-
Nilipata Uradhi Katika Kumtumikia MunguMnara wa Mlinzi—1993 | Februari 1
-
-
Baada ya kumaliza miaka minane ya shule, nilitumwa na baba yangu kwenda Chuo cha Mazoezi Kilnerton, na katika 1935, nikapokea Cheti cha Mwalimu cha Mazoezi ya Miaka Mitatu. Mmoja wa walimu niliyefanya kazi pamoja naye alikuwa mwanamke mchanga, Caroline. Tulioana, na baadaye Caroline akamzaa mtoto msichana tuliyemwita Damaris. Miaka michache baadaye, nikaja kuwa mwalimu mkuu kwenye Shule ya Sehlale katika kijiji cha Mamatsha. Kwa kuwa shule hiyo ilitegemezwa na Dutch Reformed Church, tulijiunga na kanisa hilo, tukihudhuria shughuli kwa ukawaida. Tulifanya hivyo kwa sababu hilo lilikuwa jambo la kimtindo la kufanya, lakini halikuniletea uradhi.
Hatua ya Badiliko
Jumapili moja katika 1942, tulikuwa tukijizoeza nyimbo za dini kanisani wakati kijana mmoja mweupe alipotokea mlangoni akiwa na vitabu vitatu vilivyotangazwa na Watch Tower Society—Creation, Vindication, na Preparation. Nilifikiri vitabu hivyo vingeonekana vizuri kwenye rafu ya maktaba yangu, kwa hiyo nilivikubali kwa shilingi tatu. Baadaye nilipata kujua kwamba mwanamume huyo, Tienie Bezuidenhout, alikuwa ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, wa pekee katika eneo hilo. Katika ziara ya Tienie iliyofuata, alileta gramafoni ili aweze kuwachezea marafiki sahani.
Siku moja nilipitia kurasa za kitabu Creation na kukuta ile sura “Wafu Wako Wapi?” Nilianza kuisoma nikitumaini kujifunza juu ya shangwe zinazofurahiwa mbinguni na nafsi zilizoondoka. Lakini kinyume cha matazamio yangu, kitabu hicho kilitaarifu kwamba wafu wako makaburini mwao na hawajui lolote. Mistari kutoka Biblia, kama vile Mhubiri 9:5, 10, ilinukuliwa ili kuunga mkono hilo. Sura nyingine ilikuwa na kichwa “Kuwaamsha Wafu,” na Yohana 5:28, 29 lilitajwa kuwa uthibitisho wa kwamba wafu hawana fahamu na wanangojea ufufuo. Hilo lilieleweka vizuri. Lilikuwa lenye kuridhisha.
Katika 1942, ndipo nilipokata uhusiano wangu na “Sauti ya Unabii” nikaanza kuwaambia wengine kuhusu yale mambo niliyokuwa nikijifunza kutoka vichapo vya Watch Tower Society. Mmoja wa kwanza kuitikia alikuwa rafiki, Judah Letsoalo, aliyekuwa amekuwa mmoja wa wanadarasa wenzangu kwenye Chuo cha Mazoezi Kilnerton.
Judah na mimi tuliendesha baiskeli mwendo wa kilometa 51 ili kuhudhuria kusanyiko la Mashahidi Waafrika katika Pietersburg. Baadaye, marafiki kutoka Pietersburg mara nyingi walikuja mwendo wote hadi Mamatsha ili kunisaidia niwatolee majirani wangu ujumbe wa Ufalme. Hatimaye, kwenye kusanyiko jingine katika Pietersburg, katika Desemba 1944, nilibatizwa katika kufananisha wakfu wangu kwa Yehova.
Familia Yangu na Wengine Waitikia
Caroline, Priscilla, na binti yangu Damaris, waliendelea kwenda kwenye Dutch Reformed Church. Ndipo msiba ukatokea. Caroline akazaa mtoto wetu wa pili—mtoto mvulana aliyeonekana mwenye afya nzuri tuliyeita Samuel. Lakini akawa mgonjwa ghafula na kufa. Marafiki wa kanisa la Caroline hawakutoa faraja yoyote, wakisema Mungu alimtaka mwana wetu kuwa pamoja na yeye mbinguni. Akisononeka, Caroline aliendelea kuuliza: “Kwa nini Mungu amchukue mwana wetu?”
Habari juu ya msiba wetu ilipowafikia Mashahidi katika Pietersburg, walikuja na kutupa sisi faraja ya kweli iliyotegemea Neno la Mungu. Baadaye Caroline alisema: “Yale ambayo Biblia ilisema juu ya kisababishi cha kifo, juu ya hali ya wafu, na juu ya tumaini la ufufuo yalieleweka vizuri, na nilifarijiwa sana. Nilitaka kuwa katika ulimwengu huo mpya na kumpokea mwana wangu kutoka kaburini.”
Caroline aliacha kwenda kanisani, na katika 1946 yeye, Priscilla, na Judah wakabatizwa. Upesi baada ya ubatizo wake, Judah aliondoka kuanza kazi ya kuhubiri katika eneo la mashambani liitwalo Mamahlola, na hadi siku ya leo yeye anatumikia akiwa mhudumu painia wa wakati wote.
Judah alipoondoka, nilikuwa mwanamume pekee aliyebaki kulitunza kundi letu, lililoitwa Boyne. Ndipo Gracely Mahlatji alipohamia eneo letu, na hatimaye akamwoa, Priscilla. Kila juma, Gracely na mimi tungekuwa na zamu ya kutoa hotuba za watu wote katika Kisepedi, lugha ya kienyeji ya Kiafrika. Ili fasihi ya Biblia iweze kupatikana kwa watu, Sosaiti iliniomba mimi nitafsiri fasihi katika Kisepedi. Kuliniletea uradhi mkubwa kuona watu wakifaidika kutokana na fasihi hiyo.
Ili kuendeleza kampeni yetu ya mkutano wa watu wote, tulinunua gramafoni yenye kikuza sauti kikubwa ili kucheza hotuba za Biblia kotekote katika eneo letu. Tuliazima mkokoteni wenye kuburutwa na punda ili kubeba mahali-mahali mashine hiyo nzito. Likiwa tokeo, majirani wetu walitupatia jina la utani “Watu wa Kanisa la Punda.”
Wakati uo huo kundi letu dogo liliendelea kukua. Hatimaye, dada zangu wawili wenye umri mkubwa zaidi pamoja na waume zao wakaja kuwa Mashahidi na wote walibaki waaminifu hadi vifo vyao. Pia, wengi kutoka kundi la Boyne (linaloitwa Mphogodiba sasa) waliingia kazi ya kutoa evanjeli ya wakati wote, na kadhaa kati yao wangali katika utumishi huo. Sasa, kuna makundi mawili katika eneo hili pana la vijiji vilivyotawanyika, na jumla ya wahubiri zaidi ya 70 ni wenye kutenda katika kazi ya kuhubiri.
Kazi-Maisha Mpya
Katika 1949, niliacha kufundisha shuleni nikawa mhudumu painia wa kawaida. Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa ni kutembelea wafanyakazi vibarua weusi wa mashamba walioishi kwenye mashamba ya watu weupe yaliyozunguka Vaalwater katika Transvaal. Baadhi ya wenye kumiliki mashamba hayo waliunga mkono ile sera ya ubaguzi wa rangi iliyokuwa imeanza kufuatwa karibuni na waliazimia kwamba watu weusi wapaswa watambue eti hali yao ya chini zaidi kuhusiana na watu weupe na wapaswa wawatumikie mabwana wakubwa wao weupe. Kwa hiyo nilipowahubiria wafanyakazi vibarua weusi, watu weupe fulani walinichukua kimakosa kuwa mhubiri wa kutojitiisha. Wengine hata wakanishtaki kuwa Mkomunisti wakatisha kunipiga risasi.
Niliripoti hali hiyo kwa ofisi ya tawi ya Watch Tower Society, na upesi nikahamishwa kwenye mgawo mwingine katika eneo jingine la mashambani liitwalo Duiwelskloof. Karibu na wakati huo mke wangu pia aliacha kazi yake ya kufundisha akajiunga na mimi katika utumishi wa upainia. Alasiri moja katika 1950, tulirudi kutoka utumishi wa shambani tukapata bahasha kubwa kutoka kwa Sosaiti. Kwa mshangao wetu ilikuwa na mwaliko kwangu wa kupokea mazoezi ya kuwa mwangalizi asafiriye. Kwa miaka mitatu tulitembelea makundi katika Afrika Kusini, kisha katika 1953 tukapewa mgawo kwenda Lesotho, nchi iliyo mbali na bahari katikati ya Afrika Kusini.
Huduma Katika Lesotho na Botswana
Tulipoanza kutumikia katika Lesotho, kulikuwako uvumi mwingi kwamba mara nyingi wageni walikuwa ndiyo shabaha ya uuaji wa kidesturi. Mke wangu na mimi sote tulihangaika, lakini upendo wa ndugu zetu Wasotho na ukaribishaji-wageni wao ulitusaidia tusahau hofu hizo.
Ili kutumikia makundi katika Milima ya Maluti ya Lesotho, nilikuwa nikienda kwa ndege, nikimwacha mke wangu katika nyanda za chini alikoendelea katika utumishi wa upainia hadi niliporudi. Marafiki walinisindikiza kwa fadhili kutoka kundi moja hadi jingine ili wanisaidie nisipotee milimani.
Wakati mmoja niliambiwa kwamba ili kufika kwenye kundi lililofuata tungelazimika kuvuka Mto Orange kwa farasi. Nilihakikishiwa kwamba farasi wangu alikuwa mwanana lakini nikaonywa kwamba maji yakiwa yenye nguvu mno, mara nyingi farasi hujaribu kujiondoshea mizigo yao. Nilikuwa na wasiwasi kwa sababu sikuwa mpanda farasi mwenye ujuzi wala mwogelea mwenye ujuzi. Upesi tukawa mtoni, na maji yalifika juu hadi mitandiko ya farasi. Nilihofu sana hivi kwamba niliacha hatamu na kushikilia manyoya ya farasi ya shingoni. Kilikuwa kitulizo kilichoje tulipofika kwa usalama kwenye ukingo ule mwingine!
Usiku huo sikuweza kulala usingizi kwa sababu mwili wangu ulikuwa na maumivu kutokana na kupanda farasi. Lakini maumivu hayo yalistahili, kwa sababu marafiki walionyesha uthamini mwingi kwa ziara hiyo. Nilipoanza kazi ya mzunguko katika Lesotho, kulikuwako kilele cha wahubiri 113. Leo, idadi hiyo imekua kufikia 1,649.
Katika 1956 mgawo wetu wa kuhubiri ulibadilishwa hadi Protektoreti ya Bechuanaland, inayoitwa Botswana sasa. Botswana ni nchi kubwa zaidi, na tulihitaji kusafiri miendo mirefu zaidi ili kuwafikia wahubiri. Tulisafiri ama kwa gari-moshi ama katika lori lililo wazi. Viti havikuwako, kwa hiyo tuliketi sakafuni pamoja na mizigo yetu. Mara nyingi tulifika kituo chetu tukiwa wenye vumbi na kuchoka sana. Ndugu zetu wa Kikristo walitukaribisha sikuzote, na nyuso zao zenye furaha zilituburudisha.
Wakati huo, vichapo vya Sosaiti vilikuwa vimepigwa marufuku katika Botswana, kwa hiyo kuhubiri kwetu nyumba kwa nyumba kulifanywa kwa tahadhari, bila kutumia fasihi ya Sosaiti. Wakati mmoja tulikutwa tukifanya kazi karibu na kijiji cha Maphashalala tukakamatwa. Katika kujitetea wenyewe tulisoma kutoka Biblia, tukirejezea utume wetu kama ilivyorekodiwa kwenye Mathayo 28:19, 20. Ingawa baadhi ya viongozi walivutiwa, chifu alitoa amri kwamba Mashahidi wenyeji wapigwe sana. Halafu, kwa mshangao wetu, kasisi alimsihi chifu awe na huruma atusamehe. Chifu alikubali, tukaachiliwa.
Ujapokuwa mnyanyaso na kupigwa marufuku kwa fasihi yetu, kazi ya Ufalme ilizidi kufanya maendeleo. Nilipofika Botswana, kulikuwako kilele cha wahubiri 154. Miaka mitatu baadaye marufuku ilipoondolewa, idadi hiyo ilikuwa imekua kufikia 192. Leo, kuna Mashahidi wa Yehova 777 wanaohubiri katika bara hilo.
Kufundisha na Kutafsiri
Baada ya wakati fulani, nilitumiwa kuwa mfunzi katika Shule ya Huduma ya Ufalme ya wazee wa Kikristo. Baadaye nilipata pendeleo la kuwa mfunzi katika Shule ya Utumishi wa Painia. Pia mke wangu na mimi tulitumikia katika tawi la Afrika Kusini pindi kwa pindi. Katika pindi hizo nilisaidia kutafsiri, na Caroline alifanya kazi jikoni.
Siku moja katika 1969, mwangalizi wa tawi, Frans Muller, alinikaribia na kusema: “Ndugu Thongoana, ningependa kukuona wewe na mke wako ofisini mwangu.” Humo alieleza kwamba tulikuwa miongoni mwa wale waliochaguliwa kuwa wahudhuriaji kwenye “Amani Duniani” Mkusanyiko wa 1969 katika London. Tulifurahia ule ukaribishaji-wageni wenye upendo wa ndugu zetu katika Uingereza na Scotland, na hilo liliongezea sana uthamini wetu wa udugu wa ulimwenguni pote.
Kwa miongo minne ambayo imepita, Caroline amekuwa mwandamani mwaminifu-mshikamanifu katika kazi-maisha yetu ya watoa evanjeli wa wakati wote. Tumeshiriki pamoja mambo yenye kuleta shangwe na yale yenye kuleta huzuni. Ingawa tuliwapoteza wawili kati ya watoto wetu katika kifo, binti yetu, Damaris, alikua kufikia kuwa Shahidi mzuri na akashiriki pia katika kazi ya utafsiri katika tawi la Afrika Kusini.
Afya yetu haituruhusu tena tushiriki katika kazi ya kusafiri, kwa hiyo kwa muda wa miaka michache ambayo imepita, tumekuwa mapainia wa pekee katika kundi katika Seshego, mji wa Kiafrika karibu na Pietersburg. Natumikia nikiwa mwangalizi-msimamizi. Bibila hutaarifu kwamba “mbele za uso wa [Yehova] ziko furaha tele [kushangilia mpaka kuridhika, NW],” na kwa kweli nimepata shangwe na uradhi nikimtumikia Mungu katika kusini mwa Afrika.—Zaburi 16:11.
-
-
“Habari za Asubuhi! Je, Walijua Jina la Mungu?”Mnara wa Mlinzi—1993 | Februari 1
-
-
“Habari za Asubuhi! Je, Walijua Jina la Mungu?”
IFUATAYO ni barua iliyopokewa kwenye ofisi ya tawi la Mashahidi wa Yehova katika Brazili, kutoka kwa dada wawili walio mapacha wenye miaka 12 katika jiji la Fortaleza:
“Nyuma katika 1990 tulipokuwa katika darasa la tano, shule yetu ilipanga tamasha ya maonyesho ya kisayansi, kisanii, na kitamaduni. Tulimweleza mwalimu wetu kwamba tulitaka wonyesho wetu uwe tofauti na ule ambao wanafunzi wengine walikuwa wanapanga kutayarisha. Kwa kuwa alikuwa ametusikia tukiongea juu ya Yehova na Biblia kabla ya hapo, alidokeza hivi: ‘Basi mwaweza kuandika juu ya Mungu wenu!’
“Tuliona kwamba hiyo ilikuwa fursa ya kutoa ushahidi tukaamua kutayarisha wonyesho wa fasihi ya Biblia inayokazia jina la Yehova. Tulitayarisha nakala kubwa ya maneno ya Zaburi 83:18 tukaiambatisha kwa gundi kwenye picha ya Biblia iliyofunguliwa. Pia, tuliweka kwenye meza tafsiri za Biblia tofauti-tofauti zenye jina la Yehova. Kwenye meza iyo hiyo, tulionyesha fasihi tofauti-tofauti za Biblia. Kwenye mwisho wa meza, tuliweka TV na vidiorekoda ili kuwaonyesha wageni kielelezo kimoja cha mahali ambapo jina la Yehova lilitumiwa katika sinema moja iliyopendwa sana.
“Wakati wa tamasha hiyo ya maonyesho, mtu alipokuja kwenye meza yetu, tulikuwa tukisema: ‘Habari ya asubuhi! Je, walijua jina la Mungu?’ Baada ya kumpa mgeni fursa ya kujibu, tuliendelea hivi: ‘Tazama hapa! Tafsiri kadhaa za Biblia huonyesha kwamba jina lake ni Yehova,’ tukielekeza kwenye jina hilo katika tafsiri tofauti-tofauti, kama zile za João Ferreira de Almeida, The Jerusalem Bible, na New World Translation. Kisha tulichezesha ile mandhari ambayo mwigizaji mkuu wa sinema akazia Yehova kuwa ndilo jina la Mungu. Watu walipoonyesha kupendezwa, tuliwapa gazeti au trakti yenye habari zaidi.
“Mmoja wa vijana waliokuja kwenye meza yetu aliomba kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Mwalimu wetu alichunguza kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha alipaaza sauti hivi: ‘Mamawee! Hiki ni kitabu chenye kupendeza kama nini!’ Kufikia mwisho wa tamasha hiyo ya maonyesho, tulikuwa tumeangusha vitabu 7, trakti 18, na magazeti 67. Tulijishindia mahali pa tatu katika tamasha hiyo ya maonyesho. Lakini zaidi ya hayo yote, tulifurahi sana kuwa na pendeleo la kulijulisha jina la Mungu, Yehova.”
-