-
KunyakuliwaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Mtu Akisema—
‘Je, unaamini kwamba watu watanyakuliwa?’
Unaweza kujibu hivi: ‘Nimeona kwamba watu wana maoni mbalimbali kuhusu maana ya kunyakuliwa. Maoni yako ni nini kuhusu jambo hilo? . . . Kuhusu jambo lolote, inafaa kulinganisha maoni yetu na mambo ambayo Biblia yenyewe inasema. (Tumia baadhi ya habari zilizo juu zinazohusu jambo hilo.)’
Au unaweza kusema: ‘Watu wamenieleza kwamba kunyakuliwa ni njia ambayo Wakristo watatumia kukimbia. Wengi wana maoni kwamba watatumia njia hiyo ili kuikimbia dhiki kuu inayokuja. Je, hayo ndiyo maoni yako?’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Bila shaka sisi tunataka Mungu atulinde wakati huo, nami nimetiwa moyo sana na maandiko fulani yanayoonyesha jinsi tunavyoweza kupata ulinzi huo. (Sef. 2:3)’ (2) ‘Jambo la kupendeza ni kwamba, Biblia inaonyesha kwamba Mungu atawalinda waaminifu fulani hapa hapa duniani. (Met. 2:21, 22) Hilo linapatana na kusudi la Mungu alipomuumba Adamu na kumweka katika Paradiso, sivyo?’
Pia unaweza kusema: ‘Unaposema kunyakuliwa, je, unamaanisha kwamba Wakristo wanaoishi wakati wa mwisho wa ulimwengu watachukuliwa waende mbinguni? . . . Je, umewahi kujiuliza watafanya nini watakapofika mbinguni? . . . Ona mambo ambayo andiko la Ufunuo 20:6 (na 5:9, 10) linasema. . . . Lakini watatawala nani? (Zab. 37:10, 11, 29)’
-
-
Kurudi kwa KristoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Kurudi kwa Kristo
Maana: Kabla ya kuondoka duniani, Yesu Kristo aliahidi kurudi. Matukio yenye kusisimua kuhusiana na Ufalme wa Mungu yanahusianishwa na ahadi hiyo. Tunapaswa kukumbuka kwamba kuna tofauti kati ya kuja na kuwapo. Kwa hiyo, ingawa kuja kwa mtu (kunakohusianishwa na kufika au kurudi kwake) kunatukia katika wakati fulani, huenda kuwapo kwake baada ya hapo kukaendelea kwa kipindi cha miaka kadhaa. Katika Biblia neno la Kigiriki erʹkho·mai (linalomaanisha “kuja”) linatumiwa pia kumhusu Yesu akielekeza fikira kwenye kazi muhimu katika kipindi hususa wakati wa kuwapo kwake, yaani, kazi yake aliyopewa na Yehova ya kuwaangamiza waovu kwenye vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.
Je, matukio yanayohusianishwa na kuwapo kwa Kristo yanatukia katika wakati mfupi sana au kwa kipindi cha miaka kadhaa?
Mt. 24:37-39: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo [“kuja,” UV, BHN, ZSB; Kigiriki, pa·rou·siʹa] kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. Kwa maana kama vile walivyokuwa katika siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Matukio ya “siku za Noa” yanayosimuliwa hapa yalitukia kwa kipindi cha miaka mingi. Yesu alilinganisha kuwapo kwake na yale yaliyotukia wakati huo.)
Katika Mathayo 24:37 neno la Kigiriki pa·rou·siʹa linatumiwa. Kihalisi maana yake ni “kuwa kando ya.” Kamusi Greek-English Lexicon (Oxford, 1968) ya Liddell na Scott inatoa “kuwapo, kwa watu,” kuwa maana ya kwanza ya pa·rou·siʹa. Maana ya neno hilo inaonyeshwa waziwazi katika Wafilipi 2:12, ambapo Paulo anatofautisha kuwapo kwake (pa·rou·siʹa) na kutokuwapo kwake (a·pou·siʹa). Kwa upande mwingine, neno la Kigiriki er·khoʹme·non limetumiwa katika andiko la Mathayo 24:30, linalosema kuhusu “Mwana wa binadamu akija [kutimiza kazi aliyopewa na Yehova ya kuwaangamiza waovu kwenye vita vya Har–Magedoni] juu ya mawingu ya mbinguni akiwa na nguvu na utukufu mwingi.” Watafsiri fulani hutumia ‘kuja’ kwa maneno yote mawili ya Kigiriki, lakini wale walio waangalifu zaidi huonyesha tofauti kati ya maneno hayo mawili.
Kristo atakaporudi, je, ataonekana kwa macho ya wanadamu?
Yoh. 14:19: “Bado muda kidogo zaidi na ulimwengu hautaniona tena, lakini ninyi [mitume waaminifu wa Yesu] mtaniona, kwa sababu ninaishi, nanyi mtaishi.” (Yesu alikuwa amewaahidi mitume wake kwamba angekuja tena awachukue waende mbinguni wakawe pamoja naye. Wangeweza kumwona kwa sababu wangekuwa viumbe wa roho kama yeye. Lakini ulimwengu haungemwona yeye tena. Linganisha na 1 Timotheo 6:16.)
-