-
Pata KichocheoAmkeni!—2012 | Oktoba
-
-
Pata Kichocheo
Ili uchochewe kufanya jambo lolote, lazima uone jinsi jambo hilo litakavyokufaidi.
SHULE ina faida gani? Itakusaidia kupata hekima, na Biblia inasema kwamba “hekima ni ulinzi.” (Mhubiri 7:12) Jinsi gani? Ili kuelewa jambo hilo, wazia unatembea katika mtaa hatari. Ungependelea nini—kutembea ukiwa peke yako au ukiwa na kikundi cha marafiki ambao hali fulani ikitokea watakulinda? Ukiwa na elimu nzuri, ni kana kwamba una “marafiki” wengi wenye nguvu kando yako kila wakati. Marafiki hao wanatia ndani:
Uwezo wa kufikiri. Kwenda shuleni kunaweza kukusaidia kusitawisha kile ambacho Biblia inakiita “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.” (Methali 3:21) Kupata stadi hizo kutakusaidia kutatua matatizo yako badala ya kuwatazamia wengine kila mara wakusaidie.
Uwezo wa kushirikiana na wengine. Biblia inawahimiza Wakristo wakuze sifa kama vile ustahimilivu na kujizuia. (Wagalatia 5:22, 23) Kuchangamana na watu wa aina mbalimbali shuleni kunakupa fursa nyingi za kukuza sifa hizo pamoja na sifa nyingine kama vile uvumilivu, heshima, na hisia-mwenzi—sifa ambazo zitakusaidia sana utakapokuwa mtu mzima.
Stadi utakazotumia maishani. Shule inaweza kukufundisha umuhimu wa kuwa na mazoea mazuri ya kufanya kazi, ambayo yatakusaidia kupata kazi na kuidumisha. Pia, kadiri unavyojifunza mengi kuhusu ulimwengu unaokuzunguka, ndivyo unavyojielewa vizuri na kujua mambo yaliyo muhimu kwako. (Methali 14:15) Ukiwa na usadikisho huo, utaweza kutetea kwa heshima mambo unayoamini.—1 Petro 3:15.
Jambo kuu: Kwa kuwa unahitaji elimu, hutapata faida yoyote kwa kukazia fikira mambo ambayo unachukia kuhusu shule. Badala yake, jitie motisha kwa kufikiria vichochezi vilivyotajwa hapo juu. Huenda hata ukafikiria vichochezi vingine vingi!
Anza sasa! Fikiria jambo linalokuchochea zaidi wewe utake kufanikiwa shuleni.
-
-
Fanya Mambo kwa UtaratibuAmkeni!—2012 | Oktoba
-
-
Fanya Mambo kwa Utaratibu
Unahitaji tu jitihada kidogo ili kupanga mambo kwa utaratibu, lakini unaweza kupata faida nyingi kama vile, kuokoa wakati, kutokuwa na mkazo sana, na kupata alama za juu.
WAZIA umeenda dukani kununua kitu fulani, lakini bidhaa zote zimewekwa ovyoovyo bila mpangilio wowote. Utatumia muda gani kupata kitu unachotaka? Je, haingekuwa rahisi kukipata ikiwa bidhaa zingekuwa zimepangwa kwa utaratibu na vijia vyote vya duka hilo viwe na vibandiko vinavyoonekana waziwazi? Unaweza kutumia utaratibu huohuo kuhusu mambo yako ya shule. Jinsi gani?
Panga ratiba.
“Pindi moja nilisahau kabisa kufanya kazi zangu za shuleni na pia nikasahau kufanya kazi nilizopewa nyumbani kwa sababu nilienda kumtembelea rafiki yangu mwisho juma wote,” anasema Zachary, mwenye umri wa miaka 18, anayeishi Marekani. “Jumatatu, niliwasihi sana walimu wangu wanipe muda wa kumaliza kazi zangu za shule. Sasa mimi huandika orodha ya mambo ya kufanya ili niyakumbuke.”
Kuandika orodha ya mambo ya kufanya pia kumemsaidia Celestine, mwanamke anayeishi Papua New Guinea. Anasema hivi kuhusu wakati alipokuwa shuleni: “Niliandika ratiba ya utendaji wangu wote, kutia ndani kazi za shule, mitihani, na tafrija. Kufanya hivyo kulinisaidia kujua mambo ya kutanguliza na kufanya mambo kwa wakati.”
Dokezo: Andika mambo unayotaka kufanya kwenye kijitabu kidogo, au kwenye simu yako ya mkononi au kifaa kingine cha kielektroniki.
Usiahirishe.
Ni rahisi kusema, “Nitafanya jambo hilo baadaye.” Ni afadhali kufanya mambo mapema iwezekanavyo—hasa kazi za shule.
Dokezo: Uwe na zoea la kufanya kazi za shule mara tu ufikapo nyumbani, kabla ya kuwasha televisheni au kujihusisha katika burudani nyingine yoyote.
Panga vifaa vyako vya shule.
Umewahi kufika shuleni na kugundua kwamba umesahau kitabu au kalamu? Unaweza kuepuka tatizo hilo. Jinsi gani? “Sikuzote mimi huweka vifaa vyangu vya shule kwenye mkoba wangu mapema,” anasema Aung Myo Myat, kijana anayeishi Myanmar.
Dokezo: Weka mkoba wako wa shule ukiwa nadhifu na panga vitu kwa utaratibu ili iwe rahisi kupata kitu unachotaka.
Jambo kuu: Kufanya mambo kwa utaratibu kutakusaidia usisahau vitu, usichelewe, na uwe na wakati wa kutosha wa kufanya mambo mengine yaliyo muhimu.
Anza sasa! Fikiria sehemu ambayo wewe unahitaji kuwa na utaratibu. Kisha mwombe mzazi au rafiki madokezo ya jinsi ya kuboresha sehemu hiyo.
-
-
Omba MsaadaAmkeni!—2012 | Oktoba
-
-
Omba Msaada
Kuwa na watu wanaoweza kukushauri na kukutegemeza ni muhimu sasa ukiwa shuleni na pia itakuwa muhimu hata zaidi utakapokuwa mtu mzima.
NI NANI wanaoweza kukusaidia ufanikiwe shuleni?
Familia.
“Nilipohitaji kusaidiwa kufanya kazi zangu za shuleni,” anasema Bruna, msichana mwenye umri wa miaka 18 anayeishi Brazili, “Baba yangu alinifafanulia habari hiyo, kisha akaniuliza maswali ambayo yalinisaidia kufikiri na kujipatia jibu mimi mwenyewe.”a
Dokezo: Anza kwa kumwuliza mzazi wako alifanyaje katika somo unaloliona kuwa gumu. Ikiwa alifanya vizuri, huenda akakusaidia.
Walimu.
Walimu wengi hufurahi kujua kwamba mwanafunzi anataka kufanikiwa, na hawatasita kumsaidia.
Dokezo: Unaweza kumwambia hivi mwalimu wako, “Naona somo hili kuwa gumu, na ninataka kufanikiwa. Ungependekeza nifanye nini?”
Washauri.
Labda rafiki wa familia mwenye kutegemeka anaweza kukusaidia. Kuwa na mshauri kunaweza kuwa na manufaa mara mbili: Kwanza, utapata msaada unaohitaji; na pili, utajifunza kutafuta msaada kutoka kwa watu wengine unapouhitaji—jambo ambalo litakusaidia hata katika maisha ya utu uzima. Kwa kweli, ili mtu afanikiwe katika mambo mengi, badala ya kujitegemea tu, anahitaji msaada wa watu wengine.—Methali 15:22.
Dokezo: Waulize wazazi wako ni nani anayeweza kuwa mshauri mzuri.
Jambo kuu: Usiogope kuomba msaada!
Anza sasa! Andika majina ya watu wawili au watatu ambao ungependa kuwaiga—watu ambao unawaheshimu. Je, kuna yeyote kati yao anayeweza kukusaidia na kazi zako za shule?
[Maelezo ya Chini]
a Kaka au dada yako mkubwa anaweza kukusaidia pia.
-
-
Tunza Afya YakoAmkeni!—2012 | Oktoba
-
-
Tunza Afya Yako
Kutunza afya yako kunaweza kuboresha utendaji wako shuleni na pia kuboresha maisha yako.
NI JAMBO linalopatana na akili kutunza mwili ambao Mungu alikupa. (Zaburi 139:14) Kwa mfano: Wazia kwamba una gari, lakini hulitunzi. Muda si muda, gari hilo litaharibika. Jambo hilohilo linaweza kutukia kwa mwili wako. Mwili wako unahitaji utunzaji wa aina gani?
Pumzika.
Kukosa kulala vya kutosha kunaweza kukufanya uonekane mnyonge, ujihisi mchovu, umechanganyikiwa, na hata umeshuka moyo. Tofauti na hilo, unapopumzika vya kutosha, unakuwa na nguvu nyingi. Pia kupumzika vya kutosha kunaweza kufanya ukue haraka, uboreshe utendaji wa ubongo wako, uimarishe mfumo wako wa kinga, na uboreshe hali yako ya kihisia. Bila shaka, utapata faida nyingi kwa kufanya jambo hilo linalohitaji jitihada ndogo tu!
Dokezo: Ikiwezekana, jaribu kulala saa zilezile kila usiku.
Vyakula.
Vijana hukua haraka. Kwa mfano, katika kipindi cha kati ya umri wa miaka 10 na 17, uzito wa mwili wa wavulana wengi huongezeka maradufu. Wasichana pia hukua haraka katika kipindi hicho. Miili inayokua inahitaji chakula kingi chenye lishe na kinachoupa mwili nguvu. Hakikisha kwamba unakula vizuri.
Dokezo: Usikose kula kiamsha-kinywa. Kula kiamsha-kinywa kabla ya kwenda shule kunaweza kukusaidia ukaze fikira zaidi na kuboresha kumbukumbu yako.
Mazoezi.
Biblia inakubali kwamba “mazoezi ya mwili yana faida.” (1 Timotheo 4:8, Biblia Habari Njema) Yanaweza kuimarisha misuli na mifupa, kufanya uwe na nguvu, kudhibiti uzito wako, kuongeza uwezo wako wa akili, kuboresha mfumo wako wa kinga, kupunguza mkazo, na kuboresha hali yako ya kihisia. Bila shaka, kufanya mazoezi kunaweza kufurahisha kwa kuwa unaweza kutia ndani utendaji ambao wewe hufurahia!
Jambo kuu: Kulala vya kutosha, kula vyakula vyenye lishe, na kufanya mazoezi ya kiasi kutasaidia mwili wako ufanye kazi inavyofaa. Na hilo litaboresha utendaji wako darasani.a
Anza sasa! Panga ratiba inayofaa ya kufanya mazoezi. Chunguza mazoea yako ya kulala na ya kula kwa mwezi mmoja kisha uone mahali unapohitaji kufanya marekebisho.
“Ninapofanya mazoezi ya kutembea, mimi hupata nguvu zaidi—hata kama nilikuwa mchovu nilipoanza mazoezi.”—Jason, New Zealand.
“Mimi ninafikiri kwamba Mungu aliumba chakula kiwe kama petroli kwa miili yetu, nami ninataka kutia petroli bora zaidi katika mwili wangu!”—Jill, Marekani.
“Mimi hufanya mazoezi ya kukimbia mara tatu kwa juma, na ninafanya mazoezi ya kuendesha baiskeli au kutembea mara mbili kwa juma. Mazoezi hunipa nguvu zaidi na kupunguza mkazo.”—Grace, Australia.
a Kwa habari zaidi kuhusu afya yako, ona sura ya 10 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Uwe na LengoAmkeni!—2012 | Oktoba
-
-
Uwe na Lengo
Shule inakuwa na maana zaidi—na inafurahisha zaidi—unapojua elimu inakufaidi kwa njia gani.
KWENDA shule bila kuwa na lengo lolote ni kama kukimbia mbio zisizo na mwisho. Biblia inasema hivi: “Jua unakoelekea.” (Methali 4:26, Contemporary English Version) Kuwa na lengo kutakufanya ukazie fikira jambo hususa na kutarahisisha mambo utakapoanza kufanya kazi. Unawezaje kujiwekea lengo?
Jiulize, ‘Ninapanga kujiruzuku kwa njia gani?’ Usiahirishe kujibu swali hilo. Badala yake, anza kufanya mipango mapema. Kwa nini? Linganisha jambo hilo na mfano huu: Ukitaka kwenda safari, kwanza lazima uamue unataka kwenda wapi. Kisha ukitumia ramani, utaamua ni njia ipi itakayokusaidia kufika huko kwa urahisi. Unaweza kutumia mbinu hiyo kuhusu elimu yako. Fikiria kazi unayotaka kufanya, na kisha uchague masomo yatakayokusaidia kufika unakoelekea.
Tahadhari: Vijana wengi wanataka kufanya kazi wanazopenda tu—kwa mfano wanataka kuwa wanamuziki maarufu—hivi kwamba hawataki kufikiria kufanya kazi nyingine. Ni njia gani bora zaidi ya kuchagua kazi?
Fikiria uwezo wako. Kwa mfano, je, wewe hufurahia kazi za kuwahudumia wengine? Je, wewe ni stadi katika umekanika? hesabu? uhasibu? au kurekebisha vitu?
Chunguza kazi ulizochagua. Ni kazi gani zinazopatana zaidi na uwezo wako? Badala ya kukazia fikira kazi moja tu ambayo unaiona kuwa ndiyo “inayofaa zaidi,” zungumzia kazi nyingine zinazofaa pamoja na watu wengine. Na uone mambo kihalisi. Kwa mfano, je, kazi unayotaka inaweza kupatikana katika maeneo mengine, ikiwa wakati mmoja utahama? Je, masomo unayohitaji kwa ajili ya kazi hiyo yatakuingiza katika deni kubwa?
Chunguza nafasi zilizopo. Baada ya kuamua ni kazi gani ungependa kufanya, chunguza ikiwa kuna nafasi za kuajiriwa katika eneo unamoishi. Unajua watu wowote wanaoweza kukuajiri? Ikiwa ndivyo, je, wao humwajiri mtu wakiwa na lengo la kumfunza mtu kazi hiyo? Je, kuna programu za kupata mazoezi ya kiufundi?
Dokezo: Waulize wazazi, walimu, na watu wazima walio marafiki wako. Chunguza nafasi za kazi zilizoorodheshwa kwenye magazeti au sehemu nyingine.
Jambo kuu: Ukiwa na lengo, elimu yako itakuwa na mwelekeo na kusudi.
Anza sasa! Ukiwa bado shuleni, fikiria kuhusu mambo matatu yaliyozungumziwa hapo juu. Andika malengo yako, na uyazungumzie pamoja na wazazi wako.
-