Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kunyakuliwa
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Mtu Akisema—

      ‘Je, unaamini kwamba watu watanyakuliwa?’

      Unaweza kujibu hivi: ‘Nimeona kwamba watu wana maoni mbalimbali kuhusu maana ya kunyakuliwa. Maoni yako ni nini kuhusu jambo hilo? . . . Kuhusu jambo lolote, inafaa kulinganisha maoni yetu na mambo ambayo Biblia yenyewe inasema. (Tumia baadhi ya habari zilizo juu zinazohusu jambo hilo.)’

      Au unaweza kusema: ‘Watu wamenieleza kwamba kunyakuliwa ni njia ambayo Wakristo watatumia kukimbia. Wengi wana maoni kwamba watatumia njia hiyo ili kuikimbia dhiki kuu inayokuja. Je, hayo ndiyo maoni yako?’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Bila shaka sisi tunataka Mungu atulinde wakati huo, nami nimetiwa moyo sana na maandiko fulani yanayoonyesha jinsi tunavyoweza kupata ulinzi huo. (Sef. 2:3)’ (2) ‘Jambo la kupendeza ni kwamba, Biblia inaonyesha kwamba Mungu atawalinda waaminifu fulani hapa hapa duniani. (Met. 2:21, 22) Hilo linapatana na kusudi la Mungu alipomuumba Adamu na kumweka katika Paradiso, sivyo?’

      Pia unaweza kusema: ‘Unaposema kunyakuliwa, je, unamaanisha kwamba Wakristo wanaoishi wakati wa mwisho wa ulimwengu watachukuliwa waende mbinguni? . . . Je, umewahi kujiuliza watafanya nini watakapofika mbinguni? . . . Ona mambo ambayo andiko la Ufunuo 20:6 (na 5:9, 10) linasema. . . . Lakini watatawala nani? (Zab. 37:10, 11, 29)’

  • Kurudi kwa Kristo
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Kurudi kwa Kristo

      Maana: Kabla ya kuondoka duniani, Yesu Kristo aliahidi kurudi. Matukio yenye kusisimua kuhusiana na Ufalme wa Mungu yanahusianishwa na ahadi hiyo. Tunapaswa kukumbuka kwamba kuna tofauti kati ya kuja na kuwapo. Kwa hiyo, ingawa kuja kwa mtu (kunakohusianishwa na kufika au kurudi kwake) kunatukia katika wakati fulani, huenda kuwapo kwake baada ya hapo kukaendelea kwa kipindi cha miaka kadhaa. Katika Biblia neno la Kigiriki erʹkho·mai (linalomaanisha “kuja”) linatumiwa pia kumhusu Yesu akielekeza fikira kwenye kazi muhimu katika kipindi hususa wakati wa kuwapo kwake, yaani, kazi yake aliyopewa na Yehova ya kuwaangamiza waovu kwenye vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.

      Je, matukio yanayohusianishwa na kuwapo kwa Kristo yanatukia katika wakati mfupi sana au kwa kipindi cha miaka kadhaa?

      Mt. 24:37-39: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo [“kuja,” UV, BHN, ZSB; Kigiriki, pa·rou·siʹa] kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. Kwa maana kama vile walivyokuwa katika siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Matukio ya “siku za Noa” yanayosimuliwa hapa yalitukia kwa kipindi cha miaka mingi. Yesu alilinganisha kuwapo kwake na yale yaliyotukia wakati huo.)

      Katika Mathayo 24:37 neno la Kigiriki pa·rou·siʹa linatumiwa. Kihalisi maana yake ni “kuwa kando ya.” Kamusi Greek-English Lexicon (Oxford, 1968) ya Liddell na Scott inatoa “kuwapo, kwa watu,” kuwa maana ya kwanza ya pa·rou·siʹa. Maana ya neno hilo inaonyeshwa waziwazi katika Wafilipi 2:12, ambapo Paulo anatofautisha kuwapo kwake (pa·rou·siʹa) na kutokuwapo kwake (a·pou·siʹa). Kwa upande mwingine, neno la Kigiriki er·khoʹme·non limetumiwa katika andiko la Mathayo 24:30, linalosema kuhusu “Mwana wa binadamu akija [kutimiza kazi aliyopewa na Yehova ya kuwaangamiza waovu kwenye vita vya Har–Magedoni] juu ya mawingu ya mbinguni akiwa na nguvu na utukufu mwingi.” Watafsiri fulani hutumia ‘kuja’ kwa maneno yote mawili ya Kigiriki, lakini wale walio waangalifu zaidi huonyesha tofauti kati ya maneno hayo mawili.

      Kristo atakaporudi, je, ataonekana kwa macho ya wanadamu?

      Yoh. 14:19: “Bado muda kidogo zaidi na ulimwengu hautaniona tena, lakini ninyi [mitume waaminifu wa Yesu] mtaniona, kwa sababu ninaishi, nanyi mtaishi.” (Yesu alikuwa amewaahidi mitume wake kwamba angekuja tena awachukue waende mbinguni wakawe pamoja naye. Wangeweza kumwona kwa sababu wangekuwa viumbe wa roho kama yeye. Lakini ulimwengu haungemwona yeye tena. Linganisha na 1 Timotheo 6:16.)

      Mdo. 13:34: “Yeye [Mungu] alimfufua [Yesu] kutoka kwa wafu akikusudiwa asirudi tena kwenye uharibifu.” (Miili ya kibinadamu kwa asili ni yenye kuharibika. Ndiyo sababu andiko la 1 Wakorintho 15:42, 44 hutumia neno “uharibifu” pamoja na maneno “mwili wa nyama.” Yesu hatakuwa kamwe tena na mwili kama huo.)

      Yoh. 6:51: “Mimi ndio mkate ulio hai ulioshuka kutoka mbinguni; yeyote akila mkate huu ataishi milele; na, kwa kweli, mkate ambao nitatoa ni mwili wangu kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.” (Akiisha kuutoa mwili wake, Yesu hauchukui tena. Kwa hiyo yeye hawanyimi wanadamu faida za dhabihu ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu.)

      Ona pia ukurasa wa 111-113, chini ya kichwa, “Kunyakuliwa.”

      Biblia inamaanisha nini inaposema kwamba Yesu atakuja “vivyo hivyo” kama alivyopanda mbinguni?

      Mdo. 1:9-11: “Huku [mitume wa Yesu] walipokuwa wakitazama, akainuliwa na wingu likamchukua juu kutoka machoni pao. Nao walipokuwa wakitazama angani alipokuwa ameondoka na kwenda, pia, tazama! wanaume wawili wenye mavazi meupe wakasimama kando yao, nao wakasema: ‘Wanaume wa Galilaya, kwa nini mnasimama mkitazama angani? Yesu huyu aliyepokewa juu angani kutoka kwenu atakuja vivyo hivyo kama vile ambavyo mmemwona akienda angani.’” (Ona kwamba andiko hilo linasema “vivyo hivyo,” wala si mwili uleule. Alipanda mbinguni jinsi gani? Kama mstari wa 9 unavyoonyesha, alitoweka machoni pao, na kuondoka kwake kulionwa na wanafunzi wake tu. Ulimwengu kwa ujumla haukujua yaliyokuwa yametukia. Hivyo ndivyo ingekuwa wakati wa kurudi kwa Kristo.)

      Maneno “anakuja na mawingu, na kila jicho litamwona” yanamaanisha nini?

      Ufu. 1:7: “Tazama! Anakuja na mawingu, na kila jicho litamwona, na wale waliomchoma; na makabila yote ya dunia yatajipiga-piga kwa huzuni kwa sababu yake.” (Ona pia Mathayo 24:30; Marko 13:26; Luka 21:27.)

      “Mawingu” yanawakilisha nini? Ni kutoonekana. Wakati ndege inapokuwa katika wingu zito au juu ya mawingu, kwa kawaida watu walio chini hawawezi kuiona, ingawa huenda wakasikia mngurumo wa injini zake. Yehova alimwambia Musa hivi: “Nitakujia katika wingu lenye giza.” Musa hakumwona Mungu, lakini wingu hilo lilionyesha kuwapo kusikoonekana kwa Yehova. (Kut. 19:9; ona pia Mambo ya Walawi 16:2; Hesabu 11:25.) Kama Kristo angetokea akionekana kwa macho mbinguni, ni wazi kwamba si “kila jicho” lingemwona. Kwa mfano, kama angetokea Australia, je, angeonekana Ulaya, Afrika, na Amerika?

      “Kila jicho litamwona” jinsi gani? Watatambua kutokana na matukio duniani kwamba yeye yupo ijapokuwa haonekani kwa macho. Pia likielekezea kuona ambako si kwa macho halisi, andiko la Yohana 9:41 linasema hivi: “Yesu akawaambia [Mafarisayo]: ‘Kama mngekuwa vipofu, hamngekuwa na dhambi. Lakini sasa mnasema, “Tunaona.” Dhambi yenu inabaki.’” (Linganisha na Waroma 1:20.) Baada ya kurudi kwa Kristo, watu fulani wanaamini; wanaitambua ishara ya kuwapo kwake. Wengine wanakataa uthibitisho, lakini Kristo atakapoanza kutenda akiwa yule aliyewekwa na Mungu kuwaangamiza waovu, wataona nguvu zake na kutambua kwamba uharibifu huo hautoki kwa wanadamu bali unatoka mbinguni. Watajua linalotukia kwa sababu walikuwa wameonywa mapema. Kwa sababu ya jambo linalowapata, ‘watajipiga-piga kwa kuomboleza.’

      “Wale waliomchoma” ni nani? Kihalisi, askari wa Roma ndio waliomchoma Yesu alipouawa. Lakini walikufa zamani. Kwa hiyo, maneno hayo yanamaanisha watu wanaowatendea vibaya jinsi hiyohiyo, au ‘wanaowachoma,’ wafuasi wa kweli wa Kristo wakati wa “siku za mwisho.”—Mt. 25:40, 45.

      Je, kweli inaweza kusemwa kwamba mtu ‘amekuja’ au kwamba yeye ‘yupo’ ikiwa haonekani?

      Mtume Paulo alisema kwamba yeye ‘hakuwapo katika mwili bali alikuwapo katika roho’ na kutaniko lililokuwa huko Korintho.—1 Kor. 5:3.

      Yehova alisema kwamba ‘anashuka’ ili kuvuruga lugha ya wajenzi wa mnara wa Babeli. (Mwa. 11:7) Pia alisema kwamba ‘anashuka’ ili kuwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri. Na Mungu alimhakikishia Musa kwamba “Mimi mwenyewe nitakwenda pamoja nawe” ili kuwaongoza Waisraeli kuelekea Nchi ya Ahadi. (Kut. 3:8; 33:14) Lakini hakuna mwanadamu yeyote ambaye alimwona Mungu.—Kut. 33:20; Yoh. 1:18.

      Biblia inahusianisha kuwapo kwa Kristo na matukio gani?

      Dan. 7:13, 14: “Mtu fulani kama mwana wa binadamu [Yesu Kristo] alikuwa anakuja na mawingu ya mbingu; naye akaja kwa Mzee wa Siku [Yehova Mungu], nao wakamleta karibu mbele zake Yule. Naye akapewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.”

      1 The. 4:15, 16: “Tunawaambia hivi kwa neno la Yehova, kwamba sisi tulio hai ambao tutabaki mpaka kuwapo kwa Bwana hatutawatangulia kwa vyovyote wale ambao wamelala usingizi katika kifo; kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni akiwa na mwito wenye amri, kwa sauti ya malaika mkuu na kwa tarumbeta ya Mungu, na wale walio wafu katika muungano na Kristo watafufuliwa kwanza.” (Kwa hiyo, wale watakaotawala pamoja na Kristo wangefufuliwa wawe pamoja naye mbinguni—kwanza wale waliokuwa wamekufa miaka mingi iliyopita kisha wale ambao wangekufa baada ya kurudi kwa Bwana.)

      Mt. 25:31-33: “Wakati Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu, mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi. Naye atawaweka kondoo kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto.”

      2 The. 1:7-9: “Kwenu ninyi mnaopata dhiki, kitulizo pamoja nasi wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto, anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu. Watu hao watahukumiwa adhabu ya uharibifu wa milele kutoka mbele ya Bwana na kutoka kwenye utukufu wa nguvu zake.”

      Luka 23:42, 43: “Naye [yule mtenda-maovu mwenye huruma aliyetundikwa pamoja na Yesu] akaendelea kusema: ‘Yesu, unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.’ Naye akamwambia: ‘Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.’” (Chini ya utawala wa Yesu, dunia yote itakuwa Paradiso; wafu walio katika kumbukumbu ya Mungu watafufuliwa na kupewa nafasi ya kupata uzima mkamilifu duniani milele.)

      Ona pia ukurasa wa 284-289, chini ya kichwa, “Siku za Mwisho.”

  • Kusema kwa Lugha
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Kusema kwa Lugha

      Maana: Uwezo wa pekee ambao wanafunzi fulani walipewa katika kutaniko la kwanza la Kikristo kupitia roho takatifu uliowawezesha kuhubiri au kumtukuza Mungu katika lugha nyingine.

      Je, Biblia inasema wote walio na roho ya Mungu ‘wangesema kwa lugha’?

      1 Kor. 12:13, 30: “Kwa kweli kwa roho moja sote tulibatizwa katika mwili mmoja . . . Je, wote wana zawadi za maponyo? Je, wote husema kwa lugha?” (Ona pia 1 Wakorintho 14:26.)

      1 Kor. 14:5: “Basi ningependa ninyi nyote mseme kwa lugha, lakini napendelea zaidi kwamba mtoe unabii. Kwa kweli, yeye anayetoa unabii ni mkubwa kuliko yeye anayesema kwa lugha, isipokuwa, kwa kweli, yeye atafsiri, ili kutaniko lijengwe.”

      Mtu akisema kwa maneno ya kusisimuka katika lugha ambayo hajapata kujifunza kamwe, je, hilo linaonyesha kwamba ana roho takatifu?

      Je, uwezo wa ‘kusema kwa lugha’ unaweza kutokana na chanzo kingine isipokuwa Mungu wa kweli?

      1 Yoh. 4:1: “Wapendwa, msiamini kila neno lililoongozwa na roho [“kila roho,” UV, ZSB], lakini yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu.” (Ona pia Mathayo 7:21-23; 2 Kor. 11:14, 15.)

      Kati ya wale ‘wanaosema kwa lugha’ leo ni Wapentekoste na Wabaptisti, pia Wakatoliki, Waepiskopali, Wamethodisti, Walutheri, na Wapresibiteri. Yesu alisema kwamba roho takatifu ‘itawaongoza wanafunzi wake ndani ya kweli yote.’ (Yoh. 16:13) Je, wafuasi wa kila moja ya dini hizo wanaamini kwamba wengine ambao pia ‘husema kwa lugha’ wanaongozwa katika “kweli yote”? Hilo lingewezekanaje, kwa kuwa wao wote hawapatani? Ni roho gani inayowawezesha ‘kusema kwa lugha’?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki