Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uumbaji au Mageuzi?—Sehemu ya 1: Kwa Nini Nimwamini Mungu?
    Vijana Huuliza
    • Kijana akimwelezea mwanafunzi mwenzake kwa nini anamwamini Mungu

      VIJANA HUULIZA

      Uumbaji au Mageuzi?—Sehemu ya 1: Kwa Nini Nimwamini Mungu?

      • Uumbaji au mageuzi?

      • Kwa nini ninamwamini Mungu?

      • Kueleza msimamo wangu

      Uumbaji au mageuzi?

      Je, unaamini kwamba Mungu aliumba kila kitu? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayeamini hivyo; vijana wengi (na watu wazima) wanaamini jambo hilo. Lakini wengine husema kwamba uhai na ulimwengu wote ulijitokeza wenyewe​—bila msaada wa “Mtu Mkuu Kuliko Wote.”

      Je, ulijua? Mara nyingi watu wanaoamini uumbaji na wale wanaoamini mageuzi wote husema tu kile wanachoamini bila kujua kwa nini wanaamini jambo hilo.

      • Watu fulani huamini uumbaji kwa sababu hivyo ndivyo wamefundishwa kanisani.

      • Watu wengi huamini mageuzi kwa sababu hivyo ndivyo wamefundishwa shuleni.

      Mfululizo wa makala hizi utakusaidia kuimarisha msimamo wako na kuwaeleza wengine kile unachoamini kuhusu uumbaji. Hata hivyo, kwanza, unahitaji kujiuliza swali hili la msingi:

      Kwa nini ninamwamini Mungu?

      Kwa nini swali hilo ni muhimu? Kwa sababu Biblia inakutia moyo utumie ‘nguvu zako za kufikiri.’ (Waroma 12:1) Hilo linamaanisha kwamba imani yako kumwelekea Mungu haipaswi kutegemea tu

      • hisia (Nahisi kwamba kuna mtawala mwenye mamlaka kuu)

      • maoni ya wengine (Ninaishi katika jamii inayopenda mambo ya dini)

      • kusukumwa (Wazazi wangu walinifundisha kumwamini Mungu​—siwezi kuwapinga)

      Badala yake, wewe mwenyewe unapaswa kusadiki kabisa kwamba Mungu yuko ukiwa na sababu za msingi za kukufanya uamini jambo hilo.

      Hivyo basi, ni nini kinachokusadikisha kwamba Mungu yuko? Daftari “Kwa Nini Ninamwamini Mungu?” litakusaidia upate usadikisho. Pia, unaweza kufaidika zaidi kwa kujua jinsi ambavyo vijana wengine walijibu swali hilo.

      “Ninapokuwa darasani nikimsikiliza mwalimu akieleza jinsi miili yetu inavyofanya kazi, ninakuwa na uhakika kuwa Mungu yuko. Kila sehemu ya mwili ina kazi yake, kutia ndani vitu vidogo sana, na mifumo mbalimbali hufanya kazi bila sisi wenyewe kujua. Kwa kweli mwili wa binadamu unastaajabisha sana!”​—Teresa.

      “Ninapoona jengo refu sana, meli, au gari, mimi hujiuliza, ‘Ni nani aliyetengeneza kitu hiki?’ Gari hutengenezwa na watu wenye akili nyingi sana kwa sababu vitu vidogo-vidogo sana lazima vifanye kazi vizuri ili gari liweze kusonga. Ikiwa lazima gari libuniwe na mtu fulani, basi lazima mwanadamu awe alibuniwa na mtu fulani pia.”​—Richard.

      “Unapogundua kuwa wanadamu wenye akili sana walitumia mamia ya miaka kuelewa sehemu ndogo ya ulimwengu, ni jambo lisilopatana na akili kufikiria kuwa ulimwengu mzima ulijitokeza wenyewe bila msaada wa mtu fulani mwenye akili!”​—Karen.

      “Kadiri nilivyojifunza sayansi, ndivyo nilivyoshindwa kuamini mageuzi. Kwa mfano, nimefikiria kuhusu vitu vya asili vilivyotengenezwa kwa hesabu zilizo sahihi na jinsi wanadamu walivyo tofauti sana na viumbe wengine, kutia ndani uhitaji wa kujua sisi ni nani, tumetokea wapi, na tunaelekea wapi. Mageuzi hukusudiwa kuelezea mambo hayo kwa njia inayohusisha wanyama, lakini fundisho hilo halijawahi kueleza kwa nini wanadamu ni tofauti na viumbe vingine vyote. Ninaona mtu anahitaji kuwa na ‘imani’ zaidi kuamini mageuzi kuliko kumwamini Muumba.”​—Anthony.

      Kuelezea msimamo wangu

      Vipi ikiwa wanafunzi wenzako wanakudhihaki kwa sababu unaamini kitu usichoweza kuona? Vipi ikiwa wanasema kuwa sayansi “imethibitisha” mageuzi?

      Kwanza, uwe na uhakika na unachoamini. Usiogope wala usiaibike. (Waroma 1:​16) Zaidi ya yote, kumbuka:

      1. Hauko peke yako; bado kuna watu wengi wanaomwamini Mungu. Wanatia ndani wataalamu wenye akili nyingi. Kwa mfano, kuna wanasayansi wanaoamini kuna Mungu.

      2. Watu wanaposema hawamwamini Mungu, wakati mwingine wanachomaanisha hasa ni kuwa hawamwelewi Mungu. Badala ya kutoa uthibitisho wa kuunga mkono maoni yao, wao hutokeza maswali kama vile, “Ikiwa Mungu yupo, kwa nini anaruhusu uovu na kuteseka?” Mwishowe suala hilo linahusisha hisia badala ya kutumia uwezo wa kufikiri.

      3. Wanadamu wana “uhitaji wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Hilo linatia ndani uhitaji wa kumwamini Mungu. Hivyo ikiwa mtu anasema hakuna Mungu, mtu huyo​—na si wewe​—ndiye anayewajibika kueleza kwa nini amefikia mkataa huo.​—Waroma 1:​18-​20.

      4. Ni jambo linalopatana na akili kumwamini Mungu. Jambo hilo linapatana na ukweli uliothibitishwa kwamba uhai hauwezi kujitokeza wenyewe. Hakuna uthibitisho unaoweza kuonyesha kwamba uhai ulitokana na kitu kisicho hai.

      Hivyo, unaweza kusema nini ikiwa mtu anatilia shaka imani yako kumwelekea Mungu? Fikiria mambo haya machache.

      Ikiwa mtu anasema: “Watu wasio na elimu tu ndiyo wanaomwamini Mungu.”

      Unaweza kujibu: “Je, kweli unakubaliana na maoni hayo ya watu wengi? Mimi sikubaliani nayo. Kwa kweli, utafiti mmoja uliohusisha maprofesa 1,600 wa sayansi kutoka vyuo vikuu mbalimbali vinavyoheshimika ulionyesha kuwa theluthi moja ya maprofesa hao hawakudai kuwa hawamwamini Mungu au kwamba mambo ya Mungu hayajulikani.a Je, utasema maprofesa hao hawana akili kwa sababu wanamwamini Mungu?”

      Ikiwa mtu anasema: “Ikiwa Mungu yuko, kwa nini kuna mateso mengi ulimwenguni?”

      Unaweza kujibu hivi: “Je, huenda unamaanisha kwamba huelewi jinsi Mungu anavyotenda​—au katika kisa hiki, haonyeshi kuwa atachukua hatua? [Mruhusu ajibu.] Nimepata sababu zenye kuridhisha kuhusu ni kwa nini kuna mateso mengi duniani. Lakini ili kuelewa jambo hilo ni lazima uchunguze mafundisho kadhaa ya Biblia. Je, ungependa kujua zaidi?”

      Makala inayofuata katika mfululizo huu itazungumzia sababu kwa nini fundisho la mageuzi halitoi maelezo yenye kuridhisha kuhusu chanzo chetu.

      a Chanzo cha habari: Baraza la Utafiti Kuhusu Sayansi ya Kijamii, “Dini na Hali ya Kiroho Miongoni mwa Wanasayansi wa Vyuo Vikuu,” na Elaine Howard Ecklund , Februari 5, 2007.

  • Uumbaji au Mageuzi?—Sehemu ya 2: Kwa Nini Uchunguze Nadharia ya Mageuzi?
    Vijana Huuliza
    • Wanafunzi wa shule ya sekondari wakifundishwa kwamba mageuzi ni jambo hakika

      VIJANA HUULIZA

      Uumbaji au Mageuzi?​—Sehemu ya 2: Kwa Nini Uchunguze Nadharia ya Mageuzi?

      Alex amechanganyikiwa. Sikuzote amekuwa akiamini kwamba kuna Mungu na pia anaamini katika uumbaji. Lakini leo mwalimu wake wa biolojia amesisitiza kwa uthabiti kwamba nadharia ya mageuzi ni jambo hakika linalotegemea utafiti unaoaminika wa kisayansi. Alex hataki aonekane mpumbavu. Anajiambia: ‘Kwa kweli, ikiwa wanasayansi wamethibitisha kwamba nadharia ya mageuzi ni ya kweli, mimi ni nani nipingane nao?’

      Je, umewahi kujipata katika hali kama hiyo? Labda maishani mwako umekuwa ukiamini kile ambacho Biblia inasema kwamba: “Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Hata hivyo, hivi karibuni watu wamekuwa wakijaribu kukushawishi usadiki kwamba uumbaji ni hekaya au hadithi tu na kwamba mageuzi ni jambo la hakika. Je, unapaswa kuwaamini? Kwa nini uchunguze nadharia ya mageuzi?

      • Sababu mbili kwa nini uchunguze mageuzi

      • Maswali ya kufikiria

      • Vijana wenzako wanasema nini

      Sababu mbili kwa nini uchunguze mageuzi

      1. Wanasayansi hawakubaliani kuhusu nadharia ya mageuzi. Licha ya kufanya utafiti kwa miaka mingi, wanasayansi bado hawajapata ufafanuzi mwafaka kuhusu nadharia ya mageuzi ambao wanakubaliana nao.

        Jambo la kufikiria: Ikiwa wanasayansi hawakubaliani kuhusu nadharia ya mageuzi, na wao ndio wanaopaswa kuwa wataalamu, je, itakuwa kosa kwako kutoamini nadharia hiyo?​—Zaburi 10:4.

      2. Ni jambo zito kuamini jambo fulani. Mvulana anayeitwa Zachary anasema hivi: “Ikiwa uhai wetu ulijitokeza wenyewe, basi maisha yetu na vitu vyote vilivyomo duniani havingekuwa na maana yoyote.” Na hilo ni kweli. Kwa kweli, ikiwa nadharia ya mageuzi ni ya kweli, hatungekuwa na kusudi lolote maishani. (1 Wakorintho 15:32) Kwa upande mwingine, ikiwa habari kuhusu uumbaji ni ya kweli, tunaweza kupata majibu yenye kuridhisha kuhusu kusudi la uhai na tumaini la wakati ujao.​—Yeremia 29:11.

        Jambo la kufikiria: Kujua ukweli kuhusu mageuzi na uumbaji kunaweza kuboreshaje maisha yako?​—Waebrania 11:1.

      Maswali ya kufikiria

      DAI: ‘Kila kitu ulimwenguni kilitokea kwa sababu ya mlipuko mkubwa uliotokea ghafla bila kutarajia.’

      • Ni nani au ni nini kilichosababisha mlipuko huo?

      • Ni jambo gani linalopatana na akili zaidi, kwamba kila kitu kilijitokeza chenyewe au kwamba kila kitu kilitokana na kitu fulani au mtu fulani?

      DAI: ‘Wanadamu walitokana na wanyama.’

      • Ikiwa wanadamu walitokana na wanyama au sokwe, kwa nini kuna tofauti kubwa sana kati ya uwezo wa kiakili wa wanadamu na ule wa wanyama?a

      • Kwa nini hata namna za “msingi” kabisa za uhai ni tata sana?b

      DAI: ‘Nadharia ya mageuzi ni jambo lililothibitishwa.’

      • Je, yule anayedai hivyo, amechukua hatua ya kuchunguza uthibitisho huo yeye mwenyewe?

      • Ni watu wangapi wanaoamini mageuzi kwa sababu tu wameambiwa kwamba watu wote wenye akili wanaamini hivyo pia?

      VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI

      Gwen

      Gwen

      “Wazia ikiwa mtu angekwambia kwamba mlipuko ulitokea katika kiwanda cha uchapishaji na kisha rangi ikatapanyika ukutani na kwenye paa na kufanyiza kamusi nzuri na kamilifu. Je, ungeamini jambo hilo? Vivyo hivyo ingekuwa vigumu sana kuamini kwamba kila kitu katika ulimwengu huu wetu wenye utaratibu kilitokana na mlipuko mkubwa.”

      Jessica

      Jessica

      “Wanadamu wana uwezo mkubwa unaopita ule wanaohitaji ili kuendelea kuishi. Isitoshe, tunawatunza wagonjwa na kuwasaidia wanaoteseka. Kwa kweli hatungeweza kufanya mambo hayo ikiwa tulitokea kwa njia ya mageuzi ambayo husisitiza kwamba ‘viumbe vyenye nguvu ndivyo vinavyoendelea kuishi.’”

      Julia

      Julia

      “Ikiwa ungetembea ndani ya msitu na uone chumba maridadi kilichotengenezwa kwa mbao, je, ungefikiri: ‘Hili ni jambo linalovutia wee! Lazima iwe miti hii ilianguka kwa njia barabara kabisa na kisha ikatengeneza chumba hiki.’ Bila shaka hungefikiri hivyo, kwani jambo hilo halipatani na akili hata kidogo! Hivyo basi, kwa nini tuamini kwamba kila kitu katika ulimwengu huu kilijitokeza chenyewe?”

      a Huenda watu wengine wakadai kwamba wanadamu wana uwezo mkubwa zaidi wa kiakili kwa sababu ubongo wao ni mkubwa kuliko wa sokwe. Hata hivyo, ili uone kwamba sababu hizo si sahihi, tazama broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, ukurasa wa 28.

      b Tazama broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, ukurasa wa 8 hadi wa 12.

  • Uumbaji au Mageuzi?—Sehemu ya 3: Kwa Nini Uamini Uumbaji?
    Vijana Huuliza
    • Wanafunzi wakiwa ndani ya jumba la makumbusho wakitazama mabaki ya dinosa

      VIJANA HUULIZA

      Uumbaji au Mageuzi?​—Sehemu ya 3: Kwa Nini Uamini Uumbaji?

      “Ikiwa unaamini uumbaji, watu wanaweza kufikiri kwamba wewe ni mjinga, na unashikilia imani za kitoto ulizofundishwa na wazazi wako, au umepumbazwa na dini.”​—Jeanette.

      Je, unahisi kama Jeanette anavyohisi? Ikiwa ndivyo, unaweza kuanza kutilia shaka imani yako katika uumbaji. Kwa kweli, hakuna mtu anayependa kuonwa kuwa mjinga. Ni nini kinachoweza kukusaidia?

      • Mambo yanayofanya iwe vigumu kuamini uumbaji

      • Changanua imani yako

      • Vifaa vya kukusaidia kuchunguza uthibitisho

      • Vijana wenzako wanasema nini

      Mambo yanayofanya iwe vigumu kuamini uumbaji

      1. Ukiamini uumbaji, watu watafikiri unapinga sayansi.

      “Mwalimu wangu alisema kwamba watu wanaoamini uumbaji ni wavivu sana ndio sababu hawawezi kueleza jinsi ulimwengu unavyofanya kazi.”​—Maria.

      Unalopaswa kujua: Walio na maoni kama hayo hawajui ukweli wa mambo. Wanasayansi maarufu kama vile Galileo na Isaac Newton waliamini katika Muumba. Imani yao haikupingana na upendo wao kwa sayansi. Vivyo hivyo, wanasayansi fulani leo hawaoni kwamba sayansi inapingana na imani katika uumbaji.

      Jaribu kufanya hivi: Chapa maneno (kutia ndani alama za kufungua na kufunga semi) “anaeleza kwa nini anamwamini Mungu” katika kisanduku cha kutafuta katika Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO ili upate mifano ya wanatiba na wanasayansi wanaoamini uumbaji. Ona mambo yaliyowasaidia kufikia mkataa huo.

      Jambo kuu: Kuamini uumbaji hakumaanishi kwamba unapinga sayansi. Kwa kweli, kujifunza mengi kuhusu ulimwengu unaotuzunguka kunaweza kuimarisha imani yako katika uumbaji.​—Waroma 1:​20.

      2. Ikiwa unaamini masimulizi ya Biblia ya uumbaji, watu watafikiri una msimamo mkali wa kidini.

      “Watu wengi wanafikiri kwamba kuamini uumbaji ni mzaha tu. Wanahisi kwamba simulizi la kitabu cha Mwanzo ni hadithi tu.”​—Jasmine.

      Unalopaswa kujua: Mara nyingi watu huwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu simulizi la Biblia la uumbaji. Kwa mfano, watu fulani wanaoamini uumbaji wanadai kwamba dunia iliumbwa hivi karibuni au wanadai kuwa kila kitu kilicho hai kiliumbwa katika siku sita zenye saa 24. Biblia haiungi mkono maoni hayo yote.

      • Mwanzo 1:1 husema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Jambo hilo halipingani na uthibitisho wa kisayansi kwamba dunia imekuwapo kwa mabilioni ya miaka.

      • Neno “siku” kama linavyotumiwa katika kitabu cha Mwanzo linaweza kumaanisha vipindi virefu vya nyakati. Kwa kweli, katika Mwanzo 2:4 neno “siku” limetumiwa kufafanua siku zote sita za uumbaji.

      Jambo kuu: Simulizi la Biblia kuhusu uumbaji linapatana na mambo hakika ya kisayansi.

      Changanua imani yako

      Kuamini katika uumbaji hakumaanishi “kuamini jambo bila kufikiri.” Badala yake, kunategemea sababu zenye kusadikisha. Fikiria hili:

      Mambo yote tunayopitia maishani yanakufunza kwamba palipo na ubuni, pana mbuni. Unapoona kamera, ndege, au nyumba, unafikia mkataa sahihi kwamba mtu fulani alivibuni. Kwa nini usifikie mkataa huohuo sahihi unapochunguza jicho la mwanadamu, ndege aliye angani, au sayari yetu Dunia?

      Jambo la kufikiria: Mara nyingi wahandisi huiga mambo wanayoona katika uumbaji ili waboreshe vitu wanavyobuni, nao hudai kwa haki watu watambue kazi zao. Je, ni jambo linalopatana na akili kukubali mbuni wa kibinadamu na kazi zake na bado tusikubali kuwapo kwa Muumba na ubunifu Wake wa hali ya juu sana?

      An airplane and a bird in flight

      Je, ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba ndege ya kubeba abiria ilibuniwa lakini ndege wa angani hakuumbwa?

      Vifaa vya kukusaidia kuchunguza uthibitisho

      Unaweza kuimarisha usadikisho wako katika uumbaji kwa kuchunguza uthibitisho unaopatikana katika vitu vya asili.

      Jaribu kufanya hivi: Chapa maneno (kutia ndani alama za kufungua na kufunga semi) “je, ni kazi ya ubuni?” katika kisanduku cha kutafuta cha Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO. Chagua baadhi ya vichwa vinavyokupendeza kutoka katika mfululizo wa gazeti la Amkeni! wenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?” Katika kila makala, ona jambo la pekee kuhusu uumbaji uliozungumziwa hapo. Jambo hilo linakuthibitishiaje kwamba kuna Mbuni?

      Jifunze zaidi: Tumia broshua zifuatazo kuchunguza zaidi uthibitisho wa uumbaji.

      • Uhai—Ulitokana na Muumba?

        • Dunia iko mahali panapofaa kabisa na imeumbwa kwa njia inayoweza kutegemeza uhai.​—Tazama ukurasa wa 4-​10.

        • Mifano ya ubuni inapatikana katika uumbaji.​—Tazama ukurasa wa 11-​17.

        • Simulizi la kitabu cha Mwanzo lililo katika Biblia linapatana na sayansi.​—Tazama ukurasa wa 24-​28.

      • Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai

        • Uhai haungeweza kutokea tu kutoka katika vitu visivyo hai.​—Tazama ukurasa wa 4-7.

        • Vitu vilivyo hai ni tata sana hivi kwamba haviwezi kujitokeza tu bila mwongozo wowote.​—Tazama ukurasa wa 8-​12.

        • Habari zilizo katika chembe za urithi ni za hali ya juu kuliko teknolojia ya kisasa.​—Tazama ukurasa wa 13-​21.

        • Vitu vyote vilivyo hai havikutoka katika chanzo kimoja cha zamani. Rekodi ya wanyama wa zamani inaunga mkono kutokea kwa ghafla kwa vikundi vikuu vya wanyama, na si kwamba vilitokea hatua kwa hatua.​—Tazama ukurasa wa 22-​29.

      “Ulimwengu unanisadikisha kabisa kwamba kuna Mungu, kuanzia na wanyama duniani hadi katika ulimwengu na utaratibu uliomo.”​—Thomas.

      VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI

      Hannah

      “Nilipojifunza kuhusu utata wa mimea, wanyama, na mwili wa mwanadamu katika somo la sayansi, nilishangaa sana! Sina shaka yoyote kwamba hii ni kazi ya Muumba. Ninafikiri kwamba watu wanaoamini mageuzi ndio ‘wanaoamini mambo bila kufikiri’, si wale wanaoamini uumbaji.”​—Hannah.

      Talia

      “Ninapenda kusoma makala zenye kichwa ‘Je, Ni Kazi ya Ubuni?’ katika gazeti la ‘Amkeni!’. Makala hizo zinanithibitishia kwamba mageuzi si jambo la kweli. Ni kukosa akili kufikiri kwamba kiumbe maridadi kama kipepeo au ndege mvumaji anaweza kutokea kwa aksidenti.”​—Talia.

  • Uumbaji au Mageuzi?—Sehemu ya 4: Ninawezaje Kueleza Imani Yangu Kuhusu Uumbaji?
    Vijana Huuliza
    • Shahidi tineja akiwaeleza wanafunzi wenzake imani yake kuhusu uumbaji

      VIJANA HUULIZA

      Uumbaji au Mageuzi?​—Sehemu ya 4: Ninawezaje Kueleza Imani Yangu Kuhusu Uumbaji?

      Unaamini uumbaji, lakini unaogopa kusema hivyo waziwazi shuleni. Labda vitabu unavyotumia shuleni vinaunga mkono mageuzi na una wasiwasi kwamba walimu na wanafunzi wenzako watakucheka. Unawezaje kueleza kwa ujasiri imani yako kuhusu uumbaji?

      • Unaweza kufaulu!

      • Uwe tayari

      • Vifaa vya kukusaidia kueleza imani yako

      • Vijana wenzako wanasema nini

      Unaweza kufaulu!

      Huenda ukawaza hivi: ‘Mimi siwezi kuzungumzia mambo ya sayansi na mageuzi kwa sababu sijui mambo mengi sana.’ Hivyo ndivyo Danielle alivyohisi pindi fulani. Anasema hivi: “Sikutaka kumpinga mwalimu na wanafunzi wenzangu.” Diana anakubaliana naye. Anasema: “Nilichanganyikiwa watu walipobishana nami kwa kutumia maneno ya kisayansi.”

      Hata hivyo, lengo lako si kushinda mabishano. Na jambo la kupendeza ni kwamba huhitaji kuwa na akili nyingi sana ili ueleze kwa nini inapatana na akili kuamini kwamba ulimwengu uliumbwa.

      Dokezo: Tumia mfano rahisi ulio katika Biblia kwenye Waebrania 3:4: “Kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.”

      Kijana anayeitwa Carol alichanganua wazo hilo hivi kwa kutumia kanuni iliyo katika Waebrania 3:4: “Wazia kwamba unatembea ndani ya msitu mkubwa. Hakuna ishara yoyote kwamba kuna mwanadamu anayeishi karibu. Kisha unatazama chini na kuona kijiti cha kuondolea uchafu kwenye meno. Unafikia mkataa gani? Watu wengi wangesema, ‘Mtu fulani alikuwa hapa.’ Ikiwa kitu kidogo kama kijiti cha kuondolea uchafu kwenye meno ni uthibitisho kwamba kiumbe mwenye akili alikuwa hapo, namna gani ulimwengu na vitu vyote vilivyomo?”

      Mtu akisema: “Ikiwa uumbaji ni jambo la kweli, basi Muumba alitoka wapi?”

      Unaweza kujibu hivi: “Kwa sababu tu hatuelewi kila kitu kumhusu Muumba, hilo halimaanishi kwamba hayupo. Kwa mfano, huenda humjui mtu aliyebuni simu yako ya mkononi, lakini si ni kweli kwamba unaamini ilibuniwa na mtu fulani? [Ruhusu jibu.] “Tunaweza kujua mambo mengi kumhusu Muumba. Ikiwa unataka, ningependa kukuonyesha mambo ambayo nimejifunza kumhusu.”

      Uwe tayari

      Biblia inasema kwamba unapaswa kuwa ‘tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hutaka kutoka kwako sababu ya tumaini lililo ndani yako, lakini ukifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.’ (1 Petro 3:​15) Hivyo, zingatia mambo mawili​—mambo unayosema na jinsi unavyoyasema.

      1. Mambo unayosema. Upendo wako kwa Mungu ni muhimu na unaweza kukuchochea kuwahubiria wengine. Lakini kuwaambia wengine kwamba unampenda Mungu tu huenda kusiwasadikishie kwamba Mungu aliumba vitu vyote. Huenda ikafaa zaidi kutumia mifano inayotokana na uumbaji ili kuonyesha ni kwa nini ni jambo linalopatana na akili kuamini uumbaji.

      2. Jinsi unavyoyasema. Zungumza kwa usadikisho, lakini usiwe mkaidi au mwenye dharau. Inaelekea watu watachochewa kufikiria maoni yako ukizungumza kwa heshima kuhusu imani yao na kukubali kwamba wana haki ya kufikia mikataa yao.

        “Nafikiri ni muhimu kutowashushia heshima wengine au kujionyesha kwamba unajua kila kitu. Hutapata matokeo mazuri ukiongea kwa dharau.”​—Elaine

      Vifaa vya kukusaidia kueleza imani yako

      Msichana tineja akitembea kwenye mvua

      Kuwa tayari kutetea imani yako ni kama kuwa tayari kwa ajili ya mabadiliko ya hali ya hewa

      Tineja mmoja anayeitwa Alicia anasema hivi: “Ikiwa hujajitayarisha, utakaa kimya tu ili kuepuka aibu.” Kama Alicia anavyosema, ni muhimu kujitayarisha ili ufaulu. Jenna anasema hivi, “Ninajihisi nikiwa mtulivu zaidi kuzungumzia uumbaji ikiwa nimetayarisha vizuri mfano rahisi unaounga mkono imani yangu.”

      Unaweza kupata wapi mifano kama hiyo? Vijana wengi wamefanikiwa kwa kutumia vifaa vifuatavyo:

      • Uhai—Ulitokana na Muumba?

      • Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai

      • Maajabu ya Uumbaji Yanafunua Utukufu wa Mungu (video)

      • Mfululizo ulio kwenye gazeti la Amkeni! wenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?” (Chapa maneno hayo [kutia ndani alama za kufungua na kufunga semi] “je, ni kazi ya ubuni?” kwenye sanduku lililoandikwa “tafuta” katika Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO.)

      • Tumia Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO ili kufanya utafiti zaidi.

      Pia, unaweza kufaidika kwa kurudia makala za zamani katika mfululizo wenye kichwa, “Uumbaji au Mageuzi”

      1. Sehemu ya 1: Kwa Nini Nimwamini Mungu?

      2. Sehemu ya 2: Kwa Nini Uchunguze Nadharia ya Mageuzi?

      3. Sehemu ya 3: Kwa Nini Uamini Uumbaji?

      Dokezo: Chagua mifano inayokusadikisha. Itakuwa rahisi kwako kuikumbuka, na utaieleza kwa usadikisho. Jaribu kujizoeza jinsi ya kueleza imani yako.

      VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI

      Brittany

      “Ikiwa tulitokana na mageuzi, basi kwa nini tuna sifa kama vile huruma na upendo? Sifa hizo hufanya uwafikirie wengine badala ya kujifikiria. Kusema kwamba sifa hizo zilijitokeza tu hakupatani na akili.”​—Brittany.

      Breanna

      “Katika somo la biolojia, nilijifunza kuhusu umbo la chembe zetu na jinsi zinavyofanya kazi. Ingawa somo hilo liliunga mkono mageuzi, nilichojifunza kilinisaidia kujua wazi kwamba tumetokana na Chanzo chenye hekima sana.”​—Breanna.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki