Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mashahidi wa Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Pendekezo lingine: ‘Asante kwa kuuliza swali hilo. Tungependa kuona hali zikiwa bora, sivyo? Hebu nikuulize, Wewe unaonaje yale ambayo Yesu Kristo mwenyewe alifanya? Je, ungesema kwamba njia aliyotumia kuwasaidia watu ilikuwa nzuri? . . . Sisi hujaribu kufuata mfano wake.’

      ‘Wakristo wanapaswa kuwa mashahidi wa Yesu, wala si wa Yehova’

      Unaweza kujibu hivi: ‘Hilo ni jambo lenye kupendeza. Na ni kweli kwamba tunapaswa kuwa mashahidi wa Yesu. Ndiyo sababu cheo cha Yesu katika kusudi la Mungu kinakaziwa katika vichapo vyetu. (Unaweza kutumia kitabu cha sasa au gazeti ili kuonyesha jambo hilo.) Lakini hapa pana jambo fulani ambalo huenda likawa jipya kwako. (Ufu. 1:5) . . . Yesu alikuwa “Shahidi Mwaminifu” wa nani? (Yoh. 5:43; 17:6) . . . Yesu alituwekea mfano tunaopaswa kufuata, sivyo?  . . . Kwa nini ni muhimu sana kumjua Yesu na Baba yake pia? (Yoh. 17:3)’

  • Mbingu
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Mbingu

      Maana: Makao ya Yehova Mungu na viumbe roho waaminifu; makao yasiyoonekana kwa macho ya kibinadamu. Biblia pia inatumia neno “mbingu” katika maana nyingine mbalimbali; kwa mfano: kuwakilisha Mungu mwenyewe, tengenezo lake la viumbe roho waaminifu, hali ya kuwa na kibali cha Mungu, ulimwengu unaoonekana mbali na dunia, anga inayozunguka Dunia, serikali za kibinadamu chini ya utawala wa Shetani, na serikali mpya ya mbinguni yenye uadilifu ambayo Yesu Kristo pamoja na warithi-washirika wake wamepewa mamlaka na Yehova watawale ndani yake.

      Je, sisi sote tulikuwa katika makao ya kiroho kabla hatujazaliwa tukiwa wanadamu?

      Yoh. 8:23: “[Yesu Kristo alisema:] ‘Ninyi mnatoka kwenye makao ya chini; mimi ninatoka kwenye makao ya juu. Ninyi mnatoka katika ulimwengu huu; mimi sitoki katika ulimwengu huu.’” (Yesu alitoka katika makao ya kiroho. Lakini, kama Yesu alivyosema, wanadamu wengine hawakutoka huko.)

      Rom. 9:10-12: “Rebeka alipochukua mimba ya mapacha . . . Walipokuwa bado hawajazaliwa wala kufanya jambo lolote jema au baya, ili kusudi la Mungu kuhusu kuchagua liendelee kutegemea, si matendo, bali Yeye ambaye huita, Rebeka aliambiwa: ‘Mkubwa atakuwa mtumwa wa mdogo.’” (Bila shaka, ikiwa mapacha hao, Yakobo na Esau, walikuwa wameishi katika makao ya kiroho kwa hakika wangekuwa na sifa ya kuwa wema au wabaya ikitegemea mwenendo wao huko, sivyo? Lakini hawakuwa na sifa zozote za aina hiyo mpaka baada ya kuzaliwa kwao wakiwa wanadamu.)

      Je, watu wote wema huenda mbinguni?

      Mdo. 2:34: “Daudi [ambaye Biblia inasema kwamba ni ‘mtu aliyekubalika kwa moyo wa Yehova’] hakupanda mbinguni.”

      Mt. 11:11: “Kwa kweli nawaambia ninyi, Kati ya wale waliozaliwa na wanawake hajatokea mkuu kuliko Yohana Mbatizaji; lakini mtu aliye mdogo zaidi katika ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye.” (Kwa hiyo Yohana hakuenda mbinguni alipokufa.)

      Zab. 37:9, 11, 29: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia . . . Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani. Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”

      Kama Adamu hangefanya dhambi, je, mwishowe angeenda mbinguni?

      Mwa. 1:26: “Mungu akaendelea kusema: ‘Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu, nao watawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na wanyama wa kufugwa na dunia yote na kila mnyama anayetembea juu ya dunia.’” (Mungu alikusudia Adamu aitunze dunia na wanyama waliomo. Hakuna lolote linalosemwa kuhusu kwenda kwake mbinguni.)

      Mwa. 2:16, 17: “Yehova Mungu akamwekea mtu amri hii: ‘Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.’” (Hapo mwanzoni Yehova hakukusudia mwanadamu afe siku moja. Amri ya Mungu iliyonukuliwa hapa inaonyesha kwamba alimwonya juu ya tendo ambalo lingemletea kifo. Kifo kingekuwa adhabu ya kutotii, si mlango wa kuingia katika maisha bora mbinguni. Ikiwa mwanadamu angetii, angeishi milele katika Paradiso ambayo Mungu alikuwa amempa. Ona pia Isaya 45:18.)

      Je, ni lazima mtu aende mbinguni ndipo awe na maisha yenye furaha kweli kweli?

      Zab. 37:11: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”

      Ufu. 21:1-4: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya . . . Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’”

      Mika 4:3, 4: “Hawatainua upanga, taifa juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena. Nao wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha; kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hivyo.”

      Je, Yesu aliwafungulia njia ya kwenda mbinguni wale waliokuwa wamekufa kabla ya kifo chake mwenyewe?

      Andiko la 1 Pet. 3:19, 20 linamaanisha nini? 1 Pet. 3:19, 20: “Katika hali hiyo [katika roho, baada ya kufufuliwa] pia [Yesu] alienda zake na kuwahubiria roho walio gerezani, ambao wakati fulani hawakuwa watiifu wakati subira ya Mungu ilipokuwa ikingoja katika siku za Noa, safina ilipokuwa ikijengwa, ambayo ndani yake watu wachache, yaani, nafsi [“watu,” UV, ZSB, BHN, VB] nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” (Je, hao “roho walio gerezani” walikuwa nafsi za wanadamu waliokataa kutii mahubiri ya Noa kabla ya Gharika, na je, sasa walikuwa wamefunguliwa njia ya kwenda mbinguni? Unapolinganisha andiko la 2 Petro 2:4 na Yuda 6 na Mwanzo 6:2-4 utaona kwamba roho hao walikuwa malaika, wana wa Mungu waliokuwa wamevaa miili na kuoa katika siku za Noa. Katika 1 Petro 3:19, 20 neno la Kigiriki lililotafsiriwa “roho” ni pneuʹma·sin, lakini neno lililotafsiriwa “nafsi” ni psy·khaiʹ. “Roho” hao hawakuwa nafsi zilizojivua mwili bali walikuwa malaika wasiotii; “nafsi” zinazotajwa hapa zilikuwa watu walio hai, wanadamu, Noa na nyumba yake. Kwa hiyo lazima ‘roho hao walio gerezani’ walihubiriwa ujumbe wa hukumu.)

      Andiko la 1 Petro 4:6 linamaanisha nini? “Kwa kweli, kwa kusudi hili habari njema ilitangazwa kwa wafu pia, ili wahukumiwe kuhusiana na mwili kwa maoni ya wanadamu lakini waishi kuhusiana na roho kwa maoni ya Mungu.” (Je, “wafu” hao walikuwa ni watu waliokufa kabla ya Kristo kufa? Kama ilivyokwisha kuonyeshwa, wafu si “roho walio gerezani.” Roho hao walikuwa malaika wasiotii. Na mahubiri hayo hayangeweza kuwasaidia wanadamu waliokufa kimwili kwa sababu, kama andiko la Mhubiri 9:5 linavyosema, wafu “hawajui lolote kamwe,” na andiko la Zaburi 146:4 linaongezea kwamba mtu anapokufa “mawazo yake hupotea.” Lakini andiko la Waefeso 2:1-7, 17 linamaanisha watu waliokuwa wafu kiroho na ambao walianza kuishi kiroho walipokubali habari njema.)

      Je, “Agano Jipya” huonyesha kwamba Wakristo wote wana tumaini la kuishi mbinguni?

      Yoh. 14:2, 3: “Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. Kama sivyo, ningaliwaambia ninyi, kwa sababu ninaenda kuwatayarishia ninyi mahali. Pia, nikienda na kuwatayarishia ninyi mahali, nitakuja tena nami nitawapokea ninyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo mimi, ninyi pia muwe hapo.” (Hapa Yesu anaonyesha kwamba mitume wake waaminifu, aliokuwa akisema nao, baada ya muda fulani wangekuwa katika “nyumba” ya Baba yake, mbinguni, pamoja na Yesu. Lakini yeye hasemi hapa ni wangapi wengine ambao pia wangeenda mbinguni.)

      Yoh. 1:12, 13: “Wengi kadiri ileile waliompokea [Yesu], aliwapa mamlaka ya kuwa watoto wa Mungu, kwa sababu walikuwa wakionyesha imani katika jina lake; nao walizaliwa, si kutokana na damu au kutokana na mapenzi ya mwili au kutokana na mapenzi ya mwanadamu, bali kutokana na Mungu.” (Ona kwamba muktadha, katika mstari wa 11, unaelekeza kwa Wayahudi, ‘watu wa Yesu mwenyewe.’ Wengi wao kadiri waliompokea alipokuja kwao katika karne ya kwanza wakawa watoto wa Mungu, wakiwa na tumaini la uzima wa mbinguni. Maneno katika andiko hilo yanarejezea tendo katika wakati uliopita, kwa hiyo fungu hilo halielekezi kwa watu wote ambao wamekuwa Wakristo tangu hapo.)

      Rom. 8:14, 16, 17: “Wote wanaoongozwa na roho ya Mungu, hao ndio wana wa Mungu. Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu. Basi, ikiwa sisi ni watoto, sisi pia ni warithi: warithi wa Mungu kwelikweli, lakini warithi pamoja na Kristo, mradi tu tunateseka pamoja ili pia tutukuzwe pamoja.” (Wakati maneno hayo yalipoandikwa, wote walioongozwa na roho ya Mungu walikuwa wana wa Mungu ambao tumaini lao lilikuwa kutukuzwa pamoja na Kristo. Lakini hali haikuwa hivyo sikuzote kabla ya wakati huo. Andiko la Luka 1:15 linasema kwamba Yohana Mbatizaji angejawa na roho takatifu, lakini andiko la Mathayo 11:11 linaonyesha wazi kwamba yeye hataushiriki utukufu wa Ufalme wa mbinguni. Basi, pia, baada ya kukusanywa kwa warithi wa Ufalme wa mbinguni, kungekuwako wengine ambao wangemtumikia Mungu wakiwa wafuasi wa Mwanawe na bado wasishiriki katika utukufu wa mbinguni.)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki