-
Manabii wa UwongoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Maandiko hutaja wakati mbalimbali kuhusiana na kuwapo kwa Kristo, na Mashahidi wa Yehova wamejifunza mambo hayo kwa makini sana. (Luka 21:24; Dan. 4:10-17) Yesu pia alisimulia ishara yenye mambo mengi, ambayo ingeambatana na utimizo wa unabii mbalimbali unaohusu wakati, ili kutambulisha kizazi ambacho kingeishi kione mwisho wa mfumo mbovu wa mambo wa Shetani. (Luka 21:7-36) Mashahidi wa Yehova wameonyesha uthibitisho wa kutimizwa kwa ishara hiyo. Ni kweli kwamba nyakati nyingine Mashahidi wamekosea katika kuelewa yale ambayo yangetukia kwenye mwisho wa vipindi fulani vya wakati, lakini hawajafanya kosa la kupoteza imani wala kuacha kukesha kuhusiana na kutimia kwa makusudi ya Yehova. Wameendelea kukumbuka kabisa shauri hili ambalo Yesu alitoa: “Endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.”—Mt. 24:42.
Mambo ambayo yamesahihishwa si makubwa yanapolinganishwa na kweli muhimu za Biblia ambazo wamefahamu na kuzitangaza. Baadhi ya kweli hizo ni: Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli. Yesu Kristo si sehemu ya Utatu bali yeye ni Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. Kukombolewa katika dhambi kunawezekana tu kupitia imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo. Roho takatifu si mtu bali ni nguvu za utendaji za Yehova, na lazima matunda ya roho hiyo yaonekane katika maisha ya waabudu wa kweli. Nafsi ya mwanadamu inaweza kufa, si kama wapagani wa kale walivyodai kwamba haifi; hiyo hufa, na tumaini kwa ajili ya uzima wa wakati ujao ni kupitia ufufuo. Mungu ameruhusu uovu kwa sababu ya lile suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la wanadamu. Tangu mwaka wa 1914, tumekuwa tukiishi katika siku za mwisho za mfumo mbovu wa mambo wa ulimwenguni pote. Wakristo waaminifu 144,000 pekee ndio watakaokuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo mbinguni, lakini wanadamu wengine watiifu watapata uzima wa milele katika paradiso duniani.
Jambo lingine la kufikiria kuhusu mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni hili: Je, kweli yameboresha maadili ya watu? Je, wale wanaofuata mafundisho hayo wanajulikana katika jamii zao kwa sababu ya unyoofu wao? Je, maisha ya familia zao yamekuwa bora kwa kufuata mafundisho hayo? Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangetambuliwa kwa urahisi kwa sababu ya kuwa na upendo kati yao. (Yoh. 13:35) Je, sifa hiyo inaonekana wazi kati ya Mashahidi wa Yehova? Mambo ya hakika yanaonyesha wazi.
Mtu Akisema—
‘Kasisi wangu alisema Mashahidi wa Yehova ndio manabii wa uwongo’
Unaweza kujibu hivi: ‘Hebu nikuulize, Je, alikuonyesha lolote katika Biblia linaloeleza mambo tunayoamini au kutenda na linalosema kwamba watu wa aina hiyo wangekuwa manabii wa uwongo? . . . Je, nikuonyeshe jinsi Biblia inavyoeleza manabii wa uwongo? (Kisha tumia jambo moja au zaidi kati ya yale yaliyo katika ukurasa wa 176-179.)’
Au unaweza kusema: ‘Nina hakika utakubali kwamba shtaka hilo zito linapaswa kuthibitishwa na jambo hususa. Je, kasisi wako alitaja mifano yoyote hususa? (Ikiwa mwenye nyumba anataja yanayodaiwa kuwa “matabiri” ambayo hayakutimia, tumia habari katika ukurasa wa 177, 178, na ukurasa wa 179, 180.)’
Pia unaweza kujibu: ‘Nina hakika kwamba ikiwa mtu fulani angekushtaki juu ya jambo kama hilo, ungetumia nafasi angalau kueleza msimamo wako au maoni yako, sivyo? . . . Basi, je, nikuonyeshe katika Biblia . . . ?’
-
-
Maria (Mama ya Yesu)Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Maria (Mama ya Yesu)
Maana: Mwanamke aliyechaguliwa na Mungu na kupendelewa sana ambaye alimzaa Yesu. Kuna Maria wengine watano wanaotajwa katika Biblia. Huyu alikuwa mzao wa Mfalme Daudi, wa kabila la Yuda, na binti ya Heli. Anapotajwa mara ya kwanza katika Maandiko, amechumbiwa na Yosefu, ambaye pia ni wa kabila la Yuda na mzao wa Daudi.
Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi ya Biblia kumhusu Maria?
(1) Kuwa na nia ya kusikiliza anayosema Mungu kupitia wajumbe wake hata ingawa tunayosikia huenda kwanza yakatusumbua au yakaonekana kuwa mambo yasiyowezekana.—Luka 1:26-37.
(2) Ujasiri wa kutenda kupatana na mapenzi ya Mungu ambayo amejifunza, na kumtumaini kabisa. (Ona Luka 1:38. Kama inavyoonyeshwa katika Kumbukumbu la Torati 22:23, 24, kungekuwa na matokeo mabaya ikiwa msichana Myahudi ambaye hajaolewa angepata mimba.)
(3) Nia ya Mungu kumtumia mtu bila kujali cheo chake maishani.—Linganisha Luka 2:22-24 na Mambo ya Walawi 12:1-8.
(4) Kutanguliza mambo ya kiroho. (Ona Luka 2:41; Matendo 1:14. Sheria haikuwataka wake Wayahudi wafunge safari ndefu pamoja na waume wao kwenda Yerusalemu wakati wa Pasaka kila mwaka, lakini Maria alifanya hivyo.)
(5) Kuthamini usafi wa kiadili.—Luka 1:34.
(6) Kuwa na bidii ya kufundisha watoto Neno la Mungu. (Hilo linaonekana kutokana na mambo ambayo Yesu alifanya akiwa na umri wa miaka 12. Ona Luka 2:42, 46-49.)
-