-
Je, Ulimwengu Umepoteza Mwelekeo Au La?Amkeni!—2017 | Na. 6
-
-
HABARI KUU | JE, ULIMWENGU UMEPOTEZA MWELEKEO?
Je, Ulimwengu Umepoteza Mwelekeo Au La?
MWANZONI mwa mwaka wa 2017 wanasayansi walitoa tangazo lenye kuogopesha. Mwezi Januari, kikundi cha wanasayansi kilitangaza kwamba ulimwengu umekaribia kupatwa na janga kubwa zaidi kuwahi kutokea. Wakitumia Saa ya mfano ya Maangamizi inayoonyesha jinsi wanadamu ulimwenguni pote wanavyokaribia kuangamia, wanasayansi walisogeza mbele mshale wa dakika wa saa hiyo kwa sekunde 30. Saa hiyo inaonyesha kwamba sasa hivi bado dakika mbili na nusu tu kabla ya saa sita usiku, kumaanisha kwamba ulimwengu umekaribia sana kuangamia kuliko wakati mwingine wowote kwa zaidi ya miaka 60 iliyopita!
Mwaka wa 2018, wanasayansi wanapanga kufanya uchunguzi tena ili kuona tumekaribia kwa kadiri gani mwisho wa ulimwengu. Je, Saa ya Maangamizi bado itaonyesha kwamba tumekaribia janga kubwa ambalo halijawahi kutokea? Una maoni gani? Je, ulimwengu umepoteza mwelekeo? Huenda swali hilo likaonekana kuwa gumu kwa sababu hata wataalamu wenyewe hawakubaliani kuhusu jambo hilo. Si kila mtu anayeamini kwamba kuna siku isiyoepukika ya maangamizi.
Kwa kweli, mamilioni ya watu wanaamini kwamba kutakuwa na maisha mazuri wakati ujao. Wanasema kwamba wana uthibitisho unaoonyesha kuwa wanadamu na dunia yetu itadumu milele na kwamba maisha yetu yataboreka. Je, uthibitisho huo unaaminika? Je, ulimwengu umepoteza mwelekeo au la?
-
-
Kutafuta MajibuAmkeni!—2017 | Na. 6
-
-
HABARI KUU | JE, ULIMWENGU UMEPOTEZA MWELEKEO?
Kutafuta Majibu
IKIWA una wasiwasi au hofu kwa sababu ya kusikia habari nyingi mbaya, hauko peke yako. Mwaka wa 2014, Barack Obama, aliyekuwa rais wa Marekani, alisema habari nyingi mbaya zinazoripotiwa zimefanya wengi wafikiri kwamba “ulimwengu unazunguka . . . kwa kasi sana na hakuna anayeweza kuudhibiti.”
Hata hivyo, muda mfupi baada ya kusema maneno hayo aliongea kwa shauku kuhusu mbinu zilizopo zinazoweza kutatua matatizo mengi ulimwenguni. Aliita mipango fulani ya serikali “habari njema” na kusema ana “matumaini thabiti” na ana “uhakika hali zitakuwa nzuri.” Kwa maneno mengine, alionyesha kwamba wanadamu wakiwa na nia njema wanaweza kuudhibiti ulimwengu kwa jitihada zao wenyewe na hivyo kuepuka maangamizi.
Wengi wana mtazamo kama wake. Kwa mfano, baadhi ya watu wanategemea sayansi, wakifikiri kwamba kutakuwa na maendeleo makubwa ya teknolojia yatakayoondoa matatizo ulimwenguni. Mtaalamu mmoja wa teknolojia alitabiri kwa uhakika kwamba kufikia mwaka wa 2030, “teknolojia yetu itakuwa yenye nguvu mara elfu moja zaidi na kufikia 2045, itakuwa yenye nguvu mara milioni moja zaidi.” Aliongezea hivi: “Tunaendelea vizuri sana. Ingawa matatizo tunayokabili ni makubwa sana, uwezo wetu wa kuyasuluhisha unazidi kuongezeka.”
Kihususa hali za ulimwengu ni mbaya kadiri gani? Je, kweli ulimwengu unakaribia kupatwa na maangamizi makubwa? Licha ya habari zenye tumaini zinazotolewa na baadhi ya wanasayansi na wanasiasa, watu wengi bado wana mashaka kuhusu wakati ujao. Kwa nini?
SILAHA ZINAZOWEZA KUSABABISHA MAAFA MAKUBWA. Licha ya jitihada nyingi, Umoja wa Mataifa na mashirika mengine umeshindwa kudhibiti utengenezaji wa silaha za nyuklia. Badala yake, viongozi washupavu wanakaidi sheria za kudhibiti silaha. Nchi zenye historia ya kutengeneza silaha za nyuklia zinaboresha silaha zao za zamani na kutengeneza nyingine zenye uwezo mkubwa zaidi. Nchi ambazo hazikuwa na uwezo wa kutengeneza silaha za maangamizi, sasa zina uwezo wa kuangamiza idadi kubwa sana ya watu.
Hali hii ya kujitayarisha kwa ajili ya vita vya nyuklia haijawahi kuonekana, na inafanya dunia iwe mahali hatari sana pa kuishi, hata wakati wa “amani.” Gazeti moja (Bulletin of the Atomic Scientists) linaonya hivi: “Kuwepo kwa silaha hatari sana zinazojiongoza zenyewe na zinazoweza kusababisha mauaji bila mwelekezo na usimamizi wa mwanadamu ni jambo linaloogopesha.”
AFYA YETU IMO HATARINI. Sayansi haiwezi kutatua matatizo yetu yote ya afya. Shinikizo la damu, kunenepa kupita kiasi, uchafuzi wa hewa, na matumizi ya dawa za kulevya ni mambo hatari yanayosababisha magonjwa na yanazidi kuongezeka. Watu wengi zaidi wanakufa kutokana na magonjwa mbalimbali yasiyo ya kuambukiza, kama vile, kansa, magonjwa ya moyo, na kisukari. Na wengine wengi wanazidi kuathiriwa na magonjwa mengine kama vile ugonjwa wa akili. Pia, katika miaka ya karibuni kumekuwa na milipuko ya magonjwa hatari ya kuambukiza kama vile virusi vya Ebola na Zika. Ukweli ni kwamba wanadamu hawawezi kudhibiti magonjwa, na inaonekana hakuna tumaini lolote kwamba watayakomesha.
WANADAMU WANAHARIBU MAZINGIRA. Viwanda vinaendelea kuharibu anga la dunia. Mamilioni ya watu hufa kila mwaka kwa sababu ya kupumua hewa chafu.
Watu mmoja mmoja, vikundi vya watu, na mashirika ya serikali yanaendelea kumwaga maji taka, kutupa takataka za hospitalini na za kilimo, plastiki, na takataka nyingine baharini. Kitabu kimoja (Encyclopedia of Marine Science) kinasema hivi: “Takataka hizo zenye sumu huathiri viumbe na mimea ya baharini na pia wanadamu wanaokula viumbe na mimea hiyo.”
Pia, maji safi yanapungua. Robin McKie, mwanasayansi Mwingereza ambaye ni mwandishi anaonya hivi: “Kuna upungufu wa maji ulimwenguni ambao utaathiri kila sehemu ya dunia.” Wanasiasa wanakiri kwamba upungufu huo wa maji umesababishwa hasa na wanadamu na hilo limeleta hatari kubwa.
WANADAMU WANAATHIRIWA NA MAJANGA YA ASILI. Dhoruba, vimbunga, tufani, na matetemeko ya ardhi husababisha mafuriko makubwa, maporomoko ya ardhi, na uharibifu mwingine. Leo, kuliko wakati mwingine wowote, watu wengi zaidi wanakufa au kuathiriwa kabisa na majanga hayo ya asili. Utafiti uliofanywa na Shirika la Marekani la Usimamizi wa Anga unaonyesha kuna uwezekano mkubwa kwamba kutakuwa na “dhoruba kali zaidi, joto kali kupita kiasi, na vipindi visivyo vya kawaida vya ukame na mafuriko.” Je, majanga ya asili yatawaangamiza wanadamu?
Bila shaka unaweza kuwazia mambo mengine mabaya yanayohatarisha uhai wetu. Hata hivyo, hutapata majibu yenye kuridhisha kuhusu wakati ujao kwa kuchanganua mambo yote mabaya yanayotokea leo. Huenda wengine wakawa na maoni kama hayo wanapowasikiliza wanasiasa na wanasayansi. Ingawa hivyo, kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, watu wengi wamepata majibu yanayosadikisha ya maswali kuhusu hali za ulimwengu na wakati ujao. Majibu hayo yanapatikana wapi?
