wewe ni mgeni anayekaa peke yake Yerusalemu hivi kwamba hujui mambo ambayo yametukia huko siku hizi?” Yule mtu anawauliza: “Mambo gani?”—Luka 24:17-19.
“Kuhusu Yesu Mnazareti,” wanasema. “Tulitazamia kwamba yeye ndiye angekomboa Israeli.”—Luka 24:19-21.
Kisha Kleopa na mwenzake wanasimulia mambo yaliyotokea siku hiyo. Wanasema kwamba wanawake fulani walioenda kwenye kaburi ambalo Yesu alizikwa walililipata likiwa tupu na kwamba wanawake hao walijionea mambo ya ajabu—malaika walitokea na kusema kwamba Yesu yuko hai. Wanasimulia kwamba watu wengine walienda kwenye kaburi nao “wakalikuta kama vile wale wanawake walivyosema.”—Luka 24:24.
Ni wazi kwamba wanafunzi hao wawili wamechanganyikiwa na hawajui maana ya jambo lililotokea. Yule mtu anawajibu kwa mamlaka ili kurekebisha maoni yao yasiyo sahihi, ambayo yanaathiri mioyo yao: “Enyi wasio na akili na wagumu kuamini mambo yote yaliyosemwa na manabii! Je, haikuwa lazima Kristo kupatwa na mateso haya kisha aingie kwenye utukufu wake?” (Luka 24:25, 26) Kisha anawafafanulia masimulizi mengi ya Maandiko yanayomhusu Kristo.
Mwishowe watu hao watatu wanakaribia kufika Emau. Wale wanafunzi wawili wanataka kusikia mengi zaidi, basi wanamsihi yule mtu hivi: “Kaa pamoja nasi, kwa sababu ni jioni, na siku inakaribia kwisha.” Anakubali kukaa, nao wanakula chakula. Yule mtu anaposali, na kuumega mkate, na kisha kuwapa, wanamtambua, lakini anatoweka. (Luka 24:29-31) Sasa wanajua kwa uhakika kwamba Yesu yuko hai!
Wale wanafunzi wawili wanasema kwa msisimko jinsi walivyohisi: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akizungumza nasi barabarani, na alipokuwa akitufungulia Maandiko waziwazi?” (Luka 24:32) Wanarudi haraka Yerusalemu, ambako wanawakuta mitume na watu wengine wakiwa pamoja nao. Kabla Kleopa na mwenzake hawajasimulia mambo waliyoona, wanasikia wengine wakisema: “Kwa kweli Bwana alifufuliwa naye alimtokea Simoni!” (Luka 24:34) Kisha wale wawili wanasimulia jinsi Yesu alivyowatokea. Naam, wao pia ni mashahidi wa kujionea.
Sasa wote wanashtuka—Yesu anatokea ghafla chumbani! Hawaamini jambo hilo kwa sababu walikuwa wamefunga milango kwa kuwaogopa Wayahudi. Hata hivyo, Yesu amesimama hapo katikati yao. Anasema hivi kwa utulivu: “Na muwe na amani.” Lakini wanaogopa. Kama walivyofanya hapo awali, ‘wanadhani kwamba wanaona roho.’—Luka 24:36, 37; Mathayo 14:25-27.
Ili kuthibitisha kwamba yeye si mzuka au jambo la kuwaziwa, na kwamba ana mwili wa nyama, Yesu anawaonyesha mikono na miguu yake na kusema: “Kwa nini mnahangaika, na kwa nini mna shaka mioyoni mwenu? Angalieni mikono na miguu yangu, kwamba ni mimi; niguseni mwone, kwa maana roho haina nyama na mifupa kama vile mnavyoona nilivyo.” (Luka 24:36-39) Wanashangilia sana na kushangaa lakini bado hawaamini.
Akijaribu tena kuwasaidia waamini kwamba kwa kweli ni yeye, anawauliza: “Mna chakula chochote hapa?” Wanampa kipande cha samaki wa kuchomwa, naye anakula. Kisha anasema: “Haya ndiyo maneno niliyowaambia nilipokuwa bado pamoja nanyi [kabla ya kifo changu], kwamba mambo yote yaliyoandikwa kunihusu katika Sheria ya Musa, Manabii, na Zaburi lazima yatimizwe.”—Luka 24:41-44.
Yesu alikuwa amemsaidia Kleopa na mwenzake waelewe Maandiko, na sasa anafanya hivyo kwa wote waliokusanyika: “Imeandikwa kwamba Kristo atateseka na kufufuliwa kutoka kwa wafu siku ya tatu, na kwa msingi wa jina lake, toba kwa msamaha wa dhambi ingehubiriwa katika mataifa yote—kuanzia Yerusalemu. Ninyi mtakuwa mashahidi wa mambo haya.”—Luka 24:46-48.
Kwa sababu zisizojulikana, mtume Tomasi hayupo. Siku zinazofuata, wengine wanamwambia hivi kwa shangwe: “Tumemwona Bwana.” Tomasi anajibu hivi: “Nisipoona alama za misumari kwenye mikono yake na kutia kidole changu katika alama hizo kisha niutie mkono wangu ubavuni mwake, sitaamini kamwe.”—Yohana 20:25.
Siku nane baadaye, wanafunzi wanakutana tena katika chumba wakiwa wamefunga milango, lakini pindi hii Tomasi yupo. Yesu anatokea katikati yao akiwa na mwili wa binadamu na kuwasalimia: “Na muwe na amani.” Yesu anamgeukia Tomasi na kusema: “Weka kidole chako hapa, uone mikono yangu, na ulete mkono wako uguse ubavu wangu, ili uache kuwa na shaka bali uamini.” Tomasi anasema hivi kwa mshangao: “Bwana wangu na Mungu wangu!” (Yohana 20:26-28) Naam, sasa hana shaka kwamba Yesu yuko hai akiwa na mwili wa kiroho na kwamba ni mwakilishi wa Yehova Mungu.
Yesu anamwambia: “Je, umeamini kwa sababu umeniona? Wenye furaha ni wale ambao wanaamini ingawa bado hawajaona.”—Yohana 20:29.
-