-
Kuzaliwa Mara ya PiliKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Pendekezo la ziada: Wale wa jamii ya mbinguni wanaweza kujibu hivi: ‘Ndiyo, nimezaliwa mara ya pili. Lakini Biblia inatuonya sisi sote tusiwe na uhakika mno kuhusu tumaini letu. Tunahitaji kuendelea kujichunguza ili kuhakikisha kwamba kwa kweli tunafanya yale ambayo Mungu na Kristo wanataka tufanye. (1 Kor. 10:12)’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Yesu aliwapa wanafunzi wake wa kweli jukumu gani? (Mt. 28:19, 20; 1 Kor. 9:16)’
-
-
Kuzaliwa Upya Katika Mwili MwingineKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Kuzaliwa Upya Katika Mwili Mwingine
Maana: Imani ya kwamba mtu huzaliwa tena katika mwili mwingine au mfululizo wa miili, ambayo inaweza kuwa ya mwanadamu au mnyama. Kwa kawaida, inaaminiwa kwamba “nafsi” isiyoonekana ndiyo inayozaliwa upya katika mwili mwingine. Hilo si fundisho la Biblia.
Mtu anapohisi kwamba anawajua watu ambao hajawahi kukutana nao au kwamba anajua mahali ambapo hajawahi kuwa, je, hilo linathibitisha kwamba watu huzaliwa upya katika mwili mwingine?
Je, umewahi kukutana na mwanamume au mwanamke, na kufikiri kimakosa kwamba ni mwingine aliye hai pia? Wengi wamefanya hivyo. Kwa nini? Kwa sababu watu fulani wana mazoea yanayofanana na ya wengine au huenda hata wakawa na sura inayofanana sana. Kwa hiyo, hisia ya kwamba unamjua mtu hata ikiwa hujawahi kukutana naye wakati uliopita kwa kweli haithibitishi kwamba ulimjua katika maisha mengine, sivyo?
Kwa nini huenda ukaona kwamba unatambua nyumba au mji fulani hata ingawa hujapata kuwa mahali hapo? Je, ni kwa sababu uliishi hapo wakati wa maisha ya zamani? Nyumba nyingi hujengwa kulingana na michoro inayofanana. Fanicha zinazotumiwa katika majiji yaliyo mbali huenda zikafanyizwa kulingana na vielelezo vinavyofanana. Na je, si kweli kwamba maumbo fulani ya nchi hufanana sana na yale yaliyo katika sehemu nyingine za mbali sana? Kwa hiyo, inaeleweka ni kwa nini mtu anaweza kuwa na hisia hizo, na si lazima azaliwe upya katika mwili mwingine ndipo ahisi hivyo.
Mtu anapofanyiwa kiinimacho naye akumbuke maisha ya wakati mwingine mahali pengine, je, hilo linathibitisha kwamba watu huzaliwa upya katika mwili mwingine?
Mtu anapofanyiwa kiinimacho habari nyingi zilizohifadhiwa katika ubongo zinaweza kutolewa. Watu wanaofanya kiinimacho hutoa kumbukumbu zilizohifadhiwa. Lakini kumbukumbu hizo ziliingiaje humo? Labda ulisoma kitabu fulani, ukaona sinema, au ukapata kujua watu fulani kutoka katika televisheni. Ikiwa ulijiweka mahali pa watu hao, huenda hali hiyo ilifanyiza kumbukumbu akilini mwako, kana kwamba mambo hayo yalikupata wewe mwenyewe. Huenda mambo hayo ni ya zamani sana hivi kwamba umeyasahau, lakini unapofanyiwa kiinimacho, huenda ukayakumbuka kana kwamba ni “maisha mengine.” Hata hivyo, ikiwa hivyo ndivyo ilivyo, basi kila mtu angekuwa na kumbukumbu kama hizo. Lakini sivyo ilivyo. Ni jambo linalostahili kuangaliwa kwamba mahakama kuu za majimbo kadhaa huko Marekani hazikubali ushahidi unaotolewa mtu anapofanyiwa kiinimacho. Katika mwaka wa 1980, Mahakama Kuu ya Minnesota ilitangaza kwamba “ushuhuda bora zaidi wa kitaalamu unaonyesha kwamba hakuna mtaalamu anayeweza kuamua kama kumbukumbu inayotolewa kupitia kiinimacho, au sehemu yoyote ya kumbukumbu hiyo, ni ukweli, uwongo, au ni jambo la kutungwa tu—ni kujazia mapengo kwa kutumia mambo ya kuwazia-wazia. Matokeo hayo hayategemeki kisayansi kuwa ni sahihi.” (State v. Mack, 292 N.W.2d 764) Pia, mapendekezo yanayotolewa na mwenye kufanya kiinimacho, ambayo humwathiri yule anayefanyiwa kiinimacho, huchangia kutotegemeka huko.
Je, Biblia inaunga mkono imani ya kuzaliwa upya katika mwili mwingine?
Je, andiko la Mathayo 17:12, 13 linaunga mkono imani ya kuzaliwa upya katika mwili mwingine?
Mt. 17:12, 13: “[Yesu akasema:] ‘Tayari Eliya amekuja nao hawakumtambua bali walimtendea mambo waliyotaka. Katika njia hiyo pia Mwana wa binadamu atateseka mikononi mwao.’ Ndipo wanafunzi wakafahamu kwamba alikuwa akiwaambia juu ya Yohana Mbatizaji.”
Je, hilo lilimaanisha kwamba Yohana Mbatizaji ni Eliya aliyekuwa amezaliwa upya katika mwili mwingine? Makuhani Wayahudi walipomuuliza Yohana, “Je, wewe ndiye Eliya?” alisema, “Mimi siye.” (Yoh. 1:21) Basi, Yesu alimaanisha nini? Kama malaika wa Yehova alivyotabiri, Yohana alimtangulia Masihi wa Yehova “kwa roho na nguvu za Eliya, ili kurudisha mioyo ya akina baba kwa watoto na wale wasiotii kwenye hekima inayotumika ya waadilifu, ili kuweka tayari kwa ajili ya Yehova watu waliotayarishwa.” (Luka 1:17) Kwa hiyo Yohana Mbatizaji alikuwa akitimiza unabii kwa kufanya kazi kama ile ya nabii Eliya.—Mal. 4:5, 6.
-