-
-
Biblia Inasema Nini?Amkeni!—2017 | Na. 6
-
-
Utabiri wa Saa ya Maangamizi hautatimia kwa sababu Mungu anaahidi kwamba hali ya dunia na wanadamu itakuwa nzuri wakati ujao
HABARI KUU | JE, ULIMWENGU UMEPOTEZA MWELEKEO?
Biblia Inasema Nini?
KARNE nyingi zilizopita, Biblia ilitabiri kwamba kungekuwa na hali mbaya duniani. Kwa kuongezea, Biblia ilitabiri kihususa pia kwamba hatimaye wanadamu watakuwa na maisha mazuri wakati ujao. Yale ambayo Biblia inasema hayapaswi kupuuzwa kwa sababu mambo mengi sana ambayo ilitabiri tayari yametimia kikamili.
Kwa mfano, fikiria unabii ufuatao wa Biblia:
“Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine.”—Mathayo 24:7.
“Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:1-4.
Unabii huo unaelezea kuhusu ulimwengu ambao huenda watu fulani wakasema umepoteza mwelekeo. Kwa njia fulani, ulimwengu wetu umepoteza mwelekeo—wanadamu hawana uwezo wa kuudhibiti. Biblia inasema kwamba wanadamu hawana hekima wala uwezo wa kuleta suluhisho la kudumu. Maandiko yafuatayo yanaonyesha jambo hilo:
“Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.”—Methali 14:12.
“Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—Mhubiri 8:9.
“Mwanadamu . . . hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.
Ikiwa wanadamu wangeachwa waendelee kufanya chochote wanachotaka, inaelekea kwamba ulimwengu ungeangamia. Lakini jambo hilo halitatukia! Kwa nini? Kwa sababu Biblia inasema:
Mungu “ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.”—Zaburi 104:5.
“Kizazi kinaenda, kizazi kinakuja; lakini dunia inasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Mhubiri 1:4.
“Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29.
“Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” —Zaburi 72:16.
Mafundisho hayo ya Biblia yanatupatia majibu ya wazi kabisa. Jamii ya wanadamu haitaangamizwa na uchafuzi wa mazingira, ukosefu wa chakula na maji, au ugonjwa fulani wenye kuenea duniani pote. Ulimwengu hautaangamizwa na vita vya nyuklia. Kwa nini? Kwa sababu wakati ujao wa ulimwengu wetu uko mikononi mwa Mungu. Ni kweli kwamba Mungu amewaruhusu wanadamu watumie uhuru wao wa kuchagua. Hata hivyo, watavuna matokeo ya matendo yao. (Wagalatia 6:7) Ulimwengu si kama treni iliyopoteza mwelekeo na inayoelekea kuanguka na kuharibika kabisa. Mungu ameweka mipaka au kikomo kuhusiana na uharibifu ambao wanadamu wanaweza kusababisha.—Zaburi 83:18; Waebrania 4:13.
Lakini Mungu atafanya mengi zaidi. Ataleta “wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Mambo mazuri yaliyozungumziwa katika makala hii ni kionjo tu cha maisha bora ya wakati ujao ambayo mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wamejifunza kuyahusu katika Biblia.
Mashahidi wa Yehova ni kikundi cha ulimwenguni pote cha wanaume na wanawake wa umri mbalimbali kutoka katika makabila tofauti-tofauti. Wanamwabudu Mungu wa kweli anayeitwa Yehova katika Biblia. Hawaogopi mambo yatakayotokea wakati ujao kwa sababu Biblia inasema hivi: “Kwa maana Yehova, Muumba wa mbingu, Yeye Mungu wa kweli, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu, amesema hivi: ‘Mimi ni Yehova, wala hakuna mwingine.’”—Isaya 45:18.
Makala hii imezungumzia baadhi ya mafundisho ya Biblia kuhusu wakati ujao wa dunia na wanadamu. Unaweza kupata habari zaidi katika somo la 5 la broshua Habari Njema Kutoka Kwa Mungu! iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova na inayopatikana kwenye tovuti ya www.jw.org/sw
Unaweza pia kutazama video yenye kichwa Kwa Nini Mungu Aliumba Dunia? kwenye tovuti ya www.jw.org/sw. (Tafuta kwenye MACHAPISHO > VIDEO)
-