-
Kuwasiliana na PepoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Yak. 4:7: “Basi, jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” (Ili kufanya hivyo, jifunze kwa bidii mapenzi ya Mungu na kuyafuata katika maisha yako. Huku upendo wa Mungu ukikuimarisha usiwaogope wanadamu, kataa kabisa kushiriki katika desturi zozote zinazohusiana na kuwasiliana na pepo au kutii sheria zozote za mtu mwenye kuwasiliana na pepo.)
Vaa “mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu” ambayo yanafafanuliwa katika Waefeso 6:10-18 na uwe na bidii katika kuyadumisha yote katika hali nzuri.
-
-
Kuzaliwa Mara ya PiliKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Kuzaliwa Mara ya Pili
Maana: Kuzaliwa mara ya pili kunahusisha kubatizwa katika maji (‘kuzaliwa kwa maji’) na kuzaliwa kwa roho ya Mungu, kwa njia hiyo kuwa mwana wa Mungu mwenye tumaini la kutawala katika Ufalme wa Mungu. (Yoh. 3:3-5) Yesu alizaliwa mara ya pili, hali kadhalika wale 144,000 walio warithi pamoja naye wa Ufalme wa mbinguni.
Kwa nini ni lazima Wakristo fulani ‘wazaliwe mara ya pili’?
Mungu amekusudia kushirikisha wanadamu wachache waaminifu watawale pamoja na Yesu Kristo katika Ufalme wa mbinguni
Luka 12:32: “Msiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.”
Ufu. 14:1-3: “Nikaona, na, tazama! Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] amesimama juu ya Mlima Sayuni, na pamoja naye 144,000 . . . ambao wamenunuliwa kutoka duniani.” (Ona ukurasa wa 202, 203, chini ya kichwa, “Mbingu.”)
Wanadamu hawawezi kwenda mbinguni wakiwa na miili ya nyama na damu
1 Kor. 15:50: “Hili nasema, akina ndugu, kwamba nyama na damu haviwezi kuurithi ufalme wa Mungu, wala uharibifu haurithi kutoweza kuharibika.”
Yoh. 3:6: “Kile ambacho kimezaliwa kwa mwili ni mwili, na kile ambacho kimezaliwa kwa roho ni roho.”
Ni wale tu ambao ‘wamezaliwa mara ya pili,’ na kuwa wana wa Mungu, ndio wanaoweza kutawala katika Ufalme wa mbinguni
Yoh. 1:12, 13: “Wengi kadiri ileile waliompokea [Yesu Kristo], aliwapa mamlaka ya kuwa watoto wa Mungu, kwa sababu walikuwa wakionyesha imani katika jina lake; nao walizaliwa, si kutokana na damu au kutokana na mapenzi ya mwili au kutokana na mapenzi ya mwanadamu, bali kutokana na Mungu.” (Maneno “wengi kadiri ileile waliompokea” hayamaanishi wanadamu wote ambao wamemwamini Kristo. Ona ni nani wanaorejezewa, kama inavyoonyeshwa katika mstari wa 11 [“watu wake mwenyewe,” Wayahudi]. Wanadamu wengine pia wamepata pendeleo hilohilo, lakini ni “kundi dogo” tu.)
Rom. 8:16, 17: “Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu. Basi, ikiwa sisi ni watoto, sisi pia ni warithi: warithi wa Mungu kwelikweli, lakini warithi pamoja na Kristo, mradi tu tunateseka pamoja ili pia tutukuzwe pamoja.”
1 Pet. 1:3, 4: “Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alituzaa sisi upya kwenye tumaini lililo hai kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu, kwenye urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia. Huo umewekwa akiba mbinguni kwa ajili yenu.”
Watafanya nini mbinguni?
Ufu. 20:6: “Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.”
1 Kor. 6:2: “Je, hamjui kwamba watakatifu watauhukumu ulimwengu?”
Je, mtu ambaye ‘hajazaliwa mara ya pili’ anaweza kuokolewa?
Ufu. 7:9, 10, 17: “Baada ya mambo haya [baada ya mtume Yohana kusikia hesabu ya wale ambao ‘wangezaliwa mara ya pili,’ wale ambao wangefanyiza Israeli wa kiroho na ambao wangekuwa pamoja na Kristo mbinguni; linganisha na Waroma 2:28, 29 na Wagalatia 3:26-29] nikaona, na, tazama! umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha, wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, wamevikwa kanzu nyeupe; na kulikuwa na matawi ya mitende mikononi mwao. Nao wanaendelea kupaaza sauti kubwa, wakisema: ‘Wokovu unatoka kwa Mungu wetu, anayeketi juu ya kiti cha ufalme, na Mwana-Kondoo.’ . . . ‘Mwana-Kondoo [Yesu Kristo], aliye katikati ya kile kiti cha ufalme, atawachunga, na kuwaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima.’”
Baada ya kuorodhesha watu wa imani wa kabla ya Ukristo, andiko la Waebrania 11:39, 40 lasema hivi: “Hawa wote, ijapokuwa walitolewa ushahidi kupitia imani yao, hawakupata utimizo wa ile ahadi, kwa kuwa Mungu aliona kimbele kitu bora kwa ajili yetu sisi, ili wasifanywe kuwa wakamilifu bila sisi.” (Neno hili “sisi” linamaanisha nani? Waebrania 3:1 huonyesha kwamba wao ni “washiriki wa mwito wa mbinguni.” Ni lazima basi, watu wa kabla ya Ukristo waliokuwa na imani, wawe na tumaini la uzima mkamilifu mahali pengine wala si mbinguni.)
Zab. 37:29: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”
Ufu. 21:3, 4: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”
Je, mtu anaweza kuwa na roho ya Mungu na bado ‘asiwe amezaliwa mara ya pili’?
Malaika wa Yehova alisema hivi kumhusu Yohana mbatizaji: “Naye atajazwa roho takatifu akiwa katika tumbo la uzazi la mama yake.” (Luka 1:15) Na baadaye Yesu alisema: “Kati ya wale waliozaliwa na wanawake hajatokea mkuu kuliko Yohana Mbatizaji; lakini mtu aliye mdogo zaidi katika ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye [Kwa nini? Kwa sababu Yohana hatakuwa mbinguni na hivyo hakuhitaji ‘kuzaliwa mara ya pili’]. Lakini tangu siku za Yohana Mbatizaji mpaka sasa [Yesu aliposema maneno hayo] ufalme wa mbinguni ndio mradi ambao watu wanajikaza kuufikia.”—Mt. 11:11, 12.
Roho ya Yehova ‘ilitenda kazi’ juu ya Daudi ‘ikasema’ kupitia yeye (1 Sam. 16:13; 2 Sam. 23:2), lakini hakuna mahali ambapo Biblia inasema kwamba yeye ‘alizaliwa mara ya pili.’ Hakuhitaji ‘kuzaliwa mara ya pili,’ kwa sababu, kama andiko la Matendo 2:34 linavyosema: “Daudi hakupanda mbinguni.”
Leo watu walio na roho ya Mungu wanatambuliwaje?
Ona ukurasa wa 243, 244, chini ya kichwa, “Roho.”
Mtu Akisema—
‘Mimi nimezaliwa mara ya pili’
Unaweza kujibu hivi: ‘Hilo linamaanisha kwamba unatarajia kuwa pamoja na Kristo mbinguni siku moja, sivyo? . . . Je, ungependa kujua wale watakaoenda mbinguni watafanya nini huko?’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Watakuwa wafalme na makuhani, wakitawala pamoja na Kristo. (Ufu. 20:6; 5:9, 10) Yesu alisema kwamba wangekuwa “kundi dogo” tu. (Luka. 12:32)’ (2) ‘Ikiwa wao ni wafalme, lazima pia kuwe na raia watakaotawaliwa. Hao watakuwa nani? . . . Haya ni mambo ambayo nimeona kuwa yenye kupendeza sana. (Zab. 37:11, 29; Met. 2:21, 22)’
‘Je, wewe umezaliwa mara ya pili?’
Unaweza kujibu hivi: ‘Nimeona kwamba watu wanaposema ‘kuzaliwa mara ya pili,’ hawamaanishi jambo lilelile nyakati zote. Tafadhali nieleze jinsi unavyoelewa jambo hilo?’
Au unaweza kusema: ‘Unataka kujua kama nimemkubali Yesu kuwa Mwokozi wangu na kama nimeipokea roho takatifu, sivyo? Nakuhakikishia kwamba ndivyo ilivyo; kama sivyo singekuwa nikizungumza nawe juu ya Yesu.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Lakini ninapofikiria suala la kuwa na roho takatifu, inasikitisha kuona kwamba wengi wanaodai kuwa Wakristo hawana uthibitisho wa roho hiyo. (Gal. 5:22, 23)’ (2) ‘Je, ungefurahi kuishi katika dunia hii ikiwa kila mtu angekuwa na sifa hizo za kimungu? (Zab. 37:10, 11)’
Pia unaweza kusema: ‘Ikiwa ungependa kujua kama nimemkubali Kristo kuwa Mwokozi wangu, jibu ni Ndiyo. Mashahidi wote wa Yehova wamefanya hivyo. Lakini, kwetu sisi, kuzaliwa mara ya pili kunahusisha mengi zaidi ya hilo.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Yesu aliposema juu ya kuzaliwa mara ya pili alisema kwamba jambo hilo ni la lazima ili kuingia katika Ufalme wa Mungu, yaani, kuwa sehemu ya Ufalme wa Mungu, serikali yake ya mbinguni. (Yoh. 3:5)’ (2) ‘Pia Biblia inaonyesha kwamba watu wengi wanaofanya mapenzi ya Mungu wataishi hapa duniani, wakiwa raia wenye furaha wa Ufalme huo. (Mt. 6:10; Zab. 37:29)’
Pendekezo la ziada: Wale wa jamii ya mbinguni wanaweza kujibu hivi: ‘Ndiyo, nimezaliwa mara ya pili. Lakini Biblia inatuonya sisi sote tusiwe na uhakika mno kuhusu tumaini letu. Tunahitaji kuendelea kujichunguza ili kuhakikisha kwamba kwa kweli tunafanya yale ambayo Mungu na Kristo wanataka tufanye. (1 Kor. 10:12)’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Yesu aliwapa wanafunzi wake wa kweli jukumu gani? (Mt. 28:19, 20; 1 Kor. 9:16)’
-
-
Kuzaliwa Upya Katika Mwili MwingineKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Kuzaliwa Upya Katika Mwili Mwingine
Maana: Imani ya kwamba mtu huzaliwa tena katika mwili mwingine au mfululizo wa miili, ambayo inaweza kuwa ya mwanadamu au mnyama. Kwa kawaida, inaaminiwa kwamba “nafsi” isiyoonekana ndiyo inayozaliwa upya katika mwili mwingine. Hilo si fundisho la Biblia.
Mtu anapohisi kwamba anawajua watu ambao hajawahi kukutana nao au kwamba anajua mahali ambapo hajawahi kuwa, je, hilo linathibitisha kwamba watu huzaliwa upya katika mwili mwingine?
Je, umewahi kukutana na mwanamume au mwanamke, na kufikiri kimakosa kwamba ni mwingine aliye hai pia? Wengi wamefanya hivyo. Kwa nini? Kwa sababu watu fulani wana mazoea yanayofanana na ya wengine au huenda hata wakawa na sura inayofanana sana. Kwa hiyo, hisia ya kwamba unamjua mtu hata ikiwa hujawahi kukutana naye wakati uliopita kwa kweli haithibitishi kwamba ulimjua katika maisha mengine, sivyo?
Kwa nini huenda ukaona kwamba unatambua nyumba au mji fulani hata ingawa hujapata kuwa mahali hapo? Je, ni kwa sababu uliishi hapo wakati wa maisha ya zamani? Nyumba nyingi hujengwa kulingana na michoro inayofanana. Fanicha zinazotumiwa katika majiji yaliyo mbali huenda zikafanyizwa kulingana na vielelezo vinavyofanana. Na je, si kweli kwamba maumbo fulani ya nchi hufanana sana na yale yaliyo katika sehemu nyingine za mbali sana? Kwa hiyo, inaeleweka ni kwa nini mtu anaweza kuwa na hisia hizo, na si lazima azaliwe upya katika mwili mwingine ndipo ahisi hivyo.
-