Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Siri ya 1: Kutanguliza Mambo Yanayofaa
    Amkeni!—2009 | Oktoba
    • Siri ya 1: Kutanguliza Mambo Yanayofaa

      “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.”—Wafilipi 1:10.

      Hilo linahusisha nini? Katika ndoa yenye mafanikio, kila mwenzi hutanguliza mahitaji ya mwenzake badala ya kutanguliza mahitaji, mali, kazi, marafiki, na hata watu wake wa ukoo. Mume na mke hutumia wakati mwingi pamoja na pia wakiwa na watoto wao. Wote wako tayari kujidhabihu kwa faida ya familia yao.—Wafilipi 2:4.

      Kwa nini ni muhimu? Biblia inaonyesha wazi kwamba familia ni muhimu sana. Kwa kweli, mtume Paulo aliandika kwamba mtu ambaye haiandalii familia yake mahitaji yake “ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, huenda maoni ya mtu kuhusu mambo yaliyo muhimu yakabadilika. Kwa mfano, mshauri mmoja wa familia alisema kwamba watu wengi waliohudhuria kongamano aliloandaa walitanguliza hasa kazi zao kuliko familia. Anasema ni kana kwamba walitazamia kujifunza “mbinu za kusuluhisha mambo upesi” ili “washughulikie familia zao upesi na warudi kukazia fikira kazi zao.” Tunajifunza nini? Ni rahisi kusema kwamba tunatanguliza familia yetu kuliko kufanya hivyo.

      Jaribu kufanya hivi. Jaribu kupima familia yako ni ya maana kadiri gani kwako kwa kutumia maswali yafuatayo.

      ◼ Mwenzi au mtoto wangu anapohitaji kuzungumza, je, mimi humkazia uangalifu upesi iwezekanavyo?

      ◼ Ninapozungumza na wengine kuhusu utendaji wangu, je, mara nyingi mimi hujikuta nikizungumzia mambo ambayo mimi hufanya pamoja na familia yangu?

      ◼ Je, ninaweza kukataa madaraka zaidi (kazini au kwingineko) ikiwa familia yangu inahitaji kuwa pamoja nami?

      Ikiwa jibu lako ni ndiyo kwa maswali yaliyo hapo juu, huenda ukasema kwamba unatanguliza mambo muhimu. Lakini mwenzi wako na watoto wako wangesema nini? Si maoni yetu wenyewe yanayoamua ikiwa tunatanguliza mambo muhimu zaidi. Ni hivyo pia kuhusu siri nyingine za kupata mafanikio ambazo zitazungumziwa katika kurasa zinazofuata.

      Azimia. Fikiria njia moja au mbili ambazo unaweza kuonyesha kwamba unatanguliza familia yako. (Kwa mfano: Fikiria jinsi unavyoweza kupunguza mambo yanayochukua wakati ambao ungetumia pamoja na mwenzi wako na watoto wako.)

      Mbona usiwaeleze wengine katika familia mambo ambayo umeazimia kufanya? Mtu mmoja anapoamua kubadilika, huenda wengine wakabadilika pia.

      [Picha katika ukurasa wa 3]

      Mtu mwenye mafanikio hutanguliza mwenzi wake na watoto wake

  • Siri ya 2: Kuwajibika
    Amkeni!—2009 | Oktoba
    • Siri ya 2: Kuwajibika

      “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:6.

      Hilo linahusisha nini? Wenzi wa ndoa wenye mafanikio huona ndoa yao kuwa muungano wa kudumu. Tatizo linapotokea, wao hujaribu kulisuluhisha badala ya kulitumia kama kisababu cha kuvunja ndoa yao. Wenzi wa ndoa wanapowajibika, wao hujihisi salama. Kila mmoja huamini kwamba mwenzake ataendelea kuheshimu ndoa yao.

      Kwa nini ni muhimu? Kwa njia nyingi, kuwajibika ndio msingi wa ndoa. Hata hivyo, baada ya kuzozana mara nyingi, kuwajibika kunaweza kuonekana kama mtego badala ya kuwa jambo la hiari. Kwa sababu hiyo, maneno “mpaka kifo kitutenganishe” huenda yasimaanishe jambo lolote la maana, kwani wenzi wa ndoa wanaweza kuwa wakitafuta visababu vya kutoka kwenye mkataba huo. Huenda wasivunje ndoa yao kihalisi, lakini wanaweza kujitenga kwa njia nyingine. Kwa mfano, wanaweza kunyamaza kimya wakati matatizo mazito yanapohitaji kuzungumziwa.

      Jaribu kufanya hivi. Jaribu kupima unawajibika kadiri gani kwa familia yako kwa kutumia maswali yafuatayo.

      ◼ Tunapozozana, je, mimi hujikuta nikijuta kwamba nilifunga ndoa na mwenzi wangu?

      ◼ Je, mimi hujiwazia nikiwa na mtu mwingine ambaye si mwenzi wangu?

      ◼ Je, nyakati nyingine mimi humwambia mwenzi wangu, “Ninakuacha” au “Nitatafuta mtu anayenithamini”?

      Azimia. Fikiria jambo moja au mawili ambayo unaweza kufanya ili kuwajibika zaidi. (Madokezo: Ili kuonyesha kwamba unamfikiria, mara kwa mara mwandikie mwenzi wako barua fupi, weka picha zake mahali palipo wazi kazini, au mpigie simu kila siku kutoka kazini.)

      Mbona usifikirie mambo mengine kisha umwulize mwenzi wako ni mambo gani ambayo yatampendeza zaidi?

      [Picha katika ukurasa wa 4]

      Kuwajibika kunalinda ndoa yako kama tu vyuma vilivyo kando ya barabara vinavyolinda magari yasitoke barabarani

      [Hisani]

      © Corbis/age fotostock

  • Siri ya 3: Kushirikiana
    Amkeni!—2009 | Oktoba
    • Siri ya 3: Kushirikiana

      “Wawili ni afadhali kuliko mmoja . . . Mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.”—Mhubiri 4:9, 10.

      Hilo linahusisha nini? Wenzi wa ndoa wenye mafanikio huheshimu mpango wa Mungu wa ukichwa unaotajwa katika Biblia. (Waefeso 5:22-24) Isitoshe, mume na mke hutumia maneno kama vile “yetu” na “sisi” badala ya “yangu” na “mimi.” Kunapokuwa na ushirikiano, mume na mke hawajifikirii tena kuwa waseja. Wao ni “mwili mmoja,” maneno ambayo Biblia inatumia kuonyesha uhusiano wa karibu na wenye kudumu wa ndoa.—Mwanzo 2:24.

      Kwa nini ni muhimu? Ikiwa wewe na mwenzi wako hamshirikiani, mambo madogo yanaweza kuwa makubwa huku kila mmoja akimshambulia mwenzake badala ya kushughulikia tatizo linalowakabili. Lakini ikiwa wewe na mwenzi wako mnashirikiana, mnakuwa kama marubani wawili wanaoshirikiana kuendesha ndege ileile badala ya marubani wawili walio katika ndege mbili tofauti zilizo karibu kugongana. Mnapokosa kuelewana, mnatafuta masuluhisho yanayofaa badala ya kupoteza wakati na nguvu za kihisia kwa kulaumiana na kushtakiana.

      Jaribu kufanya hivi. Jaribu kupima unashirikiana kadiri gani na mwenzi wako kwa kutumia maswali yafuatayo.

      ◼ Je, mimi huona pesa ninazochuma kuwa “zangu,” kwa kuwa mimi ndiye niliyezichuma?

      ◼ Je, mimi hujitenga na watu wa ukoo wa mwenzi wangu, hata ingawa yeye ana uhusiano wa karibu nao?

      ◼ Ili nipumzike kabisa, je, mimi huhitaji kujitenga na mwenzi wangu?

      Azimia. Fikiria njia moja au mbili ambazo unaweza kuonyesha kuwa unashirikiana na mwenzi wako.

      Mbona usimwulize mwenzi wako madokezo?

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Kushirikiana kunamaanisha ninyi ni marubani wawili wanaoshirikiana kuendesha ndege ileile

  • Siri ya 4: Kuheshimiana
    Amkeni!—2009 | Oktoba
    • Siri ya 4: Kuheshimiana

      “Kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.”—Waefeso 4:31.

      Hilo linahusisha nini? Familia zenye matatizo na hata zile zilizofanikiwa huwa na hali ya kutoelewana. Lakini familia zenye mafanikio huzungumzia mambo bila kutumia kejeli, matusi, na maneno mengine yenye kuudhi. Watu katika familia hizo hutendeana kama wanavyotaka watendewe.—Mathayo 7:12.

      Kwa nini ni muhimu? Maneno yanaweza kuwa silaha na kuwaumiza sana wengine. Methali moja ya Biblia inasema: “Afadhali kuishi jangwani, kuliko kukaa na mwanamke mgomvi na msumbufu.” (Methali 21:19, Biblia Habari Njema) Bila shaka, inaweza kusemwa hivyo kumhusu mwanamume mgomvi. Na Biblia inasema hivi kuwahusu wazazi: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.” (Wakolosai 3:21) Watoto wanaochambuliwa kila wakati wanaweza kuhisi kwamba haiwezekani kuwafurahisha wazazi wao. Wanaweza kukata tamaa kabisa.

      Jaribu kufanya hivi. Jaribu kupima kiwango cha heshima katika familia yako kwa kutumia maswali yafuatayo.

      ◼ Katika familia yangu, je, ni kawaida kwa mtu mmoja kuondoka chumbani kwa hasira kunapokuwa na hali ya kutoelewana?

      ◼ Ninapozungumza na mwenzi wangu au mtoto wangu, je, mimi hutumia yenye matusi, kama vile “mjinga,” “mpumbavu,” au maneno kama hayo?

      ◼ Je, nililelewa katika mazingira ambayo watu walizoea kutumia matusi?

      Azimia. Fikiria jambo mmoja au mawili unayoweza kufanya ili kuonyesha heshima unapozungumza. (Dokezo: Azimia kusema “mimi” badala ya “wewe.” Kwa mfano, “Mimi hujihisi nimeumia unapo . . . ,” badala ya “Kila wakati wewe . . . ”)

      Mbona usimwambie mwenzi wako mambo unayopanga kufanya ili kuonyesha heshima zaidi? Baada ya miezi mitatu, mwulize mwenzi wako ikiwa anaona mabadiliko yoyote.

      Fikiria mipaka ambayo unaweza kujiwekea ili usitumie matusi unapozungumza na watoto wako.

      Mbona usiwaombe watoto wako msamaha kwa pindi ambazo huenda ulizungumza nao kwa hasira au kwa kejeli?

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Kama tu mawimbi ya bahari yanavyoweza kumomonyoa miamba migumu, ndivyo mazoea ya kutumia maneno yenye kuumiza yanavyoweza kudhoofisha familia

  • Siri ya 5: Kuwa na Usawaziko
    Amkeni!—2009 | Oktoba
    • Siri ya 5: Kuwa na Usawaziko

      “Usawaziko wenu na ujulikane.”—Wafilipi 4:5.

      Hilo linahusisha nini? Katika familia zilizofanikiwa, waume na wake husameheana. (Waroma 3:23) Pia, wao si wakali mno kwa watoto wao wala hawawaendekezi. Wao huweka sheria zenye usawaziko nyumbani. Marekebisho yanapohitajiwa, wao huyatoa “kwa kiwango kinachofaa.”—Yeremia 30:11.

      Kwa nini ni muhimu? Biblia inasema kwamba “hekima inayotoka juu ni . . . yenye usawaziko.” (Yakobo 3:17) Mungu hatarajii ukamilifu kutoka kwa wanadamu wasio wakamilifu, kwa hiyo kwa nini wenzi wa ndoa watarajie ukamilifu kutoka kwa wenzi wao? Kwa kweli, kuchambuana kuhusu mambo madogo-madogo hutokeza chuki. Hakuboreshi hali. Ni vizuri kukubali kwamba “sisi sote hujikwaa mara nyingi.”—Yakobo 3:2.

      Wazazi wenye mafanikio huwa wenye usawaziko wanaposhughulika na watoto wao. Hawapiti kiasi wanapotoa nidhamu wala si “wagumu kupendeza.” (1 Petro 2:18) Wao huwapa uhuru vijana wanaonyesha kwamba wanaweza kuaminika. Hawajaribu kudhibiti mambo madogo-madogo. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba kujaribu kudhibiti kila jambo maishani mwa kijana ni kama “kucheza kwa fujo dansi yenye kuchosha ukijaribu kuomba mvua inyeshe. Mvua haitanyesha, lakini wewe utachoka sana.”

      Jaribu kufanya hivi. Pima una usawaziko kadiri gani kwa kujibu maswali yafuatayo.

      ◼ Ni lini mara ya mwisho ulipompongeza mwenzi wako?

      ◼ Ni lini mara ya mwisho ulipomchambua mwenzi wako?

      Azimia. Ikiwa haikuwa rahisi kwako kujibu swali la kwanza lakini ilikuwa rahisi kujibu la pili, fikiria jambo unaloweza kufanya ili uwe na usawaziko zaidi.

      Mbona usizungumze na mwenzi wako kuhusu maazimio mnayoweza kujiwekea?

      Fikiria uhuru ambao unaweza kumpa kijana wako ikiwa ameonyesha kwamba anaweza kuaminika.

      Mbona usizungumze waziwazi na kijana wako kuhusu mambo kama vile wakati anaopaswa kurudi nyumbani?

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Kama dereva mwangalifu alivyo tayari kuwapisha wengine, mtu wa familia mwenye usawaziko yuko tayari kukubali maoni ya wengine

  • Siri ya 6: Kusameheana
    Amkeni!—2009 | Oktoba
    • Siri ya 6: Kusameheana

      “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.”—Wakolosai 3:13.

      Hilo linahusisha nini? Wenzi wenye mafanikio hujifunza kutokana na mambo ambayo walifanya zamani; lakini hawaweki hesabu ya mambo mabaya waliyofanyiwa na kuyatumia kutilia chumvi kasoro za wenzi wao kwa kusema, “Wewe huchelewa kila wakati” au “Wewe siku zote hunisikilizi.” Wenzi wote wawili huona kwamba “ni jambo lenye kupendeza [mtu] anapopita kosa.”—Methali 19:11.

      Kwa nini ni muhimu? Mungu ‘yuko tayari kusamehe,’ lakini nyakati nyingine wanadamu hawafanyi hivyo. (Zaburi 86:5) Ikiwa mizozano ya zamani haitasuluhishwa, inaweza kutokeza chuki ambayo mwishowe itafanya iwe vigumu sana kusamehe. Huenda kila mwenzi akakataa kuzungumza kuhusu hisia zake na wakati uleule hajali hisia za mwenzake. Wote wanahisi wamenaswa katika ndoa isiyo na upendo.

      Jaribu kufanya hivi. Tazama picha zako na za mwenzi wako mlizopigwa mwanzoni mwa ndoa yenu au wakati wa uchumba. Jaribu kuamsha tena upendo mliokuwa nao kabla ya matatizo kuanza na kuwapofusha. Kisha fikiria kuhusu sifa ambazo zilikuvutia kwa mwenzi wako.

      ◼ Ni sifa zipi za mwenzi wako ambazo sasa zinakuvutia sana?

      ◼ Fikiria jinsi unavyoweza kuwaathiri watoto wako kwa njia nzuri kwa sababu ya kuwa mtu mwenye kusamehe.

      Azimia. Fikiria njia moja au mbili ambazo unaweza kutumia ili usihusishe mizozo ya wakati uliopita mnapozozana tena.

      Mbona usimwambie mwenzi wako ni sifa gani alizo nazo zinazokuvutia?—Methali 31:28, 29.

      Fikiria jinsi unavyoweza kuwafundisha watoto kusamehe.

      Mbona usizungumze na watoto wako kuhusu kusamehe na jinsi sifa hiyo inavyomnufaisha kila mtu katika familia?

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Unaposamehe, deni linafutwa. Usidai tena ulipwe

  • Siri ya 7: Kuweka Msingi Imara
    Amkeni!—2009 | Oktoba
    • Siri ya 7: Kuweka Msingi Imara

      Hilo linahusisha nini? Jengo lolote imara linahitaji kuwa na msingi imara, na ndivyo ilivyo na familia zenye nguvu. Familia zenye nguvu hazivumilii matatizo bila jitihada zozote, kama tu vile nyumba haiendelei kusimama kwa miaka mingi bila kuwa na msingi imara. Familia zenye mafanikio zimejengwa juu ya mwongozo unaofaa.

      Kwa nini ni muhimu? Vitabu vingi, magazeti, na programu za televisheni hutoa mashauri mengi kuhusu maisha ya familia. Washauri fulani wa ndoa wanaweza kuwahimiza wenzi wa ndoa wenye matatizo waendelee kuishi pamoja, huku wengine wakiwashauri watengane. Hata wataalamu hubadili maoni yao kuhusu mambo ya familia. Kwa mfano, mnamo 1994 mshauri mmoja maarufu ambaye hushughulika na matatizo ya vijana wanaobalehe aliandika kwamba alipoanza kufanya kazi hiyo, alihisi kwamba “ni afadhali watoto waishi pamoja na mzazi mmoja mwenye furaha badala ya kuishi na wazazi waliooana wasio na furaha. Nilidhani kwamba talaka ndilo suluhisho linalofaa badala ya kuwa katika ndoa yenye matatizo.” Hata hivyo, baada ya kufanya kazi hiyo kwa miaka 20, alibadili maoni yake. Alisema hivi: “Talaka huwaumiza watoto wengi.”

      Maoni hubadilika, lakini ushauri bora zaidi unaoweza kupatikana lazima uwe unapatana kwa njia fulani na kanuni za Neno la Mungu, Biblia. Ulipokuwa ukisoma makala hizi, huenda umeona kwamba kuna kanuni fulani ya Biblia iliyoandikwa juu kwenye ukurasa wa 3-8. Kanuni hizo zimesaidia familia nyingi kufanikiwa. Kama tu familia nyingine zote, familia zilizofanikiwa pia huwa na matatizo. Tofauti ni kwamba Biblia imewasaidia wawe na msingi imara kwa ajili ya ndoa na familia. Tungetazamia Biblia iandae msingi huo kwa sababu Mtungaji wake, Yehova Mungu, ndiye Mwanzilishi wa familia.—2 Timotheo 3:16, 17.

      Jaribu kufanya hivi. Andika orodha ya maandiko yaliyonukuliwa juu kwenye ukurasa wa 3 hadi wa 8. Andika maandiko mengine ambayo yamekusaidia. Weka orodha hiyo mahali inapoweza kupatikana kwa urahisi na usome maandiko hayo mara kwa mara.

      Azimia. Azimia kutumia Biblia katika maisha ya familia yako.

      [Picha katika ukurasa wa 8, 9]

      Familia yako ikiwa na msingi imara wa Kimaandiko, inaweza kushinda dhoruba zinazoihatarisha

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki