Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 1: Maana ya Ubatizo
    Vijana Huuliza
    • Kijana akibatizwa katika kidimbwi kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova.

      VIJANA HUULIZA

      Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 1: Maana ya Ubatizo

      Kila mwaka, vijana wengi wanaolelewa na Mashahidi wa Yehova hubatizwa. Je, unafikiria kuchukua hatua hiyo? Ikiwa ndivyo, kwanza unahitaji kuelewa maana ya kujiweka wakfu na kubatizwa.

      • Ubatizo ni nini?

      • Kujiweka wakfu kunamaanisha nini?

      • Kwa nini ubatizo ni muhimu?

      • Vijana wenzako wanasema nini

      • Maoni yasiyo sahihi na mambo hakika

      Ubatizo ni nini?

      Ubatizo unaotajwa katika Biblia unahusisha kuzamishwa kabisa ndani ya maji—wala si kunyunyiziwa maji—jambo lililo na maana ya pekee.

      • Kuzamishwa ndani ya maji wakati wa ubatizo ni tangazo la hadharani la kwamba umeacha maisha ya kufanya mapendezi yako mwenyewe.

      • Kuinuliwa kutoka ndani ya maji kunaonyesha kwamba umeanza maisha mapya ukiwa umekazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu.

      Kwa kubatizwa, unaonyesha hadharani kwamba unatambua Yehova ana mamlaka ya kuweka viwango vya mema na mabaya, na unatangaza rasmi kwamba umeahidi kwa hiari kuishi kulingana na matakwa yake.

      Jambo la kufikiria: Kwa nini ufikirie kutangaza hadharani kwamba unataka kumtii Yehova katika maisha yako yote? Ona 1 Yohana 4:19 na Ufunuo 4:11.

      Kujiweka wakfu kunamaanisha nini?

      Kabla ya kubatizwa, unapaswa kujiweka wakfu kwa Yehova faraghani. Jinsi gani?

      Katika sala yako ya kibinafsi, unamwambia Yehova kwamba unaahidi kumtumikia milele na kwamba utafanya mambo anayotaka hata hali iweje na hata watu wengine waamue kufanya nini.

      Ubatizo ni tangazo la hadharani linaloonyesha kwamba ulijiweka wakfu. Unawaonyesha wengine kwamba umejikana mwenyewe na sasa wewe ni mali ya Yehova.—Mathayo 16:24.

      Jambo la kufikiria: Kwa nini maisha yako yanakuwa bora zaidi unapokuwa mali ya Yehova? Ona Isaya 48:17, 18 na Waebrania 11:6.

      Kwa nini ubatizo ni muhimu?

      Yesu alisema kwamba wanafunzi wake walipaswa kubatizwa. (Mathayo 28:19, 20) Hivyo, ubatizo bado ni takwa kwa Wakristo. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba ni muhimu mtu abatizwe ili aweze kuokolewa.—1 Petro 3:21.

      Hata hivyo, nia yako ya kubatizwa inapaswa kuchochewa na upendo na uthamini wako kwa Yehova. Mtazamo wako unapaswa kuwa kama wa mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Nitamlipa Yehova nini kwa mema yote aliyonitendea? . . . Nami nitaliitia jina la Yehova. Nitamtimizia Yehova nadhiri zangu.”—Zaburi 116:12-14.

      Jambo la kufikiria: Yehova amekufanyia mambo gani mema, na unaweza kumlipa jinsi gani? Ona Kumbukumbu la Torati 10:12, 13 na Waroma 12:1.

      Vijana wenzako wanasema nini

      Mijin.

      “Wakfu unahusisha ahadi unayompa Yehova, na hilo ni jambo zito. Hata hivyo, kuna baraka nyingi ukiwa mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu. Yeye anaweza kututunza kwa njia bora zaidi kuliko tunavyoweza kujitunza.”—Mijin.

      Ember.

      “Yehova ameshaonyesha kwamba anakupenda. Unapobatizwa unaonyesha kwamba unampenda sana. Kubatizwa ni pendeleo na baraka kubwa!”—Ember.

      Julian.

      “Uamuzi wa kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa ni uamuzi muhimu zaidi ambao mtu anaweza kufanya. Lakini hilo lisikuogopeshe. Ikiwa umejitayarisha na unafanya hivyo ukiwa na sababu nzuri, ni uamuzi bora zaidi utakaofanya.”—Julian.

      Maoni yasiyo sahihi na mambo hakika

      MAONI YASIYO SAHIHI — Watu wazima tu ndio waliokomaa vya kutosha ili kubatizwa.

      JAMBO HAKIKA — Ukomavu unaonekana si kupitia umri bali kupitia jinsi mtu anavyompenda Yehova na utayari wake wa kumtii. Walipokuwa bado vijana, Yosefu, Samweli, na Yosia walionyesha ukomavu huo. Vijana wengi leo wanafanya hivyo.

      Biblia inasema: “Mtoto hujulikana kwa matendo yake, kama tabia yake ni safi na ya unyoofu.”—Methali 20:11.

      MAONI YASIYO SAHIHI — Ikiwa rafiki zako wanabatizwa, wewe pia unapaswa kubatizwa.

      JAMBO HAKIKA — Uamuzi wa kujiweka wakfu na kubatizwa ni wa kibinafsi unaopaswa kufanywa kutoka moyoni. Si njia au desturi ambayo unapaswa uifanye unapofikia umri fulani kwa sababu tu wengine wamefanya hivyo au kwa sababu unafikiri kwamba wengine wanakutazamia ufanye hivyo.

      Biblia inasema: “Watu wako watajitoa kwa hiari.”—Zaburi 110:3.

      MAONI YASIYO SAHIHI — Ikiwa hujabatizwa, huwajibiki kutokana na matendo yako.

      JAMBO HAKIKA — Unawajibika kwa Yehova si wakati unapobatizwa bali unapojua lililo jema na lililo baya machoni pake.

      Biblia inasema: “Ikiwa mtu anajua jinsi ya kufanya yaliyo sawa na bado hayafanyi, hiyo ni dhambi kwake.”—Yakobo 4:17.

      DOKEZO: Ikiwa daraka la kuwa Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa linaonekana kuwa lenye kulemea, kwa nini usichukue hatua ili kukabiliana na kushughulikia wasiwasi wako? Unaweza kufanya hivyo kwa kusoma Sura ya 37 katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2.

      Muhtasari: Kwa nini ubatizo ni muhimu?

      • Yesu alisema kwamba lazima wanafunzi wake wabatizwe.

      • Ubatizo ni muhimu ili kupata wokovu.

      • Ni pendeleo kubwa kumtumikia Yehova ukiwa Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa.

  • Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 2: Kujitayarisha kwa Ajili ya Ubatizo
    Vijana Huuliza
    • Msichana akifanya utafiti kuhusu ubatizo kwa kutumia Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia.

      VIJANA HUULIZA

      Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 2: Kujitayarisha kwa Ajili ya Ubatizo

      Ikiwa unaishi kulingana na viwango vya Biblia na unasitawisha urafiki na Mungu, huenda unafikiria kubatizwa. Utajuaje kwamba uko tayari kuchukua hatua hiyo?a

      Katika makala hii

      • Ninahitaji kujua mambo mengi kadiri gani?

      • Ninapaswa kufanya nini?

      • Vijana wenzako wanasema nini

      Ninahitaji kujua mambo mengi kadiri gani?

      Kujitayarisha kwa ajili ya ubatizo hakuhusishi kukariri mambo kama vile anavyofanya mtu anayetaka kufaulu mtihani wa shule. Hata hivyo, utahitaji kutumia ‘nguvu zako za kufikiri’ ili uwe na uhakika kabisa kwamba Biblia inafundisha kweli. (Waroma 12:1) Kwa mfano:

      • Je, unaamini kwamba Mungu yupo na anastahili ibada yako?

        Biblia inasema hivi: “Yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kuwa yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.

        Jiulize hivi: ‘Kwa nini ninamwamini Mungu?’ (Waebrania 3:4) ‘Kwa nini ninapaswa kumwabudu?’—Ufunuo 4:11.

        Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Uumbaji au Mageuzi?—Sehemu ya 1: Kwa Nini Nimwamini Mungu?”

      • Je, unaamini kwamba ujumbe ulio katika Biblia umetoka kwa Mungu?

        Biblia inasema hivi: “Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.”—2 Timotheo 3:16.

        Jiulize hivi: ‘Kwa nini ninaamini kwamba ujumbe unaopatikana katika Biblia si mawazo ya wanadamu?’—Isaya 46:10; 1 Wathesalonike 2:13.

        Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Biblia Inaweza Kunisaidiaje?—Sehemu ya 1: Ichunguze Biblia Yako.”

      • Je, unaamini kwamba Yehova anatumia kutaniko la Kikristo kutimiza kusudi lake?

        Biblia inasema hivi: “Na [Mungu] awe na utukufu kupitia kutaniko na kupitia Kristo Yesu kwa vizazi vyote milele na milele.”—Waefeso 3:21.

        Jiulize hivi: ‘Je, mimi huona mambo ninayojifunza kupitia Biblia katika mikutano ya Kikristo kuwa yanatoka kwa wanadamu au kwa Yehova?’ (Mathayo 24:45) ‘Je, mimi huhudhuria mikutano hata wakati ambapo wazazi wangu hawawezi kuhudhuria (ikiwa wanakuruhusu kufanya hivyo)?’—Waebrania 10:24, 25.

        Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Kwa Nini Uhudhurie Mikutano Kwenye Jumba la Ufalme?”

      Ninapaswa kufanya nini?

      Huhitaji kuwa mkamilifu ili ubatizwe. Hata hivyo, unapaswa kuthibitisha kwamba kwa kweli unataka ‘kuacha uovu na kutenda mema.’ (Zaburi 34:14) Kwa mfano:

      • Je, unaishi kulingana na viwango vya Yehova?

        Biblia inasema hivi: “Iweni na dhamiri njema.”—1 Petro 3:16.

        Jiulize hivi: ‘Nimethibitishaje kwamba ‘nguvu zangu za utambuzi’ zimezoezwa “kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa”?’ (Waebrania 5:14) ‘Ninaweza kukumbuka hali hususa ambazo niliweza kushinda uvutano wa marafiki wa kufanya mambo mabaya? Je, rafiki zangu hunitia moyo kufanya yaliyo sawa?’—Methali 13:20.

        Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Ninaweza Kuizoezaje Dhamiri Yangu?”

      • Je, unawajibika kwa matendo yako?

        Biblia inasema hivi: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Waroma 14:12.

        Jiulize hivi: ‘Je, mimi ni mnyoofu moyoni na kwa wengine?’ (Waebrania 13:18) ‘Je, mimi hukubali makosa yangu, au nina kawaida ya kuyaficha au kuwalaumu wengine?’—Methali 28:13.

        Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Nifanye Nini Ninapokosea?”

      • Je, unadumisha urafiki wako na Yehova?

        Biblia inasema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.

        Jiulize hivi: ‘Ninamkaribia Yehova kupitia njia zipi?’ Kwa mfano, ‘Je, ninasoma Biblia mara nyingi kadiri gani?’ (Zaburi 1:1, 2) ‘Je, ninasali kwa ukawaida?’ (1 Wathesalonike 5:17) ‘Je, ninataja mambo hususa katika sala zangu? Je, rafiki zangu ni rafiki za Yehova?’—Zaburi 15:1, 4.

        Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Biblia Inaweza Kunisaidiaje?—Sehemu ya 2: Fanya Usomaji wa Biblia Uwe Wenye Kufurahisha” na “Kwa Nini Ninapaswa Kusali?”

      DOKEZO: Ili kujitayarisha kwa ajili ya ubatizo, soma sura ya 37 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2. Pitia hasa mazoezi yanayopatikana kwenye ukurasa wa 308 na 309.

      a Soma makala yenye kichwa, “Nibatizwe?—Sehemu ya 1,” inayozungumzia maana na umuhimu wa kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa.

      Vijana wenzako wanasema nini

      Gabriella.

      “Mazoezi kuhusu ubatizo yanayopatikana katika kitabu Vijana Huuliza, yalinisaidia kuona mambo niliyopaswa kuboresha kabla ya kubatizwa. Yalinisaidia pia kuweka malengo ambayo ningependa kufikia baada ya ubatizo. Kujiweka wakfu kwa Yehova ni daraka kubwa sana, lakini pia ni pendeleo kubwa sana ambalo mtu anaweza kuwa nalo.”—Gabriella.

      Caleb.

      “Katika Biblia, Timotheo aliambiwa hivi: ‘Endelea kufuata mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini.’” (2 Timotheo 3:14) “Tumia wakati kujifunza Neno la Mungu ili ujithibitishie moyoni mwako kwamba linafundisha kweli. Umejiweka wakfu kwa Yehova—si kwa mtu yoyote—hivyo unapofikiria kuhusu ubatizo, jambo la muhimu kwako linapaswa kuwa jinsi Yehova anavyohisi.”—Caleb.

