-
DiniKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Unaweza kujibu hivi: ‘Bila shaka, kuna watu wanyoofu katika karibu kila dini. Lakini jambo la maana kwelikweli ni lile ambalo Neno la Mungu linasema. Linasema kuna dini ngapi za kweli? Ona yaliyoandikwa hapa katika Waefeso 4:4, 5.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Hilo linapatana na maandiko mengine. (Mt. 7:13, 14, 21; Yoh. 10:16; 17:20, 21)’ (2) ‘Basi, tatizo tulilo nalo ni kuitambua dini hiyo. Tunaweza kuitambuaje? (Unaweza kutumia habari katika ukurasa wa 65, 66.)’ (3) (Ona pia habari katika ukurasa wa 188, 189, chini ya kichwa, “Mashahidi wa Yehova.”)
‘Mimi husoma tu Biblia nyumbani na kusali kwa Mungu nipate kuielewa’
Unaweza kujibu hivi: ‘Je, umefaulu kuisoma Biblia nzima?’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Unapojitahidi kufanya hivyo, utaona jambo lenye kupendeza sana katika Mathayo 28:19, 20. . . . Jambo hilo ni muhimu kwa sababu linaonyesha kwamba Kristo anawatumia wanadamu wengine watusaidie kuelewa yanayohusika katika kuwa Mkristo wa kweli. Kupatana na hilo, Mashahidi wa Yehova wanajitolea kuwatembelea watu katika nyumba zao kwa muda wa saa moja hivi kila juma, bila malipo, ili kuzungumzia Biblia. Je, ninaweza kutumia dakika chache tu nikuonyeshe jinsi tunavyofanya?’
Ona pia ukurasa wa 64.
‘Mimi naamini kwamba dini ni jambo la kibinafsi’
Unaweza kujibu hivi: ‘Siku hizi watu wengi wana maoni hayo, na ikiwa watu hawapendezwi kikweli na ujumbe wa Biblia, sisi huwaacha na kwenda katika nyumba nyingine. Lakini je, unajua kwamba nimekuja kukuona kwa sababu Yesu aliwaagiza wafuasi wake wafanye hivyo? . . . (Mt. 24:14; 28:19, 20; 10:40)’
-
-
DuniaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Dunia
Maana: Katika Maandiko, neno “dunia” linatumiwa katika maana zaidi ya moja. Kwa kawaida tunalifikiria kuwa linamaanisha sayari yenyewe, ambayo Yehova aliiumba ikiwa na vitu vya kuendeleza uhai wa binadamu kwa kusudi la kufanya maisha yetu yaridhishe sana. Hata hivyo, tunapaswa kufahamu kwamba neno “dunia” huenda likatumiwa pia kumaanisha, kwa mfano, watu wanaoishi duniani au kikundi cha watu wenye tabia fulani.
Je, sayari ya Dunia sayari itaharibiwa katika vita vya nyukilia?
Kulingana na Biblia, kusudi la Mungu kwa dunia ni nini?
Mt. 6:10: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”
Zab. 37:29: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”
Ona pia Mhubiri 1:4; Zaburi 104:5.
Je, kuna uwezekano kwamba, kwa kuwa mataifa hayajali kusudi la Mungu, huenda yakaiharibu kabisa dunia isiweze kukaliwa?
Isa. 55:8-11: “[Neno la Yehova ni:] Kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo njia zangu zilivyo juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu. . . . Neno langu . . . halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”
Isa. 40:15, 26: “Tazama! [Kwa maoni ya Yehova Mungu] Mataifa ni kama tone kutoka katika ndoo; nayo yamehesabiwa kuwa kama mavumbi membamba juu ya mizani. . . . ‘Inueni macho yenu juu, mwone [jua, mwezi, na mabilioni ya nyota]. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye msukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.’” (Nguvu za nyukilia ambazo mataifa yametengeneza zinawaogopesha wanadamu. Lakini mabilioni ya nyota yana nguvu nyingi zaidi za nyukilia ambazo sisi hatuwezi kuzielewa. Ni nani aliyeumba na kuongoza vitu hivyo vyote vya mbinguni? Je, Yeye hawezi kuyazuia mataifa yasitumie silaha zao za nyukilia kwa njia inayoweza kuzuia kusudi lake? Jambo linaloonyesha kwamba Mungu anaweza kufanya hivyo ni jinsi alivyoharibu majeshi ya Misri wakati Farao alipotaka kuzuia ukombozi wa Israeli.—Kut. 14:5-31.)
Ufu. 11:17, 18: “Tunakushukuru wewe, Yehova Mungu, Mweza-Yote, Yeye aliyeko na aliyekuwako, kwa sababu umechukua nguvu zako kuu na kuanza kutawala ukiwa mfalme. Lakini mataifa wakawa na ghadhabu, nayo ghadhabu yako mwenyewe ikaja, na wakati uliowekwa . . . kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.”
Je, Mungu mwenyewe ataiharibu dunia kwa moto?
Je, andiko la 2 Petro 3:7, 10 (UV) linaunga mkono maoni hayo? “Mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu. . . . Siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea [“zitateketezwa,” ZSB; “itatoweka,” BHN; “zitafunuliwa,” NW].” (Ona: Kodeksi ya Sinaitiko na Vatikani MS 1209, zote mbili zikiwa za karne ya nne W.K., zinasema “zitafunuliwa.” Hati za baadaye, Kodeksi ya Aleksandrino ya karne ya 5 na hati iliyosahihishwa ya Klementina ya karne ya 16 ya Vulgata, zinasema “zitateketea.”)
Je, andiko la Ufunuo 21:1 (UV) linaonyesha kwamba dunia yetu itaharibiwa? “Kisha nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena.”
Ili ufafanuzi wa mistari hiyo uwe sahihi, lazima upatane na muktadha, pamoja na maandiko mengine ya Biblia
Ikiwa maandiko haya (2 Petro 3:7, 10 na Ufunuo 21:1) yanamaanisha kwamba Dunia halisi itateketezwa kwa moto, basi mbingu halisi (nyota na vitu vingine vya mbinguni) pia zitaharibiwa kwa moto. Hata hivyo, maoni hayo ya kijuujuu yanapingana na uhakikisho ulio katika maandiko kama vile Mathayo 6:10, Zaburi 37:29 na Zaburi 104:5, pia Methali 2:21, 22. Zaidi ya hayo, je, moto unaweza kuteketeza jua na nyota ambazo tayari ni moto sana? Kwa hiyo neno “dunia” katika maandiko yaliyotajwa hapo juu bila shaka lina maana tofauti.
Katika Mwanzo 11:1, Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 2:1, 2, Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati 16:31, Zaburi 96:1, n.k., neno “dunia” linatumiwa katika maana ya mfano, likimaanisha wanadamu, jamii ya binadamu. Je, inawezekana kwamba andiko la 2 Petro 3:7, 10 na la Ufunuo 21:1, yana maana hiyohiyo?
Ona kwamba, katika andiko la 2 Petro 3:5, 6 (pia 2:5, 9), hali hiyo inalinganishwa na Gharika ya siku za Noa, ambapo jamii ya binadamu waovu iliharibiwa, lakini Noa na nyumba yake, na pia dunia yenyewe, walihifadhiwa. Vivyo hivyo, andiko la 2 Petro 3:7 linasema kwamba wale watakaoharibiwa ni “watu wasiomwogopa Mungu.” Maoni ya kwamba katika andiko hilo “dunia” inamaanisha jamii ya binadamu waovu yanapatana kabisa na maandiko mengine ya Biblia, kama maandiko yaliyotajwa. Kile ‘kinachofunuliwa’ ni “dunia” ya mfano, au jamii ya binadamu waovu; yaani, Yehova atachoma kana kwamba kwa moto udanganyifu wote, akifichua uovu wa jamii ya binadamu wasiomwogopa Mungu na kuonyesha kwamba wanastahili kuharibiwa kabisa. Jamii hiyo ya binadamu waovu ndiyo pia “dunia ya kwanza,” inayotajwa katika Ufunuo 21:1.
Kwa hiyo, maneno ya Yesu katika Luka 21:33, (“mbingu na dunia zitapitilia mbali, lakini . . . ”) yanaweza kueleweka kuwa ni ya mfano. Vivyo hivyo, andiko la Ufunuo 21:1 linasema kuhusu “mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza.”—Ona pia Mathayo 5:18.
Je, waadilifu watapelekwa mbinguni kisha warudishwe duniani baada ya waovu kuharibiwa?
Je, andiko la Ufunuo 21:2, 3 linaunga mkono maoni hayo? Linasema: “Nikaona pia lile jiji takatifu, Yerusalemu Jipya, likishuka kutoka mbinguni kwa Mungu na limetayarishwa kama bibi-arusi aliyepambwa kwa ajili ya mume wake. Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao.’” (Je, taarifa ya kwamba Mungu “atakaa” pamoja na wanadamu na kwamba “atakuwa pamoja nao” inamaanisha kwamba yeye atakuwa na mwili wa kimwili? Hilo haliwezekani, kwa sababu Yehova alimwambia Musa hivi: “Hakuna mwanadamu anayeweza kuniona na bado aishi.” [Kut. 33:20] Kwa hiyo, basi, wale watakaokuwa sehemu ya Yerusalemu Jipya hawatarudi duniani wakiwa watu wenye mwili. Basi, Mungu ‘atakuwaje pamoja na’ wanadamu, na Yerusalemu Jipya ‘litashukaje kutoka mbinguni’? Bila shaka dokezo moja linapatikana katika andiko la Mwanzo 21:1, linalosema kwamba Mungu ‘alimjia’ Sara, akamjalia kuzaa mwana uzeeni. Andiko la Kutoka 4:31 linatuambia kwamba Mungu ‘aliwajilia’ Israeli kwa kumtuma Musa awe mkombozi. Andiko la Luka 7:16 linasema kwamba kupitia huduma ya Yesu, Mungu ‘alikuja’ kwa watu wake. [Maandiko hayo yametoka katika UV, VB, BHN] Tafsiri nyingine zinatumia maneno Mungu ‘aliwaelekezea fikira’ watu wake [NW] au ‘aliwaangalia,’ [ZSB]. Kwa hiyo maana ya andiko la Ufunuo 21:2, 3 lazima iwe kwamba Mungu ‘atawajilia,’ au atakuwa pamoja na wanadamu kupitia Yerusalemu Jipya la mbinguni, na kupitia hilo baraka zitawajia wanadamu watiifu.)
-