-
Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 1: Maana ya UbatizoVijana Huuliza
-
-
VIJANA HUULIZA
Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 1: Maana ya Ubatizo
Kila mwaka, vijana wengi wanaolelewa na Mashahidi wa Yehova hubatizwa. Je, unafikiria kuchukua hatua hiyo? Ikiwa ndivyo, kwanza unahitaji kuelewa maana ya kujiweka wakfu na kubatizwa.
Ubatizo ni nini?
Ubatizo unaotajwa katika Biblia unahusisha kuzamishwa kabisa ndani ya maji—wala si kunyunyiziwa maji—jambo lililo na maana ya pekee.
Kuzamishwa ndani ya maji wakati wa ubatizo ni tangazo la hadharani la kwamba umeacha maisha ya kufanya mapendezi yako mwenyewe.
Kuinuliwa kutoka ndani ya maji kunaonyesha kwamba umeanza maisha mapya ukiwa umekazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu.
Kwa kubatizwa, unaonyesha hadharani kwamba unatambua Yehova ana mamlaka ya kuweka viwango vya mema na mabaya, na unatangaza rasmi kwamba umeahidi kwa hiari kuishi kulingana na matakwa yake.
Jambo la kufikiria: Kwa nini ufikirie kutangaza hadharani kwamba unataka kumtii Yehova katika maisha yako yote? Ona 1 Yohana 4:19 na Ufunuo 4:11.
Kujiweka wakfu kunamaanisha nini?
Kabla ya kubatizwa, unapaswa kujiweka wakfu kwa Yehova faraghani. Jinsi gani?
Katika sala yako ya kibinafsi, unamwambia Yehova kwamba unaahidi kumtumikia milele na kwamba utafanya mambo anayotaka hata hali iweje na hata watu wengine waamue kufanya nini.
Ubatizo ni tangazo la hadharani linaloonyesha kwamba ulijiweka wakfu. Unawaonyesha wengine kwamba umejikana mwenyewe na sasa wewe ni mali ya Yehova.—Mathayo 16:24.
Jambo la kufikiria: Kwa nini maisha yako yanakuwa bora zaidi unapokuwa mali ya Yehova? Ona Isaya 48:17, 18 na Waebrania 11:6.
Kwa nini ubatizo ni muhimu?
Yesu alisema kwamba wanafunzi wake walipaswa kubatizwa. (Mathayo 28:19, 20) Hivyo, ubatizo bado ni takwa kwa Wakristo. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba ni muhimu mtu abatizwe ili aweze kuokolewa.—1 Petro 3:21.
Hata hivyo, nia yako ya kubatizwa inapaswa kuchochewa na upendo na uthamini wako kwa Yehova. Mtazamo wako unapaswa kuwa kama wa mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Nitamlipa Yehova nini kwa mema yote aliyonitendea? . . . Nami nitaliitia jina la Yehova. Nitamtimizia Yehova nadhiri zangu.”—Zaburi 116:12-14.
Jambo la kufikiria: Yehova amekufanyia mambo gani mema, na unaweza kumlipa jinsi gani? Ona Kumbukumbu la Torati 10:12, 13 na Waroma 12:1.
-
-
Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 2: Kujitayarisha kwa Ajili ya UbatizoVijana Huuliza
-
-
VIJANA HUULIZA
Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 2: Kujitayarisha kwa Ajili ya Ubatizo
Ikiwa unaishi kulingana na viwango vya Biblia na unasitawisha urafiki na Mungu, huenda unafikiria kubatizwa. Utajuaje kwamba uko tayari kuchukua hatua hiyo?a
Katika makala hii
Ninahitaji kujua mambo mengi kadiri gani?
Kujitayarisha kwa ajili ya ubatizo hakuhusishi kukariri mambo kama vile anavyofanya mtu anayetaka kufaulu mtihani wa shule. Hata hivyo, utahitaji kutumia ‘nguvu zako za kufikiri’ ili uwe na uhakika kabisa kwamba Biblia inafundisha kweli. (Waroma 12:1) Kwa mfano:
Je, unaamini kwamba Mungu yupo na anastahili ibada yako?
Biblia inasema hivi: “Yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kuwa yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.
Jiulize hivi: ‘Kwa nini ninamwamini Mungu?’ (Waebrania 3:4) ‘Kwa nini ninapaswa kumwabudu?’—Ufunuo 4:11.
Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Uumbaji au Mageuzi?—Sehemu ya 1: Kwa Nini Nimwamini Mungu?”
Je, unaamini kwamba ujumbe ulio katika Biblia umetoka kwa Mungu?
Biblia inasema hivi: “Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.”—2 Timotheo 3:16.
Jiulize hivi: ‘Kwa nini ninaamini kwamba ujumbe unaopatikana katika Biblia si mawazo ya wanadamu?’—Isaya 46:10; 1 Wathesalonike 2:13.
Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Biblia Inaweza Kunisaidiaje?—Sehemu ya 1: Ichunguze Biblia Yako.”
Je, unaamini kwamba Yehova anatumia kutaniko la Kikristo kutimiza kusudi lake?
Biblia inasema hivi: “Na [Mungu] awe na utukufu kupitia kutaniko na kupitia Kristo Yesu kwa vizazi vyote milele na milele.”—Waefeso 3:21.
Jiulize hivi: ‘Je, mimi huona mambo ninayojifunza kupitia Biblia katika mikutano ya Kikristo kuwa yanatoka kwa wanadamu au kwa Yehova?’ (Mathayo 24:45) ‘Je, mimi huhudhuria mikutano hata wakati ambapo wazazi wangu hawawezi kuhudhuria (ikiwa wanakuruhusu kufanya hivyo)?’—Waebrania 10:24, 25.
Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Kwa Nini Uhudhurie Mikutano Kwenye Jumba la Ufalme?”
Ninapaswa kufanya nini?
Huhitaji kuwa mkamilifu ili ubatizwe. Hata hivyo, unapaswa kuthibitisha kwamba kwa kweli unataka ‘kuacha uovu na kutenda mema.’ (Zaburi 34:14) Kwa mfano:
Je, unaishi kulingana na viwango vya Yehova?
Biblia inasema hivi: “Iweni na dhamiri njema.”—1 Petro 3:16.
Jiulize hivi: ‘Nimethibitishaje kwamba ‘nguvu zangu za utambuzi’ zimezoezwa “kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa”?’ (Waebrania 5:14) ‘Ninaweza kukumbuka hali hususa ambazo niliweza kushinda uvutano wa marafiki wa kufanya mambo mabaya? Je, rafiki zangu hunitia moyo kufanya yaliyo sawa?’—Methali 13:20.
Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Ninaweza Kuizoezaje Dhamiri Yangu?”
Je, unawajibika kwa matendo yako?
Biblia inasema hivi: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Waroma 14:12.
Jiulize hivi: ‘Je, mimi ni mnyoofu moyoni na kwa wengine?’ (Waebrania 13:18) ‘Je, mimi hukubali makosa yangu, au nina kawaida ya kuyaficha au kuwalaumu wengine?’—Methali 28:13.
Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Nifanye Nini Ninapokosea?”
Je, unadumisha urafiki wako na Yehova?
Biblia inasema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.
Jiulize hivi: ‘Ninamkaribia Yehova kupitia njia zipi?’ Kwa mfano, ‘Je, ninasoma Biblia mara nyingi kadiri gani?’ (Zaburi 1:1, 2) ‘Je, ninasali kwa ukawaida?’ (1 Wathesalonike 5:17) ‘Je, ninataja mambo hususa katika sala zangu? Je, rafiki zangu ni rafiki za Yehova?’—Zaburi 15:1, 4.
Je, unahitaji msaada? Ona makala yenye kichwa, “Biblia Inaweza Kunisaidiaje?—Sehemu ya 2: Fanya Usomaji wa Biblia Uwe Wenye Kufurahisha” na “Kwa Nini Ninapaswa Kusali?”
DOKEZO: Ili kujitayarisha kwa ajili ya ubatizo, soma sura ya 37 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2. Pitia hasa mazoezi yanayopatikana kwenye ukurasa wa 308 na 309.
a Soma makala yenye kichwa, “Nibatizwe?—Sehemu ya 1,” inayozungumzia maana na umuhimu wa kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa.
-
-
Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 3: Kwa Nini Ninasitasita Kubatizwa?Vijana Huuliza
-
-
VIJANA HUULIZA
Je, Nibatizwe?—Sehemu ya 3: Kwa Nini Ninasitasita Kubatizwa?
Je, wazo la kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa linakufanya uwe na wasiwasi? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia kushinda woga huo.
Katika makala hii
Vipi nikifanya kosa zito baada ya kubatizwa?
Kwa nini wengine wana wasiwasi? Huenda unamfahamu mtu ambaye alitenda dhambi nzito na akahitaji kuondolewa kutanikoni. (1 Wakorintho 5:11-13) Huenda ukahofia kwamba hilo litakupata.
“Nilipofikiria kuhusu kubatizwa, wazo la kukosea liliniogopesha. Niliwazia jinsi ambavyo hilo lingewaathiri sana wazazi wangu.”—Rebekah.
Andiko la msingi: “Mtu mwovu na aiache njia yake . . . Na arudi kwa Yehova, ambaye atamwonyesha rehema, kwa Mungu wetu, kwa maana atasamehe kwa njia kubwa.”—Isaya 55:7.
Fikiria hili: Ingawa wakosaji wasiotubu huondolewa kutoka kutanikoni, Yehova huwaonyesha rehema wale wanaotubu kwa unyenyekevu na kukubali kurekebishwa.—Zaburi 103:13, 14; 2 Wakorintho 7:11.
Licha ya hilo, ukweli wa mambo ndio huu: Hata ingawa wewe si mkamilifu, unaweza kushinda vishawishi kwa msaada wa Mungu. (1 Wakorintho 10:13) Isitoshe, ni nani anayeamua jinsi utakavyotenda? Ni wewe? Au ni mtu mwingine?
“Nilihofia kwamba ningefanya kosa zito baada ya kubatizwa, lakini nikatambua kwamba ningekuwa nikikosea ikiwa nisingebatizwa. Nilitambua kwamba sipaswi kuogopa mambo ambayo huenda yakatokea kesho yanizuie kufanya ninayopaswa kufanya leo.”—Karen.
Jambo kuu: Unaweza kuamua kuepuka kufanya dhambi nzito—kama tu watumishi wengi wa Yehova wanavyoepuka.—Wafilipi 2:12.
Je, unahitaji msaada zaidi? Ona makala “Ninaweza Kupinga Vishawishi Jinsi Gani?”
Vipi ikiwa ninaogopa wajibu unaotokana na kubatizwa?
Kwa nini wengine wana wasiwasi? Kwa mfano, huenda unawafahamu vijana ambao wamehamia mbali na familia na marafiki ili kupanua utumishi wao kwa Yehova. Huenda ukawa na wasiwasi kwamba watu watatazamia ufanye vivyo hivyo.
“Mkristo aliyebatizwa anaweza kupata mapendeleo zaidi, lakini watu fulani hawako tayari kujitoa au hali zao haziwaruhusu kufanya hivyo.”—Marie.
Andiko la msingi: “Kila mmoja na achunguze matendo yake mwenyewe, kisha atakuwa na sababu ya kushangilia kuhusiana na yeye mwenyewe, na si kwa kujilinganisha na mtu mwingine.”—Wagalatia 6:4.
Fikiria hili: Badala ya kujilinganisha na wengine, kazia fikira maneno ya Marko 12:30: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote.”
Ona kwamba unapaswa kumtumikia Yehova kwa moyo wako wote—si wa mtu mwingine. Ikiwa kweli unampenda Yehova, utatafuta njia za kumtumikia kwa kadiri ya uwezo wako.
“Ingawa ubatizo ni hatua muhimu, si mzigo mzito. Ukishirikiana na marafiki wazuri, watakusaidia. Kushughulikia majukumu mazito hatua kwa hatua kutakufanya uwe mwenye furaha. Ukiepuka kubatizwa utakuwa ukijidhuru mwenyewe.”—Julia.
Jambo kuu: Sitawisha uthamini kuelekea upendo ambao Yehova amekuonyesha. Hilo litakuchochea kumpa kilicho bora.—1 Yohana 4:19.
Je, unahitaji msaada zaidi? Ona makala “Je, Mimi Huchukua Mambo kwa Uzito?”
Vipi ikiwa ninahisi sistahili kumtumikia Yehova?
Kwa nini wengine wana wasiwasi? Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote; wanadamu si kitu wanapolinganishwa naye! Huenda ukajiuliza ikiwa kweli Yehova anajua kwamba wewe upo.
“Kwa sababu wazazi wangu ni Mashahidi wa Yehova, nilikuwa na wasiwasi kwamba nilikuwa ‘nimerithi’ tu urafiki wangu na Yehova kutoka kwao na kwamba Yehova hakuwa amenivuta kibinafsi.”—Natalie.
Andiko la msingi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba aliyenituma amvute.”—Yohana 6:44.
Fikiria hili: Uhakika wa kwamba unafikiria kubatizwa unaonyesha kwamba Yehova anakuvuta uwe na urafiki wa karibu naye. Je, isingefaa kukubali mwaliko huo?
Kumbuka pia kwamba Yehova—si wewe au mtu mwingine—ndiye anayeweka viwango kwa ajili ya wale atakaowavuta kwake. Na Neno lake linatuhakikisha kwamba ‘ukimkaribia Mungu, atakukaribia.’—Yakobo 4:8.
“Uhakika wa kwamba unafahamu kumhusu Yehova na kwamba umevutwa kwake ni uthibitisho kwamba anakupenda. Kwa hiyo, akili yako inapokuambia hustahili kumtumikia, jikumbushe kwamba yeye hakubaliani na wazo hilo. Na sikuzote Yehova yuko sahihi.”—Selina.
Jambo kuu: Ikiwa unatimiza viwango vya Biblia kwa ajili ya ubatizo, basi unastahili kumtumikia Yehova. Mbali na hilo, anastahili ibada yako.—Ufunuo 4:11.
Je, unahitaji msaada zaidi? Ona makala “Kwa Nini Ninapaswa Kusali?”
-