-
Abrahamu na Sara Walimtii MunguMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 8
Abrahamu na Sara Walimtii Mungu
Jiji la Uru lilikuwa jirani na mji wa Babeli, ambako watu waliabudu miungu mingine tofauti na Yehova. Lakini kulikuwa na mwanamume mmoja aliyeishi katika jiji la Uru, ambaye alimwabudu Yehova pekee. Mwanamume huyo aliitwa Abrahamu.
Yehova alimwambia Abrahamu hivi: ‘Nenda utoke katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako, mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha.’ Kisha Mungu akamwahidi hivi: ‘Nami nitakufanya uwe taifa kubwa, nitawafanyia watu mambo mazuri katika dunia yote kwa sababu yako.’
Ingawa Abrahamu hakujua mahali alikokuwa akienda, alimtumaini Yehova. Kwa hiyo Abrahamu na Sara mke wake, Tera baba yake, na Loti mpwa wake walitii, wakachukua mizigo yao na kuanza safari ndefu.
Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 75, yeye na familia yake walipofika katika nchi ambayo Yehova alitaka kuwaonyesha. Nchi hiyo iliitwa Kanaani. Mungu alizungumza na Abrahamu na kumwahidi hivi: ‘Nitaupa uzao wako nchi hii.’ Lakini Abrahamu na Sara walikuwa wazee sana na hawakuwa na mtoto. Kwa hiyo Yehova angetimiza ahadi hiyo jinsi gani?
“Kwa imani, Abrahamu . . . alitii kwa kutoka na kwenda mahali ambapo angepokea kuwa urithi; aliondoka, ingawa hakujua mahali alipokuwa akienda.”—Waebrania 11:8
-
-
Hatimaye Wapata Mtoto!Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 9
Hatimaye Wapata Mtoto!
Abrahamu na Sara walikuwa wameoana kwa miaka mingi. Waliacha nyumba yao nzuri huko Uru na sasa walikuwa wakiishi katika mahema. Lakini Sara hakuwa akilalamika kuhusu hali yao, kwa sababu alimtegemea Yehova.
Sara alitamani sana kupata mtoto hivi kwamba alimwambia Abrahamu hivi: ‘Ikiwa mtumishi wangu Hagari atapata mtoto na wewe, mtoto huyo atakuwa kama mwanangu.’ Baada ya muda, Hagari akajifungua mtoto aliyeitwa Ishmaeli.
Miaka mingi baadaye, Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 99 na Sara alipokuwa na miaka 89, walitembelewa na wageni watatu. Abrahamu aliwakaribisha ili wapumzike chini ya kivuli cha mti na kula chakula. Je, unajua wageni hao walikuwa nani? Walikuwa malaika! Walimwambia Abrahamu hivi: ‘Mwaka ujao wakati kama huu, wewe na mke wako mtapata mtoto.’ Sara alikuwa akiwasikiliza katika hema lake. Alicheka na kuwaza hivi: ‘Je, kwa kweli ninaweza kuzaa mtoto nikiwa mzee?’
Mwaka uliofuata, Sara alijifungua mtoto wa kiume, kama ambavyo malaika wa Yehova aliahidi. Abrahamu alimwita mtoto huyo Isaka, jina linalomaanisha “Kicheko.”
Isaka alipokuwa na umri wa miaka mitano hivi, Sara alimwona Ishmaeli akimdhihaki Isaka. Kwa kuwa alitaka kumlinda mtoto wake, alienda kwa Abrahamu na kumwomba awafukuze Hagari na Ishmaeli. Mwanzoni, Abrahamu alikataa. Lakini Yehova alimwambia Abrahamu hivi: ‘Msikilize Sara. Nitamlinda Ishmaeli. Lakini nitatimiza ahadi yangu kupitia Isaka.’
“Kwa imani, Sara pia alipokea nguvu za kupata uzao, . . . kwa kuwa alimwona kuwa mwaminifu Yule aliyekuwa ameahidi.”—Waebrania 11:11
-