Furahia Neno la Mungu
MWENYE furaha ni mtu ‘anayeifurahia sheria ya Yehova.’ Mtu huyo husoma Neno la Mungu “kwa sauti ya chini mchana na usiku.” (Zab. 1:1, 2, NW) Je, wewe una furaha hiyo? Unaweza kuzidishaje shangwe unayopata kutokana na Neno la Mungu?
Sikiliza Yehova Anaposema
Usisome maneno tu. Wazia akilini hali unazosoma. Wazia sauti za wale wanaozungumza. Unaposoma sura za kwanza za Biblia, msikilize Yehova mwenyewe akifunua hatua kwa hatua mambo yanayofanywa ili dunia imfae mwanadamu. Sikiliza anapomwambia Mwana wake, Stadi wa Kazi, kwamba wakati umefika wa kuumba wanadamu wa kwanza. Ebu wazia hali hii: Adamu na Hawa wanaasi, Mungu anawahukumu kisha anawafukuza kutoka katika Paradiso. (Mwanzo, sura ya 1-3) Staajabu unaposoma kwamba sauti kutoka mbinguni inamtambulisha Yesu Kristo kuwa Mwana wa Mungu, mpendwa, yule aliyetumwa na Mungu atoe uhai wake kwa ajili ya wanadamu. (Mt. 3:16, 17) Ebu jaribu kuwazia itikio la mtume Yohana anaposikia Yehova akitangaza hivi: “Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” (Ufu. 21:5) Hakika, inafurahisha sana kusoma Neno la Mungu kwa njia hiyo!
Endelea kusoma maandiko yaliyopuliziwa, na utajua kwamba Yehova ni mwenye utukufu na mwenye kuvutia sana. Utavutiwa sana na Mungu huyu anayetupenda, anayetutendea kwa rehema, anayetusaidia ikiwa tunajaribu kwa unyenyekevu kufanya mapenzi yake, na anayetuonyesha jinsi ya kufanikiwa katika yote tunayofanya.—Yos. 1:8; Zab. 8:1; Isa. 41:10.
Kadiri unavyotumia muda mwingi kusoma Biblia, ndivyo utakavyozidi kupata uradhi unapozidi kujua mapenzi ya Mungu. Lakini furaha yako itazidi hapo. Usomaji unapokusaidia kushughulikia matatizo kwa hekima, utajisikia kama mtunga-zaburi aliyesema: “Shuhuda zako ni za ajabu, ndiyo maana roho yangu imezishika.” (Zab. 119:129) Wewe pia utafurahi sana kufahamu kanuni zilizo katika Maandiko zinazosaidia kufinyanga kufikiri kwako na tamaa zako kwa njia ya kimungu.—Isa. 55:8, 9.
Biblia inaandaa mwongozo wa maadili unaotukinga na madhara na inatuonyesha njia ifaayo. Tunapoisoma, tunang’amua kwamba Yehova ni Baba anayejua matatizo yatakayotokea tukijiachilia tushindwe na tamaa za mwili usiokamilika. Hataki tupate madhara mabaya sana ambayo bila shaka yatatokea tukipuuza kanuni zake bora za maadili. Anatujali na anataka tufurahie njia bora zaidi ya maisha. Kusoma Neno lake kunatusaidia kufahamu zaidi kuwa ni baraka nzuri ajabu kwamba yeye ni Mungu wetu na Baba yetu wa mbinguni.
Soma Biblia Kila Siku
Mtunga-zaburi alisema hivi kuhusu mtu anayesoma Neno la Mungu kila siku: “Kila alitendalo litafanikiwa.” (Zab. 1:3) Ndiyo, japo hatujakamilika, japo tunaishi katika mfumo mwovu wa mambo wa Shetani, na japo jitihada za Ibilisi za kutuangamiza, kusoma na kuyatumia kwa ukawaida yaliyomo katika Neno la Mungu kutafanya tufanikiwe katika mambo yote yanayohusu uhusiano wetu na Yehova.
Kwa sababu tumekazwa sana na mfumo huu, tunaweza kuimarishwa tukichukua hata dakika chache muhimu kila siku kujifunza mawazo ya Muumba. Wengine ambao walifungwa gerezani kwa sababu ya imani yao waliweza kupata tu mstari mmoja-mmoja wa Biblia ulionukuliwa katika magazeti ya habari. Walikata manukuu hayo, wakayashika akilini, na kuyatafakari. Yehova alibariki jitihada zao kwa sababu walifanya kadiri hali zao zilivyoruhusu ili kujua Neno la Mungu. (Mt. 5:3) Lakini, wengi wetu wana uhuru mkubwa zaidi. Tusifikirie kwamba tutatimiza maajabu kwa kusoma haraka-haraka mstari fulani wa Biblia mara moja kwa siku. Lakini tutabarikiwa tukirekebisha hali yetu ili jambo la kwanza liwe ni kusoma sehemu fulani ya Biblia kila siku, kuitafakari, na kuitumia maishani.
Hata mipango bora inaweza kuvurugika. Mipango yetu inapovurugwa, tutangulize mambo muhimu zaidi. Kwa mfano, hatuwezi kukataa kimakusudi kunywa maji kwa siku moja au mbili. Basi hata hali gani itukie katika maisha yetu ya kila siku, na tuchukue muda fulani wa kujiburudisha kwa maji ya kweli.—Mdo. 17:11.
Soma Neno Lote la Mungu
Je, wewe umewahi kusoma Biblia nzima? Wengine wameona likiwa jambo gumu sana kusoma Biblia kuanzia Mwanzo hadi Ufunuo. Kwa hiyo, wengi waliotaka kusoma Biblia nzima walianza kwa kusoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwanza. Kwa nini? Huenda ikawa ni kwa sababu waliweza kuona kwa urahisi zaidi jinsi vitabu hivyo vya Biblia vinavyowahusu kwa sababu walitaka kufuata hatua za Kristo. Au huenda ikawa waliona kwamba si kazi ngumu kusoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo—kwa sababu yanazidi kidogo tu robo ya Biblia. Lakini baada ya kumaliza kusoma vitabu hivyo 27, waligeukia vitabu 39 vya Maandiko ya Kiebrania wakaanza kuvisoma na kuvifurahia. Kufikia wakati walipomaliza Maandiko ya Kiebrania, walikuwa na desturi ya kusoma Biblia kwa ukawaida, basi wakaendelea, wakasoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwa mara ya pili, na hawajaacha kamwe kusoma. Wewe pia uwe na zoea la kusoma Neno la Mungu kila siku maishani mwako.
Je, kuna yeyote katika familia yenu au kutanikoni ambaye hawezi kusoma? Mbona usijitolee kumsomea Biblia kwa ukawaida? Wewe utafaidika, na yeye pia atafaidika anapotafakari mambo anayoyasikia na kuyatumia maishani mwake.—Ufu. 1:3.
Baada ya muda, unaweza kuanza kufanya miradi maalumu inayohusu usomaji wa Biblia. Baadhi yake inaweza kukufanya ufahamu zaidi uhusiano uliopo baina ya sehemu mbalimbali za Biblia. Ikiwa Biblia yako ina marejeo ya pambizoni, hayo yanaweza kukuongoza kwenye habari za kihistoria na kwenye masimulizi yanayolingana na hayo. Marejeo hayo yanaweza kukusaidia utambue hali zilizofanya zaburi mbalimbali ziandikwe na vilevile hali zilizofanya mitume wa Yesu Kristo waandike barua zao. Kichapo Insight on the Scriptures kinaandaa habari za ziada chungu nzima juu ya watu, mahali-mahali, na sifa zinazotajwa katika Biblia. Chati zinaonyesha utimizo wa unabii wa Biblia, wafalme na manabii walioishi wakati ule ule mmoja, na zinakadiria tarehe za matukio mengi ya Biblia.
Unapotafakari mambo unayojifunza, utaelewa sababu zilizofanya hali fulani zisitawi miongoni mwa watu wa Mungu. Pia utaelewa sababu iliyofanya Yehova awatendee watu wake kwa njia fulani. Utaona jinsi Yehova anavyopima matendo ya serikali mbalimbali, makundi ya watu, na watu mmoja-mmoja. Jambo hili litakusaidia ufahamu zaidi njia yake ya kufikiri.
Historia ya Biblia itakupendeza zaidi unapowazia akilini eneo la matukio unayosoma. Ramani za nchi zinazotajwa katika Biblia zinaonyesha sura na vilevile umbali ulioko kati ya sehemu tofauti-tofauti. Kwa mfano, huenda Waisraeli walivukia sehemu ipi ya Bahari Nyekundu? Nchi ya Ahadi ilikuwa na ukubwa gani? Yesu alitembea kadiri gani wakati wa huduma yake duniani? Paulo aliona nini katika safari zake za umishonari? Ramani na ufafanuzi wa maeneo zinaonyesha mambo yatakayofanya usomaji wako ufurahishe. Unaweza kupata wapi ramani za nchi zinazotajwa katika Biblia? Baadhi ya ramani hizo zimo katika New World Translation of the Holy Scriptures. Mabuku ya Insight yana ramani zipatazo 70 na faharisi ya ramani mwishoni mwa buku la kwanza. Tumia Watch Tower Publications Index kutafuta ramani nyinginezo. Kama vichapo hivyo havipatikani, tumia ramani zinazochapwa kwenye Mnara wa Mlinzi ili zikusaidie unaposoma Biblia.
Katika Maandiko ya Kiebrania, Mfalme Daudi alimtukuza Yehova, akisema: “Mungu, fikira zako zina thamani nyingi kwangu; jinsi ilivyo kubwa jumla yake!” (Zab. 139:17) Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, mtume Paulo alimsifu Yehova kwa sababu Yeye “ameng’aa juu ya mioyo yetu ili kuimulika kwa ujuzi wenye utukufu juu ya Mungu kwa uso wa Kristo.” (2 Kor. 4:6) Daudi na Paulo waliishi katika karne zilizoachana sana; lakini, wote wawili walifurahia Neno la Mungu. Hata wewe unaweza kufurahia kwa kutenga wakati wa kusoma yote ambayo Yehova amekupa katika Neno lake lililopuliziwa.