      Muhtasari: Ninaweza kujitayarishaje kwa ajili ya ubatizo?

      Chunguza mambo unayoamini. Je, unaamini kwamba kuna Mungu? Je, unaamini kwamba anastahili ibada yako? Je, unaamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho? Je, unaamini kwamba Yehova anatumia tengenezo ili kutimiza kusudi lake?

      Chunguza matendo yako. Je, unaishi kulingana na viwango vya Yehova? Je, unawajibika kwa matendo yako? Je, unadumisha urafiki wako na Yehova?

  • Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 3: Kwa Nini Ninasitasita Kubatizwa?
    Vijana Huuliza
    • Mwanamume akibatizwa kwenye ziwa huku wengine wakitazama.

      VIJANA HUULIZA

      Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 3: Kwa Nini Ninasitasita Kubatizwa?

      Je, wazo la kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa linakufanya uwe na wasiwasi? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia kushinda woga huo.

      Katika makala hii

      • Vipi nikifanya kosa zito baada ya kubatizwa?

      • Vipi ikiwa ninaogopa wajibu unaotokana na kubatizwa?

      • Vipi ikiwa ninahisi sistahili kumtumikia Yehova?

      • Vijana wenzako wanasema nini

      Vipi nikifanya kosa zito baada ya kubatizwa?

      Kwa nini wengine wana wasiwasi? Huenda unamfahamu mtu ambaye alitenda dhambi nzito na akahitaji kuondolewa kutanikoni. (1 Wakorintho 5:11-13) Huenda ukahofia kwamba hilo litakupata.

      “Nilipofikiria kuhusu kubatizwa, wazo la kukosea liliniogopesha. Niliwazia jinsi ambavyo hilo lingewaathiri sana wazazi wangu.”—Rebekah.

      Andiko la msingi: “Mtu mwovu na aiache njia yake . . . Na arudi kwa Yehova, ambaye atamwonyesha rehema, kwa Mungu wetu, kwa maana atasamehe kwa njia kubwa.”—Isaya 55:7.

      Fikiria hili: Ingawa wakosaji wasiotubu huondolewa kutoka kutanikoni, Yehova huwaonyesha rehema wale wanaotubu kwa unyenyekevu na kukubali kurekebishwa.—Zaburi 103:13, 14; 2 Wakorintho 7:11.

      Licha ya hilo, ukweli wa mambo ndio huu: Hata ingawa wewe si mkamilifu, unaweza kushinda vishawishi kwa msaada wa Mungu. (1 Wakorintho 10:13) Isitoshe, ni nani anayeamua jinsi utakavyotenda? Ni wewe? Au ni mtu mwingine?

      “Nilihofia kwamba ningefanya kosa zito baada ya kubatizwa, lakini nikatambua kwamba ningekuwa nikikosea ikiwa nisingebatizwa. Nilitambua kwamba sipaswi kuogopa mambo ambayo huenda yakatokea kesho yanizuie kufanya ninayopaswa kufanya leo.”—Karen.

      Jambo kuu: Unaweza kuamua kuepuka kufanya dhambi nzito—kama tu watumishi wengi wa Yehova wanavyoepuka.—Wafilipi 2:12.

      Je, unahitaji msaada zaidi? Ona makala “Ninaweza Kupinga Vishawishi Jinsi Gani?”

      Vipi ikiwa ninaogopa wajibu unaotokana na kubatizwa?

      Kwa nini wengine wana wasiwasi? Kwa mfano, huenda unawafahamu vijana ambao wamehamia mbali na familia na marafiki ili kupanua utumishi wao kwa Yehova. Huenda ukawa na wasiwasi kwamba watu watatazamia ufanye vivyo hivyo.

      “Mkristo aliyebatizwa anaweza kupata mapendeleo zaidi, lakini watu fulani hawako tayari kujitoa au hali zao haziwaruhusu kufanya hivyo.”—Marie.

      Andiko la msingi: “Kila mmoja na achunguze matendo yake mwenyewe, kisha atakuwa na sababu ya kushangilia kuhusiana na yeye mwenyewe, na si kwa kujilinganisha na mtu mwingine.”—Wagalatia 6:4.

      Fikiria hili: Badala ya kujilinganisha na wengine, kazia fikira maneno ya Marko 12:30: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote.”

      Ona kwamba unapaswa kumtumikia Yehova kwa moyo wako wote—si wa mtu mwingine. Ikiwa kweli unampenda Yehova, utatafuta njia za kumtumikia kwa kadiri ya uwezo wako.

      “Ingawa ubatizo ni hatua muhimu, si mzigo mzito. Ukishirikiana na marafiki wazuri, watakusaidia. Kushughulikia majukumu mazito hatua kwa hatua kutakufanya uwe mwenye furaha. Ukiepuka kubatizwa utakuwa ukijidhuru mwenyewe.”—Julia.

      Jambo kuu: Sitawisha uthamini kuelekea upendo ambao Yehova amekuonyesha. Hilo litakuchochea kumpa kilicho bora.—1 Yohana 4:19.

      Je, unahitaji msaada zaidi? Ona makala “Je, Mimi Huchukua Mambo kwa Uzito?”

      Vipi ikiwa ninahisi sistahili kumtumikia Yehova?

      Kwa nini wengine wana wasiwasi? Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote; wanadamu si kitu wanapolinganishwa naye! Huenda ukajiuliza ikiwa kweli Yehova anajua kwamba wewe upo.

      “Kwa sababu wazazi wangu ni Mashahidi wa Yehova, nilikuwa na wasiwasi kwamba nilikuwa ‘nimerithi’ tu urafiki wangu na Yehova kutoka kwao na kwamba Yehova hakuwa amenivuta kibinafsi.”—Natalie.

      Andiko la msingi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba aliyenituma amvute.”—Yohana 6:44.

      Fikiria hili: Uhakika wa kwamba unafikiria kubatizwa unaonyesha kwamba Yehova anakuvuta uwe na urafiki wa karibu naye. Je, isingefaa kukubali mwaliko huo?

      Kumbuka pia kwamba Yehova—si wewe au mtu mwingine—ndiye anayeweka viwango kwa ajili ya wale atakaowavuta kwake. Na Neno lake linatuhakikisha kwamba ‘ukimkaribia Mungu, atakukaribia.’—Yakobo 4:8.

      “Uhakika wa kwamba unafahamu kumhusu Yehova na kwamba umevutwa kwake ni uthibitisho kwamba anakupenda. Kwa hiyo, akili yako inapokuambia hustahili kumtumikia, jikumbushe kwamba yeye hakubaliani na wazo hilo. Na sikuzote Yehova yuko sahihi.”—Selina.

      Jambo kuu: Ikiwa unatimiza viwango vya Biblia kwa ajili ya ubatizo, basi unastahili kumtumikia Yehova. Mbali na hilo, anastahili ibada yako.—Ufunuo 4:11.

      Je, unahitaji msaada zaidi? Ona makala “Kwa Nini Ninapaswa Kusali?”

      Vijana wenzako wanasema nini

      Skye.

      “Hupaswi kuepuka kubatizwa eti kwa sababu unaogopa hutafaulu. Ni kama kukimbia kwenye shindano la mbio. Unaweza kuamua hutakimbia kwa sababu unaogopa utaanguka. Lakini ukianguka, unaweza kuinuka tena. Huwezi kufika kwenye mstari wa mwisho ikiwa hutaanza mbio hizo.”—Skye.

      Vinicio.

      “Kuogopa aksidenti hakumzuii kijana kupata leseni ya udereva. Ndivyo ilivyo na ubatizo. Tunapaswa kukazia fikiria kudumisha urafiki mzuri na Yehova badala ya kuwa na wasiwasi kuhusu kinachoweza kutokea.”—Vinicio.

      Muhtasari: Kwa nini ninasitasita kubatizwa?

      • Kuogopa kufanya kosa zito. Unaweza kuamua kuepuka kufanya dhambi nzito—kama tu watumishi wengi wa Yehova wanavyoepuka.

      • Kuogopa wajibu. Sitawisha uthamini kuelekea upendo ambao Yehova amekuonyesha. Hilo litakuchochea kumpa kilicho bora.

      • Kuhisi kwamba hustahili. Ikiwa unatimiza viwango vya Biblia kwa ajili ya ubatizo, basi unastahili kumtumikia Yehova. Mbali na hilo, anastahili ibada yako.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki