Maoni ya Wazazi
Miaka ya kubalehe huwaletea wazazi wengi magumu mpya. Ni kwa njia gani unaweza kumsaidia mtoto wako afaulu kupitia kipindi hiki kigumu maishani—ambacho huenda kinaweza kuwa chenye kutatanisha kwake kama kilivyo kwako? Ona mambo ambayo wazazi fulani kutoka sehemu zote ulimwenguni wamesema.
MABADILIKO
“Mwanangu alipokuwa mchanga, alikuwa akikubali mashauri yangu bila ubishi. Lakini alipofikia umri wa utineja, alianza kutilia shaka mamlaka yangu. Alishuku mambo niliyoyasema na jinsi nilivyoyasema.”—Frank, Kanada.
“Mvulana wangu haongei sana kama zamani. Ni lazima nimuulize anafikiria nini badala ya kungoja anieleze. Si rahisi kumfanya akupe jibu. Atajibu—lakini si upesi.”—Francis, Australia.
“Subira ni muhimu sana. Nyakati nyingine, tunaweza kushawishiwa kuwafokea watoto wetu, lakini inafaa zaidi tunapojituliza kwanza kisha tunazungumza nao!” —Felicia, Marekani.
MAWASILIANO
“Nyakati nyingine, binti yangu huwa na mwelekeo wa kujitetea, na wakati mwingine anafikiria ninamwonea. Ni lazima nimkumbushe kwamba ninampenda, na kwamba ninajaribu kumsaidia na ningependa afanikiwe!”—Lisa, Marekani.
“Watoto wangu walipokuwa wachanga, walikuwa tayari kujieleza. Ilikuwa rahisi kujua mambo wanayofikiria. Lakini sasa lazima niwaelewe na niwaonyeshe kuwa ninawaheshimu. Hiyo ndiyo njia pekee inayoweza kufanya wanieleze yaliyo moyoni.”—Nan-hi, Korea.
“Haitoshi tu kuwazuia vijana wasifanye mambo fulani. Ni lazima tuwaeleze sababu zetu na tuwe na mazungumzo yatakayogusa mioyo yao. Tukitaka kuwachochea wajieleze, ni lazima tuwe tayari kusikiliza chochote watakachosema, hata kama ni mambo ambayo hatutaki kuyasikia.”—Dalila, Brazili.
“Ikiwa ni lazima nimtie nidhamu binti yangu, mimi hujaribu kufanya hivyo faraghani, badala ya mbele ya watu wengine.”—Edna, Nigeria.
“Nyakati nyingine ninapozungumza na kijana wangu, ninaanza kukengeushwa na shughuli nyingine za nyumbani na sikazii fikira anachosema. Anatambua hilo mara moja na nafikiri hiyo ni sababu moja inayomfanya asizungumze na mimi mara nyingi. Ninahitaji kumsikiliza kwa makini zaidi tunapoongea ili aendelee kujieleza.”—Miriam, Mexico.
KUJITEGEMEA
“Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kuwapa vijana wangu uhuru zaidi, na hilo limesababisha matatizo kati yetu. Tulizungumzia jambo hilo waziwazi pamoja. Niliwaeleza kwa nini nilikuwa na hofu, nao wakanieleza kwa nini walitaka kuwa na uhuru zaidi. Tulikubaliana kwamba wangeweza kuwa na uhuru zaidi lakini wasivuke mipaka niliyowawekea.” —Edwin, Ghana.
“Mwana wangu alitaka pikipiki. Sikukubaliana kabisa na wazo hilo na bila hata kumpa nafasi ya kutoa maoni yake, nilimkemea na kumtajia madhara yote ya kununua pikipiki. Jambo hilo lilimkasirisha na akaazimia hata zaidi kununua pikipiki! Niliamua kutumia mbinu nyingine. Nilimtia moyo kijana wangu afanye utafiti kuhusu jambo hilo, achunguze hatari, gharama, na matakwa ya kupata na kuandikisha upya leseni ya pikipiki. Nilimwambia pia atafute ushauri kutoka kwa Wakristo wakomavu kutanikoni. Nilikuja kugundua kwamba badala ya kumnyima uhuru, ni afadhali kama ningemtia moyo awe huru kueleza yaliyo moyoni mwake. Kwa njia hiyo, ningeufikia moyo wake.”—Hye-young, Korea.
“Tuliweka mipaka, lakini hatua kwa hatua tuliwapa uhuru. Kadiri walivyotumia uhuru huo vizuri, ndivyo walivyopata uhuru zaidi. Tuliwapa nafasi ya kupata uhuru zaidi, na tukawaonyesha kwamba tulitaka waweze kuupata; lakini hatukukosa kutoa nidhamu walipotumia uhuru huo vibaya.”—Dorothée, Ufaransa.
“Sikulegeza viwango vyangu. Lakini watoto wangu walipokuwa watiifu, nilikuwa tayari kuwaruhusu wafanye mambo fulani. Kwa mfano, mara kwa mara ningewaruhusu warudi nyumbani saa zikiwa zimesonga kuliko kawaida. Lakini kama wangerudi nyumbani wakiwa wamechelewa zaidi ya mara moja, wangelipia kosa hilo.” —Il-hyun, Korea.
“Kadiri mfanyakazi anavyokuwa mtiifu na kuwajibika, ndivyo mwajiri wake anavyompa madaraka zaidi. Vivyo hivyo, mwanangu anaweza kuona kwamba kadiri anavyotii na kuhakikisha kwamba hapiti mipaka tuliyomwekea, ndivyo anavyopata uhuru zaidi. Mwanangu anajua kwamba kama vile mfanyakazi anavyoadhibiwa asipotimiza majukumu yake, anaweza pia kupoteza uhuru wake iwapo hatakuwa mwenye kuwajibika.”—Ramón, Mexico.
[Blabu katika ukurasa wa 22]
“Mfunze mtoto namna ya kuishi vizuri, naye hatasahau njia hiyo hata uzeeni.”—Methali 22:6, Biblia Habari Njema
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]
MASIMULIZI YA FAMILIA
“Kuwalea Vijana Wanaobalehe Ni Jambo Zuri Ajabu”
Joseph: Binti zangu wawili wakubwa wana umri wa miaka 17 na 13, na ninaona ni muhimu kuwasikiliza na kukubali maoni yao. Kukubali udhaifu wangu—na kuwaheshimu binti zangu ninapoongea nao—husaidia tuweze kuwasiliana vizuri zaidi. Kwa ufupi, ninahisi kwamba kuwalea vijana wanaobalehe ni jambo zuri ajabu, hasa kwa sababu ya mwongozo tunaopata katika Neno la Mungu, Biblia.
Lisa: Niligundua kwamba binti yetu mkubwa alipoanza kubalehe, alihitaji nitumie wakati mwingi zaidi naye. Ninakumbuka nikitumia wakati wangu mwingi sana kumsikiliza, kuzungumza naye, na kumtia moyo. Mimi na mume wangu tunahakikisha binti zetu wanajua kwamba wanaweza kutuambia jambo lolote na tutaheshimu maoni yao. Ninajaribu kufuata shauri lenye hekima la Yakobo 1:19, linalotuambia tuwe ‘wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema.’
Victoria: Mama yangu ndiye rafiki yangu mkubwa zaidi. Sijawahi kukutana na mtu yeyote aliye mzuri na anayejali kuliko yeye—naye humtendea kila mtu hivyo. Ninahisi kwamba mama yangu anawajali watu wengine kikweli. Siwezi kupata mama mwingine kama huyu.
Olivia: Baba yangu anawajali watu wengine na ni mkarimu. Yeye huwa tayari sikuzote kuwasaidia wengine kimwili hata wakati ambapo familia yetu ina uhitaji. Anajua jinsi ya kuchukua mambo kwa uzito, lakini pia anajua kufurahia maisha kwelikweli. Yeye ni baba wa pekee, na ninafurahi sana kwamba yeye ni baba yangu!
“Hatuna Wakati wa Kuchoshwa na Maisha!”
Sonny: Binti zetu wanapokuwa na tatizo, tunaketi tukiwa familia na kulizungumzia. Kila mmoja wetu hujieleza waziwazi, na maamuzi tunayofanya yanategemea kanuni za Biblia. Mimi na Ynez tunajaribu kuhakikisha kwamba binti zetu wana marafiki wazuri waliokomaa kiroho. Rafiki zetu ni rafiki zao, na rafiki zao ni wetu pia.
Ynez: Sisi huwa na mengi ya kufanya, na tunafanya mambo yote tukiwa familia. Kwa kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova, tunashiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri, funzo la kibinafsi na la familia, na kujitolea kufanya kazi nyingine—kutia ndani kutoa msaada wakati wa misiba na ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Tunasawazisha mambo yote hayo na tafrija. Hatuna wakati wa kuchoshwa na maisha!
Kellsie: Baba yangu ni msikilizaji mzuri, na sikuzote yeye hutafuta maoni ya familia yote kabla ya kufanya uamuzi mzito. Mama yangu yuko tayari kunisikiliza ninapohitaji msaada—au mtu wa kuzungumza naye.
Samantha: Mama yangu hunifanya nijihisi kuwa mtu wa pekee sana, anayependwa, na wa maana sana—hata kama yeye hatambui jambo hilo. Yeye hunisikiliza na ananijali. Nisingependa kubadilisha urafiki wetu na kitu kingine chochote.
[Picha]
Familia ya Camera: Joseph, Lisa, Victoria, Olivia, na Isabella
Familia ya Zapata: Kellsie, Ynez, Sonny, na Samantha
[Picha katika ukurasa wa 22]
Wazazi wanaweza kutoa uhuru kwa kiasi fulani, ingawa pia wanaweka mipaka yenye usawaziko