Mamilioni Wataelekea Huko—Je, Utajiunga Nao?
◼ Wataelekea wapi? Kwenye Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova la “Ukombozi Unakaribia!” Mamia ya makusanyiko hayo ya siku tatu, ambayo yalianza Marekani mwisho-juma wa mwisho wa Mei, yamepangwa kufanywa katika miezi kadhaa ijayo katika majiji mbalimbali ulimwenguni kote. Karibu watu milioni 11 walihudhuria makusanyiko 2,981 yaliyofanywa hivi majuzi!
Katika sehemu nyingi programu itaanza saa 3:30 asubuhi kwa muziki. Ijumaa, hotuba zifuatazo zitatolewa: “Sikiliza kwa Makini Ahadi za Yehova za Ukombozi” na “Jinsi Ambavyo Yehova Humkomboa ‘Maskini Anayelilia Msaada.’” Kipindi cha asubuhi kitamalizika kwa hotuba ya msingi, “Maandalizi ya Yehova Yatakayotuwezesha Kupata ‘Ukombozi wa Milele.’”
Ijumaa alasiri kutakuwa na hotuba kama vile “Jinsi Yehova Huwatunza Walio Wazee,” “Kukombolewa Kutoka Katika Taabu Zenye Kuumiza,” na “Jinsi Malaika Wanavyotekeleza ‘Utumishi wa Watu Wote.’” Kutakuwa na mfululizo wa hotuba nne wenye kichwa “Yehova—‘Mwokoaji.’” Kisha kutakuwa na hotuba ya mwisho yenye kichwa “Hakuna Silaha Wala Ulimi Unaopinga Utakaofanikiwa.”
Jumamosi asubuhi kutakuwa na mfululizo wa hotuba tatu wenye kichwa “Endelea Katika Huduma ‘Bila Kuacha,’” na vilevile hotuba “Wakombolewa Kutoka Katika Mtego wa Mwindaji wa Ndege” na “Kuchunguza ‘Mambo Mazito ya Mungu.’” Kipindi cha asubuhi kitamalizika kwa hotuba itakayofuatwa na ubatizo wa maji kwa wale wanaostahili.
Jumamosi alasiri kutakuwa na hotuba kama vile “Uwe na Maoni Yanayopatana na Maandiko Kuhusu Matibabu,” “Ni Roho Gani Inayotawala Maisha Yako?,” “Dumisha ‘Kamba Yenye Nyuzi Tatu’ Katika Ndoa,” na “Vijana, ‘Mkumbukeni, Sasa, Muumba Wenu Mkuu.’” Hotuba ya mwisho yenye kichwa, “Je, Unaizingatia Siku ya Yehova Maishani?” itatoa shauri zuri kuhusiana na nyakati tunamoishi.
Jumapili asubuhi kutakuwa na mfululizo wa hotuba wenye kichwa “Ufalme wa Mbinguni Ni Kama . . . ” Hotuba nne za mfululizo huo zitazungumzia kifupi baadhi ya mifano ya Yesu.
Kipindi cha asubuhi kitaendelea kwa hotuba itakayotangulia sehemu muhimu ya kusanyiko, yaani, drama ya nyakati za Biblia inayotegemea kitabu cha Biblia cha Wafalme wa Kwanza sura ya 13. Hotuba ya watu wote yenye kichwa “Ukombozi Kupitia Ufalme wa Mungu Unakaribia!” itatolewa kwenye kipindi cha mwisho cha kusanyiko, Jumapili alasiri.
Fanya mipango sasa ili uhudhurie. Ili kujua mahali ambapo kusanyiko lenu litafanywa, tembelea Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova au waandikie wachapishaji wa gazeti hili. Toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, lina orodha ya mahali ambapo makusanyiko yote yatafanywa nchini Burundi, Kenya, Kongo (Kinshasa), Rwanda, Tanzania, na Uganda.