Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ni Nini Chanzo cha Ugomvi Katika Familia?
    Amkeni!—2015 | Desemba
    • Watoto wanahuzunishwa wanaposikia wazazi wakibishana

      HABARI KUU | KUDUMISHA AMANI NYUMBANI

      Ni Nini Chanzo cha Ugomvi Katika Familia?

      “KAWAIDA sisi hugombana kuhusu pesa,” anasema Sarah,a anayeishi nchini Ghana, na ambaye aliolewa na Jacob miaka 17 iliyopita. Anaeleza hivi: “Kinachonikasirisha ni kwamba mimi hufanya mengi sana ili kuitunza familia yangu lakini Jacob hanihusishi anapofanya maamuzi kuhusu pesa. Majuma kadhaa yanaweza kupita bila sisi kuzungumza.”

      Mume wake anayeitwa Jacob anasema hivi: “Ndiyo, kuna nyakati ambapo tunarushiana maneno makali. Hilo hutokea kwa sababu ya kutoelewana na kutowasiliana. Pia, mizozo hiyo hutokea kwa sababu ya kukasirika kupita kiasi hali fulani zinapotokea.”

      Nathan, aliyefunga ndoa hivi karibuni nchini India, anaeleza jinsi hali ilivyokuwa baba-mkwe wake alipomfokea mama-mkwe. Nathan anasema hivi: “Mama-mkwe alikasirika sana akatoka nje. Nilipomwuliza kwa nini alimfokea, baba-mkwe alinigeukia akifikiri ninamtukana. Ghafla sisi sote tukaanza kufokewa.”

      Huenda hata wewe umejionea jinsi maneno fulani yanayosemwa wakati usiofaa au ambayo hayajachaguliwa vizuri yanavyoweza kutokeza mzozo mkubwa nyumbani. Watu waliokuwa wakijadiliana kwa utulivu wanaweza ghafla kuanza kurushiana maneno. Kwa kuwa hakuna mtu anayeweza kuzungumza kwa njia inayofaa kila wakati, ni rahisi sana kuelewa vibaya maneno au nia ya mwenzako. Hata hivyo, inawezekana kuwa na amani na umoja.

      Unaweza kufanya nini mabishano makali yanapotokea? Unaweza kuchukua hatua gani ili kudumisha amani na utulivu katika familia? Familia zinaweza kudumishaje amani nyumbani? Tafadhali endelea kusoma.

      a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

  • Jinsi ya Kukomesha Mizozo Nyumbani
    Amkeni!—2015 | Desemba
    • Mume anamsikiliza mke wake akieleza hisia zake

      HABARI KUU | KUDUMISHA AMANI NYUMBANI

      Jinsi ya Kukomesha Mizozo Nyumbani

      UFANYE nini ikiwa inaonekana kwamba mizozo katika familia yako haiishi? Huenda mizozo hiyo imekuwa mibaya zaidi na inatukia mara nyingi zaidi. Labda hata hujui chanzo cha ugomvi huo. Lakini bado mnapendana na hamtaki kuumizana.

      Ni muhimu kukumbuka kwamba kwa kuwa tu mna maoni yanayotofautiana, haimaanishi kwamba familia yenu inasambaratika. Kinachoamua ikiwa nyumba yenu itakuwa na amani au la, si ugomvi wenyewe bali ni jinsi mnavyoushughulikia. Fikiria hatua zifuatazo zinazoweza kuwasaidia kukomesha mizozo.

      1. ACHA KULIPIZA KISASI.

      Ili kuwe na mabishano, lazima kuwe na watu wawili wanaozungumza. Lakini mmoja anaponyamaza na kusikiliza badala ya kuzungumza, mabishano huisha. Kwa hiyo, epuka kumjibu mwenzako unapokasirishwa. Dumisha heshima yako kwa kujizuia. Kumbuka, kuwa na amani katika familia ni muhimu zaidi kuliko kushinda mabishano.

      “Pasipo na kuni moto huzimika, na pasipo na mchongezi ugomvi hutulia.”​—Methali 26:20.

      2. ELEWA HISIA ZA WENGINE KATIKA FAMILIA.

      Kumsikiliza mwenzako kwanza kwa makini ukiwa na hisia-mwenzi bila kumkatiza au kumhukumu kunaweza kutuliza hasira na kudumisha amani. Badala ya kumshuku mwenzako, tambua hisia zake. Usifikiri ana nia mbaya wakati amekosea tu kwa sababu ya kutokamilika. Huenda akasema maneno yenye kuudhi bila kufikiri au kwa sababu ameumizwa hisia na si kwa sababu ana kinyongo au analipiza kisasi.

      “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.”​—Wakolosai 3:12.

      3. JIPATIE NAFASI YA KUTULIA.

      Ukikasirika, huenda ikafaa uondoke kwa busara ili utulie kidogo. Unaweza kwenda kwenye chumba kingine au ukatembee hadi utakapokuwa sawa. Kufanya hivyo si sawa na kumnyamazia mwenzako. Badala yake, huenda ni nafasi nzuri ya kusali ili Mungu akupe subira, ufahamu, na uelewaji.

      “Kabla mabishano hayajalipuka, jiondokee.”​—Methali 17:14.

      4. FIKIRIA KWA MAKINI NI NINI KINACHOHITAJI KUSEMWA NA JINSI YA KUKISEMA.

      Hakuna faida ya kutafuta maneno ya kujibizana na mwenzako. Badala yake, jaribu kusema jambo litakalotuliza hisia zilizoumizwa za mpendwa wako. Na badala ya kumwamulia mwenzako hisia zake, mwombe ajieleze na umshukuru kwa kukusaidia kuelewa hisia zake.

      “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.”—Methali 12:18.

      5. ZUNGUMZA KWA SAUTI YA CHINI NA KWA NJIA INAYOONYESHA UNATAFUTA MAPATANO.

      Mtu mmoja katika familia anapokosa subira anaweza kuamsha hasira ya mwenzake. Epuka kejeli, matusi, au kuzungumza kwa sauti ya juu, hata ikiwa unahisi umekosewa. Epuka kuwalaumu wengine kwa kusema mambo kama vile “Wewe hunijali” au “Wewe hunisikilizi kamwe.” Badala yake, mweleze mwenzi wako kwa utulivu jinsi ambavyo mwenendo wake ulivyokuathiri (“Ninaumia unapo . . . ”). Hupaswi kamwe kumsukuma mwenzako, kumpiga kofi, teke, au kumtendea kwa jeuri ya aina nyingine. Pia, hupaswi kumtukana, kumdhihaki, au kumtisha mwenzi wako.

      “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.”—Waefeso 4:31.

      6. OMBA MSAMAHA UPESI NA UELEZE UTAKACHOFANYA ILI KUREKEBISHA HALI.

      Usiache hisia zisizofaa zikufanye usahau kwamba lengo lako kuu ni kufanya amani. Kumbuka kwamba hamfaidiki mkilumbana. Lakini mkifanya amani, nyote wawili mnafaidika. Kwa hiyo, kubali kosa lako. Hata ikiwa unasadiki kwamba hujakosea, unaweza kuomba msamaha kwa sababu ya kukasirika, kwa kutenda kwa njia isiyofaa, au kwa kumkasirisha mwenzako bila kukusudia. Kudumisha amani kati yenu ni muhimu kuliko kushinda bishano. Na ukiombwa msamaha, uwe tayari kusamehe.

      “Nenda ujinyenyekeze na kumsihi sana mwenzako.”—Methali 6:3.

      Bishano linapokwisha, unaweza kufanya nini ili kuchangia amani ya familia? Jambo hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

  • Jinsi ya Kuchangia Amani Katika Familia
    Amkeni!—2015 | Desemba
    • HABARI KUU | KUDUMISHA AMANI NYUMBANI

      Jinsi ya Kuchangia Amani Katika Familia

      JE, UNAFIKIRI Biblia inaweza kukusaidia kuchangia amani katika familia yako? Tafadhali linganisha kile ambacho Biblia inasema na mambo ambayo watu waliohojiwa walisema yamewasaidia. Chunguza mambo ambayo yanaweza kukusaidia kuepuka mizozo, kudumisha amani, na kuimarisha uhusiano wenu.

      KANUNI ZA BIBLIA ZINAZOCHANGIA AMANI

      UWE NA MTAZAMO UNAOFAA KUMWELEKEA MWENZAKO.

      Familia ikitumia wakati pamoja ufukweni

      “Bila kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mkiwaona wengine kuwa ni bora kuliko ninyi, mkiendelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.”—Wafilipi 2:3, 4.

      “Tumejionea kwamba ni vizuri kumwona mwenzi wako kuwa muhimu kuliko unavyojiona au unavyowaona wengine.”—C. P., aliyefunga ndoa miaka 19 iliyopita.

      SIKILIZA KWA MAKINI NA BILA KUKATA KAULI MAPEMA.

      “Endelea kuwakumbusha . . . wasiwe wataka-vita, wawe wenye usawaziko, wakionyesha upole wote kuelekea watu wote.”—Tito 3:1, 2.

      “Unapomjibu mwenzi wako kwa ukali unatokeza uhasama wa aina fulani kati yenu. Ni muhimu kuheshimu maoni yake na kumsikiliza bila kumhukumu hata ikiwa hukubaliani naye.”—P. P., aliyefunga ndoa miaka 20 iliyopita.

      UWE MWENYE SUBIRA NA UPOLE.

      “Kwa subira kiongozi hushawishiwa, na ulimi wa upole unaweza kuvunja mfupa.”—Methali 25:15.

      “Mizozo itatokea, lakini matokeo hutegemea roho unayoonyesha. Tunahitaji kuwa na subira. Tunapofanya hivyo, tumegundua kwamba mambo hutatuliwa.”—G. A., aliyefunga ndoa miaka 27 iliyopita.

      USIMPIGE MWENZAKO WALA KUMRUSHIA MANENO.

      “Yaondoleeni mbali mambo haya yote kutoka kwenu, ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu.”—Wakolosai 3:8.

      “Ninamheshimu sana mume wangu kwa uwezo wake wa kujizuia. Sikuzote yeye huwa mtulivu na hanigombezi wala kunitukana.”—B. D., aliyefunga ndoa miaka 20 iliyopita.

      UWE TAYARI KUSAMEHE NA KUTATUA MIZOZO UPESI.

      “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”—Wakolosai 3:13.

      “Unapokabili hali ngumu, si rahisi nyakati zote kuwa mtulivu na unaweza kusema au kufanya mambo ambayo yatamuumiza mwenzi wako. Nyakati kama hizo, inafaa sana kusamehe. Huwezi kuwa na ndoa nzuri bila kumsamehe mwenzako.”—A. B., aliyefunga ndoa miaka 34 iliyopita.

      UWE NA MAZOEA YA KUTOA BILA KUTAZAMIA KUPEWA.

      “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. . . . Kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi pia.”—Luka 6:38.

      “Mume wangu anajua kinachonipendeza naye sikuzote hunifanyia mambo bila mimi kutazamia. Kwa sababu hiyo, nyakati zote mimi hujiuliza, ‘Ninaweza kufanya nini ili nimfurahishe?’ Hilo limefanya tuwe na pindi nyingi za kucheka pamoja, hadi leo.”—H. K., aliyefunga ndoa miaka 44 iliyopita.

      USICHOKE KUENDELEZA AMANI NYUMBANI

      Watu hao waliohojiwa na mwandishi wa Amkeni! wanatoka katika familia mbalimbali ambazo zimesaidiwa na Biblia kusitawisha sifa zinazochangia amani nyumbani.a Hata ikiwa baadhi ya watu katika familia zao hawaendelezi amani, wao wamejionea faida ya kuendelea kujitahidi kufanya amani, kwa kuwa Biblia inaahidi: “Wanaoshauri amani wanashangilia.”—Methali 12:20.

      a Kwa habari zaidi kuhusu jinsi unavyoweza kuwa na familia yenye furaha, ona sura ya 14 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova na kinapatikana kwenye www.jw.org/sw. Pia tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki