-
Hasira Yasababisha MauajiMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 4
Hasira Yasababisha Mauaji
Baada ya Adamu na Hawa kufukuzwa katika bustani ya Edeni, walizaa watoto wengi. Mtoto wa kwanza aliitwa Kaini, naye alikuwa mkulima, na mtoto wa pili, Abeli, alikuwa mchungaji wa wanyama.
Siku moja Kaini na Abeli walimtolea Yehova dhabihu. Je, unajua dhabihu ni nini? Ni zawadi ya pekee. Yehova alifurahishwa na dhabihu ya Abeli, lakini alichukizwa na dhabihu ya Kaini. Jambo hilo lilimkasirisha sana Kaini. Yehova alimwonya Kaini kwamba hasira ingeweza kusababisha afanye jambo baya. Hata hivyo, Kaini hakusikiliza.
Badala yake Kaini alimwambia Abeli hivi: ‘Twende shambani.’ Walipokuwa peke yao shambani, Kaini alimshambulia ndugu yake na kumuua. Yehova angefanya nini kuhusu jambo hilo? Yehova alimwadhibu Kaini kwa kumfukuza aende mbali na familia yao. Kaini hakuruhusiwa kurudi tena nyumbani.
Tunajifunza nini? Tunajifunza kwamba tunaweza kukasirika mambo yanapoenda kinyume na matarajio yetu. Tunapoona kwamba tumeanza kukasirika—au tunapoonywa na wengine kuhusu hasira—tunapaswa kukubali kurekebishwa na kujitahidi kudhibiti hisia hizo kabla hazijaanza kututawala.
Kwa sababu Abeli alimpenda Yehova na alifanya mambo mema, sikuzote Yehova atamkumbuka. Mungu atamfufua Abeli wakati atakapoifanya dunia kuwa paradiso.
“Kwanza fanya amani na ndugu yako, kisha urudi na kutoa zawadi yako.”—Mathayo 5:24
-
-
Safina ya NoaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 5
Safina ya Noa
Watu walizidi kuongezeka duniani na wengi walikuwa wakifanya mambo mabaya. Hata baadhi ya malaika wa mbinguni wakawa wabaya. Waliacha makao yao huko mbinguni na kuja duniani. Je, unajua ni kwa nini walifanya hivyo? Ili wavae miili ya wanadamu na kujichukulia wanawake.
Malaika walijichukulia wanawake na kuzaa watoto. Watoto hao walikuwa watu wenye nguvu sana na wajeuri. Waliwapiga watu. Yehova hangeruhusu hali hiyo iendelee. Hivyo, aliamua kuwaharibu watu wabaya kupitia gharika.
Lakini kulikuwa na mtu mmoja aliyekuwa tofauti na watu hao. Alimpenda Yehova. Jina lake ni Noa. Alikuwa na mke na watoto watatu, yaani, Shemu, Hamu, na Yafethi, na kila mtoto alikuwa na mke. Yehova alimwambia Noa wajenge safina, ili yeye na familia yake waokoke Gharika. Safina ilikuwa sanduku kubwa lililoelea majini. Pia, Yehova alimwambia Noa awaingize wanyama ndani ya safina ili wao pia waokoke.
Mara moja, Noa alianza kujenga safina. Noa na familia yake walijenga safina kwa karibu miaka 50. Walijenga safina kulingana na maagizo ya Yehova. Katika kipindi hicho, Noa aliwaonya watu kuhusu Gharika. Lakini hakuna mtu aliyemsikiliza.
Hatimaye, muda wa kuingia ndani ya safina ukafika. Acha tuone kile kilichotokea baadaye.
“Kama siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:37
-